Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wakristo Wote wa Kweli Ni Waeneza-evanjeli
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Januari 1
    • Wakristo Wote wa Kweli Ni Waeneza-evanjeli

      “Mwimbieni Yehova, libarikini jina lake. Tangazeni habari njema za wokovu wake siku kwa siku.”—ZABURI 96:2, NW.

      1. Ni habari gani njema ambazo watu wanahitaji kusikia, nao Mashahidi wa Yehova wameweka mfano gani mzuri wa kueneza habari hizo?

      KATIKA ulimwengu ambapo misiba hutokea kila siku, inafariji sana kujua kwamba kama isemavyo Biblia, vita, uhalifu, njaa, na uonevu vitakoma hivi karibuni. (Zaburi 46:9; 72:3, 7, 8, 12, 16) Je, kwa kweli hizo si habari njema ambazo kila mtu anahitaji kusikia? Mashahidi wa Yehova wanasadiki hivyo. Wanajulikana kila mahali kuwa watu ambao huhubiri “habari njema ya mambo mema.” (Isaya 52:7) Ni kweli kwamba Mashahidi wengi wamenyanyaswa kwa sababu ya azimio lao la kuhubiri habari njema. Lakini wanajali sana masilahi ya watu. Nao Mashahidi wamejipatia sifa nzuri kama nini ya kuwa watu wenye bidii na wavumilivu!

      2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova ni wenye bidii hivyo?

      2 Bidii ya Mashahidi wa Yehova leo ni sawa na ya Wakristo wa karne ya kwanza. Gazeti la Katoliki L’Osservatore Romano lilisema hivi kwa usahihi kuwahusu: “Wakristo wa karne ya kwanza, walipobatizwa tu, waliona kuwa wana wajibu wa kueneza Injili. Watumwa pia walieneza Injili.” Kwa nini Mashahidi wa Yehova ni wenye bidii kama Wakristo wa mapema? Kwanza, ni kwa sababu habari njema wanazotangaza zinatoka kwa Yehova Mungu. Ndiyo sababu wana bidii hiyo. Mahubiri yao yanapatana na maneno haya ya mtunga-zaburi: “Mwimbieni Yehova, libarikini jina lake. Tangazeni habari njema za wokovu wake siku kwa siku.”—Zaburi 96:2, NW.

      3. (a) Ni sababu gani ya pili inayofanya Mashahidi wa Yehova wawe wenye bidii? (b) “Wokovu wa [Mungu]” unahusisha nini?

      3 Maneno ya mtunga-zaburi yatukumbusha sababu ya pili inayofanya Mashahidi wa Yehova wawe wenye bidii. Ujumbe wao ni ujumbe wa wokovu. Watu fulani hufanya kazi zinazohusiana na mambo ya kitiba, kijamii, kiuchumi, au nyanja nyinginezo ili kuboresha maisha ya wanadamu wenzao, na wanahitaji kupongezwa kwa jitihada hizo. Lakini jambo lolote ambalo mwanadamu anaweza kumfanyia mwenzake haliwezi kuwa na manufaa sana linapolinganishwa na “wokovu wa [Mungu].” Kupitia Yesu Kristo, Yehova atawaokoa wanyenyekevu kutokana na dhambi, magonjwa, na kifo. Wale watakaonufaika wataishi milele! (Yohana 3:16, 36; Ufunuo 21:3, 4) Leo, wokovu u miongoni mwa “kazi za ajabu” ambazo Wakristo hutangaza wanapoitikia maneno haya: “Wahubirini mataifa habari za utukufu [wa Mungu] na watu wote habari za maajabu yake [“kazi zake za ajabu,” NW]. Kwa kuwa BWANA ni mkuu mwenye kusifiwa sana. Na wa kuhofiwa kuliko miungu yote.”—Zaburi 96:3, 4.

      Kielelezo cha Bwana-Mkubwa

      4-6. (a) Ni sababu gani ya tatu inayowafanya Mashahidi wa Yehova wawe wenye bidii? (b) Yesu alionyeshaje bidii katika kazi ya kuhubiri habari njema?

      4 Mashahidi wa Yehova ni wenye bidii kwa sababu hii ya tatu. Wanafuata kielelezo cha Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Mwanadamu huyo mkamilifu alikubali kwa moyo wote mgawo wa ‘kuhubiri wanyenyekevu habari njema.’ (Isaya 61:1; Luka 4:17-21) Hivyo, akawa mweneza-evanjeli, mtangazaji wa habari njema. Alisafiri Galilaya na Yudea kote, ‘akihubiri habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 4:23) Na kwa sababu alijua kwamba wengi wangekubali habari njema, aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.”—Mathayo 9:37, 38.

      5 Kupatana na sala yake, Yesu aliwazoeza wengine kuwa waeneza-evanjeli. Baada ya hapo, alituma mitume wake na kuwaambia: “Mwendapo, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbingu umekaribia.’” Je, haingefaa zaidi kama wangeanzisha miradi ambayo ingepunguza matatizo ya kijamii yaliyokuweko wakati huo? Au je, haingefaa kama wangejihusisha na siasa ili kuzuia ufisadi uliokuwa umeenea sana wakati huo? La. Badala yake, Yesu aliweka kiwango ambacho Wakristo wote walio waeneza-evanjeli wangefuata alipowaambia wafuasi wake hivi: “Mwendapo, hubirini.”—Mathayo 10:5-7.

      6 Baadaye, Yesu alituma kikundi kingine cha wanafunzi wakatangaze: “Ufalme wa Mungu umekuja karibu.” Waliporudi ili kueleza mafanikio waliyopata katika kueneza evanjeli, Yesu alifurahi sana. Alisali hivi: “Nakusifu hadharani wewe, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umeficha mambo hayo kwa uangalifu kutoka kwa wenye hekima na walio na akili, nawe umeyafunua kwa vitoto.” (Luka 10:1, 8, 9, 21) Wanafunzi wa Yesu ambao hapo awali walikuwa wavuvi wenye bidii, wakulima, na kadhalika, walikuwa kama watoto wakilinganishwa na viongozi wa kidini walioelimika sana wa taifa hilo. Lakini wanafunzi walizoezwa kutangaza habari njema zilizo bora kabisa.

      7. Baada ya Yesu kupaa mbinguni, wafuasi wake waliwahubiria nani kwanza habari njema?

      7 Baada ya Yesu kupaa mbinguni, wafuasi wake waliendelea kutangaza habari njema za wokovu. (Matendo 2:21, 38-40) Waliwahubiria nani kwanza? Je, walienda kwa mataifa ambao hawakumjua Mungu? La, waliwahubiria kwanza Waisraeli, watu ambao walimjua Yehova kwa miaka zaidi ya 1,500. Je, walikuwa na haki ya kuhubiri katika nchi ambayo Yehova alikuwa tayari akiabudiwa? Ndiyo. Yesu aliwaambia: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Waisraeli walihitaji kusikia habari njema kama tu taifa lingine lolote.

      8. Mashahidi wa Yehova leo huwaigaje wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza?

      8 Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova leo huhubiri duniani pote. Wanashirikiana na malaika aliyeonwa na Yohana ambaye “alikuwa na habari njema idumuyo milele ili aitangaze kuwa taarifa za mteremo kwa wale wakaao juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufunuo 14:6) Katika mwaka wa 2001, walihubiri katika nchi na maeneo 235, kutia ndani maeneo yanayojulikana kuwa ya Kikristo. Je, Mashahidi wa Yehova wanakosea kwa kuhubiri katika maeneo ambako tayari kuna makanisa ya Jumuiya ya Wakristo? Wengine wanasema ni kosa na hata huenda wakaona uenezaji-evanjeli huo kuwa “kuiba washiriki wao.” Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hukumbuka jinsi Yesu alivyohisi kuhusu Wayahudi wa kawaida walioishi wakati wake. Ingawa tayari walikuwa na ukuhani, Yesu hakusita kuwatangazia habari njema. ‘Alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Mashahidi wa Yehova wanapopata watu wa kawaida ambao hawamjui Yehova na Ufalme wake, je, wasite kuwahubiria habari njema kwa sababu dini fulani inadai kuwa hao ni wafuasi wake? Kwa kufuata kielelezo cha mitume wa Yesu, twajibu la. Lazima habari njema zihubiriwe “katika mataifa yote,” bila kubagua.—Marko 13:10.

      Wakristo Wote wa Mapema Walikuwa Waeneza-Evanjeli

      9. Katika karne ya kwanza, ni nani katika kutaniko la Kikristo walioshiriki kuhubiri?

      9 Ni nani walioshiriki kuhubiri katika karne ya kwanza? Kuna mambo yanayothibitisha kwamba Wakristo wote walikuwa waeneza-evanjeli. Mwandishi W. S. Williams asema: ‘Kuna ushuhuda unaoonyesha kwamba Wakristo wote katika Kanisa la mapema walihubiri injili.’ Biblia husema hivi kuhusu mambo yaliyotukia siku ya Pentekoste 33 W.K.: “Nao wote [wanaume na wanawake] wakawa wenye kujazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwaruhusu kufanya tamko.” Waeneza-evanjeli walitia ndani wanaume na wanawake, wachanga kwa wakubwa, watumwa na watu huru. (Matendo 1:14; 2:1, 4, 17, 18; Yoeli 2:28, 29; Wagalatia 3:28) Wakristo wengi walipolazimika kukimbia Yerusalemu kwa sababu ya mnyanyaso, “wale waliokuwa wametawanywa walipita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:4) Evanjeli ilienezwa na watu wote “waliokuwa wametawanywa,” wala si na watu wachache tu waliokuwa wamewekwa rasmi.

      10. Ni utume gani wenye sehemu mbili uliotimizwa kabla ya uharibifu wa mfumo wa Kiyahudi?

      10 Waliendelea kufanya hivyo katika miaka ya mapema. Yesu alitabiri hivi: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Maneno hayo yalipotimizwa katika karne ya kwanza, habari njema zilihubiriwa kotekote kabla majeshi ya Roma hayajaharibu mfumo wa kidini na wa kisiasa wa Wayahudi. (Wakolosai 1:23) Isitoshe, wafuasi wote wa Yesu walitii amri yake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Wakristo wa mapema hawakuwashauri wanyenyekevu wamwamini Yesu na kuwaacha tu wamtumikie Mungu bila mwongozo wowote, kama wafanyavyo wahubiri wengine wa siku hizi. Badala yake, waliwafundisha wawe wanafunzi wa Yesu, wakawapanga kuwa makutaniko, na kuwazoeza ili wao pia wahubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Matendo 14:21-23) Mashahidi wa Yehova leo hufuata kielelezo hicho.

      11. Ni nani leo wanaoshiriki kuwatangazia wanadamu habari njema zilizo bora kabisa?

      11 Kwa kufuata kielelezo kilichowekwa katika karne ya kwanza na Paulo, Barnaba, na wengineo, Mashahidi wengi wa Yehova wamejitoa kutumikia wakiwa mishonari katika nchi za kigeni. Kazi yao imekuwa yenye kunufaisha kwelikweli, kwa kuwa hawajihusishi na siasa au kukwepa kwa vyovyote utume wa kuhubiri habari njema. Wametii amri ya Yesu: “Mwendapo, hubirini.” Hata hivyo, wengi wa Mashahidi wa Yehova si mishonari wanaotumikia katika nchi za kigeni. Wengi wao hujipatia riziki kwa kufanya kazi ya kimwili, na wengine bado wako shuleni. Wengine wanalea watoto. Lakini Mashahidi wote huwahubiria wengine habari njema ambazo wamejifunza. Wachanga kwa wazee, wanaume kwa wanawake, hukubali kwa furaha himizo hili la Biblia: “Lihubiri neno, lifanye kwa hima katika majira yenye kufaa, katika majira yenye taabu.” (2 Timotheo 4:2) Kama watangulizi wao wa karne ya kwanza, wanaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Matendo 5:42) Wanawatangazia wanadamu habari njema zilizo bora kabisa.

      Kugeuza Watu Imani au Kueneza Evanjeli?

      12. Kugeuza watu imani kunaonwaje?

      12 Siku hizi, watu fulani husema kwamba ni hatari kugeuza watu imani. Hati moja iliyochapishwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni inazungumza juu ya “dhambi ya kugeuza watu imani.” Kwa nini? Kichapo Catholic World Report chasema: ‘Kwa sababu ya malalamiko mengi ya Kanisa la Othodoksi, kugeuza watu imani kumeanza kuonwa kama jambo linalofanywa kwa nguvu.’

      13. Ni mifano gani inayoonyesha kugeuza watu imani ambako ni hatari?

      13 Je, ni hatari kugeuza watu imani? Ndiyo. Yesu alisema kwamba kugeuza watu imani kulikofanywa na waandishi na Mafarisayo kulikuwa hatari kwa wageuzwa-imani. (Mathayo 23:15) Bila shaka ni kosa ‘kugeuza watu imani kwa nguvu.’ Kwa mfano, kulingana na mwanahistoria Yosefu, wakati Mmakabayo John Hyrcanus alipowatiisha Waidumea, “aliwaruhusu wabaki katika nchi yao maadamu wangetahiriwa na wangekuwa tayari kutii sheria za Wayahudi.” Ikiwa Waidumea wangeishi chini ya utawala wa Wayahudi, wangelazimika kufuata dini ya Wayahudi. Wanahistoria wanatuambia kwamba katika karne ya nane W.K., Charlemagne aliwashinda wapagani wa Saxon wa kaskazini mwa Ulaya na kuwalazimisha kikatili wageuze imani yao.a Hata hivyo, je, kweli Waidumea au watu wa Saxon walikuwa wamegeuza imani yao kwa unyofu? Kwa mfano, je, Mfalme Herode wa Idumea alikuwa mwaminifu kwa Sheria ya Musa iliyopuliziwa wakati alipojaribu kuua kitoto Yesu?—Mathayo 2:1-18.

      14. Baadhi ya mishonari wa Jumuiya ya Wakristo hulazimishaje watu wageuze imani yao?

      14 Je, watu hulazimishwa kugeuza imani leo? Wengine hulazimishwa kufanya hivyo. Imeripotiwa kwamba mishonari fulani wa Jumuiya ya Wakristo hutoa msaada wa masomo kwa wageuzwa-imani wakasomee ng’ambo. Au huenda wakamlazimisha mkimbizi mwenye njaa asikilize mahubiri yao ndiposa wampe chakula. Kulingana na taarifa iliyotolewa katika mwaka wa 1992 kwenye kusanyiko la makasisi wa Kanisa la Othodoksi, “mara nyingine watu hugeuzwa imani kwa kushawishiwa kwamba watapewa vitu vya kimwili na nyakati nyingine kwa kutumia nguvu.”

      15. Je, Mashahidi wa Yehova hugeuza watu imani kama wengine wafanyavyo siku hizi? Eleza.

      15 Ni kosa kulazimisha watu wabadili dini. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova hawafanyi hivyo.b Kwa hiyo, hawageuzi watu imani kama wengine wafanyavyo siku hizi. Badala yake, kama Wakristo wa karne ya kwanza, wao huhubiria kila mtu habari njema. Mtu yeyote anayekubali habari njema kwa kupenda, hutiwa moyo atwae ujuzi zaidi kwa kujifunza Biblia. Watu hao wenye kupendezwa hujifunza kuwa na imani inayotegemea kabisa ujuzi sahihi wa Biblia kuhusu Mungu na makusudi yake. Hivyo, wanaliitia jina la Mungu, Yehova, ili kupata wokovu. (Waroma 10:13, 14, 17) Ni juu yao kuamua kama watakubali au watakataa habari njema. Hawalazimishwi. Kama watu wangelazimishwa, kugeuza watu imani hakungekuwa na maana yoyote. Ili mtu akubaliwe na Mungu, lazima ibada yake itoke moyoni.—Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; 10:12.

      Kueneza Evanjeli Katika Nyakati za Kisasa

      16. Kazi ya kueneza evanjeli ya Mashahidi wa Yehova imekuaje katika nyakati za kisasa?

      16 Katika nyakati za kisasa, Mashahidi wa Yehova wamehubiri habari njema za Ufalme ili kutimiza kikamili andiko la Mathayo 24:14. Wametumia hasa gazeti Mnara wa Mlinzi kueneza evanjeli.c Katika mwaka wa 1879, matoleo ya kwanza ya Mnara wa Mlinzi yalipochapishwa, kulikuwa na jumla ya nakala zipatazo 6,000 katika lugha moja. Katika mwaka wa 2001, miaka zaidi ya 122 baadaye, jumla ya nakala 23,042,000 zilizochapishwa katika lugha 141. Ongezeko hilo linaenda sambamba na ukuzi katika kazi ya kueneza evanjeli inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. Linganisha saa elfu chache zilizotumiwa katika kazi ya kueneza evanjeli katika karne ya 19 na saa 1,169,082,225 zilizotumiwa katika kazi ya kuhubiri mnamo mwaka wa 2001. Fikiria wastani wa mafunzo ya Biblia 4,921,702 yaliyoongozwa kila mwezi bila malipo. Walitimiza kazi nyingi tena bora kama nini! Nayo ilifanywa na wahubiri wa Ufalme wapatao 6,117,666.

      17. (a) Ni miungu gani isiyo ya kweli inayoabudiwa leo? (b) Kila mtu anahitaji kujua nini bila kujali lugha yake, taifa, au cheo chake katika jamii?

      17 Mtunga-zaburi asema hivi: “Miungu yote ya watu si kitu, lakini BWANA ndiye aliyezifanya mbingu.” (Zaburi 96:5) Katika ulimwengu wa sasa, utukuzo wa taifa, ishara za kitaifa, watu mashuhuri, vitu vya kimwili, na hata mali zimeabudiwa. (Mathayo 6:24; Waefeso 5:5; Wakolosai 3:5) Mohandas K. Gandhi alisema hivi wakati mmoja: “Mimi ninaamini kabisa kwamba . . . leo bara Ulaya lina Wakristo wa jina tu. Kwa kweli bara hilo linaabudu mali.” Ukweli ni kwamba lazima habari njema zihubiriwe kila mahali. Kila mtu pasipo kujali lugha yake, taifa, au cheo chake katika jamii, anahitaji kumjua Yehova na makusudi yake. Laiti wote wangekubali maneno haya ya mtunga-zaburi: “Mpeni BWANA utukufu na nguvu. Mpeni BWANA utukufu wa jina lake”! (Zaburi 96:7, 8) Mashahidi wa Yehova husaidia wengine wajifunze kuhusu Yehova ili wampe utukufu kwa njia inayofaa. Na wale wanaosikiliza wananufaika sana. Wanapata manufaa gani? Habari hiyo itazungumziwa katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kulingana na The Catholic Encyclopedia, wakati wa Marekebisho Makuu ya Kidini, kulazimisha watu wakubali dini fulani kulionyeshwa na wito huu wa Kilatini: Cuius regio, illius et religio (Kwa msingi, wito huo wamaanisha: “Yeyote yule anayetawala nchi ndiye anayeamua dini itakayofuatwa.”)

      b Kwenye mkutano wa Tume ya Kimataifa ya Uhuru wa Kidini uliofanywa Marekani Novemba 16, 2000, mshiriki mmoja alitaja tofauti iliyopo kati ya watu wanaojaribu kulazimisha wengine wabadili imani yao na kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova. Ilisemekana kwamba Mashahidi wa Yehova wanapowahubiria watu, wanafanya hivyo kwa njia ambayo mtu anaweza kusema “Mimi sipendezwi” na afunge mlango.

      c Jina kamili la gazeti hili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.

  • Manufaa za Habari Njema
    Mnara wa Mlinzi—2002 | Januari 1
    • Manufaa za Habari Njema

      “BWANA amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo . . .kuwafariji wote waliao.”—ISAYA 61:1, 2.

      1, 2. (a) Yesu alijifunua kuwa nani, na jinsi gani? (b) Ni mambo gani yenye kunufaisha yaliyotokana na habari njema alizotangaza Yesu?

      SIKU moja ya Sabato mapema katika huduma yake, Yesu alikuwa katika sinagogi huko Nazareti. Kulingana na simulizi hilo, “a[li]pewa hati-kunjo ya nabii Isaya, naye akafungua hiyo hati-kunjo na kupata mahali palipokuwa pameandikwa: ‘Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kutangaza habari njema.’” Yesu aliendelea kusoma ujumbe huo wa kiunabii. Kisha akaketi na kusema: “Leo andiko hili ambalo mmetoka tu kusikia limetimizwa.”—Luka 4:16-21.

      2 Kwa kusema hivyo, Yesu alijitambulisha kuwa mweneza-evanjeli aliyetabiriwa, mhubiri wa habari njema na mfariji. (Mathayo 4:23) Naye alitangaza habari njema kama nini! Aliwaambia hivi wasikilizaji wake: “Mimi ni nuru ya ulimwengu. Yeye anifuataye mimi hatatembea kwa vyovyote katika giza, bali atakuwa na nuru ya uhai.” (Yohana 8:12) Pia alisema: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, nyinyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtajua kweli, na kweli itawaweka nyinyi huru.” (Yohana 8:31, 32) Naam, Yesu alikuwa na “semi za uhai udumuo milele.” (Yohana 6:68, 69) Nuru, uhai, uhuru—kwa kweli hayo ni mambo yenye kunufaisha tunayopaswa kuyathamini sana!

      3. Ni habari gani njema zilizohubiriwa na wanafunzi wa Yesu?

      3 Baada ya Pentekoste 33 W.K., wanafunzi waliendelea na kazi ya Yesu ya kueneza evanjeli. Walihubiri “habari njema [hii] ya ufalme” kwa Waisraeli na kwa watu wa mataifa. (Mathayo 24:14; Matendo 15:7; Waroma 1:16) Wale walioitikia walipata kumjua Yehova Mungu. Walikombolewa kutoka katika utumwa wa kidini na kuwa sehemu ya taifa jipya la kiroho, “Israeli wa Mungu,” ambalo washiriki wake wanatarajia kutawala milele mbinguni pamoja na Bwana wao, Yesu Kristo. (Wagalatia 5:1; 6:16; Waefeso 3:5-7; Wakolosai 1:4, 5; Ufunuo 22:5) Hilo lilikuwa jambo lenye kunufaisha kwelikweli!

      Kueneza Evanjeli Leo

      4. Kazi ya kuhubiri habari njema inatimizwaje leo?

      4 Leo, Wakristo watiwa-mafuta, wanaoungwa mkono na “umati mkubwa” unaoongezeka wa “kondoo wengine,” wanaendelea kutimiza kazi ya kiunabii ambayo hapo awali ilikuwa imepewa Yesu. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Kwa sababu hiyo, habari njema zinahubiriwa kwa kiwango kikubwa zaidi ya wakati mwingine wowote. Katika nchi na maeneo 235, Mashahidi wa Yehova wameenda ‘kuwahubiri wanyenyekevu habari njema; kuwaganga waliovunjika moyo, na kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. Kutangaza mwaka wa BWANA uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao.’ (Isaya 61:1, 2) Kwa hiyo, kazi ya Kikristo ya kueneza evanjeli inazidi kunufaisha wengi na kuwapa faraja ya kweli “wale walio katika namna yoyote ya dhiki.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

      5. Mashahidi wa Yehova hutofautianaje na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kuhusiana na kuhubiri habari njema?

      5 Ni kweli kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo hutegemeza njia mbalimbali za kueneza evanjeli. Makanisa mengi hutuma mishonari wakageuze watu imani katika nchi nyingine. Kwa mfano, The Orthodox Christian Mission Center Magazine linaripoti juu ya kazi ya mishonari wa Othodoksi nchini Madagaska, kusini mwa Afrika, Tanzania, na Zimbabwe. Hata hivyo, katika Kanisa la Othodoksi, kama ilivyo katika makanisa mengine ya Jumuiya ya Wakristo, waumini wengi hawashiriki kazi hiyo. Kinyume cha hilo, Mashahidi wote wa Yehova waliojiweka wakfu hujitahidi kueneza evanjeli. Wanatambua kwamba kutangaza habari njema ni njia moja ya kuthibitisha kwamba imani yao ni ya kweli. Paulo alisema: “Kwa moyo mtu hudhihirisha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.” Kwa kweli, imani isiyomchochea mtu kutenda, imekufa.—Waroma 10:10; Yakobo 2:17.

      Habari Njema Zinazoleta Manufaa za Milele

      6. Ni habari njema gani zinazohubiriwa leo?

      6 Mashahidi wa Yehova huhubiri habari bora zaidi ya zote. Wao hufungua Biblia zao na kuwaonyesha watu wenye kupendezwa kwamba Yesu alitoa uhai wake kuwa dhabihu ili kuwawezesha wanadamu wamkaribie Mungu, wasamehewe dhambi, na wawe na tumaini la kupata uhai udumuo milele. (Yohana 3:16; 2 Wakorintho 5:18, 19) Wanatangaza kwamba Ufalme wa Mungu umesimamishwa mbinguni chini ya Yesu Kristo, Mfalme aliyetiwa mafuta, na kwamba hivi karibuni ufalme huo utaondoa uovu duniani na kusimamia kazi ya kurudisha Paradiso. (Ufunuo 11:15; 21:3, 4) Wanatimiza unabii wa Isaya wanapowaambia jirani zao kwamba sasa ndio “mwaka wa BWANA uliokubaliwa” ambapo wanadamu bado wanaweza kuitikia habari njema. Pia wanatoa onyo kwamba hivi karibuni “siku ya kisasi cha Mungu wetu” itakuja wakati Yehova atakapowaharibu wakosaji wasiotubu.—Zaburi 37:9-11.

      7. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wameungana, na kwa nini wana muungano huo?

      7 Hizi ndizo habari njema pekee zinazoweza kuleta manufaa za milele katika ulimwengu unaokumbwa na misiba mingi. Wale wanaozikubali hujiunga na udugu wa Kikristo ulioungana wa ulimwenguni pote, usio na migawanyiko ya kitaifa, kikabila, au ya kiuchumi. ‘Wamejivika wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’ (Wakolosai 3:14; Yohana 15:12) Jambo hilo lilionekana mwaka jana katika nchi fulani ya Afrika. Asubuhi moja, milio ya bunduki ilisikika katika jiji kuu la nchi hiyo. Kulikuwa na jaribio la mapinduzi. Mapigano yalipogeuka na kuwa ya kikabila, familia moja ya Mashahidi ilishutumiwa kwa kuwapa hifadhi Mashahidi wenzao wa kabila tofauti. Familia hiyo ilisema hivi: “Ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoishi katika nyumba yetu.” Jambo lililokuwa muhimu kwao ni kuonyesha upendo wa Kikristo kwa kuwafariji watu waliokuwa na uhitaji bila kujali walikuwa wa kabila gani. Mtu fulani wa jamaa ambaye si Shahidi alisema: “Waumini wa dini nyingine zote waliwasaliti waumini wenzao. Mashahidi wa Yehova peke yao ndio hawakusalitiana.” Ripoti nyingi kama hizo kutoka nchi ambazo zimekumbwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe zinaonyesha kwamba kwa kweli Mashahidi wa Yehova ‘wana upendo kwa ushirika mzima wa ndugu.’—1 Petro 2:17.

      Habari Njema Hubadili Watu

      8, 9. (a) Watu wanaokubali habari njema hufanya mabadiliko gani? (b) Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba habari njema zina uwezo?

      8 Paulo alisema kwamba habari njema zinahusu “uhai wa sasa na ule utakaokuja.” (1 Timotheo 4:8) Habari njema hutoa tumaini zuri la wakati ujao na pia huboresha “uhai wa sasa.” Mashahidi wa Yehova wakiwa mtu mmoja-mmoja huongozwa na Neno la Mungu, Biblia, kupatanisha maisha yao na mapenzi ya Mungu. (Zaburi 119:101) Nyutu zao hubadilika kuwa mpya wanapositawisha sifa kama vile uadilifu na uaminifu-mshikamanifu.—Waefeso 4:24.

      9 Mfikirie Franco. Alikuwa mtu mwenye hasira. Mambo yalipoenda mrama, angepandwa na hasira na kuanza kuvunja-vunja vitu. Mke wake alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na mfano wao wa Kikristo ulimsaidia Franco hatua kwa hatua aone kwamba alipaswa kubadilika. Alijifunza Biblia nao hatimaye akaanza kudhihirisha matunda ya roho kama vile amani na kujidhibiti. (Wagalatia 5:22, 23) Alikuwa miongoni mwa watu 492 waliobatizwa nchini Ubelgiji katika mwaka wa utumishi wa 2001. Mfikirie pia Alejandro. Mwanamume huyo kijana alizoea sana kutumia dawa za kulevya hivi kwamba alianza kuishi katika sehemu ya kutupa takataka, akitafuta-tafuta vitu vyenye thamani ili aviuze na kupata pesa za kununua dawa hizo za kulevya. Alipokuwa na umri wa miaka 22, Mashahidi wa Yehova walimtia moyo Alejandro ajifunze Biblia, naye akakubali. Alisoma Biblia kila siku na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Alibadili maisha yake upesi sana hivi kwamba katika muda unaopungua miezi sita, alianza kueneza evanjeli na kuwa miongoni mwa watu 10,115 waliofanya hivyo mwaka jana nchini Panama.

      Habari Njema—Hunufaisha Wanyenyekevu

      10. Ni nani ambao hukubali habari njema, na mtazamo wao hubadilikaje?

      10 Isaya alitabiri kwamba habari njema zingehubiriwa kwa wanyenyekevu. Wanyenyekevu hao ni nani? Ni wale wanaotajwa katika kitabu cha Matendo kuwa ‘wenye mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’ (Matendo 13:48) Hao ni watu wanyenyekevu wanaopatikana katika jamii zote na ambao hukubali ujumbe wa ile kweli. Watu hao hutambua kwamba kufanya mapenzi ya Mungu huleta thawabu zisizoweza kulinganishwa na kitu chochote ulimwenguni. (1 Yohana 2:15-17) Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hufikiaje mioyo ya watu wanapofanya kazi yao ya kueneza evanjeli?

      11. Kulingana na Paulo, habari njema zapaswa kuhubiriwa jinsi gani?

      11 Fikiria kielelezo cha mtume Paulo, aliyewaandikia Wakorintho hivi: “Mimi, nilipowajia nyinyi, akina ndugu, nikiwatangazia siri ya Mungu, sikuja nikiwa na usemi wenye kupita kiasi wala wa hekima nikiwatangazia siri takatifu ya Mungu. Kwa maana niliamua kutojua kitu chochote miongoni mwenu ila Yesu Kristo, naye akiwa aliyetundikwa mtini.” (1 Wakorintho 2:1, 2) Paulo hakutaka kujionyesha kwa wasikilizaji wake kwamba alikuwa na elimu. Alifundisha kweli kutoka kwa Mungu, kweli inayopatikana katika Biblia leo. Ona pia kitia-moyo ambacho Paulo alimpa mweneza-evanjeli mwenzake, Timotheo: “Lihubiri neno, lifanye kwa hima.” (2 Timotheo 4:2) Timotheo alipaswa kulihubiri “neno,” ujumbe wa Mungu. Pia Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Fanya yote uwezayo kabisa ili ujionyeshe mwenyewe kuwa mwenye kukubaliwa na Mungu, mtenda-kazi asiye na lolote la kuaibikia, ukilitumia sawasawa neno la ile kweli.”—2 Timotheo 2:15.

      12. Mashahidi wa Yehova leo wanatii maneno ya Paulo na kufuata kielelezo chake jinsi gani?

      12 Mashahidi wa Yehova hufuata kielelezo cha Paulo, na vilevile hutii maneno aliyomwandikia Timotheo. Wao hutambua uwezo wa Neno la Mungu na kulitumia ifaavyo wanapojitahidi kuwaonyesha jirani zao maneno yanayofaa ya tumaini na faraja. (Zaburi 119:52; 2 Timotheo 3:16, 17; Waebrania 4:12) Kwa kweli wao hutumia ifaavyo vichapo vinavyotegemea Biblia ili watu wenye kupendezwa wajiongezee ujuzi wa Biblia kwa wakati wao. Lakini sikuzote wao hujitahidi kuwaonyesha watu Maandiko. Wanajua kwamba Neno la Mungu lililopuliziwa litaichochea mioyo ya wanyenyekevu. Na wanapolitumia kuhubiria watu, wanaimarisha imani yao pia.

      ‘Kufariji Wote Waliao’

      13. Katika mwaka wa 2001, ni matukio gani yaliyofanya kuwe na uhitaji mkubwa wa kuwafariji waliao?

      13 Mwaka wa 2001 ulikuwa na misiba mingi, na kwa sababu hiyo, watu wengi walihitaji faraja. Mnamo Septemba uliopita, kulitokea msiba mkubwa sana nchini Marekani, wakati magaidi waliposhambulia majengo mawili marefu yanayoitwa World Trade Center huko New York na makao makuu ya kijeshi ya Pentagon karibu na Washington, D.C. Nchi nzima ilitishwa kama nini na mashambulizi hayo! Misiba hiyo inapotokea, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kutimiza kazi yao ya kutoa ‘faraja kwa wote waliao.’ Tutaona jinsi wanavyofanya hivyo kwa kuchunguza mambo machache yaliyoonwa.

      14, 15. Katika pindi mbili tofauti, Mashahidi waliwezaje kutumia maandiko kwa njia yenye matokeo ili kufariji waliao?

      14 Shahidi mmoja ambaye ni mweneza-evanjeli wa wakati wote alimkaribia mwanamke fulani njiani na kumwuliza maoni yake kuhusu mashambulizi ya kigaidi yaliyotokea hivi karibuni. Mwanamke huyo alianza kulia. Alisema kwamba alihuzunika sana na kutamani kwamba angeweza kusaidia kwa njia fulani. Shahidi huyo alimwambia kwamba Mungu anapendezwa nasi sote, na kumsomea andiko la Isaya 61:1, 2. Mwanamke huyo alielewa maana ya maneno hayo yaliyopuliziwa na Mungu na akasema kwamba kila mtu analia. Alikubali trakti na kumwomba Shahidi huyo amtembelee nyumbani kwake.

      15 Mashahidi wawili waliokuwa wakieneza evanjeli walimkuta mwanamume mmoja aliyekuwa akifanya kazi katika kibanda chake. Walitaka kumwonyesha maneno yenye kufariji kutoka katika Maandiko kuhusiana na msiba uliotokea hivi karibuni katika majengo hayo ya WTC. Alipokubali, walimsomea andiko la 2 Wakorintho 1:3-7, linalotia ndani maneno haya: “Faraja . . . izidivyo kupitia Kristo.” Mwanamume huyo aliwashukuru jirani zake Mashahidi kwa kuwaeleza watu ujumbe wenye kufariji na kusema: “Mungu na abariki kazi nzuri mnayofanya.”

      16, 17. Ni mambo gani mawili yaliyoonwa yanayoonyesha jinsi Biblia inavyoweza kuwasaidia watu waliohuzunishwa au kufadhaishwa na misiba?

      16 Shahidi mmoja aliyekuwa akiwarudia watu wenye kupendezwa alikutana na mwana wa mwanamke fulani aliyeonyesha upendezi hapo awali. Shahidi huyo alisema kwamba alitaka kuwajulia hali jirani zake baada ya msiba uliokuwa umetokea hivi karibuni. Mwanamume huyo alishangaa kuona kwamba Shahidi huyo alitumia wakati wake kutembelea watu ili kuwajulia hali. Alisema kwamba alikuwa akifanya kazi karibu na majengo hayo ya World Trade Center wakati wa mashambulizi hayo, na aliona mambo yote yaliyotokea. Mwanamume huyo alipouliza kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka, Shahidi huyo alisoma mistari kadhaa kutoka katika Biblia, kutia ndani andiko la Zaburi 37:39, linalosema: “Wokovu wa wenye haki una BWANA; yeye ni ngome yao wakati wa taabu.” Kwa fadhili, mwanamume huyo alitaka kujua hali ya Shahidi huyo na familia yake, akamwomba arudi na kumshukuru sana kwa ziara hiyo.

      17 Mashahidi walipokuwa wakiwatembelea jirani zao, walikutana na mwanamke fulani ambaye ni miongoni mwa maelfu ya watu waliao ambao walifarijiwa na Mashahidi wa Yehova. Alikuwa amefadhaishwa sana na mambo yaliyotukia na alisikiliza waliposoma andiko la Zaburi 72:12-14: “Atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu, na damu yao ina thamani machoni pake.” Maneno hayo yalikuwa yenye maana kama nini! Mwanamke huyo aliwaomba Mashahidi wasome mistari hiyo tena na kuwakaribisha nyumbani kwake ili waendelee na mazungumzo. Mwishoni mwa mazungumzo, funzo la Biblia lilianzishwa.

      18. Shahidi mmoja alisaidiaje jirani zake alipoombwa asali kwa niaba yao?

      18 Shahidi mmoja hufanya kazi kwenye mkahawa fulani katika mtaa wa watu matajiri ambao hawakupendezwa sana na habari njema za Ufalme hapo awali. Watu hao walishtuliwa sana na mashambulizi hayo ya kigaidi. Ijumaa jioni baada ya shambulizi hilo, meneja wa mkahawa aliomba kila mtu atoke nje na kushika mishumaa, na kunyamaza kwa dakika chache ili kuwakumbuka watu waliokufa. Kwa kujali hisia zao, Shahidi huyo alienda nje na kusimama kimya kando ya njia. Meneja alijua kwamba mtu huyo alikuwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo baada ya kipindi hicho cha kutafakari kwa ukimya, alimwomba atoe sala kwa niaba ya wote. Shahidi huyo alikubali. Katika sala yake, alitaja jinsi watu wengi wanavyolia lakini akasema kwamba watu hao hawapaswi kuhuzunika pasipo tumaini lolote. Alitaja wakati ambapo vitendo vya kutisha vitakwisha na akasema kwamba wote wanaweza kumkaribia Mungu wa faraja kwa kupata ujuzi sahihi kutoka katika Biblia. Baada ya kusema “Ameni,” meneja huyo—akiwa pamoja na watu zaidi ya 60 waliokuwa nje ya mkahawa—alimfikia Shahidi huyo akamshukuru, na kumkumbatia, na kusema kwamba sala hiyo ndiyo sala bora zaidi aliyopata kusikia.

      Wananufaisha Jamii

      19. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba baadhi ya watu wanatambua viwango vya juu vya Mashahidi wa Yehova?

      19 Watu wengi wamesema kwamba siku hizi hasa katika jamii ambazo Mashahidi wa Yehova wanapatikana, wenyeji hufaidika kutokana na utendaji wao. Watu ambao wanachangia amani, unyofu, na maadili yanayofaa watakosaje kuwanufaisha wengine? Katika nchi moja huko Asia ya Kati, Mashahidi walikutana na afisa mstaafu wa lililokuwa shirika la upelelezi la serikali. Alisema kwamba wakati fulani alikuwa ametumwa kuchunguza dini mbalimbali. Alipowachunguza Mashahidi wa Yehova, alivutiwa na unyofu na mwenendo wao mzuri. Alivutiwa na imani yao thabiti na mafundisho yao yanayotegemea Maandiko. Mtu huyo alikubali kujifunza Biblia.

      20. (a) Ripoti ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova mwaka jana inaonyesha nini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba bado kuna kazi nyingi ya kufanya, nasi tunaonaje pendeleo letu la kueneza evanjeli?

      20 Tungeweza kusimulia mambo mengi yaliyoonwa, lakini kutokana na yale machache tuliyosimulia katika makala hii ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova walifanya kazi nyingi sana katika mwaka wa utumishi wa 2001.a Walizungumza na mamilioni ya watu, waliwafariji wengi waliolia, na kazi yao ya kueneza evanjeli ilikuwa na manufaa. Watu 263,431 walionyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kubatizwa. Idadi ya waeneza-evanjeli ulimwenguni pote iliongezeka kwa asilimia 1.7. Na idadi ya watu 15,374,986 waliohudhuria Ukumbusho unaofanywa kila mwaka wa kifo cha Yesu inaonyesha kwamba bado kuna kazi nyingi ya kufanya. (1 Wakorintho 11:23-26) Na tuendelee kuwatafuta wanyenyekevu wanaokubali habari njema. Maadamu mwaka wa Yehova uliokubaliwa ungalipo, na tuendelee kuwafariji “waliovunjika moyo.” Tuna kazi inayoridhisha kama nini! Bila shaka, sote twakubaliana na maneno haya ya Isaya: “Nitafurahi sana katika BWANA, nafsi yangu itashangilia katika Mungu wangu.” (Isaya 61:10) Mungu na aendelee kututumia anapotimiza maneno haya ya unabii: ‘Bwana MUNGU ataotesha haki na sifa mbele ya mataifa yote.’—Isaya 61:11.

      [Maelezo ya Chini]

      a Chati iliyo katika ukurasa wa 19 hadi 22 inaonyesha ripoti ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa utumishi wa 2001.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki