Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Guyana
    2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Mikutano Katika “Nyumba za Chini” na Katika Majumba ya Kukodiwa

      Tangu kazi ya kuhubiri ianze nchini Guyana, imekuwa vigumu kupata Majumba ya Ufalme yanayofaa. Katika mwaka wa 1913, ndugu kadhaa waliokuwa Georgetown walikodi chumba kwenye jengo la Somerset House, ambacho walikitumia kwa miaka 45. Kufikia mwaka wa 1970, ni makutaniko mawili tu, la Charlestown huko Georgetown na la Palmyra huko Berbice, ambayo yalikuwa na Jumba la Ufalme. Hata hivyo, miaka mitatu kabla ya hapo, idadi ya wahubiri nchini Guyana ilikuwa imepita 1,000! Kwa hiyo, makutaniko mengi yalikutanika katika majengo ya kukodiwa, ambayo mara nyingi hayakuwa yenye kupendeza.

      Kwa mfano, mwishoni mwa miaka ya 1950, Kutaniko la Wismar, karibu na Mto Demerara, liliongezeka sana hivi kwamba ndugu walilazimika kutafuta jumba linalofaa. Waliruhusiwa kutumia jengo lililoitwa Islander Hall. Walifanya mkutano wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi katikati ya juma, na Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi Jumapili jioni. Lakini haikuwa rahisi kutayarisha jumba hilo kwa ajili ya mikutano. Kwanza ndugu walivuka Mto Demerara kutoka Mackenzie hadi Wismar kwa mashua ndogo. Ndugu mmoja alibeba katoni la magazeti, mwingine katoni la vitabu, na wa tatu akabeba fomu mbalimbali na masanduku ya michango. Kila kitu kilipaswa kuwa tayari kabla ya mikutano kuanza. Baada ya mikutano, vitu hivyo vilirudishwa.

      Mikutano pia ilifanywa katika zile zilizoitwa nyumba za chini. Kwa kuwa Guyana ni nchi ambayo hukumbwa na mafuriko mara kwa mara, nyumba nyingi hujengwa juu ya nguzo za mbao au saruji. Nyumba hizo huwa na nafasi chini ambayo inaweza kutumiwa kwa shughuli nyingine, kama vile mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, nchini Guyana, watu wengi wanaamini kwamba ikiwa dini haina jengo linalofaa la mikutano, basi haina baraka za Mungu.

      Isitoshe, mikutano iliyofanywa katika nyumba za chini ilivurugwa mara kwa mara na kuifanya ikose heshima inayostahili. Wakati mmoja, kuku aliyeshtuliwa na mbwa aliruka na kuingia mahali tulipokuwa tukifanyia mikutano na kutua juu ya kichwa cha msichana wa miaka sita. Msichana huyo alipiga mayowe yaliyomshtua kila mtu. Jambo hilo lilifanya ndugu wacheke baada ya mikutano, hata hivyo, liliwakumbusha kwamba walihitaji mahali pazuri pa ibada. Isitoshe, wapya hawakuchochewa kuhudhuria mikutano hiyo ambayo ilifanywa katika Majumba ya Ufalme yaliyokuwa chini ya nyumba.

      Ujenzi wa Majumba ya Ufalme

      “Kwa miaka 32 niliyokuwa katika Kutaniko la Charity, tulikodi majumba matano mbalimbali yaliyokuwa chini ya nyumba,” asema Frederick McAlman. “Kwa kuwa tulikuwa chini ya nyumba, tulihitaji kuwa waangalifu nyakati zote ili tuzigongwe vichwa na mbao zilizokuwa juu. Mtoto wa dada mmoja aligongwa kichwa, kwa kuwa dada huyo, ambaye alikuwa amembeba, hakukadiria vizuri urefu wa mbao hiyo. Baadaye alimweleza babake, ambaye hakuwa Shahidi, yale yaliyotokea. Wazazi wake walikata kauli kwamba kutaniko hilo lilihitaji kuwa na mahali pao pa ibada. Mamake alisema atatoa kiwanja, naye babake akasema kwamba atagharimia ujenzi wa jumba hilo, nao wakafanya hivyo. Jumba hilo la Ufalme ambalo limefanyiwa ukarabati mara kadhaa, bado hutumiwa kama kituo cha ibada ya kweli katika eneo hilo. Pia, hutumiwa kama Jumba la Makusanyiko katika mzunguko huo.”

      Zamani, ilichukua miezi mingi kujenga Jumba la Ufalme. Hivyo ndivyo ilivyokuwa huko Eccles. Sherlock Pahalan, ambaye wakati huo alikuwa mzee huko Eccles anaeleza: “Tulifanya mikutano yetu katika shule. Tulijua kwamba watu wangeongezeka kama tungekuwa na Jumba la Ufalme. Lakini wahubiri wa Eccles walikuwa wachache na maskini. Hata hivyo, waliazimia kujenga Jumba la Ufalme. Nilitafuta kiwanja kinachofaa katika eneo hilo, lakini sikufanikiwa.

      “Wakati huohuo, ndugu wa Georgetown walituazima visanduku viwili vya kutengenezea matofali, nao wakatufundisha jinsi ya kutengeneza matofali ya saruji. Mwanzoni, ilichukua muda wa saa kadhaa kutengeneza matofali 12 tu, lakini baada ya kuzoea tukawa stadi, hasa akina dada. Tatizo lingine lilikuwa kupata saruji kwa kuwa iliuzwa kwa kipimo. Ilinibidi kutuma maombi ili kupata kibali cha kuuziwa saruji ya kiasi fulani. Nilikuwa nikienda kwenye gati asubuhi na mapema na kupiga foleni ili kuhakikisha kwamba tulipata saruji hiyo. Kisha ilinibidi kutafuta lori lililokuwa likienda Eccles, ambalo lilikuwa na nafasi ya kutosha kubebea saruji hiyo. Yehova alitusaidia sikuzote. Lakini bado tulihitaji kiwanja.”

      Sherlock anaongeza: “Katika mwaka wa 1972, mimi na Juliet tulienda likizo Kanada. Huko tulimtembelea binamu yangu ambaye si Shahidi. Alitueleza kwamba ana viwanja viwili huko Eccles lakini watu wa jamaa yake hawakuwa wakivitunza vizuri. Hivyo akaniomba nimsaidie. Nilimwambia kwamba ningefurahi kumsaidia, na kwamba nilikuwa nikitafuta kiwanja huko Eccles ili kujenga Jumba la Ufalme. Bila kusita, aliniambia nichague kimoja kati ya viwanja hivyo viwili.

      “Wakati wa ujenzi, tuliona uthibitisho zaidi kwamba Mungu alikuwa akitusaidia. Vifaa vingi vya ujenzi havikupatikana kwa urahisi, isipokuwa saruji, kwa hiyo tulitumia vifaa vingine tofauti na vile vilivyokusudiwa mwanzoni na kazi ikasonga mbele. Isitoshe, ni ndugu wachache tu waliokuwa na ustadi uliohitajiwa, na ilitubidi kufanya mipango mingi ili wafanyakazi wa kujitolea waweze kufika mahali pa ujenzi. Nilisafiri mamia ya kilometa kwa gari langu dogo nikiwapeleka na kuwarudisha akina ndugu. Hatimaye, ujenzi wa Jumba letu la Ufalme ulimalizika. Karl Klein wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya kuliweka wakfu, jambo ambalo tulifurahia sana.”

      Majumba ya Ufalme Yaliyojengwa Haraka

      Mpaka mwaka wa 1995, zaidi ya nusu ya makutaniko ya Guyana yalikuwa yakikutana katika majengo yaliyokodiwa, kutia ndani nyumba za chini. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ikaanzisha halmashauri ya ujenzi ya kitaifa ili kushughulikia uhitaji huo. Mnamo Oktoba mwaka huohuo, ndugu walimaliza ujenzi wa jumba lao la kwanza ambalo lilijengwa kwa muda mfupi. Jumba hilo lilijengwa katika kijiji cha Mahaicony, karibu na Mto Mahaicony, kilometa 50 hivi mashariki ya Georgetown. Majirani waliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova watajenga Jumba la Ufalme katika miisho-juma minne tu, mmoja wao alisema: “Ikiwa mtajenga kibanda cha kuku, ni sawa, lakini hamwezi kujenga nyumba ya mawe kwa muda mfupi kama huo.” Muda si muda mtu huyo alibadili maoni yake.

      Katika nchi hiyo ambamo chuki mbaya ya ubaguzi hutokea mara kwa mara, ujenzi wa Majumba ya Ufalme umeonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hufanya kazi kwa umoja wa kweli wa Kikristo, bila kubaguana kijamii au kitaifa. Mwanamke mmoja mzee aliyetazama Jumba la Ufalme likijengwa huko Mahaicony alimwambia mwangalizi mmoja wa mzunguko hivi: “Niliwaona watu kutoka jamii sita wakifanya kazi pamoja!”

  • Guyana
    2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 194]

      Jumba la Ufalme huko Orealla, Guyana

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki