Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hofu Yehova na Kushika Amri Zake
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 1
    • Jiepushe na Maovu

      4. (a) Wakristo wapaswa kusitawisha chuki ya aina gani? (b) Yehova huonaje mwenendo wenye dhambi? (Ona kielezi-chini.)

      4 Biblia hueleza kwamba “kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ni kuchukia uovu.” (Mithali 8:13) Kamusi moja ya Biblia yafafanua chuki hiyo kuwa ‘kukirihi watu na vitu visivyopendwa, vinavyokubalika, na ambavyo mtu hangependa kujihusisha navyo kamwe.’ Kwa hiyo, hofu ya kimungu inatia ndani kuchukia kabisa kila kitu ambacho ni kiovu machoni pa Yehova.b (Zaburi 97:10) Hofu hiyo hutuchochea tuache lililo ovu, kama vile sisi hujikuta tu tumeondoka kutoka kwenye ukingo wa jabali tunapohisi hatari. “Kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu,” yasema Biblia.—Mithali 16:6.

      5. (a) Tunawezaje kuimarisha hofu yetu ya kimungu na kuchukia lililo ovu? (b) Historia ya taifa la Israeli inatufundisha nini kuhusiana na habari hii?

      5 Tunaweza kuimarisha hofu hiyo inayofaa na kuchukia lililo ovu kwa kuchunguza matokeo mabaya ambayo bila shaka huletwa na dhambi. Biblia hutuhakikishia kwamba tutavuna kile tunachopanda—iwe tunapanda kulingana na mwili au kulingana na roho. (Wagalatia 6:7, 8) Kwa sababu hiyo Yehova anaeleza kinaganaga matokeo ya kupuuza amri zake na kuacha ibada ya kweli. Pasipo kulindwa na Mungu, taifa dogo na dhaifu la Israeli halingeweza kujilinda dhidi ya majirani wake wakatili na wenye nguvu. (Kumbukumbu la Torati 28:15, 45-48) Matokeo mabaya yaliyopata taifa la Israeli kwa sababu ya kutotii yaliandikwa kwa kirefu katika Biblia “kuwa onyo” ili tujifunze somo hilo na kusitawisha hofu ya kimungu.—1 Wakorintho 10:11.

      6. Twaweza kufikiria mifano gani inayopatikana katika Maandiko tunapojifunza kuhusu hofu ya kimungu? (Ona kielezi-chini.)

      6 Mbali na mambo yaliyolipata taifa la Israeli kwa ujumla, Biblia husimulia mambo yaliyowapata watu fulani waliokuwa na wivu, pupa, kiburi au waliojihusisha katika mwenendo usiofaa.c Baadhi ya watu hao walimtumikia Yehova kwa miaka mingi, lakini wakashindwa kumhofu Mungu ilipohitajika pindi fulani maishani mwao, walipatwa na matokeo mabaya. Kutafakari mifano hiyo inayopatikana katika Maandiko kwaweza kuimarisha azimio letu la kutofanya makosa kama hayo. Lingekuwa jambo lenye kusikitisha kama nini iwapo tungengoja hadi tupatwe na msiba ndipo tuzingatie shauri la Mungu! Kinyume na vile watu wengi wanavyoamini, si lazima upatwe na msiba—hasa kwa kutimiza tamaa za kibinafsi—ndio ujue ubaya wake.—Zaburi 19:7.

      7. Yehova hualika nani katika hema yake ya mfano?

      7 Sababu nyingine kubwa ya kusitawisha hofu ya kimungu ni ile tamaa ya kulinda uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunahofu kutompendeza Yehova kwa sababu tunathamini urafiki wetu pamoja naye. Ni nani anayeweza kuwa rafiki ya Mungu, na kualikwa katika hema yake ya mfano? Ni yule tu “aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki.” (Zaburi 15:1, 2) Ikiwa tunathamini uhusiano huo pamoja na Muumba wetu, tutakuwa waangalifu na kutembea kwa ukamilifu machoni pake.

      8. Ni katika njia gani baadhi ya Waisraeli katika siku za Malaki walikosa kutilia maanani urafiki wao pamoja na Mungu?

      8 Kwa kusikitisha, baadhi ya Waisraeli katika siku za Malaki hawakutilia maanani urafiki wao pamoja na Mungu. Badala ya kuhofu na kumheshimu Yehova, walitoa dhabihu za wanyama wagonjwa na vilema kwenye madhabahu yake. Pia mtazamo wao kuelekea ndoa ulionyesha kwamba hawakumhofu Mungu. Waliwataliki wake zao wa ujanani kwa sababu ndogondogo ili waoe wanawake wachanga. Malaki aliwaambia kwamba Yehova anachukia “talaka” na kwamba mtazamo wao wa hila uliwatenganisha na Mungu. Mungu angewezaje kukubali dhabihu zao huku madhabahu ikiwa imefunikwa kwa machozi ya mfano—machozi ya uchungu ya wake zao walioachwa? Kwa kutoheshimu kimakusudi viwango vyake, hali hiyo ilimfanya Yehova aulize hivi: “Hofu yangu i wapi?”—Malaki 1:6-8; 2:13-16.

      9, 10. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini kuwa rafiki za Yehova?

      9 Vivyo hivyo, leo Yehova anaona jinsi wenzi wa ndoa na watoto wengi wasio na hatia wanavyoteseka sana kwa sababu ya kuachwa na waume au baba ama na wake na akina mama wenye ubinafsi na wasio na maadili. Bila shaka anahuzunishwa na jambo hilo. Mtu ambaye ni rafiki ya Mungu ataona mambo jinsi Mungu anavyoyaona na atajitahidi kuimarisha ndoa yake, na kuepuka maoni ya watu wa ulimwengu ambao hawaheshimu kifungo cha ndoa, na pia ‘ataukimbia uasherati.’—1 Wakorintho 6:18.

      10 Katika ndoa na vilevile katika sehemu nyingine za maisha yetu, kuchukia lililo ovu machoni pa Yehova, na kuthamini sana kuwa rafiki zake, kutaleta kibali cha Yehova.

  • Hofu Yehova na Kushika Amri Zake
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 1
    • b Yehova mwenyewe huchukizwa kabisa na maovu. Kwa mfano, andiko la Waefeso 4:29 linafafanua lugha mbaya kuwa “usemi uliooza.” Neno la Kigiriki “-liooza” larejezea kihalisi tunda, samaki, au nyama iliyooza. Neno hilo linaonyesha kinaganaga jinsi tunavyopaswa kuhisi kuhusu lugha chafu au ya matusi. Vivyo hivyo, katika Maandiko mara nyingi sanamu zinaitwa “mavi.” (Kumbukumbu la Torati 29:17; Ezekieli 6:9, NW) Kama vile tunavyochukia kabisa mavi au kinyesi, ndivyo Mungu anavyochukia kabisa kila namna ya ibada ya sanamu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki