Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za Taabu
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
    • Tunapotaabishwa na Matatizo ya Afya

      10. Mfano wa Mfalme Daudi unaonyeshaje kwamba ni jambo la busara kumtumaini Yehova tunapougua ugonjwa mbaya?

      10 Je, ni jambo la busara kumtumaini Yehova tunapougua ugonjwa mbaya? Ndiyo kabisa! Yehova huwahurumia wagonjwa miongoni mwa watu wake. Zaidi ya hayo, yeye yuko tayari kuwasaidia. Kwa mfano, mfikirie Mfalme Daudi. Huenda yeye mwenyewe alikuwa mgonjwa mahututi alipoandika jinsi Mungu anavyomtendea mwadilifu anayeugua. Alisema: “BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia.” (Zaburi 41:1, 3, 7, 8) Mfalme Daudi aliendelea kumtumaini Mungu kabisa na hatimaye mfalme huyo akapona ugonjwa wake. Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunamtumaini Mungu tunapotaabishwa na matatizo ya afya?

      11. Tunapougua ugonjwa, tunaweza kumwomba nini Baba yetu wa mbinguni?

      11 Tunapougua ugonjwa, njia moja ya kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova ni kwa kumsihi katika sala atusaidie kuvumilia. Tunaweza kumwomba atusaidie tutumie “hekima kamili” ili tuweze kutafuta matibabu kulingana na hali zetu. (Mithali 3:21) Tunaweza pia kumwomba atusaidie kuwa na uvumilivu na subira ili tukabiliane na ugonjwa huo. Zaidi ya yote, tungependa kumwomba Yehova atutegemeze na kutupa nguvu za kuendelea kuwa waaminifu kwake bila kupoteza usawaziko hata jambo gani litokee. (Wafilipi 4:13) Kudumisha uaminifu wetu kwa Mungu ni muhimu zaidi hata kuliko kulinda uhai wetu wa sasa. Tukiendelea kuwa waaminifu, Mthawabishaji Mkuu atatupa afya na uhai mkamilifu milele.—Waebrania 11:6.

      12. Ni kanuni gani za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima kuhusiana na matibabu?

      12 Kumtumaini Yehova pia hutuchochea tutegemee mwongozo kutoka katika Neno lake Biblia. Kanuni zinazopatikana katika Maandiko zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima kuhusu matibabu. Kwa mfano, tukijua kwamba Biblia inashutumu “zoea la uwasiliani-roho,” tutaepuka njia yoyote ya kupima magonjwa au matibabu yanayohusisha uwasiliani-roho. (Wagalatia 5:19-21; Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Mfano mwingine wa hekima ya Biblia yenye kutegemeka ni huu: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15) Hivyo, tunapofikiria matibabu fulani, litakuwa jambo la hekima kutafuta habari zenye kutegemeka badala ya ‘kuamini kila neno.’ ‘Utimamu huo wa akili’ unaweza kutusaidia kufikiria kwa makini machaguo yetu na kufanya uamuzi unaotegemea habari kamili.—Tito 2:12.

      13, 14. (a) Ni makala gani zenye kuarifu kuhusu afya ambazo zimechapishwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!? (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 17.) (b) Ni shauri gani kuhusu jinsi ya kushughulika na magonjwa yanayodumu lililotolewa katika Amkeni! la Januari 22, 2001?

      13 Tunaweza pia kuonyesha kwamba tunamtumaini Yehova kwa kuchunguza vichapo vya mtumwa mwaminifu. Mara kwa mara, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamechapisha makala zenye kuwaarifu wasomaji kuhusu matatizo hususa ya afya na magonjwa.d Nyakati nyingine, magazeti hayo yamechapisha makala za watu ambao wamekabiliana kwa mafanikio na magonjwa na ulemavu mbalimbali. Zaidi ya hayo, makala fulani zimetoa madokezo ya Kimaandiko na vilevile mashauri kuhusu jinsi ya kuishi na matatizo ya kiafya yanayodumu.

      14 Kwa mfano, gazeti la Amkeni! la Januari 22, 2001, lilichapisha mfululizo wa makala zenye kichwa “Faraja kwa Wagonjwa.” Makala hizo zilitaja kanuni nzuri za Biblia na pia habari kutoka kwa watu waliohojiwa ambao wana ujuzi kuhusu magonjwa yenye kudhoofisha mwili ambayo wameugua kwa miaka mingi. Makala “Kuishi kwa Mafanikio na Ugonjwa Wako—Jinsi Gani?” ilitoa shauri linalofuata: Jifunze mengi kadiri uwezavyo kuhusu ugonjwa wako. (Mithali 24:5) Weka miradi unayoweza kutimiza, kutia ndani miradi ya kuwasaidia wengine, lakini kumbuka kwamba huenda usiweze kutimiza miradi ambayo wengine wanatimiza. (Matendo 20:35; Wagalatia 6:4) Epuka kujitenga na wengine. (Mithali 18:1) Wafanye wengine wafurahie kukutembelea. (Mithali 17:22) Zaidi ya yote, dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kutaniko. (Nahumu 1:7; Waroma 1:11, 12) Je, hatushukuru kwa mwongozo wenye kutegemeka ambao Yehova hutupa kupitia tengenezo lake?

  • Mtumaini Yehova Kikamili Nyakati za Taabu
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Septemba 1
    • [Sanduku katika ukurasa wa 17]

      Je, Unakumbuka Makala Hizi?

      Tunapotaabishwa na matatizo ya afya, tunatiwa moyo tunaposoma kuhusu wengine ambao wamekabiliana kwa mafanikio na magonjwa na ulemavu. Zifuatazo ni baadhi ya makala zilizochapishwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

      “Kuwezana na Hali za Udhaifu Wangu” ilikazia jinsi ya kushughulika na maoni yasiyofaa na kushuka moyo.—Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1990.

      “Hata Pafu la Chuma Halikumzuia Kuhubiri.”—Amkeni!, Januari 22, 1993.

      “Risasi Ilibadili Maisha Yangu” ilizungumzia jinsi ya kushughulika na kupooza.—Amkeni!, Oktoba 22, 1995.

      “Hamjui Uhai Wenu Utakuwa Nini Kesho” ilizungumzia jinsi ya kukabiliana na ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia.—Mnara wa Mlinzi, Desemba 1, 2000.

      “Loida Aacha Kukimya” ilizungumzia jinsi ya kushughulika na ugonjwa wa kupooza ubongo.—Amkeni!, Mei 8, 2000.

      “Matatizo Yangu ya Endometriosis.”—Amkeni!, Julai 22, 2000.

      “Pambano Langu na Ugonjwa wa Mfumo wa Kinga.”—Amkeni!, Agosti 8, 2001.

      “Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua.”—Amkeni!, Julai 22, 2002.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki