-
Jivunieni Kuwa WakristoMnara wa Mlinzi—2005 | Februari 15
-
-
Jivunieni Kuwa Wakristo
“Yeye anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.”—1 WAKORINTHO 1:31.
1. Watu wana mtazamo gani kuelekea dini?
UBARIDI kuelekea dini. Hivyo ndivyo mchanganuzi mmoja wa masuala ya kidini alivyosema hivi karibuni kuhusu mtazamo wa watu kuelekea dini yao. Alisema: “Mwelekeo uliopo katika dini za kisasa si wa kidini hata kidogo, unaweza kufafanuliwa kwa kufaa kuwa ubaridi kuelekea dini.” Alifafanua mtazamo huo kuwa “kutotaka kujishughulisha sana na dini.” Alisema kwamba watu wengi “wanamwamini Mungu . . . ; ni kwamba tu hawajishughulishi sana naye.”
2. (a) Kwa nini haishangazi kwamba watu wamekuwa na ubaridi wa kiroho? (b) Ubaridi hutokeza hatari gani kwa Wakristo wa kweli?
2 Wanafunzi wa Biblia hawashangazwi na mtazamo huo wa ubaridi. (Luka 18:8) Na mtazamo huo unatazamiwa kuhusu dini kwa ujumla. Dini ya uwongo imewapotosha watu na kuwakatisha tamaa kwa muda mrefu. (Ufunuo 17:15, 16) Hata hivyo, ni hatari kwa Wakristo wa kweli kudhihirisha mtazamo ulioenea wa kuwa na moyo nusu-nusu na kutokuwa na bidii. Tutapatwa na madhara ikiwa tutakuwa na ubaridi kuelekea imani yetu na kupoteza hamu yetu ya kweli ya Biblia na bidii yetu ya kumtumikia Mungu. Yesu alitoa onyo hili kuhusu uvuguvugu wa namna hiyo kwa Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Laodikia: “Wewe si baridi wala si moto. Laiti ungalikuwa baridi au moto. . . . Wewe ni vuguvugu.”—Ufunuo 3:15-18.
Kutambua Sisi Ni Nani
3. Wakristo wanaweza kujivunia mambo gani yanayowatambulisha?
3 Ili kupambana na ubaridi wa kiroho, Wakristo wanapaswa kutambua waziwazi wao ni nani, nao wanapaswa kujivunia kwa kadiri fulani utambulisho wao wa pekee. Tukiwa watumishi wa Yehova na wanafunzi wa Kristo, tunaweza kupata ufafanuzi wa utambulisho wetu katika Biblia. Sisi ni “mashahidi” wa Yehova, “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” tunapowaeleza wengine kwa bidii “habari njema.” (Isaya 43:10; 1 Wakorintho 3:9; Mathayo 24:14) Sisi ni watu ‘wanaopendana.’ (Yohana 13:34) Wakristo wa kweli ni watu ambao “kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Sisi ni “mianga katika ulimwengu.” (Wafilipi 2:15) Sisi hujitahidi ‘kudumisha mwenendo wetu ukiwa mzuri katikati ya mataifa.’—1 Petro 2:12; 2 Petro 3:11, 14.
4. Mwabudu wa Yehova anawezaje kujua yeye si mtu wa aina gani?
4 Pia waabudu wa kweli wa Yehova wanajua wao si watu wa aina gani. “Wao si sehemu ya ulimwengu,” kama vile Kiongozi wao Yesu Kristo hakuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 17:16) Wao hujitenga na “mataifa,” ambayo ‘yako katika giza kiakili, na kutenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu.’ (Waefeso 4:17, 18) Kwa sababu hiyo, wafuasi wa Yesu ‘hukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.’—Tito 2:12.
5. Ni nini maana ya kitia moyo ‘kujisifu katika Yehova’?
5 Kuelewa waziwazi utambulisho wetu na uhusiano wetu pamoja na Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote hutuchochea ‘tujisifu katika Yehova.’ (1 Wakorintho 1:31) Huko ni kujisifu kwa aina gani? Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajivunia Yehova kuwa Mungu wetu. Tunafuata kitia moyo hiki: “Yule anayejigamba na ajigambe kwa sababu ya jambo hili, kuwa na ufahamu na kuwa na ujuzi kunihusu mimi, kwamba mimi ni Yehova, Yeye anayeonyesha fadhili zenye upendo, haki na uadilifu duniani.” (Yeremia 9:24) ‘Tunajisifu’ kwa kuwa na pendeleo la kumjua Mungu na kutumiwa naye kuwasaidia wengine.
Ugumu Uliopo
6. Kwa nini watu fulani huona ni vigumu kudumisha utambulisho wao wa Kikristo ulio wazi?
6 Ni kweli kwamba, sikuzote si rahisi kudumisha utambulisho wetu wa Kikristo ulio wa pekee. Mwanamume mmoja kijana aliyelelewa akiwa Mkristo alikumbuka kwamba kwa kipindi fulani alikuwa na udhaifu wa kiroho. Anasema hivi: “Nyakati nyingine, nilihisi kwamba sikujua kwa nini nilikuwa Shahidi wa Yehova. Nilifunzwa kweli tangu utotoni. Nyakati nyingine nilihisi kwamba hii ilikuwa tu dini nyingine kubwa inayokubaliwa na wengi.” Huenda wengine wameruhusu vitumbuizo, vyombo vya habari, na mtazamo wa kutomwogopa Mungu uathiri utambulisho wao. (Waefeso 2:2, 3) Nyakati nyingine huenda baadhi ya Wakristo wakajitilia shaka na kuchunguza upya viwango na miradi yao.
7. (a) Ni kujichunguza kwa aina gani kunakofaa watumishi wa Mungu? (b) Hatari iko wapi?
7 Je, ni vibaya kujichunguza kwa makini kwa kiasi fulani? La. Huenda ukakumbuka kwamba mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waendelee kujichunguza wenyewe: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Hapa mtume huyo alikuwa akiwatia moyo Wakristo wajitahidi kuchunguza udhaifu wowote wa kiroho ambao huenda wakawa nao, wakiwa na kusudi la kuchukua hatua ifaayo kuurekebisha. Mkristo anapojijaribu kama yuko katika imani anapaswa kuhakikisha ikiwa maneno na matendo yake yanapatana na mambo anayodai kuamini. Hata hivyo, kujichunguza kusikofaa ambako hutuchochea kutafuta “utambulisho” wetu au kutafuta majibu yasiyohusu uhusiano wetu pamoja na Yehova au na kutaniko la Kikristo ni kwa bure na kunaweza kuwa hatari kiroho.a Hatungependa ‘imani yetu ivunjike’ kamwe.—1 Timotheo 1:19.
Sisi Pia Hupatwa na Magumu
8, 9. (a) Musa alielezaje hisia zake za kujitilia shaka? (b) Yehova alifanyaje Musa alipohisi kuwa hana uwezo? (c) Uhakikisho wa Yehova una matokeo gani juu yako?
8 Je, Wakristo ambao pindi kwa pindi hujitilia shaka wanapaswa kuhisi kuwa wameshindwa? La. Kwa kweli, wanaweza kupata faraja kwa kujua kwamba hisia hizo zimekuwako. Mashahidi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kale walipatwa nayo. Kwa mfano, fikiria Musa aliyeonyesha imani isiyo ya kawaida, ushikamanifu, na ujitoaji-kimungu. Alipopewa mgawo ulioonekana kuwa mgumu, Musa alisitasita na kuuliza hivi: “Mimi ni nani?” (Kutoka 3:11) Yaelekea jibu alilokuwa nalo akilini lilikuwa, ‘Mimi si mtu wa maana!’ au ‘Mimi sina uwezo!’ Huenda Musa alihisi hivyo kwa sababu ya mambo yaliyompata mapema maishani: Alitokana na taifa la watumwa. Alikuwa amekataliwa na Waisraeli. Hakuwa msemaji mwenye ufasaha. (Kutoka 1:13, 14; 2:11-14; 4:10) Alifanya kazi ya uchungaji, kazi ambayo ilichukiwa na Wamisri. (Mwanzo 46:34) Haishangazi kwamba alihisi hafai kuwa mkombozi wa watu wa Mungu waliokuwa utumwani!
9 Yehova alimpa Musa uhakikisho zaidi kupitia ahadi hizi mbili zenye nguvu: “Nitakuwa pamoja nawe, nayo hii ndiyo ishara kwako ya kwamba mimi ndiye niliyekutuma: Baada ya kuwatoa watu hao Misri, ninyi mtamtumikia Mungu wa kweli kwenye mlima huu.” (Kutoka 3:12) Mungu alikuwa akimwambia mtumishi wake mwenye kusita-sita kwamba angekuwa pamoja naye daima. Isitoshe, Yehova alikuwa akionyesha kwamba hakika angewakomboa watu wake. Katika karne zote, Mungu ametoa ahadi kama hizo za kuwasaidia watu wake. Kwa mfano, kupitia Musa aliliambia hivi taifa la Israeli lilipokuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi: “Iweni hodari na wenye nguvu. . . . Yehova Mungu wako ndiye anayepiga mwendo pamoja nawe. Hatakutupa wala kukuacha kabisa.” (Kumbukumbu la Torati 31:6) Pia Yehova alimhakikishia Yoshua hivi: “Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe, . . . Sitakutupa wala kukuacha kabisa.” (Yoshua 1:5) Naye anawaahidi Wakristo hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Kwa kuwa tuna msaada huo wenye nguvu, tunapaswa kujivunia kuwa Wakristo.
10, 11. Mlawi Asafu alisaidiwaje kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu pendeleo la kumtumikia Yehova?
10 Karibu karne tano baada ya kifo cha Musa, Mlawi mwaminifu aliyeitwa Asafu aliandika kwa unyoofu shaka zake kuhusu umuhimu wa kufuatilia mwenendo wa uadilifu. Alipokuwa akijitahidi kumtumikia Mungu licha ya majaribu na vishawishi, Asafu aliona watu fulani waliomdhihaki Mungu wakifanikiwa na kuwa wenye nguvu zaidi. Hilo lilimwathirije Asafu? “Mimi nami karibu miguu yangu igeuke kando,” akakiri. “Hatua zangu zilikuwa karibu kuteleza. Kwa maana niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu.” Alianza kutilia shaka umuhimu wa kuwa mwabudu wa Yehova. “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia,” akawaza Asafu. “Nami nikapata mapigo mchana kutwa.”—Zaburi 73:2, 3, 13, 14.
11 Asafu alishughulikaje na hisia hizo zenye kusumbua? Je, alipuuza hisia hizo? La. Alizitaja katika sala kwa Mungu kama tunavyoona katika Zaburi ya 73. Asafu alibadili kabisa mtazamo wake alipotembelea patakatifu pa hekalu. Akiwa huko, alitambua kwamba kujitoa kwa Mungu ndiyo njia bora zaidi. Baada ya kuthamini tena umuhimu wa kumtumikia Yehova, alifahamu kwamba Yehova anachukia ubaya na kwamba katika wakati wake unaofaa waovu wataadhibiwa. (Zaburi 73:17-19) Baada ya kurekebisha mtazamo wake, Asafu aliimarisha utambulisho wake wa kuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova. Alimwambia Mungu hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.” (Zaburi 73:23, 24) Baadaye, Asafu alijivunia Mungu wake tena.—Zaburi 34:2.
Walitambua Vizuri Wao Ni Nani
12, 13. Toa mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia ambao walijivunia uhusiano wao pamoja na Mungu.
12 Njia moja ya kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo ni kuchunguza na kuiga imani ya waabudu washikamanifu, ambao licha ya magumu walijivunia uhusiano wao pamoja na Mungu. Fikiria Yosefu, mwana wa Yakobo. Akiwa mchanga, aliuzwa kwa hila kama mtumwa na kupelekwa Misri, mamia ya kilometa mbali na baba yake mwenye kumwogopa Mungu na mbali sana na watu waliompenda na kumjali. Akiwa Misri, Yosefu hakuwa na mtu wa kumpa shauri la kimungu, naye alilazimika kukabiliana na hali ngumu zilizojaribu maadili yake na tegemeo lake katika Mungu. Hata hivyo, aliazimia kujitambulisha waziwazi kuwa mtumishi wa Mungu, naye akaendelea kuwa mwaminifu katika mambo aliyojua kuwa ya haki. Alijivunia kuwa mwabudu wa Yehova hata katika mazingira yasiyofaa, naye hakusita kuonyesha jinsi alivyohisi.—Mwanzo 39:7-10.
13 Yapata karne nane baadaye, msichana Mwisraeli aliyetekwa ambaye alikuwa mtumwa wa Naamani, mkuu wa jeshi la Siria, hakusahau kujitambulisha kuwa mwabudu wa Yehova. Nafasi ilipotokea, kwa ujasiri alitoa ushahidi mzuri kumhusu Yehova alipomtambulisha Elisha kuwa nabii wa Mungu wa kweli. (2 Wafalme 5:1-19) Miaka mingi baadaye, licha ya kuwa katika mazingira yaliyopotoka, Mfalme Yosia aliyekuwa kijana, alianzisha marekebisho ya kidini ya muda mrefu, akarekebisha hekalu la Mungu, na kurudisha ibada ya Yehova katika taifa hilo. Alijivunia imani na ibada yake. (2 Mambo ya Nyakati sura ya 34, 35) Danieli na Waebrania wenzake watatu huko Babiloni hawakusahau kujitambulisha kuwa watumishi wa Yehova, na hata walidumisha utimilifu wao chini ya mkazo na vishawishi. Ni wazi kwamba walijivunia kuwa watumishi wa Yehova.—Danieli 1:8-20.
Jivunieni Kuwa Wakristo
14, 15. Ni nini kinachotiwa ndani katika kujivunia kuwa Wakristo?
14 Watumishi hao wa Mungu walifanikiwa kwa sababu walijivunia ifaavyo msimamo wao mbele za Mungu. Namna gani sisi leo? Ni nini kinachotiwa ndani katika kujivunia kuwa Wakristo?
15 Kwanza, hii inatia ndani uthamini mwingi wa kuwa mmoja wa watu wanaoitwa kwa jina la Yehova ambao wana baraka na kibali chake. Mungu hana shaka kuhusu walio wake. Mtume Paulo ambaye aliishi katika kipindi kilichokuwa na mvurugo mkubwa wa kidini aliandika hivi: “Yehova anawajua walio wake.” (2 Timotheo 2:19; Hesabu 16:5) Yehova hujivunia “walio wake.” Anasema: “Yeye anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zekaria 2:8) Ni wazi kwamba Yehova anatupenda. Kwa hiyo, uhusiano wetu pamoja naye unapaswa kutegemea upendo mwingi kumwelekea. Paulo alisema: “Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.”—1 Wakorintho 8:3.
16, 17. Kwa nini Wakristo, vijana kwa wazee, hujivunia urithi wao wa kiroho?
16 Vijana ambao wamelelewa wakiwa Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuchunguza ikiwa utambulisho wao wa Kikristo unazidi kuwa wenye nguvu kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Hawawezi kutegemea tu imani ya wazazi wao. Paulo aliandika hivi kuhusu kila mtumishi wa Mungu: “Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au kuanguka.” Hivyo, Paulo anaendelea kusema: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:4, 12) Ni wazi kwamba, kufuata tu kwa moyo nusu-nusu dini ya wazazi hakuwezi kumsaidia kijana aendelee kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa muda mrefu.
17 Katika historia yote, kumekuwa na mstari wa mashahidi wengi wa Yehova. Ulianza na Abeli mwaminifu—ambaye aliishi yapata miaka 6,000 iliyopita—hadi “umati mkubwa” wa Mashahidi wa kisasa na waabudu wengi wa Yehova watakaoishi milele wakati ujao. (Ufunuo 7:9; Waebrania 11:4) Sisi ndio wa karibuni zaidi katika mstari huo wa waabudu hao wengi walio waaminifu. Tuna urithi wa kiroho ulio mzuri kama nini!
18. Viwango na kanuni zetu hututofautishaje na ulimwengu?
18 Pia utambulisho wetu wa Kikristo unatia ndani kanuni, sifa, na viwango ambavyo hututambulisha kuwa Wakristo. Hiyo ndiyo “Ile Njia,” njia pekee ya maisha yenye mafanikio na ya kumpendeza Mungu. (Matendo 9:2; Waefeso 4:22-24) Wakristo ‘huhakikisha mambo yote’ na ‘kushika sana yaliyo mazuri’! (1 Wathesalonike 5:21) Tunaelewa waziwazi tofauti kubwa iliyopo kati ya Ukristo na ulimwengu uliotenganishwa na Mungu. Yehova anaonyesha waziwazi tofauti iliyopo kati ya ibada ya kweli na ibada ya uwongo. Alisema hivi kupitia nabii wake Malaki: “Mtaona tena tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.”—Malaki 3:18.
19. Wakristo wa kweli hawawezi kamwe kuwa na mtazamo gani?
19 Kwa kuwa kujisifu katika Yehova ni muhimu sana katika ulimwengu huu uliovurugika, ni nini kinachoweza kutusaidia kujivunia ifaavyo Mungu wetu na kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo? Makala inayofuata ina madokezo yanayofaa. Unapofikiria madokezo hayo, unaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Wakristo wa kweli hawawezi kamwe kuwa na ubaridi kuelekea dini.
[Maelezo ya Chini]
a Hapa tunarejelea tu utambulisho wetu wa kiroho. Kwa wale wachache walio na matatizo fulani ya akili, huenda ikawabidi kumwona daktari.
-
-
Kulinda Utambulisho Wetu wa KikristoMnara wa Mlinzi—2005 | Februari 15
-
-
Kulinda Utambulisho Wetu wa Kikristo
“‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova.”—ISAYA 43:10.
1. Ni watu wa aina gani ambao Yehova huwavuta kwake?
UNAPOKUWA kwenye Jumba la Ufalme, tazama kwa makini watu wanaokuzunguka. Unaona nani katika mahali hapo pa ibada? Huenda ukaona vijana wanyoofu wakisikiliza kwa makini hekima ya Biblia. (Zaburi 148:12, 13) Pia yaelekea utaona vichwa vya familia wanaojitahidi kumpendeza Mungu huku wakiishi katika ulimwengu usioheshimu maisha ya familia. Labda utaona wazee wapendwa, wanaoishi kupatana na wakfu wao kwa Yehova wakiwa imara licha ya matatizo yanayosababishwa na uzee. (Methali 16:31) Wote wanampenda sana Yehova. Naye aliona inafaa kuanzisha uhusiano pamoja nao. Mwana wa Mungu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.”—Yohana 6:37, 44, 65.
2, 3. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kudumisha utambulisho wa Kikristo ulio wazi?
2 Je, hatufurahi kuwa kati ya watu walio na kibali na baraka za Yehova? Hata hivyo, si rahisi kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1) Inakuwa hivyo hasa kwa vijana ambao wanalelewa katika familia za Kikristo. Kijana mmoja alikiri hivi: “Ingawa nilikuwa nikihudhuria mikutano ya Kikristo, sikuwa na miradi hususa ya kiroho, na kwa kweli, sikuwa nimesitawisha tamaa ya kumtumikia Yehova.”
3 Wengine ambao huenda wakatamani kwa unyoofu kumtumikia Yehova, wanaweza kukengeushwa na msongo mkali wa marika, uvutano wa ulimwengu, na maelekeo ya dhambi. Tunapokuwa chini ya mkazo mwingi, huenda hatua kwa hatua tukapoteza utambulisho wetu wa Kikristo. Kwa mfano, leo watu wengi katika ulimwengu huona viwango vya Biblia vya maadili kuwa vimepitwa na wakati au visivyofaa katika ulimwengu wa kisasa. (1 Petro 4:4) Wengine huhisi kwamba si lazima kumwabudu Mungu kwa njia anayoonyesha. (Yohana 4:24) Katika barua yake kwa Waefeso, Paulo anautaja ulimwengu kuwa una “roho,” au mtazamo ulioenea. (Waefeso 2:2) Roho hiyo huweka mkazo juu ya watu ili wafikiri kama jamii isiyomjua Yehova.
4. Yesu alikaziaje uhitaji wa kulinda utambulisho wetu wa Kikristo ulio wazi?
4 Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, tunatambua kwamba lingekuwa jambo la kuhuzunisha kwa yeyote kati yetu—kijana au mzee—kupoteza utambulisho wetu wa Kikristo. Kuwa na maoni yanayofaa kuhusu utambulisho wa Kikristo kunaweza kutegemea tu viwango vya Yehova na mambo anayotarajia kutoka kwetu. Hiyo ni kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26; Mika 6:8) Biblia inafananisha utambulisho wetu wa Kikristo ulio wazi na mavazi ya nje, yanayovaliwa ili kuonwa na wote. Kuhusu nyakati zetu, Yesu alionya hivi: “Tazama! Ninakuja kama mwizi. Mwenye furaha ni yule anayekaa macho na kutunza mavazi yake ya nje, ili asipate kutembea akiwa uchi na watu waitazame aibu yake.”a (Ufunuo 16:15) Hatungependa kuvua sifa zetu za Kikristo na viwango vya mwenendo na kuruhusu ulimwengu wa Shetani utufinyange. Ikiwa jambo hilo lingetokea, tungepoteza ‘mavazi hayo ya nje.’ Hali hiyo ingekuwa yenye kusikitisha na yenye kuaibisha.
5, 6. Kwa nini ni muhimu kuwa thabiti kiroho?
5 Utambulisho wa Kikristo ulio wazi huwa na matokeo makubwa sana juu ya maisha ya mtu. Jinsi gani? Mwabudu wa Yehova akipoteza utambulisho wake ulio wazi, huenda akakengeushwa na kukosa mwelekeo au miradi hususa. Biblia inatuonya mara kwa mara kuhusu hali kama hiyo ya kusitasita. Mwanafunzi Yakobo alionya hivi: “Yeye anayetia shaka ni kama wimbi la bahari linaloendeshwa na upepo na kupeperushwa huku na huku. Kwa kweli, mtu huyo asidhani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu anayesitasita, asiye imara katika njia zake zote.”—Yakobo 1:6-8; Waefeso 4:14; Waebrania 13:9.
6 Tunawezaje kulinda utambulisho wetu wa Kikristo? Ni nini kinachoweza kutusaidia kuboresha uwezo wa kutambua pendeleo letu kubwa la kuwa waabudu wa Aliye Juu Zaidi? Tafadhali chunguza njia zifuatazo.
Imarisha Kabisa Utambulisho Wako wa Kikristo
7. Kwa nini ni muhimu kumwomba Yehova atuchunguze?
7 Endelea kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Kitu chenye thamani zaidi alicho nacho Mkristo ni uhusiano wake pamoja na Mungu. (Zaburi 25:14; Methali 3:32) Tukianza kuwa na shaka kuhusu utambulisho wetu wa Kikristo, tunapaswa kuchunguza kwa makini ubora na kina cha uhusiano huo. Kwa kufaa, mtunga-zaburi aliomba hivi: “Unichunguze, Ee Yehova, na kunijaribu; usafishe figo zangu na moyo wangu.” (Zaburi 26:2) Kwa nini ni muhimu kuchunguzwa na Yehova? Kwa sababu hatuwezi kuchanganua nia na maelekeo yetu ya ndani kabisa bila kukosea. Ni Yehova tu anayeweza kuelewa utu wetu wa ndani, yaani, nia yetu, mawazo yetu, na hisia zetu.—Yeremia 17:9, 10.
8. (a) Tunaweza kunufaikaje kwa kujaribiwa na Yehova? (b) Umesaidiwaje kufanya maendeleo ukiwa Mkristo?
8 Kwa kumwomba Yehova atuchunguze, tunamwalika atujaribu. Huenda akaruhusu hali fulani zitokee ambazo hufunua nia yetu ya kweli na hali yetu ya moyoni. (Waebrania 4:12, 13; Yakobo 1:22-25) Tunapaswa kukubali kujaribiwa kwa njia hiyo kwa sababu majaribu hutupa nafasi ya kuonyesha kina cha ushikamanifu wetu kwa Yehova. Kujaribiwa huko kunaweza kuonyesha kama tuko “kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yakobo 1:2-4) Na tunapojaribiwa, tunaweza kukua kiroho.—Waefeso 4:22-24.
9. Kwa nini ni muhimu kujihakikishia kwamba yale ambayo Biblia hufundisha ni kweli? Eleza.
9 Jihakikishie kweli ya Biblia. Utambulisho wetu tukiwa watumishi wa Yehova unaweza kudhoofika usipotegemea kabisa ujuzi wa Biblia. (Wafilipi 1:9, 10) Kila Mkristo, kijana au mzee anahitaji kujihakikishia na kuridhika kwamba mambo anayoamini ndiyo kweli inayopatikana katika Biblia. Paulo aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri.” (1 Wathesalonike 5:21) Vijana Wakristo wanaotoka katika familia zinazomwogopa Mungu wanapaswa kutambua kwamba hawawezi kuwa Wakristo wa kweli kwa sababu tu ya imani ya wazazi wao. Daudi, baba ya Sulemani, alimhimiza ‘amjue Mungu wa baba yake, amtumikie kwa moyo kamili.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Haingetosha tu kijana Sulemani kutazama jinsi baba yake alivyositawisha imani katika Yehova. Alipaswa kumjua Yehova yeye mwenyewe, naye alifanya hivyo. Alimsihi Mungu hivi: “Sasa unipe hekima na ujuzi ili nitoke mbele ya watu hawa na ili niingie ndani.”—2 Mambo ya Nyakati 1:10.
10. Kwa nini si vibaya kuuliza maswali manyoofu kwa nia nzuri?
10 Imani yenye nguvu husitawishwa kupitia ujuzi. Paulo alisema: “Imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba kwa kujifunza Neno la Mungu, tunaimarisha imani yetu na uhakika wetu katika Yehova, ahadi zake, na tengenezo lake. Tunaweza kupata majibu yanayotoa uhakikisho kwa kujiuliza maswali manyoofu kuhusu Biblia. Isitoshe, kwenye Waroma 12:2, tunapata shauri hili la Paulo: “Mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Tunawezaje kufanya hivyo? Kwa kupata “ujuzi sahihi wa ile kweli.” (Tito 1:1) Roho ya Yehova inaweza kutusaidia kuelewa hata habari zilizo ngumu. (1 Wakorintho 2:11, 12) Tunapaswa kusali ili kupata msaada wa Mungu tunapokosa kuelewa jambo fulani. (Zaburi 119:10, 11, 27) Yehova anataka tuelewe Neno lake, tuliamini, na kulitii. Yeye hufurahia maswali manyoofu yanayoulizwa kwa nia nzuri.
Azimia Kumpendeza Mungu
11. (a) Ni tamaa gani ya asili inayoweza kutunasa? (b) Tunawezaje kupata ujasiri wa kupinga msongo wa marika?
11 Jitahidi kumpendeza Mungu, si mwanadamu. Ni jambo la kawaida kujitambulisha na kikundi fulani. Kila mtu anahitaji marafiki, na tunapokubaliwa na wengine tunafurahi na kuhisi usalama. Wakati wa kubalehe na pia baadaye maishani, msongo wa marika unaweza kuwa wenye nguvu na kumfanya mtu atake sana kuwaiga au kuwapendeza wengine. Lakini sikuzote marafiki na marika hawapendezwi na hali yetu nzuri. Nyakati nyingine wanataka tu mtu wa kushirikiana naye katika kufanya mabaya. (Methali 1:11-19) Mkristo anaposhindwa na msongo wa marika usiofaa, kwa kawaida yeye hujaribu kuficha utambulisho wake. (Zaburi 26:4) Mtume Paulo alionya hivi: “Usiruhusu ulimwengu unaokuzunguka ufinyange tabia yako.” (Waroma 12:2, The Jerusalem Bible) Yehova huandaa nguvu tunazohitaji ili kupinga mkazo wowote ambao hufanya tujipatanishe na ulimwengu.—Waebrania 13:6.
12. Ni kanuni na kielelezo gani kinachoweza kutuimarisha tuendelee kuwa thabiti katika imani tumaini letu katika Mungu linapohusika?
12 Mkazo unapotisha kuharibu utambulisho wetu wa Kikristo, tunapaswa kukumbuka kwamba ushikamanifu wetu kwa Mungu ni muhimu zaidi kuliko maoni au maelekeo ya wengi. Maneno haya ya Kutoka 23:2 hutumika kama kanuni ya kutulinda: “Usiufuate umati kwa ajili ya makusudio maovu.” Waisraeli wengi walipotilia shaka uwezo wa Yehova wa kutimiza ahadi Zake, Kalebu alikataa kwa uthabiti kufuata walio wengi. Alikuwa na uhakika kwamba ahadi za Mungu zilikuwa zenye kutegemeka, naye alithawabishwa sana kwa msimamo wake. (Hesabu 13:30; Yoshua 14:6-11) Je, wewe pia uko tayari kupinga mkazo unaotokana na maoni ya wengi ili kulinda uhusiano wako pamoja na Mungu?
13. Kwa nini ni jambo la hekima kuwajulisha wengine msimamo wetu wa Kikristo?
13 Jitambulishe kuwa Mkristo. Ule usemi kwamba kinga ni bora kuliko tiba unaweza kutumika pia tunapotetea utambulisho wetu wa Kikristo. Katika siku za Ezra, jitihada za Waisraeli waaminifu za kufanya mapenzi ya Yehova zilipopingwa, walisema hivi: “Sisi ni watumishi wa Mungu wa mbingu na dunia.” (Ezra 5:11) Tunaweza kuishiwa na nguvu kwa woga iwapo tutaathiriwa na jinsi watu wenye uadui wanavyoitikia na pia uchambuzi wao. Ikiwa sikuzote tutajaribu kumpendeza kila mtu, hatutakuwa na matokeo sana katika kujitambulisha. Kwa hiyo, usitishwe. Sikuzote ni vizuri kuwajulisha wengine waziwazi kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa heshima na kwa uthabiti, unaweza kuwaeleza wengine viwango, imani, na msimamo wako ukiwa Mkristo. Wajulishe wengine kwamba umeazimia kudumisha viwango vya Yehova vya juu kuhusu maadili. Wajulishe waziwazi kwamba huwezi kulegeza msimamo wako wa utimilifu wa Kikristo. Onyesha kwamba unajivunia viwango vyako vya maadili. (Zaburi 64:10) Kusimama imara ukiwa Mkristo kunaweza kukutia nguvu, kukulinda, na hata kuwachochea wengine watake kumjua Yehova na watu wake.
14. Je, tunapaswa kuvunjwa moyo na dhihaka au upinzani? Eleza.
14 Naam, huenda wengine wakakudhihaki au kukupinga. (Yuda 18) Wengine wasipoitikia vizuri jitihada zako za kuwaeleza viwango vyako, usivunjike moyo. (Ezekieli 3:7, 8) Hata uwe umeazimia kadiri gani, hutawasadikisha kamwe watu wasiotaka kusadikishwa. Mkumbuke Farao. Yeye hakusadiki kwamba Musa alikuwa akisema kwa niaba ya Yehova licha ya mapigo au miujiza, na hata kifo cha mzaliwa wake wa kwanza. Kwa hiyo, usiruhusu woga wa mwanadamu ufanye uishiwe na nguvu. Tumaini na imani katika Mungu zinaweza kutusaidia kushinda woga.—Methali 3:5, 6; 29:25.
Jifunze Kutokana na Yaliyopita, Jenga kwa Ajili ya Wakati Ujao
15, 16. (a) Urithi wetu wa kiroho ni nini? (b) Tunaweza kunufaikaje kwa kutafakari urithi wetu wa kiroho tukitumia Neno la Mungu?
15 Thamini urithi wako wa kiroho. Kwa kutumia Neno la Mungu, Wakristo watanufaika kwa kutafakari urithi wao mkubwa wa kiroho. Urithi huo unatia ndani kweli ya Neno la Yehova, tumaini la uzima wa milele, na pendeleo la kumwakilisha Mungu tukiwa watangazaji wa habari njema. Je, unaweza kuona daraka lako miongoni mwa Mashahidi wake, ambao wakiwa kikundi wana pendeleo la kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme inayookoa uhai? Kumbuka kwamba Yehova tu ndiye anayetoa uhakikisho huu: “Ninyi ni mashahidi wangu.”—Isaya 43:10.
16 Unaweza kujiuliza maswali kama vile: ‘Urithi huo wa kiroho ni wenye thamani kadiri gani kwangu? Je, ninauthamini sana hivi kwamba ninatanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwangu? Je, ninauthamini sana hivi kwamba unaniimarisha kupinga kishawishi chochote kinachoweza kufanya niupoteze?’ Pia urithi wetu wa kiroho unaweza kutupa hali ya usalama wa kiroho ambayo inaweza kupatikana tu katika tengenezo la Yehova. (Zaburi 91:1, 2) Kuchunguza matukio muhimu katika historia ya tengenezo la Yehova la kisasa kunaweza kukazia akilini mwetu uhakika wa kwamba hakuna mtu au kitu chochote kinachoweza kuwaondoa watumishi wa Yehova duniani.—Isaya 54:17; Yeremia 1:19.
17. Ni nini kingine kinachohitajiwa badala ya kutegemea tu urithi wetu wa kiroho?
17 Bila shaka, hatuwezi kutegemea tu urithi wetu wa kiroho. Lazima kila mmoja wetu asitawishe uhusiano wa karibu sana pamoja na Mungu. Baada ya Paulo kujitahidi sana kujenga imani ya Wakristo huko Filipi, aliwaandikia hivi: “Kwa hiyo, wapendwa wangu, kwa jinsi ambavyo mmekuwa mkitii sikuzote, si wakati wa kuwapo kwangu tu, bali kwa utayari zaidi sasa wakati wa kutokuwapo kwangu, endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Wafilipi 2:12) Hatuwezi kumtegemea mtu mwingine ili kupata wokovu.
18. Utendaji wa Kikristo unawezaje kuboresha utambulisho wetu wa Kikristo?
18 Shiriki katika utendaji wa Kikristo kadiri uwezavyo. Inasemekana kwamba “kazi huathiri sana utu wa mtu.” Leo Wakristo wamepewa kazi muhimu sana ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Paulo alisema: “Kwa maana kama nilivyo, kwa kweli, mtume kwa mataifa, naitukuza huduma yangu.” (Waroma 11:13) Kazi yetu ya kuhubiri hututofautisha na ulimwengu, na tunapoifanya tunaboresha utambulisho wetu wa Kikristo. Kushiriki katika utendaji mwingine wa Kikristo kadiri tuwezavyo, kama vile mikutano ya Kikristo, programu za kujenga mahali pa ibada, jitihada za kuwasaidia wenye uhitaji, na mambo kama hayo, kunaweza kuimarisha utambulisho wetu wa Kikristo.—Wagalatia 6:9, 10; Waebrania 10:23, 24.
Utambulisho Ulio Wazi Huleta Manufaa Halisi
19, 20. (a) Umepata manufaa gani binafsi kwa kuwa Mkristo? (b) Ni nini hutupa msingi wa utambulisho wa kweli?
19 Ebu fikiria kwa muda mfupi baraka nyingi na manufaa tunayopata kwa sababu ya kuwa Wakristo wa kweli. Tuna pendeleo la kutambuliwa kibinafsi na Yehova. Nabii Malaki alisema hivi: “Wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.” (Malaki 3:16) Tunaweza kuonwa na Mungu kuwa marafiki wake. (Yakobo 2:23) Maisha yetu huboreshwa na kuwa na kusudi lililo wazi, yanakuwa na maana, na miradi inayofaa na yenye matokeo. Na tumepewa tumaini la kuishi milele wakati ujao.—Zaburi 37:9.
20 Kumbuka kwamba Mungu ndiye anayeamua jinsi ulivyo na thamani na pia utambulisho wako halisi wala si maoni ya watu. Huenda wengine wakatuona kulingana na viwango vya kibinadamu ambavyo vimepungukiwa. Lakini upendo wa Mungu na kupendezwa nasi binafsi hufanya tuwe wenye thamani halisi—sisi ni watu wake. (Mathayo 10:29-31) Kisha, upendo wetu kwa Mungu unaweza kutupa utambulisho na mwongozo ulio wazi zaidi maishani. “Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.”—1 Wakorintho 8:3.
[Maelezo ya Chini]
a Huenda maneno hayo yakarejelea kwa njia isiyo ya moja kwa moja kazi za ofisa wa hekalu la mlimani huko Yerusalemu. Wakati wa makesha ya usiku alitembea hekaluni ili kuona ikiwa walinzi Walawi walikuwa macho au walikuwa wamelala mahali pao pa kazi. Mlinzi yeyote aliyepatikana amelala alipigwa kwa kijiti, na huenda mavazi yake ya nje yalichomwa kama adhabu ya kumwaibisha.
-