Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Iweni Wavunaji Wenye Furaha!
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Julai 15
    • Iweni Wavunaji Wenye Furaha!

      “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.”—MATHAYO 9:37, 38.

      1. Ni nini hutusaidia kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu?

      TUNAPOKUMBUKA siku tulipobatizwa tukawa watumishi wa Yehova, iwe tulibatizwa miaka mingi au miaka michache iliyopita, huenda tukaona kana kwamba tulibatizwa juzi tu. Baada ya ubatizo, kumsifu Yehova kukawa jambo muhimu zaidi katika maisha yetu tuliyoweka wakfu kwake. Hangaiko letu kuu likawa kumtumikia Yehova kwa furaha huku tukinunua kabisa wakati unaofaa ili kuwasaidia wengine wasikie na ikiwezekana wakubali ujumbe wa Ufalme. (Waefeso 5:15, 16) Hata sasa, sisi huona wakati ukipita haraka sana tunapokuwa na shughuli nyingi, ‘tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’ (1 Wakorintho 15:58) Ingawa tunapata matatizo, furaha yetu katika kufanya mapenzi ya Yehova hutuchochea kuendelea kufanya kazi ya Bwana.—Nehemia 8:10.

      2. Ni nini kinachochangia furaha tunayopata katika kazi ya uvunaji wa mfano?

      2 Tukiwa Wakristo, tunashiriki katika kazi ya uvunaji wa mfano. Yesu Kristo alifananisha kukusanywa kwa watu kwa ajili ya uhai udumuo milele na kazi ya kuvuna. (Yohana 4:35-38) Kwa kuwa tunashiriki kazi hiyo ya kuvuna, itatia moyo kuchunguza furaha waliyopata Wakristo wa mapema katika kazi ya kuvuna. Tutachunguza mambo matatu yanayochangia furaha ambayo sisi hupata katika kazi ya kuvuna leo. Mambo hayo ni (1) ujumbe wetu wa tumaini, (2) jinsi ya kufanikiwa katika utafutaji wetu, na (3) jinsi ya kuwa na mtazamo wa kudumisha amani katika kazi ya kuvuna.

      Waliotumwa Kuwa Wavunaji

      3. Wafuasi wa mapema wa Yesu walipata furaha katika njia gani?

      3 Maisha ya wavunaji wa mapema—hasa mitume 11 wa Yesu waliokuwa waaminifu—yalibadilika sana mwaka wa 33 W.K., siku walipoenda mlimani huko Galilaya kuonana na Kristo aliyekuwa amefufuliwa. (Mathayo 28:16) Huenda “zaidi ya ndugu mia tano” walikuwepo pindi hiyo. (1 Wakorintho 15:6) Walikuwa wangali wanakumbuka kazi ambayo Yesu aliwaagiza wafanye. Aliwaambia: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Licha ya mnyanyaso mkali, walipata furaha nyingi katika kazi ya kuvuna walipoona makutaniko ya wafuasi wa Kristo yakianzishwa mahali kwingi. Baada ya muda, ‘habari njema ikahubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23; Matendo 1:8; 16:5.

      4. Wanafunzi wa Kristo walitumwa chini ya hali gani?

      4 Awali katika huduma yake huko Galilaya, Yesu alikuwa amewaita mitume wake 12 na kuwatuma hasa wakatangaze hivi: “Ufalme wa mbingu umekaribia.” (Mathayo 10:1-7) Yeye mwenyewe ‘aliondoka ili kutalii majiji na vijiji vyote vya Galilaya, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya maradhi na kila namna ya udhaifu.’ Yesu alihurumia umati “kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:35, 36) Kisha akiwa ameguswa moyo sana akawaambia wanafunzi wake: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno [Yehova Mungu] atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mathayo 9:37, 38) Miezi sita tu kabla ya kumaliza huduma yake duniani, Yesu aliona kulikuwa na uhitaji wa kuwa na wavunaji huko Yudea pia. (Luka 10:2) Katika pindi zote mbili, aliwatuma wafuasi wake wafanye kazi ya kuvuna.—Mathayo 10:5; Luka 10:3.

      Ujumbe Wetu wa Tumaini

      5. Sisi hutangaza ujumbe wa aina gani?

      5 Tukiwa watumishi wa Yehova wa siku hizi, sisi huitikia kwa furaha mwito wa kuwa wavunaji. Jambo moja ambalo huchangia sana furaha yetu ni kwamba sisi huwapelekea ujumbe wa tumaini wale waliokata tamaa na kushuka moyo. Kama wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza, tuna pendeleo lililoje kutangaza habari njema—ujumbe wa kweli wenye tumaini—kwa wale ambao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’!

