Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Macho ya Yehova Yanayong’aa’ Yanawachunguza Wote
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Oktoba 15
    • ‘Macho ya Yehova Yanayong’aa’ Yanawachunguza Wote

      “Macho [ya Yehova] yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu.”—ZAB. 11:4.

      1. Tunavutiwa na watu wa aina gani?

      UNA maoni gani kuhusu watu wanaopendezwa nawe kikweli? Unapowaomba wakueleze waziwazi maoni yao kuhusu jambo fulani, wanafanya hivyo bila kukuficha lolote. Unapohitaji msaada, wako tayari kukusaidia. Unapohitaji shauri, wanakushauri kwa upendo. (Zab. 141:5; Gal. 6:1) Bila shaka, unavutiwa na watu kama hao! Yehova na Mwana wake wanapendezwa nawe kikweli. Wanapendezwa nawe kuliko mwanadamu mwingine yeyote, na hawafanyi hivyo kwa sababu ya ubinafsi hata kidogo; wanataka kukusaidia ‘ushike imara uzima ulio wa kweli.’—1 Tim. 6:19; Ufu. 3:19.

      2. Yehova anapendezwa na watumishi wake kadiri gani?

      2 Mtunga-zaburi Daudi alieleza jinsi Yehova anavyopendezwa sana nasi aliposema hivi: “Macho [ya Yehova] yanaangalia, macho yake yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu.” (Zab. 11:4) Ndiyo, Mungu hatuangalii tu, bali pia anatuchunguza. Pia, Daudi aliandika hivi: “Umeuchunguza moyo wangu, umefanya ukaguzi wakati wa usiku . . . Utagundua kwamba sijapanga hila.” (Zab. 17:3) Bila shaka, Daudi alijua kwamba Yehova anapendezwa sana naye. Alijua kwamba Yehova angeumia na kuchukizwa ikiwa angesitawisha mawazo ya dhambi au kuwa na moyo wenye hila. Je, Yehova ni halisi kwako kama alivyokuwa kwa Daudi?

      Yehova Anaona Moyo

      3. Yehova anaonyesha jinsi gani kwamba anaelewa hali yetu ya kutokamilika?

      3 Yehova anapendezwa hasa na jinsi tulivyo kwa ndani, yaani, jinsi moyo wetu ulivyo. (Zab. 19:14; 26:2) Kwa upendo, yeye hakazii fikira makosa madogo-madogo. Kwa mfano, Sara, mke wa Abrahamu, alipokosa kumwambia malaika ukweli, inaonekana kwamba malaika huyo alitambua kuwa Sara aliogopa na kuaibika, kwa hiyo akamkaripia Sara kwa upole tu. (Mwa. 18:12-15) Ayubu alipotangaza “nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu,” Yehova hakumnyima baraka, kwa kuwa alijua kwamba Ayubu alikuwa ameteswa sana na Shetani. (Ayu. 32:2; 42:12) Vivyo hivyo, Yehova hakukasirika wakati yule mjane wa Sarefathi alipomwambia nabii Eliya waziwazi mambo yaliyokuwa moyoni mwake. Mungu alielewa kwamba mjane huyo alikuwa na huzuni nyingi baada ya mwana wake wa pekee kufa.—1 Fal. 17:8-24.

      4, 5. Yehova alionyesha fadhili kwa njia gani aliposhughulika na Abimeleki?

      4 Kwa sababu Yehova anauchunguza moyo, anawajali hata watu ambao si waamini. Fikiria jinsi alivyoshughulika na Abimeleki, mfalme wa jiji la Ufilisti la Gerari. Kwa kuwa Abimeleki hakutambua kwamba Abrahamu na Sara ni wenzi wa ndoa, alimchukua Sara ili awe mke wake. Hata hivyo, kabla ya Abimeleki kulala naye, Yehova alimwambia hivi katika ndoto: “Mimi pia nimejua kwamba katika unyoofu wa moyo wako umefanya hili, nami pia nilikuwa nikikuzuia usinitendee dhambi. Ndiyo sababu mimi sikukuruhusu umguse. Lakini sasa mrudishe mke wa huyo mwanamume, kwa maana yeye ni nabii, naye atakuombea dua. Kwa hiyo uendelee kuishi.”—Mwa. 20:1-7.

      5 Kwa hakika, Yehova angemtendea kwa ukali Abimeleki, aliyeabudu miungu ya uwongo. Lakini Mungu aliona kwamba katika kisa hicho, Abimeleki alikuwa ametenda kwa unyoofu. Kwa fadhili, Yehova alitambua jambo hilo, naye akamwambia mfalme huyo jinsi anavyoweza kupata msamaha na ‘kuendelea kuishi.’ Je, hungependa kumwabudu Mungu wa aina hiyo?

      6. Yesu alimwiga Baba yake kwa njia gani?

      6 Yesu alimwiga Baba yake kikamilifu. Alikazia fikira sifa nzuri za wanafunzi wake na alikuwa tayari kuwasamehe makosa yao. (Marko 10:35-45; 14:66-72; Luka 22:31, 32; Yoh. 15:15) Mtazamo wa Yesu ulipatana na maneno yake kwenye Yohana 3:17: “Mungu alimtuma Mwana wake ulimwenguni, si ili auhukumu ulimwengu, bali ili ulimwengu uokolewe kupitia kwake.” Ndiyo, Yehova na Yesu wanatupenda sana na wanatupenda sikuzote. Tunajua wanatupenda kwa sababu wanataka tupate uzima. (Ayu. 14:15) Upendo huo unatusaidia kuelewa kwa nini Yehova anatuchunguza, maoni yake kutuhusu, na hatua anazochukua baada ya kutuchunguza.—Soma 1 Yohana 4:8, 19.

      Kuchunguzwa kwa Upendo

      7. Yehova anatuchunguza akiwa na nia gani?

      7 Basi, ni vibaya kama nini kufikiri kwamba Yehova ni kama polisi anayetutazama akiwa mbinguni ili atukamate tunapofanya dhambi! Shetani ndiye anayetushuku na kutushtaki. (Ufu. 12:10) Hata wakati ambapo watu hawana nia mbaya, Shetani anadai kwamba wana nia mbaya! (Ayu. 1:9-11; 2:4, 5) Mtunga-zaburi aliandika hivi kumhusu Mungu: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zab. 130:3) Jibu la swali hilo ni, Hakuna hata mmoja! (Mhu. 7:20) Hata hivyo, Yehova anatuchunguza kwa rehema na fadhili kama mzazi anayejali ambaye anataka kuwalinda watoto wake wapendwa wasiumie. Mara nyingi anatuonyesha udhaifu wetu ili tuepuke kujiumiza.—Zab. 103:10-14; Mt. 26:41.

      8. Ni kwa njia gani Yehova anawafundisha na kuwatia nidhamu watumishi wake?

      8 Upendo wa Mungu unaonekana kupitia mafundisho na nidhamu anayotoa katika Maandiko na chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; Ebr. 12:5, 6) Pia, Yehova anatusaidia kupitia kutaniko la Kikristo na “zawadi katika wanadamu.” (Efe. 4:8) Zaidi ya hayo, Yehova anatutazama ili aone jinsi tunavyotumia mazoezi anayotupa kwa upendo, naye anatafuta njia za kutusaidia hata zaidi. Andiko la Zaburi 32:8 linasema hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” Basi, ni jambo la maana kama nini tumsikilize Yehova sikuzote! Tunapaswa kuendelea kuwa wanyenyekevu mbele zake, na kutambua kwamba yeye ni Mwalimu na Baba yetu mwenye upendo.—Soma Mathayo 18:4.

      9. Tunapaswa kuepuka sifa gani mbaya, na kwa nini?

      9 Kwa upande mwingine, tusiwe wagumu kamwe kwa sababu ya kiburi, kukosa imani, au “nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Ebr. 3:13; Yak. 4:6) Mara nyingi, sifa hizo mbaya zinaanza wakati mtu anapositawisha mawazo au tamaa zisizofaa. Anaweza hata kufikia hatua ya kukataa mashauri ya Biblia yanayomhusu. Anaweza hata kuendelea kuwa na mtazamo mbaya au kujiingiza sana katika mwenendo mbaya hivi kwamba anakuwa adui wa Mungu—jambo lenye kuogopesha kama nini! (Met. 1:22-31) Fikiria mfano wa Kaini, mzaliwa wa kwanza wa Adamu na Hawa.

      Yehova Anaona Mambo Yote na Anachukua Hatua Inayofaa

      10. Kwa nini Yehova alikataa toleo la Kaini, na Kaini alifanya nini?

      10 Kaini na Abeli walipomtolea Yehova toleo, hakupendezwa tu na zawadi yao bali alipendezwa pia na nia yao. Hivyo, Mungu alikubali toleo la Abeli, lililotolewa kwa imani, lakini akakataa toleo la Kaini, ambalo kwa njia fulani halikutolewa kwa imani. (Mwa. 4:4, 5; Ebr. 11:4) Badala ya kujifunza kupitia tukio hilo na kubadili mtazamo wake, Kaini alimkasirikia sana ndugu yake.—Mwa. 4:6.

      11. Kaini alionyesha jinsi gani kwamba ana moyo wenye hila, na tunajifunza nini?

      11 Yehova aliona kwamba mtazamo wa Kaini ulikuwa hatari, naye akazungumza na Kaini kwa upendo na kumwambia kwamba akitenda mema, atainuliwa. Inasikitisha kwamba Kaini alipuuza shauri la Muumba wake na kumuua ndugu yake. Moyo mbaya wa Kaini ulionekana pia alipojibu kwa dharau swali hili la Mungu: “Yuko wapi Abeli ndugu yako?” Kaini akapayuka hivi: “Sijui. Kwani mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” (Mwa. 4:7-9) Moyo unaweza kuwa wenye hila kama nini—hata unaweza kumfanya mtu adharau shauri linalotoka kwa Mungu mwenyewe! (Yer. 17:9) Hivyo basi, acheni tujifunze kupitia masimulizi hayo na kukataa haraka mawazo na tamaa zisizofaa. (Soma Yakobo 1:14, 15.) Tukishauriwa kupitia Biblia, acheni tuthamini mashauri hayo na kuona kwamba tumeyapokea kwa sababu Yehova anatupenda.

      Hakuna Dhambi ya Siri

      12. Yehova anatenda jinsi gani anapomchukulia hatua mtenda-dhambi?

      12 Huenda wengine wakafikiri kwamba ikiwa hakuna mtu yeyote anayewaona wakitenda mabaya, basi hawataadhibiwa. (Zab. 19:12) Kwa kweli, hakuna dhambi ya siri. “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Ebr. 4:13) Yehova ni Mwamuzi anayechunguza nia zetu za ndani kabisa, naye anatenda kwa haki kamilifu anapomchukulia hatua mtenda-dhambi. Yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” Hata hivyo, “hatakosa kuadhibu” wale wasiotubu ‘wanapozoea kutenda dhambi kimakusudi’ au kuonyesha mtazamo wa udanganyifu, wa kupanga hila. (Kut. 34:6, 7; Ebr. 10:26) Jambo hilo lilionekana Yehova aliposhughulika na Akani, na Anania na Safira.

      13. Huenda mawazo mabaya yalimchochea jinsi gani Akani atende mabaya?

      13 Akani alivunja waziwazi amri ya Mungu wakati alipochukua nyara kutoka katika jiji la Yeriko na kuzificha ndani ya hema lake, na inaelekea aliungwa mkono na familia yake. Dhambi yake ilipofichuliwa, Akani alionyesha kwamba alitambua uzito wa jambo alilotenda, kwa sababu alisema hivi: “Nimemtendea dhambi Yehova.” (Yos. 7:20) Akani alikuwa amesitawisha moyo mbaya kama Kaini. Pupa hasa ndiyo iliyomchochea Akani awe mdanganyifu. Kwa kuwa nyara zilizotoka Yeriko zilikuwa za Yehova, ni kana kwamba Akani alimwibia Mungu, na jambo hilo lilifanya auawe pamoja na familia yake.—Yos. 7:25.

      14, 15. Kwa nini Anania na Safira walistahili hukumu ya Mungu, nasi tunajifunza nini?

      14 Anania na mke wake, Safira, walikuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Yerusalemu. Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., hazina fulani ilianzishwa ili kushughulikia mahitaji ya kimwili ya waamini wapya kutoka nchi za mbali ambao walibaki Yerusalemu. Hazina hiyo ilitegemezwa kwa michango iliyotolewa kwa kupenda. Anania aliuza shamba, naye akatoa kiasi fulani cha pesa alizopata ziwe mchango kwa hazina hiyo. Hata hivyo, Anania alidai kwa unafiki kwamba ametoa pesa zote, na mke wake alijua vizuri kabisa jambo hilo. Inaonekana wenzi hao wa ndoa walitaka kuonwa kuwa watu wa pekee katika kutaniko. Lakini walitenda kwa udanganyifu. Yehova alimfunulia kimuujiza mtume Petro udanganyifu huo, kisha Petro akamuuliza Anania kwa nini amedanganya. Papo hapo, Anania akaanguka chini, naye akafa. Muda mfupi baadaye, Safira pia akafa.—Mdo. 5:1-11.

      15 Anania na Safira hawakufanya dhambi kwa sababu ya udhaifu wa muda mfupi. Walipanga hila na kusema uwongo ili kuwadanganya mitume. Na jambo baya hata zaidi ni kwamba ‘walimdanganya Mungu na roho takatifu.’ Hatua ambayo Yehova alichukua inaonyesha wazi kabisa kwamba yuko tayari kulilinda kutaniko lisiwe na wanafiki. Kwelikweli, “ni jambo lenye kuogopesha kuanguka mikononi mwa Mungu aliye hai”!—Ebr. 10:31.

      Endelea Kuwa Mtimilifu Nyakati Zote

      16. (a) Shetani anajitahidi jinsi gani kuwachafua watu wa Mungu? (b) Ibilisi anatumia njia gani kuwachafua watu katika eneo lenu?

      16 Shetani anajitahidi juu chini kutuchafua na kutuzuia tusikubaliwe na Yehova. (Ufu. 12:12, 17) Nia mbovu za Ibilisi zinaonekana wazi katika ulimwengu, ambao umezama katika uasherati na jeuri. Sasa ponografia (picha au habari za ngono) inaweza kupatikana kwa urahisi kupitia kompyuta au vyombo vingine vya elektroniki. Tusikubali kamwe kushindwa na mashambulizi ya Shetani. Badala yake, acheni tuseme kama mtunga-zaburi Daudi, aliyeandika hivi: “Nitatenda kwa busara katika njia isiyo na kosa. . . . Nitatembea katika utimilifu wa moyo wangu ndani ya nyumba yangu.”—Zab. 101:2.

      17. (a) Kwa nini mwishowe Yehova anafichua dhambi zilizofichwa? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      17 Leo, Yehova hafunui kimuujiza dhambi nzito na mwenendo wa udanganyifu kama alivyofanya nyakati nyingine zamani. Lakini bado anaona mambo yote, na kwa wakati wake na kwa njia yake anafichua mambo yaliyofichwa. Paulo alisema hivi: “Dhambi za watu wengine huwa wazi mbele ya watu wote, zikiongoza moja kwa moja kwenye hukumu, lakini kwa habari ya watu wengine pia dhambi zao huwa wazi baadaye.” (1 Tim. 5:24) Upendo hasa ndio unaomfanya Yehova afichue matendo mabaya. Analipenda kutaniko na anataka kulilinda likiwa safi. Pia, anawaonyesha rehema wale waliotenda dhambi na ambao sasa wametubu kikweli. (Met. 28:13) Basi, acheni tujitahidi kuendelea kuwa na moyo kamili mbele za Mungu na kukataa mambo yote yanayoweza kutuchafua.

      Endelea Kuwa na Moyo Kamili

      18. Mfalme Daudi alitaka mwana wake awe na maoni gani kumhusu Mungu?

      18 Mfalme Daudi alimwambia hivi Sulemani, mwana wake: “Mjue Mungu wa baba yako, umtumikie kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe; kwa maana Yehova anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira.” (1 Nya. 28:9) Daudi alitaka mwana wake afanye mengi zaidi kuliko kumwamini tu Mungu. Alitaka Sulemani athamini jinsi ambavyo Yehova anapendezwa sana na watumishi Wake. Je, unamthamini Yehova kwa njia hiyo?

      19, 20. Kulingana na Zaburi 19:7-11, ni nini kilichomsaidia Daudi amkaribie Mungu, nasi tunaweza kumwiga Daudi jinsi gani?

      19 Yehova anajua kwamba watu wenye mwelekeo unaofaa watavutwa kwake na kwamba ujuzi kuhusu sifa zake zenye kuvutia utachochea mioyo yao. Hivyo, Yehova anataka tumjue na kufahamu utu wake wenye kuvutia. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo? Ni kujifunza Neno lake na kuona baraka zake maishani mwetu.—Met. 10:22; Yoh. 14:9.

      20 Je, unasoma Neno la Mungu kila siku ukiwa na mtazamo unaofaa na kusali ili uweze kutumia mambo unayojifunza? Je, unaona faida za kuishi kulingana na kanuni za Biblia? (Soma Zaburi 19:7-11.) Ikiwa ndivyo, imani na upendo wako kumwelekea Yehova utazidi kukua. Naye Yehova atakukaribia na kutembea pamoja nawe akiushika mkono wako. (Isa. 42:6; Yak. 4:8) Ndiyo, Yehova atakuthibitishia kwamba anakupenda kwa kukubariki na kukulinda kiroho unapotembea katika barabara yenye nafasi ndogo inayoenda kwenye uzima.—Zab. 91:1, 2; Mt. 7:13, 14.

  • Yehova Anatutazama kwa Faida Yetu
    Mnara wa Mlinzi—2008 | Oktoba 15
    • Yehova Anatutazama kwa Faida Yetu

      “Macho [ya Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 NYA. 16:9.

      1. Kwa nini Yehova anatuchunguza?

      YEHOVA ni Baba mkamilifu. Anatujua vizuri sana hivi kwamba anajua hata “mwelekeo wa fikira” zetu. (1 Nya. 28:9) Hata hivyo, hatuchunguzi ili kupata tu makosa. (Zab. 11:4; 130:3) Badala yake, anataka kutulinda kwa upendo kutokana na jambo lolote linaloweza kuharibu uhusiano wetu pamoja naye au matarajio yetu ya kupata uzima wa milele.—Zab. 25:8-10, 12, 13.

      2. Yehova anatumia nguvu zake kwa ajili ya nani?

      2 Yehova ni Mweza-Yote, naye anaona kila kitu. Kwa sababu hiyo, anaweza kuwasaidia washikamanifu wake wakati wowote wanapomwomba msaada, naye anaweza kuwategemeza wanapopata majaribu. Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linasema: “Macho [ya Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” Ona kwamba Yehova anatumia nguvu zake kwa ajili ya wale wanaomtumikia kwa moyo kamili, moyo ulio safi na mnyoofu. Hatumii nguvu zake kwa ajili ya watu ambao ni wadanganyifu au wanafiki.—Yos. 7:1, 20, 21, 25; Met. 1:23-33.

      Tembea Pamoja na Mungu

      3, 4. Ni nini maana ya “kutembea pamoja na Mungu,” na ni mifano gani ya Biblia inayotusaidia kuelewa jambo hilo?

      3 Wengi hawaamini kwamba Muumba wa mbingu na dunia anawaruhusu wanadamu watembee pamoja naye kwa njia ya mfano. Lakini, hivyo ndivyo Yehova anavyotaka tufanye. Katika nyakati za Biblia, Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu.’ (Mwa. 5:24; 6:9) Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Ebr. 11:27) Mfalme Daudi alitembea kwa unyenyekevu pamoja na Baba yake wa mbinguni. Alisema hivi: “Kwa sababu [Yehova] yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.”—Zab. 16:8.

      4 Bila shaka, hatuwezi kuushika mkono wa Yehova na kutembea naye kihalisi. Lakini tunaweza kufanya hivyo kwa njia ya mfano. Jinsi gani? Mtunga-zaburi Asafu aliandika hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako.” (Zab. 73:23, 24) Kwa ufupi, tunatembea pamoja na Yehova tunapofuata kwa makini shauri lake, ambalo tunapokea hasa kupitia Neno lake lililoandikwa na kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45; 2 Tim. 3:16.

      5. Yehova anawatazama jinsi gani washikamanifu wake kama baba mwenye upendo, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kumhusu?

      5 Kwa kuwa Yehova anawathamini wale wanaotembea pamoja naye, anawatazama kama baba mwenye upendo, anawajali, anawalinda, na kuwafundisha. Mungu anasema hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zab. 32:8) Jiulize hivi: ‘Je, ninajiwazia nikitembea pamoja na Yehova nikiwa nimeushika mkono wake na kusikiliza hekima yake na kujua kwamba ananitazama kwa upendo? Je, mawazo, maneno, na matendo yangu yanaonyesha kwamba ninatambua kuwa Yehova yupo? Na ninapokosea, je, ninamwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo na mwenye rehema anayetaka kuwasaidia watu wanaotubu ili wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye badala ya kumwona kuwa Mungu mkali na asiyejali?’—Zab. 51:17.

      6. Yehova ana uwezo gani ambao wazazi wanadamu hawana?

      6 Nyakati nyingine, Yehova anaweza kutusaidia hata kabla hatujatenda jambo lisilofaa. Kwa mfano, anaweza kuona kwamba moyo wetu wenye hila umeanza kutamani mambo yasiyofaa. (Yer. 17:9) Katika hali kama hiyo, anaweza kuchukua hatua haraka kuliko wazazi wanadamu kwa sababu “macho yake yanayong’aa” yana uwezo wa kuona ndani yetu kabisa, kuchunguza fikira zetu za ndani kabisa. (Zab. 11:4; 139:4; Yer. 17:10) Fikiria jinsi Mungu alivyoshughulikia hali fulani iliyotokea katika maisha ya Baruku, rafiki wa karibu na mwandishi wa nabii Yeremia.

      Alimhangaikia Baruku Kama Baba Mwenye Upendo

      7, 8. (a) Baruku alikuwa nani, na ni tamaa gani zisizofaa ambazo huenda zilianza kusitawi katika moyo wake? (b) Ni kwa njia gani Yehova alimhangaikia Baruku kama baba mwenye upendo?

      7 Baruku alikuwa mwandishi stadi aliyetumikia kwa uaminifu pamoja na Yeremia katika mgawo mgumu wa kutangaza hukumu za Yehova huko Yuda. (Yer. 1:18, 19) Wakati fulani, Baruku, ambaye huenda alitoka katika familia maarufu, alianza kujitafutia mambo “makuu.” Labda alianza kusitawisha tamaa ya kichoyo ya kutaka makuu au alitamani kutajirika. Vyovyote vile, Yehova aliona kwamba mawazo hayo hatari yameanza kusitawi katika moyo wa Baruku. Akizungumza kupitia Yeremia, Yehova alishughulikia haraka jambo hilo kwa kumwambia hivi Baruku: “Umesema: ‘Ole wangu, sasa, kwa maana Yehova ameongeza huzuni juu ya maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kuugua kwangu, nami sikupata mahali pa kupumzika.’” Kisha Mungu akasema: “Unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta.”—Yer. 45:1-5.

      8 Ingawa Yehova alimpa Baruku shauri thabiti, hakutenda kwa hasira. Badala yake, alimjali kikweli kama baba mwenye upendo. Inaelekea Mungu aliona kwamba tamaa ya Baruku haikutokana na moyo mwovu au moyo uliopotoka. Pia, Yehova alijua kwamba Yerusalemu na Yuda zilikuwa katika siku za mwisho, naye hakutaka Baruku ajikwae wakati huo hatari. Kwa hiyo, ili kumsaidia mtumishi wake aone mambo waziwazi, Mungu alimkumbusha kwamba ‘Ataleta msiba juu ya wote wenye mwili,’ naye akaongeza kwamba ikiwa Baruku atatenda kwa hekima, ataishi. (Yer. 45:5) Ni kana kwamba Mungu alisema: ‘Fungua macho, Baruku. Kumbuka mambo ambayo yatapata Yuda na Yerusalemu zenye dhambi hivi karibuni. Endelea kuwa mwaminifu na uishi! Nitakulinda.’ Inaonekana Yehova aliugusa moyo wa Baruku, kwa maana Baruku alirekebisha maoni yake na kuokoka uharibifu wa Yerusalemu, uliotukia miaka 17 baadaye.

      9. Unaweza kujibu jinsi gani maswali yaliyo katika fungu?

      9 Unapotafakari kuhusu simulizi la Baruku, fikiria maswali na maandiko haya: Njia ambayo Mungu alitumia kumshughulikia Baruku inaonyesha nini kumhusu Yehova na maoni yake kuhusu watumishi wake? (Soma Waebrania 12:9.) Kwa kuwa tunaishi katika nyakati hatari, tunaweza kujifunza nini kutokana na shauri ambalo Mungu alimpa Baruku na kutokana na jinsi Baruku alivyoitikia? (Soma Luka 21:34-36.) Wazee Wakristo wanaweza kumwiga Yeremia jinsi gani katika kuonyesha kwamba wanawahangaikia watumishi wa Yehova kama Yehova anavyofanya?—Soma Wagalatia 6:1.

      Mwana Aliiga Upendo wa Baba

      10. Ni uwezo gani ambao Yesu amepewa ili atimize daraka lake akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo?

      10 Katika nyakati za kabla ya Ukristo, Yehova alifunua upendo wake kwa watu wake kupitia manabii wake na watumishi wengine waaminifu. Katika siku zetu, upendo huo unaonyeshwa hasa na Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu Kristo. (Efe. 1:22, 23) Hivyo, katika kitabu cha Ufunuo, Yesu anafananishwa na mwana-kondoo mwenye “macho saba, macho ambayo yanamaanisha roho saba za Mungu ambazo zimetumwa katika dunia nzima.” (Ufu. 5:6) Ndiyo, Yesu ana utambuzi kamili kwa sababu ametiwa nguvu kikamili na roho takatifu ya Mungu. Yeye pia anaona jinsi tulivyo kwa ndani, na hakuna jambo linalotendeka bila yeye kujua.

      11. Kristo anatimiza daraka gani, na mtazamo wake kutuelekea unaonyesha nini kuhusu mtazamo wa Baba yake?

      11 Hata hivyo, sawa na Yehova, Yesu si kama polisi anayetutazama akiwa mbinguni. Yesu anatuchunguza kwa upendo. Jina la Yesu la cheo “Baba wa Milele,” linatukumbusha daraka ambalo atatimiza katika kuwapa uzima wa milele wote wanaomwamini. (Isa. 9:6) Zaidi ya hayo, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Kristo anaweza kuwachochea Wakristo wakomavu na walio tayari kutumika, hasa wazee, kuwafariji au kuwashauri wale wanaohitaji kufarijiwa au kushauriwa.—1 The. 5:14; 2 Tim. 4:1, 2.

      12. (a) Barua kwa makutaniko saba ya Asia Ndogo zinaonyesha nini kumhusu Yesu? (b) Wazee wanaonyesha jinsi gani mtazamo wa Kristo kuelekea kondoo wa Mungu?

      12 Barua za Kristo kwa wazee wa makutaniko saba ya Asia Ndogo zinaonyesha kwamba anapendezwa sana na kondoo. (Ufu. 2:1–3:22) Katika barua hizo, Yesu alionyesha kwamba alijua mambo yaliyokuwa yakitendeka katika kila kutaniko na jinsi alivyowahangaikia sana wafuasi wake. Na anajua hata zaidi mambo yanayotendeka leo kwa kuwa maono ya Ufunuo yanatimizwa katika “siku ya Bwana.”a (Ufu. 1:10) Upendo wa Kristo unaonyeshwa mara nyingi kupitia wazee ambao wanatumikia wakiwa wachungaji wa kiroho wa kutaniko. Inapohitajika, anaweza kuwachochea wachungaji hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” kutoa faraja, kuwatia watu moyo, na kuwashauri. (Efe. 4:8; Mdo. 20:28; soma Isaya 32:1, 2.) Je, unaona kwamba jitihada zao zinaonyesha kuwa Kristo anapendezwa nawe kibinafsi?

      Msaada kwa Wakati Unaofaa

      13-15. Mungu anaweza kuamua kujibu sala zetu jinsi gani? Toa mifano.

      13 Je, umewahi kusali kwa bidii ili upate msaada na sala hiyo ikajibiwa wakati ulipotembelewa na kutiwa moyo na Mkristo mkomavu? (Yak. 5:14-16) Au labda ulipata msaada kupitia hotuba katika mkutano wa Kikristo au kichapo chetu kimoja. Mara nyingi Yehova anajibu sala katika njia hizo. Kwa mfano, baada ya mzee mmoja kutoa hotuba, alifikiwa na dada fulani ambaye alikuwa ametendewa isivyo haki majuma machache kabla ya hapo. Badala ya kulalamika kuhusu tatizo lake, dada huyo alieleza jinsi alivyothamini sana habari fulani za Kimaandiko katika hotuba hiyo. Habari hizo zilihusu hali yake na zilimfariji sana. Alifurahi kama nini kwamba alihudhuria mkutano huo!

      14 Kuhusiana na msaada tunaopata kupitia sala, fikiria mfano wa wanaume watatu waliojifunza kweli za Biblia walipokuwa gerezani na kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Kwa sababu ya kisa fulani cha jeuri, wafungwa wote katika gereza hilo walinyimwa mapendeleo fulani. Jambo hilo lilisababisha uasi. Ili kuonyesha kwamba wameasi, wafungwa waliamua kwamba hawatarudisha sahani zao baada ya kupata kiamsha-kinywa asubuhi iliyofuata. Wahubiri hao watatu wangefanya nini? Ikiwa wangeunga mkono uasi huo, wangekosa kutii shauri la Yehova kwenye Waroma 13:1. Kama hawangeunga mkono uasi huo, wangeshambuliwa na wafungwa wenzao wenye hasira.

      15 Kwa kuwa wanaume hao watatu hawangeweza kuwasiliana, walisali ili wapate hekima. Asubuhi iliyofuata, wote watatu waligundua kwamba wamefanya uamuzi uleule—walikataa kiamsha-kinywa. Walinzi walipokuja baadaye ili kukusanya sahani, wanaume hao watatu hawakuwa na sahani ambazo wangerudisha. Walifurahi kama nini kwamba “msikiaji wa sala” alisikia sala zao!—Zab. 65:2.

      Kutarajia Wakati Ujao Bila Wasiwasi

      16. Kazi ya kuhubiri inaonyesha jinsi gani kwamba Yehova anawajali watu walio kama kondoo?

      16 Kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri ni jambo lingine linaloonyesha kwamba Yehova anawahangaikia watu wenye moyo mnyoofu popote pale wanapoishi. (Mwa. 18:25) Yehova anaweza kuwaongoza watumishi wake kwa watu walio kama kondoo hata ikiwa watu hao wanaishi katika maeneo ambako habari njema hazijahubiriwa, na mara nyingi anatumia malaika ili kufanya hivyo. (Ufu. 14:6, 7) Kwa mfano, kupitia malaika, Mungu alimwongoza Filipo, mweneza-injili wa karne ya kwanza amtafute ofisa Mwethiopia na kumfafanulia Maandiko. Kulikuwa na matokeo gani? Mtu huyo alikubali habari njema na kuwa mfuasi aliyebatizwa wa Yesu.b—Yoh. 10:14; Mdo. 8:26-39.

      17. Kwa nini hatupaswi kuhangaika kupita kiasi kuhusu wakati ujao?

      17 Kadiri mfumo wa mambo wa sasa unavyokaribia kwisha, “maumivu ya taabu” yaliyotabiriwa yataendelea. (Mt. 24:8) Kwa mfano, huenda bei za vyakula zikapanda sana kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu, hali mbaya sana ya hewa, au matatizo ya kiuchumi. Huenda ikawa vigumu zaidi kupata kazi, na huenda wafanyakazi wakalazimika kufanya kazi kwa saa nyingi zaidi. Vyovyote itakavyokuwa, wote wanaotanguliza mambo ya kiroho na kuendelea kuwa na ‘jicho rahisi’ hawapaswi kuhangaika kupita kiasi. Wanajua kwamba Mungu anawapenda na atawatunza. (Mt. 6:22-34) Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Yehova alimtunza Yeremia wakati wa mwisho wenye msukosuko wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.

      18. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba anampenda Yeremia wakati Yerusalemu lilipozingirwa?

      18 Wababiloni walipokaribia kumaliza kuzingira Yerusalemu, Yeremia alifungwa katika Ua wa Walinzi. Angepata chakula jinsi gani? Ikiwa angekuwa huru, angekitafuta. Lakini sasa angeweza tu kukipata kutoka kwa watu waliokuwa karibu naye, na wengi wao walimchukia! Hata hivyo, Yeremia hakuwategemea wanadamu, bali alimtegemea Mungu ambaye aliahidi kumtunza. Je, Yehova alitimiza ahadi yake? Bila shaka! Alihakikisha kwamba kila siku Yeremia alipata “mkate wa mviringo . . . mpaka mkate wote ulipokwisha jijini.” (Yer. 37:21) Yeremia, na pia Baruku, Ebed-meleki, na wengine, waliokoka wakati huo wa njaa, magonjwa, na kifo.—Yer. 38:2; 39:15-18.

      19. Tunapongojea wakati ujao, tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      19 Ndiyo, “macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.” (1 Pet. 3:12) Je, unafurahi kwamba Baba yako wa mbinguni anakutazama? Je, unahisi ukiwa salama salimini kwa sababu unajua kwamba anakutazama kwa faida yako? Basi, azimia kuendelea kutembea pamoja na Mungu, hata mambo yawe namna gani wakati ujao. Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova, kama baba mwenye upendo, atawachunguza washikamanifu wake wote.—Zab. 32:8; soma Isaya 41:13.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa barua hizo zinawahusu hasa wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta, kanuni zake zinawahusu watumishi wote wa Mungu.

      b Mfano mwingine unaoonyesha jinsi Mungu anavyotoa mwongozo unapatikana katika Matendo 16:6-10. Andiko hilo linasema kwamba Paulo na wenzake “walikatazwa na roho takatifu” wasihubiri katika Asia na Bithinia. Badala yake, walitumwa Makedonia, ambako watu wengi wapole waliikubali injili.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki