Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Tunda la Roho’ Linamtukuza Mungu
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
    • ‘Tunda la Roho’ Linamtukuza Mungu

      “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.”—YOH. 15:8.

      1, 2. (a) Tuna nafasi gani mbalimbali za kuwatia wengine moyo? (b) Ni zawadi gani kutoka kwa Yehova ambayo inaboresha uwezo wetu wa kumtumikia?

      FIKIRIA hali hizi mbili: Mwanamke mmoja Mkristo anagundua kwamba dada mmoja kijana anaonekana anahangaishwa na jambo fulani. Dada huyo Mkristo anafanya mipango ili kuhubiri pamoja na yule dada kijana. Wanapozungumza huku wakihubiri nyumba kwa nyumba, dada huyo kijana anaanza kumweleza kile kinachomsumbua. Baadaye siku hiyo, mwanamke huyo kijana anamshukuru Yehova katika sala kwa sababu yule dada mkomavu alimjali kwa upendo; hilo ndilo jambo alilohitaji hasa. Katika kisa kingine, wenzi wawili wa ndoa wamerudi hivi karibuni kutoka nchi ya kigeni ambako walienda kuhubiri. Kwenye tafrija fulani, wenzi hao wanaposimulia kwa msisimko mambo yaliyoonwa, ndugu mmoja kijana anasikiliza kwa makini. Baada ya miaka fulani kupita, anapojitayarisha kwenda kwenye mgawo katika nchi ya kigeni, kijana huyo anafikiria wale wenzi wa ndoa na mazungumzo ambayo yalimchochea kuwa mmishonari.

      2 Labda hali hizo zinakukumbusha mtu fulani ambaye alikuchochea kufanya uamuzi wa maana katika maisha yako au mtu ambaye ulimchochea abadili maisha yake. Bila shaka, si jambo la kawaida kwa mazungumzo ya pindi moja kubadili maisha ya mtu, lakini kila siku, tuna nafasi za kuwatia wengine moyo na kuwatia nguvu. Wazia ikiwa kungekuwa na jambo fulani ambalo lingeboresha uwezo na sifa zako, na hivyo kukufanya uwe mwenye faida zaidi kwa ndugu zako na katika utumishi wa Mungu. Je, hilo halingekuwa jambo zuri ajabu? Kwa kweli, Yehova anatupatia zawadi kama hiyo, yaani, roho yake takatifu. (Luka 11:13) Roho ya Mungu inapotenda kazi katika maisha yetu, inatokeza ndani yetu sifa nzuri sana ambazo zinaboresha kila sehemu ya utumishi wetu kwa Mungu. Hiyo ni zawadi nzuri ajabu kama nini!—Soma Wagalatia 5:22, 23.

      3. (a) Tunamtukuza Mungu jinsi gani tunapositawisha ‘tunda la roho’? (b) Tutachunguza maswali gani?

      3 Sifa ambazo roho takatifu inatokeza zinaonyesha utu halisi wa Chanzo cha roho hiyo, yaani, Yehova Mungu. (Kol. 3:9, 10) Yesu alionyesha sababu ya msingi inayopaswa kuwafanya Wakristo wajitahidi kumwiga Mungu alipowaambia mitume wake hivi: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.”a (Yoh. 15:8) Tunapositawisha ‘tunda la roho,’ matokeo yanaonekana wazi kupitia jinsi tunavyosema na kutenda; na hilo linamletea Mungu wetu sifa. (Mt. 5:16) Tunda la roho linatofautiana katika njia gani na tabia za ulimwengu wa Shetani? Tunaweza kusitawisha jinsi gani tunda la roho? Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kufanya hivyo? Tutachunguza maswali au maulizo hayo tunapozungumzia sifa tatu za kwanza za tunda la roho, yaani, upendo, shangwe, na amani.

      Upendo Unaotegemea Kanuni ya Juu Zaidi

      4. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wawe na upendo wa aina gani?

      4 Upendo unaotokezwa na roho takatifu ni tofauti sana na upendo ambao kwa kawaida unaonyeshwa katika ulimwengu. Jinsi gani? Unategemea kanuni ya juu zaidi. Yesu alikazia tofauti hiyo katika Mahubiri ya Mlimani. (Soma Mathayo 5:43-48.) Alitambua kwamba hata watenda-dhambi wana mwelekeo wa kuwatendea wengine kama wanavyotendewa. Mtu hahitaji kujidhabihu ili aonyeshe “upendo” huo, badala yake upendo huo unaonyeshwa kwa kubadilishana zawadi. Ikiwa tunataka ‘kuwa wana wa Baba yetu aliye mbinguni,’ ni lazima tuwe tofauti. Badala ya kuwatendea wengine kama wanavyotutendea, tunapaswa kuwaona na kuwatendea wengine kama Yehova anavyowaona na kuwatendea. Hata hivyo, tunaweza jinsi gani kuwapenda maadui wetu kama Yesu alivyoamuru?

      5. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawapenda wale wanaotutesa?

      5 Fikiria mfano mmoja wa Biblia. Walipokuwa wakihubiri huko Filipi, Paulo na Sila walikamatwa, wakapigwa vikali, na kutupwa gerezani, miguu yao ikiwa imefungwa. Wakati huo, huenda pia mlinzi wa gereza aliwatesa. Walipowekwa huru bila kutazamia baada ya tetemeko la nchi, je, walishangilia kwamba sasa wangeweza kujilipizia kisasi juu ya mtu huyo? Hapana. Hangaiko lao la kutoka moyoni kwa ajili ya mtu huyo, yaani, upendo wao wa kujidhabihu, uliwachochea kumsaidia haraka, na hilo likafanya mlinzi huyo wa gereza na familia yake yote wawe waamini. (Mdo. 16:19-34) Vivyo hivyo, katika nyakati zetu, ndugu zetu wengi wamekuwa ‘baraka kwa wale wanaowatesa.’—Rom. 12:14.

      6. Tunaweza kuwaonyesha ndugu zetu upendo wa kujidhabihu katika njia gani? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 21.)

      6 Upendo wetu kuelekea waamini wenzetu unatia ndani mambo mengi zaidi. “Sisi tuko chini ya wajibu kuzitoa nafsi zetu kwa ajili ya ndugu zetu.” (Soma 1 Yohana 3:16-18.) Hata hivyo, mara nyingi tunaweza kuonyesha upendo wetu katika njia ndogo zaidi. Kwa mfano, tukisema au kufanya jambo ambalo linamchukiza ndugu, tunaweza kuonyesha upendo kwa kuchukua hatua ya kurudisha amani. (Mt. 5:23, 24) Namna gani ikiwa mtu fulani anatukosea? Je, tuko “tayari kusamehe,” au nyakati nyingine tuna mwelekeo wa kuweka kinyongo? (Zab. 86:5) Upendo mwingi ambao unatokezwa na roho takatifu unaweza kutusaidia kufunika makosa madogo-madogo, na kuwasamehe wengine kwa hiari au kwa kupenda ‘kama vile Yehova alivyotusamehe sisi kwa hiari.’—Kol. 3:13, 14; 1 Pet. 4:8.

      7, 8. (a) Kuna uhusiano gani kati ya kuwapenda watu na kumpenda Mungu? (b) Tunaweza kufanya nini ili tumpende Yehova zaidi? (Ona picha iliyo chini.)

      7 Tunaweza kusitawisha jinsi gani upendo wa kujidhabihu kwa ajili ya ndugu zetu? Kwa kumpenda Mungu zaidi. (Efe. 5:1, 2; 1 Yoh. 4:9-11, 20, 21) Nyakati tunazotumia kuwa karibu na Yehova tunaposoma Biblia, kutafakari, na kusali zinajenga mioyo yetu na kutusaidia kumpenda zaidi Baba yetu wa mbinguni. Hata hivyo, tunahitaji kununua wakati ili kumkaribia Mungu.

      8 Kwa mfano: Wazia ikiwa tungeweza kulisoma Neno la Mungu, kutafakari juu yake, na kusali kwa Yehova wakati fulani tu kila siku. Je, hungekuwa makini kulinda wakati huo ili jambo lolote lisivuruge wakati wako wa kuwa pamoja na Yehova? Bila shaka, hakuna mtu anayeweza kutuzuia tusisali kwa Mungu, na wengi wetu tunaweza kusoma Biblia wakati wowote tunaopenda. Hata hivyo, huenda tukahitaji kuchukua hatua fulani ili kuzuia shughuli nyingi za kila siku zisivuruge wakati wetu wa kuwa pamoja na Mungu. Je, unanunua wakati wa kutosha kila siku kumkaribia Yehova?

      “Shangwe ya Roho Takatifu”

      9. Shangwe inayotokezwa na roho takatifu ina uwezo gani?

      9 Tunda la roho linatusaidia kudumisha utulivu hata tunapopambana na matatizo. Shangwe, sifa ya pili tutakayochunguza, inaonyesha kwamba tunaweza kudumisha utulivu. Shangwe ni kama mmea ambao unaweza kusitawi hata katika mazingira magumu. Duniani pote, watumishi wengi wa Mungu ‘wamelipokea neno chini ya dhiki nyingi pamoja na shangwe ya roho takatifu.’ (1 The. 1:6) Wengine wanapambana na hali ngumu na umaskini. Hata hivyo, Yehova anawatia nguvu kupitia roho yake “ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” (Kol. 1:11) Ni nini chanzo cha shangwe hiyo?

      10. Ni nini chanzo cha shangwe yetu?

      10 Tofauti na “utajiri usio hakika” wa ulimwengu wa Shetani, hazina za kiroho ambazo tumepokea kutoka kwa Yehova zina thamani ya kudumu. (1 Tim. 6:17; Mt. 6:19, 20) Yehova ametupatia tumaini la kuishi milele wakati ujao ambalo linatuletea shangwe. Tuna shangwe ya kuwa sehemu ya undugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote. Zaidi ya yote hayo, shangwe yetu inategemea uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunahisi kama Daudi, ambaye ingawa alilazimika kuishi kama mkimbizi, alimsifu Yehova katika wimbo, akisema: “Kwa sababu fadhili zako zenye upendo ni bora kuliko uzima, midomo yangu mwenyewe itakusifu. Kwa hiyo nitakusifu muda wote wa maisha yangu.” (Zab. 63:3, 4) Hata tukipatwa na hali ngumu, tunachochewa kumsifu Mungu kwa shangwe nyingi kutoka moyoni.

      11. Kwa nini ni jambo la maana kumtumikia Yehova kwa shangwe?

      11 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana. Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni!” (Flp. 4:4) Kwa nini ni jambo la maana kwa Wakristo kutimiza utumishi wao kwa Yehova wakiwa na shangwe? Kwa sababu ya suala ambalo Shetani alitokeza kuhusiana na enzi kuu ya Yehova. Shetani anadai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Mungu kwa kupenda na kutoka moyoni. (Ayu. 1:9-11) Ikiwa tungemtumikia Yehova bila shangwe ili kutimiza wajibu tu, dhabihu yetu ya sifa haingekuwa kamili. Kwa hiyo, tunajitahidi kutii himizo hili la mtunga-zaburi: “Mtumikieni Yehova kwa kushangilia. Njooni mbele zake kwa vigelegele vya shangwe.” (Zab. 100:2) Utumishi unaotolewa kwa moyo wenye shangwe, na kwa kupenda unamletea Mungu utukufu.

      12, 13. Tunaweza kufanya nini ili kushinda hisia zisizofaa?

      12 Kwa kweli, nyakati nyingine, hata watumishi wa Yehova waliojitoa kwake wanavunjika moyo na wanapambana ili kudumisha mtazamo mzuri. (Flp. 2:25-30) Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia nyakati kama hizo? Andiko la Waefeso 5:18, 19 linasema hivi: “Endeleeni kujazwa na roho, mkijisemesha kwa zaburi na sifa kwa Mungu na nyimbo za kiroho, mkiimba na kupiga muziki katika mioyo yenu kwa Yehova.” Tunaweza kutumia jinsi gani shauri hilo?

      13 Tunapolemewa na hisia zisizofaa, tunaweza kumsihi Yehova katika sala na kujitahidi kutafakari juu ya mambo yaliyo mazuri. (Soma Wafilipi 4:6-9.) Wengine wanaona kwamba kuimba kwa sauti ya chini nyimbo zetu za Ufalme zilizorekodiwa kunawachangamsha na kuwafanya wafikiri kwa njia nzuri. Ndugu mmoja ambaye alipambana na jaribu ambalo mara nyingi lilimwacha katika hali ya kufadhaika na kuvunjika moyo, anakumbuka hivi: “Zaidi ya kusali kwa ukawaida kutoka moyoni, nilishika akilini maneno ya nyimbo chache za Ufalme. Kuimba nikiwa peke yangu kimyakimya au kwa sauti nyimbo hizo nzuri sana za kumsifu Yehova kuliniletea amani moyoni. Pia, kitabu Mkaribie Yehova kilitolewa wakati huohuo. Nilikisoma chote mara mbili mwaka uliofuata. Kilikuwa kama mafuta yenye kutuliza moyoni mwangu. Ninajua Yehova alibariki jitihada zangu.”

      “Kifungo Chenye Kuunganisha cha Amani”

      14. Amani inayotokezwa na roho takatifu inatokeza jambo gani la pekee?

      14 Katika makusanyiko yetu ya kimataifa, wajumbe wenye malezi mbalimbali wanafurahia kushirikiana na ndugu na dada zao Wakristo. Ushirika kama huo wenye kufurahisha unaonyesha amani ambayo watu wa Mungu wanafurahia leo, yaani, umoja wa ulimwenguni pote. Mara nyingi watazamaji wanashangaa wanapoona watu ambao wanatazamia wawe maadui ‘wakijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.’ (Efe. 4:3) Kwa kweli umoja huo ni wa pekee kwa sababu ya mambo ambayo wengi wao wamelazimika kushinda.

      15, 16. (a) Petro alikuwa na malezi gani, na malezi yake yalimletea tatizo gani? (b) Yehova alimsaidia Petro jinsi gani kurekebisha mtazamo wake?

      15 Si jambo rahisi kuwaunganisha watu wa malezi mbalimbali. Ili tuelewe vizuri mambo tunayohitaji kushinda ili kuwa na umoja huo, acheni tuchunguze mfano wa mtume Petro katika karne ya kwanza. Mtazamo wake kuwaelekea Watu wa Mataifa wasiotahiriwa unaweza kuonekana katika maneno yake yafuatayo: “Ninyi mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kujiunga na mtu wa jamii nyingine au kumkaribia; na bado Mungu amenionyesha sipaswi kumwita mtu yeyote kuwa najisi au si safi.” (Mdo. 10:24-29; 11:1-3) Akifuata maoni yaliyokuwa yameenea wakati huo, inaonekana kwamba tangu utotoni Petro aliamini kwamba Sheria ilimlazimisha kuwapenda Wayahudi wenzake tu. Huenda Petro alifikiri kwamba ni jambo la kawaida kabisa kuwaona Watu wa Mataifa kuwa maadui ambao walipaswa kuchukiwa.b

      16 Hebu wazia jinsi Petro alivyohisi vibaya alipokuwa akiingia ndani ya nyumba ya Kornelio. Je, mtu aliyekuwa hapo zamani na maoni yasiyofaa kuhusu Watu wa Mataifa ‘angeunganishwa kwa upatano’ pamoja nao katika “kifungo chenye kuunganisha cha amani”? (Efe. 4:3, 16) Ndiyo, kwa kuwa siku chache mapema, roho ya Mungu ilikuwa imefungua moyo wa Petro, ikamwezesha kuanza kurekebisha mtazamo wake na kushinda maoni yake ya ubaguzi. Kupitia maono, Yehova alimwonyesha Petro wazi kwamba maoni ya Mungu kuhusu watu hayaamuliwi na jamii au taifa lake. (Mdo. 10:10-15) Hivyo, Petro alimwambia Kornelio hivi: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Petro alibadilika, na akaungana kikweli na “ushirika mzima wa akina ndugu.”—1 Pet. 2:17.

      17. Kwa nini umoja ambao watu wa Mungu wanafurahia ni wa pekee?

      17 Kisa cha Petro kinatusaidia kuthamini mabadiliko makubwa ambayo yanafanyika kati ya watu wa Mungu leo. (Soma Isaya 2:3, 4.) Mamilioni ya watu “kutoka mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” wamerekebisha njia yao ya kufikiri ili kuipatanisha na “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Ufu. 7:9; Rom. 12:2) Zamani, wengi wa watu hao waliongozwa na chuki, uadui, na migawanyiko ya ulimwengu wa Shetani. Lakini kwa kujifunza Neno la Mungu na kwa msaada wa roho takatifu, wamejifunza ‘kufuatilia mambo yanayofanya kuwe na amani.’ (Rom. 14:19) Umoja huo unamletea Mungu sifa.

      18, 19. (a) Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani amani na umoja wa kutaniko? (b) Tutazungumzia nini katika habari inayofuata?

      18 Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani amani na umoja wa watu wa Mungu? Makutaniko mengi yana watu kutoka nchi za kigeni. Huenda wengine wakawa na desturi tofauti au hawazungumzi lugha yetu vizuri. Je, tunajitahidi kuwajua? Neno la Mungu linatutia moyo tufanye hivyo. Akiliandikia kutaniko la Roma, ambalo lilikuwa na waamini Wayahudi na Watu wa Mataifa, Paulo alisema hivi: “Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi, kwa kusudi la kumpa Mungu utukufu.” (Rom. 15:7) Je, kuna mtu yeyote katika kutaniko lenu ambaye unaweza kujitahidi kumjua vizuri zaidi?

      19 Tunaweza kufanya jambo gani lingine ili kuruhusu roho takatifu ifanye kazi katika maisha yetu? Habari inayofuata itajibu swali hilo tunapozungumzia sifa zinazobaki za tunda la roho.

      [Maelezo ya Chini]

      a Tunda ambalo Yesu alitaja linatia ndani ‘tunda la roho’ na “tunda la midomo” ambalo Wakristo wanamtolea Mungu kupitia kazi ya kuhubiri Ufalme.—Ebr. 13:15.

      b Andiko la Mambo ya Walawi 19:18 linasema hivi: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” Viongozi wa dini ya Kiyahudi waliamini kwamba maneno “wana wa watu wako” na “mwenzako” yaliwahusu Wayahudi tu. Sheria iliwaagiza Waisraeli wajitenge na mataifa mengine. Hata hivyo, sheria haikuunga mkono maoni yaliyoenezwa na viongozi wa kidini wa karne ya kwanza, ya kwamba watu wote ambao hawakuwa Wayahudi walikuwa maadui na hivyo walipaswa kuchukiwa wakiwa mtu mmoja-mmoja.

  • Je, Unaruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Aprili 15
    • Je, Unaruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?

      “Roho yako ni nzuri; na iniongoze katika nchi ya unyoofu.”—ZAB. 143:10.

      1, 2. (a) Taja pindi fulani ambazo Yehova alitumia roho takatifu kuwasaidia watumishi wake. (b) Je, roho takatifu inafanya kazi katika pindi za pekee tu? Eleza.

      NI JAMBO gani linalokuja akilini unapofikiria jinsi roho takatifu inavyofanya kazi? Je, unafikiria matendo yenye nguvu ya Gideoni na Samsoni? (Amu. 6:33, 34; 15:14, 15) Labda unafikiria ujasiri wa Wakristo wa mapema au utulivu wa Stefano aliposimama mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 4:31; 6:15) Namna gani shangwe nyingi ambayo tunaiona leo kwenye makusanyiko yetu ya kimataifa, utimilifu wa ndugu zetu ambao wamefungwa gerezani kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote, na ongezeko kubwa la kazi ya kuhubiri? Mifano hiyo yote inaonyesha waziwazi jinsi roho takatifu inavyofanya kazi.

      2 Je, roho takatifu inatenda kazi katika pindi za pekee au chini ya hali fulani tu zisizo za kawaida? Hapana. Neno la Mungu linasema kwamba Wakristo ‘wanatembea kwa roho,’ ‘wanaongozwa na roho,’ na ‘wanaishi kwa roho.’ (Gal. 5:16, 18, 25) Maneno yote hayo yanaonyesha kwamba roho takatifu inaweza kuendelea kuwa na uvutano katika maisha yetu. Kila siku, tunapaswa kumsihi Yehova aongoze njia yetu ya kufikiri, kusema, na kutenda akitumia roho yake takatifu. (Soma Zaburi 143:10.) Tunapoiruhusu roho hiyo itende kazi kwa uhuru katika maisha yetu, itatokeza ndani yetu tunda ambalo linawaburudisha wengine na hilo linamletea Mungu sifa.

      3. (a) Kwa nini tunahitaji kuongozwa na roho takatifu? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia?

      3 Kwa nini ni jambo la maana tuongozwe na roho takatifu? Kwa sababu kuna nguvu nyingine ambayo inataka kututawala, nguvu inayopingana na utendaji wa roho takatifu. Katika Maandiko, nguvu hiyo inaitwa “mwili,” yaani, mielekeo mibaya ya mwili wetu wenye dhambi, urithi wa kutokamilika ambao tumepokea tukiwa wazao wa Adamu. (Soma Wagalatia 5:17.) Ni nini basi kinachohusika katika kuiruhusu roho ya Mungu ituongoze? Je, kuna hatua fulani zinazofaa ambazo tunaweza kuchukua ili kupinga uvutano mbaya wa mwili wetu wenye dhambi? Acheni tuchunguze maulizo au maswali hayo tunapozungumzia sifa sita zinazobaki za ‘tunda la roho,’ yaani, “ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.”—Gal. 5:22, 23.

      Sifa ya Upole na Ustahimilivu Zinaendeleza Amani Katika Kutaniko

      4. Sifa ya upole na ustahimilivu zinasaidia jinsi gani kuleta amani katika kutaniko?

      4 Soma Wakolosai 3:12, 13. Katika kutaniko, sifa ya upole na ustahimilivu zinaenda sambamba ili kuendeleza amani. Sifa hizo mbili za tunda la roho zinatusaidia kuwatendea wengine kwa fadhili, kubaki watulivu tunapochokozwa, na kuepuka kulipiza kisasi wakati wengine wanaposema au kututendea mambo mabaya. Tukikosana na Mkristo mwenzetu, kuwa na ustahimilivu, au subira, kutatusaidia tusiache kushirikiana na ndugu au dada yetu na badala yake kufanya yote tunayoweza ili kurudisha amani. Je, kweli sifa ya upole na ustahimilivu zinahitajiwa katika kutaniko? Ndiyo, kwa sababu sisi sote si wakamilifu.

      5. Ni jambo gani lililotokea kati ya Paulo na Barnaba, na hilo linaonyesha nini?

      5 Fikiria jambo lililotokea kati ya Paulo na Barnaba. Walikuwa wametumika bega kwa bega kwa miaka mingi ili kueneza habari njema. Kila mmoja wao alikuwa na sifa nzuri. Hata hivyo, pindi moja, ‘kulitokea hasira kali kati yao, hivi kwamba wakatengana.’ (Mdo. 15:36-39) Tukio hilo linaonyesha kwamba hata watumishi waliojitoa kabisa kwa Mungu, wanakosa kuelewana nyakati fulani. Ikiwa Mkristo anakosa kuelewana na mwamini mwenzake, anaweza kufanya nini ili kuzuia hali hiyo isiwe mbaya zaidi na kusababisha ugomvi ambao unaweza kufanya uhusiano wao uharibike kabisa?

      6, 7. (a) Ni shauri gani la Kimaandiko tunaloweza kufuata kabla mazungumzo pamoja na mwamini mwenzetu hayajageuka na kuwa ugomvi mkali? (b) Kuna faida gani za ‘kuwa mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu’?

      6 Maneno “kukatokea hasira kali,” yanaonyesha kwamba Paulo na Barnaba walikosana kwa ghafula na vibaya sana. Mkristo akigundua kwamba anapandwa na hasira anapozungumzia jambo fulani na mwamini mwenzake, ni jambo la hekima kutii shauri la Yakobo 1:19, 20: “Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu; kwa maana ghadhabu ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” Ikitegemea hali, Mkristo huyo anaweza kujaribu kubadili mazungumzo, au kuzungumzia jambo hilo wakati mwingine, au anaweza kuomba kuondoka kabla mazungumzo hayajageuka na kuwa ugomvi mkali.—Met. 12:16; 17:14; 29:11.

      7 Kuna faida gani za kufuata shauri hilo? Kwa kungoja hasira itulie, kusali kuhusu jambo hilo, na kwa kufikiria njia nzuri zaidi ya kujibu, Mkristo anaruhusu roho ya Mungu imwongoze. (Met. 15:1, 28) Chini ya mwongozo wa roho ya Mungu, anaweza kuonyesha upole na ustahimilivu. Hivyo, anakuwa tayari zaidi kutii shauri la Waefeso 4:26, 29: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi . . . Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” Kwa kweli, tunapovaa upole na ustahimilivu, tunachangia amani na umoja wa kutaniko.

      Burudisha Familia Yako kwa Fadhili na Wema

      8, 9. Fadhili na wema ni nini, na sifa hizo zina matokeo gani katika mazingira ya familia?

      8 Soma Waefeso 4:31, 32; 5:8, 9. Fadhili na wema zinaburudisha kama upepo mtulivu na kinywaji baridi katika siku yenye joto. Sifa hizo zinachangia mazingira mazuri katika familia. Fadhili ni sifa yenye kuvutia ambayo inatokana na kupendezwa kikweli na wengine, na kuonyesha hivyo kwa matendo yenye faida na maneno yenye ufikirio. Wema, kama fadhili, ni sifa yenye kujenga ambayo inaonyeshwa kwa matendo yanayowafaidi wengine. Inaonyeshwa kwa kuwa na roho ya ukarimu. (Mdo. 9:36, 39; 16:14, 15) Lakini wema unatia ndani jambo lingine zaidi.

      9 Wema ni kuwa na maadili au mwenendo bora. Unatia ndani si yale tu tunayofanya, bali jambo la maana hata zaidi, jinsi tulivyo. Fikiria mwanamke anayetayarisha tunda kwa ajili ya familia yake, anapolikata anachunguza kila kipande ili kuhakikisha kwamba ni tamu na limeiva lote, na halina kasoro ndani au nje. Vivyo hivyo, wema unaotokezwa na roho takatifu unaongoza kila sehemu ya maisha ya Mkristo.

      10. Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuwasaidia washiriki wa familia wasitawishe tunda la roho?

      10 Katika nyumba ya Kikristo, ni nini kinachoweza kuwasaidia washiriki wa familia kutendeana kwa fadhili na wema? Ujuzi sahihi wa Neno la Mungu unatimiza sehemu ya maana. (Kol. 3:9, 10) Vichwa fulani vya familia wanaamua kujifunza pia kuhusu tunda la roho wakati wa jioni yao ya Ibada ya Familia kila juma. Si vigumu kujifunza kuhusu tunda la roho. Kwa kutumia vifaa vya kufanyia utafiti vinavyopatikana katika lugha yenu, chagueni habari kuhusu kila sifa ya tunda la roho. Mnaweza kuzungumzia mafungu machache kila juma, huku mkitumia majuma fulani kuzungumzia kila sifa. Mnapojifunza habari hizo, someni na kuzungumzia maandiko ambayo hayajanukuliwa. Zungumzieni njia za kutumia mambo mnayojifunza, na msali ili Yehova abariki jitihada zenu. (1 Tim. 4:15; 1 Yoh. 5:14, 15) Je, kweli funzo kama hilo linaweza kuwasaidia washiriki wa familia kutendeana kwa njia bora zaidi?

      11, 12. Familia mbili za Kikristo zilifaidika jinsi gani kwa kujifunza pamoja kuhusu fadhili?

      11 Wenzi wa ndoa vijana ambao walitaka kufanikiwa katika ndoa yao waliamua kujifunza kwa undani kuhusu tunda la roho. Wamefaidika jinsi gani? Mke anaeleza: “Kujifunza kwamba sifa ya fadhili inatia ndani uaminifu na ushikamanifu kumetusaidia kutendeana kwa njia nzuri zaidi mpaka leo. Tumejifunza kukubali maoni ya mwingine na pia kusameheana. Na tumejifunza pia kusema ‘asante’ na ‘pole’ inapofaa.”

      12 Wenzi wengine wa ndoa Wakristo, ambao walikuwa na matatizo ya ndoa, walitambua kwamba hawakutendeana kwa fadhili katika uhusiano wao. Waliamua kujifunza pamoja kuhusu fadhili. Matokeo yalikuwa nini? Mume anakumbuka: “Kujifunza sifa ya fadhili kulitusaidia kuona uhitaji wa kuaminiana na kukazia fikira sifa nzuri za mwingine badala ya kuona kwamba ana nia mbaya. Kila mmoja wetu alianza kupendezwa zaidi na mahitaji ya mwenzake. Kuwa mwenye fadhili kulitia ndani kumwomba mke wangu aeleze kwa uhuru maoni yake bila kukasirishwa na mambo aliyosema. Hilo lilimaanisha kwamba nilihitaji kuacha kuwa mwenye kiburi. Tulipoanza kutendeana kwa fadhili katika ndoa yetu, tuliacha hatua kwa hatua tabia ya kujitetea. Tulijihisi huru kwelikweli.” Je, familia yenu itafaidika kwa kujifunza kuhusu tunda la roho?

      Onyesha Imani Unapokuwa Faraghani

      13. Tunapaswa kulinda hali yetu ya kiroho kutokana na hatari gani?

      13 Wakristo wanahitaji kuruhusu roho ya Mungu iwaongoze hadharani na faraghani. Leo katika ulimwengu wa Shetani, picha chafu sana na vitumbuizo vyenye upotovu vimeenea kotekote. Hilo linahatarisha hali yetu ya kiroho. Mkristo anapaswa kufanya nini? Neno la Mungu linatushauri hivi: “Ondoeni uchafu wote na jambo lile lenye kuzidi, yaani, ubaya, na pokeeni kwa upole upandwaji wa neno lile linaloweza kuokoa nafsi zenu.” (Yak. 1:21) Acheni tuchunguze jinsi imani, ambayo ni sifa nyingine ya tunda la roho, inavyoweza kutusaidia kubaki safi mbele za Yehova.

      14. Kukosa imani kunaweza jinsi gani kumwongoza mtu kwenye mwenendo mbaya?

      14 Imani inamaanisha hasa kumwona Yehova Mungu kuwa halisi. Ikiwa Mungu si halisi kwetu, tunaweza kuanguka kwa urahisi kwenye mwenendo mbaya. Fikiria jambo ambalo liliwapata watu wa Mungu katika nyakati za kale. Yehova alimfunulia nabii Ezekieli kwamba mambo yenye kuchukiza yalikuwa yakifanywa faraghani, alisema: “Je, umeona, Ee mwana wa binadamu, mambo ambayo wazee wa nyumba ya Israeli wanafanya katika giza, kila mmoja katika vyumba vya ndani vya sanamu yake ya kuchongwa? Kwa maana wanasema, ‘Yehova hatuoni. Yehova ameiacha nchi hii.’” (Eze. 8:12) Je, umeona kile ambacho kilisababisha tatizo hilo? Hawakuamini kwamba Yehova alijua mambo waliyokuwa wakifanya. Yehova hakuwa halisi kwao.

      15. Imani yenye nguvu katika Yehova inatulinda jinsi gani?

      15 Kinyume na hilo, ona mfano wa Yosefu. Ingawa alikuwa mbali na familia yake na watu wake, Yosefu alikataa kufanya uasherati na mke wa Potifa. Kwa nini? Alisema hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwa. 39:7-9) Ndiyo, Yehova alikuwa halisi kwa Yosefu. Ikiwa Mungu ni halisi kwetu hatutatazama vitumbuizo vichafu au kufanya jambo lingine lolote faraghani ambalo tunajua linamchukiza Mungu. Tutaazimia kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Nitatembea katika utimilifu wa moyo wangu ndani ya nyumba yangu. Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.”—Zab. 101:2, 3.

      Linda Moyo Wako kwa Kuwa na Sifa ya Kujizuia

      16, 17. (a) Kama inavyoelezwa katika kitabu cha Methali, “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” alianguka jinsi gani katika dhambi? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 26, jambo kama hilo linaweza kutokea jinsi gani leo bila kujali umri wa mtu?

      16 Kujizuia au kujidhibiti, sifa ya mwisho ya tunda la roho, inatuwezesha kukataa mambo ambayo Mungu analaumu. Inaweza kutusaidia kulinda moyo wetu. (Met. 4:23) Fikiria hali inayoelezwa katika andiko la Methali 7:6-23, kuhusu jinsi “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” anavyoanguka katika kishawishi cha kahaba mmoja. Ananaswa na mtego baada ya ‘kupita barabarani, karibu na pembeni kwa mwanamke huyo.’ Labda alikuwa akitanga-tanga karibu na nyumba ya kahaba huyo kwa udadisi tu. Kwa ghafula, anakosa kutambua kwamba anaongozwa katika njia ya upumbavu na kwamba “nafsi yake mwenyewe inahusika.”

      17 Kijana huyo angeepuka jinsi gani kosa hilo hatari? Kwa kutii onyo hili: “Usipotee na kuingia katika barabara zake.” (Met. 7:25) Hapa tunaweza kujifunza somo fulani: Ikiwa tunataka roho ya Mungu ituongoze, tunahitaji kuepuka kujiingiza wenyewe katika hali zenye kushawishi. Njia moja ambayo mtu anaweza kutanga-tanga kwenye njia ya upumbavu ya yule “kijana ambaye amepungukiwa moyoni” ni kwa kutazama-tazama bila kusudi vituo mbalimbali vya televisheni au kwenda huku na huku kwenye Intaneti. Iwe mtu anakusudia au hakusudii, anaweza kuona kwa ghafula picha zinazoamsha hamu ya ngono. Hatua kwa hatua anaweza kusitawisha zoea chafu la kutazama ponografia (picha au habari za ngono), na hivyo kuharibu kabisa dhamiri yake na uhusiano wake pamoja na Mungu. Anaweza pia kupoteza uhai wake.—Soma Waroma 8:5-8.

      18. Mkristo anaweza kuchukua hatua gani ili kulinda moyo wake, na hatua hizo zinahusiana jinsi gani na kujizuia?

      18 Bila shaka, tunaweza na tunapaswa kuonyesha sifa ya kujizuia kwa kuchukua hatua papo hapo picha chafu inapotokea kwa ghafula. Lakini itakuwa vizuri zaidi tukiepuka hali hiyo mapema! (Met. 22:3) Kujizuia kunatia ndani kujilinda kwa njia mbalimbali zinazofaa na kushikamana na njia hizo. Kwa mfano, kuweka kompyuta mahali panapoonekana wazi kunaweza kutulinda. Wengine wanaona ni vizuri kutumia kompyuta au kutazama televisheni ikiwa tu kuna watu wengine nyumbani. Wengine wameamua kutotumia Intaneti. (Soma Mathayo 5:27-30.) Basi na tuchukue hatua zozote za lazima ili kujilinda wenyewe na kuilinda familia yetu ili tuweze kumwabudu Yehova tukiwa na “dhamiri njema na kutokana na imani bila unafiki.”—1 Tim. 1:5.

      19. Kuna faida gani za kuiruhusu roho takatifu ituongoze?

      19 Tunda linalotokezwa kupitia utendaji wa roho takatifu linaleta faida nyingi. Sifa ya upole na ustahimilivu zinachangia amani katika kutaniko. Fadhili na wema zinaendeleza furaha katika familia. Kuwa na imani na kujizuia kunatusaidia kubaki karibu na Yehova na kuwa safi mbele zake. Zaidi ya hayo, andiko la Wagalatia 6:8 linatuhakikishia hivi: “Yeye anayepanda kwa roho atavuna uzima wa milele kutokana na roho.” Ndiyo, kwa msingi wa fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo, Yehova atatumia roho takatifu ili kuwapa uzima wa milele wale ambao wanaruhusu roho takatifu iwaongoze.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki