Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Yehova, Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
    • Yehova, Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”

      “Wewe, Bwana [“Yehova,” “NW”], U mwema, umekuwa tayari kusamehe.—ZABURI 86:5.

      1. Mfalme Daudi aliuchukua mzigo gani wenye kulemea, naye alipataje faraja kwa ajili ya moyo wake wenye kutaabika?

      MFALME DAUDI wa Israeli la kale alijua jinsi ambavyo mzigo wenye kulemea wa dhamiri yenye hatia ungeweza kuwa mzito. Aliandika hivi: “Dhambi zangu zimenifunikiza kichwa, kama mzigo mzito zimenilemea mno. Nimedhoofika na kuchubuka sana, nimeugua kwa fadhaa ya moyo wangu.” (Zaburi 38:4, 8) Hata hivyo, Daudi alipata faraja kwa ajili ya moyo wake wenye kutaabika. Alijua kwamba ingawa Yehova huchukia dhambi, hamchukii mtenda-dhambi—ikiwa kwa kweli yeye ni mwenye kutubu na akataa mwendo wake wenye dhambi. (Zaburi 32:5; 103:3) Akiwa mwenye imani kamili katika utayari wa Yehova wa kuwaonyesha rehema wenye kutubu, Daudi alisema hivi: “Wewe, Bwana [“Yehova,” NW], U mwema, umekuwa tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.

      2, 3. (a) Tufanyapo dhambi tokeo huenda likawa tuchukue mzigo gani wenye kulemea, na kwa nini jambo hilo lafaa? (b) Kuna hatari gani katika “kumezwa” na hisia ya hatia? (c) Biblia hutupatia uhakikisho gani juu ya utayari wa Yehova wa kusamehe?

      2 Tufanyapo dhambi, huenda tokeo likawa kwamba sisi pia tutachukua mzigo wenye kulemea na wenye kuponda wa dhamiri yenye kuumiza. Hisia hiyo ya majuto ni jambo la kawaida, hata lenye manufaa. Yaweza kutusukuma kuchukua hatua chanya za kusahihisha makosa yetu. Ingawa hivyo, hisia ya hatia huwashinda nguvu Wakristo fulani. Huenda moyo wao wenye kujihukumia hatia ukasisitiza kwamba Mungu hatawasamehe kikamili, haidhuru wao ni wenye kutubu jinsi gani. “Inakuwa hisia mbaya sana ufikiriapo kwamba huenda ikawa Yehova hakupendi tena,” akasema dada mmoja, akikumbuka kosa alilokuwa amefanya. Hata baada ya kutubu na kupokea shauri lenye kusaidia kutoka kwa wazee wa kutaniko, aliendelea kuhisi asiyestahili msamaha wa Mungu. Aeleza hivi: “Namwomba Yehova msamaha wake kila siku.” ‘Tukimezwa’ na hisia ya hatia, huenda Shetani akajaribu kutufanya tukate tamaa, tuhisi kwamba hatustahili kumtumikia Yehova.—2 Wakorintho 2:5-7, 11.

      3 Lakini Yehova haoni mambo jinsi hiyo hata kidogo! Neno lake hutuhakikishia kwamba tudhihirishapo toba ya kweli na ya kuhisiwa moyoni, Yehova anapenda, hata yuko tayari, kusamehe. (Mithali 28:13) Kwa hiyo ikiwa msamaha wa Mungu umeonekana kuwa jambo usiloweza kulifikia kamwe, labda lihitajiwalo ni uelewevu bora zaidi juu ya kwa nini yeye husamehe na jinsi ambavyo yeye hufanya hivyo.

      Kwa Nini Yehova Yuko “Tayari Kusamehe”?

      4. Yehova hukumbuka nini juu ya hali yetu, na hilo huathirije jinsi atutendeavyo?

      4 Twasoma hivi: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao.” Kwa nini Yehova ana mwelekeo wa kuonyesha rehema? Mstari wenye kufuata wajibu hivi: “Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:12-14) Ndiyo, Yehova hasahau kwamba sisi tu viumbe wa mavumbi, wenye kasoro, au wenye udhaifu mbalimbali, zisababishwazo na kutokamilika. Huo usemi kwamba ajua “umbo letu” hutukumbusha kwamba Biblia humfananisha Yehova na mfinyanzi na kutufananisha na vyombo ambavyo yeye hufanyiza.a (Yeremia 18:2-6) Mfinyanzi hushika vyombo vyake vya udongo kwa imara lakini kwa uangalifu, akiwa mwenye kujali daima hali ya vyombo hivyo. Hivyo, pia, Yehova, Mfinyanzi aliye Mkuu Zaidi, hushughulika nasi kulingana na udhaifu wa hali yetu yenye dhambi.—Linganisha 2 Wakorintho 4:7.

      5. Kitabu cha Waroma hufafanuaje mshiko wenye nguvu wa dhambi juu ya hali yetu yenye dhambi?

      5 Yehova aelewa jinsi dhambi ilivyo na nguvu nyingi. Maandiko hufafanua dhambi kuwa kani yenye nguvu ambayo imemweka mwanadamu katika mshiko wake wa kufisha. Mshiko wa dhambi ni wenye nguvu jinsi gani hasa? Katika kitabu cha Waroma, mtume Paulo mwenye kupuliziwa afafanua jambo hilo hivi kwa maneno yaliyo dhahiri: Tuko “chini ya dhambi,” kama vile askari-jeshi walivyo chini ya kamanda wao (Waroma 3:9); ‘imetawala’ wanadamu sawa na mfalme (Waroma 5:21); ‘yakaa’ katika sisi (Waroma 7:17, 20); “sheria” yake hufanya kazi ndani yetu daima, kwa kweli ikijaribu kuongoza mwendo wetu. (Waroma 7:23, 25) Tuna pigano gumu kama nini la kukinza mshiko wenye nguvu wa dhambi juu ya hali yetu yenye dhambi!—Waroma 7:21, 24.

      6. Yehova huwaonaje wale watafutao rehema wakiwa na moyo wenye majuto?

      6 Kwa sababu hiyo, Mungu wetu mwenye rehema ajua kwamba utii mkamilifu hauwezekani kwetu, haidhuru mioyo yetu huenda ikataka kumtii kwa kadiri gani. (1 Wafalme 8:46) Yeye hutuhakikishia kwa upendo kwamba tutafutapo rehema zake za kibaba tukiwa na moyo wenye majuto, atatusamehe. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:17) Yehova hatakataa kamwe, wala kugeuzia mbali, moyo uliovunjika na kupondeka kwa sababu ya mzigo wenye kulemea wa hatia. Jambo hilo lafafanua vizuri kama nini utayari wa Yehova wa kusamehe!

      7. Kwa nini hatuwezi kuchukua vivi hivi rehema ya Mungu?

      7 Ingawa hivyo, je, hilo lamaanisha kwamba twaweza kuchukua vivi hivi rehema ya Mungu, tukitumia hali yetu yenye dhambi kuwa udhuru wa kufanya dhambi? La hasha! Yehova haongozwi na hisia za moyoni tu. Rehema yake ina mipaka. Hatawasamehe kamwe wale ambao kwa moyo mgumu huzoea kufanya dhambi kwa kusudi bila toba, wakiwa na nia ya kuwadhuru wengine. (Waebrania 10:26-31) Kwa upande ule mwingine, aonapo moyo “uliovunjika na kupondeka” yeye huwa “tayari kusamehe.” (Mithali 17:3) Acheni tufikirie lugha yenye kueleza mambo wazi ambayo ilitumiwa katika Biblia ili kufafanua ukamili wa msamaha wa kimungu.

      Yehova Husamehe Kikamili Jinsi Gani?

      8. Kwa kweli, Yehova hufanya nini atusamehepo dhambi zetu, na hilo lapaswa kuwa na matokeo gani juu yetu?

      8 Mfalme Daudi mwenye kutubu alisema hivi: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. Nalisema, Nitayakiri maasi yangu kwa BWANA, nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” (Zaburi 32:5, italiki ni zetu.) Usemi “ukanisamehe” ni tafsiri ya neno la Kiebrania ambalo kimsingi lamaanisha “inua,” “beba, chukua.” Matumizi yake hapa humaanisha ‘kuondolea mbali hatia, dhambi, mkiuko-sheria.’ Kwa hiyo Yehova aliziinua dhambi za Daudi na kuzichukulia mbali, kwa kusema kitamathali. (Linganisha Mambo ya Walawi 16:20-22.) Hapana shaka hilo lilipunguza hisia za hatia ambazo Daudi alikuwa akichukua. (Linganisha Zaburi 32:3.) Sisi pia twaweza kuwa na uhakika kamili katika Mungu ambaye husamehe dhambi za wale watafutao msamaha wake kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Mathayo 20:28; linganisha Isaya 53:12.) Wale ambao dhambi zao Yehova huziinua na kuzichukulia mbali hawahitaji kuendelea kuchukua mzigo wenye kulemea wa hisia za hatia kwa sababu ya dhambi za wakati uliopita.

      9. Maneno haya ya Yesu: “Utusamehe madeni yetu,” yamaanisha nini?

      9 Yesu alitumia uhusiano wa wadaiwa na wadeni ili kutoa kielezi cha jinsi ambavyo Yehova husamehe. Kwa kielelezo, Yesu alituhimiza tusali hivi: “Utusamehe madeni yetu.” (Mathayo 6:12) Hivyo Yesu alifananisha “dhambi” na “madeni.” (Luka 11:4) Tufanyapo dhambi, twapata kuwa “wadeni” kwa Yehova. Kitenzi cha Kigiriki kitafsiriwacho “kusamehe” chaweza kumaanisha “kuachilia, kuacha, deni, kwa kutolidai.” Katika maana fulani, Yehova asamehepo, yeye hufuta deni ambalo kama sivyo lingewiwa dhidi ya hesabu yetu. Hivyo watenda-dhambi wenye kutubu waweza kupokea faraja. Yehova hatadai kamwe malipo ya deni ambalo amelifuta!—Zaburi 32:1, 2; linganisha Mathayo 18:23-35.

      10, 11. (a) Ni tamathali gani ya usemi ionyeshwayo na fungu la maneno ‘-pata kufutwa,’ lipatikanalo kwenye Matendo 3:19? (b) Ukamili wa msamaha wa Yehova watolewaje kielezi?

      10 Kwenye Matendo 3:19, Biblia hutumia tamathali nyingine ya usemi iliyo dhahiri ili kufafanua msamaha wa Mungu: “Tubuni na mgeuke kabisa ili mpate kufutiwa dhambi zenu.” Fungu la maneno ‘-pata kufutwa’ ni tafsiri ya kitenzi cha Kigiriki ambacho, kitumiwapo kitamathali, chaweza kumaanisha “kuondosha, kufutilia mbali, kufuta, au kuharibu.” Kulingana na wasomi fulani, dhana ambayo imeonyeshwa ni ile ya kufuta mwandiko. Hilo liliwezekanaje? Wino uliotumiwa kwa kawaida nyakati za kale ulitengenezwa kwa mchanganyo uliotia ndani kaboni, gundi, na maji. Upesi baada ya kuandika kwa wino huo, mtu angeweza kuchukua sponji iliyolowa maji na kufutilia mbali hayo maandishi.

      11 Humo mna ufafanuzi mzuri wa ukamili wa msamaha wa Yehova. Asamehepo dhambi zetu, ni kana kwamba achukua sponji na kuzifutilia mbali. Hatuhitaji kuhofu kwamba dhambi hizo zitaathiri hukumu yake dhidi yetu wakati ujao, kwa maana Biblia hufunua jambo fulani jingine lenye kutokeza juu ya rehema ya Yehova: Asamehepo, yeye husahau!

      “Dhambi Yao Sitaikumbuka Tena”

      12. Biblia isemapo kwamba Yehova husahau dhambi zetu, je, hilo lamaanisha kwamba hawezi kuzikumbuka, na kwa nini wajibu hivyo?

      12 Kupitia nabii Yeremia, Yehova aliahidi hivi kuhusu walio ndani ya agano jipya: “Nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34) Je, hilo lamaanisha kwamba Yehova asamehepo hawezi kukumbuka dhambi tena kamwe? Haiwezekani kuwa hivyo. Biblia hutuambia juu ya dhambi za watu wengi mmoja-mmoja ambao Yehova aliwasamehe, kutia na Daudi. (2 Samweli 11:1-17; 12:1-13) Kwa wazi Yehova bado ajua makosa waliyofanya, na kwa hiyo sisi twapaswa kujua pia. Rekodi ya dhambi zao, na vilevile ile ya kutubu na kusamehewa kwao na Mungu, imehifadhiwa kwa manufaa yetu. (Waroma 15:4) Hivyo basi, Biblia humaanisha nini isemapo kwamba Yehova ‘hakumbuki’ dhambi za wale ambao yeye huwasamehe?

      13. (a) Maana ya kitenzi cha Kiebrania kitafsiriwacho ‘nitakumbuka’ yatia ndani nini? (b) Yehova anatuhakikishia nini asemapo, “Dhambi yao sitaikumbuka tena”?

      13 Kitenzi cha Kiebrania kitafsiriwacho ‘nitakumbuka’ chadokeza zaidi ya kukumbuka tu wakati uliopita. Kulingana na kichapo Theological Wordbook of the Old Testament, kitenzi hicho hutia ndani “lile dokezo la ziada la kuchukua hatua ifaayo.” Kwa hiyo katika maana hiyo, “[ku]kumbuka” dhambi huhusisha kuchukua hatua dhidi ya watenda-dhambi. Nabii Hosea aliposema kuwahusu Waisraeli wakaidi kwamba, “[Yehova] ataukumbuka uovu wao,” huyo nabii alimaanisha kwamba Yehova angechukua hatua dhidi yao kwa sababu ya kukosa kwao toba. Hivyo, sehemu iliyobaki ya huo mstari yaongeza hivi: “Atazilipiza dhambi zao.” (Hosea 9:9) Kwa upande ule mwingine, Yehova asemapo kwamba, “Dhambi yao sitaikumbuka tena,” anatuhakikishia kwamba mara asamehepo mtenda-dhambi mwenye kutubu, hatamchukulia hatua kwa sababu ya dhambi hizo wakati fulani ujao. (Ezekieli 18:21, 22) Hivyo yeye husahau katika maana ya kwamba hatukumbushi dhambi zetu kwa kurudia-rudia ili kutushtaki au ili kutuadhibu tena na tena. Kwa njia hiyo Yehova hutuwekea kielelezo bora cha kuiga katika kushughulika kwetu na wengine. Kutopatana kutokeapo, ni vema zaidi kutofuliza kukumbuka makosa ya wakati uliopita ambayo hapo awali ulikubali kusamehe.

      Vipi juu ya Matokeo?

      14. Kwa nini msamaha haumaanishi kwamba mtenda-dhambi mwenye kutubu ameondolewa matokeo yote ya mwendo wake wenye kosa?

      14 Je, utayari wa Yehova wa kusamehe humaanisha kwamba mtenda-dhambi mwenye kutubu ameondolewa matokeo yote ya mwendo wake wenye kosa? Sivyo hata kidogo. Hatuwezi kufanya dhambi bila kuadhibiwa. Paulo aliandika hivi: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Huenda tukakabili matokeo fulani ya tendo letu au matatizo, lakini baada ya kusamehe, Yehova hasababishi tupatwe na janga. Taabu zitokeapo, Mkristo hapaswi kuhisi, ‘Labda Yehova ananiadhibu kwa sababu ya dhambi za wakati uliopita.’ (Linganisha Yakobo 1:13.) Kwa upande mwingine, Yehova hatuepushi na matokeo yote ya matendo yetu yenye makosa. Talaka, mimba zisizotakiwa, maradhi ya kupitishwa kingono, kutotumainiwa au kutostahiwa na wengine—huenda hayo yote yakawa matokeo yenye kuhuzunisha ya dhambi, na Yehova hatatuhami dhidi ya mambo hayo. Kumbuka kwamba hata ingawa alimsamehe Daudi kwa sababu ya dhambi zake kuhusiana na Bath-sheba na Uria, Yehova hakumhami Daudi dhidi ya matokeo yenye kuleta msiba yaliyofuata.—2 Samweli 12:9-14.

      15, 16. Sheria iliyorekodiwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ilimnufaishaje mhasiriwa na vilevile mkosaji?

      15 Huenda dhambi zetu zikawa na matokeo mengine pia. Kwa kielelezo, fikiria simulizi katika Mambo ya Walawi sura ya 6. Hapa Sheria ya Kimusa yashughulikia hali ambamo mtu afanya kosa zito kwa kukamata bidhaa za Mwisraeli mwenzake kupitia upokonyaji, unyang’anyi, au upunjaji. Kisha mtenda-dhambi akana kwamba hana hatia, hata kuwa mwenye kuthubutu sana hivi kwamba aapa isivyo kweli. Hali hii ni kisa kinachohusisha bishano lisilo na ithibati kutoka pande zote mbili. Hata hivyo, baadaye mkosaji awa na dhamiri iliyojaa huzuni naye atubu dhambi yake. Ili kupata msamaha wa Mungu, yambidi afanye mambo matatu zaidi: arudishe alichokuwa amechukua, amlipe mhasiriwa faini ya asilimia 20, na atoe mwana-kondoo akiwa toleo la hatia. Kisha, sheria yasema hivi: “Huyo kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele za BWANA, naye atasamehewa.”—Mambo ya Walawi 6:1-7; linganisha Mathayo 5:23, 24.

      16 Sheria hiyo ilikuwa uandalizi wenye rehema kutoka kwa Mungu. Ilimnufaisha mhasiriwa, ambaye mali yake ilirudishwa na ambaye hapana shaka alihisi kitulizo kikubwa mkosaji alipokubali kosa lake hatimaye. Wakati uleule, sheria ilimnufaisha mtu ambaye dhamiri yake mwishowe ilimsukuma kukubali hatia yake na kusahihisha kosa lake. Kwa kweli, ikiwa angalikataa kufanya hivyo, asingepata msamaha kutoka kwa Mungu.

      17. Yehova hutarajia tufanye nini, wakati ambapo wengine wameumizwa na dhambi zetu?

      17 Ijapokuwa hatuko chini ya Sheria ya Kimusa, jambo hilo hutupa ufahamu wenye kina na wenye thamani juu ya akili ya Yehova, kutia na maoni yake juu ya msamaha. (Wakolosai 2:13, 14) Wakati ambapo wengine wameumizwa au kuhasiriwa na dhambi zetu, Yehova hupendezwa tufanyapo tuwezalo ili ‘kusahihisha kosa.’ (2 Wakorintho 7:11) Hilo huhusisha kukiri dhambi yetu, tukikubali hatia yetu, na hata kumwomba radhi mhasiriwa. Kisha twaweza kumwomba Yehova kwa msingi wa dhabihu ya Yesu na kupata kitulizo cha dhamiri safi na uhakikisho wa kwamba tumesamehewa na Mungu.—Waebrania 10:21, 22.

      18. Huenda msamaha wa Yehova ukaandamana na nidhamu gani?

      18 Kama mzazi yeyote mwenye upendo, huenda Yehova akatoa msamaha pamoja na kipimo fulani cha nidhamu. (Mithali 3:11, 12) Huenda Mkristo mwenye kutubu akalazimika kuacha pendeleo la kutumikia akiwa mzee, mtumishi wa huduma, au painia. Huenda akaumia kupoteza kwa kipindi fulani cha wakati mapendeleo ambayo yalikuwa yenye thamani kwake. Hata hivyo, nidhamu hiyo haimaanishi kwamba amepoteza upendeleo wa Yehova au kwamba Yehova amemnyima msamaha. Kwa kuongezea, lazima tukumbuke kwamba nidhamu kutoka kwa Yehova ni ithibati ya upendo wake kwetu. Kuipokea na kuitumia hutunufaisha sana na kwaweza kuongoza kwenye uhai udumuo milele.—Waebrania 12:5-11.

      19, 20. (a) Ikiwa umefanya makosa, kwa nini hupaswi kuhisi kwamba huwezi kupata rehema ya Yehova? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala yenye kufuata?

      19 Inaburudisha kama nini kujua kwamba twatumikia Mungu aliye “tayari kusamehe”! Yehova huona zaidi ya dhambi zetu na makosa yetu. (Zaburi 130:3, 4) Ajua kilicho mioyoni mwetu. Ukihisi kwamba moyo wako umevunjika na kupondeka kwa sababu ya makosa ya wakati uliopita, usikate kauli kwamba huwezi kupata rehema ya Yehova. Yajapokuwa makosa ambayo huenda ukawa umefanya, ikiwa umetubu kikweli, ukachukua hatua za kusahihisha kosa, na kusali kwa bidii ili kupata msamaha wa Yehova kwa msingi wa damu ya Yesu iliyomwagwa, waweza kuwa na uhakika kamili kwamba maneno haya ya 1 Yohana 1:9 yatumika kukuhusu: “Ikiwa twaungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na mwadilifu hata kutusamehe dhambi zetu na kutusafisha ukosefu wote wa uadilifu.”

      20 Biblia yatutia moyo tuige msamaha wa Yehova katika shughuli zetu kati ya mmoja na mwenzake. Hata hivyo, wengine wafanyapo dhambi dhidi yetu twaweza kutarajiwa kusamehe na kusahau kwa kadiri gani? Jambo hilo litazungumziwa katika makala yenye kufuata.

  • ‘Endeleeni Kusameheana kwa Hiari’
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
    • ‘Endeleeni Kusameheana kwa Hiari’

      “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari.”—WAKOLOSAI 3:13.

      1. (a) Ni kwa nini huenda ikawa Petro alikuwa amefikiri kwamba alikuwa mkarimu alipodokeza kwamba tuwasamehe wengine “mpaka mara saba”? (b) Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba twapaswa kusamehe “mpaka mara sabini na saba”?

      “BWANA, ni mara ngapi ndugu yangu atafanya dhambi dhidi yangu nami nimsamehe? Mpaka mara saba?” (Mathayo 18:21) Huenda ikawa Petro alifikiri alikuwa mwenye ukarimu sana katika dokezo lake. Wakati huo, pokeo la kirabi lilisema kwamba mtu hakupaswa kutoa msamaha zaidi ya mara tatu kwa kosa lilelile.a Kisha wazia mshangao wa Petro, Yesu alipomjibu hivi: “Nakuambia, si, Mpaka mara saba, bali, Mpaka mara sabini na saba”! (Mathayo 18:22) Huko kurudia nambari saba kulikuwa sawa na kusema “kwa wakati usio dhahiri.” Kwa maoni ya Yesu, kwa kweli hakuna mipaka kwa mara ambazo Mkristo apaswa kuwasamehe wengine.

      2, 3. (a) Ni katika hali gani ambamo huenda ikaonekana vigumu kusamehe wengine? (b) Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba kuwasamehe wengine ni kwa manufaa yetu?

      2 Hata hivyo, si rahisi sikuzote kulitumia shauri hilo. Ni nani kati yetu hajahisi kichomi cha umivu lisilo la haki? Labda mtu fulani uliyemtumaini alifunua siri. (Mithali 11:13) Huenda maneno yasiyofikiriwa ya rafiki wa karibu yakawa ‘yalikuchoma kama upanga.’ (Mithali 12:18) Huenda ikawa kutendwa vibaya na mtu fulani uliyempenda au kumtumaini kulisababisha majeraha makubwa. Mambo hayo yatokeapo, huenda itikio letu kiasili likawa kukasirika. Huenda tukawa na mwelekeo wa kuacha kuzungumza na mkosaji, tukimwepa kabisa ikiwezekana. Huenda ikaonekana kwamba, kumsamehe kungemruhusu mkosaji atuumize bila kuadhibiwa. Lakini, tukisitawisha uchungu wa moyo, twaishia kujiumiza.

      3 Kwa hiyo Yesu atufundisha tusamehe—“mpaka mara sabini na saba.” Hakika mafundisho yake hayatatudhuru kamwe. Kila alichofundisha kilitokana na Yehova, ‘Yule atufundishaye ili tupate faida.’ (Isaya 48:17; Yohana 7:16, 17) Kiakili, ni lazima liwe jambo lenye manufaa sana kwetu kusamehe wengine. Kabla ya kuzungumzia kwa nini twapaswa kusamehe na jinsi tuwezavyo kufanya hivyo, huenda ikasaidia kwanza kubainisha msamaha ni nini na sio nini. Huenda dhana yetu juu ya msamaha ikaathiri uwezo wetu wa kusamehe tukosewapo na wengine.

      4. Kusamehe wengine hakumaanishi nini, lakini msamaha hufasiliwaje?

      4 Kuwasamehe wengine kwa sababu ya kutukosea kibinafsi hakumaanishi kwamba tunaruhusu au kupunguza yale waliyofanya; wala hakumaanishi kuwaruhusu wengine watutumie isivyo haki. Kwa vyovyote, Yehova atusamehepo, hakika hapunguzi uzito wa dhambi zetu, naye hataruhusu kamwe wanadamu wenye dhambi wakanyage-kanyage rehema yake. (Waebrania 10:29) Kulingana na kichapo Insight on the Scriptures, msamaha hufasiliwa kuwa “tendo la kumsamehe mkosaji; kuacha kuhisi uchungu kumwelekea kwa sababu ya kosa lake na kuacha madai yote ya malipo.” (Buku la 1, ukurasa wa 861)b Biblia hutuandalia sababu nzuri za kuwasamehe wengine.

      Kwa Nini Tuwasamehe Wengine?

      5. Ni sababu gani ya maana ya kusamehe wengine ambayo imeonyeshwa kwenye Waefeso 5:1?

      5 Sababu ya maana ya kuwasamehe wengine yaonyeshwa kwenye Waefeso 5:1: “Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” Twapaswa kuwa “waigaji wa Mungu” katika jambo gani? Maneno “kwa hiyo” yaunganisha huo usemi na mstari unaotangulia, ambao wasema hivi: “Iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.” (Waefeso 4:32) Ndiyo, kwa habari ya msamaha, twapaswa kuwa waigaji wa Mungu. Kama vile mvulana mdogo hujaribu kuwa tu kama baba yake, sisi, tukiwa watoto ambao Yehova apenda sana, yatupasa tutake kuwa kama Baba yetu wa kimbingu mwenye kusamehe. Lazima Yehova awe apendezwa kama nini kutazama chini kutoka mbinguni na kuona watoto wake wa kidunia wakijaribu kuwa kama yeye kwa kusameheana!—Luka 6:35, 36; linganisha Mathayo 5:44-48.

      6. Ni katika njia gani kuna tofauti kubwa kati ya msamaha wa Yehova na msamaha wetu?

      6 Ni kweli, hatuwezi kamwe kusamehe kikamilifu kama vile Yehova hufanya. Lakini hiyo ndiyo sababu zaidi twapaswa kusameheana. Fikiria hili: Kuna tofauti kubwa kati ya msamaha wa Yehova na msamaha wetu. (Isaya 55:7-9) Tuwasamehepo wale ambao wamefanya dhambi dhidi yetu, mara nyingi sisi hufanya hivyo kwa kufahamu kwamba huenda siku moja tukahitaji watufanyie vivyo hivyo. Kwa habari ya wanadamu, sikuzote inakuwa hali ya watenda-dhambi kuwasamehe watenda-dhambi. Hata hivyo, kwa habari ya Yehova msamaha ni wa upande mmoja sikuzote. Yeye hutusamehe, lakini hatutahitaji kumsamehe kamwe. Ikiwa Yehova, ambaye hafanyi dhambi, aweza kutusamehe kwa upendo na kwa ukamili hivyo, je, haitupasi sisi wanadamu wenye dhambi kujaribu kusameheana?—Mathayo 6:12.

      7. Uhusiano wetu wenyewe na Yehova waweza kuathiriwaje vibaya, tukikataa kusamehe wengine wakati ambapo kuna msingi wa rehema?

      7 La maana hata zaidi, tukikataa kusamehe wengine wakati ambapo kuna msingi wa rehema, jambo hilo laweza kuathiri vibaya uhusiano wetu na Mungu. Yehova hatuombi tu tusameheane; yeye hutarajia tufanye hivyo. Kulingana na Maandiko, sehemu ya kichocheo chetu cha kuwa wenye kusamehe ni ili kwamba Yehova apate kutusamehe au kwa sababu ametusamehe. (Mathayo 6:14; Marko 11:25; Waefeso 4:32; 1 Yohana 4:11) Ikiwa basi, hatuko tayari kuwasamehe wengine wakati ambapo kuna sababu nzuri ya kufanya hivyo, je twaweza kwa hakika kutarajia msamaha huo kutoka kwa Yehova?—Mathayo 18:21-35.

      8. Kwa nini kuwa wenye kusamehe ni kwa manufaa yetu?

      8 Yehova huwafundisha watu wake “njia iliyo njema, iwapasayo kuiendea.” (1 Wafalme 8:36) Atuagizapo tusameheane, twaweza kuwa na uhakika kwamba apendezwa sana na manufaa yetu. Ikiwa na sababu nzuri Biblia hutuambia “[tuiachie] nafasi hasira.” (Waroma 12:19) Uchungu wa moyo ni mzigo wenye kulemea ulio mzito kuuchukua maishani. Tukiuweka moyoni, huo mzigo hula mawazo yetu kabisa, hutupokonya amani, na kukomesha shangwe yetu. Hasira ya muda mrefu, kama wivu, yaweza kudhuru afya yetu ya kimwili. (Mithali 14:30) Na tunapopatwa na hayo yote, huenda mkosaji akawa hajui kabisa msukosuko wetu! Muumba wetu mwenye upendo ajua kwamba twahitaji kusamehe wengine waziwazi si kwa faida yao tu bali pia kwa faida yetu. Kwa kweli, shauri la Kibiblia la kusamehe ndilo, ‘njia iliyo njema kuiendea.’

      “Endeleeni Kuchukuliana Mtu na Mwenzake”

      9, 10. (a) Ni hali za aina gani ambazo si lazima zitake msamaha rasmi? (b) Ni nini lidokezwalo na usemi “endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake”?

      9 Huenda majeraha ya kimwili yakawa mikwaruzo midogo hadi kufikia majeraha makubwa, na yote hayataki kadiri ileile ya uangalifu. Hisia zilizojeruhiwa ziko vivyo hivyo—majeraha fulani ni makubwa kuliko mengine. Je, kwa kweli twahitaji kufanya kila kosa dogo litupatalo katika mahusiano yetu na wengine liwe jambo kubwa? Maudhiko madogo-madogo, madharau, na udhia mbalimbali ni sehemu ya maisha na si lazima yatake msamaha rasmi. Ikiwa tuna sifa ya kuwa mmoja ambaye huepuka kabisa wengine kwa sababu ya kila tamausho dogo na ambaye wakati huo asisitiza kwamba waombe radhi kabla ya kuwatendea tena katika njia ya hisani, huenda tukawalazimisha wajiendeshe kwa tahadhari nyingi washirikianapo nasi—au tukawalazimisha kutoshirikiana kwa ukaribu sana nasi!

      10 Badala yake, ni afadhali zaidi “kuwa na sifa ya kuwa wenye kukubali sababu.” (Wafilipi 4:5, Phillips) Tutumikiapo bega kwa bega tukiwa viumbe wasiokamilika, twaweza kiakili kutarajia kwamba huenda ndugu zetu wakatuudhi mara kwa mara, na huenda tukawafanyia vivyo hivyo. Andiko la Wakolosai 3:13 latushauri hivi: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake.” Usemi huo wadokeza kuwa na subira kuelekea wengine, tukivumilia tabia yao tusiyopendezwa nayo au vitabia ambavyo huenda tukavipata kuwa vyenye kuudhi. Subira na kujizuia huko kwaweza kutusaidia kukabiliana na makosa madogo-madogo tupatayo katika kushughulika kwetu na wengine—bila kuvuruga amani ya kutaniko.—1 Wakorintho 16:14.

      Majeraha Yawapo Makubwa Zaidi

      11. Wengine wafanyapo dhambi dhidi yetu, ni nini liwezalo kutusaidia tuwasamehe?

      11 Hata hivyo, namna gani ikiwa wengine wafanya dhambi dhidi yetu, wakisababisha jeraha lenye kuonekana? Ikiwa hiyo dhambi si zito mno, huenda tukapata ugumu kidogo wa kutumia shauri la Biblia la ‘kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.’ (Waefeso 4:32) Utayari kama huo wa kusamehe wapatana na maneno haya ya Petro yaliyopuliziwa: “Juu ya mambo yote, iweni na upendo wenye juhudi nyingi nyinyi kwa nyinyi, kwa sababu upendo hufunika wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8) Kukumbuka kwamba sisi pia ni watenda-dhambi hutusaidia kuachilia makosa ya wengine. Tusamehepo hivyo, twaachilia uchungu wa moyo badala ya kuusitawisha. Tokeo ni kwamba, huenda ikawa uhusiano wetu na mkosaji hautapatwa na madhara yoyote ya kudumu, nasi pia twasaidia kuhifadhi amani yenye thamani ya kutaniko. (Waroma 14:19) Halafu, huenda kumbukumbu la jambo alilofanya likafifia.

      12. (a) Huenda tukahitaji kuchukua hatua gani ya kwanza ili kumsamehe mtu fulani ambaye ametuumiza sana? (b) Maneno yaliyo kwenye Waefeso 4:26 huonyeshaje kwamba twapaswa kusuluhisha mambo haraka?

      12 Ingawa hivyo, namna gani mtu fulani akifanya dhambi dhidi yetu katika njia iliyo nzito zaidi, wakituumiza sana? Kwa kielelezo, huenda rafiki mwenye kutumainika akawa alifunua mambo fulani ya kibinafsi kabisa ambayo ulimwambia kisiri. Wahisi kuwa umeumizwa, kuaibishwa, na kusalitiwa sana. Umejaribu kuliondoa akilini, lakini jambo hilo haliondoki. Katika kisa kama hicho, huenda ukalazimika kuchukua hatua fulani ya kwanza ili kusuluhisha hilo tatizo, labda kwa kusema na mkosaji. Ni jambo la hekima kufanya hivyo kabla ya hilo jambo kupata nafasi ya kusitawi. Paulo alituhimiza kwa bidii hivi: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi [yaani, kwa kuweka au kutenda kulingana na hasira yetu]; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Shauri la Paulo ni lenye kani nyingi hata zaidi tufikiriapo uhakika wa kwamba miongoni mwa Wayahudi, mshuko-jua ulitia alama kumalizika kwa siku moja na kuanza kwa siku mpya. Kwa sababu hiyo, shauri ni: Suluhisheni hilo jambo upesi!—Mathayo 5:23, 24.

      13. Tumfikiapo mtu fulani aliyetukosea, lengo letu lapaswa liwe nini, na ni madokezo gani yawezayo kutusaidia tulifikie?

      13 Wapaswa kumfikiaje mkosaji? “[Tafuta] sana amani na kuifuatia,” lasema andiko la 1 Petro 3:11. Basi, lengo lako si kuonyesha hasira bali ni kufanya amani na ndugu yako. Ili kulifikia lengo hilo, ni afadhali kuepuka maneno na ishara za mwili zenye ukali; huenda hizo zikatokeza itikio hilohilo kutoka kwa yule mtu mwingine. (Mithali 15:18; 29:11) Kwa kuongezea, epuka taarifa zenye kutiwa chumvi kama, “Sikuzote wewe . . . !” au, “Wewe kamwe . . . !” Huenda taarifa hizo zenye kutiwa chumvi zikamfanya ajitetee tu. Badala yake, acha toni ya sauti yako na sura ya uso wako iwasilishe kwamba wataka kutatua jambo fulani ambalo limekuumiza sana. Uwe mahususi katika kueleza jinsi uhisivyo juu ya lililotukia. Mpe mtu yule mwingine nafasi ya kueleza matendo yake. Sikiliza lile ambalo ataka kusema. (Yakobo 1:19) Kufanya hivyo kutakuwa na faida gani? Andiko la Mithali 19:11 laeleza hivi: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” Huenda kuelewa hisia za yule mtu mwingine na kuelewa sababu za matendo yake kukaondoa mawazo na hisia hasi kumwelekea. Tuishughulikiapo hali tukiwa na mradi wa kufanya amani na kudumisha mtazamo huo, yaelekea sana kwamba kutokuelewana kokote kwaweza kusuluhishwa, kuomba radhi kufaako kukafanywa, na msamaha kutolewa.

      14. Tusamehepo wengine, twapaswa kusahau katika maana gani?

      14 Je, kusamehe wengine kwamaanisha kwamba lazima kwa kweli tusahau yaliyotukia? Kumbuka kielelezo cha Yehova mwenyewe kuhusu habari hiyo, kama kilivyozungumziwa katika makala iliyotangulia. Biblia isemapo kwamba Yehova husamehe dhambi zetu, hilo halimaanishi kwamba hawezi kuzikumbuka. (Isaya 43:25) Badala yake, yeye husahau katika maana ya kwamba mara atusamehepo, dhambi hizo haziathiri hukumu yake dhidi yetu katika wakati ujao fulani. (Ezekieli 33:14-16) Vivyo hivyo, kuwasamehe wanadamu wenzetu si lazima kumaanishe kwamba hatutaweza kukumbuka waliyofanya. Hata hivyo, twaweza kusahau katika maana ya kwamba dhambi hizo haziathiri hisia zetu dhidi ya mkosaji au hatutokezi jambo hilo tena wakati ujao. Hilo jambo likiwa limesuluhishwa hivyo, haingefaa kupiga porojo juu yake; wala halingekuwa jambo lenye upendo kumwepuka mkosaji kabisa, ukimtendea kana kwamba ametengwa. (Mithali 17:9) Ni kweli, huenda ikachukua wakati fulani kwa uhusiano wetu naye kupona, huenda tusionee shangwe ukaribu uleule wa hapo awali. Lakini bado twampenda akiwa ndugu yetu Mkristo na kufanya yote tuwezayo kudumisha mahusiano yenye amani.—Linganisha Luka 17:3.

      Lionekanapo Kuwa Jambo Lisilowezekana Kusamehe

      15, 16. (a) Je, Wakristo watakiwa kumsamehe mkosaji ambaye si mwenye kutubu? (b) Twaweza kutumiaje shauri la Biblia lipatikanalo kwenye Zaburi 37:8?

      15 Ingawa hivyo, namna gani ikiwa wengine wafanya dhambi dhidi yetu katika njia ambayo hutokeza majeraha makubwa zaidi, na bado hakuna ukiri wa dhambi, wala toba, wala kuomba radhi kwa upande wa mkosaji? (Mithali 28:13) Maandiko yaonyesha wazi kwamba Yehova hasamehei watenda-dhambi wagumu, wasiotubu. (Waebrania 6:4-6; 10:26, 27) Namna gani sisi? Kichapo Insight on the Scriptures chasema hivi: “Wakristo hawatakiwi kuwasamehe wale wazoeao dhambi ya kimakusudi yenye nia ya kuwadhuru wengine bila toba. Hao hupata kuwa adui za Mungu.” (Buku la 1, ukurasa wa 862) Hakuna Mkristo ambaye amekuwa mhasiriwa wa utendewaji usio wa haki kabisa, wenye kuchukiza, au mwovu apaswaye kuhisi alazimishwa kumsamehe, au kumwia radhi, mkosaji ambaye si mwenye kutubu.—Zaburi 139:21, 22.

      16 Kwa kueleweka, huenda wale ambao wamekuwa wahasiriwa wa utendewaji mabaya wakahisi umizo na hasira. Hata hivyo, kumbuka kwamba kuweka hasira na uchungu wa moyo kwaweza kuwa jambo lenye kutudhuru sana. Tukingojea ukiri au uombaji radhi ambao hauji kamwe, huenda tukafadhaika zaidi na zaidi tu. Huenda kushikilia huo ukosefu wa haki kukatufanya tufulize kuwa na hasira, kukiwa na matokeo yenye kuangamiza kabisa afya yetu ya kiroho, kihisia-moyo, na kimwili. Kwa kweli, twamruhusu yule aliyetuumiza aendelee kutuumiza. Kihekima Biblia hushauri hivi: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Kwa hiyo, Wakristo fulani wameona kwamba baada ya muda fulani waliweza kufanya uamuzi wa kusamehe katika maana ya kuacha kuweka uchungu wa moyo—bila kupunguza uzito wa kosa, lakini wakikataa kuliwa kabisa na hasira. Wakiacha jambo hilo kabisa mikononi mwa Mungu wa haki, walipata kitulizo kingi, wakaweza kuendelea kuishi bila hisia za uchungu wa moyo.—Zaburi 37:28.

      17. Ni uhakikisho gani wenye faraja uandaliwao na ahadi ya Yehova ambayo imerekodiwa kwenye Ufunuo 21:4?

      17 Jeraha liwapo kubwa sana, huenda tusifanikiwe kulifuta kabisa akilini mwetu, angalau si katika mfumo huu wa mambo. Lakini Yehova aahidi ulimwengu mpya ambamo “atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Lolote ambalo huenda tukalikumbuka wakati huo halitasababisha umizo kubwa, au umivu, ambalo huenda likalemea mioyo yetu sasa.—Isaya 65:17, 18.

      18. (a) Kwa nini kuna uhitaji wa kuwa wenye kusamehe katika shughuli zetu na ndugu na dada zetu? b) Wengine wafanyapo dhambi dhidi yetu, ni katika maana gani twaweza kusamehe na kusahau? (c) Jambo hilo latunufaishaje?

      18 Kwa sasa, lazima tuishi na kufanya kazi pamoja tukiwa ndugu na dada wasio wakamilifu, wanadamu wenye dhambi. Sisi sote hufanya makosa. Mara kwa mara, sisi hutamaushana na hata kuumizana. Yesu alijua vema kwamba tungehitaji kusamehe wengine, “si, Mpaka mara saba, bali, Mpaka mara sabini na saba”! (Mathayo 18:22) Ni kweli, hatuwezi kusamehe kabisa kama vile Yehova husamehe. Lakini, katika visa vilivyo vingi ndugu zetu wafanyapo dhambi dhidi yetu, twaweza kuwasamehe katika maana ya kuushinda uchungu wa moyo na twaweza kusahau katika maana ya kutoacha jambo hilo liathiri hisia zetu dhidi yao katika wakati ujao usio dhahiri. Tusamehepo na kusahau hivyo, twasaidia kuhifadhi si amani ya kutaniko tu bali pia amani yetu wenyewe ya akili na moyo. Zaidi ya yote, tutaonea shangwe amani ambayo ni Yehova tu, Mungu wetu mwenye upendo awezaye kuiandaa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki