Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mungu Anataka Uwe Rafiki Yake
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 1

      Mungu Anataka Uwe Rafiki Yake

      Mungu anataka uwe rafiki yake. Je, umewahi kuwazia kwamba waweza kuwa rafiki ya Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu wote? Abrahamu, aliyeishi zamani za kale, aliitwa rafiki ya Mungu. (Yakobo 2:23) Watu wengine pia wanaotajwa katika Biblia walikuwa rafiki za Mungu nao walibarikiwa sana. Leo, watu kutoka sehemu zote za dunia wamekuwa rafiki za Mungu. Wewe pia unaweza kuwa rafiki ya Mungu.

      Kuwa rafiki ya Mungu ni bora kuliko kuwa rafiki ya binadamu yeyote. Mungu hawavunji moyo kamwe rafiki zake wenye uaminifu-mshikamanifu. (Zaburi 18:25) Kuwa rafiki ya Mungu ni bora kuliko kuwa na mali. Tajiri anapokufa, fedha zake huchukuliwa na watu wengine. Hata hivyo, wale wanaofurahia urafiki pamoja na Mungu wana kitu fulani chenye thamani ambacho hakuna mtu awezaye kuwanyang’anya.—Mathayo 6:19.

      Huenda watu fulani wakajaribu kukuzuia usijifunze juu ya Mungu. Hata huenda baadhi ya rafiki zako na familia yako wakajaribu kukuzuia. (Mathayo 10:36, 37) Watu wengine wakikucheka au kukutisha, jiulize hivi, ‘Je, mimi nataka kumpendeza nani—binadamu au Mungu?’ Fikiria jambo hili: Ikiwa mtu fulani angekuambia uache kula chakula, je, ungemtii? La, hasha! Unahitaji chakula ili uishi. Mungu aweza kukufanya uishi milele! Kwa hiyo, usiache kamwe mtu yeyote akuzuie usijifunze jinsi ya kuwa rafiki ya Mungu.—Yohana 17:3.

  • Mungu Ndiye Rafiki Bora Uwezaye Kuwa Naye
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 2

      Mungu Ndiye Rafiki Bora Uwezaye Kuwa Naye

      Kuwa rafiki ya Mungu ndilo jambo bora zaidi kwako. Mungu atakufundisha jinsi ya kuwa mwenye furaha na mwenye usalama; atakuweka huru kutokana na imani nyingi zisizo za kweli na mazoea yanayodhuru. Atasikiliza sala zako. Atakusaidia ufurahie amani ya ndani na uwe na uhakika. (Zaburi 71:5; 73:28) Mungu atakusaidia wakati wa matatizo. (Zaburi 18:18) Na Mungu anakutolea zawadi yake ya uhai udumuo milele.—Waroma 6:23.

      Umkaribiapo Mungu, utawakaribia rafiki za Mungu. Wao watakuwa rafiki zako pia. Kwa kweli, watakuwa kama ndugu na dada zako. Watafurahia kukufundisha juu ya Mungu nao watakusaidia na kukutia moyo.

      Sisi hatulingani na Mungu. Unapojitahidi kuwa rafiki ya Mungu, lazima uelewe jambo moja muhimu. Kuwa rafiki ya Mungu si sawa na kuwa rafiki ya mtu mnayelingana. Mungu ni wa kale zaidi na mwenye hekima zaidi, naye ana nguvu zaidi kuliko sisi. Yeye ndiye Mtawala aliye na haki ya kututawala. Basi tukitaka kuwa rafiki zake, ni lazima tumsikilize na kufanya mambo anayotuambia tufanye. Tukifanya hivyo, tutapata mema sikuzote.—Isaya 48:18.

  • Unahitaji Kujifunza Juu ya Mungu
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 3

      Unahitaji Kujifunza Juu ya Mungu

      Ili uwe rafiki ya Mungu, unahitaji kujifunza juu yake. Je, rafiki zako wanajua jina lako, nao hulitumia? Ndiyo. Mungu pia akutaka ujue jina lake na kulitumia. Jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18; Mathayo 6:9) Lazima pia ujifunze mambo yanayompendeza na yale yasiyompendeza. Unahitaji kujua rafiki zake na adui zake. Kumjua mtu huchukua muda. Biblia inasema kwamba inafaa kutenga wakati wa kujifunza juu ya Yehova.—Waefeso 5:15, 16.

      Rafiki za Mungu hufanya mambo yanayompendeza. Wafikirie rafiki zako. Ukiwatendea mabaya na kufanya mambo wanayochukia, je, wataendelea kuwa rafiki zako? La, hasha! Vivyo hivyo, ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, unahitaji kufanya mambo yanayompendeza.—Yohana 4:24.

      Si dini zote hutokeza urafiki na Mungu. Yesu, ambaye ndiye rafiki wa karibu zaidi wa Mungu, alizungumza juu ya barabara mbili. Barabara moja ni pana nayo imejaa watu. Barabara hiyo huongoza kwenye uharibifu. Barabara ile nyingine ni nyembamba nayo ina watu wachache wanaoitembea. Barabara hiyo huongoza kwenye uhai udumuo milele. Kwa hiyo, ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, lazima ujifunze njia ya kweli ya kumwabudu.—Mathayo 7:13, 14.

  • Jinsi Unavyoweza Kujifunza Juu ya Mungu
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 4

      Jinsi Unavyoweza Kujifunza Juu ya Mungu

      Unaweza kujifunza juu ya Yehova kwa kusoma Biblia. Zamani za kale, Mungu aliteua wanadamu fulani ili waandike mawazo yake. Maandishi hayo yanaitwa Biblia. Leo sisi hujifunza juu ya Mungu kwa kuisoma Biblia. Kwa kuwa Biblia ina neno la Yehova, au ujumbe wake, hiyo pia huitwa Neno la Mungu. Tunaweza kuamini mambo ambayo Biblia husema kwa sababu Yehova hawezi kamwe kusema uwongo. “Haiwezekani Mungu kusema uwongo.” (Waebrania 6:18) Neno la Mungu lina kweli ndani yake.—Yohana 17:17.

      Biblia ni mojawapo ya zawadi za Mungu zenye thamani sana kwetu. Ni kama barua ambayo baba mwenye upendo amewaandikia watoto wake. Hiyo hutuambia juu ya ahadi ya Mungu ya kuibadili dunia iwe mahali pazuri sana pa kuishi—paradiso. Hutuambia mambo aliyofanya wakati uliopita, mambo anayofanya sasa, na yale atakayofanya wakati ujao kwa ajili ya watoto wake waaminifu. Biblia pia hutusaidia kutatua matatizo yetu na kupata furaha.—2 Timotheo 3:16, 17.

      Mashahidi wa Yehova ni rafiki za Mungu; watakusaidia uelewe mambo ambayo Biblia hufundisha. Waambie tu kwamba unataka kujifunza Biblia. Hawatakuambia ulipe pesa ili wakufundishe. (Mathayo 10:8) Tena, unaweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mikutano hiyo hufanyiwa mahali pa ibada paitwapo Majumba ya Ufalme. Ukihudhuria mikutano ya Kikristo, ujuzi wako juu ya Mungu utaongezeka haraka.

      Unaweza kujifunza juu ya Mungu kutokana na vitu alivyoumba. Kwa mfano, Biblia inasema hivi: “Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwanzo 1:1, Biblia Habari Njema) Yehova alipoumba “mbingu,” aliumba jua. Basi jambo hilo linatufundisha nini juu ya Mungu? Linatufundisha kwamba Yehova ana nguvu nyingi. Yeye tu ndiye angeweza kuumba kitu chenye nguvu kama jua. Pia latufundisha kwamba Yehova ni mwenye hekima, kwa sababu ilihitaji hekima ili kuumba jua, ambalo hutoa joto na nuru nalo halikwishi kamwe.

      Uumbaji wa Yehova waonyesha kwamba yeye anatupenda. Wazia aina mbalimbali za matunda yaliyo duniani. Yehova angeweza kutupatia aina moja tu ya tunda—au hata kutotupatia tunda lolote. Badala yake, Yehova alitupatia aina nyingi za matunda yenye maumbo, ukubwa, rangi, na ladha mbalimbali. Mambo hayo yaonyesha kuwa Yehova ni Mungu mwenye upendo na vile vile mkarimu sana, mwenye kujali na mwenye fadhili.—Zaburi 104:24.

  • Rafiki za Mungu Wataishi Katika Paradiso
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • Somo La 5

      Rafiki za Mungu Wataishi Katika Paradiso

      Paradiso haitakuwa kama ulimwengu tunamoishi leo. Mungu hakutaka kamwe dunia ijae matatizo na huzuni, maumivu na kuteseka. Wakati ujao, Mungu ataifanya dunia iwe paradiso. Paradiso itakuwaje? Hebu tuone mambo ambayo Biblia inasema:

      Watu wema. Paradiso itakuwa makao ya rafiki za Mungu. Watatendeana mema. Wataishi kulingana na njia za Mungu za uadilifu.—Mithali 2:21.

      Chakula tele. Njaa haitakuwako katika Paradiso. Biblia inasema hivi: “Na uwepo wingi wa nafaka [au, chakula] katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

      Nyumba nzuri na kazi yenye kufurahisha. Katika dunia iliyo Paradiso, kila familia itakuwa na makao yake binafsi. Kila mtu atafanya kazi inayoleta furaha ya kweli.—Isaya 65:21-23.

      Amani ulimwenguni kote. Watu hawatakuwa wakipigana wala kufa vitani. Neno la Mungu linasema hivi: “[Mungu] avikomesha vita.”—Zaburi 46:8, 9.

      Afya njema. Biblia yaahidi hivi: “Hapana mwenyeji [wa Paradiso] atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Pia, hakuna mtu atakayekuwa kilema wala kipofu wala kiziwi wala hakuna yeyote atakayeshindwa kuongea.—Isaya 35:5, 6.

      Mwisho wa maumivu, huzuni, na kifo. Neno la Mungu lasema hivi: “Kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

      Watu wabaya hawatakuwako. Yehova anaahidi hivi: “Waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:22.

      Watu watapendana na kuheshimiana. Ukosefu wa haki, kuonewa, pupa, na chuki hazitakuwapo tena. Watu wataungana nao wataishi kulingana na njia za Mungu za uadilifu.—Isaya 26:9.

  • Paradiso Iko Karibu!
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 6

      Paradiso Iko Karibu!

      Mambo mabaya yanayotendeka duniani leo yanaonyesha kwamba Paradiso iko karibu. Biblia ilisema kwamba tungeona nyakati mbaya kabla tu ya Paradiso kuja. Sasa tunaishi katika nyakati hizo! Yafuatayo ni baadhi ya mambo ambayo Biblia ilisema yangetendeka:

      Vita vikubwa-vikubwa. “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme.” (Mathayo 24:7) Unabii huo umetimia. Tangu mwaka wa 1914, kumekuwapo vita viwili vya ulimwengu na vita vingine vingi vidogo-vidogo. Mamilioni ya watu wamekufa katika vita hivyo.

      Magonjwa yanayoenea sana. Kungekuwako “mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza.” (Luka 21:11) Je, hilo limetimia? Ndiyo. Kansa, ugonjwa wa moyo, kifua kikuu, malaria, UKIMWI, na magonjwa mengine yameua mamilioni ya watu.

      Ukosefu wa chakula. Duniani kote kuna watu ambao hawana chakula cha kutosha. Kila mwaka, mamilioni ya watu hufa njaa. Hiyo ni ishara nyingine ya kwamba Paradiso itakuja hivi karibuni. Biblia inasema hivi: “Kutakuwa na upungufu wa chakula.”—Marko 13:8.

      Matetemeko ya dunia. “Kutakuwa . . . matetemeko ya dunia mahali pamoja baada ya pengine.” (Mathayo 24:7) Jambo hilo pia limetimia leo. Watu zaidi ya milioni moja wamekufa katika matetemeko ya dunia tangu mwaka wa 1914.

      Watu waovu. Watu wangekuwa “wapenda-fedha” na “wenye kujipenda wenyewe.” Wangekuwa “wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.” Watoto wangekuwa “wasiotii wazazi.” (2 Timotheo 3:1-5) Je, wewe hukubali kwamba kuna watu wengi wa aina hiyo leo? Hawamheshimu Mungu hata kidogo, nao huwasumbua wale wanaojaribu kujifunza juu ya Mungu.

      Uhalifu. Pia kungekuwako “kuongezeka kwa uasi-sheria.” (Mathayo 24:12) Haikosi utakubali kwamba uhalifu ni mbaya sana kuliko ulivyokuwa miaka kadhaa iliyopita. Kila mahali, watu wamo katika hatari ya kunyang’anywa vitu, kudanganywa, au kuumizwa.

      Mambo hayo yote yanaonyesha kuwa Ufalme wa Mungu uko karibu. Biblia inasema hivi: “Mwonapo mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:31) Ufalme wa Mungu ni nini? Ni serikali ya mbinguni ya Mungu ambayo italeta Paradiso hapa duniani. Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali za wanadamu.—Danieli 2:44.

  • Onyo la Wakati Uliopita
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 7

      Onyo la Wakati Uliopita

      Yehova hataruhusu watu wabaya waiharibu Paradiso. Rafiki zake peke yao ndio watakaoishi humo. Ni nini kitakachowapata watu wabaya? Ili upate jibu, fikiria kisa halisi cha Noa. Noa aliishi maelfu ya miaka iliyopita. Alikuwa mtu mzuri ambaye sikuzote alijitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Lakini watu wale wengine duniani walifanya mambo mabaya. Basi, Yehova akamwambia Noa kwamba Angeleta furiko ili awaharibu watu wote hao waliokuwa waovu. Alimwambia Noa ajenge safina ili yeye na familia yake wasife wakati ambapo Furiko lingekuja.—Mwanzo 6:9-18.

      Noa na familia yake walijenga safina. Noa aliwaonya watu kwamba Furiko linakuja, lakini hawakumsikiliza. Waliendelea kufanya mambo mabaya. Baada ya safina kujengwa, Noa aliwaingiza wanyama ndani ya safina hiyo, naye pamoja na familia yake wakaingia ndani. Kisha Yehova akaleta mvua kubwa. Mvua hiyo ilinyesha siku 40, mchana na usiku. Maji yalijaa dunia yote.—Mwanzo 7:7-12.

      Watu waovu walipoteza uhai wao, lakini Noa na familia yake wakaokolewa. Yehova aliwapitisha salama katika Furiko naye akawaweka katika dunia iliyosafishwa na kuondolewa uovu. (Mwanzo 7:22, 23) Biblia yasema kwamba wakati unakuja ambapo Yehova atawaharibu tena watu wanaokataa kufanya mambo mema. Watu wema hawataharibiwa. Wataishi milele katika dunia Paradiso.—2 Petro 2:5, 6, 9.

      Leo watu wengi hufanya mambo mabaya. Ulimwengu umejaa matatizo. Yehova huwatuma Mashahidi wake tena na tena ili wawaonye watu, lakini watu wengi hawataki kuyasikiliza maneno ya Yehova. Hawataki kubadili njia zao. Hawataki kukubali yale ambayo Mungu anasema kuhusu mabaya na mema. Ni nini kitakachowapata watu hao? Je, siku moja watabadilika? Wengi wao hawatabadilika. Wakati unakuja ambapo watu waovu wataharibiwa nao hawataishi tena kamwe.—Zaburi 92:7.

      Dunia haitaharibiwa; itafanywa paradiso. Wale wanaokuwa rafiki za Mungu wataishi milele katika Paradiso hiyo duniani.—Zaburi 37:29.

  • Adui za Mungu Ni Nani?
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 8

      Adui za Mungu Ni Nani?

      Adui mkuu wa Mungu ni Shetani Ibilisi. Yeye ni kiumbe cha roho aliyemwasi Yehova. Shetani anaendelea kupigana na Mungu naye huwasababishia wanadamu matatizo makubwa. Shetani ni mwovu. Yeye ni mwongo na mwuaji.—Yohana 8:44.

      Viumbe wengine wa roho waliungana na Shetani katika uasi wake dhidi ya Mungu. Biblia huwaita viumbe hao roho waovu. Kama Shetani, roho waovu ni adui za wanadamu. Wanapenda kuwaumiza watu. (Mathayo 9:32, 33; 12:22) Yehova atamharibu Shetani na roho wake waovu milele. Wana wakati mfupi tu unaobaki wa kuwasababishia wanadamu matatizo.—Ufunuo 12:12.

      Ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, lazima usifanye mambo ambayo Shetani anataka ufanye. Shetani na roho waovu humchukia Yehova. Wao ni adui za Mungu, nao wanataka kukufanya uwe adui ya Mungu. Ni lazima uchague yule unayetaka kumpendeza—Shetani au Yehova. Ukiwa unataka uhai udumuo milele, lazima uchague kufanya mapenzi ya Mungu. Shetani ana mbinu na njia nyingi za kudanganya watu. Yeye anawadanganya watu wengi.—Ufunuo 12:9.

  • Rafiki za Mungu Ni Nani?
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 9

      Rafiki za Mungu Ni Nani?

      Yesu Kristo ni Mwana wa Yehova, naye ndiye rafiki yake wa karibu zaidi na anayependwa zaidi. Kabla ya Yesu kuishi duniani akiwa mwanadamu, aliishi mbinguni akiwa kiumbe cha roho chenye uweza. (Yohana 17:5) Kisha akaja duniani kuwafundisha watu kweli juu ya Mungu. (Yohana 18:37) Pia alitoa uhai wake wa kibinadamu ili awaokoe wanadamu watiifu kutoka katika dhambi na kifo. (Waroma 6:23) Sasa Yesu ndiye Mfalme wa Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni ambayo italeta Paradiso hapa duniani.—Ufunuo 19:16.

      Malaika ni rafiki za Mungu pia. Malaika hawakuanza uhai wao hapa duniani wakiwa wanadamu. Waliumbiwa huko mbinguni kabla ya Mungu kuiumba dunia. (Ayubu 38:4-7) Kuna mamilioni ya malaika. (Danieli 7:10) Hao rafiki za Mungu wanaoishi mbinguni wanataka wanadamu wajifunze kweli juu ya Yehova.—Ufunuo 14:6, 7.

      Mungu ana rafiki duniani pia; yeye huwaita mashahidi wake. Shahidi aliye mahakamani husema mambo anayojua kuhusu mtu au kitu fulani. Mashahidi wa Yehova huwaambia watu wengine mambo wanayojua juu ya Yehova na kusudi lake. (Isaya 43:10) Kama vile malaika, Mashahidi wanataka kukusaidia wewe ujifunze kweli juu ya Yehova. Wanataka wewe pia uwe rafiki ya Mungu.

  • Jinsi ya Kupata Dini ya Kweli
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • Somo La 10

      Jinsi ya Kupata Dini ya Kweli

      Ukitaka kuwa rafiki ya Mungu, ni lazima ushirikiane na dini inayokubaliwa na Mungu. Yesu alisema kwamba “waabudu wa kweli” wangemwabudu Mungu kwa kupatana na “kweli.” (Yohana 4:23, 24) Kuna njia moja tu ya kweli ya kumwabudu Mungu. (Waefeso 4:4-6) Dini ya kweli huongoza kwenye uhai udumuo milele, na dini isiyo ya kweli huongoza kwenye uharibifu.—Mathayo 7:13, 14.

      Unaweza kuitambua dini ya kweli kwa kuwaangalia washiriki wake. Kwa kuwa Yehova ni mwema, lazima waabudu wake wa kweli wawe watu wema. Kama vile mchungwa mwema huzaa machungwa mema, vivyo hivyo dini ya kweli hutokeza watu wema.—Mathayo 7:15-20.

      Rafiki za Yehova wanaiheshimu sana Biblia. Wanajua kwamba Biblia imetoka kwa Mungu. Wao huruhusu mambo ambayo inasema yaongoze maisha yao, yatatue matatizo yao, na yawasaidie kujifunza juu ya Mungu. (2 Timotheo 3:16) Wao hujitahidi kutenda mambo wanayofundisha.

      Rafiki za Yehova hupendana. Yesu aliwaonyesha watu upendo kwa kuwafundisha juu ya Mungu, na kwa kuwaponya wale waliokuwa wagonjwa. Washiriki wa dini ya kweli pia huwapenda watu wengine. Kama vile Yesu, hawawadharau maskini wala watu wa kabila tofauti. Yesu alisema kwamba watu wangewajua wanafunzi wake kwa jinsi wanavyopendana.—Yohana 13:35.

      Rafiki za Mungu huheshimu jina la Mungu, Yehova. Ikiwa mtu fulani angekataa kutumia jina lako, je, angekuwa rafiki yako wa karibu? La! Tunapokuwa na rafiki, sisi hulitumia jina lake nasi huwaambia wengine mambo mema juu yake. Kwa hiyo, wale wanaotaka kuwa rafiki za Mungu wapaswa kulitumia jina lake na kuzungumza na wengine juu yake. Yehova anataka sisi tufanye hivyo.—Mathayo 6:9; Waroma 10:13, 14.

      Kama alivyofanya Yesu, rafiki za Mungu huwafundisha watu juu ya Ufalme wa Mungu. Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoifanya dunia kuwa paradiso. Rafiki za Mungu huwaeleza wengine habari njema hizo juu ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

      Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuwa rafiki za Mungu. Wao wanaiheshimu Biblia nao wanapendana. Pia, wao hutumia na kuheshimu jina la Mungu na kuwafundisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Mashahidi wa Yehova ndio wanaofuata dini ya kweli duniani leo.

  • Ikatae Dini Isiyo ya Kweli!
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 11

      Ikatae Dini Isiyo ya Kweli!

      Shetani na roho wake waovu hawataki wewe umtumikie Mungu. Wanataka ikiwezekana wamgeuze kila mtu kutoka kwa Mungu. Wao hujaribu jinsi gani kufanya hivyo? Njia moja wanayotumia ni dini isiyo ya kweli. (2 Wakorintho 11:13-15) Dini ambayo haifundishi kweli kutoka kwa Biblia ni dini isiyo ya kweli. Dini isiyo ya kweli ni kama fedha bandia—huenda zikaonekana halisi, lakini hazina thamani yoyote. Dini isiyo ya kweli yaweza kukuletea matatizo mengi.

      Mambo ya kidini yasiyo ya kweli hayawezi kumpendeza Yehova, Mungu wa kweli. Yesu alipokuwa duniani, kulikuwepo kikundi cha watu wa kidini waliotaka kumwua. Walifikiri kwamba ibada yao ndiyo ya kweli. Walisema hivi: “Tuna Baba mmoja, Mungu.” Je, Yesu alikubaliana nao? La! Aliwaambia hivi: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi.” (Yohana 8:41, 44) Leo, watu wengi hufikiri kuwa wanamwabudu Mungu, na kumbe, wanamtumikia hasa Shetani na roho wake waovu!—1 Wakorintho 10:20.

      Kama vile mti uliooza uzaavyo matunda mabaya, ndivyo dini isiyo ya kweli itokezavyo watu wanaofanya mambo mabaya. Ulimwengu umejaa matatizo kwa sababu ya mambo mabaya ambayo watu hufanya. Kuna ukosefu wa adili, mapigano, wizi, kuonewa, mauaji, na ubakaji. Watu wengi wanaofanya mambo mabaya hayo wana dini, lakini dini yao haiwachochei kutenda mambo mazuri. Hawawezi kuwa rafiki za Mungu wasipoacha kutenda mambo mabaya.—Mathayo 7:17, 18.

      Dini isiyo ya kweli huwafundisha watu waombe sanamu. Mungu anasema watu wasiombe sanamu. Na kwa kweli haifai kufanya hivyo. Je, ungefurahi iwapo mtu fulani angeongea na picha yako tu, wala haongei nawe kamwe? Je, mtu huyo angeweza kuwa rafiki yako wa kweli? La, haingewezekana. Yehova anataka watu waongee naye, wala hataki waongee na sanamu au picha, ambazo hazina uhai.—Kutoka 20:4, 5.

      Dini isiyo ya kweli hufundisha kwamba ni sawa kuwaua watu wakati wa vita. Yesu alisema kwamba rafiki za Mungu wangependana. Hatuui watu tunaowapenda. (Yohana 13:35) Hata ni makosa kwetu kuwaua watu wabaya. Adui za Yesu walipokuja kumkamata, hakuwaruhusu wanafunzi wake wampiganie.—Mathayo 26:51, 52.

      Dini isiyo ya kweli hufundisha kwamba watu waovu watateseka katika moto wa helo. Ingawa hivyo, Biblia hufundisha kwamba dhambi huongoza kwenye kifo. (Waroma 6:23) Yehova ni Mungu wa upendo. Je, Mungu mwenye upendo angeweza kutesatesa watu milele? Bila shaka la! Katika Paradiso, kutakuwako dini moja tu, ile inayokubaliwa na Yehova. (Ufunuo 15:4) Dini zote zinazotegemea uwongo wa Shetani zitaondolewa.

  • Ni Nini Hutokea Wakati wa Kifo?
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 12

      Ni Nini Hutokea Wakati wa Kifo?

      Kifo ni kinyume cha uhai. Kifo ni kama usingizi mzito. (Yohana 11:11-14) Wafu hawawezi kusikia, kuona, kusema, wala kuwaza lolote. (Mhubiri 9:5, 10) Dini isiyo ya kweli hufundisha kwamba wafu huenda katika ulimwengu wa roho ili waishi na babu zao wa kale waliokufa. Biblia haifundishi hivyo.

      Wafu hawawezi kutusaidia, wala hawawezi kutudhuru. Kwa kawaida, watu hufanya matambiko na kutoa dhabihu ambazo wanaamini kuwa zitawafurahisha wafu. Mambo hayo yanamchukiza Mungu kwa sababu yanategemea mojawapo ya uwongo mbalimbali wa Shetani. Vivyo hivyo, mambo hayo hayawezi kuwapendeza wafu, kwa kuwa hawana uhai. Hatupaswi kuogopa wala kuabudu wafu. Tunapaswa kumwabudu Mungu peke yake.—Mathayo 4:10.

      Wafu wataishi tena. Yehova atawaamsha wafu warudi kwenye uhai katika dunia paradiso. Jambo hilo litatendeka wakati ujao. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Mungu aweza kuwaamsha watu ambao wamekufa kama vile wewe uwezavyo kumwamsha mtu kutoka usingizini.—Marko 5:22, 23, 41, 42.

      Wazo la kwamba sisi hatufi ni uwongo ambao Shetani Ibilisi anaeneza. Shetani na roho wake waovu hufanya watu wafikiri kwamba roho za wafu ziko hai nazo husababisha magonjwa na matatizo mengine. Shetani huwadanganya watu, nyakati nyingine kupitia ndoto na maono. Yehova huwashutumu wale wanaojaribu kuongea na wafu.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

  • Uganga Na Uchawi Ni Mambo Mabaya
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 13

      Uganga Na Uchawi Ni Mambo Mabaya

      Shetani anataka wewe ufanye mambo ya kiganga. Watu wengi hutoa dhabihu kwa babu zao wa kale waliokufa au kwa roho ili ziwalinde wasipate madhara. Wao hufanya hivyo kwa sababu wanaogopa nguvu za ulimwengu wa roho. Watu hao huvaa pete au bangili za kiganga. Wao hunywa au kusugua mwilini mwao “dawa” zinazodhaniwa kuwa zina nguvu za kiganga. Watu fulani huficha katika nyumba zao au chini ya ardhi vyombo vinavyoaminiwa kuwa na nguvu za kulinda. Wengine nao hutumia “dawa” za kiganga kwa sababu wanaamini kuwa zitawaletea mafanikio katika biashara, mitihani shuleni, au uchumba.

      Ukitaka ulinzi bora zaidi dhidi ya Shetani, wapaswa kuwa rafiki ya Yehova. Yehova Mungu na malaika zake wana nguvu nyingi zaidi kuliko Shetani na roho wake waovu. (Yakobo 2:19; Ufunuo 12:9) Yehova ana hamu ya kutumia nguvu zake kuwasaidia rafiki zake—wale wenye uaminifu-mshikamanifu kabisa kwake.—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

      Neno la Mungu linasema hivi: “Msifanye kuloga.” Yehova hushutumu uganga na uchawi kwa sababu mazoea hayo yanaweza kumfanya mtu atawaliwe moja kwa moja na Shetani Ibilisi.—Mambo ya Walawi 19:26.

  • Rafiki za Mungu Huepuka Mabaya
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 14

      Rafiki za Mungu Huepuka Mabaya

      Shetani huwashawishi watu wafanye mambo mabaya. Mtu anayetaka kuwa rafiki ya Mungu lazima achukie mambo ambayo Yehova huchukia. (Zaburi 97:10) Hapa pana mambo kadhaa ambayo rafiki za Mungu huyaepuka:

      Dhambi zinazohusu ngono. “Usizini.” (Kutoka 20:14) Ni kosa pia kufanya ngono kabla ya ndoa.—1 Wakorintho 6:18.

      Ulevi. “Walevi . . . hawatarithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:10.

      Uuaji, Utoaji-Mimba. “Usiue.”—Kutoka 20:13.

      Wizi. “Usiibe.”—Kutoka 20:15.

      Kusema Uwongo. Yehova huchukia “ulimi wa uongo.”—Mithali 6:17.

      Jeuri na Hasira Isiyodhibitiwa. Yehova humchukia “mwenye kupenda udhalimu [“jeuri,” NW].” (Zaburi 11:5) “Kazi za mwili [hutia ndani] . . . hasira za ghafula.”—Wagalatia 5:19, 20.

      Kucheza Kamari. “Mkome kuchangamana katika ushirika pamoja na yeyote . . . ambaye ni . . . mtu mwenye pupa.”—1 Wakorintho 5:11.

      Chuki za Kijamii na za Kikabila. “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi.”—Mathayo 5:43, 44.

      Mambo ambayo Mungu anatuambia hutunufaisha. Si rahisi sikuzote kuepuka kufanya mambo mabaya. Yehova na Mashahidi wake wanaweza kukusaidia kuepuka kufanya mambo yanayomchukiza Mungu.—Isaya 48:17; Wafilipi 4:13; Waebrania 10:24, 25.

  • Rafiki za Mungu Hufanya Mambo Mema
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 15

      Rafiki za Mungu Hufanya Mambo Mema

      Ukiwa na rafiki unayempenda na kumheshimu, wewe hujaribu kuwa kama yeye. “BWANA yu mwema, mwenye adili,” Biblia yasema. (Zaburi 25:8) Ili tuwe rafiki za Mungu, ni lazima tuwe watu wema na wenye adili. Biblia inasema hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.” (Waefeso 5:1, 2) Hapa pana njia kadhaa za kufanya hivyo:

      Wasaidie wengine. “Acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote.”—Wagalatia 6:10.

      Fanya kazi kwa bidii. “Mwibaji na asiibe tena, bali acheni afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema.”—Waefeso 4:28.

      Dumu ukiwa safi kimwili na kiadili. “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.”—2 Wakorintho 7:1.

      Watendee washiriki wa familia yako kwa upendo na heshima. “Acheni kila mtu . . . kati yenu ampende hivyo mke wake kama yeye mwenyewe; kwa upande mwingine, mke apaswa kuwa na staha yenye kina kirefu kwa mume wake. Watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu.”—Waefeso 5:33–6:1.

      Wapende wengine. “Acheni tuendelee kupendana, kwa sababu upendo ni wa kutoka kwa Mungu.”—1 Yohana 4:7.

      Tii sheria za nchi. “Acheni kila nafsi iwe katika ujitiisho kwa [serikali] . . . Walipeni wote haki zao, kwa yeye atakaye kodi, kodi.”—Waroma 13:1, 7.

  • Onyesha Upendo Wako Kwa Mungu
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 16

      Onyesha Upendo Wako Kwa Mungu

      Ili uendelee kuwa na rafiki, wahitaji kuzungumza naye. Wewe humsikiliza, naye hukusikiliza. Pia wewe huwaambia watu wengine mambo mema juu ya rafiki yako. Hali iko hivyo kuhusiana na kuwa rafiki ya Mungu. Fikiria mambo ambayo Biblia inasema kuhusu hilo:

      Zungumza na Yehova kwa ukawaida katika sala. “Dumuni katika sala.”—Waroma 12:12.

      Soma Neno la Mungu, Biblia. “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

      Wafundishe wengine juu ya Mungu. “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . [mkiwafundisha] kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20.

      Wakaribie rafiki za Mungu. “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima.”—Mithali 13:20.

      Hudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, . . . [tukitiana] moyo.”—Waebrania 10:24, 25.

      Unga mkono kazi ya Ufalme. “Acheni kila mmoja [atoe] kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.”—2 Wakorintho 9:7.

  • Ili Uendelee Kuwa Na Rafiki, Ni Lazima Uwe Rafiki
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 17

      Ili Uendelee Kuwa Na Rafiki, Ni Lazima Uwe Rafiki

      Urafiki hutegemea upendo. Kadiri ujifunzavyo juu ya Yehova, ndivyo utakavyozidi kumpenda. Uzidipo kumpenda Mungu, hamu yako ya kumtumikia itaongezeka pia. Hamu hiyo itakuchochea kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo. (Mathayo 28:19) Unaweza kuwa rafiki ya Mungu milele kwa kujiunga na familia yenye furaha ya Mashahidi wa Yehova. Unapaswa kufanya nini?

      Ni lazima uonyeshe upendo wako kwa Mungu kwa kutii sheria zake. “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.”—1 Yohana 5:3.

      Tenda mambo unayojifunza. Yesu alisimulia hadithi inayoonyesha jambo hilo. Mtu mwenye hekima alijenga nyumba yake juu ya mwamba. Mpumbavu naye akajenga nyumba yake juu ya mchanga. Dhoruba na mvua kubwa ilipokuja, nyumba iliyojengwa juu ya mwamba haikuanguka, lakini nyumba iliyojengwa juu ya mchanga ilianguka kwa kishindo kikubwa. Yesu alisema kuwa wale wanaosikia mafundisho yake na kuyatenda ni kama yule mtu mwenye hekima aliyejenga juu ya mwamba. Lakini wale wanaosikiliza mafundisho yake wala wasiyatende ni kama yule mpumbavu aliyejenga juu ya mchanga. Wewe ungependa kuwa mtu wa aina gani?—Mathayo 7:24-27.

      Wakfu. Wakfu wamaanisha kwamba usali kwa Yehova na kumwambia kuwa unataka kufanya mapenzi yake milele. Kufanya mapenzi ya Mungu huonyesha kwamba wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo.—Mathayo 11:29.

      Ubatizo. “Ubatizwe na uoshe dhambi zako kwa kuitia jina lake.”—Matendo 22:16.

      Mtumikie Mungu kikamili. “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.”—Wakolosai 3:23.

  • Uwe Rafiki ya Mungu Milele!
    Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu!
    • SOMO LA 18

      Uwe Rafiki ya Mungu Milele!

      Kupata rafiki huhitaji jitihada; wahitaji kujitahidi ili uendelee kuwa na rafiki. Jitihada zako za kuwa rafiki ya Mungu na kuendelea kuwa rafiki yake zitabarikiwa sana. Yesu aliwaambia hivi wale waliomwamini: “Kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:32) Hilo lamaanisha nini?

      Unaweza kufurahia uhuru sasa. Unaweza kuwa huru kutokana na mafundisho yasiyo ya kweli ambayo Shetani ameeneza. Unaweza kuwa na tumaini tofauti na mamilioni ya watu wasiomjua Yehova ambao hawana tumaini maishani. (Waroma 8:22) Rafiki za Mungu hata hawana “hofu ya kifo.”—Waebrania 2:14, 15.

      Unaweza kufurahia uhuru katika ulimwengu mpya wa Mungu. Unaweza kufurahia uhuru mzuri kama nini wakati ujao! Katika dunia Paradiso, hakutakuwako vita, magonjwa, na uhalifu. Umaskini na njaa hazitakuwako. Uzee na kifo havitakuwako. Hakutakuwako hofu, kuonewa, na ukosefu wa haki. Biblia yasema hivi kumhusu Mungu: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.

      Rafiki za Mungu wataishi milele. Uhai wa milele ni zawadi yenye thamani ambayo Mungu atawapa wote wanaojitahidi kuwa rafiki zake. (Waroma 6:23) Ebu wazia tu mambo ambayo uhai usio na mwisho utamaanisha kwako!

      Utakuwa na wakati wa kufanya mambo mengi. Labda unataka kujifunza kucheza ala fulani ya muziki. Au labda unataka kujifunza kuchora picha au kuwa seremala. Huenda unataka kujifunza kuhusu wanyama au mimea. Au labda unataka kusafiri na kuona nchi mbalimbali na watu mbalimbali. Kuwa na uhai udumuo milele kutafanya mambo hayo yote yawezekane!

      Utakuwa na wakati wa kupata rafiki wengi. Kuishi milele kutakuwezesha ujue watu wengine wengi ambao wamekuwa rafiki za Mungu. Utapata kujua vipawa na sifa zao njema, nao watakuwa rafiki zako pia. Utawapenda, nao watakupenda. (1 Wakorintho 13:8) Kuwa na uhai usio na mwisho kutakupa nafasi ya kuwa rafiki ya kila mtu duniani! Jambo zuri zaidi ya yote ni kwamba urafiki wako pamoja na Yehova utazidi kuongezeka nguvu kadiri karne zipitavyo. Na uwe rafiki ya Mungu milele!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki