-
Mfalme Apata Thawabu kwa Sababu ya Imani YakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
28. Hezekia afanya kosa gani katika uamuzi wakati fulani baada ya kuponywa kwa njia ya mwujiza?
28 Ingawa Hezekia ni mwaminifu, yeye si mkamilifu. Afanya uamuzi wenye kosa zito muda fulani baada ya Yehova kumponya. Isaya aeleza: “Wakati huo Merodaki-baladani, mwana wa Baladani, mfalme wa Babeli, alipeleka barua na zawadi kwa Hezekia; kwa maana amepata habari kwamba amekuwa hawezi, na kwamba amepona. Hezekia akawafurahia, akawaonyesha nyumba yake yenye vitu vyake vya thamani, fedha na dhahabu, na manukato, na marhamu ya thamani, na nyumba yote yenye silaha zake za vita, na vitu vyote vilivyoonekana katika hazina zake; hapakuwa na kitu nyumbani mwake wala katika ufalme wake asichowaonyesha.”—Isaya 39:1, 2.b
29. (a) Huenda Hezekia ana nia gani awaonyeshapo wajumbe wa Wababiloni mali zake? (b) Matokeo ya uamuzi wenye kosa wa Hezekia yatakuwa nini?
29 Hata baada ya kushindwa kabisa na malaika wa Yehova, Ashuru yaendelea kuwa tisho kwa mataifa mengi, kutia ndani Babiloni. Labda Hezekia alitaka kumfurahisha mfalme wa Babiloni ili awe mshirika wake wakati ujao. Hata hivyo, Yehova hataki wakazi wa Yuda washirikiane na adui zao; anataka wamtumaini yeye! Kupitia nabii Isaya, Yehova amfunulia Hezekia mambo ya wakati ujao: “Siku zinakuja, ambazo vitu vyote vilivyomo nyumbani mwako, na hivyo vilivyowekwa akiba na baba zako hata leo, vitachukuliwa mpaka Babeli; hapana kitu cho chote kitakachosalia . . . Na baadhi ya wana wako utakaowazaa, watakaotoka kwako, watawachukulia mbali; nao watakuwa matowashi katika jumba la mfalme wa Babeli.” (Isaya 39:3-7) Naam, taifa lilelile ambalo Hezekia alijaribu kulifurahisha hatimaye litapora hazina za Yerusalemu na kuwatumikisha raia zake. Hatua ya Hezekia ya kuwaonyesha Wababiloni hazina zake yachochea tu tamaa yao yenye pupa.
30. Hezekia alionyeshaje mtazamo mzuri?
30 Labda likirejezea tukio ambalo Hezekia aliwaonyesha Wababiloni hazina zake, andiko la 2 Mambo ya Nyakati 32:26 lataarifu hivi: “Hezekia akajinyenyekeza kwa ajili ya huku kutukuka kwa moyo wake, yeye na wenyeji wa Yerusalemu, hata haikuwajia hasira ya BWANA siku za Hezekia.”
31. Hatimaye mambo yalimwendeaje Hezekia, na hilo latufundisha nini?
31 Licha ya kutokamilika kwake, Hezekia alikuwa mtu mwenye imani. Alijua kwamba Mungu wake, Yehova, ni mtu halisi aliye na hisia. Akiwa chini ya mkazo, Hezekia alisali kwa Yehova kwa bidii, na Yehova akamjibu. Yehova Mungu alimpa amani kwa siku zilizobaki za maisha yake, na Hezekia akawa mwenye shukrani kwa hayo. (Isaya 39:8)
-
-
Mfalme Apata Thawabu kwa Sababu ya Imani YakeUnabii wa Isaya I—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
b Baada ya kushindwa kwa Senakeribu, mataifa jirani yalimletea Hezekia zawadi za dhahabu, fedha, na vitu vingine vyenye thamani. Twasoma kwenye 2 Mambo ya Nyakati 32:22, 23, 27 kwamba “Hezekia akawa na mali nyingi mno na heshima” na kwamba “hata yeye akatukuka tangu wakati ule machoni pa mataifa yote.” Huenda zawadi hizo zilimwezesha kujaza tena nyumba yake ya hazina, ambayo alikuwa ameiacha tupu alipowalipa Waashuri ushuru.
-