-
Kwa Nini Wengi Hawana TumainiAmkeni!—2008 | Mei
-
-
Kwa Nini Wengi Hawana Tumaini
Mambo yanayotendeka ulimwenguni pote yanafanya watu waogope wakati ujao. Majiji mengi sasa yana kamera za kuwachunguza raia. Kwa sababu ya kuogopa ugaidi, viwanja vingi vya ndege vyenye shughuli nyingi vimekaribia kufanana na kambi za kijeshi. Idadi inayozidi kuongezeka ya wezi na watu wanaowatendea watoto vibaya kingono hutumia Intaneti kuvizia watu wasiojua makusudio yao mabaya. Matatizo ya kimazingira kama vile uchafuzi, ukataji miti, kutoweka kwa viumbe, na kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni kunatishia uhai katika sayari yetu.
INGAWA matatizo hayo hayangewaziwa makumi ya miaka iliyopita, leo yanawahangaisha watu ulimwenguni pote. Kwa sababu nzuri, watu wengi hujiuliza ulimwengu huu unapatwa na nini na maisha yao na ya watoto wao yatakuwaje wakati ujao. Je, utafika wakati ambapo watu wataogopa kupanda basi, gari-moshi, au ndege? Bei ya vitu ikizidi kupanda na mali-asili zikizidi kutumiwa vibaya, je, vizazi vijavyo vitapata matibabu bora, chakula kizuri, na vyanzo vya nishati vya kutosha?
“Wakati ujao unatisha kwelikweli,” alisema waziri wa afya wa Kanada alipozungumza kuhusu gharama za matibabu zinazozidi kuongezeka. Pia, watu wana wasiwasi mwingi kuhusu vyakula na vyanzo vya nishati. Kwa nini? Ili kupunguza matumizi ya mafuta yanayochimbuliwa ardhini, nchi fulani zinatumia pesa nyingi ili kutokeza mafuta kutokana na vyanzo vingine, kama vile ethanoli, inayotokana na mimea. Hivyo, kwa mara ya kwanza katika historia, ardhi haipaswi tu kuwaandalia wanadamu chakula bali pia kutokeza mafuta kwa ajili ya magari. Tayari watu wanakabili tatizo la kuongezeka kwa bei ya chakula.
Wakati huohuo, pengo kati ya matajiri na maskini linazidi kuongezeka na kuzidisha mizozo ya kijamii. “Katika miaka kumi ya kwanza katika karne hii ya 21, maendeleo makubwa katika hali njema ya binadamu na vilevile hali mbaya sana ya umaskini,” inasema ripoti ya Shirika la Afya Ulimwenguni. “Katika baadhi ya nchi maskini sana, watu wanaishi umepungua nusu ya miaka ambayo watu katika nchi tajiri sana wanaishi.” Hali hiyo inasababishwa hasa na magonjwa na msukosuko wa kijamii na kiuchumi katika nchi zenye serikali zisizo imara.
Zaidi ya hayo, unapofikiria tisho la kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni kunakoweza kusababisha kuenea kwa majangwa na hali mbaya sana ya hewa, si ajabu kwamba watu wengi wanaochunguza hali ya ulimwengu wana wasiwasi kuhusu wakati ujao. Gazeti Bulletin of the Atomic Scientists, ambalo linarekebisha Saa ya Maangamizi, lilizungumzia hofu ya wakati ujao mbaya “huku wanasayansi wakiendelea kuchunguza jinsi [kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni] kunavyoathiri mifumo ya ikolojia ya Dunia.”
Je, wakati wetu ujao ni mbaya kadiri hiyo? Je, tumaini letu pekee la wakati ujao mzuri linategemea viongozi wa kibiashara, kisiasa, kidini, na kisayansi? Watu fulani wanauliza, ‘Tuna tumaini gani lingine? Tulijiletea matatizo hayo sisi wenyewe; nasi tunapaswa kuyasuluhisha.’ Wengine wanahisi kwamba wanadamu hawawezi kusuluhisha matatizo hayo na ni Mungu tu anayeweza kutuletea wakati ujao salama. Ikiwa ndivyo ilivyo, tuna uhakika gani kwamba Mungu anatujali na atatuzuia tusijiangamize wenyewe? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Je, tumaini letu pekee la wakati ujao mzuri linategemea viongozi wa kibiashara, kisiasa, kidini, na kisayansi?
-
-
Je, Wanadamu Wanaweza Kutuhakikishia Wakati Ujao Wenye Furaha?Amkeni!—2008 | Mei
-
-
Je, Wanadamu Wanaweza Kutuhakikishia Wakati Ujao Wenye Furaha?
Umetoka tu kuhamia nyumba imara na maridadi iliyojengwa kwa matofali. Umekuwa ukitamani sana nyumba kama hiyo. Unatazamia wakati ujao mzuri! Lakini baada ya miaka michache tu, nyumba hiyo inaharibika na lazima ibomolewe. Unahuzunika sana. Lakini si wewe tu. Nyumba nyingine katika eneo lenu zimeanza kuharibika pia. Uchunguzi unaonyesha kwamba nyumba hizo zimeharibika kwa sababu ya kasoro za ujenzi na matofali mabovu.
KAMA nyumba hiyo, ulimwengu unakabili matatizo makubwa. Licha ya majaribio mengi ya kisiasa na kijamii, na maendeleo makubwa sana katika sayansi na tekinolojia, inaonekana kwamba misingi ya jamii inabomoka. Katika nchi kadhaa, uasi-sheria na machafuko ni mambo ya kawaida. Je, hali mbaya za wanadamu zitawasukuma watatue matatizo yao, waanzishe serikali nzuri hatimaye? Fikiria yale ambayo watu fulani wamesema kuhusu historia ya wanadamu.
“Tumejaribu Kila Kitu”
Katika jitihada za kufanya ulimwengu uwe mahali bora zaidi, wasomi mbalimbali kuanzia mwanafalsafa Mgiriki Plato mpaka mwanafalsafa wa kisiasa na msoshalisti Mjerumani Karl Marx wamependekeza mifumo mingi ya utawala. Kumekuwa na matokeo gani? Makala katika gazeti New Statesman ilisema hivi: “Hatujamaliza umaskini wala kutokeza amani ulimwenguni. Badala yake, inaonekana kwamba tumepata matokeo yaliyo kinyume. Si kwamba hatujajaribu. Tumejaribu kila kitu kuanzia serikali ambazo hudhibiti uchumi mpaka zile ambazo hukubali soko huru; kuanzia Ushirika wa Mataifa hadi kurundika silaha za nyuklia. Tumepigana ‘vita [vingi] vya kukomesha vita’ hivi kwamba tunaamini hatuwezi kukomesha vita, na ni kana kwamba majiji yetu yanashambuliwa.” Makala hiyo iliongeza hivi: “Tulianza karne [ya 20] tukiwa na matumaini makubwa kwamba wanasayansi wangetuokoa na tunaimalizia bila kuamini hata neno moja wanalosema.”
Katika 2001, Eric Hobsbawm, profesa mstaafu wa uchumi na historia ya kijamii katika Chuo Kikuu cha London aliandika kwamba serikali za wanadamu “zinakabili kipindi ambapo utendaji wa wanadamu umeharibu sana mazingira na dunia yote.” Suluhisho la matatizo hayo “halitapendwa na wengi. Katika nchi nyingi, watu wanapenda vitu ambavyo kwa njia ya moja kwa moja au njia nyingine vinadhuru mazingira. Hali hiyo inaonyesha kwamba demokrasia haitafanikiwa wala hakuna tumaini kwa dunia.”
Akitazamia kwamba hivi karibuni wanadamu watapatwa na matatizo makubwa, Stephen Hawking, mwanasayansi na mwandishi aliuliza hivi: “Katika ulimwengu uliovurugika kisiasa, kijamii, na kimazingira, wanadamu wanaweza kuendeleaje kuishi kwa miaka mingine 100?”
Kwa Nini Wanadamu Hawajafaulu?
Biblia tu ndiyo inayotoa maelezo yenye kuridhisha kuhusu kwa nini wanadamu wameshindwa kabisa kujitawala. Kwanza, Biblia inatueleza waziwazi hali ya wanadamu. Kwa mfano, fikiria kweli hizi nne za msingi.
Sisi sote si wakamilifu. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kama tu vile matofali mabovu yanavyoweza kufanya jengo liharibike hatua kwa hatua na kuporomoka, ndivyo kutokamilika kwa wanadamu kulikorithiwa kunavyoweza kudhoofisha jamii. Kutokamilika kunaonyeshwa kupitia mambo kama vile mielekeo ya ufisadi, ukosefu wa unyoofu, pupa, na kutumia mamlaka vibaya. Hayo si mambo mapya. Miaka 3,000 hivi iliyopita, mwandikaji mwenye hekima wa Biblia aliandika: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.
Viongozi wa serikali na mahakimu wanakubali kwamba hatujakamilika na tuna udhaifu, nao hujaribu kukabiliana na hali hizo kwa kutunga sheria nyingi. Lakini wanajua kwamba hawawezi kuweka sheria za kuwalazimisha watu wapendane au watii sheria kwa hiari.
Kifo kinatupata. “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake [au nguvu za uhai] hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:3, 4) Mfalme Sulemani wa Israeli la kale ambaye anasemekana kuwa mtawala mwenye hekima zaidi, aliona matokeo ya kazi yake ngumu kuwa ubatili. Aliandika hivi: “Nami, naam mimi, nikachukia kazi yangu yote iliyo ngumu ambayo niliifanya kwa bidii chini ya jua, ambayo ningemwachia mtu ambaye angekuja baada yangu. Na ni nani anayejua kama atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo, atachukua usimamizi wa kazi yangu yote iliyo ngumu . . . Hilo pia ni ubatili.”—Mhubiri 2:18, 19.
Hatuna uwezo wa kujitawala kwa mafanikio. “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Hata ikiwa wanadamu wangekuwa wakamilifu, Biblia inafundisha kwamba kulingana na kusudi la awali la Mungu, Mungu hakuwapa haki ya kujitawala wala uwezo wa kufanya hivyo kwa mafanikio. Kwa mfano, kwa nini watu huudhiwa na wazo la mwanadamu mwingine au kikundi cha watu kuwaambia wanachopaswa kufanya au kuwawekea viwango vya maadili? Ni kwa sababu tuliumbwa ili tupate mwongozo kutoka kwa mamlaka ya juu zaidi. Mamlaka hiyo ni Mungu.—Isaya 33:22; Matendo 4:19; 5:29.
Wanadamu wanaongozwa na mtawala asiyeonekana. “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu”—Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Ikiwa wakurugenzi wa kampuni fulani ni wafisadi sana na hawawezi kuchukuliwa hatua yoyote, mfanyakazi wa kawaida angefanya nini ili kurekebisha hali? Hawezi kufanya mengi. Ndivyo ilivyo kuhusu kutatua matatizo yanayosababishwa na watawala wasioonekana wa ulimwengu huu, yaani, roho waovu wanaofanya kazi chini ya uongozi wa Shetani. Biblia inawataja watawala hao kuwa “serikali,” “mamlaka,” “watawala wa ulimwengu wa giza hili,” na “majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:12.
Hata hivyo, Biblia haifunui tu udhaifu wa wanadamu na watawala wa ulimwengu wasioonekana. Inatupa pia habari njema kuhusu suluhisho la matatizo yetu yote na hivyo kutupa msingi imara wa kuwa na tumaini.
Muumba Wetu Atatuokoa!
Ikiwa tungeachwa bila msaada wowote hatungeweza kusuluhisha matatizo hayo. Hata mwanadamu mwenye akili nyingi zaidi, mwenye nguvu nyingi zaidi, au tajiri zaidi hana uwezo wa kubadili yoyote kati ya mambo manne yaliyotajwa katika makala hii.a Lakini kama tutakavyoona katika makala inayofuata, Muumba wetu hajatusahau wala kutuacha. Kwa kweli, akiwa mwenye haki ya kutawala, ataondoa kipingamizi chochote kinachozuia tusiwe na furaha. (1 Yohana 4:8) Isitoshe, atafanya hivyo hivi karibuni. Tunajuaje?
Kama ilivyoelezwa katika toleo la mwezi jana la gazeti hili, matukio ya ulimwengu na hali katika jamii zinaonyesha wazi kwamba tuko ndani kabisa ya “siku za mwisho” za ulimwengu huu. (2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:3-7) Ulimwengu huu hautaharibiwa kwa maangamizi makubwa ya nyuklia au kwa kugongana na sayari ndogo au kwa njia nyingine ambayo itawaharibu watu wazuri na wabaya bila kubagua. Badala yake, Mungu ndiye atakayeleta uharibifu huo kwa kuwaangamiza waovu, kutia ndani wale wanaosisitiza wanadamu waendelee kutawala. (Zaburi 37:10; 2 Petro 3:7) Wakati huohuo, Mungu atakomesha matatizo yote yanayosababishwa na wale wanaompinga.b—2 Wathesalonike 1:6-9.
Baada ya hayo, Muumba atatatua matatizo yetu ya utawala kwa kuukabidhi utawala unaoitwa “ufalme wa Mungu” mamlaka kamili juu ya dunia. (Luka 4:43) Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, serikali hiyo ya ulimwengu wote italeta wakati ujao mzuri ajabu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Je, Ufadhili Ndilo Suluhisho?” kwenye ukurasa wa 19.
b Swali “Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?” linajibiwa kwenye ukurasa wa 106 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
“MATOFALI MABOVU” YA JAMII YA WANADAMU
◼ Sisi sote si wakamilifu.
◼ Kifo kinatupata.
◼ Hatuna uwezo wa kujitawala kwa mafanikio.
◼ Wanadamu wanaongozwa na mtawala asiyeonekana.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
WANADAMU HAWATAIHARIBU DUNIA!
Kusudi la Muumba la kuifanya dunia iwe makao salama yenye amani kwa ajili ya wanadamu wanaomwogopa Mungu linaungwa mkono na Biblia. Fikiria maandiko yafuatayo.
“Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”—Zaburi 104:5.
“Umeiweka dunia imara, ili ipate kuendelea kusimama.”—Zaburi 119:90.
“Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Mhubiri 1:4.
“Dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.
“[Yehova ndiye] Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
-
-
Wakati Ujao Salama Chini ya Utawala wa MunguAmkeni!—2008 | Mei
-
-
Wakati Ujao Salama Chini ya Utawala wa Mungu
HIVI karibuni hatutahitaji kuhangaikia wakati ujao kwa kuwa Mungu atachukua mamlaka juu ya sayari yetu Dunia kwa kusimamisha serikali yake, inayoitwa Ufalme wa Mungu. Yesu Kristo alikuwa na taraja hilo zuri akilini alipowafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
Ufalme wa Mungu hautashirikiana na viongozi wa kisiasa wala kuwatumia kutawala. Badala yake, utaondoa kila sehemu ya utawala wa kibinadamu, kama inavyoonyeshwa katika unabii ufuatao wa Danieli kuhusu “siku za mwisho,” kipindi ambacho tunaishi sasa. (2 Timotheo 3:1) “Katika siku za wafalme hao, Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [za wanadamu], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Maneno hayo hayawafariji au kuwapa tumaini watu wanaopendelea utawala wa wanadamu, lakini kwa wote wanaotamani kuwa chini ya enzi kuu ya Mungu kupitia Ufalme wake, maneno hayo yanatoa ahadi nzuri ajabu.
Wakati Ujao Mzuri!
Ufalme wa Mungu utakapotawala juu ya dunia yote, raia wake hawatagawanywa na siasa, jamii, dini, au mipaka ya kitaifa. Badala yake, watakuwa undugu wa ulimwenguni pote uliounganishwa na kweli ya kiroho na upendo wa kweli. (Yohana 13:34, 35; 17:3, 17) Naam, chini ya utawala wa Ufalme, “mwadilifu atachipuka,” na kutakuwa na “wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.”—Zaburi 72:7.
Mbali na mambo hayo, Ufalme wa Mungu utawainua wanadamu wanaojitiisha wafikie ukamilifu wa akili na mwili, utaondoa magonjwa yote, mateso, na kifo. (Ufunuo 21:3, 4) Matokeo yatakuwa nini? Sayari yetu itakuwa paradiso na hivyo kusudi la awali la Mungu lililotajwa huko Edeni litatimizwa.a—Mwanzo 1:28.
Habari Njema ya Kweli
Alipokuwa akitoa ishara yenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitia ndani jambo fulani muhimu sana. (Mathayo 24:3-7) Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
Kulingana na mapenzi ya Mungu, mnamo 2007 Mashahidi wa Yehova milioni saba hivi katika nchi 236 waliwahubiria majirani wao ujumbe wa Ufalme, na kwa shangwe wakatumia zaidi ya saa bilioni 1.4 katika kazi hiyo. Kwa nini Mashahidi wanasadiki kabisa ahadi zilizo katika Biblia? Jibu ni rahisi. Kama makala inayofuata itakavyoonyesha, nyakati zote Mungu hutimiza neno lake.—Waroma 3:4.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Maoni ya Biblia: Je, Dunia Itakuwa Paradiso?” kwenye ukurasa wa 10.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Biblia inasema kwamba kutakuwa na “wingi wa amani”
-
-
Wakati Ujao Unaotegemeka!Amkeni!—2008 | Mei
-
-
Wakati Ujao Unaotegemeka!
Umefika katika njia panda. Ishara moja inasema, “Wategemee wanadamu na ahadi zao.” Nyingine inasema, “Mtegemee Mungu na Ufalme wake.” Utafuata njia gani?
NI JAMBO la hekima kumtegemea Mungu. “Mtu anayenisikiliza,” Mungu anasema, “atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.” (Methali 1:33) Tunamsikiliza Muumba wetu kwa kufuata mafundisho yaliyo katika Biblia, tukitambua kwamba yanategemeka. (2 Timotheo 3:16) Je, kuna sababu nzuri za kuyategemea? Bila shaka! Kwa mfano, kama tulivyoona katika makala iliyotangulia katika mfululizo huu, Biblia pekee ndiyo inayoeleza kwa usahihi kwa nini wanadamu hawawezi kujitawala kwa mafanikio. Je, hukubali kwamba yale ambayo Biblia inasema yanapatana na mambo hakika?
Usahihi huohuo unaonekana pia katika unabii wa Biblia. Kwa mfano, Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na hali mbaya sana ambazo zingeonyesha kwamba hizi ndizo “siku za mwisho.” Tunaweza kujionea hali hizo. (Mathayo 24:3-7; 2 Timotheo 3:1-5) Biblia hata ilitabiri kwamba wanadamu wangeiharibu sayari yetu. Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ lasema andiko la Ufunuo 11:18.
Maneno hayo yalipoandikwa miaka 2,000 hivi iliyopita, uchafuzi wa hewa, bahari, na ardhi; kuongezeka kwa kiwango cha joto ulimwenguni; na kutoweka kwa jamii za viumbe ambako kumesababishwa na wanadamu, ni baadhi ya mambo ambayo hayangewaziwa hata kidogo. Lakini sivyo ilivyo leo! Ndiyo, Mungu hawezi kusema uwongo. Kila kitu kilichoandikwa katika Neno lake hutimizwa nyakati zote.a (Tito 1:2; Waebrania 6:18) Kwa kweli, Mungu anahusianisha jina lake na kutimizwa kwa neno lake.
Jina Unaloweza Kulitegemea!
Kama vile sahihi inavyohalalisha hundi, ndivyo jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, linavyoandaa uhakikisho kuhusu ahadi zote zilizorekodiwa katika Biblia.b Mwandikaji wa Biblia ambaye Mungu alimjali kwa upendo mara nyingi alisema hivi: “Tumelitegemea jina lake takatifu.”—Zaburi 33:21; 34:4, 6.
Likihusianisha jina la Mungu na sifa yake akiwa baba mwenye kujali, Methali 18:10 linasema: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.” Hali kadhalika, Waroma 10:13 linasema: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” Bila shaka, jina la kibinafsi la Mungu si hirizi inayomlinda mtu asipatwe na mabaya. Badala yake, Mungu mwenyewe ndiye anayewaokoa, na wale wanaomwitia kama andiko hilo linavyosema wanafanya hivyo kwa sababu wanamtegemea kabisa, wakijua vizuri kwamba kila mara yeye hutimiza ahadi zake. Zaburi 91:14 inasema hivi: “Kwa sababu ameweka upendo wake juu yangu [Yehova], mimi nitamwokoa pia. Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.”
Jiulize, ‘Ninamtegemea nani—Mungu au mwanadamu?’ Mashahidi wa Yehova wamechagua kumtegemea Mungu na Ufalme wake, si kwa sababu tu wanaamini mambo bila msingi au bila kufikiri, lakini kwa sababu imani yao inategemea usadikisho wenye nguvu unaotokana na ujuzi sahihi wa Biblia. (Waebrania 11:1; 1 Yohana 4:1) Kwa sababu hiyo, hawaogopi wakati ujao bali ‘wanashangilia katika tumaini’ lililowekwa mbele yao. Wanakutia moyo uwe na tumaini jangavu kama lao.—Waroma 12:12.
[Maelezo ya Chini]
a Ona toleo la pekee la Novemba (Mwezi wa 11) 2007 la gazeti hili, linalozungumzia kwa urefu swali “Je, Unaweza Kuitegemea Biblia?”
b Ona sanduku “Jina na Uhakikisho.”
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Kama vile sahihi inavyohalalisha hundi, ndivyo jina la Mungu linavyoandaa uhakikisho kuhusu ahadi zote zilizo katika Biblia
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
JINA NA UHAKIKISHO
Jina la Mungu, Yehova, si kibandiko tu.c Jinsi gani? Jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Kwa maneno rahisi, Mungu ana upendo, nguvu, na hekima ya kuwa chochote anachohitaji kuwa ili kutimiza kusudi na neno lake. Kwa mfano, anaweza kuwa Mwokozi wa waadilifu, Mwangamizaji wa waovu, Msikiaji wa sala, au Baba mwenye upendo—chochote anachochagua kuwa.
“Mimi ni Mungu,” asema Yehova, “Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho . . . Yeye anayesema, ‘Shauri langu mwenyewe litasimama, na kila jambo ambalo ni mapenzi yangu nitafanya.’” (Isaya 46:9, 10) Kwa kuwa nyakati zote Mungu hushikamana na ahadi yake na kwa kuwa jina lake, au sifa yake, inahusika, Neno lake lililoandikwa litatimia hakika. “Mungu si mwanadamu kwamba aseme uwongo.”—Hesabu 23:19.
[Maelezo ya Chini]
c Jina Yehova linatofautiana kabisa na majina ya cheo kama vile Mweza-Yote, Muumba, Mungu, na Bwana. Jina hilo linapatikana mara elfu saba hivi katika maandishi ya awali ya Biblia Takatifu. Mungu alijipa jina hilo. Andiko la Kutoka 3:15 linasema hivi: “Jehova . . . hili ndilo jina langu milele.”—The Old Testament in Swahili (Mombasa).
-