Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Desemba 1
    • Wachukiwa kwa Sababu ya Imani Yao

      “Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.”—MATHAYO 10:22.

      1, 2. Je, waweza kusimulia mambo halisi yaliyoonwa ambayo Mashahidi wa Yehova wamevumilia kwa sababu ya kutenda kulingana na itikadi zao za kidini?

      MWENYE duka mmoja anayefuatia haki wa kisiwa cha Krete akamatwa zaidi ya mara nyingi na kupelekwa tena na tena mbele ya mahakama za Ugiriki. Kwa jumla, yeye atumikia kifungo cha zaidi ya miaka sita gerezani, mbali na mke wake na watoto wake watano. Huko Japani mwanafunzi mwenye umri wa miaka 17 afukuzwa shuleni, ingawa yeye ni mwenye tabia njema na huwa wa kwanza katika darasa lake lenye wanafunzi 42. Katika Ufaransa watu wengi sana waachishwa kazi mara moja, hata ingawa wana sifa nzuri sana ya kufanya kazi kwa bidii na kwa kudhamiria. Mambo hayo halisi yaliyoonwa yana ufanani gani?

      2 Watu wote wanaohusika ni Mashahidi wa Yehova. “Uhalifu” wao ni nini? Kimsingi, ni kutenda kulingana na itikadi zao za kidini. Kwa kutii mafundisho ya Yesu Kristo, huyo mwenye duka alikuwa akifundisha wengine imani yake. (Mathayo 28:19, 20) Alipatikana na hatia chini ya sheria ya kale ya Ugiriki ambayo hufanya kugeuza watu imani kuwe kosa la jinai. Yule mwanafunzi alifukuzwa kwa sababu dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia haingemruhusu ashiriki mazoezi ya kendo (ustadi wa Kijapani wa kupigana kwa upanga). (Isaya 2:4) Nao walioachishwa kazi katika Ufaransa walijulishwa kwamba sababu pekee ya kufukuzwa kwao ilikuwa kwamba, walijitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova.

      3. Kwa nini kuteseka sana kwa Mashahidi wa Yehova mikononi mwa wanadamu wengine si tukio la kawaida kwa kulinganishwa?

      3 Magumu hayo yaliyowapata ni mifano hasa ya yale ambayo Mashahidi wa Yehova wamevumilia hivi majuzi katika nchi fulani. Hata hivyo, kwa Mashahidi wa Yehova walio wengi, kuteseka sana mikononi mwa wanadamu wengine ni tukio lisilo la kawaida kwa kulinganishwa. Watu wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa sababu ya mwenendo wao mwema—sifa ambayo haimpi mtu yeyote sababu halali ya kuwadhuru. (1 Petro 2:11, 12) Wao hawali njama au kushiriki katika mwenendo wenye kuumiza. (1 Petro 4:15) Kinyume cha hilo, wao hujaribu kuishi kupatana na kanuni ya Biblia ya kuwa wenye kujitiisha kwanza kwa Mungu, kisha kwa serikali za kilimwengu. Wao hulipa kodi zitakwazo na sheria na hujitahidi sana ‘kuwa wenye kufanya amani na watu wote.’ (Waroma 12:18; 13:6, 7; 1 Petro 2:13-17) Katika kazi yao ya kufundisha Biblia, wao hutia watu moyo wastahi sheria, kanuni za kifamilia, na maadili. Serikali nyingi zimewasifu kwa kuwa raia wenye kutii sheria. (Waroma 13:3) Hata hivyo, kama vile fungu la kwanza lionyeshavyo, nyakati nyingine wamekuwa shabaha ya mnyanyaso—hata kupigwa marufuku na serikali katika nchi fulani. Je, hilo litushangaze?

      “Gharama” ya Kuwa Mwanafunzi

      4. Kulingana na Yesu, mtu angeweza kutarajia nini anapokuwa mmoja wa wanafunzi wake?

      4 Yesu Kristo alionyesha waziwazi kinachohusishwa na kuwa mwanafunzi wake. “Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake,” akawaambia wafuasi wake. “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” Yesu alichukiwa “bila sababu.” (Yohana 15:18-20, 25; Zaburi 69:4; Luka 23:22) Wanafunzi wake wangetarajia kufanyiwa hivyohivyo—kunyanyaswa bila msingi halali. Aliwaonya mara nyingi hivi: “mtakuwa vitu vya kuchukiwa.”—Mathayo 10:22; 24:9.

      5, 6. (a) Ni kwa sababu gani Yesu aliwahimiza waliotazamiwa kuwa wafuasi wake ‘wakadirie gharama?’ (b) Kwa nini basi tusitatanike tunapokabili upinzani?

      5 Kwa sababu hiyo, Yesu aliwahimiza waliotazamiwa kuwa wafuasi ‘wakadirie gharama’ ya kuwa wanafunzi. (Luka 14:28, Biblia Habari Njema) Kwa nini? Si ili waamue kama watakuwa wafuasi wake au la, bali ni ili waazimie kutimiza yanayohusika. Ni lazima tuwe tayari kuvumilia majaribu yoyote au magumu ambayo huambatana na pendeleo hilo. (Luka 14:27) Hakuna yeyote atulazimishaye kumtumikia Yehova tukiwa wafuasi wa Kristo. Ni uamuzi wa hiari na pia wenye kutegemea ujuzi. Twajua kimbele kwamba zaidi ya baraka ambazo sisi hupata kutokana na kuingia katika uhusiano ulio wakfu pamoja na Mungu, tutakuwa “vitu vya kuchukiwa.” Kwa hiyo sisi hatutataniki tukabilipo upinzani. ‘Tumekadiria gharama,’ na tuko tayari kabisa kuilipa.—1 Petro 4:12-14.

      6 Kwa nini wengine, kutia ndani mamlaka fulani za kiserikali, watake kupinga Wakristo wa kweli? Ili kupata jibu, inafaa kuchunguza vikundi viwili vya kidini vya karne ya kwanza W.K. Vikundi vyote viwili vilichukiwa—lakini kwa sababu tofauti kabisa.

      Wenye Kuchukia na Kuchukiwa

      7, 8. Ni mafundisho gani yaliyodhihirisha kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, na ni mtazamo gani uliositawi miongoni mwa Wayahudi kama tokeo?

      7 Kufikia karne ya kwanza W.K., Israeli lilikuwa chini ya utawala wa Waroma, na kwa ujumla, dini ya Kiyahudi, yaani, mfumo wa kidini wa Kiyahudi, ilikandamizwa na viongozi kama vile Mafarisayo na waandishi. (Mathayo 23:2-4) Viongozi hao washupavu walizichukua kanuni za Sheria ya Kimusa kuhusu kujitenga na mataifa na kuzipotoa ili zifanye kudharauliwa kwa wasio Wayahudi kuwe takwa. Katika kufanya hivyo, walitokeza dini iliyofanya wasio Wayahudi wachukiwe, nao wasio Wayahudi wakawachukia Wayahudi pia.

      8 Haikuwa vigumu kwa viongozi wa kidini kutetea kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, kwa kuwa wakati huo Wayahudi waliwaona wasio Wayahudi kuwa viumbe wenye kuchukiza. Viongozi wa kidini walifundisha kwamba mwanamke Myahudi hapaswi kuwa peke yake pamoja na wasio Wayahudi, kwa kuwa “wanashukiwa kuwa waasherati.” Mwanamume Myahudi hapaswi “kubaki peke yake pamoja nao kwa kuwa wanashukiwa kumwaga damu.” Maziwa yaliyokamwa na asiye Myahudi hayangeweza kutumiwa isipokuwa Myahudi awe alikuwapo ili kutazama ukamaji huo. Kwa sababu ya uvutano wa viongozi wao, Wayahudi walisitawisha hali ya kujitenga na ya kutojihusisha kabisa na wengine.—Linganisha Yohana 4:9.

      9. Ufundishaji wa viongozi Wayahudi kuhusu wasio Wayahudi ulikuwa na matokeo gani?

      9 Mafundisho hayo kuwahusu wasio Wayahudi hayakusaidia kukuza mahusiano mazuri baina ya Wayahudi na wasio Wayahudi. Wasio Wayahudi walikuja kuwaona Wayahudi kuwa wachukiaji wa wanadamu wote. Tacitus, mwanahistoria Mroma (aliyezaliwa yapata mwaka wa 56 W.K.), alisema kuwahusu Wayahudi kwamba “wanawachukia wanadamu wale wengine wote sawa na vile wanavyowachukia maadui.” Tacitus pia alidai kwamba wasio Wayahudi waliopata kuwa wageuzwa-imani wa Kiyahudi walifundishwa kukana nchi yao na kutoheshimu familia zao na rafiki zao. Kwa ujumla, Waroma waliwavumilia Wayahudi, ambao walikuwa wengi sana wasiweze kushambuliwa. Lakini uasi wa Wayahudi mwaka wa 66 W.K. ulichochea ulipizaji kisasi wenye ukatili wa Waroma, ukiongoza kwenye kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.

      10, 11. (a) Sheria ya Kimusa ilitaka wageni watendeweje? (b) Twajifunza nini kutokana na yaliyoipata Dini ya Kiyahudi?

      10 Maoni hayo kuhusu wageni yalilinganaje na aina ya ibada iliyoonyeshwa katika Sheria ya Kimusa? Sheria ilitokeza hali ya kujitenga na mataifa, lakini jambo hilo lilikusudiwa kuwalinda Waisraeli, hasa ibada yao safi. (Yoshua 23:6-8) Hata hivyo, Sheria ilitaka kwamba wageni watendewe kwa haki na kwa usawa na kwamba wapokewe kwa ukaribishaji-wageni—maadamu tu hawakukosa kutii sheria za Israeli kwa kutojali. (Mambo ya Walawi 24:22) Kwa kuacha maana ifaayo iliyothibitishwa wazi katika Sheria kuhusiana na wageni, viongozi wa kidini Wayahudi wa wakati wa Yesu walitokeza aina ya ibada iliyofanya wageni wachukiwe, nao wakaichukia pia. Mwishowe, taifa la Wayahudi la karne ya kwanza lilipoteza upendeleo wa Yehova.—Mathayo 23:38.

      11 Je, kuna somo tunalopata kutokana na hayo? Ndiyo, kunalo. Mtazamo wa kujiona kuwa waadilifu na bora kushinda wengine, ambao huwadharau wale wenye itikadi za kidini tofauti na zetu, hauwakilishi ibada safi ya Yehova, wala haumpendezi. Fikiria Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza. Hawakuwachukia wasio Wakristo, wala hawakuasi dhidi ya Roma. Hata hivyo, walikuwa “vitu vya kuchukiwa.” Kwa nini? Na nani?

      Wakristo wa Mapema Walichukiwa na Nani?

      12. Ni wazi kadiri gani kutokana na Maandiko kwamba Yesu hutaka wafuasi wake wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu wasio Wakristo?

      12 Ni wazi kutokana na mafundisho ya Yesu kwamba alikusudia wanafunzi wake wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu wasio Wakristo. Kwa upande mmoja, alisema kwamba wafuasi wake wangejitenga na ulimwengu—yaani, wangeepuka kabisa mitazamo na mwenendo uliohitilafiana na njia za uadilifu za Yehova. Wangeendelea kutokuwamo katika mambo ya vita na siasa. (Yohana 17:14, 16) Kwa upande mwingine, badala ya kutetea kudharauliwa kwa wasio Wayahudi, Yesu aliwaambia wafuasi wake ‘wawapende maadui wao.’ (Mathayo 5:44) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu cha kunywa.” (Waroma 12:20) Pia aliwaambia Wakristo ‘wafanye lililo jema kuelekea wote.’—Wagalatia 6:10.

      13. Kwa nini viongozi wa kidini Wayahudi waliwapinga sana wanafunzi wa Kristo?

      13 Hata hivyo, punde si punde wanafunzi wa Kristo walijipata wakiwa “vitu vya kuchukiwa” kutokana na vyanzo vitatu. Cha kwanza kilikuwa viongozi wa kidini Wayahudi. Si ajabu kwamba Wakristo walivuta uangalifu wao upesi! Wakristo walikuwa na kanuni za juu za maadili na uaminifu-maadili, nao walitoa ujumbe wenye kuchochea tumaini kwa bidii nyingi sana. Maelfu ya watu waliacha Dini ya Kiyahudi na kukubali Ukristo. (Matendo 2:41; 4:4; 6:7) Kwa viongozi wa kidini Wayahudi, wanafunzi wa Yesu Wayahudi walikuwa tu waasi-imani! (Linganisha Matendo 13:45.) Viongozi hao wenye hasira walihisi kwamba Ukristo ulibatilisha mapokeo yao. Kwani hata uliyakataa maoni yao kuhusu wasio Wayahudi! Kuanzia mwaka wa 36 W.K. na kuendelea, wasio Wayahudi wangeweza kuwa Wakristo, wakishiriki imani ileile na kufurahia mapendeleo yaleyale waliyofurahia Wayahudi Wakristo.—Matendo 10:34, 35.

      14, 15. (a) Kwa nini Wakristo walichukiwa na waabudu wapagani? Toa kielelezo. (b) Wakristo wa mapema walikuja kuwa “vitu vya kuchukiwa” na kikundi gani cha tatu?

      14 Pili, Wakristo walichukiwa na waabudu wapagani. Kwa kielelezo, katika Efeso la kale, utengenezaji wa vihekalu vya fedha vya mungu-mke Artemisi ulikuwa biashara yenye faida. Lakini Paulo alipohubiri huko, Waefeso wengi waliitikia, wakiacha kuabudu Artemisi. Biashara yao ikiwa imetishwa, wafua-fedha walifanya ghasia. (Matendo 19:24-41) Jambo sawa na hilo lilitokea baada ya Ukristo kuenea hadi Bithinia (sasa kaskazini-magharibi mwa Uturuki). Muda mfupi baada ya kukamilishwa kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, gavana wa Bithinia, Plini Mchanga, aliripoti kwamba mahekalu ya wapagani yaliachwa na kwamba uuzaji wa chakula cha wanyama wa kutolewa dhabihu ulishuka sana. Wakristo walilaumiwa—na kunyanyaswa—kwa kuwa ibada yao haikuruhusu kuwepo kwa dhabihu za wanyama na sanamu. (Waebrania 10:1-9; 1 Yohana 5:21) Kwa wazi, kuenea kwa Ukristo kuliathiri mambo fulani yenye kunufaisha yaliyohusiana na ibada ya kipagani, nao waliopoteza biashara na fedha waliuchukia.

      15 Tatu, Wakristo walipata kuwa “vitu vya kuchukiwa” na Waroma wenye kutukuza taifa. Mwanzoni, Waroma waliwajua Wakristo kuwa kikundi kidogo cha kidini ambacho yaelekea kilikuwa kishupavu. Hata hivyo, baada ya muda, kudai tu kuwa Mkristo kukawa kosa lililostahili adhabu ya kifo. Kwa nini raia wenye kufuata haki, wanaoishi maisha ya Kikristo wangeonekana kuwa watu wastahilio mnyanyaso na kifo?

      Kwa Nini Wakristo wa Mapema Walichukiwa Katika Ulimwengu wa Roma?

      16. Wakristo walijitenga na ulimwengu katika njia zipi, na kwa nini hilo lilifanya wachukiwe katika ulimwengu wa Waroma?

      16 Kimsingi, Wakristo walichukiwa katika ulimwengu wa Roma kwa kutenda kulingana na itikadi zao za kidini. Kwa kielelezo, walijitenga na ulimwengu. (Yohana 15:19) Kwa hiyo, hawakuwa na nyadhifa za kisiasa, nao walikataa utumishi wa kijeshi. Tokeo likawa kwamba, “waliwakilishwa wakiwa wafu kwa habari ya ulimwengu, wasiofaa kwa jambo lolote maishani,” asema mwanahistoria Augustus Neander. Kutokuwa sehemu ya ulimwengu pia kulimaanisha kuepuka njia mbovu za ulimwengu mfisadi wa Waroma. “Zile jumuiya ndogo-ndogo za Wakristo zilikuwa zikiusumbua ulimwengu wa kipagani wenye kutamani sana anasa kwa uchaji na adabu zao,” aeleza mwanahistoria Will Durant. (1 Petro 4:3, 4) Huenda Waroma wakawa walijaribu kuwanyamazisha Wakristo hao wenye kusumbua kwa kuwanyanyasa na kuwaua.

      17. Ni nini kionyeshacho kwamba kazi ya kuhubiri ya Wakristo wa karne ya kwanza ilikuwa na matokeo?

      17 Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu kwa bidii isiyoridhiana. (Mathayo 24:14) Kufikia mwaka wa 60 W.K., Paulo angeweza kusema kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23) Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, wafuasi wa Yesu walikuwa wamefanya wanafunzi kotekote katika Milki ya Waroma—katika Asia, Ulaya, na Afrika! Hata washiriki fulani wa “nyumbani mwa Kaisari” wakawa Wakristo.a (Wafilipi 4:22) Kuhubiri huko kwa bidii kulichochea chuki. Neander asema: “Ukristo ulienea hatua kwa hatua miongoni mwa watu wa kila tabaka, ukatisha kuangamiza dini ya taifa.”

      18. Kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine kuliwafanyaje Wakristo wasipatane na serikali ya Waroma?

      18 Wafuasi wa Yesu walimpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine. (Mathayo 4:8-10) Yawezekana sehemu hii ya ibada yao, zaidi ya nyingine yoyote, ndiyo iliyowafanya wasipatane na Roma. Waroma walivumilia dini nyinginezo, maadamu tu wafuasi wake walishiriki pia katika kuabudu maliki. Wakristo wa mapema hawangeweza kabisa kushiriki katika ibada kama hiyo. Walijiona kuwa wenye kuwajibika kwa mamlaka iliyo juu zaidi kuliko hiyo ya Serikali ya Waroma, yaani, Yehova Mungu. (Matendo 5:29) Tokeo likawa kwamba, Mkristo alionwa kuwa adui wa Serikali, hata awe alikuwa raia mwema kadiri gani kuhusiana na mambo yale mengine yote.

      19, 20. (a) Ni nani hasa waliohusika na uchongezi mbaya ulioenezwa kuwahusu Wakristo waaminifu? (b) Ni mashtaka gani yasiyo ya kweli yaliyozushwa dhidi ya Wakristo?

      19 Bado kuna sababu nyingine iliyofanya Wakristo waaminifu wawe “vitu vya kuchukiwa” katika ulimwengu wa Waroma: Uchongezi mbaya kuwahusu uliaminika kwa urahisi, nao viongozi Wayahudi walihusika kwa kiwango kikubwa katika kuueneza. (Matendo 17:5-8) Paulo alipokuwa Roma akingojea kufanyiwa kesi na Maliki Nero wapata mwaka wa 60 au 61 W.K., viongozi Wayahudi walisema hivi kuwahusu Wakristo: “Kweli kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Bila shaka, Nero alisikia hadithi za uchongezi kuwahusu. Katika mwaka wa 64 W.K., alipolaumiwa kwa moto ulioteketeza Roma, yaripotiwa kwamba Nero aliwasingizia Wakristo waliokuwa tayari wamesemwa vibaya. Yaonekana jambo hilo lilitokeza mnyanyaso mkubwa wenye jeuri uliokusudiwa kuwaangamiza Wakristo kabisa.

      20 Mara nyingi mashtaka hayo yasiyo ya kweli dhidi ya Wakristo yalikuwa mchanganyiko wa uwongo na upotoaji wa itikadi zao. Wao waliitwa waatheisti kwa sababu waliabudu Mungu mmoja na hawakumwabudu maliki. Kwa kuwa washiriki fulani wa familia wasio Wakristo walipinga jamaa zao Wakristo, Wakristo walishtakiwa kwa kuvunja familia. (Mathayo 10:21) Waliitwa wala-watu, shtaka ambalo vyanzo fulani vyasema, lilitegemea kupotoshwa kwa maneno ya Yesu aliyotamka kwenye Mlo wa Jioni wa Bwana.—Mathayo 26:26-28.

      21. Wakristo walikuwa “vitu vya kuchukiwa” kwa sababu gani mbili?

      21 Kwa hiyo, Wakristo waaminifu walikuwa “vitu vya kuchukiwa” na Waroma kwa sababu mbili za msingi: (1) itikadi zao zilizotegemea Biblia, na (2) mashtaka yasiyo ya kweli dhidi yao. Hata sababu iwe nini, wapinzani walikuwa na lengo moja—kukandamiza Ukristo. Bila shaka, wachochezi halisi wa mnyanyaso huo wa Wakristo walikuwa wapinzani wenye uwezo upitao wa kibinadamu, majeshi yasiyoonekana ya roho waovu.—Waefeso 6:12.

      22. (a) Ni kielelezo gani kionyeshacho kwamba Mashahidi wa Yehova hujitahidi sana ‘kufanya lililo jema kuelekea wote’? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 11.) (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      22 Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wa nyakati za kisasa wamekuwa “vitu vya kuchukiwa” katika nchi mbalimbali. Hata hivyo, wao hawawachukii wasio Mashahidi; wala hawajapata kuanzisha maasi dhidi ya serikali. Kinyume cha hilo, wanajulikana ulimwenguni pote kwa kuonyesha upendo wa kweli ambao huvuka mipaka yote ya kijamii, kitaifa, na kikabila. Basi, ni kwa nini wamenyanyaswa? Nao huitikiaje upinzani? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

  • Kutetea Imani Yetu
    Mnara wa Mlinzi—1998 | Desemba 1
    • Kutetea Imani Yetu

      “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi.”—1 PETRO 3:15.

      1, 2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawashangazwi na upinzani, lakini wao hutamani nini?

      KATIKA nchi zilizo nyingi, Mashahidi wa Yehova hujulikana na wengi kuwa watu wenye kufuata haki na walio safi kiadili. Wengi huwaona kuwa majirani wema wasiosababisha matatizo yoyote. Lakini, kinyume cha hilo, Wakristo hawa wapenda-amani wamenyanyaswa isivyo haki—nyakati za vita na za amani. Wao hawashangazwi na upinzani huo. Kwa kweli, wao huutarajia. Wanajua kwamba Wakristo waaminifu katika karne ya kwanza W.K. walikuwa “vitu vya kuchukiwa,” kwa hiyo, mbona wale wanaojitahidi kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo leo watarajie kutendwa tofauti? (Mathayo 10:22) Isitoshe, Biblia husema: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.”—2 Timotheo 3:12.

      2 Mashahidi wa Yehova hawatafuti kunyanyaswa, wala hawafurahii shida—faini, vifungo, au kutendwa kikatili—ziwezazo kuletwa na mnyanyaso. Wao hutamani “kuishi maisha yaliyo shwari na matulivu” ili waweze kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu bila kizuizi. (1 Timotheo 2:1, 2) Wao huthamini uhuru wa kidini wa kuendelea na ibada yao walio nao katika nchi nyingi, nao hufanya kwa kudhamiria yale wawezayo “kufanya amani na watu wote,” kutia ndani watawala wa serikali za kibinadamu. (Waroma 12:18; 13:1-7) Kwa nini, basi, wao ni “vitu vya kuchukiwa”?

      3. Sababu moja inayofanya Mashahidi wa Yehova wachukiwe isivyo haki ni gani?

      3 Kusema kweli, Mashahidi wa Yehova wamechukiwa isivyo haki kwa sababu zilezile zilizofanya Wakristo wa mapema wanyanyaswe. Kwanza, Mashahidi wa Yehova hutenda kulingana na itikadi zao za kidini katika njia ambazo huwafanya wasipendwe na wengine. Kwa kielelezo, wao huhubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme wa Mungu, lakini mara nyingi watu hukosa kuelewa bidii yao, wakiona kuhubiri kwao kuwa “kugeuza imani kwa jeuri.” (Linganisha Matendo 4:19, 20.) Wao pia hawajiingizi katika siasa na vita vya mataifa, na nyakati nyingine jambo hilo limechukuliwa kimakosa kumaanisha kwamba, Mashahidi si raia waaminifu-washikamanifu.—Mika 4:3, 4.

      4, 5. (a) Mashahidi wa Yehova wamekuwaje shabaha ya mashtaka yasiyo ya kweli? (b) Ni nani ambao mara nyingi wamekuwa wachochezi wakuu wa kunyanyaswa kwa watumishi wa Yehova?

      4 Pili, Mashahidi wa Yehova wamekuwa shabaha za mashtaka yasiyo ya kweli—uwongo ulio wazi na kuwasilishwa kulikopotoka kwa itikadi zao. Katika nchi fulani, hilo limefanya washambuliwe isivyo haki. Isitoshe, kwa sababu wao hutafuta matibabu yasiyohusisha damu ambayo hupatana na tamaa yao ya kutii amri ya Biblia ya ‘kujiepusha na damu,’ wameitwa isivyofaa “waua-watoto kimakusudi” na pia “madhehebu ya kujiua.” (Matendo 15:29) Lakini ukweli ni kwamba Mashahidi wa Yehova huthamini sana uhai, nao hutafuta kupata utunzaji wa kitiba bora zaidi ambao waweza kupatikana kwa ajili yao wenyewe na watoto wao. Shtaka la kwamba watoto wengi wa Mashahidi wa Yehova hufa kila mwaka kwa sababu ya kukataa kutiwa damu mishipani halina msingi wowote. Kwa kuongezea, kwa kuwa kweli ya Biblia haiwaathiri washiriki wa familia kwa kiwango kilekile, Mashahidi hulaumiwa pia kwa kuvunja familia. Hata hivyo, wale wanaowafahamu Mashahidi wa Yehova wanajua kwamba wao hustahi sana maisha ya familia na hujaribu kufuata amri za Biblia kwamba mume na mke wapendane na kustahiana na kwamba watoto wawatii wazazi wao, wawe waamini au la.—Waefeso 5:21–6:3.

      5 Katika visa vingi, wachochezi wakuu wa mnyanyaso wa watumishi wa Yehova wamethibitika kuwa wapinzani wa kidini ambao wametumia uwezo walio nao na wenye mamlaka na vyombo vya habari kujaribu kukandamiza utendaji wa Mashahidi. Yatupasa sisi Mashahidi wa Yehova tuitikieje upinzani huo—uwe watokana na itikadi zetu na mazoea yetu au watokana na mashtaka yasiyo ya kweli?

      “Hali Yenu ya Kukubali Sababu na Ijulikane kwa Watu Wote”

      6. Kwa nini ni jambo la maana kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu wale walio nje ya kutaniko la Kikristo?

      6 Kwanza kabisa, twahitaji kuwaona ifaavyo walio na itikadi za kidini zilizo tofauti na zetu, kuwaona jinsi Yehova awaonavyo. La sivyo, twaweza kuchochea isivyo lazima uhasama au shutuma kutoka kwa wengine. “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote,” akaandika mtume Paulo. (Wafilipi 4:5) Kwa sababu hiyo, Biblia hutuhimiza kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu wale walio nje ya kutaniko la Kikristo.

      7. Ni nini kihusikacho katika kufuliza kujitunza wenyewe “bila doa kutokana na ulimwengu”?

      7 Kwa upande mmoja, Maandiko hutuonya waziwazi kabisa ‘tufulize kujitunza wenyewe bila doa kutokana na ulimwengu.’ (Yakobo 1:27; 4:4) Hapa, neno “ulimwengu” kama ilivyo kwenye sehemu nyingi katika Biblia, hurejezea jamii ya binadamu wasio Wakristo wa kweli. Sisi huishi katikati ya jamii hiyo ya watu; sisi hukutana nao kazini, shuleni, ujiranini, na kwingineko. (Yohana 17:11, 15; 1 Wakorintho 5:9, 10) Hata hivyo, sisi hufuliza kujitunza wenyewe bila doa kutokana na ulimwengu kwa kuepuka kabisa mitazamo, usemi, na mwenendo ambao huhitilafiana na njia za Mungu za uadilifu. Pia ni muhimu tutambue hatari ya kushirikiana kwa ukaribu na ulimwengu huu, hasa kushirikiana na wale ambao hupuuza kabisa viwango vya Yehova.—Mithali 13:20.

      8. Kwa nini shauri la kubaki bila doa kutokana na ulimwengu halitupi sababu yoyote ya kuwadharau wengine?

      8 Hata hivyo, shauri la kubaki bila doa kutokana na ulimwengu halitupi sababu yoyote ya kuwadharau kabisa wale wasio Mashahidi wa Yehova. (Mithali 8:13) Kumbuka kielelezo cha viongozi wa kidini wa Kiyahudi, waliozungumziwa katika makala iliyotangulia. Aina ya dini waliyositawisha haikupata upendeleo wa Yehova; wala haikuchangia kuwepo kwa uhusiano mzuri pamoja na wasio Wayahudi. (Mathayo 21:43, 45) Kwa sababu ya kujiona, wanaume hao washupavu waliwadharau wale wasio Wayahudi. Sisi hatuwi na maoni finyu kama hayo, tukiwatendea wasio Mashahidi kwa kuwadharau. Kama mtume Paulo, tamaa yetu ni kwamba wale wote wasikiao ujumbe wa kweli wa Biblia wapate upendeleo wa Mungu.—Matendo 26:29; 1 Timotheo 2:3, 4.

      9. Maoni ya Kimaandiko yaliyosawazika yapaswa kuathirije mazungumzo yetu kuhusu wale wenye itikadi tofauti na zetu?

      9 Maoni ya Kimaandiko yaliyosawazika yapaswa kuathiri jinsi tuzungumzavyo kuhusu wasio Mashahidi. Paulo alimwagiza Tito awakumbushe Wakristo kisiwani Krete “wasiseme kwa ubaya juu ya yeyote, wasiwe wataka-vita, wawe wenye kukubali sababu, wakionyesha wazi upole wote kuelekea watu wote.” (Tito 3:2) Ona kwamba Wakristo hawakupaswa kusema kwa ubaya juu ya “yeyote”—hata juu ya Wakrete wasio Wakristo, ambao baadhi yao walijulikana kwa kusema uwongo, ulafi, na uzembe. (Tito 1:12) Kwa hiyo, halingekuwa jambo lenye kupatana na Maandiko kwetu kutumia maneno yenye kudharau tunaporejezea watu wenye itikadi tofauti na zetu. Mtazamo wa kujiona kuwa bora kushinda wengine hautawavuta wengine kwenye ibada ya Yehova. Badala yake, tunapowaona na kuwatendea wengine kupatana na kanuni zifaazo za Neno la Yehova, sisi ‘huremba fundisho’ la Mungu.—Tito 2:10.

      Wakati wa Kunyamaza na Wakati wa Kusema

      10, 11. Yesu alionyeshaje kwamba alijua (a) “wakati wa kunyamaza”? (b) “wakati wa kusema”?

      10 Kuna “wakati wa kunyamaza na wakati wa kusema,” lasema andiko la Mhubiri 3:7. (NW) Basi, hapa ndipo pana tatizo: kuamua wakati wa kuwapuuza wapinzani na wakati wa kusema ili kutetea imani yetu. Tunaweza kujifunza mengi kutokana na kielelezo cha mmoja ambaye sikuzote alikuwa mkamilifu katika busara—Yesu. (1 Petro 2:21) Alijua “wakati wa kunyamaza.” Kwa mfano, wakati makuhani wakuu na wanaume wazee walipomshtaki isivyo haki mbele ya Pilato, Yesu “hakutoa jibu.” (Mathayo 27:11-14) Hakutaka kusema jambo lolote ambalo lingeweza kuzuia kutekelezwa kwa mapenzi ya Mungu juu yake. Badala yake, alichagua kuacha matendo yake yamtetee. Alijua kwamba hata ile kweli haingebadili akili na mioyo yao yenye kiburi. Kwa hiyo, alipuuza shtaka lao, akikataa kimakusudi kusema.—Isaya 53:7.

      11 Hata hivyo, Yesu pia alijua ulipofika “wakati wa kusema.” Mara kwa mara, alipambana na wachambuzi wake kwa kusema waziwazi na hadharani, akikanusha mashtaka yao yasiyo ya kweli. Kwa kielelezo, waandishi na Mafarisayo walipojaribu kumwaibisha mbele ya umati, wakimshtaki kwa kufukuza roho waovu kupitia Beelzebubi, Yesu aliamua kutoachilia mashtaka hayo. Kwa kutumia mantiki yenye kuwavuruga na pia kielezi chenye nguvu, aliubatilisha uwongo huo. (Marko 3:20-30; ona pia Mathayo 15:1-11; 22:17-21; Yohana 18:37.) Vivyo hivyo, Yesu alipokokotwa mbele ya Sanhedrini baada ya kusalitiwa na kukamatwa, Kayafa, Kuhani wa Cheo cha Juu alidai kwa hila hivi: “Kwa Mungu aliye hai nakuweka chini ya kiapo utuambie kama wewe ndiwe Kristo Mwana wa Mungu!” Huu pia ulikuwa “wakati wa kusema,” kwa kuwa kunyamaza kungefasiriwa kuwa kukana kwamba alikuwa Kristo. Kwa hiyo Yesu alijibu: “Mimi ndiye.”—Mathayo 26:63, 64; Marko 14:61, 62.

      12. Ni hali zipi zilizowasukuma Paulo na Barnaba waseme kwa ujasiri huko Ikoniamu?

      12 Fikiria pia kielelezo cha Paulo na Barnaba. Andiko la Matendo 14:1, 2 lasema: “Katika Ikoniamu wakaingia pamoja katika sinagogi la Wayahudi na kusema kwa namna ambayo umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki ukapata kuwa waamini. Lakini Wayahudi ambao hawakuamini wakazichochea na kuzivuta vibaya nafsi za watu wa mataifa dhidi ya akina ndugu.” Tafsiri ya Biblia Habari Njema yasema: “Lakini Wayahudi wengine waliokataa kuwa waumini walichochea na kutia chuki katika mioyo ya watu wa mataifa mengine ili wawapinge hao ndugu.” Kwa kutoridhika na kukataa kwao wenyewe ujumbe huo, Wayahudi wapinzani walianza kampeni ya mashtaka yasiyoweza kuthibitishwa, wakijaribu kuwafanya wasio Wayahudi wawabague Wakristo.a Lazima chuki yao kwa Ukristo iwe ilikuwa yenye kina kirefu kama nini! (Linganisha Matendo 10:28.) Paulo na Barnaba walihisi huo ulikuwa “wakati wa kusema,” ili wanafunzi wapya wasije wakavunjwa moyo na kuaibishwa hadharani. “Kwa hiyo wao [Paulo na Barnaba] wakatumia muda mrefu wakisema kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova,” aliyeonyesha kibali chake kwa kuwapa nguvu za kufanya ishara za kimuujiza. Hilo lilifanya baadhi yao wawe “upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume.”—Matendo 14:3, 4.

      13. Katika kushughulika na shutumu, kwa kawaida “wakati wa kunyamaza” ni lini?

      13 Basi, twapaswa kuitikiaje tunaposhutumiwa? Yote hayo hutegemea hali. Hali nyingine hututaka tutumie kanuni ya kwamba kuna “wakati wa kunyamaza.” Jambo hilo huwa hivyo hasa wakati ambapo wapinzani wenye kuazimia hujaribu kutuingiza katika mabishano yasiyo na maana. Hatupaswi kusahau kwamba watu wengine hawataki kuijua kweli hata kidogo. (2 Wathesalonike 2:9-12) Ni kazi bure kujaribu kusababu na wale ambao kwa kiburi wameamua mioyoni mwao kutoamini. Isitoshe, kama tungejishughulisha na kujadiliana na kila anayetushambulia kwa mashtaka yasiyo ya kweli, tungeweza kukengeushwa tutoke katika utendaji ulio wa maana zaidi na wenye kuthawabisha zaidi—ule wa kuwasaidia wenye mioyo ya haki ambao kwa kweli wanataka kujifunza kweli ya Biblia. Kwa hiyo, tunapokabili wapinzani wanaoazimia kueneza uwongo kutuhusu, shauri lililopuliziwa ni: “Mwaepuke.”—Waroma 16:17, 18; Mathayo 7:6.

      14. Twaweza kutetea imani yetu mbele ya wengine katika njia zipi?

      14 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba hatutetei imani yetu. Kwa kuwa pia kuna “wakati wa kusema.” Kwa kufaa, sisi huhangaikia watu wenye mioyo myeupe ambao wamepata kusikia uchambuzi wenye kutukashifu. Sisi tuko tayari kuwaeleza wengine waziwazi juu ya usadikisho wetu wa moyoni; kwa kweli sisi hufurahia fursa hiyo. Petro aliandika: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwenu sababu ya tumaini lililo katika nyinyi, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15) Watu wenye kupendezwa kikweli waulizapo kuthibitishiwa itikadi tunazothamini sana, waulizapo kuhusu mashtaka yasiyo ya kweli yenye kuzushwa na wapinzani, ni wajibu wetu kutetea imani yetu, tukitoa majibu kamili ya Biblia. Kwa kuongezea, mwenendo wetu mwema waweza kutoa ushahidi mkubwa. Watazamaji walio tayari kusikiliza waonapo kwamba sisi hujaribu kikweli kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu, wanaweza kuona kwa urahisi kwamba mashtaka yanayofanywa dhidi yetu si ya kweli.—1 Petro 2:12-15.

      Namna Gani Utangazaji Wenye Uchongezi?

      15. Kuna kielelezo gani kimoja cha jinsi Mashahidi wa Yehova wameshambuliwa kwa habari zilizopotoka katika vyombo vya habari?

      15 Mara kwa mara, Mashahidi wa Yehova wameshambuliwa kwa habari zilizopotoka katika vyombo vya habari. Kwa kielelezo, Agosti 1, 1997, gazeti la habari la Urusi lilichapisha makala yenye uchongezi iliyodai kwamba, kati ya mambo mengine, Mashahidi kwa hakika huwataka washiriki wao ‘wakatae wake zao, waume wao, na wazazi wao iwapo hawaelewi na iwapo imani yao ni tofauti na yao.’ Mtu yeyote anayewafahamu Mashahidi wa Yehova kikweli anajua kwamba shtaka hilo si la kweli. Biblia huonyesha kwamba Wakristo wapaswa kuwatendea washiriki wa familia wasioamini kwa upendo na staha, nao Mashahidi hujitahidi sana kufuata mwelekezo huo. (1 Wakorintho 7:12-16; 1 Petro 3:1-4) Hata hivyo, makala hiyo ilichapwa, na hivyo wasomaji wengi wakapotoshwa. Twaweza kuteteaje imani yetu tunaposhtakiwa isivyo kweli?

