Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • UPENDO WA KINDUGU WAONYESHWA HUKO HAITI

      Januari 12, 2010, tetemeko kubwa sana la nchi liliharibu mji mkuu wa Haiti, Port-au-Prince, na maeneo yanayolizunguka. Mamia ya maelfu waliuawa, na wengine wengi wakaachwa bila makao. Maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipoteza makao, na 154 wakafa. Wengine wengi walijeruhiwa vibaya au wakaponea chupuchupu.

      Acloque alikuwa nyumbani tetemeko hilo lilipopiga. Kuta zilipasuka na mawe yakaporomoka na kumfanya anaswe katikati ya sakafu na dari lililoporomoka. Hata hivyo, hakuumizwa vibaya na akaanza kupapasa-papasa gizani kwa mikono yake. Acloque anakumbuka: “Niligusa ndoo yenye maji. Singeweza kuisogeza, lakini ningeweza kuingiza vidole ndani ya maji na kutia matone kadhaa mdomoni. Pia nilipata jiwe fulani na nikalitumia kugongagonga ili niweze kupata msaada.” Alianza kusali ili apate msaada na akaendelea kugongagonga kwa kutumia jiwe hilo na kusubiri.

      Acloque anasema: “Sikuwa na saa na sikujua ilikuwa saa ngapi. Mwanzoni nililia na kumsihi Yehova aniokoe. Lakini kadiri wakati ulivyopita, nilibadili sala zangu. ‘Najua utanifufua,’ nikasali. ‘Lakini mimi ni kijana! Nisipokufa, ninaweza kuendelea kukutumikia.’”

      Pole kwa pole, Acloque alisikia uhai wake ukiendelea kufifia na mwishowe hata akapoteza nguvu za kugongagonga kwa lile jiwe. Kisha akapoteza fahamu.

      Acloque alipopata fahamu, waokoaji Mashahidi walikuwa wakijaribu kumtoa. Anasimulia hivi: “Ghafula nilihisi jiwe limeanguka karibu na mguu wangu. Nilitambua kwamba iwapo wangeendelea kubomoa, wangeniumiza goti, kwa hiyo nilipitisha mkono wangu kwenye nafasi fulani na kuushika mkono wa mwokoaji mmoja.” Punde si punde Acloque aliokolewa. Alikuwa amekaa chini ya mabomoko hayo kwa siku nne.

      JITIHADA ZA HARAKA ZA KUTOA MSAADA

      Saa 24 baada ya tetemeko hilo, daktari wa kwanza aliwasili kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Jamhuri ya Dominika. Kisha Mashahidi wengi sana ambao ni madaktari na wale wanaotoa msaada waliwasili, pamoja na vifaa vilivyotolewa kama mchango. Hospitali ya muda ilisimamishwa kwenye eneo la ofisi ya tawi na zaidi ya Mashahidi 1,000 na watu wasio Mashahidi walitibiwa.

      Kati ya wagonjwa hao kulikuwa na wasichana wawili, na wote walikuwa wamepoteza mkono wa kulia. “Kama tu wagonjwa wengine waseja waliokuwa wamepoteza viungo,” anakumbuka Mylène, mjitoleaji mmoja, “walikuwa na wasiwasi kwamba hawatawahi kuolewa au kuwa na familia.” Kwa sababu hiyo, Mylène aliwasiliana na dada ambaye anafahamiana naye kutoka Ufaransa aliyekuwa amepoteza mkono wake katika aksidenti ya gari alipokuwa mtoto na akawaomba awatie moyo akina dada hao wawili. Dada huyo kutoka Ufaransa alituma barua-pepe yenye picha yake akiwa na mume wake na watoto wao wawili. Picha hiyo iliwafariji sana wasichana hao, ambao sasa wanajitahidi kukabiliana na hali zao mpya.

      Mbali na chakula, mavazi, na dawa, waokokaji walihitaji makao upesi. Mashahidi waliokuwa wakijitolea kutoka Haiti na nchi nyingine walijenga zaidi ya makao 1,700 ya muda ili familia za Mashahidi zilizokuwa zimepoteza makao ziweze kujikinga kutokana na mvua na wawe na usalama wa kadiri. Kufikia mwezi wa Juni, vikundi vya kutoa msaada vilikuwa vimeanza kujenga Majumba ya Ufalme ya muda, na mwezi wa Julai (Mwezi wa 7) wenye mamlaka walitoa vibali vya kwanza vya kujenga Majumba ya Ufalme ya kudumu.

      MATIBABU YA KIMWILI, KIHISIA, NA KIROHO

      Mnamo Machi daktari Shahidi ambaye ni mtaalamu wa kushughulika na mfadhaiko unaokuja baada ya kupatwa na matukio mabaya alikutana na wazee wa makutaniko 115 yaliyokumbwa na tetemeko hilo. Daktari huyo aliwapa wazee hao mapendekezo yanayofaa ya jinsi wanavyoweza kuwategemeza kiroho washiriki wa kutaniko waliokuwa wameathiriwa kihisia. Baada ya hapo, daktari huyo alikutana na akina ndugu na dada zaidi ya 100 waliohitaji matibabu ya pekee.

      Muda mfupi baada ya tetemeko hilo, David Splane wa Baraza Linaloongoza alienda Haiti kuwafariji na kuwatia moyo akina ndugu. Ndugu Splane, ambaye anaweza kuzungumza Kifaransa, aliwatolea akina ndugu hotuba katika kusanyiko la mzunguko na akawa na mkutano na familia ya Betheli, wamishonari, na waangalizi wa mzunguko. Wote walithamini sana upendo wake na utunzaji mwororo wa Baraza Linaloongoza.

      Licha vizuizi vilivyoonekana kuwa haviwezi kushindwa, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Krioli cha Haiti ilikamilishwa, ikachapishwa, na kutumwa kwenye ofisi ya tawi. Biblia hizo mpya ziliwasili saa chache tu kabla ya kutolewa katika kusanyiko la wilaya la Julai. Katika matukio yote ya mwaka wa 2010, kuanzia jitihada za mwanzo za kutoa msaada hadi sasa, kila mtu anayehusika ameona na kuhisi mwongozo na utegemezo wa kudumu wa Yehova kwa njia kubwa au ndogo. Tena na tena, bidhaa zilizohitajika, usafiri, na wafanyakazi walifika kwa wakati unaofaa kabisa na kwa njia za pekee sana ambazo haziwezi kusemwa kuwa hazikuongozwa na mtu fulani. Mmishonari mmoja ambaye ametumikia kwa miaka mingi alisema, “Ulihitaji kuwa hapa ili utambue wazi kwamba mkono wa Yehova ulikuwa ukitenda.”

  • Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
    2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 33]

      Madaktari Mashahidi waliwasili punde tu baada ya tetemeko ▸

      [Picha katika ukurasa wa 33]

      Wajitoleaji Mashahidi kutoka Haiti na nchi za nje walijenga zaidi ya makao 1,700 ya muda

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki