Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
    • Badiliko la Ajabu Latokea

      Je, programu hii ya kiwango kikubwa kweli imelainisha mioyo iliyo migumu ya wafungwa? Acheni wasimulie.

      “Sijapata kamwe kuwajua wazazi wangu kwa sababu waliniacha nilipokuwa mdogo, nami nilikuja kukosa kwa uchungu sana hisi za kupendwa,” akiri Zdzisław, mwanamume ambaye kiasili ni mwenye kutafakari. “Mapema katika maisha yangu, nilihusika na uhalifu, hatimaye nikaua kimakusudi. Hisia ya hatia ilinisukuma nifikirie kujiua, nami nilikuwa nikitafuta sana tumaini la kweli. Ndipo, katika 1987, nikapata gazeti Mnara wa Mlinzi. Kutokana nalo nilijifunza juu ya tumaini la ufufuo na uhai wa milele. Nikitambua kwamba bado kulikuwa na tumaini, niliacha lile wazo la kujiua nami nikaanza kujifunza Biblia. Sasa nimejifunza maana ya upendo kutoka kwa Yehova na akina ndugu.” Tangu 1993, huyu muuaji kimakusudi wa zamani amekuwa akitumikia akiwa mtumishi wa huduma na painia-msaidizi, na mwaka uliopita akawa painia wa kawaida.

      Kwa upande ule mwingine, Tomasz, alikubali mara moja funzo la Biblia. “Hata hivyo, hiyo haikuwa hatua ya moyo mweupe,” yeye akiri. “Nilikuwa najifunza tu kwa sababu nilitaka kujionyesha nilipokuwa nikieleza wengine itikadi za Mashahidi wa Yehova. Lakini sikuwa nikifanya mengi sana kuhusu kweli ya Biblia. Siku moja, niliazimia nami nikaenda kwenye mkutano wa Kikristo. Wafungwa waliobatizwa walinikaribisha kwa uchangamfu. Nilitambua kwamba badala ya kujaribu kujionyesha na ujuzi, nilipaswa kulainisha moyo wangu ulio mgumu na kugeuza akili yangu.” Tomasz alianza kujivika utu mpya wa Kikristo. (Waefeso 4:22-24) Leo, yeye ni Shahidi aliyejiweka wafu na kubatizwa naye hufurahia kuhubiri seli hadi seli.

      Msongo Kutoka kwa Marafiki wa Zamani

      Wale waliojifunza kweli ya Biblia wakiwa gerezani walipata msongo mkali kutoka kwa marafiki wa zamani katika jela na kutoka kwa maafisa wa gereza. Mmoja wao akumbuka: “Nilikuwa nikidhihakiwa kila mara na kudharauliwa. Lakini nilikumbuka maneno yenye kutia moyo ya akina ndugu. ‘Endelea kutoa sala kwa Yehova,’ wakaniambia. ‘Soma Biblia yako nawe utahisi amani ya kindani.’ Kwa kweli hilo lilinisaidia.”

      “Wafungwa wenzangu hawakukosa kuniambia maneno makali,” asema Ryszard, ndugu mwenye nguvu aliyebatizwa. “‘Waweza kwenda kwenye mikutano yako, lakini usijaribu kujitokeza na kujifanya wewe ni bora zaidi, Sawa?’ walikuwa wakinionya. Nilipofanya mabadiliko maishani mwangu kwa sababu ya kutumia kanuni za Biblia, ilinibidi niteseke kwa sababu hiyo. Walipindua kitanda changu, wakatupa fasihi zangu za Biblia, na kuchafua sehemu yangu katika seli. Nilitoa sala kwa Yehova anipe nguvu ya kujidhibiti kisha kwa utulivu nikaanza kufanya hiyo sehemu yangu ya seli iwe nadhifu. Baada ya muda fulani, mashambulio hayo yalikoma.”

      “Wafungwa wenzetu waonapo kwamba tumefanya uamuzi imara wa kumtumikia Yehova,” wasimulia ndugu wengine wafungwa waliobatizwa, “msongo wa aina tofauti hutokea. Wao huelekea kusema hivi, ‘Kumbuka, haupaswi kunywa, kuvuta sigareti, au kudanganya tena.’ Aina hiyo ya msongo humsaidia mtu adhibiti mwili wake, akiacha haraka maovu yoyote au uraibu wowote. Pia husaidia mtu asitawishe matunda ya roho.”—Wagalatia 5:22, 23.

  • Mioyo Migumu Ianzapo Kuitikia
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Oktoba 15
    • Jerzy, aliyebatizwa Juni asimulia: “Ijapokuwa nilikuwa nimesikia kweli ya Biblia miaka kadhaa iliyopita, nilikuwa na moyo mgumu kwelikweli. Upunjaji, talaka kutoka kwa mke wangu wa kwanza, uhusiano wa haramu na Krystyna, mtoto nje ya kifungo cha ndoa, na kurudi-rudi gerezani—ndivyo yalivyokuwa maisha yangu.” Alipoona jinsi wahalifu wengine sugu walivyokuja kuwa Mashahidi wakiwa gerezani, alianza kujiuliza mwenyewe, ‘Je, siwezi kuwa mtu mzuri pia?’ Aliomba funzo la Biblia naye akaanza kuja kwenye mikutano. Hata hivyo, wakati wa badiliko la maana kwake ulikuja alipojua kutoka kwa mwendesha mashtaka wa umma kwamba Krystyna alikuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova miaka mitatu mapema. “Nilishangaa sana!” asema Jerzy. “Nilifikiri, ‘Vipi mimi? Nafanya nini?’ Nilitambua kwamba ili nikubaliwe na Yehova, ilinibidi nirekebishe maisha yangu.” Tokeo likawa kwamba, muungano wenye furaha ulitokea gerezani—pamoja na Krystyna na binti yao mwenye umri wa miaka 11, Marzena. Kabla ya muda mrefu, walihalalisha ndoa yao. Ingawa bado yumo gerezani, anamokuwa na nyakati za heri na shari, majuzi Jerzy alijifunza lugha ya ishara naye anaweza kuwasaidia wafungwa viziwi.

      Mirosław alikuwa tayari amehusika na mambo ya uhalifu alipokuwa katika shule ya msingi. Alipendezwa sana na vile rafiki zake walivyokuwa wakifanya, na upesi akaanza kufanya vivyo hivyo. Alinyang’anya na kupiga watu wengi. Kisha akajipata gerezani. “Nilipojipata gerezani, nilimgeukia kasisi ili nipate msaada,” akiri Mirosław. “Lakini nilitamaushwa sana. Basi nikaamua kwamba ningejiua kwa kunywa sumu.” Siku hiyo hiyo aliyopanga kujiua, alihamishwa hadi kwenye seli nyingine. Hapo alipata nakala ya Mnara wa Mlinzi iliyoongea kuhusu kusudi la uhai. “Habari sahili iliyo wazi ilithibitika kuwa tu kile nilichohitaji,” yeye aongezea. “Sasa nilitaka kuishi! Kwa hiyo, nilisali kwa Yehova na kuwaomba Mashahidi funzo la Biblia.” Alifanya maendeleo ya haraka katika funzo lake la Biblia naye akabatizwa katika 1991. Sasa yeye hutumikia akiwa painia-msaidizi gerezani, akiwa na pendeleo la kuhubiri seli hadi seli.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki