Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Thawabu Bora kwa Ajili ya Utumishi Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
    • Wakati wa miezi ya kiangazi yenye joto, tulikuwa na funzo la Biblia Jumapili alasiri, tukitumia makala ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi. Baadaye, saa mbili kamili, tulikutana sokoni Leicester kwa ajili ya hotuba ya watu wote iliyofanyika nje. Usiku mmoja watu 200 walisikiliza. Utendaji huu uliweka misingi ya makutaniko mengi ambayo sasa yako Leicester na kandokando.

  • Thawabu Bora kwa Ajili ya Utumishi Mtakatifu
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 1
    • Mkusanyiko Mkubwa Wakati wa Vita

      Vita ya ulimwengu ya pili ilizuka Septemba 1939, na kufikia mwaka wa 1941 vita ilikuwa kali zaidi. Ndege za mabomu za Ujerumani zilishambulia mchana na usiku, na umeme ulizimwa kotekote katika taifa. Chakula kilikuwa haba, na kilichopatikana kiligawanywa sawasawa. Usafiri ulikuwa mchache sana, hata kwa garimoshi. Vijapokuwa vizuizi hivyo vilivyoonekana kuwa visivyoshindwa, Septemba 3-7, 1941 tulifanya mkusanyiko wa kitaifa wa siku tano.

      Jumba la De Montfort Hall la Leicester lilichaguliwa kuwa mahali pa mkusanyiko kwa sababu jiji la Leicester liko katikati ya Uingereza. Kwa kuwa nilikuwa katika kiwanda cha mbao, niliweza kusaidia kutengeneza ishara za matangazo. Pia nilipanga usafiri wa wakusanyikaji wa mahali hapo. Kwa kununua tikiti mapema na kulipa zaidi ya bei ya kawaida, tramu za Leicester ziliendelea kusafiri hata Jumapili.

      Kwa sababu kulikuwa na vizuizi vya usafiri, tumaini letu lilikuwa kwamba labda Mashahidi 3,000 wangeweza kuja. Wazia ule msisimko wajumbe 10,000 waliposema kwamba wangekuwako! Lakini wangekaa wapi? Kwa fadhili raia wa Leicester waliwaalika wengi wakae nyumbani kwao. Kwa kuongezea, watu wapatao elfu moja walikaa katika mahema yaliyosimamishwa katika uwanja ulio kilometa tatu kutoka mahali pa mkusanyiko. Camp Gideon, kama tulivyopaita, paliamsha upendezi mkubwa katika jumuiya.

      Mahema makubwa meupe yalikodiwa ili yatumiwe kwa ajili ya idara mbalimbali za mkusanyiko na ili kuandaa mahali pa kukaa umati mkubwa uliomiminika. Ilipopambanuliwa kwamba katika mbalamwezi, mahema hayo yangelengwa na ndege za mabomu za Nazi, yalifunikwa haraka. Watu wote walihangaishwa na vita, na hasa kutoshiriki kwa Mashahidi katika vita. Mamia ya Mashahidi walikuwa gerezani wakati huo kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo wenye kutegemea Biblia.—Isaya 2:4; Yohana 17:16.

      Gazeti la habari Sunday Pictorial, la Septemba 7, 1941, liliripoti hivi: “Ni jambo lenye kushangaza kukuta watu 10,000, wengi wao vijana, wakitumia juma zima kuzungumza juu ya dini bila kutaja vita, ila tu liwe jambo lisilo muhimu.

      “Niliuliza ikiwa hao Mashahidi walikuwa na washiriki wowote Ujerumani. Ndiyo, niliambiwa, na karibu wote, wapatao 6,000, walikuwa katika kambi za mateso.”

      Huyo mwandishi wa habari aliongeza kusema hivi: “Oh, ndiyo, ni kweli kwamba askari wa Nazi ndio maadui, lakini Mashahidi wanafanya machache sana kuwahusu, ila tu kuuza trakti na kusikiliza hotuba mbalimbali.”

      Kwa ujumla maelezo ya gazeti la habari juu yetu yalikuwa hasi, na wapinzani hata waligeukia jeuri katika majaribio yasiyo na mafanikio ili kuvuruga mkusanyiko wetu. Hata hivyo, gazeti la habari Daily Mail la London lilikubali hivi, likiwa na wivu kwa kiasi fulani: “Hiyo mipango ilikuwa mitulivu, isiyojitanguliza, na yenye matokeo.”

      Tulishtakiwa kwamba tulisababisha upungufu wa ugavi wa sigareti katika jiji hilo. Lakini gazeti la habari The Daily Mail lilieleza hivi: “Wala Leicester wala Tobacco Controller hawawezi kulalamika kwamba Mashahidi wanamaliza ugavi wa sigareti za Leicester. Wao hawavuti sigareti.” Pia, malalamiko ya kwamba wakaaji wenyeji walinyanganywa chakula na Mashahidi yaliondolewa ilipoelezwa kwamba walikuwa wameleta sehemu kubwa ya ugavi wao wa chakula walipokuja. Kwa hakika, mwishoni mwa mkusanyiko, mikate 150 yenye uzani wa kilogramu 1.8 ilichangwa kwa Leicester Royal Infirmary—mchango mkubwa nyakati hizo za upungufu wa chakula.

      Huo mkusanyiko uliboresha hali ya kiroho ya Mashahidi wapatao 11,000 katika Uingereza. Walisisimka kwamba watu wapatao 12,000 walihudhuria! Wajumbe walishiriki kwa shangwe katika kutoa ushahidi katika barabara za Leicester kwa kiwango kisicho na kifani, nao walitembelea vijiji vya mbali wakiwa na utoaji mbalimbali kwa kutumia kinanda cha gramafoni.

      Hotuba kuu za mkusanyiko zilikuwa mirekodi iliyofanywa mwezi uliotangulia ya hotuba zilizotolewa kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova wa siku tano katika St. Louis, Missouri, Marekani. Mrekodi wa hotuba ya Ndugu Rutherford “Watoto wa Mfalme” ulikuwa jambo kuu la mkusanyiko. Kwa kuwa haikuwezekana kuingiza kutoka nchi za nje nakala za kitabu Children kilichotolewa St. Louis, chapa ya pekee ya kitabu kilichojalidiwa kwa karatasi ilitokezwa baadaye Uingereza. Nakala yake ilipelekewa kila mtoto aliyekuwa amehudhuria huo mkusanyiko.

      Mkutano wa Pekee wa Kila Mwaka wa Leicester

      Baada ya vita ongezeko la wapiga-mbiu wa Ufalme katika Uingereza lilikuwa la kustaajabisha! Kufikia mapema miaka ya 1980, idadi ya makutaniko katika Leicester ilikuwa imekua kufikia kumi. Kisha tukafahamishwa kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilikuwa limeamua kuwa na mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society katika Leicester mwaka wa 1983. Nikiwa mwangalizi wa jiji la Leicester, upesi nilihusika katika matayarisho, kutia na kukodi De Montfort Hall tena.

      Washiriki 13 wa Baraza Linaloongoza walikuja kutoka makao makuu ya Sosaiti ya Brooklyn kwa ajili ya tukio hilo. Jumla ya wajumbe 3,671—wakati huu kutoka ulimwenguni pote, na hasa wale wa zamani—walijaza huo ukumbi. Wengine 1,500 zaidi walisikiliza programu hiyo katika Jumba la Kusanyiko la karibu.

      Albert D. Schroeder, aliyekuwa amekuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society huko London wakati wa mkusanyiko wetu wa Leicester uliofanywa wakati wa vita, alisimamia mkutano huo wa kila mwaka. Akikumbuka ya nyuma juu ya mkusanyiko wa mwaka wa 1941, Ndugu Schroeder aliuliza hivi: “Ni wangapi kati yenu mlio nasi leo waliokuwapo wakati huo?” Zaidi ya nusu ya wasikilizaji waliinua mikono yao. “Loo! Ni muungano ulioje kwa nyinyi nyote waaminifu, wenye uaminifu-mshikamanifu!” akasema kwa mkazo. Kwa kweli lilikuwa jambo lisiloweza kusahaulika.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki