-
Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?Mnara wa Mlinzi—1996 | Agosti 15
-
-
Lakini kwenye Mathayo 24:3, 27, 37, 39, Mathayo alitumia neno tofauti, nomino isiyopatikana kwingineko katika Gospeli: pa·rou·siʹa. Kwa kuwa Mungu alipulizia uandikaji wa Biblia, kwa nini alimchochea Mathayo kuchagua neno hilo la Kigiriki katika mistari hiyo alipokuwa akiandika Gospeli yake katika Kigiriki? Linamaanisha nini, na kwa nini tutake kujua?
11. (a) Maana ya pa·rou·siʹa ni nini? (b) Vielelezo kutoka katika maandishi ya Yosefo huonyeshaje wazi uelewevu wetu wa pa·rou·siʹa? (Ona kielezi-chini.)
11 Moja kwa moja, pa·rou·siʹa humaanisha “kuwapo.” Kamusi ya Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine yasema hivi: “PAROUSIA, . . . [kihalisi], kuwapo, para, pamoja, na ousia, kuwa (kutoka eimi, kuwa), huonyesha kuwasili na kuwapo pamoja kunakofuata. Kwa mfano, katika barua fulani ya mafunjo, mwanamke asema juu ya umuhimu wa parousia yake mahali fulani ili ashughulikie mambo yanayohusu mali yake.” Kamusi nyingine hueleza kwamba pa·rou·siʹa, huonyesha ‘ziara ya mtawala.’ Basi, halimaanishi muda wa kuwasili tu, bali kuwapo kunakoendelea tangu kuwasili. Kwa kupendeza, hivyo ndivyo mwanahistoria Myahudi Yosefo, aliyeishi wakati uleule wa mitume, alivyotumia pa·rou·siʹa.a
12. Biblia yenyewe hutusaidia kuthibitishaje maana ya pa·rou·siʹa?
12 Hiyo maana “kuwapo” inaonyeshwa wazi na fasihi za kale, hata hivyo Wakristo wanapendezwa hasa na jinsi Neno la Mungu hutumia pa·rou·siʹa. Jibu ni lilelile—kuwapo. Twaona hivyo kutokana na vielelezo katika barua za Paulo. Kwa mfano, aliwaandikia Wafilipi hivi: “Kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe.” Alisema pia juu ya kukaa nao ili waweze kuchachawa “kwa sababu ya kuwapo [pa·rou·siʹa] [kwake] pamoja [nao] tena.” (Wafilipi 1:25, 26; 2:12) Tafsiri nyingine husema “kuwa kwangu pamoja nanyi tena” (Weymouth; New International Version); “ninapokuwa pamoja nanyi tena” (Jerusalem Bible; New English Bible); na “mnapokuwa nami miongoni mwenu mara nyingine tena.” (Twentieth Century New Testament) Kwenye 2 Wakorintho 10:10, 11, Paulo alitofautisha ‘kuwapo kwake mwenyewe’ na ‘kutokuwapo.’ Katika vielelezi hivi yeye bila shaka hakuwa akisema juu ya kukaribia au kuwasili kwake; alitumia pa·rou·siʹa kwa maana ya kuwapo.b (Linganisha 1 Wakorintho 16:17.) Namna gani kuhusu marejezo kwenye pa·rou·siʹa ya Yesu? Je, yana maana ya “kuja” kwake, au yanaonyesha kuwapo kunakoendelea?
13, 14. (a) Kwa nini tufikie mkataa kwamba pa·rou·siʹa huendelea kwa wakati fulani? (b) Ni jambo gani ambalo lazima lisemwe kuhusu urefu wa pa·rou·siʹa ya Yesu?
13 Wakristo watiwa-mafuta kwa roho katika siku ya Paulo walipendezwa na pa·rou·siʹa ya Yesu. Lakini Paulo aliwaonya ‘wasidanganywe.’ Kwanza lazima “mtu wa kuasi” aonekane, ambaye amethibitika kuwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Paulo aliandika kwamba “yule [mtu wa kuasi] ambaye kuja [“kuwapo,” “NW”] kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za u[w]ongo.” (2 Wathesalonike 2:2, 3, 9, italiki ni zetu.) Kwa wazi, pa·rou·siʹa, au kuwapo, kwa yule “mtu wa kuasi” hakukuwa kuwasili kwa muda tu; kungeendelea kwa wakati fulani, ambapo katika huo ishara za uwongo zingetokezwa. Kwa nini hili ni jambo la maana?
14 Fikiria mstari unaotangulia tu: “Ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake.” (Italiki ni zetu.) Sawa na vile kuwapo kwa “mtu wa kuasi” kungekuwa kwa kipindi fulani cha wakati, kuwapo kwa Yesu kungeendelea kwa muda fulani na upeo wako ungekuwa uangamizo wa yule “mwana wa uharibifu.”—2 Wathesalonike 2:8.
-
-
Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?Mnara wa Mlinzi—1996 | Agosti 15
-
-
a Vielelezo kutoka kwa Yosefo: Kwenye Mlima Sinai umeme na ngurumo “zilitangaza kwamba Mungu alikuwapo [pa·rou·siʹa] hapo.” Udhihirisho wa kimuujiza katika tabenakulo “ulionyesha kuwapo [pa·rou·siʹa] kwa Mungu.” Kwa kumwonyesha mtumishi wa Elisha yale magari yenye kuzunguka-zunguka, Mungu “alidhihirisha kwa mtumishi wake nguvu [zake] na kuwapo [pa·rou·siʹa] kwake.” Ofisa Mroma Petronius alipojaribu kuwatuliza Wayahudi, Yosefo alidai kwamba ‘Mungu alimwonyesha Petronius kuwapo [pa·rou·siʹa] kwake kwa kutuma mvua. Yosefo hakutumia pa·rou·siʹa kumaanisha kukaribia tu au kuwasili kwa muda. Lilimaanisha kuwapo kwenye kuendelea, hata kusikoonekana. (Kutoka 20:18-21; 25:22; Mambo ya Walawi 16:2; 2 Wafalme 6:15-17)—Linganisha Antiquities of the Jews, Kitabu cha 3, sura ya 5, fungu la 2 [80]; sura ya 8, fungu la 5 [202]; Kitabu cha 9, sura ya 4, fungu la 3 [55]; Kitabu cha 18, sura ya 8, fungu la 6 [284].
b Katika kamusi ya A Critical Lexicon and Concordance to the English and Greek New Testament, E. W. Bullinger huonyesha kwamba pa·rou·siʹa humaanisha ‘kuwa au kupata kuwapo, basi, kuwapo, kuwasili; kuja kunakotia ndani wazo la kukaa kwa kudumu kuanzia kuja huko na kuendelea.’
-