-
Je, Mungu Anatujali?Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
SEHEMU YA 1
Je, Mungu Anatujali?
ULIMWENGU leo umejaa matatizo. Mamilioni ya watu hukabiliana na vita, misiba ya asili, magonjwa, umaskini, ufisadi, na maovu mengine. Huenda wewe pia unakabili mahangaiko kila siku. Ni nani anayeweza kutusaidia? Kuna yeyote anayetujali?
Mungu anatupenda sana hata kuliko jinsi mama anavyompenda mtoto wake
Tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anatujali kikweli. Anasema hivi katika Neno lake Takatifu: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.”a
Je, haifariji kujua hivyo? Mungu anatupenda sana hata kuliko jinsi mama anavyompenda mtoto wake—mojawapo ya hisia zenye nguvu sana za mwanadamu. Mungu hatatuacha kamwe! Tayari ametusaidia kwa njia ya kustaajabisha. Jinsi gani? Kwa kutuonyesha siri ya kuwa na maisha yenye furaha—imani ya kweli.
Kuwa na imani ya kweli kutakupa furaha. Imani hiyo itakusaidia kuepuka matatizo mengi na itakusaidia kushughulikia kwa mafanikio matatizo ambayo huwezi kuepuka. Pia itakusaidia kumkaribia Mungu na kukupa amani ya akili na ya moyoni. Imani ya kweli itakuwezesha kuwa na wakati ujao ulio bora—uzima wa milele katika Paradiso!
Hata hivyo, imani ya kweli ni nini? Na unaweza kuisitawisha jinsi gani?
-
-
Imani ya Kweli Ni Nini?Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
SEHEMU YA 2
Imani ya Kweli Ni Nini?
Kama pesa, lazima imani iwe ya kweli ili iwe yenye thamani
KUWA na imani ya kweli kunahusisha mengi kuliko kuamini tu kwamba kuna Mungu. Kuna mamilioni ya watu wanaoamini kuna Mungu lakini wanatenda maovu kimakusudi. “Imani” ya aina hiyo ni kama pesa bandia. Inaonekana kuwa halisi lakini kwa kweli haina thamani. Hivyo basi, imani ya kweli ni nini?
Imani ya kweli inategemea ujuzi sahihi wa Maandiko Matakatifu. Maandishi hayo yaliyoongozwa na roho hutuambia ukweli kumhusu Mungu nayo hutuwezesha kumjua. Yanafunua sheria zake, makusudi yake, na mafundisho yake. Mafundisho hayo yanatia ndani:
Mungu ni mmoja. Hakuna aliye sawa naye.
Yesu si Mungu Mweza-Yote. Yeye ni nabii wa Mungu.
Mungu hushutumu ibada ya sanamu ya kila aina.
Wanadamu wanakabili siku ya hukumu.
Wanadamu wengi wasio na hesabu watafufuliwa waishi katika Paradiso.
Imani ya kweli hutuchochea kutenda mema. Matendo ya aina hiyo humtukuza Mungu na pia hutunufaisha na kuwanufaisha wengine. Matendo hayo mema hutia ndani mambo kama vile
kumwabudu Mungu.
kusitawisha sifa zinazokubaliwa na Mungu—hasa upendo.
kukataa mawazo na tamaa mbaya.
kudumisha imani katika Mungu licha ya majaribu.
kuwafundisha wengine kuhusu Mungu.
Imani ya kweli hutokeza matendo mema
Unaweza kusitawisha Imani ya Kweli Jinsi Gani?
Imani ni kama msuli, huwa na nguvu unapotumiwa
Mwombe Mungu akusaidie. Nabii Musa alisali kwa Mungu: “Nijulishe, tafadhali, njia zako, nipate kukujua, ili nipate kibali machoni pako.”a Mungu alisikia na kujibu sala yake. Musa alikuwa mfano mzuri wa mtu mwenye imani. Mungu atakusaidia wewe pia usitawishe imani ya kweli.
Tenga wakati wa kujifunza Maandiko Matakatifu. Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu, kutia ndani Taurati, Zaburi, na Injili, yanaweza kupatikana katika Biblia Takatifu, kitabu ambacho kimetafsiriwa na kusambazwa zaidi ulimwenguni. Je, una nakala ya maandishi hayo yaliyoongozwa na roho?
Tumia shauri la Maandishi Matakatifu katika maisha yako ya kila siku. Imani ni kama msuli, huwa na nguvu unapotumiwa. Unapotenda kulingana na imani, inakuwa na nguvu pia. Utajionea mwenyewe kwamba shauri la Mungu linafanya kazi. Bila shaka, mashauri yaliyo katika Maandiko Matakatifu yameboresha maisha ya watu wengi. Endelea kusoma ili uone mifano kadhaa.
-
-
Mashauri Yenye Hekima Yanayoboresha MaishaImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 3
Mashauri Yenye Hekima Yanayoboresha Maisha
WAZIA kwamba daktari mpya amehamia eneo lenu. Huenda mwanzoni usimwamini. Lakini namna gani ikiwa baadhi ya rafiki zako wametibiwa naye na afya yao imekuwa nzuri? Huenda wewe pia ungefikiria kumwona daktari huyo, sivyo?
Kwa njia fulani, Maandiko Matakatifu ni kama daktari huyo. Watu fulani huogopa kutafuta mashauri ya Maandiko hayo. Lakini wanapoyatumia mashauri yaliyomo, maisha yao huwa mazuri sana. Ona mifano kadhaa.
Kutatua Matatizo Katika Ndoa
“Mapema katika ndoa yetu, nilihisi kwamba mume wangu, Dumas, alikuwa akinipuuza,” akumbuka Sumiatun. “Mara nyingi kwa sababu ya kutamaushwa, nilimtukana, nikamtupia vitu, na hata kumpiga. Nyakati nyingine ningekasirika sana mpaka ningezirai.
“Dumas alipoanza kujifunza Maandiko Matakatifu, nilimdhihaki. Hata hivyo, nilikuwa nikisikiliza kwa siri yale aliyokuwa akijifunza nikiwa katika chumba kingine. Siku moja, nilisikia mistari fulani ikisomwa: ‘Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana . . . Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.’ (Waefeso 5:22, 33) Maneno hayo yalinigusa moyo. Nikamwomba Mungu anisamehe kwa kumtukana mume wangu, na nikamwomba Mungu anisaidie kuwa mke bora. Muda si muda, Dumas nami tukaanza kujifunza Maandiko pamoja.”
Dumas na Sumiatun
Pia, Maandiko matakatifu yanasema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28) Sumiatun asema: “Kujifunza mambo hayo kulikuwa na matokeo mazuri kwetu. Nilianza kumpa Dumas chai alipofika nyumbani kutoka kazini na nilizungumza naye kwa fadhili. Dumas naye alinipenda zaidi na kunisaidia kufanya kazi za nyumbani. Sote tulijitahidi ‘kuwa wenye fadhili, wenye huruma nyororo, wenye kusameheana kwa hiari.’ (Waefeso 4:32) Hivyo, hatua kwa hatua tukaanza kupendana na kuheshimiana. Kwa zaidi ya miaka 40 sasa, ndoa yetu imekuwa yenye furaha. Mashauri yenye hekima katika Neno la Mungu yaliokoa ndoa yetu!”
Kudhibiti Hasira
“Nilikuwa mwenye hasira kali,” asema Tayib. “Mara nyingi nilijiingiza katika ugomvi na kuwatisha wengine kwa bunduki. Pia nilizoea kumpiga mke wangu, Kustriyah, na kumwangusha sakafuni. Watu wengi waliniogopa.
Kustriyah na Tayib husali pamoja kila usiku
“Siku moja, nilisoma maneno haya ya Yesu: ‘Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi.’ (Yohana 13:34) Maneno hayo yalinigusa moyo sana, nami nikaazimia kubadilika. Nilipopandwa na hasira, nilimwomba Mungu anisaidie niwe mtulivu. Baada ya muda, hasira yangu ilipungua. Mimi na mke wangu, tulitumia shauri hili la Waefeso 4:26, 27: ‘Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.’ Tulisoma Maandiko na kusali pamoja kila usiku. Kufanya hivyo kulituondolea mahangaiko ya siku na kutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu.
“Sasa ninajulikana kuwa mtu mwenye amani. Mke na watoto wangu wananipenda na kuniheshimu. Nina marafiki wengi, na ninahisi kuwa karibu na Mungu. Kwa kweli mimi ni mwenye furaha.”
Kushinda Mazoea ya Kutumia Dawa za Kulevya
Goin
“Nilikuwa nikishirikiana na genge la vijana, nilikuwa mvutaji sugu wa sigara, na mara nyingi usiku nililala barabarani nikiwa mlevi,” asema Goin. “Pia nilitumia na kuuza dawa haramu—bangi na dawa nyingine za kulevya—ambazo nilificha ndani ya fulana yangu ya kuzuia risasi. Ingawa nilionekana na kutenda kama jasiri, nyakati zote niliishi kwa woga.
“Kisha mtu fulani akanionyesha andiko hili: ‘Mwanangu, usiisahau sheria yangu . . . kwa sababu utaongezewa urefu wa siku na miaka ya uzima na amani.” (Methali 3:1, 2) Nilitamani maisha marefu na yenye amani! Pia nilisoma: ‘Wapendwa, kwa kuwa tuna ahadi hizi, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.’ (2 Wakorintho 7:1) Hivyo basi, nikaacha kutumia dawa za kulevya, nikavunja uhusiano wangu pamoja na lile genge, nami nikaanza kumtumikia Mungu.
“Kwa zaidi ya miaka 17 sasa, sijatumia dawa za kulevya. Nina afya nzuri, familia yenye furaha, marafiki wazuri, na dhamiri safi. Na badala ya kulala barabarani nikiwa mlevi, mimi hulala kitandani kwa utulivu kila usiku.”
Kushinda Ubaguzi
“Nikiwa kijana, nilikuwa mhalifu,” akumbuka Bambang, “nami niliwachukia sana watu wa kabila fulani dogo.
“Hata hivyo, baada ya muda, nilianza kumtafuta Mungu. Katika harakati zangu za kumtafuta, nikakutana na kikundi fulani kilichokuwa kikijifunza Maandiko Matakatifu. Nilisalimiwa kwa shauku na watu wa kabila lilelile nililokuwa nikilichukia! Pia nilitambua kwamba katika kikundi hicho cha kujifunza, watu wa jamii tofauti-tofauti walichangamana kwa furaha. Nilishangaa! Ndipo nikaelewa andiko linalosema: ‘Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.’—Matendo 10:34-35.
“Leo, sina chuki kuwaelekea wengine. Baadhi ya rafiki zangu ni wa kabila nililokuwa nikilichukia. Kupitia Maandiko Matakatifu, Mungu amenifundisha kuwa na upendo.”
Sasa, Bambang, hufurahia kushirikiana na watu wa jamii tofauti-tofauti
Kuacha Jeuri
“Nilipokuwa ningali kijana, nilifungwa gerezani mara tatu—mara mbili kwa kuiba na mara moja kwa kumdunga mtu kisu,” asema Garoga. “Baadaye, nikajiunga na kikundi cha waasi na kuwaua watu wengi. Baada ya mapigano hayo, niliongoza kikundi cha wahalifu kilichofanya unyang’anyi wa kimabavu. Niliandamana na walinzi wangu kila mahali. Nilikuwa mtu jeuri na hatari sana.
Garoga si jeuri tena bali sasa yeye ni mwalimu anayeheshimika wa Neno la Mungu
“Kisha, siku moja, nikasoma andiko hili: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya.’ (1 Wakorintho 13:4, 5) Maneno hayo yaligusa moyo wangu. Nilihamia eneo lingine, nikajifunza Maandiko, na kutumia mashauri yake maishani mwangu.
“Mimi si mjeuri tena. Badala yake, ninaheshimiwa nikiwa mwalimu wa Neno la Mungu. Maisha yangu yana kusudi na ni yenye kuridhisha kwelikweli.”
Neno la Mungu Lina Nguvu
Masimulizi hayo na mengine mengi yanathibitisha kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Waebrania 4:12) Mashauri yake ni rahisi, yana hekima, na ni yenye kujenga.
Je, Maandiko Matakatifu yanaweza kukusaidia pia? Ndiyo, yanaweza kukusaidia kutatua tatizo lolote unalokabili. “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.
Hivyo basi, acheni tuchunguze mafundisho kadhaa ya msingi yaliyo katika Maandiko Matakatifu.
-
-
Mungu Ni Nani?Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 4
Mungu Ni Nani?
WATU huabudu miungu mingi. Lakini Maandiko Matakatifu hufundisha kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli. Hana kifani, ni mkuu sana, na ni wa milele. Aliumba kila kitu mbinguni na duniani, na akatupa uhai. Kwa hiyo, yeye peke yake ndiye anayestahili kuabudiwa.
Sheria ilitolewa kupitia nabii Musa ikiwa “neno lililosemwa kupitia malaika”
Mungu ana jina moja tu la kibinafsi. Jina hilo ni YEHOVA. Mungu alimwambia Musa: “Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, ‘Yehova Mungu wa mababu zenu, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu.’ Hilo ndilo jina langu mpaka wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.” (Kutoka 3:15) Jina Yehova linapatikana katika Maandiko Matakatifu mara 7,000 hivi. Kama andiko la Zaburi 83:18 linavyosema kumhusu Mungu, “wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”
Kitabu cha Kukunjwa cha kale cha Bahari ya Chumvi kilicho na maandishi yanayoonyesha jina la Mungu
Hakuna mtu ambaye amewahi kumwona Mungu. Mungu alimwambia Musa: “Huwezi kuuona uso wangu, kwa sababu hakuna mwanadamu anayeweza kuniona na bado aishi.” (Kutoka 33:20) Mungu anaishi mbinguni na hakuna mtu anayeweza kumwona. Ni kosa kutengeneza au kutumia sanamu, picha, au mfano wa Mungu katika sala. Yehova Mungu aliamuru hivi kupitia nabii Musa: “Usijifanyie sanamu ya kuchongwa wala umbo lililo kama kitu chochote kilicho juu mbinguni wala kilicho chini duniani wala kilicho ndani ya maji chini ya dunia. Usiviinamie wala kushawishiwa kuvitumikia, kwa sababu mimi Yehova Mungu wako ni Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.” (Kutoka 20:2-5) Baadaye, kupitia nabii Isaya, Mungu alisema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe, wala sitazipa sanamu za kuchongwa sifa yangu.”—Isaya 42:8.
Watu fulani humwamini Mungu lakini huenda wakamwona kuwa asiyeweza kujulikana wala kufikiwa, wanayepaswa kumwogopa badala ya kumpenda. Una maoni gani? Je, Mungu anapendezwa na wewe? Unaweza kwa kweli kumjua, au hata kumkaribia? Acha tuone kile ambacho Maandiko yanasema kuhusu sifa za Mungu.
-
-
Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na KifaniImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 5
Kuthamini Sifa za Mungu Zisizo na Kifani
MAANDIKO Matakatifu hufunua sifa nyingi nzuri za Mungu na kutusaidia kumjua. Kwa mfano, Maandiko hutuambia kuhusu sifa nne kuu za Mungu—nguvu, haki, hekima, na upendo. Acheni tuchunguze kila moja ya sifa hizo.
Nguvu Zake Hazina Mipaka
Mungu ana nguvu nyingi
Yehova alimwambia Abrahamu: “Mimi ni Mungu Mweza-Yote.” (Mwanzo 17:1) Nguvu zake hazina kifani, hazina mipaka, wala haziwezi kwisha. Mungu aliumba ulimwengu wote mzima kwa nguvu zake.
Mungu hatumii nguvu zake vibaya kamwe. Sikuzote anazitumia kwa njia inayofaa na kwa kusudi. Anatumia nguvu zake kwa njia inayopatana kabisa na sifa yake ya haki, hekima, na upendo.
Yehova hutumia nguvu zake kuwasaidia watumishi wake waaminifu. “Macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Je, huvutiwi na Mungu huyo mwenye nguvu nyingi lakini mwenye kujali?
Mungu Mwenye Haki
“Yehova ni mpenda-haki.” (Zaburi 37:28) Sikuzote yeye hufanya yaliyo sawa na haki kulingana na viwango vyake vikamilifu.
Mungu hana ubaguzi
Mungu huchukia ukosefu wa haki. ‘Hamtendei yeyote kwa upendeleo wala hakubali rushwa.’ (Kumbukumbu la Torati 10:17) Huwapinga wanaowakandamiza wengine, naye hutenda kwa niaba ya wanaoonewa, kutia ndani ‘mjane yeyote au mvulana asiye na baba.’ (Kutoka 22:22) Mungu huwatendea wanadamu wote bila ubaguzi. “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Haki ya Yehova imesawazishwa kikamili. Yeye hawaendekezi watu wala si mkali kupita kiasi. Huwaadhibu wakosaji wasiotubu lakini huwaonyesha rehema wanaotubu. “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. Yeye hataendelea kutafuta makosa wakati wote, wala hataendelea kuweka kinyongo mpaka wakati usio na kipimo. Hakututendea kulingana na dhambi zetu; wala kuleta juu yetu kile tunachostahili kulingana na makosa yetu.” (Zaburi 103:8-10) Pia, Mungu hukumbuka na kuwapa thawabu watumishi wake washikamanifu. Je, hupaswi kumtegemea Mungu huyu mwenye haki?
Mungu Mwenye Hekima
Maandiko Matakatifu yana hekima ya Mungu
Yehova ndiye chanzo cha hekima yote. “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!” (Waroma 11:33) Hekima yake haina kifani na haina mwisho.
Hekima ya Mungu inaonekana waziwazi katika uumbaji. Mtunga-zaburi alisema: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima.”—Zaburi 104:24.
Hekima ya Mungu inafunuliwa pia katika Maandiko Matakatifu. Mfalme Daudi aliandika: “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zaburi 19:7) Hebu wazia—unaweza kujifunza kutokana na hekima ya Mungu isiyo na mipaka! Je, utafanya hivyo?
“Mungu Ni Upendo”
Sifa kuu ya Yehova ni upendo. Maandiko yanasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Upendo huchochea na kuongoza kila anachofanya.
Mungu hutuonyesha upendo kwa njia nyingi. Yeye hutupa vitu vizuri. “Alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Bila shaka, “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yakobo 1:17) Kupitia zawadi yenye thamani sana ya Maandiko, Mungu hutufunulia kweli kumhusu na kuhusu sheria na kanuni zake zenye upendo. Yesu alisali hivi: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.
Hekima ya Mungu inayoonekana katika uumbaji hutuchochea kumheshimu
Pia, Mungu hutusaidia tunapopata matatizo. “Mtupie Yehova mzigo wako, Naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” (Zaburi 55:22) Mungu hutusamehe dhambi zetu. “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe; na fadhili zenye upendo ni nyingi kwa wale wote wanaokuitia.” (Zaburi 86:5) Hata ametuahidi uzima wa milele. “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Utaonyesha jinsi gani kwamba unathamini upendo wa Mungu? Je, utampenda pia?
Mkaribie Mungu
Kusali na kutafakari kuhusu sifa za Mungu kutakusaidia kumkaribia zaidi
Mungu anataka umjue vizuri. Neno lake linahimiza: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Mungu alimwita nabii mwaminifu Abrahamu (Ibrahimu) “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Yehova anataka wewe pia uwe rafiki yake.
Kadiri unavyozidi kujifunza kumhusu Mungu, ndivyo utakavyohisi kuwa karibu naye na kuwa mwenye furaha zaidi. “Mwenye furaha ni mtu” ambaye “mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Hivyo basi, endelea kujifunza Maandiko Matakatifu. Tafakari sifa na kazi za Mungu. Onyesha kwamba unampenda Mungu kwa kutumia mambo unayojifunza. “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Basi, sali kama alivyosali mtunga-zaburi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe. Nitembeze katika kweli yako.” (Zaburi 25:4, 5) Utapata kujua kwamba Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.
-
-
Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 6
Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?
MUNGU aliumba dunia iwe makao yanayowafaa wanadamu. Neno lake linasema: “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”—Zaburi 115:16.
Kabla ya kumuumba mtu wa kwanza, Adamu, Mungu alichagua sehemu ndogo ya dunia iliyoitwa Edeni na huko akatengeneza bustani nzuri. Maandiko yanasema kwamba mto Efrati na mto Tigri (Hidekeli) ilitoka katika bustani ya Edeni.a Inadhaniwa kwamba bustani ya Edeni ilikuwa katika sehemu ambayo leo ni mashariki mwa Uturuki. Ndiyo, bustani ya Edeni ilikuwa duniani!
Mungu alimuumba Adamu na kumweka katika bustani ya Edeni “ailime na kuitunza.” (Mwanzo 2:15) Baadaye, Mungu akamuumbia Adamu mke—Hawa. Mungu akawaamuru wenzi hao: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Bila shaka, Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
Hata hivyo, Adamu na Hawa walimwasi Mungu kwa kuvunja sheria yake kimakusudi. Hivyo, Mungu akawaondoa kutoka katika bustani ya Edeni. Paradiso ikapotea. Nayo madhara yaliyosababishwa na dhambi ya Adamu yakaendelea. Maandiko yanasema: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.
Je, Yehova alitupilia mbali kusudi lake la awali—kwamba dunia iwe paradiso inayokaliwa na watu wenye furaha? Hapana! Mungu anasema: ‘Neno langu linalotoka katika kinywa changu, halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.’ (Isaya 55:11) Paradiso itarudishwa duniani!
Maisha katika Paradiso yatakuwa namna gani? Fikiria ahadi za Kimaandiko zinazoonyeshwa katika kurasa mbili zinazofuata.
a Andiko la Mwanzo 2:10-14 husema: “Kulikuwa na mto unaotoka katika Edeni ili kuinywesha bustani maji, na kutoka hapo ukaanza kugawanyika na kuwa vichwa vinne. Jina la ule wa kwanza ni Pishoni . . . jina la mto wa pili ni Gihoni . . . jina la mto wa tatu ni Hidekeli [au, Tigri]; ndio unaoelekea upande wa mashariki wa Ashuru. Na mto wa nne ni Efrati.” Mito miwili ya kwanza haijulikani wala mahali ilipokuwa hapajulikani.
-
-
Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia ManabiiImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 7
Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia Manabii
MANABII wa kale walimwamini Mungu. Waliamini ahadi zake na kuishi kulingana nazo. Ahadi hizo zilitia ndani nini?
Mara baada ya Adamu na Hawa kuasi katika Edeni, Mungu aliahidi kwamba angemchagua mtu ambaye angeponda kichwa cha “nyoka” anayewakilisha “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani,” na kumharibu milele. (Mwanzo 3:14, 15; Ufunuo 12:9, 12) Mtu huyo angethibitika kuwa nani?
Miaka 2,000 baada ya kutoa unabii huo, Yehova alimwahidi nabii Abrahamu kwamba Yule Anayekuja angetokana na uzao wake. Mungu alimwambia Abrahamu: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.
Mnamo 1473 K.W.K., Mungu alimpa nabii Musa habari zaidi kuhusu “uzao” huo. Musa aliwaambia wana wa Israeli: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kumbukumbu la Torati 18:15) Kama Musa, nabii huyo anayekuja angetoka miongoni mwa wana wa Abrahamu.
Pia, nabii huyo angekuwa mzao wa Mfalme Daudi naye angekuwa mfalme mkuu. Mungu alimwahidi Mfalme Daudi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ (2 Samweli 7:12, 13) Mungu pia alifunua kwamba mzao huyo wa Daudi ataitwa “Mkuu wa Amani,” akaongeza: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo.” (Isaya 9:6, 7) Ndiyo, Kiongozi huyo mwadilifu atairudisha amani na haki ulimwenguni pote. Lakini angetokea wakati gani?
“Uzao” ulioahidiwa . . . ungetokana na uzao wa Abrahamu, ungekuwa nabii kama Musa, ungetokana na ukoo wa Daudi, ungetokea mwaka wa 29 W. K., ungemponda nyoka, Shetani
Baadaye malaika Gabrieli alimwambia hivi nabii wa Mungu, Danieli: “Nawe ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.” (Danieli 9:25) Hayo yalikuwa majuma 69 ya miaka—kila juma likiwa na miaka 7—ambayo jumla yake ni miaka 483. Ilianza mwaka wa 455 K.W.K. mpaka mwaka wa 29 W.K.a
Je, kweli Masihi, nabii aliye kama Musa na ambaye ni “uzao” uliosubiriwa kwa muda mrefu, alikuja mwaka wa 29 W.K.? Acheni tuone.
a Ona ukurasa wa 197-199 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Masihi AtokeaImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 8
Masihi Atokea
MIAKA zaidi ya 500 baada ya Danieli kutoa unabii, malaika wa Mungu, Gabrieli alimtokea msichana bikira aitwaye Maria, mzao wa Mfalme Daudi. Gabrieli akamwambia, “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” (Luka 1:28) Hata hivyo, Maria aliogopa. Salamu ya Gabrieli ilikuwa na maana gani?
Gabrieli alimwambia Maria kwamba atamzaa Masihi
Gabrieli akaeleza: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu; na, tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na . . . ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:30-33) Hiyo ilikuwa habari njema kama nini! Maria angemzaa Masihi, “uzao” uliosubiriwa sana!
Mwaka uliofuata, Yesu alizaliwa Bethlehemu. Usiku huo, malaika aliwatangazia hivi wachungaji: “Tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa . . . kwa sababu leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” (Luka 2:10, 11) Baadaye, familia ya Yesu ilihamia Nazareti, ambako alikulia.
Mnamo mwaka wa 29 W.K.—mwaka hususa ambao Masihi alitazamiwa kutokea—Yesu alianza kutumikia akiwa nabii wa Mungu, akiwa “na umri wa karibu miaka 30.” (Luka 3:23) Watu wengi wakaja kutambua kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Wakasema: “Nabii mkuu ameinuliwa katikati yetu.” (Luka 7:16, 17) Hata hivyo, Yesu alifundisha nini?
Yesu aliwafundisha watu kumpenda na kumwabudu Mungu: Alisema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja, nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:29, 30) Pia, alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.
Yesu aliwahimiza watu wapendane: Alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31) Pia alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo; hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.”—Mathayo 7:12.
Yesu alikuwa na bidii ya kuwatangazia wengine Ufalme wa Mungu: Alisema, “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini Ufalme wa Mungu ni wa maana sana?
Maandiko yanafundisha kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia. Yesu, yule Masihi, ndiye ambaye Mungu amemteua kuwa Mfalme. Katika maono, nabii Danieli aliona mapema Mungu akimkabidhi Masihi “utawala na heshima na ufalme,” mbinguni. (Danieli 7:14) Ufalme huo utaifanya dunia yote kuwa Paradiso na kuwapa watumishi wa Mungu zawadi ya uzima wa milele. Je, hizo si habari njema?
-
-
Kujifunza Kutoka kwa Masihi KiongoziImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 9
Kujifunza Kutoka kwa Masihi Kiongozi
MUNGU alitabiri kwamba atamweka rasmi Masihi kuwa Kiongozi wa watu wote. Mungu anajua ni kiongozi wa aina gani tunayehitaji naye alimchagua Kiongozi bora zaidi. Masihi alithibitika kuwa Kiongozi wa aina gani? Jenerali mwenye nguvu? Mwanasiasa mwenye ustadi? Mwanafalsafa mwenye hekima? Kulingana na Maandiko Matakatifu, Masihi alikuwa nabii Yesu Kristo aliyekuwa tofauti na wengine wote.—Mathayo 23:10.
Mungu alihakikisha kwamba Yesu alizaliwa akiwa mkamilifu na mtakatifu. Zaidi ya hayo, Yesu alishinda jitihada zote za Shetani za kutaka kumpotosha. Kwa maneno na matendo, Yesu alionyesha kikamilifu jinsi ambavyo Mungu hutumia nguvu zake na vilevile haki, hekima, na upendo. Ona jinsi tunavyoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu.
Yesu alipenda sana kuwasaidia wengine
Yesu alitumia nguvu alizopewa na Mungu ili kuwasaidia wengine. Yesu aliwajali watu kwelikweli, naye alitumia nguvu zake kwa ukarimu kutosheleza mahitaji yao. Alisema, “Ninausikitikia umati, kwa sababu . . . hawana chakula.” (Marko 8:2) Kisha kimuujiza, Yesu akaulisha umati mkubwa wa watu waliokuja kumsikiliza akifundisha.
Yesu pia alisafiri sana, akifundisha na “kuponya kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu katikati ya watu.” (Mathayo 4:23) Haishangazi kwamba umati wa watu ulimfuata, na “umati wote ulikuwa ukitafuta kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka na kuwaponya wote.” (Luka 6:19) Bila shaka, Yesu alikuja, “si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28)a Ni viongozi wangapi wa kibinadamu wanaoonyesha roho hiyo ya kujidhabihu?
Yesu aliwapenda watoto
Yesu alionyesha haki ya Mungu. Yesu alifuata maagizo yote ya sheria ya Mungu na kuishi kulingana na kanuni zinazopatikana katika sheria hiyo. Kama Maandiko yalivyotabiri, ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema, “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zaburi 40:8) Yesu aliwatendea wote—matajiri kwa maskini, wanaume kwa wanawake, watoto kwa watu wazima—kwa adabu, heshima, na bila ubaguzi, kama afanyavyo Mungu. Wakati fulani wanafunzi wa Yesu waliwakemea wazazi waliokuwa wakiwaleta watoto kwa Yesu. Lakini Yesu akawaambia: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.”—Marko 10:14.
Yesu alionyesha hekima ya Mungu. Yesu aliwaelewa watu vizuri. “Yeye mwenyewe alijua kile kilichokuwa ndani ya mwanadamu.” (Yohana 2:25) Maadui wa Yesu walipotuma watu wamkamate, watu hao walikiri: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” Yesu alipata wapi hekima yake? Alieleza hivi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.”—Yohana 7:16, 46.
Yesu aliwahurumia na kuwaponya wagonjwa
Yesu alionyesha upendo wa Mungu. Pia, Yesu aliwahurumia watu. Mwanamume mmoja aliyekuwa ‘amejaa ukoma’ alimwomba: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Akimsikitikia, Yesu “akaunyoosha mkono wake, akamgusa, na kusema: ‘Ninataka. Takasika.’ Na mara moja ule ukoma ukamtoka.” (Luka 5:12, 13; Marko 1:41, 42) Kwa kweli Yesu alitaka sana kumwondolea maumivu mtu huyo aliyekuwa akiteseka.
Je, Yesu anakujali wewe pia? Yesu mwenyewe ajibu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.”—Mathayo 11:28, 29.
Yesu ndiye Kiongozi bora tunayeweza kupata. Hivyo basi anatuhimiza: ‘Jifunzeni kutoka kwangu.’ Je, utaukubali mwaliko wake wenye kugusa moyo? Ukifanya hivyo utakuwa na maisha yenye furaha.
a Unaweza kupata maelezo zaidi kuhusu fidia katika sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
-
-
Kumfunua Adui wa ImaniImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 10
Kumfunua Adui wa Imani
MUDA mrefu kabla Yehova Mungu hajaiumba dunia, aliwaumba malaika mbinguni. Hata hivyo, baada ya muda fulani, malaika mmoja alianza kutamani ibada ambayo ni haki ya Mungu. Kwa kutenda kulingana na tamaa hiyo, malaika huyo alijifanya mwenyewe Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani,” yaani, mtu anayempinga Mungu. Shetani alimpinga Mungu jinsi gani?
Shetani alitumia nyoka kumdanganya Hawa
Shetani alimshawishi Hawa asimtii Mungu. Kwa hila, alidokeza kwamba Yehova Mungu alikuwa akiwanyima kitu fulani kizuri kwa kuwakataza kula matunda ya mti fulani. Bila haya, alimwita Mungu mwongo na kudokeza kwamba Hawa anapaswa kukataa kuongozwa na Mungu, akisema: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:5) Kwa ujinga Hawa akaamini uwongo wa Shetani. Akavunja amri ya Mungu na kumshawishi Adamu kufanya vivyo hivyo. Tangu wakati huo, Shetani amekuwa adui ya wale walio na imani ya kweli. Naye ameendelea kuwadanganya watu mpaka leo. Jinsi gani?
Imani Iliyopotoka Yaenea
Shetani ametumia ibada ya sanamu na mapokeo ya kibinadamu kuwapotosha watu
Shetani alitumia ibada ya sanamu na mapokeo ya kibinadamu kuwapotosha wana wa Israeli. Yesu, yule Masihi, aliwaambia viongozi wao wa kidini kwamba kwa sababu wamefundisha “amri za wanadamu kuwa mafundisho,” ibada yao ilikuwa ya bure. (Mathayo 15:9) Taifa hilo lilipomkataa Masihi, Mungu alilikataa pia. Yesu aliwaambia: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mathayo 21:43) Wafuasi wa Kristo wakawa ndiyo watu wanaokubaliwa na Mungu.
Kisha Shetani akafanya juu chini kuwapotosha wafuasi wa Yesu. Je, alifani-kiwa? Katika mfano wa kinabii, Yesu alitabiri kile ambacho kingetokea. Katika mfano huo, mtu fulani alipanda mbegu nzuri za ngano katika shamba. Baadaye, adui akapanda magugu katikati ya ngano. Mazao yote yaliachwa yakue hadi wakati wa mavuno. Kisha magugu yakatenganishwa na ngano na kuharibiwa. Lakini ngano ikakusanywa na kuhifadhiwa katika ghala la mwenye shamba.
Kisha Yesu akawafafanulia wanafunzi wake maana ya mfano huo. Yeye mwenyewe ndiye Mpandaji. “Nayo mbegu nzuri,” akaendelea, “hiyo ni wana wa ufalme; lakini magugu ni wana wa yule mwovu, na yule adui aliyepanda ni Ibilisi. Yale mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo, na wavunaji ni malaika.” (Mathayo 13:38, 39) Yesu aliwafananisha wanafunzi wake wa kweli na ngano. Lakini Shetani alipanda wanafunzi wa uwongo, kama magugu, katikati ya wafuasi hao wa kweli wa Yesu. Hivyo, kama Yesu mwenyewe alivyotabiri, karne nyingi baada ya kifo chake, wanafunzi wa uwongo walitokea. Wanafunzi hao walichochea mafundisho ya waasi imani, kama vile Utatu, wazo la kwamba kuna watu watatu katika Mungu mmoja. Pia, wanafunzi hao wasio wa kweli walianza kuabudu sanamu na kujiingiza katika siasa. Ni wachache tu waliofuata mafundisho ya Yesu.
Imani ya Kweli Yadumu
Hata hivyo, kama Yesu alivyofafanua, mwishowe mabadiliko yangetokea. Malaika wa Mungu watawatenga wale wasio na imani ya kweli ili waharibiwe. Kisha, wale wenye imani ya kweli watatambuliwa kwa urahisi. Mwishowe, Shetani Ibilisi, adui wa zamani wa imani, ataharibiwa pia. Ndiyo, imani ya kweli itadumu!
Lakini, unaweza kuwatambua jinsi gani watu wenye imani ya kweli leo? Sehemu inayofuata itajibu swali hilo.
Malaika wa Mungu wanawatafuta watu wanaotamani kuwa na imani ya kweli
-
-
Kuonyesha Imani ya Kweli LeoImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 11
Kuonyesha Imani ya Kweli Leo
WATU wengi leo hudai kwamba wana imani. Hata hivyo, Yesu alifundisha kwamba ni watu wachache tu ambao wangekuwa na imani ya kweli. Alisema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.
Leo watu huonyesha kwamba wana imani ya kweli jinsi gani? “Kwa matunda yao mtawatambua,” Yesu akasema. “Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.” (Mathayo 7:16, 17) Hivyo basi, imani ya kweli huzaa “matunda mazuri.” Huwachochea watu kuwa na sifa zinazokubaliwa na Mungu. Jinsi gani?
Tumia Nguvu kwa Njia Inayofaa
Watu walio na imani ya kweli hutumia nguvu na mamlaka yao kumtukuza Mungu na kuwanufaisha wengine. Yesu alifundisha: “Yeyote yule anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu.” (Marko 10:43) Vivyo hivyo, wanaume wenye imani ya kweli si wakatili, wawe nyumbani au kwingineko. Wanawapenda wake zao, wanawaheshimu, na kushughulikia mahitaji yao kwa upendo. Maandiko yanasema: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) “Waume, endeleeni kukaa nao vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa ninyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, kusudi sala zenu zisizuiwe.”—1 Petro 3:7.
Kwa upande mwingine, mke ambaye ana imani ya kweli “anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Wake wanapaswa ‘kuwapenda waume zao na kuwapenda watoto wao.’ (Tito 2:4) Akina baba na mama walio na imani ya kweli hutenga wakati kuwa pamoja na watoto wao na kuwafundisha sheria na kanuni za Mungu. Wanapokuwa nyumbani, kazini, na penginepo, wao huwatendea wengine kwa staha na heshima. Wanafuata shauri hili la Kimaandiko: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.”—Waroma 12:10.
Watumishi wa Mungu hutii amri hii ya Kimaandiko: “Usikubali rushwa.” (Kutoka 23:8) Hawatumii kamwe mamlaka yao ili kujinufaisha. Badala yake, wao hutafuta fursa za kuwasaidia wengine, hasa walio na uhitaji. Wanatii shauri hili: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu hupendezwa vema na dhabihu za namna hiyo.” (Waebrania 13:16) Kwa hiyo, wanajionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Dumisha Viwango vya Mungu vya Haki
Watu wenye imani hutii sheria za Mungu kwa hiari, na kwao “amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Wanajua kwamba “sheria ya Yehova ni kamilifu . . . Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae.”—Zaburi 19:7, 8.
Imani ya kweli huwachochea pia kukataa kila aina ya ubaguzi. Hawapendelei watu wa jamii fulani, nchi fulani, au cheo fulani, badala yake, wanafuata mfano wa Mungu. “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.
Imani ya kweli huwachochea watu “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Pia, mtu mwenye imani huepuka porojo na uchongezi wenye kuumiza. Kuhusu mtu anayekubaliwa na Mungu, mtunga-zaburi Daudi aliandika: “Hakuchongea kwa ulimi wake. Hakumfanyia mwenzake jambo lolote baya.”—Zaburi 15:3.
Jifunze Hekima Kutoka kwa Mungu
Wale walio na imani ya kweli hutegemeza mafundisho yao katika Maandiko Matakatifu. Wanaamini kwamba “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Timotheo 3:16) Katika mahusiano yao pamoja na wengine, wao huonyesha “hekima inayotoka juu,” ambayo ni “safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema.” (Yakobo 3:17) Wanajiepusha na mapokeo yasiyofaa na kuwasiliana na pepo, nao ‘hujilinda na sanamu.’—1 Yohana 5:21.
Onyesha Upendo wa Kweli
Nabii Musa alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Kumbukumbu la Torati 6:5) Watu wenye imani huwa na upendo wa aina hiyo kumwelekea Mungu. Wanaliheshimu jina la Mungu, Yehova. Wao ‘humshukuru Yehova, na kuliitia jina lake’ kwa imani. (Zaburi 105:1) Watumishi wa Mungu hutii amri hii pia: “Nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” (Mambo ya Walawi 19:18) Wao hukataa jeuri na hujaribu kuwa “wenye kufanya amani na watu wote.” (Waroma 12:18) Kwa njia ya mfano, ‘wamefua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu.’ (Isaya 2:4) Kwa sababu hiyo, wana “upendo kati [yao] wenyewe” na wanafurahia undugu wa ulimwenguni pote. (Yohana 13:35) Je, unaweza kuwatambua watu wa aina hiyo leo?
-
-
Onyesha Kwamba Una Imani ya Kweli!Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 12
Onyesha Kwamba Una Imani ya Kweli!
MUNGU anawatahadharisha watumishi wake kwamba watazamie majaribu ya imani. Neno lake linasema: “Iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Huenda Shetani akajaribu kuvunja imani yako jinsi gani?
Umewahi kupata upinzani wa aina hii?
Shetani anaweza kutumia watu wengine, hata wapendwa wako, kukushinikiza usisome Maandiko Matakatifu. Kuhusu hilo, Yesu alitabiri: “Adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mathayo 10:36) Huenda watu wa familia na marafiki wasio na nia mbaya wasijue kweli nzuri ajabu zinazopatikana katika Neno la Mungu. Au huenda wakaogopa jinsi wengine watakavyowaona. Hata hivyo, Maandiko yanasema: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” (Methali 29:25) Ukiacha kujifunza Maandiko ili uwafurahishe wanadamu, je, hilo litamfurahisha Mungu? Bila shaka hapana! Kwa upande mwingine, tunapoonyesha imani ya kweli, Mungu hutusaidia. “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:39.
Kumbuka kisa cha Dumas, kilichotajwa mapema. Mwanzoni, mke wake alimdhihaki kwa sababu ya imani yake. Lakini baadaye alijiunga naye kujifunza Neno la Mungu. Vivyo hivyo, ukiendelea kutenda mema, huenda ukawachochea marafiki na wapendwa wako kutenda mema. Katika visa vingi, mtu wa familia ‘amevutwa bila neno kupitia mwenendo ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa,’ ya yule ambaye anaonyesha imani ya kweli.—1 Petro 3:1, 2.
Shetani hujaribu kuwafanya watu wafikiri kwamba wana shughuli nyingi sana wasiweze kujifunza Maandiko. Angependa matatizo ya maisha—mahangaiko ya kibinafsi na mahangaiko kuhusu pesa—‘yalisonge neno’ ili imani yako ‘ikose kuzaa matunda.’ (Marko 4:19) Kataa maoni hayo yasiyofaa! Maandiko yanasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ndiyo, kuendelea kujifunza mengi kumhusu Mungu na Yesu, yule Masihi, ni muhimu ili kuishi milele katika Paradiso!
Mwombe Mungu akusaidie
Mfikirie Musa aliyekuwa mmoja wa watu wa nyumba ya mfalme wa Misri. Angeweza kufuatilia mali, umashuhuri, na mamlaka. Hata hivyo, Musa alichagua “kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda.” Kwa nini? “Aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:24, 25, 27) Ndiyo, Musa alikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Alitanguliza mapenzi ya Mungu badala ya kufuatilia mambo ya kibinafsi, na Mungu akambariki sana. Ukifanya hivyo, Mungu atakubariki pia.
Huenda ukawa shabaha ya Shetani katika njia mbalimbali. Hata hivyo si lazima akunase. Neno la Mungu linatuhimiza: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Unaweza kumpinga jinsi gani?
Endelea kujifunza Maandiko Matakatifu. Soma Neno la Mungu kila siku. Jifunze mafundisho yake. Tumia mashauri yake. Kwa kufanya hivyo, ‘utachukua mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,’ ambayo yatakusaidia kukinga mashambulizi ya Shetani.—Waefeso 6:13.
Shirikiana na watu wenye imani ya kweli. Watafute wengine wanaosoma, wanaojifunza, na kutumia Maandiko Matakatifu. Watu hao ‘huchocheana katika upendo na matendo mazuri, . . . wakitiana moyo.’ Watakusaidia ukue katika imani.—Waebrania 10:24, 25.
Shirikiana na wengine walio na imani
Mkaribie Yehova. Mwombe Mungu akusaidie, na umtumaini. Usisahau kamwe kwamba Mungu anataka kukusaidia. ‘Mtupie [Mungu] mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:6, 7) “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.
Shetani humdhihaki Mungu akisema kwamba hakuna mtu anayeweza kumtumikia Mungu chini ya majaribu. Hata hivyo, una nafasi ya kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo! Mungu anasema: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Ndiyo, azimia kuonyesha kwamba una imani ya kweli!
-
-
Imani ya Kweli Huongoza Kwenye Furaha ya MileleImani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
-
-
Sehemu ya 13
Imani ya Kweli Huongoza Kwenye Furaha ya Milele
MAANDIKO Matakatifu yanasema: “mwadilifu—ataishi kwa njia ya imani.” (Waroma 1:17) Maneno hayo yana ahadi nzuri inayokuhusu wewe. Kwa njia gani?
Baada ya kumaliza kazi yake duniani, Yesu, yule Masihi, alipanda mbinguni ili kuwa na Mungu. Wanafunzi wake walipokuwa wakitazama, “akainuliwa na wingu likamchukua juu kutoka machoni pao.” (Matendo 1:9) Akiwa mbinguni, Mungu alimweka rasmi kuwa Mfalme wa mbinguni mwenye nguvu. Hivi karibuni, Yesu, “mwana wa binadamu,” atawasili “katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.” (Mathayo 25:31, 32) Mambo hayo yatatokea wakati gani?
Maandiko Matakatifu yanatabiri wakati ambapo kungekuwa na taabu ulimwenguni ambayo ingekuwa ishara ya kwamba karibuni Masihi atayahukumu mataifa. Yesu alieleza kile ambacho ishara hiyo ingehusisha: “Taifa litasimama kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi, na katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni na upungufu wa chakula; kutakuwa na mambo yenye kuogopesha.”—Luka 21:7, 10, 11.
Matatizo yaliyopo yanaonyesha kwamba karibuni Masihi atayahukumu mataifa
Leo, tunaona waziwazi maneno ya Yesu yakitimizwa. Karibuni Yesu atakuja kuwaharibu waovu. Mwishowe, hata Shetani ataharibiwa! Dunia yote itakuwa paradiso. Watu wote wataishi kwa amani hata pamoja na wanyama. “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao. Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote.” (Isaya 11:6, 9) “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ . . . Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.” (Isaya 33:24; 35:5) Hata wafu watafufuliwa. “Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote,” na “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Isaya 25:8; Ufunuo 21:4) Kisha, kusudi la awali la Mungu kuhusu dunia litatimizwa. Hilo ni tumaini zuri kama nini!
Endelea Kukua Katika Imani
Mungu atawapa watu wa aina gani zawadi ya kuishi katika Paradiso? Watu wenye imani—imani ya kweli!
Kumbuka kwamba imani ya kweli inategemea ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. Kwa hiyo, endelea kumjua Mungu na Yesu vizuri!
Watu wenye imani watafurahia Paradiso milele!
Imani ya kweli huambatana na matendo ya uadilifu. Neno la Mungu linasema: “Imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Kwa kufanya matendo hayo mazuri, utakuwa ukionyesha sifa nzuri za Mungu—nguvu, haki, hekima, na upendo. Endelea kujitahidi kusitawisha sifa hizo nzuri!
Kusitawisha imani ya kweli kutakuletea thawabu nyingi. Bila shaka, hiyo ndiyo siri ya kuwa na maisha yenye furaha—sasa na kuendelea mpaka wakati ujao usio na mwisho!
-