-
Aliwatetea Watu wa MunguMnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
Je, cheo hicho kipya kingemfanya awe na kiburi?
Bila shaka, hapana! Esta aliendelea kumheshimu Mordekai, baba yake mlezi. Hakufunua kwamba yeye ni Myahudi. Zaidi ya hayo, Mordekai alipomweleza kuhusu njama ya kumuua Ahasuero, kwa utii Esta alimweleza mfalme, na watu waliopanga njama hiyo wakauawa. (Esta 2:20-23) Bado alionyesha imani yake kwa Mungu kwa kuwa mnyenyekevu na mtiifu. Leo, utii hauonekani kuwa sifa nzuri, badala yake uvunjaji wa sheria na uasi ndiyo mambo ya kawaida. Lakini watu walio na imani ya kweli wanathamini utii kama vile Esta.
-
-
Aliwatetea Watu wa MunguMnara wa Mlinzi—2011 | Oktoba 1
-
-
Mordekai akatuma ujumbe kwa malkia, akimwomba Esta aingilie kati kwa kuzungumza na mfalme ili kuwatetea “watu wake mwenyewe.”—Esta 4:4-8.
Bila shaka, Esta aliingiwa na wasiwasi alipopata ujumbe huo. Lilikuwa jaribu kubwa sana la imani yake. Aliogopa na jambo hilo lilionekana wazi katika jibu lake kwa Mordekai. Esta alimkumbusha sheria ya mfalme. Ikiwa angeenda mbele ya mfalme bila kuitwa, angeuawa. Lakini mtu hangeuawa ikiwa mfalme angemnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu. Je, Esta alikuwa na sababu yoyote ya kutazamia kwamba hangeuawa, hasa akikumbuka kilichompata Vashti alipokataa kwenda mbele ya mfalme alipoagizwa kufanya hivyo? Alimwambia Mordekai kwamba mfalme hakuwa amemwita kwenda mbele yake kwa siku 30! Kwa sababu hakuwa ameitwa kwa siku nyingi, Esta hakujua ikiwa alikuwa amepoteza kibali cha mfalme ambaye hisia zake zilibadilika-badilika.d—Esta 4:9-11.
Mordekai alimjibu Esta kwa uhakika ili kuimarisha imani yake. Alimhakikishia kwamba ikiwa hangechukua hatua, wokovu wa Wayahudi ungetoka katika chanzo kingine. Lakini angewezaje kutazamia kuepuka kifo wakati ambapo Wayahudi wangeanza kuuawa? Mordekai alionyesha imani yake yenye nguvu kwa Yehova, ambaye hangeacha kamwe watu wake waangamizwe na ahadi zake zikose kutimizwa. (Yoshua 23:14) Kisha, Mordekai akamuuliza Esta: “Ni nani anayejua ikiwa si kwa ajili ya wakati kama huu kwamba umefikia heshima ya kifalme?” (Esta 4:12-14) Mordekai alimtegemea kabisa Yehova, Mungu wake. Je, sisi tunafanya hivyo?—Methali 3:5, 6.
Imani Yenye Nguvu Yafanya Asiogope Kifo
Sasa Esta alipaswa kufanya uamuzi. Alimwomba Mordekai awaambie Wayahudi wenzake waungane naye katika kufunga kwa siku tatu, na akamalizia ujumbe wake kwa maneno ambayo kwa muda mrefu yameonyesha imani na ujasiri: “Nikiangamia, na niangamie.” (Esta 4:15-17) Bila shaka, alisali kwa bidii sana katika siku hizo tatu kuliko wakati mwingine wowote maishani mwake. Mwishowe, wakati ukafika. Esta alijipamba na kuvalia mavazi bora ya kifalme ili avutie mbele ya mfalme. Kisha, akaingia mbele yake.
Kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa makala hii, Esta aliingia katika ua wa mfalme. Tunaweza tu kuwazia jinsi alivyohangaika akilini na moyoni na jinsi alivyosali kwa bidii. Aliingia ndani ya ua, mahali ambapo angeweza kumwona Ahasuero akiwa ameketi kwenye kiti chake cha ufalme. Labda aliutazama uso wa mfalme ili ajaribu kutambua hisia zake. Ikiwa Esta alihitaji kungoja kwa muda fulani, lazima alihisi kana kwamba amengoja kwa muda mrefu sana. Lakini muda huo ulipita na mume wake akamwona. Kwa kweli, alishangaa lakini akatulia. Kisha, akamnyooshea fimbo yake ya enzi ya dhahabu!—Esta 5:1, 2.
Esta alikuwa amefaulu kuzungumza na mfalme. Alikuwa ameamua kumtetea Mungu wake na watu wake, akiwawekea mfano mzuri watumishi wote waaminifu wa Mungu.
-