-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ongezeko Kubwa Huko Baramita
Baramita ni eneo lingine nchini Guyana ambako wenyeji wengi wamekubali ujumbe wa Ufalme. Eneo la Baramita ambalo liko kaskazini-magharibi mwa Guyana, ni makao ya Wahindi wa kabila la Wakaribu. Wakaribu ni baadhi ya wakaaji wa kwanza kabisa wa eneo la Karibea, na jina hilo linalotokana na jina la kabila hilo. Lugha yao inaitwa Kikaribu.
Ruby Smith ambaye ni Mkaribu, alianza kupendezwa na kweli mwaka wa 1975 alipopewa trakti na nyanya yake. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 181.) Ruby alikuwa na umri wa miaka 16 wakati huo. Alifanya maendeleo ya kiroho na kubatizwa mwaka wa 1978 kwenye Kusanyiko la “Imani Ishindayo.” Muda mfupi baadaye, familia yao ilihamia Georgetown kwa sababu za kibiashara. Huko, Ruby aliolewa na Eustace Smith. Eustace hakuongea Kikaribu, hata hivyo, yeye na Ruby walitaka sana kuhamia Baramita ili kuwaeleza jamaa za Ruby na watu wengine ujumbe wa Ufalme. Ruby anasema: “Yehova aliona yaliyokuwa mioyoni mwetu naye alijibu sala zetu kwa sababu mwaka wa 1992, tulienda Baramita.”
Ruby anaongeza: “Tulipofika Baramita, nilianza kuhubiri mara moja. Tulifanyia mikutano yetu chini ya nyumba yetu ndogo, ambayo ilikuwa meta 1.5 hivi juu ya ardhi. Muda si muda, watu wakawa wengi sana wasiweze kutoshea katika nyumba hiyo, hivyo tukaazima mahema. Habari kuhusu mikutano hiyo zilipoenea, hudhurio liliongezeka na kufikia watu 300! Kwa kuwa nilisoma Kikaribu kwa ufasaha, nilipewa mgawo wa kufasiri Mnara wa Mlinzi. Watu hao wote waliwezaje kusikia? Tulitumia maikrofoni ya bei rahisi inayotumia mawimbi ya FM, na wengi kati ya wasikilizaji walibeba redio zao ambazo zilinasa mawimbi hayo ya sauti.
“Wakati huo, mimi na Eustace tuliona kwamba kikundi hicho kilihitaji Jumba la Ufalme. Kwa hiyo, baada ya kukadiria gharama na kuzungumzia mradi huo pamoja na wengine, tulianza kujenga. Ndugu yangu Cecil Baird alitoa vifaa vingi vilivyotumiwa katika ujenzi, nao wengine wakasaidia kwa kufanya kazi. Ujenzi ulianza Juni 1992 na kuisha mapema mwaka uliofuata, kabla tu ya Ukumbusho. Tulishangaa kuwaona watu 800 waliokuja kusikiliza hotuba ambayo ilitolewa na Gordon Daniels, mwangalizi anayesafiri.
“Kikundi cha Baramita kimekuwa kutaniko tangu Aprili 1, 1996, na Jumba la Ufalme liliwekwa wakfu Mei 25, mwaka huohuo. Tangu wakati huo jumba hilo limepanuliwa na sasa linatoshea watu zaidi ya 500, na ndugu wanaweza kulitumia kwa makusanyiko ya mzunguko na ya pekee. Naam, sasa kutaniko hilo ambalo mwanzoni lilikuwa kikundi kidogo tu, lina wahubiri wapatao 100, nayo Mikutano ya Watu Wote huhudhuriwa na wastani wa watu 300. Watu 1,416 wamehudhuria Ukumbusho!”
Arusi Kubwa Sana!
Katika wilaya ya Baramita, wanaume na wanawake wengi waliokuwa wakiishi pamoja bila kufunga ndoa walihalalisha ndoa zao kupatana na kanuni za Biblia. Lakini ilikuwa vigumu kwa baadhi yao kupata vyeti muhimu, kama vile vyeti vya kuzaliwa. Hata hivyo, baada ya juhudi nyingi na pia kusaidiwa na akina ndugu kujua tarehe zao za kuzaliwa na habari nyingine, watu hao waliweza kufunga ndoa.
Pindi moja, wenzi 79 walifunga ndoa kwenye sherehe ileile. Hotuba ya arusi ilitolewa na Adin Sills, wa Halmashauri ya Tawi. Siku tatu baadaye, watu 41, wengi wao wakiwa baadhi ya wale waliofunga ndoa, waliomba kuwa wahubiri.
Hali katika eneo lote la Baramita imekuwa bora sana kwa kuwa watu wengi wanapendezwa na Neno la Mungu. Jumba la Ufalme lilipokuwa likiwekwa wakfu, mzee mmoja alisema: “Sasa Baramita ni eneo lenye utulivu na amani. Hiyo ni kwa sababu zaidi ya asilimia 90 ya watu wa eneo hilo huhudhuria mikutano kwa ukawaida.”
Katika mwaka wa 1995, wilaya ya Baramita ilikumbwa na ukame mbaya. Watu wa Yehova walifanyaje? Wakati huo Gillian Persaud alikuwa mwalimu huko Baramita. Aliposikia kwamba ndege ndogo imetua kwenye uwanja mdogo uliokuwa karibu, dada huyo alitimua mbio ili kuzungumza na rubani kabla ndege hiyo haijaondoka. Alimwomba rubani huyo ampeleke Georgetown, ambako alienda moja kwa moja hadi kwenye ofisi ya tawi ili kueleza hali ya akina ndugu.
