-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mnamo mwaka wa 1944 vichapo vyote vya watu wa Yehova vilipigwa marufuku. Ripoti moja katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1946 inasema: “Mashahidi wa Yehova hawakuruhusiwa kuwa na Biblia yoyote, hata kama haikuwa na maelezo ya Watch Tower na hata kama ilikuwa imechapishwa na vyama vingine vya Biblia.”
Katika Aprili mwaka wa 1946, Nathan Knorr kutoka makao makuu alitembelea Guyana. Aliandamana na William Tracy, aliyekuwa amehitimu Shule ya Gileadi muda mfupi kabla ya hapo. Walikuja ili kuwatia ndugu moyo na kuiomba serikali iondoe marufuku. Katika mkutano uliofanywa huko Georgetown, Ndugu Knorr aliwaeleza ndugu na watu wenye kupendezwa 180 waliokuwa wamekusanyika kwamba, wanafunzi wa zamani wa Yesu hawakuwa na Biblia wala vitabu vya kuwasaidia katika huduma. Hata hivyo, Yehova aliwabariki kwa ongezeko kubwa. Kwa nini? Kwa sababu waliendelea kuhubiri. Kwa hiyo, hapana shaka kwamba Mungu angewabariki watumishi wake wa siku hizi kama wangeendelea kuhubiri bila kuacha.
Wakati huohuo, ndugu waliendelea kutafuta njia za kisheria ili marafuku hiyo iondolewe. Kwa mfano, mwaka mmoja hivi baada ya vita kwisha, ndugu hao walipata sahihi za watu 31,370 kwenye waraka wa kupinga marufuku hiyo. Waraka huo ulipelekewa serikali. Isitoshe, ili watu wa Guyana wajue yaliyokuwa yakiendelea, tengenezo la Yehova lilichapisha trakti iliyoeleza mambo kinaganaga. Kichwa cha trakti hiyo kilisema: “BIBLIA TAKATIFU YAPIGWA MARUFUKU HUKU GUIANA YA UINGEREZA—WATU 31,000 WATIA SAHIHI WARAKA NA KUTAKA GAVANA awarudishie uhuru wa ibada wakaaji wote wa koloni hii, hata wawe wa dini gani.”
Ndugu Knorr pia alimtembelea W. L. Heape, aliyekuwa waziri wa koloni hiyo na kuomba marufuku iondolewe. Baada ya mazungumzo yao ya dakika 30, Ndugu Knorr alimpa Bw. Heape nakala ya kitabu kimoja cha funzo (“The Truth Shall Make You Free”), naye akamwomba akisome kwa makini. Bw. Heape alisema kwamba atakisoma. Isitoshe, alimwambia Ndugu Knorr kwamba marufuku juu ya vichapo vyetu ilikuwa ikizungumziwa na wanachama tisa wa kamati ya usimamizi wakati huohuo! Bw. Heape alisema kweli, kwa kuwa mnamo Juni 1946, gavana alitangaza kuondolewa kwa marufuku hiyo.
Muda mfupi baadaye, ndugu walipokea katoni 130 zenye vumbi zilizokuwa zimezuiliwa, ambazo zilikuwa na vitabu na vijitabu 11,798. Wahubiri wa Ufalme, ambao wakati huo walikuwa 70, walifurahi sana kuweza kuwatolea watu vichapo tena, nao wakavigawa vyote kwa muda wa majuma kumi tu. Mwezi wa Agosti, ndugu walianza pia kuhubiri barabarani, na walipata matokeo mazuri. “Magazeti yetu yalikuwa rahisi kugawa, karibu sawa na magazeti ya kila siku,” yasema ofisi ya tawi.
Hata wakati wa marufuku, ndugu waliendelea kupata chakula muhimu cha kiroho, kwa sababu ya jitihada za ndugu fulani aliyefanya kazi kwenye posta kuu huko Georgetown. Ndugu huyo anaandika: “Nilihisi kwamba nilikuwa na wajibu wa kuhakikisha kwamba nakala za Mnara wa Mlinzi zimefika kwenye ofisi ya tawi. Dada walisaidia kupiga chapa au kurudufisha nakala za funzo kwa kutumia mashine ya kunakili, kisha familia mbalimbali zikapewa nakala hizo kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.”
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
1944: Vichapo vyote vya Mashahidi wa Yehova vyapigwa marufuku.
1946: Marufuku yaondolewa mwezi wa Juni. Wamishonari wa kwanza kutoka Shule ya Gileadi wafika.
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 147]
Mnamo Juni 1946, tangazo hili lilitolewa, na hivyo marufuku juu ya vichapo vyetu ikaondolewa nchini Guyana
-