-
Yehova Ni Fungu LanguMnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
-
-
Yehova Ni Fungu Langu
“Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.”—HES. 18:20.
1, 2. (a) Walawi walikuwa katika hali gani kuhusiana na urithi wa nchi? (b) Yehova aliwapa Walawi ahadi gani?
BAADA ya Waisraeli kuchukua sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi, Yoshua alianza kazi ya kugawa nchi hiyo kwa kura. Alifanya kazi hiyo akishirikiana na Kuhani Mkuu Eleazari pamoja na wakuu wa makabila. (Hes. 34:13-29) Walawi hawakupaswa kupewa urithi wa nchi kama ule ambao yale makabila mengine yalipewa. (Yos. 14:1-5) Kwa nini kabila la Lawi halikuwa na eneo, au fungu, katika ile Nchi ya Ahadi? Je, walisahauliwa?
2 Jibu linapatikana katika maneno ambayo Yehova aliwaambia Walawi. Ili kukazia kwamba hakuwa amewaacha, Yehova aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako na urithi wako katikati ya wana wa Israeli.” (Hes. 18:20)
-
-
Yehova Ni Fungu LanguMnara wa Mlinzi—2011 | Septemba 15
-
-
Yehova Aliwatunza Walawi
3. Ni nini kilichomfanya Mungu awachukue Walawi kwa ajili ya utumishi wake?
3 Kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria, vichwa vya familia walitumikia wakiwa makuhani katika familia zao. Mungu alipowapa Sheria, alichagua watu fulani kutoka katika kabila la Lawi ili watumike daima wakiwa makuhani na wasaidizi. Alifanya hivyo jinsi gani? Mungu alipowaangamiza wazaliwa wa kwanza huko Misri, aliwatakasa wazaliwa wa kwanza wa Israeli, na kuwaweka kando ili wawe wake, wawe mali yake. Kisha Mungu akafanya badiliko hili kubwa: “Nawachukua Walawi . . . mahali pa wazaliwa wote wa kwanza katikati ya wana wa Israeli.” Kwa kuwa hesabu ya watu ilionyesha kwamba wazaliwa wa kwanza wa Israeli walikuwa wengi kuliko Walawi, bei ya fidia au ukombozi ililipwa ili kujazia tofauti hiyo. (Hes. 3:11-13, 41, 46, 47) Hivyo, Walawi wangeweza kutimiza daraka lao la kumtumikia Mungu wa Israeli.
4, 5. (a) Mungu alimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa fungu la Walawi? (b) Mungu aliwatunza Walawi jinsi gani?
4 Mgawo huo ulimaanisha nini kwa Walawi? Yehova alisema kwamba angekuwa fungu lao kumaanisha kwamba badala ya kupewa urithi wa nchi, walikabidhiwa pendeleo lenye thamani sana la utumishi. Wangepata urithi wa kuwa “ukuhani wa Yehova.” (Yos. 18:7) Mistari mingine inayozunguka andiko la Hesabu 18:20 inaonyesha kwamba jambo hilo halikufanya wawe maskini kimwili. (Soma Hesabu 18:19, 21, 24.) Walawi walipaswa kupewa “kila sehemu ya kumi katika Israeli iwe urithi wao kwa sababu ya utumishi wao.” Wangepokea asilimia 10 ya mazao yote ya Waisraeli na ya wanyama walioongezeka. Kisha Walawi walipaswa kutoa sehemu ya 10 ya vitu walivyopokea kuwa mchango, “ule ulio bora zaidi,” ili kutegemeza ukuhani.a (Hes. 18:25-29) Makuhani walipewa pia “michango yote mitakatifu” ambayo wana wa Israeli walimletea Mungu mahali pake pa Ibada. Hivyo, washiriki wa ukuhani walikuwa na sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova angewatunza.
5 Inaonekana kwamba Sheria ya Musa iliwaagiza Waisraeli watoe sehemu nyingine ya kumi. Familia za Waisraeli zilitumia sehemu hiyo kununua vyakula na vinywaji na pia kujifurahisha wakati wa makusanyiko matakatifu kila mwaka. (Kum. 14:22-27) Hata hivyo, mwishoni mwa kila mwaka wa tatu na wa sita wa mzunguko wa sabato wa miaka saba, sehemu hiyo ya kumi iliwekwa kwenye malango ili kuwasaidia maskini na pia Walawi. Kwa nini Walawi walipewa pia msaada huo? Kwa sababu ‘hawakuwa na fungu wala urithi’ katika Israeli.—Kum. 14:28, 29.
6. Kwa kuwa kabila la Lawi halikuwa na fungu la nchi katika Israeli, Walawi wangeishi wapi?
6 Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Walawi hawakugawiwa nchi yoyote, wangeishi wapi?’ Mungu aliwapa mahali pa kuishi. Aliwapa majiji 48 pamoja na viwanja vya malisho vilivyozunguka majiji hayo. Majiji hayo yalitia ndani majiji sita ya makimbilio. (Hes. 35:6-8) Hivyo, Walawi walikuwa na mahali pa kuishi wakati ambapo hawakuwa wakitumika katika patakatifu pa Mungu. Yehova aliwatunza kabisa wale ambao walijitoa wenyewe katika utumishi wake. Ni wazi kwamba Walawi walionyesha kuwa Yehova ni fungu lao kwa kutegemea uwezo na utayari wake wa kuwatunza.
7. Walawi walihitaji kuwa na nini ili Yehova awe fungu lao?
7 Sheria haikutaja adhabu yoyote ambayo Mwisraeli angepata ikiwa angekosa kutoa sehemu ya kumi. Watu walipopuuza kutoa sehemu ya kumi, makuhani na Walawi waliumia. Ndivyo ilivyokuwa katika siku za Nehemia. Matokeo yalikuwa kwamba Walawi walilazimika kufanya kazi katika mashamba yao, na kupuuza huduma yao. (Soma Nehemia 13:10.) Ni wazi kwamba Walawi walipata tu mahitaji yao wakati taifa hilo lilipotii Sheria ya Yehova. Zaidi ya hayo, makuhani na Walawi wenyewe walihitaji kuwa na imani katika Yehova na njia yake ya kuwaandalia mahitaji yao.
-