      6. Mitume walifanya kazi gani katika karne ya kwanza?

      6 Kufikia katikati ya karne ya kwanza, mtume Paulo alikuwa na shughuli nyingi za kuhubiri habari njema. Hapana shaka alifanikiwa katika kazi yake ya kuvuna, kwa kuwa alipowaandikia Wakristo wa Korintho yapata mwaka wa 55 W.K., alisema: “Nawajulisha nyinyi, akina ndugu, habari njema niliyowatangazia, mliyoipokea pia, ambayo katika hiyo mwasimama pia.” (1 Wakorintho 15:1) Mitume na Wakristo wengine wa mapema walikuwa wavunaji wenye bidii. Ingawa Biblia haituambii ni mitume wangapi waliookoka matukio yenye kuogofya yaliyomalizika kwa kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., tunajua kwamba mtume Yohana alikuwa bado anahubiri miaka 25 hivi baadaye.—Ufunuo 1:9.

      7, 8. Ni ujumbe gani wa tumaini ambao watumishi wa Yehova wamekuwa wakitangaza kwa uharaka zaidi sasa kuliko wakati mwingineo wowote?

      7 Kisha kwa karne nyingi, makasisi waasi-imani wa Jumuiya ya Wakristo ambao ndio “mtu wa uasi-sheria” wakawa ndio wenye kuongoza. (2 Wathesalonike 2:3) Hata hivyo, mwishoni mwa karne ya 19, wale waliojitahidi kuishi kupatana na mafundisho ya Ukristo wa awali, walianza kutangaza ujumbe wa tumaini, ujumbe wa Ufalme. Kwa kweli, tangu toleo lake la kwanza (Julai 1879), gazeti hili limekuwa na vichwa ambavyo vimetia ndani maneno, “Unaotangaza Kuwapo kwa Kristo,” “Unaotangaza Ufalme wa Kristo,” au “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.”

      8 Ufalme wa mbinguni wa Mungu ulisimamishwa mwaka wa 1914 mikononi mwa Yesu Kristo, na sasa tunatangaza ujumbe wa tumaini kwa uharaka zaidi kuliko wakati mwingineo wowote. Kwa nini? Kwa sababu mojawapo ya mambo mazuri yatakayotimizwa na utawala wa Ufalme huo wa Mungu ni kuondolewa hivi karibuni kwa mfumo huu mwovu. (Danieli 2:44) Je, kunaweza kuwa na ujumbe mwingine bora zaidi? Tunapata furaha nyingi sana kwa kushiriki kutangaza Ufalme kabla ya “dhiki kubwa” kuanza.—Mathayo 24:21; Marko 13:10.

      Jinsi ya Kufanikiwa Katika Utafutaji

      9. Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo gani, nao watu waliitikiaje ujumbe wa Ufalme?

      9 Jambo jingine ambalo huchangia furaha yetu tukiwa wavunaji ni mafanikio tunayopata katika kutafuta wale wanaokuwa wanafunzi na kujiunga nasi katika kazi ya kuvuna. Katika mwaka wa 31-32 W.K., Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: “Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mwingiamo, tafuteni kabisa ni nani humo anayestahili.” (Mathayo 10:11) Kama ionyeshwavyo na itikio lao kwa ujumbe wa Ufalme, si watu wote waliostahili. Hata hivyo, wanafunzi wa Yesu walihubiri kwa bidii habari njema kokote ambako watu wangepatikana.

      10. Paulo alitafutaje wale wanaostahili?

      10 Baada ya kifo na ufufuo wa Yesu, kazi ya kutafuta wanaostahili iliendelea kwa bidii. Paulo alisababu na Wayahudi katika masinagogi yao na pia watu waliokuwa sokoni huko Athene. Alipotoa ushahidi kwenye Areopago katika jiji hilo la Ugiriki, “wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini, miongoni mwao pia wakiwamo Dionisio, hakimu wa mahakama ya Areopago, na mwanamke mmoja aitwaye jina Damarisi, na wengine mbali na hao.” Kokote ambako Paulo alienda, aliweka kielelezo kizuri katika kuhubiri “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.”—Matendo 17:17, 34; 20:20.

      11. Ni njia zipi za kufanya huduma zilizotumiwa miaka iliyopita?

      11 Katika miongo ya mwisho ya karne ya 19, Wakristo watiwa-mafuta walitafuta kwa ujasiri wale wanaostahili. Katika makala yenye kichwa, “Walitiwa Mafuta Kuhubiri,” gazeti la Kiingereza Zion’s Watch Tower la Julai/Agosti 1881 lilisema: “Habari njema zinahubiriwa ‘wapole’ walio tayari na wanaoweza kusikiliza ili kutokeza miongoni mwao watawala wenzi wa Kristo ambao ni mwili wake.” Mara nyingi watu waliofanya kazi ya Mungu ya kuvuna waliwafikia watu waliokuwa wakitoka katika makanisa yao na kuwapa trakti zenye ujumbe wa Kimaandiko uliokusudiwa kuamsha upendezi wa wale wanaostahili. Baada ya kuchunguza kwa makini matokeo mazuri ya kutoa ushahidi kwa njia hiyo, gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1903, liliwasihi wavunaji wagawanye trakti “kutoka nyumba hadi nyumba, Jumapili alasiri.”

      12. Tumefanyaje kazi yetu ya kuhubiri iwe na matokeo mazuri zaidi? Toa mfano.

      12 Katika miaka ya karibuni, tumepanua huduma yetu kwa kuzungumza na watu mahali kwingineko badala ya nyumbani kwao. Njia hiyo imekuwa na matokeo mazuri katika nchi ambako kwa sababu ya hali za kiuchumi na kufuatilia mambo ya starehe, watu hawapatikani nyumbani tunapowatembelea. Wakati Mashahidi wawili kutoka Uingereza walipoona kwamba wageni walikuwa wakiondoka kwa ukawaida kwa basi baada ya kujifurahisha kwa siku moja kwenye ufuo wa bahari, walipiga moyo konde, wakapanda basi hizo na kuwatolea wasafiri magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Waligawanya nakala 229 za magazeti hayo kwa muda wa mwezi mmoja. Wanaripoti hivi: “Kwa sababu tunajua kwamba Yehova yu pamoja nasi daima, sisi hatuogopi kutoa ushahidi kwenye ufuo wa bahari, maeneo ya biashara, au maeneo mengineyo magumu.” Walipata watu waliokubali kupelekewa magazeti kwa ukawaida, wakaanzisha funzo la Biblia, na wote wawili wakatumikia wakiwa mapainia-wasaidizi.

      13. Ni marekebisho gani katika huduma yetu yanayohitajika katika maeneo fulani?

      13 Tunapoendelea kutafuta wanaostahili, huenda tukahitaji kuchunguza huduma yetu kwa makini katika maeneo fulani. Imekuwa kawaida kwa Mashahidi wengi kushiriki mahubiri ya kutoka nyumba hadi nyumba Jumapili asubuhi. Lakini wameona kwamba hawapati matokeo sana katika maeneo fulani wanapotembelea watu Jumapili asubuhi kwa sababu huenda wenye nyumba wakawa wanalala. Mashahidi wengi wamerekebisha ratiba yao na sasa wanatafuta watu baadaye mchana, labda baada ya mikutano ya Kikristo. Na utafutaji huo umefanikiwa kwelikweli. Mwaka uliopita idadi ya watangazaji wa Ufalme iliongezeka kwa asilimia 2.3. Jambo hilo humtukuza Bwana-mkubwa wa mavuno na hutufurahisha.

      Dumisheni Amani Katika Kazi ya Kuvuna

      14. Tunapeleka ujumbe wetu tukiwa na mtazamo gani, na kwa nini?

      14 Sababu nyingine inayofanya tuwe wenye furaha inahusiana na mtazamo wa kudumisha amani tunapofanya kazi ya kuvuna. “Mnapokuwa mkiingia ndani ya hiyo nyumba,” Yesu akasema, “salimuni hao watu wa nyumbani; na ikiwa hiyo nyumba inastahili, acheni amani mwitakiayo ije juu yayo.” (Mathayo 10:12, 13) Salamu hiyo katika Kiebrania na pia katika Kigiriki cha Biblia humaanisha ‘Nakutakia mema.’ Mtazamo huo ndio hutuongoza tunapowahubiria watu habari njema. Tunatumaini kwamba wataitikia ifaavyo ujumbe wa Ufalme. Wale wanaoitikia wana taraja la kupatanishwa na Mungu wanapotubu dhambi zao, kugeuka na kufanya mapenzi yake. Amani pamoja na Mungu huongoza kwenye uhai udumuo milele.—Yohana 17:3; Matendo 3:19; 13:38, 48; 2 Wakorintho 5:18-20.

      15. Tunawezaje kudumisha mtazamo wa amani hata watu wasipoitikia ifaavyo tunapohubiri?

      15 Tunaweza kudumishaje amani yetu hata watu wasipoitikia ifaavyo? Yesu aliagiza: “Ikiwa [nyumba hiyo] haistahili, acheni amani itokayo kwenu irudi juu yenu.” (Mathayo 10:13) Simulizi la Luka kuhusu kutumwa kwa wanafunzi 70 latia ndani maneno haya ya Yesu: “Ikiwa rafiki wa amani yumo, amani yenu itatulia juu yake. Lakini ikiwa hayumo, itawarudia nyinyi.” (Luka 10:6) Tunapozungumza na watu habari njema, tunafanya hivyo kwa njia ifaayo tukiwa wachangamfu na wenye amani. Ikiwa mwenye nyumba anaonyesha ubaridi, analalamika, au anasema jambo fulani baya, basi tutaacha ujumbe wetu wa amani ‘uturudie.’ Lakini mambo hayo hayatukoseshi amani, ambayo ni mojawapo ya matunda ya roho takatifu ya Yehova.—Wagalatia 5:22, 23.

      Mradi Mzuri kwa Wavunaji

      16, 17. (a) Tunakuwa na mradi gani tunapofanya ziara za kurudia? (b) Tunaweza kuwasaidiaje wale walio na maswali ya Biblia?

      16 Tukiwa wavunaji tunafurahi kushiriki kukusanya watu kwa ajili ya uhai udumuo milele. Nasi hufurahi kama nini wakati mtu tunayehubiria anapoitikia ifaavyo na kutaka kujifunza mengi zaidi, na kuwa “rafiki wa amani”! Labda ana maswali mengi ya Biblia na tunaona kwamba haiwezekani kuyajibu yote katika ziara moja. Kwa kuwa huenda isifae kukaa sana wakati wa ziara ya kwanza, tunaweza kufanya nini? Tunaweza kuweka mradi kama ule uliopendekezwa miaka 60 iliyopita.

      17 “Mashahidi wote wa Yehova wapaswa kuwa tayari kuongoza mafunzo ya kigezo ya Biblia.” Maneno hayo yalikuwa katika kijitabu cha tatu katika mfululizo wa vijitabu viitwavyo Funzo la Kigezo (Model Study) vilivyochapishwa kuanzia mwaka wa 1937 hadi 1941. Kijitabu hicho kiliendelea kusema: “Watangazaji wote [wa Ufalme] wapaswa kuwa na bidii kuwasaidia katika kila njia iwezekanayo watu wenye nia njema wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Wapaswa kuwarudia watu hao na kujibu maswali mbalimbali . . . , kisha kuanzisha funzo la kigezo . . . haraka iwezekanavyo.” Naam, tunafanya ziara za kurudia tukiwa na mradi wa kuanzisha funzo la Biblia nyumbani na kuliongoza kwa ukawaida.a Kuwa wenye urafiki na kumhangaikia kwa upendo mtu anayependezwa hutuchochea kutayarisha vema na kuongoza funzo kwa mafanikio.

      18. Tunaweza kuwasaidiaje wapya wawe wanafunzi wa Yesu Kristo?

      18 Kwa msaada wa kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele na broshua kama vile Mungu Anataka Tufanye Nini?, tunaweza kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani yenye matokeo na hivyo kushiriki kuwasaidia waliopendezwa karibuni kuwa wanafunzi. Tunapojitahidi kumwiga Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, yaelekea wanafunzi hao wa Biblia watajifunza pia kutokana na amani na furaha yetu, unyofu wetu, na heshima yetu kwa viwango na miongozo ya Yehova. Tunapowasaidia wapya kupata majibu ya maswali yao, acheni tufanye yote tuwezayo kuwafunza jinsi ya kujibu wale wanaowauliza maswali. (2 Timotheo 2:1, 2; 1 Petro 2:21) Tukiwa wavunaji wa mfano, hapana shaka tunaweza kuwa wenye furaha kwamba mwaka uliopita wa utumishi, wastani wa mafunzo ya Biblia ya nyumbani 4,766,631 yaliongozwa ulimwenguni pote. Tunafurahi hasa iwapo sisi binafsi tu miongoni mwa wavunaji wanaoshiriki kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani.

      Endelea Kufurahia Kazi ya Kuvuna

      19. Kwa nini kulikuwa na sababu nzuri za kufurahia kazi ya kuvuna wakati wa huduma ya Yesu na muda mfupi baadaye?

      19 Kulikuwa na sababu nzuri za kufurahia kazi ya kuvuna wakati wa huduma ya Yesu na muda mfupi baadaye. Wakati huo wengi waliitikia ifaavyo habari njema. Walifurahi hata zaidi wakati wa Pentekoste 33 W.K., kwa kuwa watu wapatao 3,000 walikubali mwelekezo wa Petro, wakapokea roho takatifu ya Mungu, na kuwa sehemu ya taifa la Mungu la Israeli wa kiroho. Naam, idadi yao iliendelea kuongezeka, na furaha ikazidi kuwa nyingi kwa kuwa ‘Yehova aliendelea kuongeza kwao kila siku wale wenye kuokolewa.’—Matendo 2:37-41, 46, 47; Wagalatia 6:16; 1 Petro 2:9.

      20. Ni nini ambacho hutuletea furaha nyingi katika kazi yetu ya kuvuna?

      20 Wakati huo, unabii huu wa Isaya ulikuwa unatimia: “[Ewe Yehova] umeliongeza taifa, umezidisha furaha yao; wanafurahi mbele zako, kama furaha ya wakati wa mavuno, kama watu wafurahivyo wagawanyapo nyara.” (Isaya 9:3) Ingawa leo tunaona kwamba taifa hilo la watiwa-mafuta ‘limeongezwa’ na karibu limekamilika kabisa, tunafurahi sana tunapoona idadi ya wavunaji wengine ikiongezeka mwaka baada ya mwaka.—Zaburi 4:7; Zekaria 8:23; Yohana 10:16.

      21. Tutazungumzia nini katika makala ifuatayo?

      21 Bila shaka tuna sababu nzuri za kuendelea kufurahia kazi ya kuvuna. Ujumbe wetu wa tumaini, kutafuta wanaostahili, na mtazamo wetu wa kudumisha amani, hutuletea furaha tukiwa wavunaji. Hata hivyo, mambo hayo huwachochea wengi watende isivyofaa. Mtume Yohana alitendwa isivyofaa. Alifungwa kwenye kisiwa cha Patmosi “kwa ajili ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” (Ufunuo 1:9) Basi, tunaweza kudumishaje furaha tunaponyanyaswa na kupingwa? Ni nini kitakachotusaidia kukabiliana na mtazamo wa wengi tunaohubiria sasa ambao unazidi kuwa mgumu? Makala yetu ifuatayo inatoa msaada wa Kimaandiko katika kujibu maswali hayo.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwanza, mafunzo yalipangwa katika sehemu ambako vikundi vya watu wanaopendezwa wangeweza kukusanywa pamoja. Hata hivyo, muda si muda mafunzo pia yalifanywa na watu mmoja-mmoja au familia—Ona kichapo Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 574, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Endeleeni Katika Kazi ya Kuvuna!
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Julai 15
    • Endeleeni Katika Kazi ya Kuvuna!

      “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha.”—ZABURI 126:5.

      1. Kwa nini ‘tumwombe Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi’ leo?

      BAADA ya safari ya tatu ya Yesu Kristo kwenda kuhubiri huko Galilaya, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” (Mathayo 9:37) Hali ilikuwa vivyo hivyo huko Yudea. (Luka 10:2) Hali ikoje leo, ikiwa mavuno yalikuwa mengi karibu miaka 2,000 iliyopita? Katika mwaka uliopita wa utumishi, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 6,000,000 waliendelea na kazi yao ya uvunaji wa mfano miongoni mwa watu 6,000,000,000 ulimwenguni, ambao wengi wao ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ Kwa hiyo, kama ilivyokuwa karne zilizopita, leo himizo la Yesu kwamba ‘tuombe Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake’ linafaa.—Mathayo 9:36, 38.

      2. Ni nini ambacho hufanya tutambuliwe na watu?

      2 Yehova Mungu aliye Bwana-mkubwa wa mavuno, amejibu ombi la kutuma wafanyakazi zaidi. Inafurahisha kama nini kushiriki katika kazi hii ya kuvuna inayoelekezwa na Mungu! Ingawa sisi ni wachache tukilinganishwa na mataifa, kuhubiri Ufalme kwa bidii na kufanya wanafunzi hufanya tutambuliwe na watu. Katika nchi nyingi tunatajwa sana katika vyombo vya habari. Katika vipindi fulani vya televisheni waigizaji wamesikika wakisema, ‘hao ni Mashahidi wa Yehova,’ mlango unapobishwa. Naam, utendaji wetu wa Kikristo tukiwa wavunaji wa mfano unajulikana sana katika karne hii ya 21.

      3. (a) Tunajuaje kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme ya karne ya kwanza ilitambuliwa? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba malaika wanategemeza huduma yetu?

      3 Katika karne ya kwanza watu pia walitambua kuhubiriwa kwa Ufalme nao waliwanyanyasa watangazaji wa habari njema. Hivyo, mtume Paulo aliandika: “Yaonekana kwangu kwamba Mungu ametuweka sisi mitume mwisho katika wonyesho wa hadharani kama watu waliowekewa kifo, kwa sababu [sisi mitume] tumekuwa kitu cha kutazamwa mahali pa michezo kwa ulimwengu, na kwa malaika, na kwa wanadamu.” (1 Wakorintho 4:9) Vivyo hivyo, kuendelea kwetu kutangaza Ufalme licha ya mnyanyaso hufanya tutambuliwe na watu, jambo ambalo ni muhimu kwa malaika. Andiko la Ufunuo 14:6 lasema: “Nami [mtume Yohana] nikaona malaika mwingine akiruka katika mbingu ya kati, naye alikuwa na habari njema idumuyo milele ili aitangaze kuwa taarifa za mteremo kwa wale wakaao juu ya dunia, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” Naam, tunategemezwa na malaika katika huduma yetu—kazi yetu ya kuvuna!—Waebrania 1:13, 14.

      “Vitu vya Kuchukiwa”

      4, 5. (a) Yesu aliwapa wanafunzi wake onyo gani? (b) Kwa nini watumishi wa Mungu wa leo ni “vitu vya kuchukiwa”?

      4 Mitume wa Yesu walipotumwa kuwa wavunaji, walitii agizo lake la kuwa “wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa.” Yesu aliongezea kusema: “Jilindeni dhidi ya watu; kwa maana watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa. . . . Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 10:16-22.

      5 Leo sisi ni “vitu vya kuchukiwa” kwa sababu “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu,” Shetani Ibilisi, ambaye ni adui mkuu wa Mungu na watu Wake. (1 Yohana 5:19) Ingawa adui zetu huona mafanikio yetu ya kiroho wao hawakubali kwamba mafanikio hayo yametokana na Yehova. Wapinzani huona jinsi tunavyofurahia kazi ya kuvuna. Wao hustaajabu kuona jinsi tulivyo na umoja! Huenda wakakiri shingo upande kwamba tuna umoja wanaposafiri nchi nyingine na kuona kwamba kazi ile Mashahidi wa Yehova wanayofanya huko ndiyo ileile wanayofanya nchini mwao. Bila shaka, tunajua kwamba katika wakati ufaao, hata adui zetu watamtambua Yehova, ambaye ndiye mtegemezaji wetu na chanzo cha umoja wetu.—Ezekieli 38:10-12, 23.

      6. Tuna uhakikisho gani tunaposhiriki katika kazi ya kuvuna, lakini ni swali gani linalozuka?

      6 Bwana-mkubwa wa mavuno amempa Mwana wake, Yesu Kristo, “mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Hivyo, Yehova humtumia Yesu kuelekeza kazi ya kuvuna hapa duniani kupitia malaika wa mbinguni na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye ametiwa mafuta. (Mathayo 24:45-47; Ufunuo 14:6, 7) Lakini tunawezaje kukabili upinzani wa adui zetu na bado tudumishe furaha yetu tunapoendelea na kazi ya kuvuna?

      7. Yatupasa kujitahidi kudumisha mtazamo gani tunapopingwa au kunyanyaswa?

      7 Tunapokabili upinzani au hata mnyanyaso wa moja kwa moja, acheni tutafute msaada wa Mungu ili tudumishe mtazamo kama wa Paulo. Aliandika: “Tunapotukanwa, twabariki; tunaponyanyaswa, twahimili; tunapoharibiwa sifa, twasihi sana.” (1 Wakorintho 4:12, 13) Mara kwa mara mtazamo huo pamoja na huduma yetu ya hadharani tunayofanya kwa busara, hubadili mtazamo wa wapinzani.

      8. Unapata uhakikisho gani kutokana na maneno ya Yesu kwenye Mathayo 10:28?

      8 Hata tisho la kifo halipunguzi bidii yetu tukiwa wavunaji. Tunatangaza kwa ujasiri ujumbe wa Ufalme waziwazi kadiri iwezekanavyo. Nasi hupata uhakikisho wenye kutia moyo kutokana na maneno haya ya Yesu: “Msiwe wenye kuwahofu wale wauuao mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mhofuni yeye awezaye kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:28) Tunajua kwamba Baba yetu wa mbinguni ndiye Mpaji wa uhai. Yeye huwathawabisha wale wanaodumisha uaminifu-maadili kwake na kuendelea kuvuna kwa uaminifu.

      Ujumbe Wenye Kuokoa Uhai

      9. Watu wengine waliyaonaje maneno ya Ezekieli, na hali ikoje leo?

      9 Nabii Ezekieli alipotangaza kwa ujasiri ujumbe wa Yehova kwa “mataifa wanaoasi,” yaani, falme za Israeli na Yuda, watu fulani walipendezwa na yale aliyosema. (Ezekieli 2:3) “Tazama,” Yehova akasema, “wewe umekuwa kwao kama wimbo mzuri sana, wa mtu mwenye sauti ipendezayo, awezaye kupiga kinanda vizuri.” (Ezekieli 33:32) Ingawa walipendezwa na maneno ya Ezekieli, walishindwa kutenda kupatana nayo. Hali ikoje leo? Wakati watiwa-mafuta na wenzao wanapotangaza ujumbe wa Yehova kwa ujasiri, wengine hupenda kusikia juu ya baraka za Ufalme, lakini hawaitikii kwa uthamini, wawe wanafunzi, na kujiunga na kazi ya kuvuna.

      10, 11. Katika nusu ya kwanza ya karne ya 20, ni nini kilichofanywa ili kutangaza ujumbe wetu wenye kuokoa uhai, na matokeo yalikuwa nini?

      10 Kwa upande mwingine, wengine wameitikia ifaavyo kazi ya kuvuna na wameshiriki kutangaza ujumbe wa Mungu. Kwa mfano, wakati wa mfululizo wa mikusanyiko ya Kikristo iliyoanza mwaka wa 1922 hadi 1928, ujumbe wa hukumu juu ya mfumo wa mambo wa Shetani ulio mwovu ulitangazwa waziwazi. Vituo vya redio vilitangaza hukumu hizo zilizotolewa kwenye makusanyiko. Baadaye, watu wa Mungu waligawanya mamilioni ya nakala zenye ujumbe huo.

      11 Mwishoni mwa miaka ya 1930, kazi ya kutoa ushahidi ilianza kufanywa kwa njia nyingine—maandamano ya kutangaza habari. Mwanzoni, watu wa Yehova walivaa mabango yaliyotangaza hotuba za watu wote. Baadaye walibeba mabango yakiwa na maneno kama “Dini ni mtego na hila” na “Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme.” Walipoandamana barabarani, walivutia wapita-njia. ‘Jambo hilo lilifanya Mashahidi wa Yehova wajulikane sana na kuwafanya wawe jasiri,’ akaeleza ndugu mmoja ambaye alishiriki kwa ukawaida katika kazi hiyo kwenye barabara zenye watu wengi za London, Uingereza.

      12. Mbali na ujumbe wa hukumu ya Mungu, tumekazia nini katika huduma yetu, na ni nani ambao sasa wameungana kuhubiri habari njema?

      12 Tunapotangaza ujumbe wa hukumu ya Mungu, sisi pia hukazia baraka zilizoahidiwa ambazo ni sehemu ya ujumbe wa Ufalme. Kutoa ushahidi kwa ujasiri ulimwenguni hutusaidia kutafuta wanaostahili. (Mathayo 10:11) Wengi wa mabaki ya watiwa-mafuta waliitikia wito wa kuvuna katika miaka ya 1920 na 1930. Kisha kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1935, habari nzuri zilitolewa kuhusu baraka ambazo “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” watapata katika paradiso duniani wakati ujao. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Wamesikiliza ujumbe wa hukumu ya Mungu na wameungana na watiwa-mafuta katika kuhubiri habari njema zenye kuokoa uhai.

      13, 14. (a) Tunaweza kupata faraja gani kutokana na Zaburi 126:5, 6? (b) Tukiendelea kupanda na kutia maji matokeo yatakuwa nini?

      13 Watu wanaofanya kazi ya Mungu ya kuvuna, na hasa wale wanaonyanyaswa, wanapata faraja kubwa kutokana na maneno haya ya Zaburi 126:5, 6: “Wapandao kwa machozi watavuna kwa kelele za furaha. Ingawa mtu anakwenda zake akilia, azichukuapo mbegu za kupanda. Hakika atarudi kwa kelele za furaha, aichukuapo miganda yake.” Maneno ya mtunga-zaburi kuhusu kupanda na kuvuna yanaonyesha jinsi Yehova alivyowajali na kuwabariki mabaki ambao walirudi kutoka utekwani Babiloni ya kale. Walifurahia sana kuwekwa huru, lakini huenda walilia walipopanda mbegu kwenye ardhi iliyokuwa ukiwa ambayo haikuwa imelimwa kwa muda wa miaka 70 walipokuwa uhamishoni. Hata hivyo, wale walioendelea na kazi ya kupanda na kujenga walipata matokeo na uradhi.

      14 Huenda tukalia tunapojaribiwa au wakati sisi au waamini wenzetu wanapoteseka kwa sababu ya uadilifu. (1 Petro 3:14) Huenda mwanzoni kazi yetu ya kuvuna isiwe rahisi kwa sababu inaweza kuonekana kana kwamba jitihada zetu katika huduma hazina matokeo. Lakini tukiendelea kupanda na kutia maji, mara nyingi Mungu atakuza kwa kadiri tusiyotarajia. (1 Wakorintho 3:6) Jambo hilo linadhihirishwa na matokeo ya ugawanyaji wetu wa Biblia na vichapo vinavyotegemea Maandiko.

      15. Toa mfano wa manufaa ya vichapo vya Kikristo katika kazi ya kuvuna.

      15 Fikiria mfano wa mwanamume aitwaye Jim. Mamake alipokufa, alipata miongoni mwa vitu vyake nakala ya kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation?a Alikisoma kwa makini. Alipozungumza na Shahidi mmoja aliyekutana naye barabarani, Jim alikubali Shahidi huyo amtembelee na funzo la Biblia likaanzishwa. Jim alifanya maendeleo ya kiroho haraka, akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Aliwaambia watu wengine katika familia yake mambo aliyokuwa amejifunza. Hivyo, dada yake na ndugu yake wakawa Mashahidi wa Yehova, na baadaye Jim akapata pendeleo la kujitolea kutumikia wakati wote kwenye Betheli huko London.

      Wadumisha Furaha Licha ya Mnyanyaso

      16. (a) Kwa nini tumefanikiwa katika kazi ya kuvuna? (b) Yesu alitoa onyo gani kuhusu matokeo ya habari njema, lakini sisi huzungumza na watu tukiwa na mtazamo gani?

      16 Kwa nini kumekuwa na mafanikio hayo katika kazi ya kuvuna? Kwa sababu Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wametii maagizo ya Yesu: “Lile niwaambialo nyinyi katika giza, lisemeni katika nuru; na lile msikialo lanong’onwa, lihubirini kutoka paa za nyumba.” (Mathayo 10:27) Hata hivyo, tunaweza kutarajia magumu, kwa kuwa Yesu alionya: “Ndugu atakabidhi ndugu kwenye kifo, na baba mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe.” Yesu aliendelea kusema: “Msifikiri nilikuja kuweka amani juu ya dunia; nilikuja kuweka, si amani, bali upanga.” (Mathayo 10:21, 34) Yesu hakuwa na nia ya kutenganisha familia kimakusudi. Lakini nyakati nyingine habari njema zingetenganisha familia. Ndivyo ilivyo kwa watumishi wa Mungu leo. Tunapotembelea familia, nia yetu si kuzitenganisha. Tunatamani kila mtu akubali habari njema. Kwa hiyo, tunajaribu kuzungumza na kila mshiriki wa familia kwa njia ya fadhili na ya huruma na hilo hufanya ujumbe wetu uvutie wale ‘walio na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’—Matendo 13:48.

      17. Wale wanaouunga mkono enzi kuu ya Mungu wanakuwaje tofauti, na tuna mfano gani wa jambo hilo?

      17 Ujumbe wa Ufalme umewafanya wale wanaounga mkono enzi kuu ya Mungu wawe tofauti. Kwa mfano, fikiria jinsi waabudu wenzetu walivyojitokeza kuwa tofauti kwa sababu ‘walilipa Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu’ wakati wa Utawala wa Nazi huko Ujerumani. (Luka 20:25) Tofauti na viongozi wa kidini na wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ambao ni Wakristo kwa jina tu, watumishi wa Yehova walikuwa thabiti, wakakataa kuvunja kanuni za Biblia. (Isaya 2:4; Mathayo 4:10; Yohana 17:16) Profesa Christine King, mwandishi wa kitabu The Nazi State and the New Religions, alisema: ‘Utawala wa [Nazi] ulishindwa na Mashahidi pekee, kwa kuwa ingawa utawala huo uliwaua kwa wingi, wao waliendelea na kazi yao ya kutoa ushahidi na mnamo Mei 1945, Mashahidi wa Yehova walikuwa bado wanaendelea na kazi yao ilhali Utawala wa Nazi ulikuwa umetoweka.’

      18. Watu wa Yehova huonyesha mtazamo gani licha ya mnyanyaso?

      18 Mtazamo ambao huonyeshwa na watu wa Yehova wanapokabili mnyanyaso ni muhimu sana. Ingawa huenda wenye mamlaka katika ulimwengu wakavutiwa na imani yetu, wao hustaajabu kwamba sisi hatuna chuki wala uchungu. Kwa mfano, mara nyingi Mashahidi waliookoka yale Maangamizi Makubwa ya Nazi huonyesha furaha na uradhi wanapokumbuka mambo yaliyowapata. Wanajua kwamba Yehova aliwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Wakorintho 4:7) Baadhi yetu ambao ni watiwa-mafuta wana uhakika kwamba ‘majina yao yameandikwa mbinguni.’ (Luka 10:20) Uvumilivu wao hutokeza tumaini ambalo haliongozi kwenye kukata tamaa, nao wavunaji waaminifu wanaotarajia kuishi duniani wana uhakika huo.—Waroma 5:4, 5.

      Endelea na Kazi ya Kuvuna

      19. Ni njia zipi zenye matokeo ambazo zimetumiwa katika huduma ya Kikristo?

      19 Hatujui ni kwa muda mrefu kadiri gani Yehova ataturuhusu tufanye kazi ya uvunaji wa mfano. Kwa sasa, yatupasa kukumbuka kwamba wavunaji wana njia mahususi za kufanya kazi yao. Vivyo hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba uaminifu wetu katika kutumia njia za kuhubiri zilizojaribiwa utakuwa na matokeo. Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Nawasihi sana nyinyi, iweni waigaji wangu.” (1 Wakorintho 4:16) Paulo alipokutana na wazee wa Efeso huko Mileto, aliwakumbusha kwamba yeye hakuepuka kuwafundisha “hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.” (Matendo 20:20, 21) Timotheo, mwandamani wa Paulo, alijifunza njia za mtume huyo za kufundisha kwa hiyo angeweza kuwafunza Wakorintho njia hizo. (1 Wakorintho 4:17) Mungu alibariki njia za Paulo za kufundisha, kama vile atakavyobariki uvumilivu wetu katika kuhubiri habari njema hadharani kutoka nyumba hadi nyumba, kwenye ziara za kurudia, kwenye mafunzo ya Biblia, na popote pale watu wanapoweza kupatikana.—Matendo 17:17.

      20. Yesu alionyeshaje kwamba uvunaji mkubwa wa kiroho ulikuwa karibu, na jambo hilo limethibitikaje kuwa kweli katika miaka ya karibuni?

      20 Baada ya kumtolea ushahidi mwanamke Msamaria karibu na Sikari mwaka wa 30 W.K., Yesu alizungumzia uvunaji wa kiroho. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Inueni macho yenu mtazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa. Tayari mvunaji anapokea mshahara na kukusanya matunda kwa ajili ya uhai udumuo milele, ili mpanzi na mvunaji wapate kushangilia pamoja.” (Yohana 4:34-36) Labda Yesu alikuwa tayari ameona matokeo ya mazungumzo yake na mwanamke Msamaria, kwa kuwa kutokana na ushuhuda wa mwanamke huyo, wengi walimwamini Yesu. (Yohana 4:39) Katika miaka ya karibuni, nchi mbalimbali zimeondolea Mashahidi wa Yehova vizuizi au kuhalalisha kazi yao, hivyo kutokeza maeneo mapya ya kuvunwa. Matokeo yamekuwa kwamba uvunaji mkubwa wa kiroho unaendelea. Naam, ulimwenguni pote tunapata baraka nyingi tunapoendelea kwa furaha na uvunaji wa kiroho.

      21. Kwa nini tuna sababu ya kuendelea tukiwa wavunaji wenye furaha?

      21 Mavuno yanapokuwa tayari, lazima wafanyakazi wavune kwa uharaka. Lazima wafanye kazi bila kukawia. Leo, tunahitaji kufanya kazi kwa bidii na kwa uharaka kwa sababu tunaishi katika “wakati wa mwisho.” (Danieli 12:4) Naam, tunakabili majaribu, lakini leo kuna uvunaji mkubwa wa waabudu wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote. Kwa hiyo, hii ni siku ya kushangilia. (Isaya 9:3) Basi, tukiwa wavunaji wenye furaha, acheni tuendelee na kazi ya kuvuna!

      [Maelezo ya Chini]

      a Kilichochapishwa na kugawanywa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki