Matukio Muhimu ya Mwaka Uliopita
INAPENDEZA kuona yale ambayo Yehova anatimiza kupitia watu wake duniani pote. Kitabu hiki cha mwaka kinaripoti kuhusu maendeleo katika eneo la lugha ya ishara na kinaeleza jinsi ambavyo Idara ya Uandikaji hufanya utafiti. Jisomee kuhusu makusanyiko yetu ya kimataifa na ujifunze mambo yenye kupendeza kuhusu kitabu chetu kipya cha nyimbo. Pata habari za hivi karibuni kuhusu kesi mbalimbali ulimwenguni pote, habari kutoka Haiti, na ofisi za tawi zilizowekwa wakfu hivi karibuni. Tunatumaini kwamba utafurahia kusoma na kutiwa moyo na habari hizo.
‘MUNGU ANATAKA VIZIWI WAMJUE’
Hebu fikiria yale yanayotukia katika eneo la lugha ya ishara. Salvatore, anayeishi Marekani, ni kiziwi na mke wake ni Shahidi wa Yehova. Ingawa amejua kweli ya Biblia kwa miaka mingi, hakufanya maendeleo yoyote ya kiroho. Mke wake alipendekeza kwamba asome Biblia kila siku kwa mwaka mzima. Hata hivyo, hakuelewa alichokuwa akisoma, hivyo akakata tamaa. “Sitawahi kumpenda Yehova,” akasema.
Maisha ya Salvatore yalianza kubadilika alipoambiwa kwamba kulikuwa na sehemu ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika DVD ya Lugha ya Ishara ya Marekani. Baada ya kusoma kwa undani Neno la Mungu katika lugha ya ishara, alisema hivi kwa msisimuko, “Kwa hakika Mungu alitaka nimjue!” Salvatore alijifunza Biblia, na sasa anamtumikia Yehova kwa furaha akiwa Shahidi aliyebatizwa.
Kama Salvatore, watu wengine viziwi ulimwenguni pote wamehisi jinsi Yehova anavyowapenda na kuwajali kupitia DVD za Biblia na vichapo vingine katika lugha ya ishara na pia vichapo vinavyopakuliwa kutoka kwenye Intaneti. Kwa sasa kuna vichapo katika lugha 46 za ishara, na bado vingine vitatolewa katika lugha nyingine 13. Gazeti Mnara wa Mlinzi linapatikana katika lugha tisa za ishara, na sehemu za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya zimetolewa katika lugha za ishara za Brazili, Italia, Kolombia, Marekani, Mexico, na Urusi.
Kila mara inapendeza sana kuona jinsi ambavyo vichapo katika lugha ya ishara vinagusa mioyo ya wapya. Natsue, mwanamke kiziwi huko Japani anasema hivi: “Nilianza kujifunza Biblia katika mwaka wa 1981 nikitumia vichapo vilivyoandikwa katika Kijapani. Kwa kuwa sikuelewa chochote na familia yangu ilianza kunipinga, niliacha kujifunza.”
Mnamo Aprili (Mwezi wa 4) 2007, mhubiri mmoja alinionyesha DVD Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! katika Lugha ya Ishara ya Kijapani. Hiyo ilikuwa miaka 26 tangu nianze kujifunza Biblia. Mara moja, nilianza tena kujifunza na nikaona kwamba mahitaji yangu ya kiroho yanatoshelezwa. Nilibatizwa Novemba (Mwezi wa 11) 2008.”
Leo, kuna wahubiri viziwi zaidi ya 16,000 ulimwenguni pote. Kwa ishara zao za nyuso na mikono, wanamsifu Yehova katika lugha ya ishara. Utegemezo wanaopata kutoka kwa vitabu, broshua, video, na drama za Biblia 30 ambazo zimetafsiriwa katika lugha mbalimbali za ishara zinawahakikishia kwamba Yehova anawapenda na anathamini utumishi wao mshikamanifu.
Ofisi za tawi 54 ambazo hutafsiri vichapo katika lugha ya ishara zinapokea barua nyingi za shukrani kutoka kwa ndugu na dada na watu wanaopendezwa katika maeneo ya lugha ya ishara. Barua hizo zinaonyesha jinsi ambavyo viziwi wanafurahia kuelewa kweli zenye kina katika lugha yao ya ishara. Ona maneno ya Emi, kutoka Japani, ambaye wazazi wake ni viziwi.
“Wazazi wangu walibatizwa miaka mingi kabla yangu,” anasema Emi, “lakini ilikuwa vigumu sana kwao kuelewa vichapo vilivyoandikwa katika Kijapani. Walipokosa kuelewa jambo, waliniomba niwafafanulie. Sasa wanaweza kuzungumza kuhusu kweli wakiwa na uhakika. Mama yangu alisema hivi, ‘Nilianza kuelewa Biblia kwa undani baada ya vichapo kutafsiriwa katika lugha ya ishara.’ Vichapo hivyo vimewasaidia kumkaribia Yehova zaidi na tumekuwa na uhusiano wa karibu zaidi katika familia yetu.”
‘KUFUATA KWA UANGALIFU MAMBO YOTE KWA USAHIHI’
Yesu alisema kwamba mtumwa mwaminifu angekuwa na busara alipowapa watumishi wake wa nyumbani “chakula chao kwa wakati unaofaa.” Hivyo Kristo alionyesha kwamba wale wanaoandaa “chakula” hicho wangekuwa wenye bidii, waangalifu, na wenye busara walipoandaa chakula cha kiroho kwa waabudu wa kweli wa Mungu.—Mt. 24:45-47.
Leo, ndugu watiwa-mafuta wa Kristo hutumia Idara ya Uandikaji huko Brooklyn, New York, kuandaa chakula cha kiroho kupitia magazeti, broshua, vitabu, na vichapo vingine vilivyochapishwa na vya kielektroniki. Kama tu chakula cha kimwili, chakula hicho cha kiroho lazima kitayarishwe vizuri. Hata waandikaji wa Biblia, ambao waliongozwa na roho takatifu, walihakikisha kwamba waliandika habari sahihi iliyokuwa imefanyiwa utafiti kwa uangalifu. Kwa mfano, Luka alizungumza na watu waliojionea matukio yenyewe na ‘akafuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’—Luka 1:1-4.
Idara ya Uandikaji hufuata kielelezo hicho cha ‘kufuata kwa uangalifu mambo yote kwa usahihi.’ Lakini wanaweza kupata wapi habari zinazoaminika? Ingawa Intaneti ni njia rahisi ya kupata habari nyingi haraka, watafiti wetu hawategemei blogu au Tovuti za watu wasiojulikana au wasio na ujuzi. Kwa mfano, Wikipedia, ambayo ni ensaiklopedia inayopatikana kwenye mtandao inaonya kwamba baadhi ya makala zake kwenye tovuti hiyo “huwa na habari ambazo hazikufanyiwa utafiti kwa undani, au zimepotoshwa,” na kuongezea kwamba “wale wanaotumia tovuti hiyo wanapaswa kutahadhari.” Kwa hiyo, Idara ya Uandikaji hutafuta vitabu vya marejeo vinavyotumiwa na wengi, makala zilizoandikwa na wataalamu wanaojulikana, na vitabu vilivyochapishwa na wachapishaji wanaojulikana.
Idara ya Uandikaji ina maktaba kubwa iliyo na maelfu ya vitabu. Pia, watafiti wetu hutumia maktaba za umma na za shule zilizo karibu. Wanaweza pia kupata vichapo hususa kutoka vyanzo vingine kwa kuazima vitabu kutoka kwa maktaba nyingine. Mojawapo ya maktaba kubwa ya chuo kikuu fulani ambayo watafiti wetu hutumia ina karibu vitabu milioni tano, majarida 58,000, filamu milioni 5.4 ndogondogo zenye habari nyingi, na maelfu ya habari zilizohifadhiwa kwenye kompyuta. Idara ya Uandikaji pia ina hifadhi kubwa ya makala zilizokatwa kutoka kwa magazeti, mambo yaliyoonwa, na habari za kihistoria kutoka idara hiyo na pia kutoka ofisi zetu za tawi ulimwenguni pote ambazo husahihishwa mara kwa mara.
Kama andiko la Mhubiri 12:12 linavyotukumbusha: “Hakuna mwisho wa kutungwa kwa vitabu vingi.” Hata vyanzo vya habari vyenye kutegemeka huenda vikawa na habari zisizo sahihi. Kwa hiyo, sisi huhakikisha jinsi gani kwamba habari ni sahihi na inategemeka?
Kwa mfano, hebu fikiria habari ifuatayo inayopatikana katika broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? kuhusu hariri inayotokezwa na buibui ambayo ni mojawapo ya vitu vigumu sana duniani: “Ukizidishwa ukubwa utoshane na uwanja wa mpira, utando wa hariri hiyo wenye unene wa sentimita moja ulio na fumwele zinazoachana kwa umbali wa sentimita 4, unaweza kusimamisha ndege kubwa ya abiria ikiwa mwendoni!” Ingawa habari hiyo ilipatikana katika gazeti moja la kisayansi linalojulikana sana, gazeti hilo halikuwa chanzo halisi cha habari hiyo, na habari iliyokuwa katika chanzo halisi haikueleweka waziwazi. Hivyo, ilibidi tuwasiliane na mtafiti aliyesema maneno hayo kwa mara ya kwanza na kujua jinsi alivyofikia mkataa huo. Pia watafiti wetu walihitaji kujua fomula na kanuni nyingine zinazohitajika ili kupiga hesabu ambayo ingewaonyesha utando huo wa hariri ungeathiriwa kadiri gani unaposimamisha ndege kubwa ya abiria. Baada ya kufanya utafiti kwa saa nyingi na kufanya hesabu kwa uangalifu, walithibitisha ukweli wa habari hiyo yenye kustaajabisha.
Hata hivyo, nyakati nyingine huenda vyanzo vinavyotegemeka vikakosa kupatanisha habari kwa usahihi. Kwa mfano: Inasemekana kwamba Gandhi alimwambia hivi Lord Irwin alipokuwa kwenye hekalu lake: “Nchi yako na yangu zitakapopatana juu ya mafundisho yaliyotolewa na Kristo katika Mahubiri haya ya Mlimani, hatutakuwa tumetatua matatizo ya nchi zetu tu, bali pia yale ya ulimwengu mzima.” Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa kwa makini kuhusu maneno hayo ulionyesha kwamba hakuna uthibitisho wowote kwamba Lord Irwin aliwahi kumtembelea Gandhi kwenye hekalu lake, na basi hilo likazusha maswali kuhusu ni wapi, wakati gani, na ikiwa kweli Gandhi alisema maneno hayo. Kwa sababu hiyo, vichapo vyetu havinukuu tena maneno hayo.
Au huenda umesoma kuhusu mazungumzo ya Sir Isaac Newton kuhusu kitu kilichotengenezwa ili kuonyesha jinsi mfumo wa jua unavyofanya kazi. Inaripotiwa kwamba mtu mmoja anayeamini kwamba hakuna Mungu aliyemtembelea Newton alimwuliza: “Ni nani aliyetengeneza kitu hiki?” Newton alipomjibu, “Hakuna!” mtu huyo alisema, “Unadhani mimi ni mjinga!” Inasemekana kwamba Newton alimwambia mtu huyo kwamba kitu hicho cha hali ya chini kikilinganishwa na mfumo mkubwa wa jua kinathibitisha kwamba lazima kuwe na mbuni au mtengenezaji. Ingawa kisa hicho kinavutia, vyanzo vya kihistoria na pia wasomi na wale walioandika wasifu wa Newton, hawana uthibitisho wowote kwamba kulikuwa na mazungumzo kama hayo. Jambo la kushangaza ni kwamba kisa hicho kinatajwa kwa mara ya kwanza mwanzoni mwa miaka ya 1800, lakini hakitaji jina la Newton bali jina la msomi Mjerumani Athanasius Kircher. Hivyo, Idara yetu ya Uandikaji haitaji tena kisa hicho katika vichapo vyetu.
Nyakati nyingine hata taarifa ndogo zinahitaji kufanyiwa utafiti zaidi ili kuthibitisha usahihi wake. Kwa mfano, katika simulizi la maisha yake, huenda ndugu akasema kwamba alizaliwa Chekoslovakia katika mwaka wa 1915. Lakini nchi ya Chekoslovakia ilianza kuwepo katika mwaka wa 1918. Kwa hiyo, ndugu huyo alizaliwa wapi? Huenda watafiti wetu wakahitaji kuchunguza ramani za zamani au rekodi za historia ili kupata jibu hilo.
Pia, huenda ndugu fulani akaandika katika simulizi la maisha yake kwamba alibatizwa huko San Francisco tarehe fulani hususa. Hata hivyo, uchunguzi unaofanywa kwa uangalifu huenda ukafunua kwamba hakukuwa na kusanyiko lolote katika jiji hilo tarehe hiyo iliyotajwa. Kosa hilo linaweza kurekebishwa jinsi gani? Nyakati nyingine huenda mtu asikumbuke mambo yote kwa usahihi. Huenda ndugu asisahau mahali alipobatizwa, lakini huenda asikumbuke kwa usahihi tarehe aliyobatizwa. Inawezekana kupata habari sahihi kwa kuchunguza na kulinganisha vyanzo mbalimbali vya habari.
Kwa ufupi, Idara ya Uandikaji hutumia tu habari zilizo sahihi na za kweli, hata inapohusu mambo yanayoonekana kuwa madogo. Kwa kufanya hivyo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anaweza kuendelea kuandaa chakula cha kiroho kinachomletea heshima yule “Mungu wa ukweli,” Yehova.—Zab. 31:5.
TULISAIDIWA ‘KUENDELEA KUKESHA’
Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walithamini sana programu iliyotolewa kwa wakati unaofaa katika Makusanyiko ya Wilaya ya “Endeleeni Kukesha!” katika mwaka wa 2009. Kati ya waliohudhuria kulikuwa na wajumbe zaidi ya 200,000 kutoka nchi 136 walioalikwa kwenye makusanyiko ya kimataifa 37. Makusanyiko hayo yalifanyiwa Afrika Kusini, Austria, Chile, Côte d’Ivoire, Ghana, Italia, Kenya, Korea, Marekani, Mexico, Myanmar, Peru, Poland, Trinidad na Tobago, Ufaransa, na Ujerumani. Kilele cha jumla cha waliohudhuria makusanyiko hayo ya kimataifa kilikuwa 1,495,045, na watu 15,730 walibatizwa.
Kusudi la makusanyiko ya kimataifa ni nini? Baraza Linaloongoza hupanga makusanyiko hayo kila baada ya miaka michache katika majiji yaliyo mahali panapofaa—nyakati nyingine katika nchi ambako Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku. Makusanyiko hayo huwaimarisha akina ndugu na pia kuchochea kazi ya kuhubiri habari njema katika nchi hizo.
Makusanyiko hayo pia huwapa ndugu zetu nafasi ya pekee ya kujionea ‘kifungo cha kipekee cha muungano’ ambacho undugu wa ulimwenguni pote hufurahia. (Kol. 3:14) Inafurahisha kama nini kuona katika makusanyiko hayo upendo, amani, na umoja unaoshinda tofauti za kitaifa, kitamaduni, na lugha! Upendo wa kweli unaonyeshwa na watu kutoka maeneo mbalimbali wanapochangamana pamoja wakati wa vipindi vya mapumziko—wakila pamoja, wakipeana zawadi ndogo na anwani, wakipigwa picha, na kukumbatiana katika upendo wa kindugu. Wajumbe na wenyeji wengi huvalia nguo zao za kitamaduni.
Sehemu ya pekee katika makusanyiko ya kimataifa ni “Ripoti Kutoka Nchi Nyingine,” zilizotolewa siku zote nne za kusanyiko. Mwangalizi mmoja anayesafiri kutoka Italia alisema kwamba ripoti hizo ziliwasaidia wote waliohudhuria “wahisi kwamba wao ni sehemu ya undugu wa kweli wa kimataifa unaofuatilia lengo lilelile, yaani, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme.” Ilichangamsha moyo kama nini kusikia masimulizi ya wamishonari na watumishi wengine wa wakati wote ambao walikuwa wakizuru nchi yao kutoka katika migawo yao katika nchi za kigeni! Mifano yao mizuri inaendelea kuwatia moyo wazee na vijana!
Ilifurahisha sana kuwa na washiriki wa Baraza Linaloongoza katika makusanyiko hayo ya kimataifa ambao walitoa maagizo ya wakati unaofaa kutoka katika Biblia na kututia moyo kwa upendo! Hotuba zilizotolewa na washiriki wa Baraza Linaloongoza pamoja na “Ripoti Kutoka Nchi Nyingine” zilitafsiriwa moja kwa moja kwa faida ya watu wa vikundi vya lugha mbalimbali waliokuwa wakisikiliza programu. Kwa mfano, katika kusanyiko la pili la kimataifa huko Honolulu, Hawaii, Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba nne katika Kiingereza, ambazo zilitafsiriwa moja kwa moja katika Kichuuk, Kiiloko, Kijapani, Kimandarin, Kimarshall, na Kisamoa.
Linapopanga makusanyiko ya kimataifa, Baraza Linaloongoza hufikiria ukubwa wa mahali ambapo kusanyiko litafanyiwa, idadi ya Mashahidi katika eneo hilo na idadi ya Mashahidi kutoka nchi nyingine watakaohudhuria, na ikiwa kuna mahali pa kulala pa kutosha kwa ajili ya wajumbe. Baada ya hapo, ndugu wanaotegemeka katika kila jiji ambapo kusanyiko litafanywa wanatafuta vibali kutoka kwa wenye mamlaka na kuwasiliana na wasimamizi wa mahali ambapo makusanyiko yatafanyiwa.
Kwa kuwa mara nyingi viwanja vikubwa vya michezo hutumiwa kwa ajili ya makusanyiko hayo, mipango na kazi nyingi itahitaji kufanywa ili kuhakikisha kwamba ni mahali penye kuheshimika kwa ajili ya ibada ya Yehova. Kwa mfano, nchini Peru, kwa sababu kulikuwa na mchezo wa kandanda kabla ya kusanyiko, akina ndugu hawangeweza kuingia kwenye uwanja huo kuusafisha na kupanga mambo hadi usiku wa kuamkia kusanyiko. Ingawa ni wajitoleaji 3,000 walioombwa kusaidia, ndugu na dada zaidi ya 7,000 walifikia kwenye uwanja huo saa 12 jioni na kufanya kazi usiku wote ili kuutayarisha.
Mwishoni mwa kusanyiko la kimataifa lililofanywa Long Beach, California, Marekani, wanaume watatu ambao hudumisha uwanja huo walisema hivi: “Tumeona dini nyingi zikitumia uwanja huu, lakini hakuna dini yoyote inayoweza kufanya mambo ambayo nyinyi hufanya. Jambo hilo linastaajabisha sana.” Mmoja wa wanaume hao alikiri kwamba Mashahidi wa Yehova walipobisha mlango wake, alikuwa akisema, “Endeleeni kubisha, sitafungua.” Lakini sasa anasema kwamba akina ndugu wakibisha mlango wake, atafungua na kuwasikiliza. Mmoja wa wanaume hao hata alichochewa kusema, “Sijawahi kuwa mfuasi wa dini yoyote, lakini sasa ninataka kuwa mfuasi wa dini hii.”
Ushahidi mkubwa ulitolewa katika majiji yote ambapo makusanyiko yalifanywa na hilo lilimletea Yehova utukufu! Na tunamshukuru sana Yehova kwa kutuandalia makusanyiko hayo yaliyoimarisha imani ili ‘tuendelee kukesha’!—Mt. 24:42.
KUMWIMBIA YEHOVA SIFA
Kumwimbia Yehova nyimbo za sifa ni sehemu muhimu ya ibada yetu. Hivyo, katika makusanyiko ya mwaka wa 2009, watumishi wa Mungu walishangilia sana walipoambiwa kuhusu kitabu kipya cha nyimbo, Mwimbieni Yehova. Lakini kwa nini kitabu kipya cha nyimbo kilihitajika?
Mara kwa mara, tumerekebisha vitabu vyetu vya nyimbo ili vipatane na nuru inayozidi kuongezeka. (Met. 4:18) Matayarisho ya kitabu hicho kipya cha nyimbo yaliandaa nafasi ya marekebisho yaliyohitajiwa katika maneno ya nyimbo zetu. Maneno yaliyochaguliwa yanafanya iwe rahisi kujua maana ya wimbo unapoimbwa na iwe rahisi kukumbuka maneno hayo. Ili iwe rahisi kukariri, nyimbo nyingi zimefupishwa. Inapofaa, korasi zimeongezwa ili kurudia mawazo makuu. Kwa kuongezea, jitihada zilifanywa ili kila silabi iwe na noti yake badala ya silabi kadhaa kuwa chini ya noti moja.
Kitabu chetu cha zamani cha Mwimbieni Yehova Sifa kilipochunguzwa kwa makini iligunduliwa kwamba baadhi ya muziki ulihitaji kurekebishwa ili uimbwe kwa urahisi. Kwa sababu hiyo, nyimbo nyingine sasa zina sauti ya chini ili iwe rahisi kuimba noti za juu. Pia, baadhi ya nyimbo hazikuwa zikiimbwa kulingana na zilivyoandikwa katika kitabu. Kwa hiyo, muziki wa nyimbo nyingine umebadilishwa ili upatane na jinsi ambavyo nyimbo hizo zilikuwa zikiimbwa na ndugu zetu ulimwenguni pote.
Mambo hususa, kama vile jinsi muziki unavyochapishwa kwenye kurasa, yalifikiriwa kwa uzito. Ingawa nyimbo ndefu zimewekwa katika kurasa mbili ili kutosha hata lugha zenye maneno marefu, nyimbo zimepangwa kwa njia ya kwamba mtu hahitaji kugeuza ukurasa anapoimba. Hakuna nyimbo zenye urefu unaozidi mistari mitatu.
Kazi hiyo kubwa ya kutayarisha kitabu kipya cha nyimbo ilifanywa jinsi gani? Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 2007, kikundi cha watungaji na wataalamu wa nyimbo walialikwa kusaidia Baraza Linaloongoza katika kazi hiyo. Nyimbo zote katika kitabu cha nyimbo cha awali zilikaguliwa kwa uangalifu ili kutambua matatizo katika mafundisho, msisitizo wa maneno, na matatizo ya muziki. Ilikuwa wazi kwamba muziki fulani wa awali ulikuwa sawa lakini nyimbo zilihitaji maneno mapya. Nyimbo nyingine zilizokuwa na maneno yanayofaa zilihitaji mabadiliko makubwa katika muziki. Kisha Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza ikaidhinisha orodha fulani ya habari zinazoweza kufikiriwa ili kutunga nyimbo kwa ajili ya mikutano ya Kikristo, makusanyiko, na programu za kuweka wakfu.
Isitoshe, watungaji hao walichunguza tena njia ambayo akina ndugu hutumia kuimba katika mikutano. Ili kutokeza nyimbo zenye kuvutia lakini zenye heshima, waliepuka muziki unaosikika kama nyimbo zinazoimbwa katika makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Wakati huohuo, hawakutaka nyimbo za kumsifu Yehova ziwe kama zile zinazopendwa sana na makanisa ya wokovu au walokole.
Kazi hiyo yote ilipokuwa ikiendelea, Baraza Linaloongoza lilichunguza kwa uangalifu sana muundo na maneno ya kila wimbo. Nyimbo kadhaa kati za zile mpya ambazo Baraza Linaloongoza halikuwa linazifahamu zilirekodiwa na waimbaji ili Baraza Linaloongoza lizisikilize na kuzichunguza. Mara tu nyimbo hizo zilipoidhinishwa, zilitumwa kwenye ofisi za tawi zinazotafsiri ili maneno yatafsiriwe na vitabu vya nyimbo katika lugha hizo vitolewe wakati mmoja na vya Kiingereza.
Isitoshe, katika mwaka wa 2007, Baraza Linaloongoza lilipanga ili kikundi cha waimbaji kirekodi nyimbo zitakazoyasaidia makutaniko yajifunze nyimbo hizo. Kwa miaka mingi, okestra ya wajitoleaji kutoka nchi 14 imekuwa ikikutana huko Patterson, New York, mara mbili kwa mwaka ili kurekodi muziki utakaotumiwa katika programu za elimu za Mashahidi wa Yehova, kutia ndani drama, video, na muziki kwa ajili ya makusanyiko. Ndugu na dada hao waliojitoa, ambao wengi wao ni watumishi wa wakati wote, wametumia wakati na mali zao kusafiri na kurekodi muziki kwa faida ya undugu wa ulimwenguni pote. Wote ni wanamuziki stadi. Muziki ambao okestra hiyo hurekodi hutumwa kwenye ofisi za tawi ulimwenguni pote ili utumiwe katika makusanyiko na kwa ajili ya nyimbo za sauti katika lugha mbalimbali. Nyingi kati ya nyimbo hizo za sauti zilizoimbwa katika ofisi mbalimbali zinaweza kupakuliwa katika Tovuti yetu ya www.jw.org.
Watu wamesema nini kuhusu kitabu chetu kipya cha nyimbo, Mwimbieni Yehova? Barua hii kutoka kwa dada mmoja inafanana na barua nyingi sana za uthamini ambazo tumepokea: “Tafadhali niruhusu nianze barua hii kwa kushukuru sana kwa nyimbo mpya maridadi katika kitabu chetu kipya cha nyimbo. Nyimbo hizo zinagusa moyo, zinaimarisha imani, na zinafariji—ni zawadi yenye kupendeza kutoka kwa Yehova.”
Tunatumaini kwamba kitabu cha nyimbo Mwimbieni Yehova kitawafariji na kuwatia moyo akina ndugu ulimwenguni pote. Iwe tuko peke yetu au tumekutanika pamoja na waabudu wenzetu, na tukitumie kuonyesha jinsi tunavyompenda Baba yetu wa mbinguni, Yehova!
“MTAKOKOTWA NA KUPELEKWA MBELE YA MAGAVANA NA WAFALME . . . ILI KUWA USHAHIDI”
Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba wangepelekwa “mahakamani,” na mbele ya “magavana na wafalme.” Hata hivyo, alisema kwamba hilo lingetukia “ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” (Mt. 10:17, 18) Katika mwaka ambao umepita, Mashahidi wa Yehova wameona utimizo wa maneno ya Yesu. Na kama Bwana wao alivyosema, kutendewa kwao isivyofaa kumewapa nafasi nzuri za kutoa ushahidi.
Armenia
Vahan Bayatyan, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alihukumiwa kifungo cha miaka miwili na nusu gerezani kwa kukataa utumishi wa jeshi kwa sababu ya dhamiri yake. Baada ya kushindwa kesi yake na ile ya rufani katika mahakama za Armenia, alituma ombi kwa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) katika mwaka wa 2003. Mwishowe, Oktoba 27, 2009 (27/10/2009), ECHR ilikubaliana na uamuzi wa Armenia kwa sababu ya kanuni za kisheria ambazo zimefuatwa kwa miaka 50. Hata hivyo, hakimu mmoja aliyepinga uamuzi huo alisema kwamba uamuzi huo “haupatani na viwango vya kisasa vya nchi za Ulaya kuhusu suala la kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri.”
Kwa sababu ya umuhimu wa suala hilo, Mahakama ya Ulaya ilikubali jambo hilo lizungumziwe katika Kamati Kuu. Kesi hiyo ilipangwa kusikizwa huko Strasbourg, Ufaransa, Novemba 24, 2010. Uamuzi wa Kamati Kuu haukuwa umejulikana wakati ripoti hii ilipokuwa ikichapishwa.
Azerbaijan
Bado Mashahidi wa Yehova wanapata matatizo kuingiza vichapo vya kidini nchini humo. Wenye mamlaka huidhinisha vichapo fulani vya kidini viingizwe nchini lakini wanakataa vingine kwa sababu wanadai kwamba “habari iliyomo inakazia hasa imani ya Mashahidi wa Yehova na kudharau hisia za dini nyingine za Kikristo.” Kwa sababu hiyo, nyumba za baadhi ya akina ndugu na dada zimevamiwa na vichapo vyao vya kibinafsi vinavyotegemea Biblia vikachukuliwa.
Aprili 25, 2010, katika jiji la Qazax, karibu Mashahidi 250 wa Yehova walikuwa wakirudi kutoka kusanyiko huko Georgia katika mabasi matano makubwa na gari moja dogo. Polisi wa forodha mpakani walichukua vichapo vyao vya Biblia, kutia ndani Biblia 33. Mashahidi wengi, kutia ndani wazee na wasiojiweza, walikaa mpakani kwa saa nane hivi kabla ya kuruhusiwa kuendelea na safari yao. Ili kuzuia visa kama hivyo na ili kuhakikisha kwamba akina ndugu huko Azerbaijan wanaendelea kupokea chakula chao cha kiroho, jambo hilo limepelekwa mbele ya Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu.
Belarus
Novemba 6, 2009, Dmitry Smyk, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alipigwa faini ya rubi 3,500,000 (dola 1,154 za Marekani) kwa kukataa utumishi wa kijeshi. Ndugu Smyk alisema hivi: “Ninajaribu kuwa mwaminifu kwa Biblia katika kila sehemu ya maisha yangu, na kufuata mafundisho yake. Hilo linatia ndani kwamba mtu hapaswi kuzoezwa au kushiriki katika vita.”—Isa. 2:1-4.
Ingawa Katiba ya Belarus inahakikisha kwamba mtu ana haki ya kuchagua utumishi wa badala wa kiraia, hakuna uandalizi wa kisheria wa kufanya hivyo. Ndugu Smyk anasema, “Imeandikwa kwamba nina haki ya kuchagua utumishi wa badala wa kiraia, lakini uhalisi wa mambo ni kwamba siwezi kupewa haki yangu.”
Ili kurekebisha kosa hilo la kisheria, Februari 18, 2010 (18/2/2010), rais wa Belarus aliunda kamati ya kuandika sheria kuhusu utumishi wa badala. Muda mfupi baada ya hapo, mahakama hiyo ilisema kwamba Ndugu Smyk hakuwa na hatia na ikafuta faini kubwa aliyokuwa ametozwa. Kwa kuwa Mashahidi wengine vijana nchini Belarus wanakabili suala hilohilo na hawataki kujifunza vita, inatazamiwa kwamba hivi karibuni serikali itatoa uandalizi wa utumishi wa badala wa kiraia.
Ubelgiji
Kufikia mwaka wa 1993, ofisi ya tawi huko Brussels haikuwa ikitozwa kodi, kama tu majengo mengine yote ya kidini nchini Ubelgiji. Hata hivyo, katika mwaka wa 1993, wasimamizi wa kodi walibadili msimamo wao na kudai kodi ilipwe. Walisema kwamba Betheli haishughulikii tu mambo ya kidini, kwamba mojawapo ya makusudi yake ni kupata faida ya kifedha, na kwamba Wanabetheli hawahusiki wakati wote na utendaji wao wa kidini. Mwishowe katika mwaka wa 2008, kesi hiyo ilifikishwa mbele ya mahakama ya chini, lakini hakimu aliwapa wasimamizi wa kodi ushindi. Rufani ilikatwa, na Mei 4, 2010 (4/5/2010), mahakama ya rufani ilibadili uamuzi wa mahakama hiyo ya chini. Katika uamuzi ulioandikwa, mahakimu watatu walisema: “Maisha ya Betheli, kwa Mashahidi wanaoishi huko, yanahusianishwa na usadikisho mkubwa wa kidini unaodai kwamba wajitoe kabisa katika utumishi wa Mungu. . . . Watumishi hao wote ni washiriki wa Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote, na wanaishi, wanasali, wanaimba, na kujifunza Biblia pamoja. Pia wao husaidia katika ibada ya asubuhi.”
Eritrea
Mashahidi wa Yehova nchini Eritrea wanaendelea kuvumilia matatizo mengi wanapojitahidi kumtumikia Mungu kwa uaminifu. Kwa sasa kuna Mashahidi 58 gerezani, kutia ndani wanawake na watoto wadogo. Kwa sababu ya vizuizi vyenye kukandamiza vya serikali na hatari ya kukamatwa wakati wowote, ni vigumu kupata habari kuhusu wale walio gerezani. Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wamejaribu kupunguza mateso ya waabudu wenzao nchini Eritrea kupitia njia mbalimbali. Mashahidi wamezungumza na maofisa wa Wizara ya Mashauri ya Nchi za Kigeni ya Marekani, Muungano wa Ulaya, na ubalozi mbalimbali. Pia wamekutana na maofisa wengi wa Pembe ya Afrika, kama vile wawakilishi wa Muungano wa Afrika. Hivi karibuni, Mashahidi wa Yehova wametuma barua na orodha ya wafungwa ambao si wa umri unaostahili kuandikishwa jeshini kwa mabalozi 18 wa Eritrea ulimwenguni pote. Barua hiyo ilimwomba Rais Afewerki awaachilie wafungwa ambao si wa umri unaostahili kuandikishwa jeshini, kutia ndani watoto na wazee. Hata hivyo, serikali haijatoa jibu lolote kufikia leo.
Ugiriki
Januari 15, 2010 (15/1/2010), mahakama ya juu zaidi nchini Ugiriki, Kamati ya Nchi, ilifikia uamuzi kwamba Shahidi wa Yehova anayeitwa Evangelos Delis, alikuwa na haki ya kukataa kutumika akiwa askari-jeshi wa akiba. Ndugu Delis alikuwa jeshini kabla ya kuwa Shahidi wa Yehova, lakini alipoitwa kufanya mazoezi ya askari-jeshi wa akiba, alichochewa na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kukataa mazoezi hayo. Ingawa Jeshi lilikataa ombi lake la kukataa mazoezi hayo kwa sababu ya dhamiri, Kamati ya Nchi, ikitaja vipengee vya Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu, ilisema kwamba mtu ana haki ya kubadili dini yake hata baada ya kuwa ametumikia katika jeshi na ana haki ya kukataa mambo kwa sababu ya dhamiri kupatana na imani yake mpya ya kidini. Uamuzi huo wenye kupendeza wa mahakama ya juu zaidi nchini Ugiriki utawanufaisha sana watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri nchini humo na pia katika nchi nyingine, kama vile Armenia, Azerbaijan, Korea Kusini, na Uturuki.
Ureno
Septemba 25, 2009 (25/9/2009), Wizara ya Haki ilisema kwamba shirika la Association of Jehovah’s Witnesses limeidhinishwa bila kupingwa kuwa Jamii ya Kidini Ambayo Imekuwepo kwa Muda Mrefu. Sasa Mashahidi wa Yehova nchini Ureno wamepewa usajili wa juu zaidi kisheria na kidini, na hilo litawasaidia sana kutimiza huduma yao. Msimamo wao mpya wa kisheria utawapa watu wa Yehova faida nyingi. Zinatia ndani kuwa na wahudumu waliowekwa rasmi kuandikisha ndoa kisheria katika Majumba ya Ufalme na vilevile mamlaka ya kuingia hospitalini na gerezani kuwapa watu wowote wanaotaka msaada wa kiroho.
Puerto Riko
Januari 27, 2010, Mahakama Kuu ya Puerto Riko ilifanya uamuzi muhimu sana kwa kutegemeza haki ya mtu mzima kukataa matibabu ya aina fulani. Mahakama hiyo pia ilitambua haki ya mgonjwa kutumia mwongozo wa mapema kuteua mwakilishi wa kitiba ambaye atazungumza kwa niaba yake anapopoteza fahamu. Shahidi wa Yehova anayeitwa Victor Hernandez, aliandika mwongozo wa mapema kabla ya kwenda hospitalini. Hapo awali, mahakama fulani ilikuwa imekataa kutegemeza uamuzi wa kitiba wa Ndugu Hernandez’ kama alivyokuwa ameandika na ulioungwa mkono na mwakilishi wake wa kitiba. Ikibadili uamuzi wa mahakama hiyo, Mahakama Kuu ilitambua kwamba “mtu ana haki ya msingi ambayo haiwezi kupingwa ya kulinda mwili wake.” Mbali na kuwafaidi Mashahidi wa Yehova zaidi ya 25,000 nchini Puerto Riko, ushindi huo unawafaidi wagonjwa wengine wote katika kisiwa hicho.
Urusi
Katika miaka ya hivi karibuni utendaji unaoongozwa kwa roho wa watu wa Yehova umekabili matatizo makubwa zaidi tangu kusambaratika kwa Muungano wa Sovieti. Desemba 8, 2009 (8/12/2009), Mahakama Kuu ya Urusi iliunga mkono uamuzi wa mahakama ya chini huko Rostov ya kufutilia mbali shirika la kidini la Taganrog, kuchukua umiliki wa Jumba lake la Ufalme, na kutangaza kuwa 34 kati ya vichapo vyetu vinasemekana kuwa ni vya watu wenye msimamo mkali wa kidini, kutia ndani vichapo fulani vinavyosomwa sana kama vile kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, na ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu.’
Majuma machache baadaye, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Altay, kusini mwa Urusi, ilitoa uamuzi kama huo kuhusu shirika letu la kidini la jiji la Gorno-Altaysk, na kuorodhesha vitabu vingine 18 kuwa vya watu wenye msimamo mkali wa kidini. Kwa sasa, maamuzi hayo ya mahakama yamefanya isiwezekane kuingiza kichapo chochote kati ya vile vilivyotajwa nchini Urusi. Isitoshe, maamuzi hayo ya mahakama yamewafanya maadui wa Kristo wawe na ujasiri wa kuwatisha na kuwavamia wafuasi wake wenye amani katika majiji kadhaa. Tangu uamuzi wa Desemba 8, kumekuwa na visa zaidi ya 300 vilivyoripotiwa vya uvamizi, watu kukamatwa, nyumba kusakwa, na kukatizwa kwa ibada.
Kwa sababu ya tisho hilo linalozidi kuongezeka, Baraza Linaloongoza liliidhinisha kusambazwa kwa nakala milioni 12 za trakti ya pekee yenye kichwa Could It Happen Again? A Question for the Citizens of Russia (Je, Inaweza Kutendeka Tena? Swali kwa Raia wa Urusi). Trakti hiyo ilionyesha mambo yanayofanana kati ya uonevu ambao Mashahidi wa Yehova walipata wakati wa Ukomunisti na matatizo yanayowapata leo. Mashahidi wa Yehova walisambaza trakti hiyo ya pekee katika nchi yote ya Urusi kuanzia Februari 26 hadi 28, 2010. Licha ya hali mbaya ya hewa, ambayo ilifikia nyuzi 40 Selsiasi chini ya sufuri, makutaniko mengi yalisambaza trakti zote katika siku mbili tu.
Ili kupinga trakti hiyo, Aprili 26, 2010, Wizara ya Nchi Inayosimamia Mawasiliano, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ya Umma (Roskomnadzor) ilifuta leseni yetu ya kuingiza magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!
Hata hivyo, “mkono wa Yehova haujawa mfupi mno kwamba usiweze kuokoa.” (Isa. 59:1) Juni 10, 2010 (10/6/2010), Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR) ilipitisha uamuzi muhimu dhidi ya Urusi na kutetea masilahi ya Ufalme. Uamuzi wa kesi hiyo, iliyoitwa Jehovah’s Witnesses of Moscow v. Russia, ulisema kwamba kufutilia mbali na kupiga marufuku utendaji wa Jamii ya Mashahidi wa Yehova ya Moscow kulifanywa kinyume cha sheria na ni kuingilia haki za msingi za kibinadamu za kufikiri, kuwa na dhamiri, na kuwa na dini. Kufutiliwa mbali na kupigwa marufuku kumeendelea tangu Machi 26, 2004 huko Moscow, na hilo limefanya Mashahidi watendewe vibaya na kudhulumiwa. Uamuzi huo ulisema waziwazi kwamba serikali ya Urusi “ina daraka la kisheria . . . la kukomesha mambo ambayo Mahakama iliona yanafanywa kinyume cha sheria na kurekebisha madhara yaliyosababishwa.”
Uamuzi huo usiopingwa ulitaja pia ushindi tisa wa Mashahidi wa Yehova huko Afrika Kusini, Hispania, Japani, Kanada, Marekani, Uingereza, na Urusi, kutia ndani maamuzi mengine manane yaliyopitishwa na Mahakama hiyohiyo kuwatetea Mashahidi wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, mahakama hiyo ilithibitisha kwamba ECHR inaendelea kuamini kwamba kesi za awali ziliamuliwa kwa usahihi. Ikitaja maamuzi ya mapema ya Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu, mahakama hiyo ilisema kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuwa na hatia ya mashtaka yaliyoletwa dhidi yao na wenye mamlaka nchini Urusi.
Mahakama hiyo ilisema hivi: “Jamii ya Mashahidi wa Yehova ilikuwepo na ilitenda kazi kisheria huko Moscow kwa zaidi ya miaka 12, kuanzia 1992 hadi 2004. Wakati wote ambapo jamii hiyo ilikuwepo kisheria, wazee na washiriki wake hawakupatikana wakiwa wametenda uhalifu wowote au kosa la kisheria au la kijamii.” Kwa sababu hiyo, mahakama hiyo ilisema kwamba haki za Mashahidi wa Yehova zilikuwa zimeingiliwa na kwamba “Serikali ina daraka la kisheria . . . kuweka . . . sheria zinazopaswa kufuatwa na mashirika ya kisheria ya eneo lao ili kukomesha uvunjaji wa sheria uliopatikana na Mahakama [ya ECHR].”
Septemba 9, 2010, serikali ya Urusi iliomba ikiwa kesi hiyo inaweza kupelekwa kwenye Kamati Kuu. Hiyo bila shaka ni kwa sababu hawataki kutenda upesi kupatana na uamuzi uliotolewa. Iwe Yehova atakubali Kamati Kuu ichunguze uamuzi huo au la, tuna hakika kwamba ushahidi mkubwa utaendelea kutolewa.
Serbia
Mwishowe, baada ya mapambano ya kisheria yaliyoendelea kwa karibu miaka minne, Wizara ya Serbia ya Mambo ya Kidini iliorodhesha “Jehovah’s Witnesses—Christian Religious Community” katika Orodha ya Jamii ya Makanisa na ya Dini za Serbia. Kabla ya wakati huo, wizara hiyo ilikuwa imekataa maombi matatu ya kuandikishwa, ingawa vikundi vya Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati fulani, wamekuwepo katika eneo hilo tangu miaka ya mapema ya 1920. Hata hivyo, baada ya Mahakama Kuu ya Serbia kutoa maamuzi mawili yaliyotutetea, Wizara ya Mambo ya Kidini ilikubali maombi yetu na kutuandikisha.
Zamani, maadui wetu—wakisaidiwa na vyombo vya habari—mara nyingi walijaribu kuonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni madhehebu hatari. Bila shaka, kuandikishwa kisheria kuwa jamii ya kidini kutawasaidia watu wanyoofu nchini Serbia kuona kwamba Mashahidi wa Yehova ni raia wazuri wanaoiheshimu sheria na si tisho kwa jamii au watu mmojammoja. Jambo la kwanza lenye kupendeza lililotokezwa na kuandikishwa huko ni kwamba vichapo vya Biblia na vifaa vingine vinayotumiwa mikutanoni na katika mahubiri vinaweza kuingizwa nchini bila kulipa kodi zozote.
Slovenia
Novemba 27, 2009, “Jehovah’s Witnesses—Christian Religious Community” iliorodheshwa katika orodha ya makanisa na jamii nyingine za kidini inayosimamiwa na serikali ya Jamhuri ya Slovenia. Msimamizi wa Ofisi ya Jamii za Kidini ya serikali aliwaambia wawakilishi wetu kwamba kati ya mashirika na vikundi 40 vya kidini nchini Slovenia, “Jehovah’s Witnesses—Christian Religious Community” ndilo shirika la nane kufaulu kuandikishwa tena chini ya Sheria mpya ya Uhuru wa Kidini. Kuandikishwa huko kutawawezesha wahudumu wa wakati wote kupata faida fulani zinazotolewa na serikali kwa ajili ya watu wanaojihusisha na utendaji wa kidini wa wakati wote.
Uturuki
Mashahidi wa Yehova huko Mersin walikuwa wakitumia Jumba lao la Ufalme kwa miaka 20 hivi. Kisha, mnamo Agosti 2003, lilifungwa na wenye mamlaka eti kwa sababu lilijengwa mahali sheria hairuhusu majengo kama hayo yajengwe. Licha ya jitihada za ndugu zetu kutatua suala hilo kwa kukata rufani mahakamani, Desemba 30, 2009, mahakama ya juu zaidi nchini Uturuki ilikataa rufani na kuunga mkono ofisi ya gavana wa Mersin. Kesi hiyo sasa imepelekwa kwa ECHR.
UPENDO WA KINDUGU WAONYESHWA HUKO HAITI
Januari 12, 2010, tetemeko kubwa sana la nchi liliharibu mji mkuu wa Haiti, Port-au-Prince, na maeneo yanayolizunguka. Mamia ya maelfu waliuawa, na wengine wengi wakaachwa bila makao. Maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipoteza makao, na 154 wakafa. Wengine wengi walijeruhiwa vibaya au wakaponea chupuchupu.
Acloque alikuwa nyumbani tetemeko hilo lilipopiga. Kuta zilipasuka na mawe yakaporomoka na kumfanya anaswe katikati ya sakafu na dari lililoporomoka. Hata hivyo, hakuumizwa vibaya na akaanza kupapasa-papasa gizani kwa mikono yake. Acloque anakumbuka: “Niligusa ndoo yenye maji. Singeweza kuisogeza, lakini ningeweza kuingiza vidole ndani ya maji na kutia matone kadhaa mdomoni. Pia nilipata jiwe fulani na nikalitumia kugongagonga ili niweze kupata msaada.” Alianza kusali ili apate msaada na akaendelea kugongagonga kwa kutumia jiwe hilo na kusubiri.
Acloque anasema: “Sikuwa na saa na sikujua ilikuwa saa ngapi. Mwanzoni nililia na kumsihi Yehova aniokoe. Lakini kadiri wakati ulivyopita, nilibadili sala zangu. ‘Najua utanifufua,’ nikasali. ‘Lakini mimi ni kijana! Nisipokufa, ninaweza kuendelea kukutumikia.’”
Pole kwa pole, Acloque alisikia uhai wake ukiendelea kufifia na mwishowe hata akapoteza nguvu za kugongagonga kwa lile jiwe. Kisha akapoteza fahamu.
Acloque alipopata fahamu, waokoaji Mashahidi walikuwa wakijaribu kumtoa. Anasimulia hivi: “Ghafula nilihisi jiwe limeanguka karibu na mguu wangu. Nilitambua kwamba iwapo wangeendelea kubomoa, wangeniumiza goti, kwa hiyo nilipitisha mkono wangu kwenye nafasi fulani na kuushika mkono wa mwokoaji mmoja.” Punde si punde Acloque aliokolewa. Alikuwa amekaa chini ya mabomoko hayo kwa siku nne.
JITIHADA ZA HARAKA ZA KUTOA MSAADA
Saa 24 baada ya tetemeko hilo, daktari wa kwanza aliwasili kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Jamhuri ya Dominika. Kisha Mashahidi wengi sana ambao ni madaktari na wale wanaotoa msaada waliwasili, pamoja na vifaa vilivyotolewa kama mchango. Hospitali ya muda ilisimamishwa kwenye eneo la ofisi ya tawi na zaidi ya Mashahidi 1,000 na watu wasio Mashahidi walitibiwa.
Kati ya wagonjwa hao kulikuwa na wasichana wawili, na wote walikuwa wamepoteza mkono wa kulia. “Kama tu wagonjwa wengine waseja waliokuwa wamepoteza viungo,” anakumbuka Mylène, mjitoleaji mmoja, “walikuwa na wasiwasi kwamba hawatawahi kuolewa au kuwa na familia.” Kwa sababu hiyo, Mylène aliwasiliana na dada ambaye anafahamiana naye kutoka Ufaransa aliyekuwa amepoteza mkono wake katika aksidenti ya gari alipokuwa mtoto na akawaomba awatie moyo akina dada hao wawili. Dada huyo kutoka Ufaransa alituma barua-pepe yenye picha yake akiwa na mume wake na watoto wao wawili. Picha hiyo iliwafariji sana wasichana hao, ambao sasa wanajitahidi kukabiliana na hali zao mpya.
Mbali na chakula, mavazi, na dawa, waokokaji walihitaji makao upesi. Mashahidi waliokuwa wakijitolea kutoka Haiti na nchi nyingine walijenga zaidi ya makao 1,700 ya muda ili familia za Mashahidi zilizokuwa zimepoteza makao ziweze kujikinga kutokana na mvua na wawe na usalama wa kadiri. Kufikia mwezi wa Juni, vikundi vya kutoa msaada vilikuwa vimeanza kujenga Majumba ya Ufalme ya muda, na mwezi wa Julai (Mwezi wa 7) wenye mamlaka walitoa vibali vya kwanza vya kujenga Majumba ya Ufalme ya kudumu.
MATIBABU YA KIMWILI, KIHISIA, NA KIROHO
Mnamo Machi daktari Shahidi ambaye ni mtaalamu wa kushughulika na mfadhaiko unaokuja baada ya kupatwa na matukio mabaya alikutana na wazee wa makutaniko 115 yaliyokumbwa na tetemeko hilo. Daktari huyo aliwapa wazee hao mapendekezo yanayofaa ya jinsi wanavyoweza kuwategemeza kiroho washiriki wa kutaniko waliokuwa wameathiriwa kihisia. Baada ya hapo, daktari huyo alikutana na akina ndugu na dada zaidi ya 100 waliohitaji matibabu ya pekee.
Muda mfupi baada ya tetemeko hilo, David Splane wa Baraza Linaloongoza alienda Haiti kuwafariji na kuwatia moyo akina ndugu. Ndugu Splane, ambaye anaweza kuzungumza Kifaransa, aliwatolea akina ndugu hotuba katika kusanyiko la mzunguko na akawa na mkutano na familia ya Betheli, wamishonari, na waangalizi wa mzunguko. Wote walithamini sana upendo wake na utunzaji mwororo wa Baraza Linaloongoza.
Licha vizuizi vilivyoonekana kuwa haviwezi kushindwa, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha ya Krioli cha Haiti ilikamilishwa, ikachapishwa, na kutumwa kwenye ofisi ya tawi. Biblia hizo mpya ziliwasili saa chache tu kabla ya kutolewa katika kusanyiko la wilaya la Julai. Katika matukio yote ya mwaka wa 2010, kuanzia jitihada za mwanzo za kutoa msaada hadi sasa, kila mtu anayehusika ameona na kuhisi mwongozo na utegemezo wa kudumu wa Yehova kwa njia kubwa au ndogo. Tena na tena, bidhaa zilizohitajika, usafiri, na wafanyakazi walifika kwa wakati unaofaa kabisa na kwa njia za pekee sana ambazo haziwezi kusemwa kuwa hazikuongozwa na mtu fulani. Mmishonari mmoja ambaye ametumikia kwa miaka mingi alisema, “Ulihitaji kuwa hapa ili utambue wazi kwamba mkono wa Yehova ulikuwa ukitenda.”
KUWEKWA WAKFU KWA OFISI ZA TAWI KUNAMTUKUZA MUNGU
Februari 13, 2010, ni siku isiyoweza kusahaulika kwa Mashahidi wa Yehova katika Visiwa vya Solomon. Stephen Lett, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya kuwekwa wakfu katika majengo mapya ya ofisi ya tawi ya eneo hilo. Kati ya watu 368 waliohudhuria kulikuwa na Shahidi wa kwanza katika eneo hilo, Clement Fa’abasua. Mwezi mmoja kabla ya hapo kulikuwa na siku ya wageni kwa ajili ya wote wanaoishi karibu na ofisi hiyo ya tawi, na watu 273 walitembezwa. Mgeni mmoja, ambaye ni mchoraji wa ramani za ujenzi, aliandika hivi katika gazeti moja maarufu nchini humo: “Kwa ujumla, majengo yote [ya ofisi ya tawi] yanapata alama za juu kabisa. Ni kielelezo kwa jamii ya Visiwa vya Solomon ili vijionee kile kinachoweza kufanywa katika eneo hili hata iwe ni nani anayetumia majengo yenyewe. Inaweza kusemwa kwamba mchora-ramani, wajenzi kutoka maeneo mbalimbali, na wasimamizi wametokeza kito katika paradiso yetu.”
Programu ya kuwekwa wakfu isiyoweza kusahaulika ilifanywa katika ofisi ya tawi ya Estonia Jumamosi (Siku ya Posho), Aprili 3, 2010. Watu 438 waliohudhuria walifurahia kabisa programu hiyo, ambayo ilitia ndani hotuba ya kuwekwa wakfu iliyotolewa na Christian Muntean, kutoka katika ofisi ya tawi ya Ugiriki. Jengo la orofa mbili, lililokuwa kwenye uwanja kando ya ofisi hiyo, lilikuwa limenunuliwa kutoka kwa kampuni ya maji ya eneo hilo. Jengo hilo lililorekebishwa linatia ndani studio za kurekodi sauti na video na vilevile darasa la shule, kama vile Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja.
Ofisi ya tawi katika nchi jirani ya Latvia ilifanya programu yake ya kuwekwa wakfu April 10, 2010. Baada ya habari njema kuhubiriwa kwa mara ya kwanza huko Latvia mnamo 1918, kazi yetu ilipata upinzani mkali kwa makumi ya miaka. Hata hivyo, sasa kazi ya kuhubiri inakua huko Latvia na wajumbe 248 kutoka nchi tisa walikuwa pamoja na akina ndugu na dada kumsikiliza Christian Muntean akitoa hotuba ya kuwekwa wakfu.
Jumamosi, Mei 8, 2010, zaidi ya watu 2,200 walifurahia hotuba ya kuwekwa wakfu iliyotolewa katika ofisi ya tawi ya Paraguai na Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza. Nyumba ya makazi yenye vyumba 32 na jengo jipya lenye ofisi lilijengwa, na majengo ya makazi yaliyokuwepo yalirekebishwa na kujengwa upya. Zaidi ya hilo, tangi la maji linaloweza kubeba maji ya lita 40,000 lilijengwa. Tangu mwanzo, wenye mamlaka wa eneo hilo wamefurahishwa sana na ubora wa kazi ambayo imefanywa na wajitoleaji wa kimataifa na wa eneo hilo. Ofisa mmoja alisema kwamba majengo mengine ya kidini yamekuwa na matatizo mengi lakini Mashahidi wa Yehova walikuwa na sifa ya kufanya kila kitu kwa usahihi. Kwa sababu hiyo, ilikuwa rahisi sana kupata vibali vya ujenzi kwa ajili ya ofisi ya tawi.
Jumamosi, Mei 29, 2010, kwenye ofisi ya tawi ya Papua New Guinea, akina ndugu na dada 500 hivi kutoka nchi 12 walikusanyika kusikia hotuba ya kuwekwa wakfu ikitolewa na Winston Payne, wa ofisi ya tawi ya Australia. Majengo yaliyopanuliwa ya ofisi hiyo yalitia ndani jengo la orofa nne lenye vyumba vya kulala, chumba cha kulia chakula, jikoni, na dobi; jengo la huduma nyingine lililo na Jumba la Ufalme; na ofisi ya tafsiri yenye nafasi kubwa sana. Wasikilizaji walitia ndani kikundi cha Mashahidi waliokuwa wametembea kwa siku sita kupitia milima yenye miamba ili kuhudhuria tukio hilo. Kikundi hicho kilikuwa kimevalia mavazi ya kitamaduni ya Orokaiva na waliwakaribisha wageni wengine kwa uchangamfu wakicheza dansi na kuimba. Akiwa na machozi, dada mmoja ambaye alibatizwa miaka mingi iliyopita alieleza hisia ambazo zilifanana na za watu wengi aliposema, “Leo ninahisi ni kana kwamba tayari niko katika Paradiso!”
‘ENDELEENI KUZAA MATUNDA MENGI’
Hakuna shaka kwamba jitihada zenye umoja za Mashahidi wa Yehova zinaendelea kumtukuza Mungu. “Baba yangu hutukuzwa katika hili,” Yesu akasema, “kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi na kujionyesha kuwa wanafunzi wangu.” (Yoh. 15:8) Wakiwa na baraka na mwongozo wenye upendo wa Yehova, wataendelea ‘kutembea kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili wanapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu, wakifanywa kuwa na nguvu kwa nguvu zote kwa kadiri ya uwezo wake wenye utukufu ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.’—Kol. 1:10, 11.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Natsue alianza tena kujifunza Biblia
[Picha katika ukurasa wa 11]
Watafiti walihakikisha habari kwa uangalifu
[Picha katika ukurasa wa 13]
Korea
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mexico
[Picha katika ukurasa wa 14]
Afrika Kusini
[Picha katika ukurasa wa 15]
Stephen Lett katika moja ya makusanyiko ya kimataifa huko Hawaii
[Picha katika ukurasa wa 22]
Dmitry Smyk
[Picha katika ukurasa wa 25]
Evangelos Delis
[Picha katika ukurasa wa 25]
Cheti kilichotolewa na Wizara ya Haki
[Picha katika ukurasa wa 33]
Madaktari Mashahidi waliwasili punde tu baada ya tetemeko ▸
[Picha katika ukurasa wa 33]
Wajitoleaji Mashahidi kutoka Haiti na nchi za nje walijenga zaidi ya makao 1,700 ya muda
[Picha katika ukurasa wa 34]
“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo” ilitolewa katika lugha ya Krioli cha Haiti
[Picha katika ukurasa wa 36]
Ofisi ya tawi ya Estonia ilipanuliwa
[Picha katika ukurasa wa 37]
Ofisi ya tawi ya Paraguai
[Picha katika ukurasa wa 37]
Winston Payne alitoa hotuba ya kuwekwa wakfu ya ofisi ya tawi ya Papua New Guinea