      16, 17, na sanduku kwenye ukurusa wa 16. (a) Mnara wa Mlinzi lilisema nini wakati mmoja juu ya jinsi ya kuitikia habari zisizo za kweli katika vyombo vya habari? (b) Ni chini ya hali zipi ambapo Mashahidi wa Yehova waweza kuchukua hatua dhidi ya ripoti zisizofaa katika vyombo vya habari?

      16 Hapa tena, pana “wakati wa kunyamaza na wakati wa kusema.” Wakati mmoja, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilieleza jambo hilo hivi: “Tuwe tunapuuza habari za uwongo katika vyombo vya habari au tuwe tunatetea kweli kwa njia ifaayo yategemea hali, mchocheaji wa uchambuzi, na lengo lake.” Katika visa vingine huenda ikawa afadhali kupuuza ripoti zisizofaa, hivyo kutokueneza zaidi uwongo huo.

      17 Katika visa vingine huenda ukawa “wakati wa kusema.” Huenda mwandishi wa habari au ripota mwenye kutumainika akawa alipashwa habari zisizo za kweli kuhusu Mashahidi wa Yehova na huenda akafurahia habari za kweli kutuhusu. (Ona sanduku “Kusahihisha Habari Iliyowasilishwa Isivyo Kweli.”) Iwapo ripoti zisizofaa katika vyombo vya habari zachochea ubaguzi wenye kuzuia kazi yetu ya kuhubiri, huenda wawakilishi wa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society wakachukua hatua ya kwanza kutetea kweli kwa njia zifaazo.b Kwa kielelezo, huenda wazee wanaostahili wakapewa mgawo wa kuwasilisha mambo ya hakika, kama vile katika programu za televisheni, ambapo kutojitokeza huenda kukadokeza kwamba Mashahidi wa Yehova hawana jibu lolote. Mashahidi mmoja-mmoja hutenda kwa hekima kulingana na mwelekezo wa Watch Tower Society na wawakilishi wake katika mambo hayo.—Waebrania 13:17.

      Kutetea Kisheria Habari Njema

      18. (a) Kwa nini hatuhitaji ruhusa ya serikali za kibinadamu ili kuhubiri? (b) Sisi huchukua hatua gani tunaponyimwa ruhusa ya kuhubiri?

      18 Mamlaka yetu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu hutoka mbinguni. Yesu aliyetupa utume wa kufanya kazi hii amepewa “mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18-20; Wafilipi 2:9-11) Kwa sababu hiyo, hatuhitaji ruhusa ya serikali za kibinadamu ili kuhubiri. Hata hivyo, sisi hutambua kwamba kuwa na uhuru wa kidini huchangia kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme. Katika nchi ambako tuna uhuru wa kuendelea na ibada yetu, sisi tutatumia utaratibu wa kisheria ili kuulinda. Mahali ambapo tumenyimwa uhuru huo, tutajitahidi kuupata kupatana na utaratibu wa kisheria. Hatukusudii kuongoa jamii, bali “kutetea na kuthibitisha kisheria habari njema.”c—Wafilipi 1:7.

      19. (a) Huenda matokeo ya ‘kumlipa Mungu vitu vya Mungu’ yakawa nini? (b) Tumeazimia kufanya nini?

      19 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, twamtambua Yehova kuwa ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu. Sheria yake ni kuu kuliko zote. Sisi hutii serikali za kibinadamu kwa kudhamiria, hivyo ‘tukimlipa Kaisari vitu vya Kaisari.’ Lakini hatutaruhusu kitu chochote kituzuie tusitimize wajibu ulio muhimu zaidi—‘kumlipa Mungu vitu vya Mungu.’ (Mathayo 22:21) Twaelewa kikamili kwamba kufanya hivyo kutatufanya tuwe “vitu vya kuchukiwa” na mataifa, lakini twakubali jambo hilo kuwa sehemu ya gharama ya kuwa wanafunzi. Rekodi ya kisheria ya Mashahidi wa Yehova katika karne ya 20, ni ushuhuda wa azimio letu la kutetea imani yetu. Kwa msaada na utegemezo wa Yehova, tutaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema.”—Matendo 5:42.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kichapo Matthew Henry’s Commentary on the Whole Bible chaeleza kwamba wapinzani Wayahudi “walijishughulisha na kuwaendea kimakusudi [wasio Wayahudi] waliowafahamu, na kuwaambia yale yote akili zao au nia zao mbaya zingeweza kutunga, ili kuwafanya wawe na maoni yenye kudharau na yasiyofaa kuhusu Ukristo.”

      b Baada ya makala hiyo yenye uchongezi kuchapishwa katika gazeti la habari la Urusi (lililotajwa katika fungu la 15), Mashahidi wa Yehova walikata rufani kwa baraza la sheria liitwalo Russian Federation Presidential Judicial Chamber for Media Disputes wakiomba mashtaka hayo yasiyo ya kweli ambayo yaliandikwa katika makala hiyo yachunguzwe tena. Hivi majuzi mahakama ilitoa uamuzi ulioliadhibu vikali gazeti hilo la habari kwa kuchapa makala hiyo yenye kukashifu.—Ona Amkeni!, Novemba 22, 1998, ukurasa wa 26-27.

      c Ona makala “Kulinda Kisheria Habari Njema,” kwenye ukurasa wa 19-22.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki