Hesabu
34 Yehova akaendelea kumwambia Musa: 2 “Wape Waisraeli maagizo haya: ‘Mtakapoingia katika nchi ya Kanaani,+ nchi mtakayoirithi, hii ndiyo itakayokuwa mipaka ya nchi hiyo ya Kanaani.+
3 “‘Mpaka wenu wa kusini utaanzia nyika ya Zini kando ya Edomu, na upande wa mashariki mpaka huo wa kusini utaanzia mwisho wa Bahari ya Chumvi.+ 4 Kisha mpaka huo utapinda na kwenda upande wa kusini wa mwinuko wa Akrabimu,+ nao utaendelea mpaka Zini na kuishia upande wa kusini wa Kadesh-barnea.+ Kisha utaenda Hasar-adari+ na kuendelea mpaka Asimoni. 5 Mpaka huo utapinda huko Asimoni na kuelekea kwenye Bonde la Misri na kuishia kwenye Bahari ya Mediterania.+
6 “‘Mpaka wenu wa magharibi utakuwa Bahari Kuu* na pwani. Huo utakuwa mpaka wenu wa magharibi.+
7 “‘Huu ndio utakaokuwa mpaka wenu wa kaskazini: Mtaweka alama kuanzia Bahari Kuu mpaka Mlima Hori.+ 8 Kutoka Mlima Hori mtaweka alama mpaka Lebo-hamathi,*+ nao utaishia Sedadi.+ 9 Kisha utaendelea hadi Zifroni na kuishia Hasar-enani.+ Huo utakuwa mpaka wenu wa kaskazini.
10 “‘Kisha mtaweka alama ya mpaka wenu wa mashariki kuanzia Hasar-enani hadi Shefamu. 11 Mpaka huo utaanzia Shefamu hadi Ribla, upande wa mashariki wa Aini, nao utashuka na kuvuka mteremko wa mashariki wa Bahari ya Kinerethi.*+ 12 Kisha utaendelea mpaka Yordani na kuishia kwenye Bahari ya Chumvi.+ Hiyo ndiyo itakayokuwa nchi yenu+ na mipaka inayoizunguka.’”
13 Kwa hiyo Musa akawapa Waisraeli maagizo haya: “Hiyo ndiyo nchi mtakayoigawanya kwa kura na kuimiliki,+ kama Yehova alivyoamuru kwamba makabila tisa na nusu yapewe nchi hiyo. 14 Kwa maana kabila la Rubeni kulingana na koo zao,* kabila la Gadi kulingana na koo zao,* na nusu ya kabila la Manase tayari yamechukua urithi wao.+ 15 Makabila hayo mawili na nusu tayari yamechukua urithi wao upande wa mashariki wa Yordani karibu na Yeriko, upande wa mapambazuko ya jua.”+
16 Yehova akaendelea kumwambia Musa, 17 “Haya ndiyo majina ya wanaume watakaowagawia nchi ili mwimiliki: kuhani Eleazari+ na Yoshua+ mwana wa Nuni. 18 Nanyi mtachukua mkuu mmoja kutoka katika kila kabila ili awasaidie kuigawanya nchi mtakayorithi.+ 19 Haya ndiyo majina ya wanaume hao: kutoka kabila la Yuda,+ Kalebu+ mwana wa Yefune; 20 kutoka kabila la wana wa Simeoni,+ Shemueli mwana wa Amihudi; 21 kutoka kabila la Benjamini,+ Elidadi mwana wa Kisloni; 22 kutoka kabila la wana wa Dani,+ mkuu mmoja, Buki mwana wa Yogli; 23 kutoka kwa wana wa Yosefu,+ kwa ajili ya kabila la wana wa Manase,+ mkuu mmoja, Hanieli mwana wa Efodi; 24 kutoka kabila la wana wa Efraimu,+ mkuu mmoja, Kemueli mwana wa Shiftani; 25 kutoka kabila la wana wa Zabuloni,+ mkuu mmoja, Elisafani mwana wa Parnaki; 26 kutoka kabila la wana wa Isakari,+ mkuu mmoja, Paltieli mwana wa Azani; 27 kutoka kabila la wana wa Asheri,+ mkuu mmoja, Ahihudi mwana wa Shelomi, 28 na kutoka kabila la wana wa Naftali,+ mkuu mmoja, Pedaheli mwana wa Amihudi.” 29 Hao ndio wanaume ambao Yehova aliamuru wawagawie Waisraeli ardhi katika nchi ya Kanaani.+