-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Wahindi Wenyeji Wakubali Habari Njema
Alipokuwa akihubiri sokoni huko Charity, mapema miaka ya 1970, Frederick McAlman alimwachia Monica Fitzallen, Mhindi mwenyeji, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 176.) Monica, ambaye aliishi katika eneo lililotengewa Wahindi wenyeji, alirudi nyumbani na magazeti hayo. Pindi fulani alipokuwa mgonjwa, Monica aliyasoma na kutambua kwamba mambo yaliyosema ni ya kweli. Muda si muda, akawa ndiye mhubiri pekee wa habari njema katika eneo hilo, naye akabatizwa mwaka wa 1974.
Monica anasema: “Nilihubiri nyumba kwa nyumba kwa bidii, na nilifurahia kuwaeleza watu wa eneo letu mambo mapya niliyokuwa nimejifunza. Hata hivyo, ili kufika nyumbani kwao, ilinibidi kusafiri kwa mashua kwenye mito na vijito. Idadi ya watu wenye kupendezwa ilipoongezeka, nilianza kufanya mikutano pamoja nao, na tulisoma na kuzungumzia habari kwenye kitabu cha kujifunzia Biblia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele.”
Je, bidii ya Monica ilikuwa na matokeo? Ndiyo, kwa kuwa sasa kuna wahubiri wengine 13 katika eneo hilo, kutia ndani mumewe, mwanaye na mke wake, na mjukuu wake msichana. Zamani, ndugu katika kikundi hicho kidogo walikuwa wakisafiri kwa muda wa saa 12 kwa mtumbwi hadi Kutaniko la Charity, lililokuwa karibu zaidi. Lakini sasa wanafanya mikutano katika eneo lao, na hudhurio huwa mara tatu zaidi ya wahubiri!
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 176-177]
Nilijifunza Neno la Mungu Kupitia Barua
Monica Fitzallen
Alizaliwa: 1931
Alibatizwa: 1974
Maisha Yake: Kwa kuwa aliishi mbali, Monica alijifunza Biblia kupitia barua kwa miaka miwili na aliwahubiria sana Wahindi wenyeji. Yeye hukariri maandiko anayotumia katika huduma kwa kuwa sasa yeye ni kipofu.
Ninaishi katika eneo lililotengewa Wahindi wenyeji linaloitwa Waramuri, ambalo liko karibu na Mto Moruka, katika wilaya ya kaskazini-magharibi mwa Guyana. Nilipopata kweli mapema katika miaka ya 1970, kutaniko la karibu lilikuwa Charity, karibu na Mto Pomeroon. Ili kufika huko, nilisafiri kwa muda wa saa 12 kwa mtumbwi.
Nilikutana na Mashahidi wa Yehova nilipokuwa nikinunua vitu huko Charity. Frederick McAlman alinipa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Niliyakubali, nikayapeleka nyumbani, na kuyaweka kwenye sanduku, ambamo yalikaa kwa miaka miwili. Kisha nikawa mgonjwa na sikuweza kutoka kitandani kwa muda fulani, nami nikashuka moyo sana. Ndipo nilipoyakumbuka magazeti hayo. Niliyasoma na mara moja nikatambua kweli.
Wakati huo, mume wangu Eugene, alianza kutafuta kazi naye akaamua kusafiri kuelekea upande wa chini wa mto hadi Charity. Nilikuwa nimeanza kupata nafuu, hivyo nikaenda naye. Hata hivyo, sababu yangu kuu ya kwenda huko ilikuwa kuwatafuta Mashahidi wa Yehova. Sikuhitaji kuwatafuta sana, kwa kuwa mwanamke mmoja Shahidi alikuja nyumbani kwetu. Nilimwuliza, “Je, wewe ni mmoja wa watu wa Mnara wa Mlinzi?” Alipojibu ndiyo, nilimwuliza kumhusu mtu niliyekuwa nimekutana naye sokoni miaka miwili iliyopita. Alienda kumtafuta Frederick McAlman mara moja, ambaye alikuwa akihubiri na wahubiri fulani katika eneo lililokuwa karibu.
Wote wawili waliporudi, Ndugu McAlman alinionyesha jinsi ya kujifunza Biblia kwa kutumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilikubali kujifunza. Kwa kuwa mimi na Eugene tulihitaji kurudi nyumbani, nilijifunza kupitia barua. Nilijifunza vitabu viwili kwa njia hiyo—kitabu Kweli na “Mambo Mawili Yasiyobadilika Asiyoweza Mungu Kusema Uongo.” Nilipokuwa nikijifunza kitabu Kweli, niliacha Kanisa la Anglikana na kuwa mhubiri. Kasisi aliniandikia hivi: “Usiwasikilize Mashahidi wa Yehova. Wao huielewa Biblia kijuujuu tu. Nitakuja kuzungumzia jambo hilo nawe.” Lakini hakuja kamwe.
Kwa kuwa hakukuwa na wahubiri wengine katika eneo hilo, niliwaeleza majirani wangu mambo mapya niliyojifunza. Pia nilimhubiria mume wangu, ambaye ninafurahi kusema kwamba alibatizwa mwaka mmoja baada yangu. Leo Eugene ni mmoja kati ya wahubiri wetu 14.
Katika miaka ya karibuni, magonjwa ya macho yamenifanya niwe kipofu, kwa hiyo sasa mimi hukariri maandiko ninayotumia katika huduma. Hata hivyo, namshukuru Yehova kwa kuwa bado ninaweza kumtumikia.
-
-
Guyana2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Eugene na Monica Fitzallen
-