James Thompson, ambaye wakati huo alikuwa katika Halmashauri ya Tawi, anasema: “Baraza Linaloongoza lilituruhusu kupeleka chakula na bidhaa nyingine kwa ndege huko Baramita. Pia tulipanga wahubiri 36 wapelekwe kwa ndege hadi Georgetown kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Kwa wengi wao, hiyo ilikuwa mara yao ya kwanza kuhudhuria kusanyiko.”
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 181-183]
Yehova Amenipa ‘Maombi ya Moyo Wangu’
Ruby Smith
Alizaliwa: 1959
Alibatizwa: 1978
Maisha yake: Yeye ni Mkaribu na alikuwa mstari wa mbele katika kuhubiri habari njema huko Baramita, eneo la Wahindi wenyeji nchini Guyana.
Niliwasiliana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza mwaka wa 1975. Nilikuwa na umri wa miaka 16. Nyanya yangu alipokea trakti kutoka kwa mwanaye wa kambo na kuniomba nimtafsirie, kwa kuwa hakuweza kusoma Kiingereza. Nilishangazwa na ahadi za Biblia zilizozungumziwa katika trakti hiyo, hivyo nikajaza sehemu ya nyuma na kuituma kwenye ofisi ya tawi. Vichapo nilivyoomba vilipofika, nilivisoma na kuanza kuwaeleza wengine juu ya kweli za Kimaandiko nilizojifunza. Nilianza na nyanya yangu na shangazi yangu. Kwa kusikitisha, baba yangu hakupenda utendaji wangu.
Muda si muda, nyanya yangu na shangazi yangu wakaanza kuhubiri. Baadhi ya wanakijiji walikuja nyumbani kwetu ili kujifunza Biblia. Kadiri nilivyosoma, ndivyo nilivyotambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko maishani ili kumpendeza Yehova. Hiyo ilitia ndani kukiri kwa baba yangu kwamba nilikuwa nimeiba kitu fulani katika karakana yake na kupatana na ndugu yangu. Baada ya kusali sana, nilifaulu kufanya yote hayo.
Wakati huohuo, ofisi ya tawi ilipanga ili painia wa pekee, Sheik Bakhsh, atembelee eneo letu. Hata hivyo, Ndugu Bakhsh hakuweza kukaa kwa muda mrefu, kwa hiyo yeye na ndugu mwingine, Eustace Smith, ambaye baadaye alikuja kuwa mume wangu, walijifunza nami kupitia barua.
Katika mwaka wa 1978, nilienda Georgetown kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Imani Ishindayo.” Nilipofika katika mji huo mkuu, nilienda moja kwa moja hadi kwenye ofisi ya tawi kuwaeleza kwamba ninataka kubatizwa. Walipanga ili Albert Small azungumzie pamoja nami maswali ambayo wazee huzungumzia pamoja na wale wanaotaka kubatizwa. Nilifurahi kama nini kurudi Baramita nikiwa mtumishi wa Yehova aliyebatizwa!
Nilianza kuhubiri mara moja kwa bidii nyingi sana. Wengi walipendezwa, kwa hiyo nikawaomba baadhi yao wajenge mahali pa ibada. Huko, nilifasiri gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza kila Jumapili katika Kikaribu. Hata hivyo, baba yangu alipinga utendaji wangu naye akasisitiza nisiwe nikitoka nyumbani Jumapili. Kwa hiyo nilikuwa nikirekodi makala hizo kwenye kanda kwa siri na kumpa mmoja wa ndugu zangu azipeleke kwenye mikutano. Kufikia wakati huu, karibu watu 100 walikuwa wakihudhuria kwa ukawaida.
Muda mfupi baadaye, familia yetu ilihamia Georgetown kwa sababu za kibiashara, naye nyanya yangu akahamia kwenye kijiji cha Matthews Ridge. Shangazi yangu alibaki Baramita lakini akaacha kuwahubiria wengine habari njema. Kwa hiyo utendaji wa Ufalme ukakoma kwa muda.
Nikiwa huko Georgetown, nilikutana na Eustace Smith, na muda mfupi baadaye tukaoana. Hata ingawa Eustace hakuweza kuongea Kikaribu, sisi wawili tulitaka kwenda Baramita ili kuwasaidia watu wenye kupendezwa. Katika mwaka wa 1992 tamaa yetu ilitimia. Mara tu tulipofika, tulianza kuhubiri na kupanga mikutano. Muda si muda, hudhurio liliongezeka na kufikia 300 hivi!
Pia tulipanga kuwe na darasa la kujifunza kusoma na kuandika baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi. Yolande, mtoto wetu wa kwanza, alisaidia kufundisha darasa hilo. Alipoanza kusaidia, alikuwa na umri wa miaka 11 na alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Leo, yeye na binti yetu wa pili, Melissa, ni mapainia wa kawaida.
Katika mwaka wa 1993, Yehova alibariki kutaniko la Baramita likapata Jumba la Ufalme. Pia alitupa “zawadi katika wanadamu” ambao waliongea Kikaribu na walioweza kuliongoza kutaniko. (Efe. 4:8) Kuanzia Aprili 1, 1996, Baramita likawa kutaniko rasmi. Pia ninafurahi kusema kwamba mama yangu, nyanya yangu, na karibu ndugu na dada zangu wote wako katika kutaniko hilo. Kwa kweli, Yehova amenipa ‘maombi ya moyo wangu.’—Zab. 37:4.
[Picha]
Mimi na Eustace leo
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 184]
Kusanyiko la mzunguko huko Baramita, mwaka wa 2003
[Picha katika ukurasa wa 185]
Watu wengi wilayani Baramita wamekubali kweli ya Biblia
-