-
Barua Kutoka kwa Baraza LinaloongozaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
Ikiwa wewe ni mwanamume uliyebatizwa, unaweza kufanya nini ili ustahili kuwa mtumishi wa huduma na baadaye mzee wa kutaniko? Kadiri maelfu ya wapya wanavyoendelea kumiminika katika tengenezo la Mungu, ndivyo kunavyokuwa na uhitaji mkubwa wa ndugu wanaostahili kuongoza. Kitabu hiki kitakusaidia kuelewa mambo yanayohusika ili ‘ujitahidi’ kufikia mapendeleo hayo ya kiroho.—1 Tim. 3:1.
Tunasali kwa dhati kwamba kitabu hiki kitakusaidia kutambua sehemu yako katika mpango wa Yehova na kuithamini. Tunawapenda sana ninyi nyote na tunaendelea kusali kwamba mtakuwa miongoni mwa wale ambao wataendelea kushangilia milele katika kumwabudu Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Zab. 37:10, 11; Isa. 65:21-25.
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova
-
-
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya YehovaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 1
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
ULIMWENGUNI pote, kuna mashirika mengi ya kidini, kisiasa, kibiashara, na kijamii yenye mpangilio, malengo, maoni, na falsafa mbalimbali. Lakini kuna tengenezo moja lililo tofauti kabisa na mashirika mengine yote. Neno la Mungu linaonyesha waziwazi kwamba tengenezo hilo ni Mashahidi wa Yehova.
2 Inafurahisha kwamba umeanza kushirikiana na tengenezo la Yehova. Baada ya kujihakikishia mwenyewe mapenzi ya Mungu, sasa unayafanya. (Zab. 143:10; Rom. 12:2) Wewe ni mhudumu mwenye bidii anayeshirikiana na ushirika wenye upendo wa akina ndugu ulimwenguni pote. (2 Kor. 6:4; 1 Pet. 2:17; 5:9) Kama vile Neno la Mungu linavyoahidi, kufanya hivyo kunakuletea baraka na furaha nyingi. (Met. 10:22; Marko 10:30) Kwa kufanya mapenzi ya Yehova kwa uaminifu, unatayarishwa kufurahia uzima wa milele wakati ujao.—1 Tim. 6:18, 19; 1 Yoh. 2:17.
3 Muumba wetu Mkuu ana tengenezo la pekee la ulimwenguni pote linaloongozwa kitheokrasi. Hilo linamaanisha kwamba Yehova ndiye anayelitawala akiwa Kichwa cha wote. Tunamtumaini kabisa. Yeye ndiye Mwamuzi wetu, Mpaji-sheria wetu, na Mfalme wetu. (Isa. 33:22) Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye utaratibu, amefanya mipango inayotuwezesha ‘kufanya kazi pamoja naye’ ili kutimiza kusudi lake.—2 Kor. 6:1, 2.
4 Mwisho wa mfumo huu wa mambo unapozidi kukaribia, tunasonga mbele tukiongozwa na Mfalme aliyeteuliwa, Kristo Yesu. (Isa. 55:4; Ufu. 6:2; 11:15) Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangefanya kazi kubwa zaidi kuliko zile alizofanya wakati wa huduma yake hapa duniani. (Yoh. 14:12) Hilo lingewezekana kwa sababu baada ya muda kupita na idadi yao kuongezeka, wafuasi wa Yesu wangefika maeneo ya mbali zaidi. Wangetangaza habari njema ya Ufalme hadi sehemu za mbali za dunia.—Mt. 24:14; 28:19, 20; Mdo. 1:8.
5 Tayari unabii huo umetimia. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema waziwazi, kazi ya kutangaza habari njema itakoma wakati uliowekwa wa Yehova utakapofika. Kulingana na Neno la Mungu la kinabii, ni wazi kwamba ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha imekaribia.—Yoeli 2:31; Sef. 1:14-18; 2:2, 3; 1 Pet. 4:7.
Tunahitaji kuongeza jitihada katika kazi ambayo Mungu alitupatia. Ili tufanikiwe kufanya hivyo, tunapaswa kujua vizuri jinsi tengenezo la Mungu linavyofanya kazi na kushirikiana nalo kikamili
6 Tunapotambua mapenzi ya Yehova katika siku hizi za mwisho, tunahitaji kuongeza jitihada katika kazi aliyotupatia. Ili tufanikiwe kufanya hivyo, tunapaswa kujua vizuri jinsi tengenezo la Mungu linavyofanya kazi na kushirikiana nalo kikamili. Utendaji wa tengenezo hilo unategemea kanuni za Kimaandiko, kutia ndani amri, sheria, maagizo, miongozo, na mafundisho yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.—Zab. 19: 7-9.
7 Watu wa Yehova wanapofuata mwongozo huo wa Biblia, wanashirikiana na kufanya kazi kwa amani na umoja. (Zab. 133:1; Isa. 60:17; Rom. 14:19) Ni nini kinachowaunganisha ndugu na dada zetu ulimwenguni pote? Ni upendo. Tunachochewa na upendo na tumejivika upendo. (Yoh. 13:34, 35; Kol. 3:14) Kwa kufuata njia hiyo inayompendeza Mungu, tunaenda sambamba na sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova.
SEHEMU YA KIMBINGU YA TENGENEZO LA YEHOVA
8 Nabii Isaya, Ezekieli, na Danieli waliona maono ya sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova. (Isa., sura ya 6; Eze., sura ya 1; Dan. 7:9, 10) Mtume Yohana pia alipata maono ya mpangilio wa kimbingu na kutueleza juu yake katika kitabu cha Ufunuo. Alimwona Yehova kwenye kiti chenye utukufu cha ufalme pamoja na malaika, waliokuwa wakitangaza hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza-Yote, aliyekuwako na aliyeko na anayekuja.” (Ufu. 4:8) Yohana pia alimwona “mwanakondoo . . . akiwa amesimama katikati ya kile kiti cha ufalme,” yaani, Yesu Kristo, Mwanakondoo wa Mungu.—Ufu. 5:6, 13, 14; Yoh. 1:29.
9 Maono hayo ya Yehova akiwa ameketi kwenye kiti cha ufalme yanaonyesha kwamba yeye ndiye Kichwa cha tengenezo hilo. Kitabu cha 1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12 kinasema hivi kuhusu cheo chake kikuu: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na fahari na utukufu, kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova. Wewe Ndiye unayejikweza mwenyewe ukiwa mkuu juu ya vyote. Utajiri na utukufu hutoka kwako, nawe hutawala kila kitu, na mkononi mwako mna nguvu na uwezo, na mkono wako unaweza kumfanya mtu awe mkuu na unaweza kuwapa wote nguvu.”
10 Akiwa mfanyakazi mwenzi wa Yehova, Yesu Kristo ana cheo cha juu mbinguni, naye amepewa mamlaka kubwa. Kwa kweli, Mungu ‘alivitiisha vitu vyote chini ya miguu yake, na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.’ (Efe. 1:22) Mtume Paulo alisema hivi kumhusu Yesu: “Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu kuliko kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe—la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi—na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Flp. 2:9-11) Kwa hiyo, tunaweza kuutumaini kabisa uongozi mwadilifu wa Yesu Kristo.
11 Katika maono, nabii Danieli alimwona Mzee wa Siku kwenye kiti Chake cha ufalme mbinguni na malaika “elfu kwa maelfu [walioendelea] kumhudumia, na elfu kumi mara elfu kumi [waliosimama] mbele zake.” (Dan. 7:10) Biblia inawaita malaika hao “roho kwa ajili ya utumishi mtakatifu, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu.” (Ebr. 1:14) Malaika hao wote wamepangwa katika ‘viti vya ufalme, utawala, serikali, na mamlaka.’—Kol. 1:16.
12 Tukitenga wakati ili kutafakari kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova, tunaweza kuelewa jinsi Isaya alivyohisi ‘alipomwona Yehova, akiwa ameketi juu ya kiti cha ufalme kilicho juu na kilichoinuliwa’ na ‘maserafi wakiwa wamesimama juu yake.’ Isaya alisema: “Ole wangu! Kwa maana ni kama nimekufa, kwa maana mimi ni mtu asiye na midomo safi, nami ninaishi kati ya watu wasio na midomo safi; kwa maana macho yangu yamemwona Mfalme, Yehova wa majeshi mwenyewe!” Kwa kweli, Isaya aliogopa na kunyenyekea alipotambua ukubwa wa tengenezo la Yehova. Alichochewa sana na jambo hilo hivi kwamba mwito ulipotolewa kutoka mbinguni kuhusu kazi ya pekee ya kutangaza hukumu za Yehova, Isaya aliitikia hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:1-5, 8.
13 Vivyo hivyo, watu wa Yehova huchochewa wanapolitambua na kulithamini tengenezo lake. Tengenezo linaposonga mbele, sisi hujitahidi kwenda nalo sambamba. Tunajitahidi kuonyesha kwamba tunalitumaini tengenezo la Yehova leo.
TENGENEZO LA YEHOVA LINASONGA MBELE
14 Katika sura ya kwanza ya unabii wa Ezekieli, Yehova anaonekana akiendesha gari kubwa sana la kimbingu. Gari hilo lenye fahari linawakilisha sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova. Analiendesha gari hilo katika maana ya kwamba analielekeza ifaavyo na kulitumia kutimiza kusudi lake.—Zab. 103:20.
15 Kila gurudumu la gari hilo lina gurudumu lingine ndani yake lenye ukubwa uleule. Ndiyo sababu inasemekana kwamba magurudumu hayo yaliweza “kwenda upande wowote kati ya zile pande nne.” (Eze. 1:17) Magurudumu hayo yanaweza kubadili mwelekeo mara moja. Hata hivyo, haimaanishi kwamba gari hilo linajielekeza lenyewe tu. Yehova haliachi tengenezo lake liende popote linapotaka. Andiko la Ezekieli 1:20 linasema hivi: ‘Lilienda popote ambapo roho ililielekeza kwenda.’ Kwa hiyo, Yehova ndiye hufanya tengenezo lake liende mahali popote ambapo roho yake inalielekeza. Basi, tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninaenda sambamba na tengenezo hilo?’
16 Kwenda sambamba na tengenezo la Yehova kunahusisha mengi zaidi ya kuhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani. Kwanza kabisa, kwenda sambamba na tengenezo kunahusisha kufanya maendeleo na kukua kiroho. ‘Tunahakikisha mambo muhimu zaidi’ na kwenda sambamba na programu ya ulishaji wa kiroho. (Flp. 1:10; 4:8, 9; Yoh. 17:3) Pia, lazima tukumbuke kwamba kila shirika au tengenezo linahitaji kuwa na utaratibu na ushirikiano mzuri. Kwa hiyo tunapaswa kutambua umuhimu wa kutumia kikamili vipaji, mali, na ujuzi wa kiroho ambao Yehova ametupatia ili tutimize kazi yake. Tunapoenda sambamba na gari la kimbingu la Yehova, maisha yetu yanapatana na ujumbe tunaotangaza.
17 Kwa msaada wa tengenezo la Yehova, sote tunaendelea kufanya mapenzi ya Mungu. Kumbuka kwamba Mwendeshaji wa gari hilo la kimbingu ni Yehova. Kwa hiyo, kwenda sambamba na gari hilo kunaonyesha kwamba tunamheshimu na kumtumaini Yehova, Mwamba wetu. (Zab. 18:31) Biblia inaahidi hivi: “Yehova atawapa nguvu watu wake. Yehova atawabariki watu wake kwa amani.” (Zab. 29:11) Tukiwa sehemu ya tengenezo la Yehova leo, tunapata nguvu kutoka kwake na kuwa na amani anayowapa watu walio katika tengenezo lake. Naam, hatuna shaka hata kidogo kwamba tutaendelea kupata baraka nyingi tunapofanya mapenzi ya Yehova sasa na milele.
-
-
Kutambua Jukumu la Kristo Katika Mpango wa MunguTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 2
Kutambua Jukumu la Kristo Katika Mpango wa Mungu
“HAPO mwanzo Mungu aliziumba mbingu na dunia,” na kila kitu alichofanya kilikuwa “chema sana.” (Mwa. 1:1, 31) Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tumaini zuri sana la wakati ujao. Hata hivyo, uasi katika Edeni ulivuruga kwa muda furaha ya wanadamu. Ingawa hivyo, kusudi la Yehova kwa dunia na wanadamu halikubadilika. Mungu alidokeza kwamba wazao watiifu wa Adamu wangekombolewa. Ibada ya kweli ingerudishwa, na Mungu angemharibu yule mwovu pamoja na kazi zake mbovu. (Mwa. 3:15) Kwa mara nyingine tena kila kitu kingekuwa “chema sana.” Yehova angetimiza jambo hilo kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. (1 Yoh. 3:8) Kwa hiyo, tunapaswa kutambua jukumu la Kristo katika mpango wa Mungu.—Mdo. 4:12; Flp. 2:9, 11.
JUKUMU LA KRISTO
2 Tunapofikiria jukumu la Kristo katika mpango wa Mungu, tunatambua kwamba jukumu lake linahusisha mambo mengi. Yesu ni Mkombozi wa wanadamu, ni Kuhani Mkuu, ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo, na sasa ni Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Kutafakari majukumu hayo hutufanya tuthamini sana mpango wa Mungu na huzidisha upendo wetu kwa Kristo Yesu. Biblia hufafanua majukumu yake mbalimbali.
Yesu anatimiza jukumu la msingi katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova kwa wanadamu
3 Wakati wa huduma ya Kristo hapa duniani, ilionekana wazi kwamba wanadamu watiifu kwa Mungu wangepatanishwa kupitia Yesu. (Yoh. 14:6) Akiwa Mkombozi wa wanadamu, Yesu alijitoa awe fidia badala ya wengi. (Mt. 20:28) Kwa hiyo, Yesu anafanya mengi zaidi ya kutuwekea mfano wa kumtumikia Mungu. Anatimiza jukumu la msingi katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova kwa wanadamu. Yeye ndiye njia pekee inayotuwezesha kupata tena kibali cha Mungu. (Mdo. 5:31; 2 Kor. 5:18, 19) Kupitia kifo cha Yesu cha kidhabihu na ufufuo wake, wanadamu watiifu wamefunguliwa njia ya kupata baraka za milele chini ya utawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu.
4 Akiwa Kuhani Mkuu, Yesu anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu” na kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za wafuasi wake waliojiweka wakfu hapa duniani. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kwa maana hatuna kuhani mkuu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali tuna yule ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama tulivyojaribiwa, lakini hakutenda dhambi.” Kisha, Paulo akawatia moyo wale wanaomwamini Yesu Kristo watumie kikamili mpango huo wa kupatanishwa na Mungu, aliposema: “Basi na tukikaribie kiti cha ufalme cha fadhili zisizostahiliwa tukiwa na uhuru wa kusema, ili tupokee rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa tunapohitaji msaada.”—Ebr. 4:14-16; 1 Yoh. 2:2.
5 Pia, Yesu ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo. Kama ilivyokuwa kwa wafuasi wake wa karne ya kwanza, leo hatuhitaji kiongozi wa kibinadamu. Yesu huongoza kupitia roho takatifu na kupitia wachungaji walio chini yake na chini ya Baba yake wa mbinguni wanapolitunza kundi la Mungu. (Ebr. 13:17; 1 Pet. 5:2, 3) Yehova alitabiri hivi kumhusu Yesu: “Tazameni! Nilimfanya awe shahidi kwa mataifa, Kiongozi na kamanda kwa mataifa.” (Isa. 55:4) Yesu alithibitisha kutimizwa kwa unabii huo alipowaambia hivi wanafunzi wake: “Wala msiitwe viongozi, kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—Mt. 23:10.
6 Akionyesha kwamba anataka na yuko tayari kutusaidia, Yesu anatoa mwaliko huu: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Kwa kuwa Yesu Kristo anaongoza kutaniko la Kikristo kwa upole na kwa njia ambayo hutuburudisha, amethibitika kuwa “mchungaji mwema” anayemwiga Baba yake wa mbinguni, Yehova Mungu.—Yoh. 10:11; Isa. 40:11.
7 Akieleza jambo lingine kuhusu jukumu la Yesu Kristo, Paulo alisema hivi katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho: “Lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu atakapoweka maadui wote chini ya miguu yake. Lakini vitu vyote vitakapotiishwa kwake, ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yule aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.” (1 Kor. 15:25, 28) Kabla ya kuja duniani, Yesu alikuwa “mfanyakazi stadi” wa Mungu, na ndiye aliyekuwa wa kwanza kuumbwa na Mungu. (Met. 8:22-31) Mungu alipomtuma duniani, Yesu alifanya mapenzi ya Mungu nyakati zote. Alivumilia jaribu kubwa zaidi na kufa akiwa mwaminifu kwa Baba yake. (Yoh. 4:34; 15:10) Kwa kuwa Mwana wake aliendelea kuwa mshikamanifu hadi kifo, Mungu alimfufua na kumrudisha mbinguni na kumpa haki ya kuwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni. (Mdo. 2:32-36) Kwa hiyo, Kristo Yesu amepewa jukumu kubwa na Mungu la kuongoza maelfu ya viumbe wa roho wenye nguvu katika kukomesha utawala wa wanadamu na kuondoa uovu wote duniani. (Met. 2:21, 22; 2 The. 1:6-9; Ufu. 19:11-21; 20:1-3) Kisha, Ufalme wa mbinguni wa Mungu ukiongozwa na Kristo, utaitawala dunia yote.—Ufu. 11:15.
INAMAANISHA NINI KUTAMBUA JUKUMU LA KRISTO?
8 Yesu Kristo ni mkamilifu na ametuwekea mfano bora. Amepewa jukumu la kututunza. Ili tufaidike na utunzaji wake wenye upendo, tunapaswa kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na kwenda sambamba na tengenezo linalosonga mbele.
9 Katika karne ya kwanza, wafuasi wa Yesu walielewa kikamili jukumu la Kristo katika mpango wa Mungu. Walionyesha hivyo kwa kufanya kazi kwa umoja chini ya ukichwa wa Kristo, wakifuata mwongozo wake uliotolewa kupitia roho takatifu. (Mdo. 15:12-21) Mtume Paulo alizungumzia umoja wa kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta alipoandika hivi: “Tukisema ukweli, kupitia upendo na tuendelee kukua katika mambo yote ndani ya Kristo, ambaye ni kichwa. Kupitia kwake mwili wote unaunganishwa na kushirikiana kila kiungo kinapofanya kazi yake. Na kila kiungo kinapofanya kazi vizuri, hilo linafanya mwili ukue na kujijenga katika upendo.”—Efe. 4:15, 16.
10 Kila mshiriki wa kutaniko anaposhirikiana na wengine, na wote wanapofanya kazi kwa upatano chini ya ukichwa wa Kristo, tunapata ongezeko na kudumisha roho nzuri ya upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Yoh. 10:16; Kol. 3:14; 1 Kor. 12:14-26.
11 Matukio ya ulimwengu yanayotimiza unabii wa Biblia yanathibitisha waziwazi kwamba Yesu Kristo alikabidhiwa mamlaka ya Ufalme tangu mwaka wa 1914. Sasa anatawala kati ya maadui wake. (Zab. 2:1-12; 110:1, 2) Hilo linamaanisha nini kwa wale wanaoishi duniani sasa? Hivi karibuni Yesu atatimiza jukumu lake akiwa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana atakapotekeleza hukumu ya Mungu dhidi ya maadui wake. (Ufu. 11:15; 12:10; 19:16) Kisha, ahadi ambayo Yehova alitoa mwanzoni mwa uasi wa wanadamu itatimia kwa wale walio kwenye mkono wa kuume wa Kristo. (Mt. 25:34) Tunafurahi sana kutambua jukumu la Kristo katika mpango wa Mungu! Na tuendelee kuwa na umoja tunapotimiza huduma ya ulimwenguni pote chini ya uongozi wa Kristo katika hizi siku za mwisho.
-
-
“Wakumbukeni Wale Wanaoongoza Kati Yenu”Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 3
“Wakumbukeni Wale Wanaoongoza Kati Yenu”
MANENO hayo ya mtume Paulo, yanapatikana kwenye Waebrania 13:7. Kuanzia Pentekoste 33 W.K. na kuendelea, mitume waaminifu wa Bwana Yesu Kristo walitimiza jukumu hilo wakiwa baraza linaloongoza ambalo lilielekeza kutaniko jipya la Kikristo. (Mdo. 6:2-4) Kufikia mwaka wa 49 W.K., baraza linaloongoza lilitia ndani mitume wa Yesu na Wakristo wengine. Suala la tohara lilipoamuliwa, baraza linaloongoza lilitia ndani “mitume na wazee huko Yerusalemu.” (Mdo. 15: 1, 2) Walikuwa na jukumu la kuamua mambo yaliyowahusu Wakristo kila mahali. Walituma barua na maagizo ambayo yaliimarisha makutaniko na kuwezesha wanafunzi kufikiri na kutenda kwa umoja. Makutaniko yalitii na kufuata mwongozo wa baraza linaloongoza na hivyo yakapata baraka za Yehova na kusitawi.—Mdo. 8:1, 14, 15; 15:22-31; 16:4, 5; Ebr. 13:17.
2 Baada ya mitume wote kufa, ule uasi imani mkubwa ukatokea. (2 The. 2:3-12) Kama Yesu alivyotabiri katika mfano wake wa ngano na magugu, ngano (Wakristo watiwa-mafuta) ilisongwa na magugu (Wakristo wa uwongo). Kwa karne nyingi, vikundi hivyo viliruhusiwa kukua pamoja mpaka wakati wa mavuno, yaani, “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 13:24-30, 36-43) Wakristo mmoja-mmoja waliotiwa mafuta waliendelea kufurahia kibali cha Yesu wakati huo, lakini hakukuwa na baraza linaloongoza wala njia iliyo wazi duniani ambayo Yesu alitumia kuwaelekeza wafuasi wake. (Mt. 28:20) Hata hivyo, alitabiri kwamba kungekuwa na mabadiliko wakati wa mavuno.
3 “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara?” Baada ya kuuliza swali hilo, Yesu Kristo alitoa mfano uliokuwa sehemu ya “ishara” aliyotaja kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3, 42-47) Yesu alionyesha kwamba mtumwa huyo mwaminifu angeendelea kuwaandalia watu wa Mungu chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa.” Kama vile Yesu alivyotumia kikundi cha wanaume—badala ya mtu mmoja—kuongoza katika karne ya kwanza, mtumwa mwaminifu ambaye Yesu anamtumia wakati wa mwisho wa mfumo wa mambo si mtu mmoja.
KUMTAMBUA “MTUMWA MWAMINIFU NA MWENYE BUSARA”
4 Yesu alimweka rasmi nani awalishe wafuasi wake? Kwa kufaa, angewatumia Wakristo watiwa-mafuta walio duniani. Biblia inawaita “ukuhani wa kifalme” ambao wameagizwa “‘[watangaze] kotekote sifa bora’ za Yule aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9; Mal. 2:7; Ufu. 12:17) Je, watiwa-mafuta wote walio duniani ndio wanaofanyiza mtumwa mwaminifu? Hapana. Yesu alipolisha kimuujiza umati wa wanaume 5,000, bila kuhesabu wanawake na watoto, aliwagawia wanafunzi wake chakula, kisha wanafunzi wakaugawia umati. (Mt. 14:19) Alitumia watu wachache kulisha wengi. Leo, anaandaa chakula cha kiroho kwa njia hiyohiyo.
5 Kwa hiyo, “msimamizi mwaminifu, mwenye busara,” ni kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta wanaohusika moja kwa moja katika kutayarisha na kusambaza chakula cha kiroho wakati wa kuwapo kwa Kristo. (Luka 12:42) Katika kipindi chote cha siku za mwisho, ndugu watiwa-mafuta ambao hufanyiza yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” wametumikia pamoja katika makao makuu. Leo, ndugu hao watiwa-mafuta ni Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.
6 Kristo anatumia baraza hilo kutangaza ujumbe kuhusu utimizo wa unabii wa Biblia na kutoa mwongozo kwa wakati unaofaa kuhusu kufuata kanuni za Biblia maishani. Chakula hicho cha kiroho hugawanywa kupitia makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10; Gal. 6:16) Katika nyakati za Biblia, mtumwa aliyeaminika, au msimamizi wa nyumba alisimamia shughuli za nyumbani. Vivyo hivyo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amepewa jukumu la kusimamia watu wa nyumba ya imani. Jukumu hilo linatia ndani kusimamia mali halisi, kazi ya kuhubiri, programu za makusanyiko, kuweka rasmi waangalizi mbalimbali katika tengenezo, na kazi ya kutayarisha machapisho ya Biblia, na yote hayo yanawanufaisha ‘watumishi wa nyumbani.’—Mt. 24:45.
7 Hivyo basi, ‘watumishi wa nyumbani’ ni nani? Kwa ufupi, ni wale wanaolishwa. Mwanzoni, wote walikuwa watiwa-mafuta. Baadaye, watumishi wa nyumbani wakaja kutia ndani umati mkubwa wa “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Vikundi vyote viwili vinafaidika na chakula cha kiroho kinachotayarishwa na mtumwa mwaminifu.
Ni muhimu sana tutii na kufuata maagizo ya wale wanaoongoza kwa sababu wanaendelea kutulinda ili tusipatwe na madhara ya kiroho
8 Wakati wa dhiki kuu, Yesu atakapokuja kutangaza na kutekeleza hukumu juu ya mfumo huu mwovu, atamweka rasmi mtumwa mwaminifu “asimamie mali zake zote.” (Mt. 24:46, 47) Wale wanaofanyiza mtumwa mwaminifu watapokea thawabu yao mbinguni. Kisha watiwa-mafuta wote 144,000, watatawala na Kristo mbinguni. Ingawa hakutakuwa tena na mtumwa mwaminifu na mwenye busara duniani, Yehova na Yesu watawaongoza raia waaminifu wa Ufalme wa Kimasihi hapa duniani kupitia wale watakaoteuliwa kuwa “wakuu.”—Zab. 45:16.
KWA NINI TUWAKUMBUKE “WALE WANAOONGOZA”?
9 Tuna sababu nyingi za kuwakumbuka “wale wanaoongoza” na kuonyesha kwamba tunawatumaini. Tunafaidikaje kwa kufanya hivyo? Mtume Paulo alisema: “Wanaendelea kuwalinda ninyi kama wale watakaotoa hesabu, ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa huzuni, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Ebr. 13:17) Ni muhimu sana tutii na kufuata maagizo ya wale wanaoongoza kwa sababu wanaendelea kutulinda ili tusipatwe na madhara ya kiroho.
10 Katika andiko la 1 Wakorintho 16:14, Paulo alisema: “Mambo yote mnayofanya yafanyeni kwa upendo.” Maamuzi yanayofanywa kwa niaba ya watu wa Mungu hutegemea sifa hii bora ya upendo. Kuhusiana na upendo, andiko la 1 Wakorintho 13:4-8 linasema: “Upendo ni wenye subira na fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” Kwa kuwa upendo ndio msingi wa maamuzi yote yanayofanywa ili kuwanufaisha watumishi wa Yehova, tuna hakika kwamba tutalindwa ikiwa tutatii mwongozo huo. Isitoshe, mwongozo huo ni uthibitisho wa upendo wa Yehova.
11 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, Yehova anatumia wanaume wasio wakamilifu kuwaongoza watu wake. Hata zamani Yehova alitumia wanadamu wasio wakamilifu kutimiza mapenzi yake. Noa alijenga safina na kuhubiri kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia siku hizo. (Mwa. 6:13, 14, 22; 2 Pet. 2:5) Musa aliteuliwa kuwaongoza watu wa Mungu kutoka Misri. (Kut. 3:10) Wanaume wasio wakamilifu waliongozwa na roho takatifu kuandika Biblia. (2 Tim. 3:16; 2 Pet. 1:21) Leo, ingawa Yehova anatumia wanaume wasio wakamilifu kuongoza kazi ya kuhubiri na kufundisha, hilo halifanyi tusilitumaini tengenezo la Mungu. Badala yake, tunaimarishwa kwa sababu tunajua kwamba bila msaada wa Yehova, tengenezo halingeweza kufanya mambo linayotimiza. Kupitia hali nyingi ngumu na mambo ambayo amejionea, mtumwa mwaminifu amedhihirisha kwamba roho ya Mungu inaongoza mambo. Sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova imepata baraka nyingi. Kwa hiyo, tunaiunga mkono kikamili na kuitumaini kabisa.
JINSI TUNAVYOIUNGA MKONO
12 Wale ambao wamepewa majukumu kutanikoni wanaonyesha kwamba wanaunga mkono wale wanaoongoza kwa kukubali na kutimiza kwa uaminifu majukumu yao. (Mdo. 20:28) Tukiwa watangazaji wa Ufalme, tunashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Ili tufaidike kikamili na chakula kingi cha kiroho kinachotayarishwa na mtumwa mwaminifu, tunajitayarisha na kuhudhuria mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Sisi hufaidika sana kwa kutiana moyo tunaposhirikiana kwa uhuru na ndugu zetu katika mikutano na makusanyiko hayo ya Kikristo.—Ebr. 10:24, 25.
13 Tunapotoa vitu vyetu vya kimwili ili kuunga mkono tengenezo, tunaonyesha kwamba tunalitumaini kabisa. (Met. 3:9, 10) Tunapoona kwamba ndugu zetu wana uhitaji wa kimwili, tunawasaidia bila kukawia. (Gal. 6:10; 1 Tim. 6:18) Tunafanya hivyo kwa roho ya upendo wa kindugu, tukiwa macho sikuzote ili kuonyesha kwamba tunamshukuru Yehova na tengenezo lake kwa sababu ya wema ambao ametuonyesha.—Yoh. 13:35.
14 Njia nyingine ambayo tunaonyesha kwamba tunaunga mkono tengenezo ni kwa kukubali maamuzi yanayofanywa. Hilo linatia ndani kufuata kwa unyenyekevu mwongozo wa ndugu waliowekwa rasmi, kama vile waangalizi wa mzunguko na wazee wa makutaniko. Ndugu hao ni miongoni mwa “wale wanaoongoza” ambao tunapaswa kuwatii na kuwanyenyekea. (Ebr. 13:7, 17) Ingawa huenda tusielewe kikamili sababu ya maamuzi fulani, tunajua kwamba tukiyaunga mkono, tutapata faida za kudumu. Matokeo ni kwamba Yehova hutubariki tunapotii Neno lake na tengenezo lake. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunamtii Bwana wetu, Yesu Kristo.
15 Naam, tuna sababu nyingi za kumtumaini mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Shetani, mungu wa mfumo huu wa mambo, anajitahidi juu chini kulivunjia heshima jina la Yehova na tengenezo lake. (2 Kor. 4:4) Usijiruhusu kamwe unaswe na mbinu zenye uovu za Shetani! (2 Kor. 2:11) Anajua kwamba ana “kipindi kifupi cha wakati” kabla hajatupwa ndani ya abiso, naye ameazimia kuwapotosha Wakristo wengi iwezekanavyo wamwasi Mungu. (Ufu. 12:12) Hata hivyo, kadiri Shetani anavyozidisha jitihada zake, na tuendelee kumkaribia Yehova zaidi. Acheni tuendelee kumtumaini Yehova na njia anayotumia kuwaelekeza watu wake leo. Tukifanya hivyo, tutakuwa na undugu wenye umoja.
-
-
Mipango na Usimamizi Katika KutanikoTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 4
Mipango na Usimamizi Katika Kutaniko
KATIKA barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, mtume Paulo alieleza kweli muhimu kumhusu Mungu. Aliandika hivi: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” Kisha, akieleza zaidi kuhusu mikutano ya kutaniko, alisema hivi: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 Kor. 14:33, 40.
2 Mwanzoni mwa barua hiyohiyo, mtume Paulo alionya kuhusu ugomvi uliokuwa katika kutaniko la Korintho. Paulo aliwahimiza akina ndugu ‘waseme kwa upatano’ na ‘waunganishwe kabisa katika akili ileile na njia ileile ya kufikiri.’ (1 Kor. 1:10, 11) Kisha aliwashauri kuhusu mambo mbalimbali yaliyokuwa yakivuruga umoja wa kutaniko. Akitumia mfano wa mwili wa mwanadamu, alionyesha uhitaji wa kuwa na umoja na ushirikiano. Aliwahimiza washiriki wote wa kutaniko la Kikristo, haidhuru walikuwa na majukumu gani, watunzane kwa upendo. (1 Kor. 12:12-26) Ushirikiano mzuri miongoni mwa wale walio kutanikoni unadhihirisha kwamba kutaniko lingekuwa limepangwa vizuri.
3 Hata hivyo, kutaniko la Kikristo lilipaswa kuwa na mpangilio gani? Ni nani ambaye angelipanga? Lingekuwa na muundo gani? Ni nani wangepewa majukumu? Biblia inajibu maswali hayo.—1 Kor. 4:6.
MPANGILIO WA KITHEOKRASI
4 Kutaniko la Kikristo lilianzishwa katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Tunajifunza nini kuhusu kutaniko hilo la karne ya kwanza? Lilipangwa na kusimamiwa kitheokrasi, yaani, lilikuwa chini ya utawala wa Mungu (Kigiriki, the·osʹ na kraʹtos). Maneno hayo mawili ya Kigiriki yanapatikana kwenye 1 Petro 5:10, 11. Masimulizi ya Biblia kuhusu mambo yaliyotendeka Yerusalemu karibu miaka 2,000 iliyopitia yanathibitisha wazi kwamba kutaniko hilo la Wakristo watiwa-mafuta lilianzishwa na Mungu. (Mdo. 2:1-47) Lilikuwa jengo lake, nyumba yake. (1 Kor. 3:9; Efe. 2:19) Leo, kutaniko la Kikristo linafuata utaratibu na mpangilio ambao ulianzishwa katika karne ya kwanza.
Leo, kutaniko la Kikristo linafuata utaratibu na mpangilio ambao ulianzishwa katika karne ya kwanza
5 Kutaniko la mapema lilianza na wanafunzi 120 hivi. Andiko la Yoeli 2:28, 29 lilitimizwa wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi hao. (Mdo. 2:16-18) Hata hivyo siku hiyohiyo, karibu watu wengine 3,000 walibatizwa katika maji na kujiunga na kutaniko hilo la watiwa-mafuta. Walikuwa wamekubali ujumbe kumhusu Kristo nao “wakaendelea kujitoa kwa bidii kwa fundisho la mitume.” Kisha, “Yehova akaendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa.”—Mdo. 2:41, 42, 47.
6 Kulikuwa na ongezeko kubwa katika kutaniko la Yerusalemu hivi kwamba kuhani mkuu wa Wayahudi akalalamika kuwa wanafunzi walijaza Yerusalemu fundisho lao. Makuhani wengi Wayahudi walikuwa miongoni mwa wanafunzi wapya waliojiunga na kutaniko huko Yerusalemu.—Mdo. 5:27, 28; 6:7.
7 Yesu alisema: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Na hivyo ndivyo ilivyokuwa, mateso makali yalipotokea Yerusalemu baada ya kifo cha Stefano, wanafunzi waliokuwa wakiishi huko walitawanyika katika eneo lote la Yudea na Samaria. Lakini popote walipoenda, waliendelea kutangaza habari njema na kuwafundisha watu wengi zaidi, kutia ndani baadhi ya Wasamaria. (Mdo. 8:1-13) Baadaye, habari njema ilihubiriwa kwa watu wa mataifa ambao hawakuwa wametahiriwa, yaani, wale ambao hawakuwa Wayahudi. (Mdo. 10:1-48) Kwa sababu ya kazi hiyo kubwa ya kuhubiri watu wengi walikubali kuwa wanafunzi na makutaniko mapya yakaanzishwa nje ya Yerusalemu.—Mdo. 11:19-21; 14:21-23.
8 Ni mipango gani iliyofanywa ili kuhakikisha kwamba kila kutaniko jipya lililoanzishwa lilipangwa na kusimamiwa kitheokrasi? Kupitia mwongozo wa roho ya Mungu mpango wa kuwa na wachungaji wa kutunza kundi ulianzishwa. Katika safari yao ya kwanza ya umishonari, Paulo na Barnaba waliwaweka rasmi wazee kwenye makutaniko waliyoyatembelea. (Mdo. 14:23) Mwandishi wa Biblia, Luka, anasimulia kuhusu mkutano ambao mtume Paulo alifanya pamoja na wazee wa kutaniko la Efeso. Paulo aliwaambia: “Jiangalieni wenyewe na kundi lote, ambalo kati yake roho takatifu imewaweka ninyi rasmi muwe waangalizi, mlichunge kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:17, 28) Walistahili kuwa wazee kwa sababu walitimiza matakwa ya Kimaandiko. (1 Tim. 3:1-7) Tito, mfanyakazi mwenzi wa Paulo alipewa mamlaka ya kuwaweka rasmi wazee katika makutaniko ya Krete.—Tito 1:5.
9 Makutaniko mengi zaidi yalipoendelea kuanzishwa, mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu waliendelea kutumikia wakiwa waangalizi wakuu wa kutaniko la Kikristo la duniani pote katika karne ya kwanza. Walitumikia wakiwa baraza linaloongoza.
10 Alipoliandikia kutaniko la Efeso, mtume Paulo alieleza kwamba kutaniko la Kikristo lingedumisha umoja na kuendelea kujitiisha chini ya ukichwa wa Yesu Kristo ikiwa tu lingetii mwongozo wa roho ya Mungu. Mtume huyo aliwahimiza Wakristo wa Efeso wasitawishe unyenyekevu na kudumisha “roho ya umoja” wakishirikiana kwa amani na wote walio kutanikoni. (Efe. 4:1-6) Kisha akanukuu Zaburi 68:18 na kuonyesha jinsi ambavyo Yehova aliandaa wanaume wenye sifa za kiroho zilizowastahilisha kushughulikia mahitaji ya kutaniko wakiwa mitume, manabii, waeneza-injili, wachungaji, na walimu. Wanaume hao, wakiwa zawadi kutoka kwa Yehova, wangeimarisha kutaniko zima lifikie ukomavu wa kiroho na kumpendeza Mungu.—Efe. 4:7-16.
MAKUTANIKO YANAFUATA MFANO WA MITUME
11 Leo, utaratibu kama huo wa tengenezo unafuatwa katika makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova. Makutaniko hayo yote hufanyiza kutaniko la ulimwenguni pote ambalo kiini chake ni watiwa-mafuta. (Zek. 8:23) Yesu Kristo amefanya hilo liwezekane. Kama alivyoahidi, ameendelea kuwa pamoja na wanafunzi wake watiwa-mafuta “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Watu wanaojiunga na kutaniko linalopanuka wanakubali habari njema ya Mungu, wanajiweka wakfu kwa Yehova bila masharti, na kisha hubatizwa na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. (Mt. 28:19, 20; Marko 1:14; Mdo. 2:41) Wanamtambua “mchungaji mwema,” Yesu Kristo, kuwa ndiye Kichwa cha kundi zima, ambalo hufanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta pamoja na “kondoo wengine.” (Yoh. 10:14, 16; Efe. 1:22, 23) Walio katika ‘kundi hilo moja’ hudumisha umoja kwa kutambua na kuwa washikamanifu kwa ukichwa wa Kristo na kwa kujitiisha chini ya njia anayoitumia, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ambaye Kristo amemweka rasmi. Acheni tuendelee kuitegemea na kuitumaini kabisa njia hiyo.—Mt. 24:45.
KAZI YA MASHIRIKA YA KIDINI
12 Mashirika kadhaa yameanzishwa ili kusaidia kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa na kufanikisha kuhubiriwa kwa habari njema ya Ufalme kabla ya mwisho kuja. Mashirika hayo yanatambulika kisheria katika nchi mbalimbali na yanafanya kazi kwa ushirikiano. Yanarahisisha kazi ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote.
OFISI ZA TAWI
13 Ofisi ya tawi inapoanzishwa, Halmashauri ya Tawi yenye wazee watatu au zaidi huwekwa rasmi ili kusimamia kazi katika nchi moja au zaidi ambazo zinasimamiwa na tawi hilo. Ndugu mmoja wa halmashauri hiyo hutumikia akiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi.
14 Makutaniko yaliyo chini ya kila ofisi ya tawi yamepangwa katika mizunguko. Mizunguko hiyo ina ukubwa mbalimbali, ikitegemea eneo, lugha na vilevile idadi ya makutaniko yaliyo chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi. Mwangalizi wa mzunguko huwekwa rasmi ili atembelee makutaniko yote katika mzunguko. Ofisi ya tawi humpa mwangalizi wa mzunguko mwongozo wa jinsi ya kushughulikia majukumu yake.
15 Makutaniko hukubaliana na mipango ya tengenezo ambayo hutolewa kwa manufaa ya wote. Wanawaunga mkono wazee waliowekwa rasmi kusimamia kazi katika ofisi za tawi, mizunguko, na makutanikoni. Wanategemea chakula cha kiroho kinachotolewa kwa wakati unaofaa na mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Naye mtumwa mwaminifu leo, hujitiisha kikamili chini ya ukichwa wa Kristo, anashikamana na kanuni za Biblia, na kufuata mwelekezo wa roho takatifu. Sisi sote tunapofanya kazi kwa umoja, tunapata matokeo sawa na yale waliyopata Wakristo wa karne ya kwanza: “Kwa kweli makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Mdo. 16:5.
-
-
Waangalizi Wanaochunga KundiTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 5
Waangalizi Wanaochunga Kundi
WAKATI wa huduma yake duniani, Yesu alithibitika kuwa “mchungaji mwema.” (Yoh. 10:11) Alipoona umati uliokuwa ukimfuata, ‘aliwasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mt. 9:36) Petro na mitume wengine waliona jinsi alivyowapenda na kuwajali watu. Yesu alikuwa tofauti sana na wachungaji wa uwongo wa Israeli waliolipuuza kundi hivi kwamba kondoo wakatawanyika na kuwa na njaa ya kiroho! (Eze. 34:7, 8) Mfano mzuri wa Yesu akiwa mwalimu na jinsi alivyowajali kondoo, hata akafa kwa ajili yao, uliwafundisha mitume wake jinsi ya kuwasaidia wale wenye imani wamrudie Yehova, “mchungaji na mwangalizi wa nafsi” zao.—1 Pet. 2:25.
c2 Pindi moja alipokuwa akizungumza na Petro, Yesu alikazia umuhimu wa kulisha na kuchunga kondoo. (Yoh. 21:15-17) Bila shaka Petro alichochewa sana na jambo hilo hivi kwamba baadaye aliwahimiza hivi wazee katika kutaniko la mapema la Kikristo: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wenu, mkiwa waangalizi, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari mbele za Mungu; si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; si kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:1-3) Maneno ya Petro yanawahusu waangalizi wa makutaniko leo. Wazee wanaiga mfano wa Yesu kwa kutumikia kwa hiari na kwa hamu wakiweka mfano mzuri kwa kundi na kuongoza katika utumishi wa Yehova.—Ebr. 13:7.
Wazee wanaiga mfano wa Yesu kwa kutumikia kwa hiari na kwa hamu wakiweka mfano mzuri kwa kundi na kuongoza katika utumishi wa Yehova
3 Tunashukuru kwamba tuna waangalizi kutanikoni ambao wamewekwa rasmi na roho takatifu. Tunafaidika sana kutokana na utunzaji wao. Kwa mfano, waangalizi huwaimarisha na kuhangaikia mahitaji ya wote kutanikoni. Kila juma, wanaongoza mikutano ya kutaniko, ambapo imani ya wote huimarishwa. (Rom. 12:8) Jitihada zao za kulilinda kundi lisipate madhara, kama vile watu waovu, zinachangia usalama wetu. (Isa. 32:2; Tito 1:9-11) Wakiwa mstari wa mbele katika huduma ya shambani wanatuchochea pia tuhubiri habari njema kwa bidii na kwa ukawaida kila mwezi. (Ebr. 13:15-17) Yehova amefanya mipango ya kulijenga kutaniko kupitia ‘wanaume aliotoa kuwa zawadi.’—Efe. 4:8, 11, 12.
SIFA ZA KUSTAHILI KUWA MWANGALIZI
4 Ili kuhakikisha kwamba kutaniko linatunzwa inavyofaa, wanaume wanaowekwa rasmi kuwa waangalizi wanapaswa kutimiza matakwa yanayotajwa katika Neno la Mungu. Wanapotimiza sifa hizo, ndipo tu inapoweza kusemwa kwamba wamewekwa rasmi na roho takatifu. (Mdo. 20:28) Bila shaka, viwango vya Kimaandiko kwa ajili ya waangalizi Wakristo ni vya juu, kwa sababu kuwa mwangalizi ni jukumu zito. Hata hivyo, viwango hivyo si vya juu sana hivi kwamba haviwezi kufikiwa na wanaume Wakristo ambao wanampenda Yehova kikweli na walio tayari kutumiwa naye. Watu wote wanapaswa kuona wazi kwamba waangalizi ni watu wanaofuata kanuni za Biblia katika maisha yao ya kila siku.
Ili kuhakikisha kwamba kutaniko linatunzwa inavyofaa, wanaume wanaowekwa rasmi kuwa waangalizi wanapaswa kutimiza matakwa yanayotajwa katika Neno la Mungu
5 Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo na barua yake kwa Tito, mtume Paulo alitaja matakwa ya msingi ya Kimaandiko ambayo waangalizi wanapaswa kutimiza. Tunasoma hivi katika 1 Timotheo 3:1-7: “Ikiwa mwanamume anajitahidi kuwa mwangalizi, anatamani kazi njema. Mwangalizi anapaswa kuwa mtu asiyelaumika, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi katika mazoea, mwenye utimamu wa akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji wageni, mwenye uwezo wa kufundisha, si mlevi, si mkatili, bali mwenye usawaziko, si mgomvi, si mtu anayependa pesa, mwanamume anayeisimamia nyumba yake vizuri, mwenye watoto wanaojitiisha na kuchukua mambo kwa uzito (kwa maana ikiwa mtu hajui jinsi ya kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kutaniko la Mungu?), si mtu aliyegeuka hivi karibuni, ili asije akawa na kiburi na kuanguka katika hukumu aliyohukumiwa Ibilisi. Pia, anapaswa kushuhudiwa vema na watu walio nje ili asianguke katika shutuma na mtego wa Ibilisi.”
6 Paulo alimwandikia hivi Tito: “Nilikuacha Krete ili urekebishe mambo yaliyokuwa na kasoro na kuweka rasmi wazee katika jiji moja baada ya lingine, kama nilivyokuagiza: ikiwa kuna mwanamume asiye na shtaka, mume wa mke mmoja, mwenye watoto wanaoamini ambao hawana mashtaka ya kuwa wapotovu au waasi. Mwangalizi ni msimamizi aliyechaguliwa na Mungu, hivyo hapaswi kuwa na shtaka, asiwe mshupavu, asiwe mwenye kukasirika upesi, asiwe mlevi, asiwe mkatili, asiwe na pupa ya mapato yasiyo ya haki, bali awe mkaribishaji wageni, anayependa mema, mwenye utimamu wa akili, mwadilifu, mshikamanifu, anayejidhibiti, anayefuata kikamili neno la uaminifu katika ustadi wake wa kufundisha, ili aweze kutia moyo kwa fundisho lenye manufaa na pia kuwakaripia wale ambao hulipinga.”—Tito 1:5-9.
7 Ingawa huenda matakwa ya Kimaandiko ya kuwa mwangalizi yakaonekana kuwa magumu mwanzoni, wanaume Wakristo hawana sababu ya kutojitahidi kufikia pendeleo hilo. Waangalizi wanapoonyesha sifa nzuri za Kikristo, wanawachochea wengine kutanikoni wafanye vivyo hivyo. Paulo aliandika kwamba ‘wanaume wakiwa zawadi’ wametolewa “ili kuwarekebisha watakatifu, kwa ajili ya kutimiza huduma, na kuujenga mwili wa Kristo, mpaka sote tuwe na umoja katika imani na tuwe na ujuzi sahihi kumhusu Mwana wa Mungu, na kuwa mtu aliyekomaa kabisa, na kufikia kiwango cha kimo kamili cha Kristo.”—Efe. 4:8, 12, 13.
8 Waangalizi hawapaswi kuwa wavulana tu au watu waliogeuka hivi karibuni. Badala yake, wanapaswa kuwa watu wenye uzoefu katika maisha ya Kikristo, wenye ujuzi mwingi wa Biblia, wanaoelewa vizuri Maandiko, na wanaolipenda sana kutaniko. Wana ujasiri wa kuongea na kuwarekebisha wakosaji, na hivyo kuwalinda kondoo dhidi ya mtu yeyote anayetaka kuwatumia vibaya. (Isa. 32:2) Waangalizi wanapaswa kutambuliwa kwa urahisi na ndugu na dada kutanikoni kuwa wanaume wakomavu kiroho, wanaolipenda na kulijali kikweli kundi la Mungu.
9 Wale ambao wana sifa za kustahili kuwa waangalizi wanatenda kwa hekima katika maisha yao. Ikiwa amefunga ndoa, mwangalizi anapaswa kuishi kupatana na viwango vya Kikristo kuhusu ndoa, yaani, awe mume wa mke mmoja na anayeisimamia nyumba yake vizuri. Ikiwa mwangalizi ana watoto wanaoamini ambao wanajitiisha na kuchukua mambo kwa uzito na hawana mashtaka ya kuwa wapotovu au waasi, ndugu na dada kutanikoni wanaweza kumtumaini na kumwomba ushauri kuhusu familia na maisha ya Kikristo. Pia, mwangalizi ni mtu asiyelaumika na hapaswi kuwa na shtaka na awe mwenye kushuhudiwa vema hata na watu walio nje. Hana mashtaka yoyote kwa sababu ya mwenendo usiofaa ambao unaweza kuharibu sifa nzuri ya kutaniko. Si mtu ambaye amekaripiwa hivi karibuni kwa sababu ya kosa zito. Wengine kutanikoni wanachochewa kuiga mfano wake mzuri na wana hakika kwamba mwangalizi huyo atahangaikia hali yao ya kiroho.—1 Kor. 11:1; 16:15, 16.
10 Wanaume hao wanaostahili wanalitumikia kutaniko la Kikristo kama walivyofanya wale wanaume wazee wa Israeli waliotajwa kuwa “wenye hekima na busara na wenye uzoefu.” (Kum. 1:13) Haimaanishi kwamba wazee Wakristo ni wakamilifu, lakini wanajulikana kutanikoni na katika jamii kuwa wanaume waaminifu na wenye kumwogopa Mungu ambao maisha yao yameonyesha kwamba wamekuwa wakiishi kupatana na kanuni za Mungu. Kwa sababu ya kuwa wasiolaumika, wana uhuru wa kusema kutanikoni.—Rom. 3:23.
11 Wanaume wanaostahili kuwa waangalizi wanaonyesha kiasi katika mazoea na wanaposhughulika na wengine. Hawapaswi kuwa washupavu. Badala yake, wanapaswa kuwa na usawaziko na wanaojidhibiti. Wanapaswa kuwa na kiasi katika kula, kunywa, tafrija, mambo wanayopenda, na burudani. Wanakunywa pombe kwa kiasi ili wasishtakiwe kwa madai ya ulevi au wasiwe na shtaka la kuwa walevi. Mtu ambaye hisi zake zimepumbazwa na pombe hushindwa kujidhibiti, naye hawezi kushughulikia mahitaji ya kiroho ya kutaniko.
12 Ili kusimamia kutaniko inafaa mtu awe mwenye utaratibu. Tabia yake njema inaonekana wazi katika mwonekano wake, nyumbani kwake, na katika shughuli zake za kila siku. Mtu wa namna hiyo huepuka kuahirisha mambo; anaona kinachohitajiwa na kuchukua hatua mara moja. Anashikamana na kanuni za Biblia.
13 Mwangalizi anapaswa kuwa na usawaziko. Anapaswa kuwa na uwezo wa kufanya kazi kwa umoja na kushirikiana na wengine katika baraza la wazee. Anapaswa kuwa na maoni yanayofaa kujihusu na hapaswi kudai mengi kutoka kwa wengine. Mwangalizi mwenye usawaziko hashikilii sana maoni yake, wala haoni maoni yake kuwa bora kuliko ya wazee wenzake. Wengine wanaweza kuwa na sifa au uwezo fulani ambao yeye hana. Usawaziko wake hutokana na kufanya maamuzi yanayotegemea Maandiko na kujitahidi kumwiga Yesu Kristo. (Flp. 2:2-8) Mzee si mgomvi au mkatili, bali anawaheshimu wengine, akiwaona kuwa bora kuliko yeye. Si mshupavu, akisisitiza kila mara kwamba njia yake au maoni yake yanapaswa kukubalika. Hapaswi kuwa mwenye kukasirika upesi, bali anapaswa kushughulika na wengine kwa amani.
14 Pia, yule anayestahili kutumikia akiwa mwangalizi kutanikoni anapaswa kuwa mwenye utimamu wa akili. Hilo linamaanisha awe mtulivu, na asiyefanya uamuzi haraka-haraka. Anazijua vizuri kanuni za Yehova na jinsi zinavyotumika. Mtu mwenye utimamu wa akili yuko tayari kukubali ushauri na mwongozo. Yeye si mnafiki.
15 Paulo alimkumbusha Tito kwamba mwangalizi ni mtu anayependa mema. Anapaswa kuwa mwadilifu na mshikamanifu. Sifa hizo zitaonekana anaposhughulika na wengine na anapotetea kwa uthabiti yale yaliyo sawa na yaliyo mema. Hayumbi-yumbi katika ujitoaji wake kwa Yehova naye daima hufuata kanuni za uadilifu. Anaweza kutunza siri. Pia, ni mkaribishaji wageni, yuko tayari kujitolea yeye mwenyewe na mali yake ili kuwanufaisha wengine.—Mdo. 20:33-35.
16 Ili awe mwangalizi mzuri, anapaswa kuwa mwenye uwezo wa kufundisha. Kulingana na maneno ya Paulo kwa Tito, mwangalizi anapaswa kuwa “anayefuata kikamili neno la uaminifu katika ustadi wake wa kufundisha, ili aweze kutia moyo kwa fundisho lenye manufaa na pia kuwakaripia wale ambao hulipinga.” (Tito 1:9) Ana uwezo wa kujadiliana, kuthibitisha, kushinda vipingamizi, na kutumia Maandiko kwa njia itakayowasadikisha wengine na kuimarisha imani yao. Mwangalizi anatumia uwezo huo wa kufundisha katika nyakati zinazofaa na katika nyakati ngumu. (2 Tim. 4:2) Anahitaji kuwa na subira ili aweze kumkaripia kwa upole mtu aliyekosea au kumsadikisha mtu mwenye shaka na kumchochea afanye mambo mazuri kwa imani. Kuwa na uwezo wa kufundisha watu wengi au mtu mmoja-mmoja kunaonyesha kwamba mwangalizi anatimiza sifa hiyo muhimu.
17 Ni muhimu sana wazee wawe na bidii katika huduma. Inapaswa kuonekana wazi pia kwamba wanajitahidi kumwiga Yesu, ambaye aliona kuhubiri habari njema kuwa jambo kuu maishani mwake. Yesu aliwapenda wanafunzi wake, akiwasaidia wawe waeneza-injili wenye matokeo. (Marko 1:38; Luka 8:1) Wazee wanaposhiriki kwa bidii katika huduma licha ya kuwa na shughuli nyingi, hilo huchochea kutaniko zima liwe na bidii kama hiyo. Wazee wanapohubiri na familia zao na ndugu na dada wengine kutanikoni, wote ‘hutiwa moyo.’—Rom. 1:11, 12.
18 Huenda ikaonekana kwamba waangalizi wanatazamiwa kutimiza matakwa mengi sana. Bila shaka hakuna mwangalizi anayeweza kutimiza kikamili viwango hivyo vya juu vilivyo katika Biblia, lakini hakuna mzee yeyote kutanikoni anayepaswa kupungukiwa sana na mojawapo ya sifa hizo hivi kwamba upungufu huo uonwe kuwa udhaifu mkubwa. Baadhi ya wazee wanaweza kuonyesha zaidi sifa fulani, na wengine waonyeshe zaidi sifa tofauti. Matokeo ni kwamba baraza la wazee litakuwa na sifa zote nzuri zinazohitajiwa ili kulisimamia kutaniko la Mungu inavyofaa.
19 Wazee, wakiwa baraza, wanapowapendekeza wanaume wawekwe rasmi kuwa waangalizi, itafaa wakumbuke maneno haya ya mtume Paulo: “Ninamwambia kila mtu kati yenu asijifikirie mwenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri, bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama Mungu alivyompa kipimo cha imani.” (Rom. 12:3) Kila mzee anapaswa kujiona kuwa mdogo kati ya wote. Hakuna anayepaswa kuwa “mwadilifu kupita kiasi” wakati wa kuchunguza sifa za kustahili za mwingine. (Mhu. 7:16) Kuyajua vizuri matakwa ya Maandiko yanayohusu waangalizi, kutasaidia baraza la wazee kuamua ikiwa ndugu anayefikiriwa anafikia viwango hivyo kwa kadiri inayofaa. Wazee wanapompendekeza ndugu fulani, watafanya hivyo bila ubaguzi wala unafiki wakikumbuka kwamba ndugu huyo si mkamilifu. Watampendekeza kwa njia inayoonyesha kwamba wanaheshimu viwango vya Yehova vya uadilifu na kwa manufaa ya kutaniko. Watasali na kufuata mwelekezo wa roho takatifu ya Mungu wanapochanganua kila pendekezo. Hilo ni mojawapo ya majukumu mazito waliyo nayo, na wanapolitimiza, wanapaswa kutii himizo hili la Paulo: “Usiharakishe kamwe kuweka mikono yako juu ya mwanamume yeyote.”—1 Tim. 5:21, 22.
TUNDA LA ROHO
20 Maisha ya wanaume wenye sifa za kiroho hudhihirisha wazi kwamba wanaongozwa na roho takatifu, na wanaonyesha sifa za tunda la roho maishani. Paulo anaorodhesha sifa tisa za tunda la roho, nazo ni “upendo, shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Waangalizi hao huwaburudisha akina ndugu na husaidia kuliunganisha kutaniko ili litoe utumishi mtakatifu. Mwenendo wao na matokeo mazuri ya kazi zao huonyesha kwamba wamewekwa rasmi na roho takatifu.—Mdo. 20:28.
WANAUME WANAOENDELEZA UMOJA
21 Ni muhimu wazee wafanye kazi pamoja ili kuendeleza umoja kutanikoni. Licha ya kwamba wana utu tofauti, wazee hudumisha umoja wa baraza kwa kuwasikiliza wengine kwa heshima, hata ingawa huenda wasikubaliane katika kila jambo wanalojadili. Maadamu hakuna kanuni ya Biblia inayovunjwa, kila mzee anapaswa kuwa tayari kukubali maoni ya wengine na kuunga mkono uamuzi wa mwisho wa baraza la wazee. Kuwa tayari kukubali maoni ya wengine huonyesha kwamba mtu anaongozwa na “hekima inayotoka juu,” ambayo ni “yenye kufanya amani, yenye usawaziko.” (Yak. 3:17, 18) Hakuna mzee anayepaswa kufikiri kwamba yeye ni bora kuliko wengine, wala hakuna mzee anayepaswa kuwatawala wengine. Baraza la wazee linaposhirikiana kwa faida ya kutaniko, kwa kweli linashirikiana na Yehova.—1 Kor., sura ya 12; Kol. 2:19.
KUJITAHIDI KUWA MWANGALIZI
22 Wanaume wakomavu kiroho wanapaswa kutamani kuwa waangalizi. (1 Tim. 3:1) Hata hivyo, mzee anahitaji kuwa tayari kufanya kazi na kujidhabihu. Anapaswa kuwa tayari kushughulikia mahitaji ya ndugu na dada, na kuwatunza kiroho. Ili mtu awe mwangalizi ni lazima ajitahidi kutimiza viwango vilivyowekwa katika Maandiko.
HUENDA HALI ZIKABADILIKA
23 Ndugu ambaye ametumikia kwa uaminifu kwa muda mrefu anaweza kuwa mgonjwa au kudhoofika kimwili. Labda kwa sababu ya umri kusonga, huenda asiweze kutimiza majukumu ya mwangalizi. Hata hivyo, bado anapaswa kuheshimiwa na kuonwa kuwa mzee maadamu amewekwa rasmi. Hahitaji kuacha kuwa mzee kwa sababu ya hali au udhaifu wake. Bado anastahili kuonyeshwa heshima mara mbili kama wazee wengine wanaofanya kazi kwa bidii na kulichunga kundi kwa kadiri ya uwezo wao.
24 Hata hivyo ndugu akihisi kwamba ingefaa aache uangalizi kwa sababu hali zake zimebadilika naye hawezi kutumikia kikamili, anaweza kuamua kuacha. (1 Pet. 5:2) Bado anapaswa kuheshimiwa. Anaweza kufanya mengi kwa manufaa ya kutaniko, hata ingawa hana migawo na majukumu ya wazee.
MAJUKUMU MBALIMBALI KUTANIKONI
25 Wazee wana majukumu mbalimbali kutanikoni. Kuna mratibu wa baraza la wazee, mwandishi, mwangalizi wa utumishi, kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, na mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha. Wazee wengi hutumikia wakiwa waangalizi wa vikundi. Wazee walio na majukumu hayo hutumikia kwa kuendelea. Bila shaka, ndugu aliye na mojawapo ya majukumu hayo akihama, au ikiwa hawezi kutimiza kwa sababu ya afya, au ikiwa hastahili kwa sababu ya kutotimiza matakwa ya Kimaandiko, mzee mwingine huchaguliwa kushughulikia mgawo huo. Katika makutaniko yenye waangalizi wachache, huenda mzee mmoja akashughulikia migawo kadhaa mpaka ndugu wengine watakapostahili kuwa wazee.
26 Mratibu wa baraza la wazee huwa mwenyekiti katika mikutano ya baraza la wazee. Hivyo, anashirikiana kwa unyenyekevu na wazee wengine kulitunza kundi la Mungu. (Rom. 12:10; 1 Pet. 5:2, 3) Anapaswa kuwa mwenye utaratibu na mwenye uwezo wa kusimamia mambo kwa bidii.—Rom. 12:8.
27 Mwandishi hutunza rekodi za kutaniko na kuwajulisha wazee kuhusu barua au mawasiliano mengine muhimu. Ikiwa kuna uhitaji, mzee mwingine au mtumishi wa huduma anayestahili anaweza kupewa mgawo wa kumsaidia.
28 Mipango ya utumishi wa shambani na mambo mengine yanayohusiana na utumishi husimamiwa na mwangalizi wa utumishi. Yeye hupanga kuvitembelea kwa ukawaida vikundi vyote vya utumishi. Katika mwisho juma mmoja kwa mwezi yeye hutembelea kikundi tofauti. Katika makutaniko ambayo yana vikundi vichache vya utumishi, anaweza kutembelea kila kikundi mara mbili kwa mwaka. Wakati wa ziara yake, ataongoza mikutano ya utumishi wa shambani, atahubiri pamoja na kikundi, na kuwasaidia wahubiri katika ziara za kurudia na mafunzo yao ya Biblia.
WAANGALIZI WA VIKUNDI
29 Mojawapo ya mapendeleo ya pekee katika kutaniko ni kuwa mwangalizi wa kikundi. Majukumu yake yanatia ndani (1) kupendezwa na hali ya kiroho ya kila mtu katika kikundi chake cha utumishi wa shambani; (2) kumsaidia kila mmoja katika kikundi ashiriki kwa ukawaida, apate matokeo mazuri, na awe na shangwe katika huduma; na (3) kuwasaidia na kuwazoeza watumishi wa huduma katika kikundi chake ili wafanye bidii na kustahili kukabidhiwa majukumu kutanikoni. Baraza la wazee huchagua ndugu wanaostahili zaidi kutimiza mgawo huo.
30 Kwa sababu ya majukumu yanayohusika, ikiwezekana, waangalizi wa vikundi wanapaswa kuwa wazee. Au mtumishi wa huduma mwenye uwezo anaweza kutumikia hadi mzee atakapochukua mahali pake. Mtumishi wa huduma anayetumikia katika pendeleo hilo anaitwa mtumishi wa kikundi, kwa kuwa yeye si mwangalizi kutanikoni. Badala yake, anatimiza majukumu yake chini ya mwelekezo wa wazee.
31 Wajibu muhimu wa mwangalizi wa kikundi ni kuongoza katika huduma ya shambani. Ndugu na dada katika kikundi watachochewa ikiwa atahubiri kwa ukawaida, kwa bidii, na kwa shauku. Kwa kuwa wahubiri wanathamini na kutiwa moyo kutokana na msaada wanaopata wakiwa pamoja na ndugu zao, ingekuwa vyema kupanga ratiba ya mahubiri ya kikundi inayowafaa wengi. (Luka 10:1-16) Mwangalizi wa kikundi anahitaji kuhakikisha kwamba siku zote kuna eneo la kutosha la kuhubiri. Ataongoza mkutano wa utumishi wa shambani na kuwapanga wahubiri kwa ajili ya mahubiri ya siku hiyo. Ikiwa hatakuwepo, anapaswa kupanga mzee mwingine, mtumishi wa huduma au, ikiwa wote hawatakuwepo, apange mhubiri anayestahili atimize majukumu hayo ili wahubiri wapate mwongozo wanaohitaji.
32 Mwangalizi wa kikundi anapaswa kupanga mapema kwa ajili ya ziara ya mwangalizi wa utumishi, akiwataarifu wale walio katika kikundi chake kuhusu ziara hiyo na kuwasaidia waitarajie kwa hamu. Wote katika kikundi wakijulishwa kikamili kuhusu mpango huo, watauunga mkono kwa moyo wote.
33 Kuna kusudi zuri la kuwa na watu wachache kwenye kikundi. Hilo humwezesha mwangalizi wa kikundi awafahamu vizuri wote katika kikundi. Akiwa mchungaji mwenye upendo, yeye humpenda sana kila mhubiri. Anajitahidi kumsaidia na kumtia moyo kila mmoja ahubiri na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Pia, anajitahidi sana kufanya yote awezayo ili kumsaidia kila mmoja abaki imara kiroho. Wagonjwa na wale walioshuka moyo watanufaika kwa kutembelewa. Dokezo au ushauri mzuri unaweza kuwachochea wengine wajitahidi kufikia mapendeleo zaidi kutanikoni na hivyo kuwa msaada mkubwa kwa ndugu zao. Kwa kawaida mwangalizi wa kikundi atajitahidi kuwasaidia wale walio katika kikundi chake. Hata hivyo, akiwa mzee na mchungaji, anawahangaikia kwa upendo wahubiri wote kutanikoni na yuko tayari kumsaidia yeyote mwenye uhitaji.—Mdo. 20:17, 28.
34 Jukumu mojawapo la mwangalizi wa kikundi ni kusaidia kukusanya ripoti za utumishi wa shambani katika kikundi chake. Kisha anampatia mwandishi ripoti hizo. Kila mhubiri anaweza kumsaidia mwangalizi wa kikundi kwa kutoa ripoti yake ya utumishi kwa wakati. Wahubiri wanaweza kufanya hivyo kwa kumpa moja kwa moja mwangalizi wa kikundi ripoti zao ifikapo mwisho wa kila mwezi au kwa kuweka kwenye sanduku la ripoti za utumishi wa shambani lililo kwenye Jumba la Ufalme.
HALMASHAURI YA UTUMISHI YA KUTANIKO
35 Kuna kazi fulani zinazofanywa na Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, ambayo imefanyizwa na mratibu wa baraza la wazee, mwandishi, na mwangalizi wa utumishi. Kwa mfano, halmashauri ya utumishi huidhinisha matumizi ya Jumba la Ufalme kwa ajili hotuba ya ndoa, ya maziko, na huwapangia wahubiri vikundi vya utumishi. Pia huidhinisha maombi ya utumishi wa painia wa kawaida na msaidizi na maombi ya utumishi mwingine. Halmashauri ya utumishi hufanya kazi chini ya mwelekezo wa baraza la wazee.
36 Majukumu hususa ya ndugu hao, pamoja na kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha, na ndugu wengine katika baraza la wazee, hutolewa na ofisi ya tawi.
37 Katika kila kutaniko baraza la wazee hukutana pindi kwa pindi ili kuzungumzia mambo yanayohusiana na maendeleo ya kiroho ya kutaniko. Mbali na mkutano wa wazee unaofanywa wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko, wazee wa kutaniko hufanya mkutano mwingine miezi mitatu hivi baada ya mwangalizi kuwatembelea. Bila shaka, wazee wanaweza kufanya mkutano wakati wowote kunapokuwa na uhitaji.
JINYENYEKEZENI
38 Waangalizi ni wanadamu wasio wakamilifu; hata hivyo kila mtu kutanikoni anahimizwa ajinyenyekeze kwao kwa sababu ni mpango wa Yehova. Atawatoza waangalizi hesabu kwa sababu ya matendo yao. Wanamwakilisha Yehova na utawala wake wa kitheokrasi. Andiko la Waebrania 13:17 linasema: “Watiini wale wanaoongoza kati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuwalinda ninyi kama wale watakaotoa hesabu, ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa huzuni, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” Kwa kuwa Yehova hutumia roho takatifu kumweka rasmi ndugu fulani, basi Yehova ataitumia roho takatifu hiyohiyo kumwondoa ndugu fulani asitumikie akiwa mwangalizi ikiwa haonyeshi sifa za tunda la roho na maisha yake hayapatani na matakwa ya Maandiko.
39 Je, hatuthamini kutoka moyoni bidii na mfano mzuri wa waangalizi wa kutaniko? Alipoliandikia kutaniko la Thesalonike, Paulo aliwahimiza hivi: “Tunawaomba, akina ndugu, waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na wanaowasimamia katika Bwana na kuwaonya ninyi; na mwafikirie kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.” (1 The. 5:12, 13) Bidii nyingi ya waangalizi wa kutaniko hurahisisha utumishi wetu kwa Mungu na kutuletea shangwe zaidi. Pia, katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, Paulo alitaja kuhusu mtazamo ambao ndugu na dada kutanikoni wanapaswa kusitawisha kuelekea waangalizi, aliposema: “Wazee wanaosimamia kwa njia nzuri wanastahili heshima mara mbili, hasa wale wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha.”—1 Tim. 5:17.
MAJUKUMU MENGINE KATIKA TENGENEZO
40 Nyakati nyingine, wazee fulani huteuliwa ili watumikie wakiwa washiriki wa Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa. Wengine ni washiriki wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali nao hutembelea hospitali na madaktari ili kuwahimiza waendelee kuwatibu Mashahidi wa Yehova bila kutumia damu. Waangalizi wengine huendeleza masilahi ya Ufalme kwa kusaidia kujenga na kudumisha Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko au kuwa washiriki wa Halmashauri za Makusanyiko. Wote katika tengenezo wanathamini sana bidii ya ndugu hao na utayari wao wa kujitoa kwa njia hiyo. Bila shaka, ‘tunaendelea kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo.’—Flp. 2:29.
MWANGALIZI WA MZUNGUKO
41 Baraza Linaloongoza hufanya mipango ili wazee wanaostahili wawekwe rasmi kuwa waangalizi wa mzunguko. Ofisi ya tawi huwapa waangalizi hao mgawo wa kutembelea kwa ukawaida makutaniko yaliyo katika mzunguko wao mara mbili kwa mwaka. Pia, mara kwa mara huwatembelea mapainia wanaotumikia katika maeneo ya mbali. Wao hupanga jinsi watakavyotembelea makutaniko nao hujulisha kila kutaniko mapema ili wote wafaidike na ziara hiyo.
42 Mratibu wa baraza la wazee ndiye anayeongoza kupanga mambo ili ziara hiyo iwaburudishe wote kiroho. (Rom. 1:11, 12) Baada ya kupata taarifa ya ziara hiyo na habari kuhusu mahitaji ya mwangalizi wa mzunguko na mke wake (ikiwa ameoa), mratibu wa baraza la wazee hufanya mipango kupitia ndugu mbalimbali ili kuandaa mahali pa kulala na mambo mengine muhimu. Mratibu huhakikisha kwamba wote, kutia ndani mwangalizi wa mzunguko, wanajulishwa mipango hiyo.
43 Mwangalizi wa mzunguko atawasiliana na mratibu wa baraza la wazee kuhusu ratiba ya mikutano, kutia ndani mikutano ya utumishi wa shambani. Ratiba hiyo itapangwa kulingana na mapendekezo ya mwangalizi wa mzunguko, na vilevile miongozo kutoka ofisi ya tawi. Wote wanapaswa kujulishwa mapema kuhusu wakati na mahali pa kila mkutano wa kutaniko, mkutano wa mapainia, mkutano wa wazee na watumishi wa huduma, na pia mikutano ya utumishi wa shambani.
44 Mwangalizi wa mzunguko hukagua Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri, rekodi ya hudhurio la mikutano, rekodi ya maeneo, na faili ya hesabu Jumanne mchana. Hilo litamwezesha kufahamu mahitaji ya kutaniko na kuona jinsi anavyoweza kuwasaidia wale wenye migawo ya kutunza rekodi hizo. Mratibu wa baraza la wazee anapaswa kuhakikisha kwamba mwangalizi wa mzunguko amepata mapema rekodi hizo.
45 Wakati wa ziara yake, mwangalizi wa mzunguko huzungumza na ndugu mmoja-mmoja kwa kadiri anavyoweza—kwenye mikutano, katika utumishi wa shambani, wakati wa chakula, na katika pindi nyingine. Pia, hukutana na wazee na watumishi wa huduma, na kutoa ushauri unaofaa wa Kimaandiko, mapendekezo, na kuwatia moyo ili kuwasaidia kutekeleza majukumu yao ya kulichunga kundi lililo chini ya uangalizi wao. (Met. 27:23; Mdo. 20:26-32; 1 Tim. 4:11-16) Yeye pia hufanya mkutano pamoja na mapainia ili kuwatia moyo katika kazi yao na kuwasaidia kutatua matatizo yoyote ambayo huenda wanakabili katika huduma.
46 Ikiwa kuna mambo mengine yanayohitaji kushughulikiwa, mwangalizi wa mzunguko atajitahidi kusaidia kwa kadiri anavyoweza katika juma hilo. Ikiwa mambo hayo hayatamalizika katika juma hilo, anaweza kuwasaidia wazee au wale wanaohusika kufanya utafiti wa Kimaandiko unaohusu jambo hilo. Ikiwa ofisi ya tawi inahitaji kuchukua hatua yoyote, yeye pamoja na wazee wataipa ofisi ya tawi habari kamili kuhusu jambo hilo.
47 Anapotembelea kutaniko, mwangalizi wa mzunguko huhudhuria mikutano ya kawaida ya kutaniko. Huenda ratiba ya mikutano hiyo ikabadilishwa mara kwa mara kupatana na maagizo yanayopatikana katika barua zinazotumwa na ofisi ya tawi. Atatoa hotuba zinazokusudiwa kutia moyo, kuchochea, kuagiza, na kuimarisha kutaniko. Atajitahidi kuwasaidia akina ndugu wazidishe upendo wao kwa Yehova, Yesu Kristo, na tengenezo.
48 Mojawapo ya malengo makuu ya ziara ya mwangalizi wa mzunguko ni kuwatia moyo wahubiri washiriki kwa bidii katika huduma ya shambani na kutoa madokezo yanayofaa. Wengi kutanikoni wanaweza kubadili ratiba zao ili washiriki kikamili katika huduma ya shambani katika juma hilo, labda kwa kufanya upainia msaidizi katika mwezi wa ziara. Wanaopenda kuhubiri pamoja naye au mke wake wanaweza kufanya mipango mapema. Kuna faida nyingi za kwenda na mwangalizi wa mzunguko au mke wake katika mafunzo ya Biblia na ziara za kurudia. Jitihada zako za kuunga mkono kwa ukamili mahubiri katika juma hilo la pekee zinathaminiwa sana.—Met. 27:17.
49 Kila mwaka, makusanyiko mawili ya mzunguko hufanywa katika kila mzunguko. Mwangalizi wa mzunguko ndiye anayesimamia mipango ya makusanyiko hayo. Mwangalizi wa mzunguko huteua ndugu wanaosimamia makusanyiko hayo, yaani, mwangalizi wa kusanyiko na msaidizi wake. Wanapaswa kushirikiana na mwangalizi wa mzunguko wanaposhughulikia mipango ya kusanyiko. Hilo litamwezesha mwangalizi wa mzunguko kuzingatia hasa programu ya kusanyiko. Mwangalizi wa mzunguko huchagua ndugu wengine wenye uwezo ili kusimamia idara mbalimbali. Pia hupanga hesabu za mzunguko zikaguliwe baada ya kila kusanyiko. Kwa mwaka, kusanyiko moja la mzunguko litatembelewa na mwakilishi wa ofisi ya tawi atakayekuwa msemaji anayezuru. Kwa sababu ya umbali au mahali pa kusanyiko kuwa padogo, baadhi ya mizunguko imegawanywa katika visehemu na kusanyiko la mzunguko hufanywa katika kila kisehemu.
50 Mwangalizi wa mzunguko hutuma ripoti yake moja kwa moja kwenye ofisi ya tawi mwishoni mwa kila mwezi. Ikiwa alitumia kiasi fulani cha pesa kwa ajili ya mambo kama vile usafiri, chakula, malazi, na mambo mengine muhimu ili kutimiza kazi yake, na hakurudishiwa gharama hizo na kutaniko alilotembelea juma hilo, basi anaweza kutuma gharama hizo kwenye ofisi ya tawi. Wawakilishi wanaosafiri wana hakika kwamba kama Yesu alivyoahidi, watapata mahitaji yao ya kimwili wakiendelea kuutafuta kwanza Ufalme wa Yehova. (Luka 12:31) Makutaniko yanapaswa kukumbuka kwamba yana pendeleo la kuwaonyesha ukarimu wazee hao wanaojitolea kuwatumikia.—3 Yoh. 5-8.
HALMASHAURI YA TAWI
51 Katika kila ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, ndugu watatu au zaidi ambao ni wakomavu na wanaostahili kiroho hutumikia wakiwa Halmashauri ya Tawi inayosimamia kazi ya kuhubiri katika nchi zilizo chini ya ofisi yao ya tawi. Mmoja wao hutumikia akiwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi.
52 Wale wanaotumikia katika Halmashauri ya Tawi hushughulikia mambo yanayohusu makutaniko yote katika eneo lao. Halmashauri hiyo husimamia kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme katika eneo lao na kuhakikisha kwamba kuna makutaniko na mizunguko ya kusimamia vizuri mahitaji ya eneo lao. Halmashauri ya Tawi husimamia utendaji wa wamishonari, mapainia wa pekee, wa kawaida, na wasaidizi. Kunapokuwa na makusanyiko, ndugu hao hufanya mipango na kutoa migawo ili kuhakikisha kwamba ‘mambo yote yanatendeka kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.
53 Halmashauri ya Nchi huwekwa rasmi katika nchi fulani zilizo chini ya Halmashauri ya Tawi iliyo katika nchi nyingine. Hilo hufanya kazi isimamiwe vizuri katika nchi ambayo kuna Halmashauri ya Nchi. Halmashauri hiyo hushughulikia mambo katika Makao ya Betheli na ofisi, hushughulikia barua, ripoti, na utendaji wa shambani kwa ujumla. Halmashauri ya Nchi hushirikiana na Halmashauri ya Tawi ili kuendeleza masilahi ya Ufalme.
54 Baraza Linaloongoza ndilo huwaweka rasmi washiriki wa Halmashauri za Tawi na Halmashauri za Nchi.
WAWAKILISHI WA MAKAO MAKUU
55 Mara kwa mara, Baraza Linaloongoza hupanga ndugu wanaostahili watembelee kila ofisi ya tawi duniani. Ndugu anayepewa mgawo huo anaitwa mwakilishi wa makao makuu. Kazi yake kuu ni kuitia moyo familia ya Betheli na kuisaidia Halmashauri ya Tawi kutatua matatizo au maswali ambayo huenda wakawa nayo kuhusiana na kazi ya kuhubiri na kufundisha. Ndugu huyo hukutana na baadhi ya waangalizi wa mzunguko, na pindi kwa pindi na wamishonari. Anapofanya hivyo, yeye huzungumza nao kuhusu matatizo na mahitaji yao, na kuwatia moyo kuhusiana na utendaji wao muhimu zaidi wa kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi.
56 Mwakilishi wa makao makuu hupendezwa sana na mambo yanayotimizwa katika eneo analotembelea kuhusiana na kuhubiriwa kwa Ufalme na utendaji mwingine unaofanywa na makutaniko. Ikiwa ana wakati, huenda pia akatembelea ofisi za utafsiri. Mwakilishi wa makao makuu anapotembelea ofisi za tawi, yeye pia hushiriki kadiri anavyoweza katika kazi ya kuhubiri Ufalme.
Tunapoendelea kujinyenyekeza kwa waangalizi wanaolichunga kundi, tunaunganishwa pamoja na Kichwa cha kutaniko, Kristo Yesu
WAANGALIZI WENYE UPENDO
57 Tunanufaishwa sana na bidii na upendo tunaoonyeshwa na Wakristo hao wakomavu. Tunapoendelea kujinyenyekeza kwa waangalizi wanaolichunga kundi, tunaunganishwa pamoja na Kichwa cha kutaniko, Kristo Yesu. (1 Kor. 16:15-18; Efe. 1:22, 23) Matokeo ni kwamba roho ya Mungu huenea katika makutaniko ulimwenguni pote, nalo Neno la Mungu huongoza kazi duniani pote.—Zab. 119:105.
-
-
Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi MuhimuTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 6
Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu
MTUME Paulo aliliandikia kutaniko la Filipi hivi: “Paulo na Timotheo, watumwa wa Kristo Yesu, kwa watakatifu wote katika muungano na Kristo Yesu walio huko Filipi, pamoja na waangalizi na watumishi wa huduma.” (Flp. 1:1) Ona kwamba aliwataja pia watumishi wa huduma. Wanaume hao kwa kweli walitimiza jukumu muhimu sana ili kuwasaidia wazee wakati huo. Ndivyo ilivyo leo. Watumishi wa huduma hufanya utumishi muhimu ambao unawasaidia wazee na kuchangia utaratibu mzuri katika kutaniko.
2 Je, unawajua watumishi wa huduma katika kutaniko lenu? Je, unajua kazi wanazofanya kwa faida yako na kutaniko zima? Bila shaka Yehova anathamini sana jitihada za wanaume hao. Paulo aliandika hivi: “Wanaume wanaohudumu vizuri wanajipatia sifa nzuri na uhuru mwingi wa kusema katika imani iliyo katika Kristo Yesu.”—1 Tim. 3:13.
SIFA ZA KIMAANDIKO ZA WATUMISHI WA HUDUMA
3 Watumishi wa huduma wanatarajiwa kuishi maisha ya Kikristo, wawe wanaume wenye kutegemeka wanaoshughulikia migawo yao kwa njia nzuri. Jambo hilo ni wazi tunapochunguza yale ambayo Paulo alisema kuhusu sifa zao katika barua yake kwa Timotheo: “Vilevile watumishi wa huduma wanapaswa kuchukua mambo kwa uzito, si wenye ndimi mbili, si wenye kunywa divai nyingi, si wenye pupa ya mapato yasiyo ya haki, wakiishika siri takatifu ya imani kwa dhamiri safi. Pia, wanapaswa kwanza kujaribiwa kama wanafaa; ndipo watumike wakiwa wahudumu, kwa kuwa hawana shtaka. Watumishi wa huduma wanapaswa kuwa waume wa mke mmoja, wanaosimamia vizuri watoto wao na nyumba zao wenyewe.” (1 Tim. 3:8-10, 12) Watumishi wa huduma wakishika viwango vya juu kutaniko litalindwa dhidi ya shutuma zinazoweza kutokea kuhusu wanaume wanaopewa majukumu ya pekee.
4 Iwe wao ni vijana au wana umri mkubwa watumishi wa huduma wanashiriki katika huduma kila mwezi. Wanamwiga Yesu kwa kuwa na bidii katika huduma. Kupitia bidii hiyo, wana maoni kama ya Yehova, ambaye anapenda watu waokolewe.—Isa. 9:7.
5 Wanaume wanaotumika wakiwa watumishi wa huduma huweka mfano mzuri kupitia mavazi, kujipamba, usemi, mtazamo, na mwenendo wao. Wana utimamu wa akili, sifa ambayo huwafanya waheshimiwe na wengine. Kwa kuongezea, wanachukua kwa uzito uhusiano wao na Yehova na mapendeleo yao ya utumishi kutanikoni.—Tito 2:2, 6-8.
6 Wanaume hao ‘wamejaribiwa kama wanafaa.’ Hata kabla ya kuwekwa rasmi, wamethibitika kuwa wanaume wenye bidii. Wameonyesha kwamba wanatanguliza masilahi ya Ufalme katika maisha yao na wanajitahidi kufikia mapendeleo yoyote ya utumishi wanayoweza kufikia. Kwa kweli wao huweka mfano mzuri kutanikoni.—1 Tim. 3:10.
JINSI WANAVYOTUMIKIA
7 Watumishi wa huduma hufanya utumishi mbalimbali kwa ajili ya ndugu na dada zao, na hivyo kuruhusu waangalizi kuwa na wakati wa kukazia fikira ufundishaji na majukumu ya uchungaji. Baraza la wazee linapowapa migawo watumishi wa huduma, hufikiria uwezo wa kila mmoja na mahitaji ya kutaniko.
Watumishi wa huduma hufanya utumishi mbalimbali kwa ajili ya ndugu na dada zao, na hivyo kuruhusu waangalizi kuwa na wakati wa kukazia fikira ufundishaji na majukumu ya uchungaji
8 Hebu fikiria baadhi ya kazi zao: Mtumishi wa huduma mmoja anaweza kupewa mgawo wa kushughulikia machapisho ili tupate machapisho kwa ajili yetu na kwa ajili ya huduma. Wengine hupewa mgawo wa kutunza hesabu za kutaniko au kutunza rekodi za maeneo. Baadhi yao hushughulikia maikrofoni, mfumo wa sauti, hutumikia wakiwa wakaribishaji na kuwasaidia wazee kwa njia mbalimbali. Kuna kazi nyingi inayohitaji kufanywa ili kudumisha na kusafisha Jumba la Ufalme, hivyo kwa kawaida watumishi wa huduma huombwa wasaidie kutimiza majukumu hayo.
9 Katika makutaniko fulani, huenda ikawezekana kumkabidhi kila mtumishi wa huduma mojawapo ya migawo hiyo. Katika makutaniko mengine huenda mtumishi mmoja wa huduma akapewa migawo kadhaa. Nyakati nyingine, watumishi wa huduma kadhaa wanaweza kushughulikia mgawo fulani. Ikiwa hakuna watumishi wa huduma wa kutosha, baraza la wazee linaweza kupanga ndugu waliobatizwa ambao ni mfano mzuri washughulikie migawo hiyo muhimu. Hivyo wanaweza kupata uzoefu utakaowasaidia baadaye watakapostahili kuwa watumishi wa huduma. Ikiwa hakuna akina ndugu, dada ambaye ni mfano mzuri anaweza kuombwa kushughulikia mambo fulani, ingawa hatapendekezwa kuwa mtumishi wa huduma. Mtu ambaye ni mfano mzuri anaweka kielelezo kizuri katika mambo ya kimwili na ya kiroho. Anapaswa kuwa mfano mzuri kwa wengine katika mazoea yake ya kuhudhuria mikutano, kushiriki katika huduma, maisha ya familia, burudani anazochagua, mavazi na kujipamba, na mambo mengine.
10 Katika makutaniko yenye wazee wachache, watumishi wa huduma wenye uwezo wanaweza kuombwa kupitia na wale wanaotaka kubatizwa maswali yanayohusu mafundisho. Maswali hayo yanapatikana katika Nyongeza “Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo.” Kwa kuwa “Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo” inahusu mambo mazito ya kibinafsi, mzee anapaswa kushughulikia sehemu hiyo.
11 Ikiwa kuna sababu zinazofaa, mara kwa mara huenda baraza la wazee likaona inafaa kubadili baadhi ya migawo ya watumishi wa huduma. Hata hivyo, kuna faida kubwa kuwaacha akina ndugu waendelee kufanya migawo ileile kwa kipindi fulani ili wapate uzoefu na ustadi.
12 Ikitegemea hali ya kutaniko, watumishi wa huduma wanaweza kupewa migawo mingine ikiwa ‘maendeleo yao yanaonekana wazi kwa watu wote.’ (1 Tim. 4:15) Ikiwa hakuna wazee wa kutosha, mtumishi wa huduma anaweza kuwekwa kuwa msaidizi wa mwangalizi wa kikundi au katika visa fulani, kuwa mtumishi wa kikundi, akifanya kazi chini ya uangalizi wa wazee. Watumishi wa huduma wanaweza kupewa migawo fulani kwenye Mkutano wa Huduma na Maisha kutia ndani kuongoza Funzo la Biblia la Kutaniko kunapokuwa na uhitaji, na kutoa hotuba za watu wote. Watumishi wa huduma wanaweza kupewa mapendeleo mengine kunapokuwa na uhitaji hususa na ikiwa wanastahili kutimiza migawo hiyo. (1 Pet. 4:10) Wanapowasaidia wazee, watumishi wa huduma wanapaswa kujitoa wenyewe kwa hiari.
13 Ingawa kazi yao ni tofauti na kazi ya wazee, bado ni sehemu ya utumishi mtakatifu kwa Mungu unaofaidi kutaniko. Baada ya muda, ikiwa watumishi wa huduma wanatimiza vizuri majukumu yao na wanastahili kuwa wachungaji na walimu, wanaweza kupendekezwa kuwa wazee.
14 Ikiwa wewe ni ndugu kijana au umebatizwa karibuni, je, unajitahidi kustahili kuwa mtumishi wa huduma? (1 Tim. 3:1) Kwa kuwa watu wengi wanakuja katika kweli kila mwaka, wanaume wanaostahili kiroho wanahitajiwa ili washughulikie majukumu kutanikoni. Unaweza kustahili kwa kusitawisha tamaa ya kuwatumikia wengine. Unaweza kufanya hivyo kwa kutafakari mfano mzuri wa Yesu. (Mt. 20:28; Yoh. 4:6, 7; 13:4, 5) Tamaa yako itaongezeka unapoona shangwe inayotokana na kuwatumikia wengine. (Mdo. 20:35) Kwa hiyo, jitolee kuwasaidia wengine, saidia kudumisha Jumba la Ufalme, au kujitolea kutoa hotuba za wanafunzi katika Mkutano wa Huduma na Maisha. Pia, ili ustahili unapaswa kusitawisha sifa za kiroho na kuwa na funzo la kibinafsi kwa ukawaida. (Zab. 1:1, 2; Gal. 5:22, 23) Isitoshe, ndugu anayejitahidi kufikia mapendeleo anaonyesha kuwa anategemeka na ni mwaminifu anapopewa migawo kutanikoni.—1 Kor. 4:2.
15 Watumishi wa huduma wanawekwa rasmi na roho takatifu kwa manufaa ya kutaniko. Wote kutanikoni wanaweza kuonyesha kwamba wanathamini bidii ya watumishi wa huduma kwa kushirikiana nao wanapotimiza migawo yao. Kwa njia hiyo, kutaniko litaonyesha kwamba linathamini mpango wa Yehova wa kudumisha utaratibu kutanikoni.—Gal. 6:10.
-
-
Mikutano ‘Inayotuchochea Katika Upendo na Matendo Mazuri’Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 7
Mikutano ‘Inayotuchochea Katika Upendo na Matendo Mazuri’
KWA miaka mingi, watu wa Yehova wamekuwa wakikusanyika kwa utaratibu mzuri. Katika Israeli la kale, wanaume wote walienda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe kuu tatu. (Kum. 16:16) Katika karne ya kwanza, Wakristo walikusanyika kwa ukawaida katika nyumba za watu. (Flm. 1, 2) Siku hizi tunafurahia kuhudhuria mikutano, na makusanyiko. Kwa nini watu wa Mungu hukusanyika? Jambo kuu ni kwa sababu ni sehemu muhimu ya ibada yetu.—Zab. 95:6; Kol. 3:16.
2 Pia, mikutano huwafaidi wale wanaohudhuria. Kuhusu Sherehe ya Vibanda ya kila mwaka wa saba, Waisraeli waliambiwa hivi: “Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo na mkaaji mgeni aliye ndani ya malango yako, ili wasikilize na ili wajifunze, kwa maana ni lazima wamwogope Yehova Mungu wenu na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria hii.” (Kum. 31:12) Ni wazi kwamba kusudi kuu la kukusanyika ni ‘kufundishwa na Yehova.’ (Isa. 54:13) Pia, tunaposhirikiana katika mikutano tunapata fursa za kufahamiana, kutiana moyo, na kuimarishana.
MIKUTANO YA KUTANIKO
3 Mitume waliokusanyika baada ya Pentekoste 33 W.K., walijitoa wenyewe kwa fundisho la mitume, na “siku baada ya siku walikuwa wakihudhuria daima kwenye hekalu kwa umoja.” (Mdo. 2:42, 46) Baadaye, Wakristo walipokutana kwa ajili ya ibada, walisoma maandiko yaliyoongozwa na roho, kutia ndani barua zilizoandikwa na mitume na wanafunzi wengine Wakristo. (1 Kor. 1:1, 2; Kol. 4:16; 1 The. 1:1; Yak. 1:1) Pia, walisali pamoja wakiwa kutaniko. (Mdo. 4:24-29; 20:36) Nyakati nyingine, wamishonari walisimulia mambo waliyojionea katika huduma. (Mdo. 11:5-18; 14:27, 28) Walizungumzia mafundisho ya Biblia na jinsi unabii mbalimbali ulivyotimizwa. Walipewa mwongozo kuhusu mwenendo wa Kikristo na ujitoaji kwa Mungu. Walitiwa moyo wawe watangazaji wenye bidii wa habari njema.—Rom. 10:9, 10; 1 Kor. 11:23-26; 15:58; Efe. 5:1-33.
Katika siku hizi za mwisho, tunahitaji zaidi kitia-moyo ambacho tunapata tunapokutana kwa ukawaida
4 Siku hizi, mikutano ya Kikristo hufuata utaratibu kama wa mikutano iliyofanywa siku za mitume. Tunatii himizo hili lililoongozwa na roho kwenye Waebrania 10:24, 25: “Na acheni tufikiriane . . . bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” Katika siku hizi za mwisho, tunahitaji zaidi kitia-moyo ambacho tunapata tunapokutana kwa ukawaida ili tudumishe nguvu zetu za kiroho na utimilifu wa Kikristo. (Rom. 1:11, 12) Tukiwa Wakristo, tunaishi katika kizazi kilicho kombo na kilichopotoka. Tumekataa mwenendo mpotovu na tamaa za ulimwengu. (Flp. 2:15, 16; Tito 2:12-14) Kwa kweli, hakuna mahali pengine bora kuliko kushirikiana na watu wa Yehova! (Zab. 84:10) Na ni jambo gani lingine lenye faida kuliko kujifunza na kuzungumzia Neno la Mungu? Acheni tuchunguze baadhi ya mikutano ambayo imepangwa kwa faida yetu.
MKUTANO WA MWISHO JUMA
5 Sehemu ya kwanza ya mkutano wa mwisho juma hutia ndani hotuba inayotegemea Biblia hasa kwa ajili ya watu wote, ambao baadhi yao huenda wamehudhuria kwa mara ya kwanza. Hotuba hiyo ya watu wote hutimiza lengo muhimu la kutosheleza mahitaji ya kiroho ya wahubiri kutanikoni na wapya.—Mdo. 18:4; 19:9, 10.
6 Kristo Yesu, mitume wake, na washiriki wenzao walifanya mikutano ya watu wote kama ile inayofanywa leo katika makutaniko ya watu wa Yehova. Bila shaka, Yesu alikuwa msemaji bora zaidi duniani. Ilisemwa hivi kumhusu: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Yoh. 7:46) Yesu alizungumza kwa mamlaka, na kuwashangaza wasikilizaji wake. (Mt. 7:28, 29) Wale waliozingatia ujumbe wake walifaidika sana. (Mt. 13:16, 17) Mitume waliiga mfano wake. Katika andiko la Matendo 2:14-36, tunasoma kuhusu hotuba yenye kusisimua ambayo Petro alitoa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Wengi walichochewa kutenda kulingana na mambo waliyoyasikia. Baadaye, watu wakawa waamini baada ya kusikiliza hotuba ya Paulo huko Athene.—Mdo. 17:22-34.
7 Vivyo hivyo, mamilioni ya watu leo wamefaidika na hotuba za watu wote zinazotolewa katika makutaniko kila juma, na vilevile hotuba zinazotolewa kwenye makusanyiko. Hotuba hizo hutukumbusha mafundisho ya Kikristo na kutuchochea kuwa na bidii katika kazi ya Ufalme. Tunapowaalika watu wanaopendezwa na wengine kwa ujumla, tunaweza kuwasaidia wengi wajifunze mafundisho ya msingi ya Biblia.
8 Habari mbalimbali huzungumziwa katika hotuba za watu wote. Hotuba huzungumzia mafundisho ya Biblia, unabii, hali zinazowakabili vijana, maadili ya Kikristo, kanuni za Kimaandiko, na ushauri kuhusu maisha ya familia na ndoa. Baadhi ya hotuba huzungumzia maajabu ya uumbaji wa Yehova. Hotuba nyingine hukazia imani, ujasiri, na utimilifu wa watu wanaotajwa katika Biblia na kukazia jinsi tunavyoweza kuwaiga.
9 Ili tufaidike kikamili na hotuba za watu wote, ni muhimu tusikilize kwa makini, tufungue maandiko yanayotajwa na msemaji na kufuatana naye anapoyasoma na kuyafafanua. (Luka 8:18) Kwa hiyo, tunapohakikisha mambo yanayozungumziwa, tutaazimia kufuata mambo tunayojifunza na kuyatumia maishani.—1 The. 5:21.
10 Ikiwa kuna wasemaji, bila shaka kutaniko litakuwa na hotuba ya watu wote kila juma. Mara nyingi, hilo linawezekana kwa kuwaalika wasemaji kutoka katika makutaniko ya karibu. Ikiwa hakuna wasemaji wa kutosha, hotuba hizo zitatolewa kwa kadiri inavyowezekana.
11 Sehemu ya pili ya mkutano wa mwisho juma ni Funzo la Mnara wa Mlinzi, mazungumzo ya maswali na majibu yanayotegemea makala za Mnara wa Mlinzi toleo la funzo. Yehova anatupatia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kupitia Funzo la Mnara wa Mlinzi.
12 Mara nyingi makala za funzo huzungumzia jinsi ya kutumia kanuni za Biblia katika maisha ya kila siku. Huwaimarisha Wakristo ili wapinge “roho ya ulimwengu” na mwenendo mchafu. (1 Kor. 2:12) Kupitia Mnara wa Mlinzi tunapata nuru mpya kuhusu mafundisho ya Biblia na unabii, na hivyo kutusaidia kwenda sambamba na kweli na kubaki kwenye njia ya waadilifu. (Zab. 97:11; Met. 4:18) Kuhudhuria na kushiriki katika Funzo la Mnara wa Mlinzi kunaweza kutusaidia kushangilia katika tumaini la ulimwengu mpya wenye uadilifu wa Yehova. (Rom. 12:12; 2 Pet. 3:13) Ushirika wetu wa Kikristo hutusaidia kusitawisha tunda la roho na kuimarisha tamaa yetu ya kumtumikia Yehova kwa bidii. (Gal. 5:22, 23) Tunaimarishwa ili tuvumilie majaribu na kujenga “msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao” ili ‘tuushike imara uzima ulio wa kweli.’—1 Tim. 6:19; 1 Pet. 1:6, 7.
13 Tufanye nini ili tufaidike na chakula hicho cha kiroho? Tunapaswa kutayarisha mapema, tukiwa familia au peke yetu, kusoma maandiko yaliyotajwa, na kutoa maelezo bila kusoma moja kwa moja. Kufanya hivyo kutakazia kweli hiyo moyoni mwetu, na wengine watafaidika wanaposikiliza maelezo yetu ya imani. Tunaposikiliza kwa makini maelezo ya wengine, tutafaidika na habari inayozungumziwa kila juma.
MKUTANO WA KATIKATI YA JUMA
14 Tunakusanyika kila juma kwenye Jumba la Ufalme kwa ajili mkutano mwingine unaoitwa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Mkutano huo una sehemu tatu ambazo zinatusaidia kujipatia “sifa za kustahili” kuwa wahudumu wa Mungu. (2 Kor. 3:5, 6) Ratiba na habari zitakazozungumziwa zinatolewa katika toleo la kila mwezi la Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Pia, daftari hilo lina mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo katika utumishi wa shambani.
15 Sehemu ya kwanza ya mkutano huo inayoitwa Hazina za Neno la Mungu, inatusaidia kufahamu vizuri masimulizi ya Biblia na kujifunza jinsi tunavyoweza kuyatumia. Sehemu hii inahusisha hotuba, usomaji, na majadiliano yanayotegemea usomaji wa Biblia wa juma hilo. Pia katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha kuna sehemu ya mazoezi na mifano ambayo inatusaidia kufundisha masimulizi hayo. Kuichunguza Biblia kwa kina kutatunufaisha maishani mwetu na katika kufundisha ili ‘tuwe na uwezo kamili, tukiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Tim. 3:16, 17.
16 Sehemu ya pili ya mkutano huo, inayoitwa Boresha Huduma Yako, imekusudiwa kuwapa wote fursa ya kufanya mazoezi kwa ajili ya huduma na kuboresha uwezo wao wa kuhubiri na kufundisha. Mbali na migawo ya wanafunzi, video za mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo katika huduma hutazamwa na kuzungumziwa. Sehemu hii ya mkutano hutusaidia kujipatia ‘ulimi wa waliofundishwa ili tujue jinsi ya kumjibu neno yeye aliyechoka.’—Isa. 50:4.
17 Sehemu ya tatu, inaitwa Maisha ya Mkristo, sehemu hii inazungumzia jinsi ya kutumia kanuni za Biblia maishani. (Zab. 119:105) Jambo muhimu katika sehemu hii ni Funzo la Biblia la Kutaniko. Funzo la Biblia la Kutaniko linahusisha maswali na majibu kama Funzo la Mnara wa Mlinzi.
18 Kila mwezi tunapopokea Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha, mratibu wa baraza la wazee, au mzee mwingine anayemsaidia, atalichunguza kwa makini na kupanga ratiba. Kila juma, mzee ambaye ni mwalimu mzuri na amependekezwa na baraza la wazee atakuwa mwenyekiti wa mkutano. Jukumu lake ni kuhakikisha kwamba mkutano unaanza na kumalizika kwa wakati na kuwapongeza na kuwashauri wale walio na migawo ya wanafunzi.
19 Tunapojitayarisha, kuhudhuria na kushiriki kwa ukawaida Mkutano wa Huduma na Maisha, tutayajua Maandiko, tutaelewa kanuni za Biblia, tutakuwa na ujasiri wa kuhubiri habari njema, na ustadi wa kufundisha wanafunzi. Wale wote ambao wanahudhuria lakini hawajabatizwa watanufaika na ushirika mzuri na kujengwa na mazungumzo ya kiroho. Ili kujitayarisha vizuri kwa ajili ya mkutano huo na mikutano mingine, tunaweza kufanya utafiti katika Watchtower Library, JW Library®, Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO™ au maktaba ya Jumba la Ufalme. Maktaba hiyo ina machapisho ya Mashahidi wa Yehova, kutia ndani Fahirisi, Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova, tafsiri mbalimbali za Biblia, na vitabu vingine muhimu vya marejeo. Mtu yeyote anaweza kutumia maktaba hiyo ya Jumba la Ufalme kabla au baada ya mikutano.
MIKUTANO YA UTUMISHI WA SHAMBANI
20 Mara kadhaa katikati ya juma na mwishoni mwa juma, vikundi vya wahubiri vitafanya mkutano mfupi kabla ya utumishi wa shambani. Kwa kawaida mikutano hiyo hufanywa kwenye nyumba za watu au mahali pengine panapofaa. Jumba la Ufalme linaweza kutumiwa pia. Kuwa na vikundi vidogo katika sehemu tofauti-tofauti hufanya iwe rahisi kwa wahubiri kufika kwenye mkutano wa utumishi na kufika haraka kwenye eneo. Wahubiri wanaweza kujipanga haraka na kwenda kwenye eneo bila kukawia. Pia, mwangalizi wa kikundi anaweza kuwasaidia wote walio kwenye kikundi chake. Ingawa kuna faida za vikundi kukutana kwenye maeneo tofauti-tofauti, nyakati nyingine huenda hali zikalazimu vikundi kadhaa vikutane pamoja. Kwa mfano, kukiwa na wahubiri wachache wanaoenda utumishi katikati ya juma, ni vizuri kuunganisha vikundi kadhaa au kutaniko zima likutane kwenye Jumba la Ufalme au mahali pengine panapofaa. Jambo hilo litasaidia wahubiri wapate waandamani. Pia, kutaniko linaweza kuona inafaa kukutanika kwenye Jumba la Ufalme wakati wa sikukuu za kilimwengu. Au kutaniko linaweza kuamua kuwa na mkutano mmoja wa utumishi wa shambani baada ya Funzo la Mnara wa Mlinzi.
21 Ikiwa vikundi vinakutanika sehemu tofauti, mwangalizi wa kikundi huongoza mkutano wa utumishi wa shambani. Mara kwa mara, mwangalizi wa kikundi anaweza kupanga ili msaidizi wake au ndugu mwingine anayestahili aongoze mkutano huo. Ndugu anayeongoza anapaswa kuzungumzia mambo yatakayowasaidia wahubiri katika utumishi wa shambani. Mipango ya kuhubiri hufanywa, kisha mhubiri mmoja huombwa atoe sala. Kisha, bila kukawia kikundi kitaelekea kwenye eneo. Mikutano hiyo inapaswa kufanywa kwa dakika tano au saba, lakini inapaswa kufupishwa zaidi ikiwa inafanywa baada ya mkutano wa kutaniko. Wahubiri waliohudhuria wanapaswa kutiwa moyo, kupewa maagizo, na mwongozo. Wapya au wale wanaohitaji msaada wanaweza kupangwa na wahubiri wenye uzoefu ili wazoezwe.
MIPANGO YA MIKUTANO KATIKA MAKUTANIKO MAPYA AU MADOGO
22 Wanafunzi wanapoongezeka, idadi ya makutaniko huongezeka pia. Kwa kawaida, ombi la kuanzishwa kwa kutaniko jipya hutumwa na mwangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, kwa sababu ya hali fulani, huenda vikundi vidogo vikaona inafaa zaidi kushirikiana na kutaniko la karibu.
23 Nyakati nyingine, makutaniko madogo yanaweza kuwa na akina dada peke yao. Inapokuwa hivyo, dada anayetoa sala kutanikoni au kuongoza mikutano anapaswa kufunika kichwa chake, kulingana na mpango wa Kimaandiko. (1 Kor. 11:3-16) Mara nyingi wanaongoza wakiwa wameketi wakitazama kikundi. Akina dada hawapaswi kuhutubia kutaniko wakiwa wamesimama jukwaani. Badala yake wanasoma na kuzungumzia habari zilizotayarishwa na tengenezo, au wanaweza kutumia njia nyingine kama vile mazungumzo au onyesho. Ofisi ya tawi itamwomba dada mmoja awe akiwasiliana na ofisi na kushughulikia mikutano. Baadaye, ndugu wanapostahili, watashughulikia majukumu hayo.
MAKUSANYIKO YA MZUNGUKO
24 Kila mwaka, mipango hufanywa ili makutaniko yaliyo katika mzunguko yawe na makusanyiko mawili ya mzunguko, kila kusanyiko hufanywa kwa siku moja. Nyakati hizo za shangwe humpa kila mmoja nafasi ya ‘kupanuka’ katika ushirika wa Kikristo. (2 Kor. 6:11-13) Tengenezo la Yehova hutayarisha vichwa vya Kimaandiko na sehemu mbalimbali za makusanyiko hayo kulingana na uhitaji. Habari hutolewa kwa njia mbalimbali kama vile hotuba, maonyesho, maigizo, mtu anayejizungumzia, na mahojiano. Maagizo hayo huwajenga wote waliohudhuria. Kwenye makusanyiko hayo, mipango hufanywa ili wanafunzi wapya waonyeshe wakfu wao kwa Yehova kupitia ubatizo.
MAKUSANYIKO YA ENEO
25 Kila mwaka, makusanyiko makubwa hufanywa. Yanaitwa makusanyiko ya eneo na kwa kawaida hufanywa kwa siku tatu na yanahudhuriwa na makutaniko ya mizunguko kadhaa. Hata hivyo, huenda ofisi ndogo za tawi zikaona kwamba ni rahisi na ingefaa makutaniko yote yaliyo chini yake yakusanyike mahali pamoja. Mipango ya makusanyiko hayo hutofautiana katika nchi mbalimbali ikitegemea hali au mwongozo wa tengenezo. Mara kwa mara, makusanyiko ya kimataifa au ya pekee hufanywa katika nchi fulani na huenda yakahudhuriwa na maelfu ya Mashahidi kutoka nchi mbalimbali. Kwa miaka mingi, watu wengi wamejifunza habari njema kwa sababu ya kutangazwa kwa makusanyiko hayo makubwa ya Mashahidi wa Yehova.
26 Makusanyiko ni pindi za shangwe ambazo waabudu wa Yehova huungana ili kuabudu. Nuru zaidi ya kweli hufunuliwa kwenye makusanyiko hayo. Katika baadhi ya makusanyiko, machapisho mapya hutolewa kwa ajili ya funzo la kibinafsi na la kutaniko, na pia kwa ajili huduma ya shambani. Kwenye makusanyiko pia kunakuwa na ubatizo. Makusanyiko husaidia sana kuwaimarisha watu ili wakue kiroho. Makusanyiko huthibitisha kwamba watu wa Yehova ni undugu wa kimataifa wa Wakristo waliojiweka wakfu ambao wana alama inayowatambulisha kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Yoh. 13:35.
27 Tunapohudhuria mikutano ya kutaniko na makusanyiko ya watu wa Yehova, tunaimarishwa ili tufanye mapenzi ya Yehova. Pia, tunalindwa dhidi ya mtazamo wa ulimwengu unaoweza kudhoofisha imani yetu ya Kikristo. Mikutano hiyo yote humletea Yehova sifa na utukufu. (Zab. 35:18; Met. 14:28) Tunathamini kwamba Yehova ameandaa pindi hizo za kuwaburudisha kiroho watu wake waliojiweka wakfu katika nyakati hizi za mwisho.
MLO WA JIONI WA BWANA
28 Mara moja kila mwaka, makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova huadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo, au Mlo wa Jioni wa Bwana. (1 Kor. 11:20, 23, 24) Huo ndio mkutano muhimu zaidi wa watu wa Yehova katika mwaka. Tumeagizwa waziwazi tuadhimishe Ukumbusho huo.—Luka 22:19.
29 Tarehe ya Ukumbusho hulingana na tarehe ya Pasaka inayotajwa katika Biblia. (Kut. 12:2, 6; Mt. 26:17, 20, 26) Pasaka ilikuwa mwadhimisho wa kila mwaka ambao uliwakumbusha Waisraeli siku waliyotoka Misri, mwaka wa 1513 K.W.K. Wakati huo, Yehova alichagua siku ya 14 ya mwezi wao wa kwanza kuwa tarehe ambayo wangemla mwana-kondoo wa Pasaka na kutoka utumwani Misri. (Kut. 12:1-51) Tarehe hiyo hupatikana kwa kuhesabu siku 13 kuanzia wakati mwezi mpya unapoonekana huko Yerusalemu, karibu Machi 21 hivi. Kwa kawaida, kila mwaka mwadhimisho wa Ukumbusho huangukia tarehe ambayo mwezi mpevu huonekana kwa mara ya kwanza baada ya Machi 21.
30 Andiko la Mathayo 26:26-28 linataja maneno ya Yesu kuhusu jinsi Ukumbusho unavyopaswa kuadhimishwa. Ukumbusho si desturi yenye mafumbo, bali ni mlo wa mfano ambao unaliwa na wale waliochaguliwa kuwa warithi pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni. (Luka 22:28-30) Wakristo wengine wote waliojiweka wakfu na watu wanaopendezwa hutiwa moyo kuhudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana wakiwa watazamaji. Wanapohudhuria, wanaonyesha kwamba wanathamini maandalizi ambayo Yehova Mungu amefanya kupitia Mwanaye, Yesu Kristo, kwa faida ya wanadamu wote. Kabla ya Ukumbusho, hotuba ya pekee ya watu wote hutolewa ili kuwafanya watu watazamie kwa hamu tukio hilo na kuwachochea wanaopendezwa wajifunze Biblia.
31 Mashahidi wa Yehova hutazamia kwa hamu pindi za kukusanyika pamoja kwenye mikutano, ambako ‘tunafikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ (Ebr. 10:24) Mtumwa mwaminifu na mwenye busara huwa macho ili kupanga mikutano hiyo kulingana na mahitaji yetu ya kiroho. Watumishi wote wa Yehova pamoja na watu wote wanaopendezwa wanahimizwa kuthamini sana mpango wa kukusanyika pamoja kwa ukawaida. Watumishi wa Mungu huunganishwa kwa umoja wanapothamini maandalizi ambayo Yehova anafanya kupitia tengenezo lake. Jambo muhimu zaidi, tunamsifu na kumtukuza Yehova.—Zab. 111:1.
-
-
Wahudumu wa Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 8
Wahudumu wa Habari Njema
YEHOVA alimtuma Mwanaye, Yesu Kristo, ili atuwekee kielelezo bora cha kuiga. (1 Pet. 2:21) Mtu anapokuwa mfuasi wa Yesu, anahubiri habari njema akiwa mhudumu wa Mungu. Akionyesha kwamba jambo hilo lingeburudisha kiroho, Yesu alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.” (Mt. 11:28, 29) Wote ambao wamekubali mwaliko huo wameona ahadi hiyo ikitimia!
2 Akiwa Mhudumu Mkuu wa Mungu, Yesu alichagua watu fulani wawe wafuasi wake. (Mt. 9:9; Yoh. 1:43) Aliwazoeza katika huduma na kuwatuma wafanye kazi ileile aliyokuwa akifanya. (Mt. 10:1–11:1; 20:28; Luka 4:43) Baadaye aliwatuma wengine 70 wakatangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Luka 10:1, 8-11) Yesu alipowatuma wanafunzi wake, aliwaambia hivi: “Yeyote anayewasikiliza ninyi ananisikiliza mimi pia. Na yeyote anayewapuuza ninyi ananipuuza mimi pia. Isitoshe, yeyote anayenipuuza mimi anampuuza pia Yule aliyenituma.” (Luka 10:16) Kwa kusema hivyo, Yesu alikazia jukumu zito alilowapa wanafunzi wake. Walipaswa kumwakilisha Yesu na Mungu Aliye Juu Zaidi! Ndivyo ilivyo leo kwa wale wanaokubali mwaliko huu wa Yesu: Njoo “uwe mfuasi wangu.” (Luka 18:22; 2 Kor. 2:17) Mungu anawapa wale wanaokubali mwaliko huo utume wa kuhubiri habari njema ya Ufalme na kufundisha.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
3 Kwa kuwa tumekubali mwaliko wa Yesu na kumfuata, tumebarikiwa ‘kumjua’ Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yoh. 17:3) Tumefundishwa njia za Yehova. Ametusaidia kufanya upya akili yetu, kuvaa utu mpya, na kupatanisha maisha yetu na viwango vyake vya uadilifu. (Rom. 12:1, 2; Efe. 4:22-24; Kol. 3:9, 10) Kwa kuwa tunathamini mambo hayo kutoka moyoni, tumechochewa tujiweke wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji. Tunapobatizwa tunakuwa wahudumu waliowekwa rasmi.
4 Sikuzote kumbuka kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu tukiwa na mikono isiyo na hatia na moyo safi. (Zab. 24:3, 4; Isa. 52:11; 2 Kor. 6:14–7:1) Kupitia imani katika Yesu Kristo, tumepata dhamiri safi. (Ebr. 10:19-23, 35, 36; Ufu. 7:9, 10, 14) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wafanye mambo yote kwa utukufu wa Mungu ili wasiwakwaze wengine. Pia, mtume Petro alionyesha kwamba mwenendo mzuri wa Kikristo unaweza kuwavuta wasioamini waikubali kweli. (1 Kor. 10:31, 33; 1 Pet. 3:1) Unawezaje kumsaidia mtu astahili kuwa mhudumu wa habari njema?
WAHUBIRI WAPYA
5 Mara tu unapoanza kuongoza funzo la Biblia na mtu anayependezwa, mtie moyo awaambie wengine mambo anayojifunza. Anaweza kuwahubiria isivyo rasmi watu wa ukoo, marafiki, wafanyakazi wenzake, na watu wengine. Hiyo ni hatua muhimu ya kuwafundisha wapya kuwa wafuasi wa Yesu Kristo wakiwa wahudumu wa habari njema. (Mt. 9:9; Luka 6:40) Mwanafunzi mpya anapokua kiroho na kuzoea kuhubiri isivyo rasmi, bila shaka ataomba kuhubiri rasmi pamoja na kutaniko.
KUTIMIZA MATAKWA
6 Kabla ya kumwalika mtu ahubiri pamoja nawe nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza, unapaswa kuhakikisha kwamba anatimiza matakwa fulani. Mtu anapohubiri pamoja nasi anajitambulisha kuwa Shahidi wa Yehova. Hivyo ni wazi kwamba amepatanisha maisha yake na viwango vya Yehova vya uadilifu na anaweza kuwa mhubiri wa kutaniko ambaye hajabatizwa.
7 Unapojifunza na mtu na kuzungumzia kanuni za Biblia, inaelekea utamfahamu vizuri. Huenda umeona kwamba anaishi kupatana na yale anayojifunza. Hata hivyo, wazee wangependa kuzungumzia mambo fulani pamoja nawe na mwanafunzi wako.
8 Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wazungumzie mambo hayo pamoja nawe na mwanafunzi wa Biblia. Katika makutaniko yenye wazee wachache, mzee na mtumishi wa huduma wanaweza kushughulikia jambo hilo. Ndugu waliochaguliwa wanapaswa kufanya hivyo bila kukawia. Mwanafunzi akitoa ombi siku ya mkutano wa kutaniko, huenda ikawezekana kwa ndugu hao kuzungumza nawe na mwanafunzi wako baada ya mkutano. Kikao kinapaswa kuwa chenye kustarehesha. Kabla mwanafunzi hajakubaliwa kuwa mhubiri, mambo yafuatayo yanapaswa kuzingatiwa:
(1) Anaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu.—2 Tim. 3:16.
(2) Anajua na kuamini mafundisho ya msingi ya Maandiko ili atakapoulizwa maswali, ajibu kulingana na Biblia bali si mafundisho ya dini za uwongo au maoni yake mwenyewe.—Mt. 7:21-23; 2 Tim. 2:15.
(3) Anatii amri ya Biblia ya kushirikiana na watu wa Yehova kwenye mikutano ya kutaniko ikiwa ana uwezo wa kufanya hivyo.—Zab. 122:1; Ebr. 10:24, 25.
(4) Anajua yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu uasherati, kutia ndani ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa, uzinzi, kuwa na wake wengi, na kufanya ngono na mtu wa jinsia moja, na anaishi kupatana na mafundisho hayo. Ikiwa mtu huyo anaishi na mtu wa jinsia tofauti ambaye si mtu wake wa ukoo, ni lazima wawe wamefunga ndoa kisheria.—Mt. 19:9; 1 Kor. 6:9, 10; 1 Tim. 3:2, 12; Ebr. 13:4.
(5) Anatii amri ya Biblia inayokataza ulevi na hatumii dawa za kulevya isipokuwa kwa ajili ya matibabu.—2 Kor. 7:1; Efe. 5:18; 1 Pet. 4:3, 4.
(6) Anaona umuhimu wa kuepuka kushirikiana na watu wasioheshimu viwango vya Biblia.—1 Kor. 15:33.
(7) Amevunja kabisa ushirika na dini zote za uwongo ambazo huenda alishirikiana nazo. Ameacha kuhudhuria ibada hizo na hategemezi shughuli zao wala kushiriki katika shughuli hizo.—2 Kor. 6:14-18; Ufu. 18:4.
(8) Hajihusishi hata kidogo na mambo ya kisiasa ya ulimwengu.—Yoh. 6:15; 15:19; Yak. 1:27.
(9) Anaamini na kuishi kupatana na kile kinachosemwa katika Isaya 2:4 kuhusu mizozo ya mataifa.
(10) Anatamani kabisa kuwa Shahidi wa Yehova.—Zab. 110:3.
9 Ikiwa wazee hawana uhakika jinsi mwanafunzi anavyoelewa baadhi ya mambo hayo, wanaweza kusoma na kuzungumzia maandiko yaliyotajwa. Ni muhimu aelewe kwamba wale wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova katika kazi ya kuhubiri lazima waishi kupatana na matakwa hayo ya Kimaandiko. Maelezo yake yatawasaidia wazee kujua kama anaelewa matakwa hayo na ikiwa anastahili kuanza kushiriki katika huduma ya shambani.
10 Wazee wanapaswa kumweleza bila kukawia ikiwa anastahili. Mara nyingi jambo hilo hufanywa mwishoni mwa mazungumzo. Ikiwa anastahili, wazee watamkaribisha kwa uchangamfu kuwa mhubiri. (Rom. 15:7) Anapaswa kutiwa moyo ashiriki katika huduma ya shambani haraka iwezekanavyo na atoe ripoti ya utumishi wa shambani mwishoni mwa mwezi. Wazee wanaweza kumweleza kwamba mwanafunzi wa Biblia anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa na kutoa ripoti ya utumishi wa shambani kwa mara ya kwanza, Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri yenye jina lake huwekwa kwenye faili ya kutaniko. Wazee hukusanya taarifa hizo za kibinafsi kutoka kwa mhubiri ili tengenezo liweze kushughulikia utendaji wa kidini wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote na ili mhubiri ashiriki katika shughuli za kiroho na kupokea msaada wa kiroho. Zaidi ya hilo, wazee wanaweza kuwakumbusha wahubiri wapya kwamba taarifa zozote za kibinafsi hushughulikiwa kulingana na Sera ya Mashahidi wa Yehova ya Kulinda Taarifa Ulimwenguni Pote inayopatikana kwenye tovuti ya jw.org.
11 Kufahamiana vizuri na mhubiri mpya na kupendezwa kikweli na yale anayotimiza kunaweza kumtia moyo. Kunaweza kumchochea kutoa ripoti ya utumishi wa shambani kwa ukawaida kila mwezi na kujitahidi zaidi kumtumikia Yehova.—Flp. 2:4; Ebr. 13:2.
12 Wazee wanapoona kwamba mwanafunzi wa Biblia anastahili kushiriki katika huduma ya shambani, itafaa apewe kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova. Atakapotoa ripoti yake ya utumishi wa shambani kwa mara ya kwanza, kutaniko litatangaziwa kwamba yeye ni mhubiri mpya ambaye hajabatizwa.
KUWASAIDIA VIJANA
13 Watoto wanaweza pia kustahili kuwa wahubiri wa habari njema. Yesu aliwapokea watoto wadogo na kuwabariki. (Mt. 19:13-15; 21:15, 16) Ingawa ni jukumu la wazazi kuwasaidia watoto wao, wengine kutanikoni wanaweza kuwasaidia vijana ambao wamechochewa kushiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Ikiwa wewe ni mzazi, mfano wako mzuri katika huduma ya shambani utawachochea sana watoto wako wamtumikie Mungu kwa bidii. Mtoto ambaye ni mfano mzuri na anayetamani kuonyesha imani yake kwa kuwahubiria wengine habari njema, anaweza kusaidiwaje?
14 Ni vizuri wazazi wazungumze na mmoja wa wazee wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ili kuona ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri. Mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili (mmoja wao akiwa mshiriki wa halmashauri ya utumishi) wakutane na mtoto huyo na mzazi mmoja au wote wawili ambao ni waamini, au mlezi wake. Ikiwa mtoto ana ujuzi wa msingi wa kweli za Biblia na anaonyesha wazi kwamba anataka kushiriki katika utumishi, jambo hilo litathibitisha kwamba amefanya maendeleo. Baada ya kufikiria mambo hayo na mengine yanayowahusu watu wazima, wazee hao wanaweza kuamua ikiwa mtoto huyo anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. (Luka 6:45; Rom. 10:10) Wanapokutana na mtoto, hakuna haja ya kuzungumzia baadhi ya mambo ambayo kwa kawaida yanawahusu watu wazima tu.
15 Wakati wa mazungumzo, wazee wanapaswa kumpongeza mtoto kwa maendeleo yake na kumtia moyo ajitahidi kufikia ubatizo. Kwa kuwa wazazi wamejitahidi kumfundisha mtoto wao kweli, wao pia wanastahili kupongezwa. Ili kuwasaidia wazazi kumsaidia zaidi mtoto wao, wazee wanapaswa kuwaonyesha habari yenye kichwa “Ujumbe kwa Wazazi Wakristo,” kwenye ukurasa wa 179-181.
WAKFU NA UBATIZO
16 Ikiwa umemjua na kumpenda Yehova kwa kupatanisha maisha yako na matakwa yake na kwa kushiriki katika huduma ya shambani, unahitaji kuimarisha uhusiano wako pamoja naye. Jinsi gani? Kwa kujiweka wakfu kwake na kuonyesha wakfu huo kwa kubatizwa katika maji.—Mt. 28:19, 20.
17 Kuweka wakfu humaanisha kutenga kwa ajili ya kusudi takatifu. Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha kusali kwake na kumwahidi kwamba utatumia maisha yako kumtumikia na kutembea katika njia zake. Humaanisha kumwabudu yeye peke yake milele. (Kum. 5:9) Hilo ni jambo la kibinafsi unalofanya faraghani. Hakuna mtu anayeweza kufanya hivyo kwa niaba yako.
18 Hata hivyo, haitoshi tu kumwambia Yehova faraghani kwamba unataka kuwa mali yake. Unahitaji kuwaonyesha wengine kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu. Unafanya hivyo kwa kubatizwa katika maji, kama Yesu alivyofanya. (1 Pet. 2:21; 3:21) Ikiwa umeamua kumtumikia Yehova na unataka kubatizwa, unapaswa kufanya nini? Unapaswa kumwambia mratibu wa baraza la wazee. Atapanga wazee kadhaa wazungumze nawe ili kuhakikisha kwamba unatimiza matakwa ya Mungu kwa ajili ya wale wanaotaka kubatizwa. Kwa habari zaidi, tafadhali soma “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kwenye ukurasa wa 182-184 wa kitabu hiki na “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” kwenye ukurasa wa 185-207.
RIPOTI YA MAENDELEO YA HUDUMA
19 Kwa miaka mingi, ripoti za maendeleo ya ibada safi ulimwenguni pote zimewatia moyo watu wa Yehova. Tangu Yesu Kristo alipowaambia wanafunzi wake kwamba habari njema ingehubiriwa duniani kote, Wakristo wa kweli wametamani sana kujua jinsi ambavyo kazi hiyo ingetimizwa.—Mt. 28:19, 20; Marko 13:10; Mdo. 1:8.
20 Wafuasi wa Yesu walifurahia kusikiliza ripoti za maendeleo ya kazi ya kuhubiri. (Marko 6:30) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinatuambia kwamba kulikuwa na watu 120 hivi roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Muda mfupi baadaye idadi ya wanafunzi iliongezeka hadi 3,000 hivi, kisha 5,000 hivi. Iliripotiwa kwamba ‘Yehova aliendelea kuwaongezea kila siku watu waliokuwa wakiokolewa’ na kwamba “umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 1:15; 2:5-11, 41, 47; 4:4; 6:7) Habari hizo za ongezeko ziliwatia moyo sana wanafunzi! Ripoti hizo zenye kusisimua ziliwachochea kuendelea kufanya kazi waliyopewa na Mungu, licha ya mateso makali yaliyoanzishwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi!
21 Karibu mwaka wa 60 na 61 W.K., Paulo katika barua yake kwa Wakolosai aliandika kwamba habari njema ilikuwa ikizaa “matunda na kuongezeka ulimwenguni kote” na “ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:5, 6, 23) Wakristo wa karne ya kwanza walitii Neno, na roho takatifu iliwatia nguvu kutimiza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kabla ya mfumo wa mambo wa Kiyahudi kufikia mwisho wake mwaka wa 70 W.K. Wakristo hao waaminifu walitiwa moyo kwelikweli kusikia ripoti za matokeo ya kazi hiyo!
Je, unajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja?
22 Vivyo hivyo, tengenezo la Yehova la kisasa hujitahidi kuweka rekodi sahihi za kazi inayofanywa ili kutimiza Mathayo 24:14 inayosema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna kazi inayopaswa kufanywa haraka. Kila mmoja wetu anapaswa ajitahidi kutimiza kikamili huduma kabla ya mwisho kuja. Yehova atahakikisha kwamba kazi hiyo inakamilika, na tukishiriki kuifanya, tutapata kibali chake.—Eze. 3:18-21.
RIPOTI YAKO YA UTUMISHI WA SHAMBANI
23 Tunapaswa kuripoti nini? Fomu ya Ripoti ya Utumishi wa Shambani inayochapishwa na tengenezo ina mambo yanayopaswa kuripotiwa. Hata hivyo, maelezo na ufafanuzi ufuatao, utakusaidia sana.
24 Katika safu ya “Machapisho (Yaliyochapishwa na ya Kielektroniki),” andika jumla ya machapisho yote iwe ni yaliyochapishwa au ya kielektroniki uliyowapa watu ambao si Mashahidi waliobatizwa. Katika safu ya “Video Ambazo Zilionyeshwa” andika jumla ya video zote ambazo ulionyesha.
25 Unaporipoti “Ziara za Kurudia,” jumlisha ziara zote za kurudia ulizofanya kwa kusudi la kuchochea upendezi ulioonyeshwa na mtu ambaye si Shahidi aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Ziara ya kurudia inaweza kufanywa kwa kumtembelea mtu kibinafsi, kwa kuandika barua, kupiga simu, kutuma ujumbe kupitia simu au barua pepe, au kumpelekea chapisho fulani. Kila mara unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani, unaweza kuhesabu ziara ya kurudia. Mzazi anaweza kuhesabu ziara moja ya kurudia kila juma anapoongoza ibada ya familia ikiwa kuna mtoto ambaye hajabatizwa.
26 Ingawa funzo la Biblia huongozwa kila juma, huripotiwa kama funzo moja tu kwa mwezi. Wahubiri wanapaswa kuandika idadi ya mafunzo ya Biblia yaliyoongozwa katika mwezi. Mafunzo ya Biblia ambayo yanaweza kuripotiwa yanatia ndani watu wote ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kuhesabu funzo la Biblia unapojifunza na ndugu au dada asiyetenda unapoombwa na mshiriki wa halmashauri ya utumishi au unapojifunza na mhubiri aliyebatizwa karibuni ambaye hajamaliza kitabu Furahia Maisha Milele!
27 Ni muhimu kutoa ripoti sahihi ya “Saa.” Kwa kawaida huo ni muda unaotumia unapohubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, unapofanya ziara za kurudia, unapoongoza mafunzo ya Biblia, au unapowahubiria rasmi au isivyo rasmi watu ambao si Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa. Wahubiri wawili wanapohubiri pamoja, wote wanaweza kuhesabu saa, lakini mmoja tu ndiye atakayehesabu ziara ya kurudia au funzo la Biblia litakaloongozwa. Wazazi wawili wanaoshirikiana kuwafundisha watoto wao wakati wa Ibada ya Familia wanaweza kuhesabu saa moja kwa juma. Ndugu wanaweza kuhesabu muda wanaotumia kutoa hotuba za watu wote. Mkalimani wa hotuba ya watu wote anaweza pia kuhesabu muda huo. Muda unaotumiwa kwa shughuli nyingine muhimu kama vile, kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani, kuhudhuria mkutano wa utumishi, shughuli za kibinafsi wakati wa utumishi, na kadhalika hauhesabiwi.
28 Kila mhubiri atatumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kusali na kuamua muda aliotumia kutoa ushahidi. Baadhi ya wahubiri wanahubiri katika maeneo yenye watu wengi, na wengine huhubiri katika maeneo yasiyo na watu wengi hivyo wanatumia muda mwingi kusafiri. Maeneo yanatofautiana; maoni ya wahubiri kuhusu huduma yao hutofautiana. Baraza Linaloongoza haliweki sheria jinsi makutaniko yanavyohesabu muda uliotumika katika utumishi wa shambani, wala hakuna mtu aliyeteuliwa ili kuwahukumu wengine kuhusu jambo hilo.—Mt. 6:1; 7:1; 1 Tim. 1:5.
29 Muda unaotumia katika utumishi wa shambani unapaswa kuripotiwa saa nzima-nzima. Hata hivyo, mhubiri asiyejiweza kwa sababu ya uzee, ulemavu, ugonjwa au udhaifu mwingine wowote, anaweza kuripoti utumishi wa dakika 15, 30, na 45. Hata ikiwa alitoa ushahidi kwa dakika 15 tu kwa mwezi, anaweza kuripoti muda huo. Atahesabiwa kuwa mhubiri wa Ufalme anayetenda. Mhubiri ambaye hajiwezi kwa mwezi mmoja au miezi kadhaa, labda kwa sababu ya ugonjwa au jeraha kubwa, anaweza pia kuhusishwa katika mpango huo. Mpango huo unawahusu wale tu wenye udhaifu mkubwa wa kimwili. Halmashauri ya utumishi itaamua ikiwa mhubiri anastahili kuhusishwa katika mpango huo.
REKODI YA KUTANIKO YA MHUBIRI
30 Ripoti yako ya utumishi wa shambani ya kila mwezi huandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri. Rekodi hizo ni za kutaniko unaloshirikiana nalo. Ukitaka kuhamia kutaniko lingine, hakikisha unawajulisha wazee. Mwandishi atahakikisha kwamba rekodi zako zinatumwa kwenye kutaniko unalohamia. Kwa kufanya hivyo, wazee wa kutaniko unalohamia watakukaribisha na wataendelea kukusaidia kiroho. Ikiwa utakuwa mbali na kutaniko lako kwa muda usiozidi miezi mitatu, tafadhali endelea kutuma ripoti yako ya utumishi katika kutaniko lako.
KWA NINI TUNARIPOTI UTUMISHI WETU WA SHAMBANI?
31 Je, nyakati nyingine wewe husahau kutoa ripoti yako ya utumishi wa shambani? Bila shaka sote tunahitaji kukumbushwa mara kwa mara. Lakini tukisitawisha mtazamo unaofaa na tukielewa umuhimu wa kuripoti utumishi wetu wa shambani, inaweza kuwa rahisi kukumbuka kufanya hivyo.
32 Wengine wameuliza: “Kwa kuwa Yehova anajua yale ambayo ninafanya katika utumishi wake, kwa nini nitoe ripoti kutanikoni?” Ni kweli kwamba Yehova anajua yale tunayofanya, naye anajua ikiwa tunamtumikia kwa nafsi yote au tunafanya kidogo kwa kulinganisha na uwezo wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova alirekodi siku ambazo Noa alikaa ndani ya safina na miaka ambayo Waisraeli walisafiri jangwani. Mungu aliweka rekodi ya wale waliokuwa waaminifu na wale ambao hawakutii. Alirekodi jinsi nchi ya Kanaani ilivyotekwa hatua kwa hatua na mambo yaliyotimizwa na waamuzi waaminifu wa Israeli. Naam, alirekodi habari nyingi sana kuhusu matendo ya watumishi wake. Alitumia roho yake kuongoza kuandikwa kwa matukio hayo, na hivyo kutuonyesha umuhimu wa kuandika rekodi sahihi.
33 Matukio ya kihistoria yaliyoandikwa katika Biblia yanaonyesha usahihi wa ripoti na rekodi za watu wa Yehova. Katika visa vingi, masimulizi ya Biblia hayangekuwa yenye kuchochea ikiwa hesabu kamili haingetajwa. Fikiria mifano ifuatayo: Mwanzo 46:27; Kutoka 12:37; Waamuzi 7:7; 2 Wafalme 19:35; 2 Mambo ya Nyakati 14:9-13; Yohana 6:10; 21:11; Matendo 2:41; 19:19.
34 Ingawa ripoti hizo hazionyeshi kila jambo tunalofanya katika utumishi wetu kwa Yehova, zinatimiza kusudi muhimu katika tengenezo la Yehova. Katika karne ya kwanza, baada ya kuhubiri, mitume wa Yesu waliripoti “mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.” (Marko 6:30) Nyakati nyingine, ripoti zinaweza kuonyesha mambo hususa yanayohitaji kushughulikiwa katika sehemu fulani ya huduma yetu. Takwimu zinaweza kuonyesha kama kuna maendeleo katika utendaji fulani, na vilevile ikiwa hakuna ongezeko kubwa la wahubiri. Huenda wahubiri wanahitaji kutiwa moyo au kuna matatizo yanayopaswa kushughulikiwa. Waangalizi wanaohusika watachunguza ripoti hizo na kujitahidi kurekebisha hali yoyote ambayo huenda inazuia maendeleo ya mtu mmoja-mmoja au ya kutaniko lote.
35 Pia, ripoti hulisaidia tengenezo kujua maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Ni maeneo gani yenye matokeo mazuri? Ni maeneo gani yenye ukuzi mdogo? Ni machapisho gani yanayohitajiwa ili kuwasaidia watu wajifunze kweli? Ripoti husaidia tengenezo kujua machapisho yanayohitajiwa katika maeneo mbalimbali ulimwenguni na kisha huhakikisha kwamba yanapatikana.
36 Wengi wetu hutiwa moyo na ripoti. Je, hatusisimuki tunaposikia kuhusu mambo ambayo ndugu zetu wanatimiza wanapohubiri habari njema ulimwenguni pote? Ripoti za ongezeko hutusaidia kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyopanuka. Mambo yaliyoonwa huchangamsha moyo, huzidisha bidii yetu na kutuchochea tushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri. (Mdo. 15:3) Ni muhimu kila mmoja wetu atoe ripoti ya utumishi wa shambani na hilo huonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu ulimwenguni pote. Kupitia jambo hilo dogo tunaonyesha kwamba tunatii mipango ya tengenezo la Yehova.—Luka 16:10; Ebr. 13:17.
KUJIWEKEA MALENGO
37 Hatuna sababu yoyote ya kulinganisha utumishi wetu wa shambani na wa mtu mwingine. (Gal. 5:26; 6:4) Hali za watu hutofautiana sana. Kwa upande mwingine, tunaweza kupata faida nyingi sana tukiweka malengo halisi tunayoweza kufikia ili kupima maendeleo yetu katika huduma. Tukifikia malengo hayo tutaridhishwa na mambo tuliyotimiza.
38 Ni wazi kwamba sasa Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu watakaookoka ile “dhiki kuu.” Tunaishi wakati ambapo unabii huu wa Isaya unatimia: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Ufu. 7:9, 14; Isa. 60:22) Ni heshima kubwa sana kuwa wahudumu wa habari njema katika siku hizi za mwisho!—Mt. 24:14.
-
-
Njia za Kuhubiri Habari NjemaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 9
Njia za Kuhubiri Habari Njema
YESU KRISTO alihubiri habari njema kwa bidii, akiwawekea mfano mzuri wafuasi wake. Alichukua hatua ya kuwatafuta watu, akizungumza nao na kuwafundisha nyumbani kwao na hadharani. (Mt. 9:35; 13:36; Luka 8:1) Yesu alizungumza na watu binafsi, aliwafundisha wanafunzi wake faraghani, na hata alihutubia maelfu ya watu. (Marko 4:10-13; 6:35-44; Yoh. 3:2-21) Alitumia kila pindi aliyopata kuwatia watu moyo na kuwapa tumaini. (Luka 4:16-19) Hakuacha nafasi ya kuhubiri impite hata alipohitaji kupumzika au kula. (Marko 6:30-34; Yoh. 4:4-34) Tunaposoma masimulizi ya huduma ya Yesu yaliyoongozwa na roho, je, hatuchochewi kuiga mfano wake? Bila shaka tunachochewa kumwiga, kama mitume walivyochochewa.—Mt. 4:19, 20; Luka 5:27, 28; Yoh. 1:43-45.
2 Fikiria nafasi ambazo Wakristo wanazo za kushiriki katika kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo miaka 2,000 hivi iliyopita.
KUHUBIRI NYUMBA KWA NYUMBA
3 Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunatambua umuhimu wa kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa utaratibu, yaani, nyumba kwa nyumba. Tumetumia sana njia hiyo hivi kwamba ni alama inayotutambulisha. Faida za kutumia njia hii ili kuwafikia mamilioni ya watu katika muda mfupi zimeonyeshwa pia na ongezeko kubwa tunalopata. (Mt. 11:19; 24:14) Kuhubiri nyumba kwa nyumba hutupatia fursa ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova na jirani zetu.—Mt. 22:34-40.
4 Mahubiri ya nyumba kwa nyumba hayakubuniwa hivi karibuni na Mashahidi wa Yehova. Mtume Paulo alisema kwamba aliwafundisha watu nyumbani kwao. Akiwaeleza waangalizi huko Efeso kuhusu huduma yake, alisema hivi: “Tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, . . . sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha . . . nyumba kwa nyumba.” Kupitia njia hiyo na nyinginezo, Paulo alitoa “ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:18, 20, 21) Wakati huo, watawala Waroma walichochea ibada ya sanamu na watu wengi ‘walionekana kuwa wanaogopa sana miungu.’ Watu walihitaji kumtafuta kwa haraka “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo,” ambaye wakati huo alikuwa “anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.”—Mdo. 17:22-31.
5 Leo kuna uhitaji mkubwa hata zaidi wa kuwapelekea watu habari njema haraka. Mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unakaribia kwa kasi sana. Tunachochewa kuongeza bidii yetu tunapotambua uhitaji huo. Hakuna njia nyingine bora ya kuwatafuta watu wenye njaa ya kiroho kuliko njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ambayo imetumiwa kwa muda mrefu. Bado ina matokeo mazuri leo kama ilivyokuwa katika siku za Yesu na mitume.—Marko 13:10.
6 Je, unashiriki kikamili katika huduma ya nyumba kwa nyumba? Ikiwa ndivyo, uwe na hakika kwamba unamfurahisha Yehova. (Eze. 9:11; Mdo. 20:35) Huenda isiwe rahisi kwako kuhubiri nyumba kwa nyumba. Labda una udhaifu wa kimwili au watu wengi katika eneo lenu hawataki kusikiliza. Au kuna vizuizi vya serikali. Huenda wewe ni mwenye haya, na unaogopa kuzungumza na watu usiowafahamu. Kwa sababu hiyo, kila mara unapohubiri nyumba kwa nyumba unakuwa na wasiwasi. Usikate tamaa. (Kut. 4:10-12) Ndugu zako pia wanakabili hali kama hizo katika maeneo mengine.
7 Yesu aliwaahidi wanafunzi wake hivi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Ahadi hiyo hutuimarisha tunapofanya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Tunahisi kama mtume Paulo aliyesema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.” (Flp. 4:13) Unga mkono kikamili mipango ya kutaniko ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Unapohubiri na wengine, watakutia moyo na kukusaidia kuboresha ustadi wako. Sali ili ushinde vizuizi ambavyo huenda ukakabili, na ujitahidi kuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii.—1 Yoh. 5:14.
8 Unapowatangazia wengine habari njema, utapata nafasi za kuwaeleza ‘sababu ya tumaini ulilo nalo.’ (1 Pet. 3:15) Utafahamu vizuri zaidi tofauti kati ya wale walio na tumaini la Ufalme na wale wasio na tumaini. (Isa. 65:13, 14) Utaridhika kwa kujua kwamba umetii amri ya Yesu ya ‘kuacha nuru yako iangaze,’ na huenda hata ukawa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue Yehova na wapate kweli inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mt. 5:16; Yoh. 17:3; 1 Tim. 4:16.
9 Mipango hufanywa ili kuhubiri nyumba kwa nyumba katikati ya juma na pia mwisho juma. Makutaniko fulani hupanga kuhubiri jioni katika maeneo ambayo ni vigumu kuwapata watu nyumbani mchana. Huenda watu wakawa tayari kuwakaribisha wageni alasiri au jioni badala ya asubuhi.
KUWATAFUTA WALE WANAOSTAHILI
10 Yesu aliwaagiza wanafunzi wake ‘wawatafute’ wale wanaostahili. (Mt. 10:11) Hakuwatafuta watu wenye mwelekeo unaofaa kwa kuhubiri tu nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, alitumia kila nafasi aliyopata ili kuhubiri rasmi au isivyo rasmi. (Luka 8:1; Yoh. 4:7-15) Pia, mitume waliwahubiria watu katika maeneo mbalimbali.—Mdo. 17:17; 28:16, 23, 30, 31.
Lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana
11 Vivyo hivyo, lengo letu ni kumpelekea kila mtu ujumbe wa Ufalme inapowezekana. Hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kuiga njia ambazo Yesu na wanafunzi wake walitumia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha na vilevile kubadilikana kulingana na nyakati na hali za watu katika eneo letu. (1 Kor. 7:31) Kwa mfano, wahubiri wamefanikiwa kuwapata watu katika sehemu zao za biashara. Katika nchi nyingi, wahubiri wamepata matokeo kwa kuhubiri barabarani, bustani za kupumzikia, maegesho ya magari, au popote pale watu wanapopatikana. Makutaniko fulani yamepanga kuhubiri kwa kutumia meza au vigari vyenye machapisho katika eneo lao. Isitoshe, ofisi ya tawi inaweza kupanga mahubiri ya pekee ya hadharani katika barabara zenye watu wengi sana katika majiji, kwa kutumia wahubiri wa makutaniko mbalimbali. Matokeo ni kwamba watu wasiopatikana nyumbani wanaweza kupata habari njema mahali pengine.
12 Tunapokutana na watu wanaopendezwa na ujumbe wa Biblia katika maeneo ya umma, tunaweza kuwapa chapisho linalowafaa. Ili kusitawisha upendezi, unaweza kumpa anwani au namba yako ya simu na kupanga kumrudia, au umwonyeshe tovuti ya jw.org, au umwelekeze kwenye eneo lililo karibu naye ambapo mikutano ya kutaniko hufanywa. Huenda kuwahubiria watu katika maeneo ya umma ikawa njia nzuri ya kupanua huduma yako na utakayofurahia.
13 Hata hivyo, kazi ya Wakristo leo haihusu tu kutangaza habari njema. Ili ufanikiwe kuwasaidia wengine waikubali kweli inayoongoza kwenye uzima, unahitaji kuwarudia tena na tena watu waliopendezwa ili wafanye maendeleo na kuwa Wakristo wakomavu.
KUFANYA ZIARA ZA KURUDIA
14 Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Lakini pia aliwaambia: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mt. 28:19, 20) Unaweza kupata shangwe katika utumishi wa Yehova ukifanya ziara za kurudia. Huenda watu uliowahubiria habari njema wakafurahi ukiwatembelea tena. Unapozungumza nao habari zaidi kuhusu Biblia, unaweza kuimarisha imani yao katika Mungu na kuwasaidia kutambua uhitaji wao wa kiroho. (Mt. 5:3) Ukipanga kurudi wakati unaofaa na ukijitayarisha vizuri, huenda ukaanzisha funzo la Biblia. Unapaswa kuwa na lengo hilo unapofanya ziara za kurudia. Sisi hupanda mbegu ya kweli na vilevile kuitia maji.—1 Kor. 3:6.
15 Huenda ikawa vigumu kwa wengine kufanya ziara za kurudia. Labda umezoea kuhubiri kifupi habari njema na unafurahia kufanya hivyo. Lakini huenda ukaogopa kumrudia mwenye nyumba ili kuendeleza mazungumzo ya Biblia. Matayarisho mazuri yatakusaidia kuwa na ujasiri. Tumia mapendekezo yanayotolewa katika mkutano wa katikati ya juma. Pia, unaweza kupanga kuhubiri na mhubiri mwenye uzoefu ili akusaidie.
KUONGOZA MAFUNZO YA BIBLIA
16 Alipokuwa akizungumza na mtu aliyegeuzwa imani na kuwa Myahudi ambaye alikuwa akisoma Neno la Mungu, mweneza-injili Filipo alimwuliza hivi: “Je, kweli unajua unayosoma?” Mwanamume huyo alijibu: “Kwa kweli, ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?” Masimulizi ya Biblia kwenye Matendo sura ya 8 yanaeleza kwamba Filipo ‘alimtangazia habari njema kumhusu Yesu,’ akianza na andiko ambalo mtu huyo alikuwa akisoma. (Mdo. 8:26-36) Hatujui Filipo alizungumza naye kwa muda gani, lakini Filipo alimweleza waziwazi habari njema hivi kwamba mtu huyo akaamini na akaomba kubatizwa. Kisha akawa mwanafunzi wa Yesu Kristo.
17 Watu wengi leo hawajui mafundisho ya Biblia, na huenda tukahitaji kuwarudia mara nyingi na kujifunza nao kwa majuma au miezi kadhaa, au hata mwaka mmoja au zaidi ili wawe na imani na wastahili kubatizwa. Hata hivyo, ukiwasaidia kwa subira na upendo watu wanyofu wawe wanafunzi, utapata thawabu kama Yesu alivyosema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Mdo. 20:35.
18 Bila shaka, ungependa kuongoza funzo la Biblia ukitumia machapisho yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo. Kwa kutumia maagizo yanayotolewa kwenye mkutano wa katikati ya juma na kwa kuhubiri na walimu wenye uzoefu kutanikoni, utafaulu kuongoza mafunzo yenye matokeo, na kuwasaidia wengine wawe wanafunzi wa Yesu Kristo.
19 Ikiwa unahitaji kusaidiwa kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia, zungumza na mzee yeyote au Shahidi mwenye ustadi wa kuongoza mafunzo ya Biblia. Mapendekezo yanayopatikana katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha na ambayo huzungumziwa kwenye mkutano huo yatakusaidia pia. Mtegemee Yehova na usali kuhusu tamaa yako ya kuongoza funzo. (1 Yoh. 3:22) Kwa hiyo, jitahidi kuongoza angalau funzo moja la Biblia mbali na funzo ambalo huenda unaongoza katika familia yako. Ukiongoza mafunzo ya Biblia, utapata shangwe zaidi katika huduma.
KUWAELEKEZA WANAOPENDEZWA KWENYE TENGENEZO LA YEHOVA
20 Tunapowasaidia watu wamjue Yehova Mungu na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, wanajiunga na kutaniko. Wanafunzi wa Biblia watafanya maendeleo ya kiroho na kukomaa ikiwa watalifahamu tengenezo la Yehova na kushirikiana nalo. Ni muhimu tuwafundishe jinsi ya kufanya hivyo. Unaweza kuwasaidia kwa kutumia broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? na video zilizotayarishwa kwa kusudi hilo. Unaweza pia kutumia habari iliyo katika Sura ya 4 ya kitabu hiki.
21 Mara tu mnapoanza kujifunza Biblia, msaidie mwanafunzi aone kwamba Yehova anatumia tengenezo kutimiza kazi ya kuhubiri inayoendelea duniani. Mweleze faida za machapisho ya kujifunzia Biblia na jinsi yanavyotayarishwa na kusambazwa ulimwenguni pote na wafanyakazi wa kujitolea ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu. Mwalike mwanafunzi wako wa Biblia mwende pamoja kwenye Jumba la Ufalme. Mweleze jinsi mikutano inavyofanywa na umtambulishe kwa akina ndugu na dada. Msaidie pia afahamiane na Mashahidi wengine kwenye makusanyiko. Katika pindi hizo, mwache mwanafunzi ajionee jinsi waabudu wa Yehova wanavyopendana, jambo linalowatambulisha Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:35) Mtu anayependezwa akiendelea kulithamini tengenezo la Yehova, atazidi kumkaribia Yehova.
KUTUMIA MACHAPISHO YA BIBLIA
22 Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kwa bidii Neno la Mungu. Walinakili kwa mkono Maandiko waliyotumia kujifunza wao binafsi na kutanikoni. Waliwahimiza watu wasome Neno la Mungu la kweli. Nakala walizonakili zilikuwa chache na hivyo walizithamini sana. (Kol. 4:16; 2 Tim. 2:15; 3:14-17; 4:13; 1 Pet. 1:1) Leo, Mashahidi wa Yehova hutumia mbinu za kisasa kuchapisha mamia ya mamilioni ya Biblia na machapisho ya kujifunzia Biblia. Machapisho hayo yanatia ndani trakti, broshua, vitabu, na magazeti katika lugha nyingi.
23 Unapowahubiria wengine habari njema, tumia machapisho ya kujifunzia Biblia yanayoandaliwa na tengenezo la Yehova. Unapotafakari jinsi ambavyo umefaidika kwa kusoma na kujifunza machapisho ya Mashahidi wa Yehova, utachochewa kuwapa wengine pia.—Ebr. 13:15, 16.
24 Watu wengi sana hutegemea kupata habari katika Intaneti. Kwa hiyo, mbali na machapisho ya Biblia, tovuti yetu rasmi ya jw.org ni njia nyingine nzuri ya kutangaza habari njema. Watu ulimwenguni pote wanaweza kutumia kompyuta zao kusoma au kusikiliza Biblia na machapisho ya Biblia yakisomwa katika mamia ya lugha. Watu wanaosita kuzungumza nasi au wanaoishi katika maeneo ambayo hayana Mashahidi wengi wa Yehova wanaweza kuchunguza mambo tunayoamini kwa kutumia jw.org wakiwa nyumbani kwao.
25 Kwa hiyo, tunawajulisha watu kuhusu jw.org kila tunapopata fursa. Mwenye nyumba anapouliza swali kuhusu imani yetu, tunaweza kutumia simu au kompyuta kumwonyesha jibu papo hapo. Tunapokutana na mtu anayezungumza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama, tunaweza kumwelekeza kwenye tovuti yetu ili asome Biblia na machapisho ya Biblia katika lugha yake. Wahubiri wengi wametumia mojawapo ya video zilizo kwenye tovuti hiyo kuanzisha mazungumzo ya Biblia.
MAHUBIRI YASIYO RASMI
26 Yesu aliwaambia hivi wale waliokuwa wakimsikiliza: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu. . . . Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:14-16) Wanafunzi hao waliishi kulingana na viwango vya Mungu kwa kumwiga Yesu aliyesema: “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.” Yesu aliwawekea Wakristo mfano kwa kuacha “nuru ya uzima” iangaze kwa faida ya wote ambao wangesikiliza.—Yoh. 8:12.
27 Mtume Paulo pia alituwekea mfano mzuri. (1 Kor. 4:16; 11:1) Alipokuwa Athene, kila siku aliwahubiria watu aliokutana nao sokoni. (Mdo. 17:17) Wakristo huko Filipi waliiga mfano wake. Kwa sababu hiyo, Paulo aliwaandikia hivi: Mnaishi “katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka, ambao kati yao mnaangaza kama mianga katika ulimwengu.” (Flp. 2:15) Sisi pia tunaweza kuacha kweli ya Ufalme iangaze kupitia maneno na matendo yetu tunapopata nafasi ya kuwaambia wengine habari njema. Ni kweli kwamba mfano wetu mzuri wa kuwa wanyofu na waadilifu unaweza kuonyesha sisi ni tofauti na ulimwengu. Hata hivyo, tukizungumza na watu kuhusu habari njema, watajua sababu inayotufanya tuwe tofauti.
28 Mashahidi wengi wa Yehova huwahubiria habari njema watu wanaokutana nao kila siku kazini, shuleni, kwenye usafiri wa umma, au katika shughuli zao za kila siku. Tunaposafiri, tunaweza kuzungumza na wasafiri wenzetu. Kila mmoja wetu anapaswa kuwa tayari kutoa ushahidi katika mazungumzo yoyote ya kawaida. Acheni tuwe tayari kuzungumza na wengine wakati wowote.
29 Tutachochewa kuzungumza na wengine tukikumbuka kwamba kwa kufanya hivyo tunamsifu Muumba wetu na kuliheshimu jina lake. Isitoshe, tunaweza kuwasaidia watu wenye moyo mnyoofu wamjue Yehova ili wao pia wamtumikie na kuwa na tumaini la kupata uzima kwa msingi wa imani katika Yesu Kristo. Yehova hupendezwa sana na jitihada hizo na kuuona huo kuwa utumishi mtakatifu.—Ebr. 12:28; Ufu. 7:9,10.
ENEO
30 Mapenzi ya Yehova ni kwamba ujumbe wa Ufalme uhubiriwe kwa utaratibu ulimwenguni pote, mijini na vijijini. Ili kutimiza hilo, makutaniko na watu binafsi wanaohubiri maeneo ya mbali hupewa eneo na ofisi ya tawi. (1 Kor. 14:40) Hilo linapatana na mpango wa Mungu uliofuatwa katika karne ya kwanza. (2 Kor. 10:13; Gal. 2:9) Kazi ya kuhubiri Ufalme inapopanuka haraka katika siku hizi za mwisho, tutapata matokeo mazuri ikiwa kuna utaratibu mzuri wa kuhubiri maeneo ya kutaniko.
31 Mwangalizi wa utumishi ndiye anayesimamia mipango hiyo. Mtumishi wa huduma anaweza kuwagawia wahubiri maeneo. Kuna aina mbili za maeneo, maeneo ya vikundi na maeneo ya kibinafsi ya wahubiri. Katika kutaniko lenye eneo dogo, waangalizi wa vikundi huwa na maeneo ambayo huhubiriwa na wahubiri wa vikundi vyao. Katika kutaniko lenye eneo kubwa, wahubiri wanaweza kupewa eneo la kibinafsi.
32 Mhubiri aliye na eneo la kibinafsi anaweza kuhubiri eneo hilo wakati ambapo hakuna mpango wa mkutano wa utumishi wa shambani au kama hawezi kufika kwenye kikundi. Kwa mfano, wahubiri fulani huchukua eneo lililo karibu na mahali wanapofanya kazi nao huhubiri wakati wa mapumziko ya mchana au baada ya kazi. Familia fulani huchukua eneo la kibinafsi karibu na nyumbani kwao na kuhubiri wakati wa jioni. Kuwa na eneo la kibinafsi lililo karibu humsaidia mhubiri atumie wakati mwingi zaidi katika utumishi wa shambani. Eneo la kibinafsi linaweza pia kuhubiriwa na kikundi. Kama ungependa kuwa na eneo la kibinafsi unaweza kumwomba mtumishi wa maeneo.
33 Iwe ni eneo la kikundi lililopewa mwangalizi wa kikundi au eneo la kibinafsi lililopewa mhubiri, mtu aliyepewa eneo hilo atajitahidi kadiri awezavyo kuzungumza na mtu fulani katika kila nyumba. Mipango ya kuhubiri eneo kikamili inapaswa kufuata sheria za kulinda taarifa zinazotumiwa. Kila mwangalizi wa kikundi au mhubiri anayepewa eneo anapaswa kujitahidi kulikamilisha kwa miezi minne. Mara tu anapomaliza, anapaswa kumjulisha mtumishi wa maeneo. Ikitegemea na hali, mwangalizi wa kikundi au mhubiri anaweza kubaki na eneo hilo ili alihubiri tena au anaweza kumrudishia mtumishi wa maeneo.
34 Wahubiri wote kutanikoni wakishirikiana, eneo linaweza kuhubiriwa kikamili. Pia, eneo moja halitahubiriwa na wahubiri tofauti-tofauti wakati uleule, jambo linaloweza kuwaudhi wenye nyumba. Tukifanya hivyo, tutaonyesha kwamba tunawajali ndugu zetu na watu walio katika eneo.
KUSHIRIKIANA KUWAHUBIRIA WATU WA KILA LUGHA
35 Wanadamu wote wanahitaji kujifunza kumhusu Yehova Mungu, Mwana wake, na Ufalme. (Ufu. 14:6, 7) Tungependa kuwasaidia watu wa lugha zote waliitie jina la Yehova ili waokolewe na wavae utu mpya wa Kikristo. (Rom. 10:12, 13; Kol. 3:10, 11) Tunakabili changamoto gani tunapohubiri maeneo yenye watu wanaozungumza lugha mbalimbali? Tunawezaje kukabiliana na hali hizo ili watu wengi iwezekanavyo wasikie ujumbe wa Ufalme katika lugha wanayoelewa vizuri?—Rom. 10:14.
36 Maeneo hupangwa kulingana na lugha. Kwa hiyo, wahubiri wa makutaniko yenye maeneo ya lugha tofauti-tofauti wanaweza kuhubiri eneo lilelile. Katika maeneo hayo, ni vizuri wahubiri wa kila kutaniko wajitahidi kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kutaniko lao. Hilo linahusika pia wakati wa kampeni za kila mwaka za kugawa mialiko. Hata hivyo, wahubiri wanapohubiri hadharani na isivyo rasmi, wanaweza kuzungumza na mtu yeyote na kutoa machapisho ya lugha yoyote.
37 Katika visa fulani, makutaniko ya lugha tofauti yanaweza kushindwa kuhubiri kikamili maeneo yao kwa ukawaida. Katika visa kama hivyo, waangalizi wa utumishi wa makutaniko yanayohusika wanapaswa kuwasiliana ili kupanga utaratibu unaofaa wa kuhubiri eneo lote. Hilo litampa kila mtu nafasi ya kusikia ujumbe wa Ufalme na kuzuia makutaniko tofauti kuhubiri eneo lilelile kwa wakati mmoja.—Met. 15:22.
38 Tunapaswa kufanya nini ikiwa mwenye nyumba anazungumza lugha tofauti? Tusifikiri kwamba wahubiri wanaozungumza lugha yake watamtembelea. Wahubiri fulani wamejifunza utangulizi mfupi wa lugha zinazozungumzwa katika eneo lao. Tunaweza kumwonyesha mtu jinsi ya kusoma au kupakua machapisho ya lugha yake kwenye tovuti yetu rasmi ya jw.org, au tunaweza kupanga kumletea machapisho ya lugha yake.
39 Mwenye nyumba akionyesha upendezi, tunapaswa kujaribu kumtafuta mhubiri anayezungumza lugha anayoelewa. Pia tunaweza kumwelekeza kwenye kutaniko la karibu linalofanya mikutano kwa lugha yake. Ikiwa anapenda kuwasiliana na mhubiri anayezungumza lugha yake, tunaweza kumwelekeza jinsi ya kujaza habari zake za mawasiliano kwenye Tovuti ya jw.org. Kisha, ofisi ya tawi itajitahidi kupata mhubiri aliye karibu, kikundi, au kutaniko linaloweza kumsaidia zaidi.
40 Tunapaswa kuendelea kumtembelea mtu huyo anayependezwa mpaka atakapotembelewa na mhubiri anayezungumza lugha yake. Katika visa fulani, huenda ofisi ya tawi ikawajulisha wazee kwamba hawakumpata mhubiri anayezungumza lugha ya mtu huyo. Ikiwa ndivyo, tunapaswa kujitahidi kuendeleza upendezi wa mwenye nyumba. Ikiwezekana tunaweza kujifunza naye Biblia, labda kwa kutumia machapisho ya lugha yake. Tukitumia vizuri picha na kumwomba mtu huyo asome maandiko yaliyonukuliwa, atapata ujuzi fulani wa msingi wa Biblia. Labda ana mtu wa ukoo anayejua lugha yake na lugha ya kutaniko ambaye anaweza kumtafsiria ujumbe.
41 Ili kumwelekeza mtu anayependezwa kwenye tengenezo la Mungu, tunapaswa kumwalika ahudhurie mikutano yetu, ingawa huenda asielewe kikamili mambo yanayozungumziwa. Maandiko yanaposomwa, tunaweza kumsaidia kuyapata katika Biblia ya lugha yake ikiwa inapatikana. Anaposhirikiana na wengine kutanikoni, anaweza kuimarishwa na kusaidiwa kufanya maendeleo zaidi ya kiroho.
42 Vikundi vidogo: Kikundi kidogo hufanyizwa na wahubiri wanaotumia lugha tofauti na ile inayotumiwa na kutaniko lao, ingawa hakuna mzee au mtumishi wa huduma anayestahili kuongoza mikutano katika lugha hiyo kila juma. Ofisi ya tawi inaweza kutambua kutaniko kuwa linalosimamia kikundi kidogo ikiwa matakwa yafuatayo yametimizwa:
(1) Kuna idadi ya kutosha ya watu katika eneo ambao wanazungumza lugha nyingine tofauti na lugha ya kutaniko.
(2) Angalau kuna wahubiri wachache wanaojua au wako tayari kujifunza lugha hiyo.
(3) Baraza la wazee liko tayari kuongoza mipango ya mahubiri katika lugha hiyo.
Ikiwa baraza la wazee liko tayari kusimamia kikundi kidogo, wazee wanapaswa kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko. Huenda anajua makutaniko mengine yanayojitahidi kuwahubiria watu wa lugha hiyo na anaweza kuandaa habari muhimu itakayowasaidia kujua kutaniko linaloweza kusimamia kikundi hicho kidogo kwa njia bora zaidi. Baada ya kuamua ni kutaniko gani litakalosimamia, wazee wanaweza kuandika barua kwa ofisi ya tawi na kuomba idhini ya kutambuliwa rasmi kama kutaniko linalosimamia kikundi kidogo.
43 Vikundi: Ofisi ya tawi inaweza kutambua kutaniko kuwa linalosimamia kikundi ikiwa matakwa yafuatayo yametimizwa:
(1) Kuwe na idadi ya kutosha ya watu wanaopendezwa na uwezekano wa ongezeko katika eneo la lugha hiyo.
(2) Angalau idadi ndogo ya wahubiri wanaozungumza au wanaojifunza lugha hiyo.
(3) Mzee au mtumishi wa huduma anayestahili anapatikana ili kusimamia na kuongoza angalau mkutano mmoja katika juma—au sehemu ya mkutano wa kila juma, kama vile hotuba ya watu wote au Funzo la Mnara wa Mlinzi—katika lugha hiyo.
Matakwa hayo yanapotimizwa kwa kiwango kinachofaa, baraza la wazee litaandikia ofisi ya tawi barua yenye habari kamili na kuomba kutambuliwa rasmi kuwa kutaniko linalosimamia kikundi. Mzee au mtumishi wa huduma anayesimamia kikundi hicho ataitwa “mwangalizi wa kikundi” au “mtumishi wa kikundi” akiwa na jukumu la kutunza kikundi hicho.
44 Baada ya kikundi kuanzishwa, baraza la wazee la kutaniko linalosimamia kikundi hicho litaamua ikiwa sehemu nyingine za mikutano ya kutaniko zinapaswa kuongezwa na ni mara ngapi kwa mwezi zinapaswa kufanywa. Mikutano ya utumishi wa shambani inaweza pia kupangwa kwa ajili ya kikundi hicho. Washiriki wote watakuwa chini ya usimamizi wa baraza la wazee linalotegemeza kikundi hicho. Wazee watatoa mwongozo wenye usawaziko na kuchukua hatua zifaazo ili kushughulikia mahitaji ya kikundi hicho. Mwangalizi wa mzunguko anapohubiri pamoja na kikundi hicho katika juma la ziara yake kwa kutaniko linalotegemeza, ataandikia ofisi ya tawi ripoti fupi kuhusu maendeleo ya kikundi hicho na kutaja mahitaji hususa. Baada ya muda, huenda kikundi hicho kikastahili kuwa kutaniko. Ikiwa wote wanaohusika wanafuata miongozo ya kitheokrasi, Yehova atafurahi.—1 Kor. 1:10; 3:5, 6.
MAHUBIRI YA VIKUNDI
45 Kila Mkristo aliyejiweka wakfu ana wajibu wa kuwahubiria wengine habari njema. Kuna njia nyingi za kufanya hivyo, lakini wengi wetu hufurahia kuhubiri pamoja na wahubiri wengine. (Luka 10:1) Kwa hiyo, makutaniko hukutana kwa ajili ya utumishi wa shambani katika mwisho juma na pia katikati ya juma. Kunapokuwa na sikukuu, tunapata pia nafasi za kuhubiri tukiwa kikundi, kwa kuwa ndugu wengi hawaendi kazini. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko hupanga mahali pa mikutano ya utumishi wa shambani na wakati unaowafaa wengi wakati wa mchana na jioni.
46 Mahubiri ya vikundi huwasaidia wahubiri kufanya kazi pamoja na hivyo ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:12) Wahubiri wapya wanaweza kuhubiri na wahubiri wenye ustadi na uzoefu ili wasaidiwe. Katika maeneo fulani huenda ikawa jambo la hekima kwa wahubiri wawili au zaidi kuhubiri pamoja kwa sababu ya usalama. Hata ikiwa unapanga kuhubiri peke yako katika eneo, kukutana na wengine katika kikundi kunaweza kuwatia moyo. Kujua tu kwamba wengine wanahubiri katika eneo lilelile kunaweza kukupa ujasiri. Mapainia na wengine hawapaswi kuhisi kwamba ni lazima wahudhurie kila mkutano wa utumishi wa shambani uliopangwa na kutaniko, hasa ikiwa mikutano hiyo hufanywa kila siku. Hata hivyo, inaelekea kwamba wanaweza kuunga mkono angalau mikutano kadhaa ya utumishi wa shambani kila juma.
47 Acheni sote tuige mfano uliowekwa na Yesu na mitume wake! Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kushiriki kikamili katika kazi muhimu ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Luka 9:57-62.
-
-
Njia za Kupanua Huduma YakoTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 10
Njia za Kupanua Huduma Yako
YESU alipowaagiza wanafunzi wake wahubiri Ufalme, aliwaambia hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.” Kulikuwa na kazi nyingi, basi akaongeza hivi: “Mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo ya kutimiza huduma yao. Alionyesha umuhimu wa kazi hiyo aliposema: “Hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.”—Mt. 10:23.
2 Leo pia, kuna kazi nyingi ya kufanya katika huduma ya shambani. Lazima habari njema ya Ufalme ihubiriwe kabla ya mwisho kuja, na muda unayoyoma! (Marko 13:10) Kwa kuwa shamba ni ulimwengu, tunakabili hali kama ya Yesu na wanafunzi wake, ingawa kwa kiwango kikubwa zaidi. Idadi yetu ni ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya wanadamu ulimwenguni, lakini tuna hakika kwamba Yehova atatusaidia. Habari njema ya Ufalme itahubiriwa ulimwenguni pote, na wakati uliowekwa na Yehova utakapofika, mwisho utakuja. Je, tutatanguliza Ufalme wa Mungu maishani ili tutimize huduma yetu kikamili? Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kitheokrasi?
3 Akieleza matakwa ya Yehova kwa watumishi wake waliojiweka wakfu, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Tunapaswa kumtumikia Mungu kwa nafsi yote. Hilo linamaanisha kuwa tunaonyesha kwamba tumejiweka wakfu na tumejitoa kikamili kwa kufanya yote tunayoweza katika utumishi wa Yehova. (2 Tim. 2:15) Kila mmoja wetu anaweza kupanua utumishi wake katika njia mbalimbali ikitegemea hali na uwezo wake. Hebu fikiria baadhi ya njia hizo, na uamue malengo ya kitheokrasi unayoweza kujiwekea unapotimiza huduma yako.
KUWA MHUBIRI WA KUTANIKO
4 Wote wanaokubali kweli wana pendeleo la kutangaza habari njema. Hiyo ndiyo kazi kuu ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Kwa kawaida, mwanafunzi wa Yesu Kristo huanza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema mara tu anaposikia ujumbe huo. Hivyo ndivyo Andrea, Filipo, Kornelio, na wengine walivyofanya. (Yoh. 1:40, 41, 43-45; Mdo. 10:1, 2, 24; 16:14, 15, 25-34) Je, inamaanisha kwamba mtu anaweza kuzungumza na wengine kuhusu habari njema kabla hajabatizwa? Ndiyo! Mara tu mtu anapostahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa kutanikoni, anaweza kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Anaweza pia kushiriki katika sehemu mbalimbali za huduma ikitegemea hali na uwezo wake.
5 Mhubiri anapobatizwa, bila shaka yuko tayari kufanya yote anayoweza ili awasaidie wengine wajifunze habari njema. Wanaume na wanawake wana pendeleo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Ni pendeleo kushiriki hata kwa sehemu ndogo katika kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, tukipanua huduma yetu na kufikia mapendeleo zaidi ya utumishi tutakuwa na furaha sana.
KUTUMIKIA KATIKA MAENEO YENYE UHITAJI MKUBWA
6 Huenda eneo la kutaniko lenu huhubiriwa kwa ukawaida na ushahidi mzuri unatolewa. Ikiwa ndivyo, huenda ukahisi kwamba unaweza kupanua huduma yako kwa kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. (Mdo. 16:9) Ikiwa unatumikia ukiwa mzee au mtumishi wa huduma, huenda kuna kutaniko lingine ambalo litathamini msaada wako. Mwangalizi wenu wa mzunguko anaweza kukupendekezea jinsi ya kusaidia kutaniko lingine katika mzunguko wenu. Ikiwa ungependa kutumikia katika eneo lingine nchini kwenu, ofisi ya tawi inaweza kukupatia habari zaidi.
7 Je, ungependa kutumikia katika nchi nyingine? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufikiria jambo hilo kwa makini. Kwa nini usizungumzie jambo hilo na wazee wa kutaniko lenu? Bila shaka, hilo litakuwa badiliko kubwa kwako na kwa wale watakaoenda nawe. (Luka 14:28) Hata hivyo, ikiwa hukusudii kukaa kwa muda mrefu, huenda ikafaa ufikirie kutumikia katika eneo lililo nchini kwenu.
8 Katika nchi fulani, ndugu wanaosimamia kazi ni wapya katika kweli. Kwa unyenyekevu, ndugu wenyeji wako tayari kuwaachia wazee wenye uzoefu wanaohamia katika makutaniko yao waongoze mambo. Ikiwa wewe ni mzee na unafikiria kuhamia katika nchi kama hizo, kumbuka kwamba lengo lako si kuchukua mapendeleo ya ndugu wenyeji. Badala yake, tumikia pamoja nao. Watie moyo wafanye maendeleo na wakubali majukumu kutanikoni. (1 Tim. 3:1) Uwe na subira ikiwa mambo fulani hayafanywi kama yanavyofanywa katika nchi yenu. Tumia uzoefu wako ukiwa mzee kuwasaidia akina ndugu. Kisha, ikiwa wakati fulani utalazimika kurudi katika nchi yenu, wazee wenyeji watakuwa na uwezo wa kusimamia kutaniko.
9 Kabla ofisi ya tawi haijakupa majina ya makutaniko yanayoweza kufaidika na msaada wako, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lenu itahitaji kutuma barua ya kukupendekeza. Barua hiyo inahitajiwa hata kama wewe ni mzee, mtumishi wa huduma, painia, au mhubiri. Halmashauri ya utumishi itatuma barua ya kukupendekeza pamoja na ombi lako moja kwa moja kwenye ofisi ya tawi ya nchi unayotaka kutumikia.
KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINE
10 Ili upanue huduma yako, huenda ukafikiria kujifunza lugha nyingine, kutia ndani lugha ya alama. Kama una lengo la kujifunza kuhubiri katika lugha nyingine, unaweza kuzungumza na wazee na mwangalizi wa mzunguko. Wanaweza kukupa madokezo na kukutia moyo. Kupitia mwelekezo wa ofisi ya tawi, mizunguko fulani imepanga madarasa ya lugha ili kuwazoeza wahubiri wenye uwezo na mapainia kuhubiri katika lugha nyingine.
UTUMISHI WA PAINIA
11 Wahubiri wote wanapaswa kujua matakwa ya msingi ya utumishi wa painia msaidizi, wa kawaida, na wa pekee na pia utumishi mwingine wa wakati wote. Painia anapaswa kuwa Mkristo aliyebatizwa mwenye mfano mzuri ambaye hali zake zinamruhusu kutumia saa hususa kuhubiri habari njema. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko huidhinisha maombi ya utumishi wa upainia msaidizi na wa kawaida, nayo ofisi ya tawi huweka rasmi mapainia wa pekee.
12 Mhubiri anaweza kuwa painia msaidizi kwa angalau mwezi mmoja, miezi kadhaa mfululizo, au kwa kuendelea, ikitegemea hali zake. Wahubiri wengi wa Ufalme hufanya upainia msaidizi katika pindi za pekee, kama vile majira ya Ukumbusho au mwezi wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Wengine huamua kuwa mapainia wakati wa likizo. Wahubiri waliobatizwa wanaosoma wanaweza kujiandikisha kuwa mapainia wasaidizi shule zinapofungwa. Wahubiri wanaweza kuchagua kuwa mapainia wasaidizi kwa punguzo la takwa la saa kila mwezi wa Machi na Aprili na mwezi wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Hata hali zako ziweje, ikiwa una maadili mazuri, ikiwa unaweza kupanga kutimiza takwa lililowekwa la saa, na unaamini kwamba unaweza kutumikia kwa mwezi mmoja au zaidi ukiwa painia msaidizi, wazee watafurahia kufikiria ombi lako la kushiriki katika pendeleo hilo la utumishi.
13 Ili ustahili kuwa painia wa kawaida, unapaswa kuwa na uwezo wa kutimiza takwa la saa kwa mwaka. Ukiwa painia wa kawaida, unapaswa kushirikiana kwa ukaribu na kutaniko lenu. Mapainia wenye bidii ni baraka kutanikoni, huwachochea wahubiri washiriki katika huduma ya shambani na hata kuwatia moyo wawe mapainia. Hata hivyo, kabla ya kujaza ombi la kuwa painia wa kawaida, lazima uwe umebatizwa angalau miezi sita iliyopita na uwe mhubiri mwenye mfano mzuri.
14 Kwa kawaida mapainia wa pekee huchaguliwa kati ya mapainia wa kawaida ambao wamekuwa na matokeo mazuri katika huduma. Lazima wawe na hali zitakazowaruhusu kutumikia popote ambapo ofisi ya tawi itawatuma. Mara nyingi wao hutumwa kwenye maeneo ya mbali ili watafute watu wanaopendezwa na kuanzisha makutaniko mapya. Nyakati nyingine, mapainia wa pekee hutumwa kwenye makutaniko yanayohitaji kusaidiwa kuhubiri eneo lao kubwa. Baadhi ya mapainia wa pekee ambao pia ni wazee hutumwa ili kusaidia makutaniko madogo, hata yasiyo na uhitaji hususa wa kuhubiri. Mapainia wa pekee hupokea pesa kidogo ili kugharimia mahitaji yao. Baadhi ya mapainia wa pekee huwekwa rasmi kwa muda.
WAMISHONARI
15 Halmashauri ya Utumishi ya Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi wamishonari, kisha Halmashauri ya Tawi ya nchi wanayotumikia huwapa mgawo wa kuhubiri katika maeneo yenye watu wengi. Wao hutimiza mengi katika kuimarisha kazi ya kuhubiri na kuyatia nguvu makutaniko. Kwa kawaida, wamishonari huzoezwa kwenye Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Wao hupewa makao na pesa kidogo ili kugharimia mahitaji yao.
KAZI YA MZUNGUKO
16 Wale wanaowekwa rasmi na Baraza Linaloongoza kuwa waangalizi wa mzunguko hupata mazoezi na uzoefu kwanza kwa kutumikia wakiwa waangalizi badala wa mzunguko. Wanaume hao wanaipenda huduma na ndugu zao pia. Ni mapainia wenye bidii, wanajifunza Biblia kwa bidii, na ni wasemaji na walimu wazuri. Wanaonyesha kwa kiwango kikubwa tunda la roho, ni wenye usawaziko na busara. Ikiwa ndugu ameoa, mkewe anapaswa kuwa painia mwenye mwenendo mzuri anayewatendea wengine vizuri. Ni mhubiri mwenye matokeo mazuri. Pia, anatambua wajibu wake wa kujitiisha akiwa mke Mkristo, hazungumzi kwa niaba ya mumewe au kutawala mazungumzo. Waangalizi wa mzunguko na wake zao huwa na ratiba yenye mambo mengi, kwa hiyo wale wanaojitahidi kufikia utumishi huo wanapaswa kuwa na afya nzuri. Mapainia hawatumi maombi ya kufanya kazi ya mzunguko. Badala yake, wanamwambia mwangalizi wao wa mzunguko tamaa yao, naye huwapa madokezo ya kufikia pendeleo hilo.
SHULE ZA KITHEOKRASI
17 Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme: Waeneza-injili zaidi wa Ufalme wanahitajiwa ili kuhubiri maeneo yasiyohubiriwa kwa ukawaida na kuimarisha makutaniko kiroho. Kwa hiyo, ndugu na dada waseja na wenzi wa ndoa wanaweza kujaza maombi ya kupata mazoezi ya pekee katika Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Baada ya kuhudhuria shule hiyo, wahitimu hutumwa wakiwa mapainia wa kawaida kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa katika nchi yao. Hata hivyo, wale ambao hali zao zinawaruhusu wanaweza kupewa migawo mingine nchini mwao au katika nchi nyingine. Huenda wachache wakatumwa wakiwa mapainia wa pekee wa muda au wa kudumu. Mapainia ambao wangependa kuhudhuria shule hii wanaweza kujua matakwa kwenye mkutano unaofanywa wakati wa kusanyiko la eneo.
18 Shule ya Gileadi: Ndugu na dada waseja na wenzi wa ndoa wanaochaguliwa kuhudhuria shule hii wanazungumza Kiingereza na wanatumikia wakiwa watumishi wa pekee wa wakati wote. Wana uwezo wa kuimarisha kazi ya kuhubiri au kutumikia kwenye ofisi ya tawi. Tayari wameonyesha kwamba wanafurahia kuwatumikia ndugu zao na wanaweza kuwasaidia wengine kwa fadhili kujifunza na kufuata mwongozo wa Kimaandiko na wa kitheokrasi. Halmashauri ya Tawi huwaomba wanafunzi watume maombi. Wahitimu wa shule hii hupewa mgawo wa kuhubiri au kutumikia kwenye ofisi ya tawi katika nchi yao au nchi nyingine.
UTUMISHI WA BETHELI
19 Kutumikia Betheli ni pendeleo la pekee. Jina Betheli linamaanisha “Nyumba ya Mungu,” na vituo hivyo vya utendaji wa kitheokrasi vinastahili kabisa kuitwa hivyo. Ndugu na dada wanaotumikia Betheli hufanya kazi muhimu inayohusisha kutayarisha, kutafsiri, na kusambaza machapisho ya Biblia. Utumishi wao unathaminiwa sana na Baraza Linaloongoza, ambalo husimamia na kuelekeza makutaniko duniani kote. Wanabetheli wengi ambao ni watafsiri, huishi na kufanya kazi katika maeneo ya ofisi yao ya tawi ambayo lugha wanayotafsiri huzungumzwa. Hilo huwasaidia kusikia lugha hiyo ikizungumzwa katika shughuli za kila siku. Pia, wanaweza kujionea ikiwa watu wanaelewa lugha iliyotumiwa katika machapisho yaliyotafsiriwa.
20 Kazi nyingi inayofanywa Betheli inahitaji nguvu nyingi. Kwa hiyo, hasa ndugu vijana waliojiweka wakfu na kubatizwa, wenye nguvu na afya nzuri ndio wanaoitwa Betheli. Ikiwa kuna uhitaji katika ofisi ya tawi inayosimamia nchi yenu na ungependa kutumikia Betheli, unaweza kupata habari zaidi kuhusu matakwa unayopaswa kutimiza kutoka kwa wazee wa kutaniko lako.
KUTUMIKIA KATIKA KAZI YA UJENZI
21 Ujenzi wa majengo ya kitheokrasi ni utumishi mtakatifu, kama ule uliofanywa wakati wa ujenzi wa hekalu la Sulemani. (1 Fal. 8:13-18) Ndugu na dada wengi huonyesha bidii ya pekee kwa kutumia wakati na mali zao ili kushiriki katika kazi hiyo.
22 Je, unaweza kusaidia? Ikiwa wewe ni mhubiri aliyebatizwa na ungependa kushiriki katika kazi hiyo, ndugu wanaosimamia ujenzi katika eneo lenu watathamini msaada wako, na ikiwa huna ujuzi watakuzoeza. Ikiwa ungependa kusaidia, kwa nini usiwajulishe wazee? Baadhi ya wahubiri wanaostahili wamejitolea kushiriki katika ujenzi wa majengo ya kitheokrasi katika nchi nyingine.
23 Kuna fursa nyingi za kushiriki katika utumishi wa ujenzi. Wahubiri waliobatizwa ambao ni mfano mzuri na wana ujuzi fulani, wanaweza kujitolea katika maeneo yaliyo karibu na kwao wakitumikia wakiwa wajitoleaji wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi. Wengine wanaweza kwenda kujitolea maeneo ya mbali na kwao kwa kipindi fulani cha wakati, na hutumwa na ofisi ya tawi kwa majuma mawili hadi miezi mitatu wakitumikia wakiwa wajitoleaji wa ujenzi. Wale wanaotumwa na ofisi ya tawi kutumikia kwa muda mrefu wanaitwa watumishi wa ujenzi. Mtumishi wa ujenzi anayepewa mgawo katika nchi nyingine anaitwa mtumishi wa ujenzi kutoka nchi nyingine. Kikundi cha Ujenzi kinafanyizwa na watumishi na wajitoleaji wa ujenzi na huongoza katika kila mradi wa ujenzi kikisaidiwa na wajitoleaji wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi wa eneo hilo pamoja na wajitoleaji kutoka kutaniko ambalo ujenzi unafanywa. Vikundi vya Ujenzi huhama kutoka mradi mmoja hadi mwingine ulio chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi.
UNA MALENGO GANI YA KIROHO?
24 Ikiwa umejiweka wakfu kwa Yehova, bila shaka unatamani kumtumikia milele. Hata hivyo, kwa sasa una malengo gani ya kiroho? Kuwa na malengo ya kiroho kutakusaidia utumie nguvu na mali zako kwa hekima. (1 Kor. 9:26) Kujiwekea malengo kama hayo hukusaidia kukua kiroho na kutakusaidia kuzingatia mambo muhimu zaidi unapojitahidi kufikia mapendeleo mengine ya utumishi.—Flp. 1:10; 1 Tim. 4:15, 16.
25 Mtume Paulo alituwekea mfano mzuri wa kuiga tunapomtumikia Mungu. (1 Kor. 11:1) Paulo alijitahidi sana kumtumikia Yehova. Alitambua kwamba Yehova alikuwa amempa nafasi nyingi za kumtumikia. Paulo aliwaandikia hivi ndugu huko Korintho: “Nimefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.” Je, sivyo ilivyo kwetu pia? Naam, tuna nafasi nyingi za kumtumikia Yehova tunaposhirikiana na kutaniko, hasa katika kuhubiri habari njema ya Ufalme. Lakini kama Paulo, tunatambua kwamba kupita katika ‘mlango huo mkubwa’ kunahusisha kukabiliana na “wapinzani wengi.” (1 Kor. 16:9) Paulo alikuwa tayari kujitia nidhamu. Ona alivyosema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Kor. 9:24-27) Je, unamwiga Paulo?
Kuwa na malengo ya kiroho kutakusaidia utumie nguvu na mali zako kwa hekima
26 Kila mmoja wetu anaweza kujiwekea malengo ya kitheokrasi kulingana na hali zake. Wengi wanashiriki katika utumishi wa wakati wote kwa sababu walijiwekea malengo ya kitheokrasi mapema maishani. Walipokuwa bado watoto, wazazi wao waliwatia moyo wajiwekee malengo. Hivyo, wamefurahia baraka nyingi katika utumishi wa Yehova na hawajuti kamwe. (Met. 10:22) Malengo mengine mazuri tunayoweza kujiwekea ni kama vile kushiriki katika utumishi wa shambani kila juma, kuanzisha na kuongoza funzo la Biblia, au kutenga wakati zaidi wa kutayarisha mikutano. Jambo muhimu ni kubaki washikamanifu na kutimiza huduma yetu kikamili. Tukifanya hivyo, tutamletea Yehova sifa na kufikia lengo letu kuu zaidi la kumtumikia milele.—Luka 13:24; 1 Tim. 4:7b, 8.
-
-
Mipango ya Mahali pa IbadaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 11
Mipango ya Mahali pa Ibada
WAABUDU wa kweli wa Yehova wanaamuriwa wakusanyike pamoja ili wafundishwe na watiane moyo. (Ebr. 10:23-25) Mahali pa kwanza ambapo Waisraeli, watu waliochaguliwa na Mungu, walikusanyika kwa ajili ya ibada paliitwa “hema la ibada, yaani, hema la mkutano.” (Kut. 39:32, 40) Baadaye, Sulemani mwana wa Daudi alijenga nyumba, au hekalu, kwa utukufu wa Mungu. (1 Fal. 9:3) Baada ya hekalu hilo kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., Wayahudi walipanga kukutana kwenye majengo yaliyoitwa masinagogi ili kumwabudu Mungu. Baada ya muda, hekalu lilijengwa tena, na kwa mara nyingine likawa kituo cha ibada ya kweli. Yesu alifundisha kwenye masinagogi na pia hekaluni. (Luka 4:16; Yoh. 18:20) Yesu alifanya mkutano hata kwenye mlima.—Mt. 5:1–7:29.
2 Baada ya Yesu kuuawa, Wakristo walikusanyika katika sehemu za umma na kwenye nyumba za watu ili kufundisha Maandiko na kushirikiana na waamini wenzao. (Mdo. 19:8, 9; Rom. 16:3, 5; Kol. 4:15; Flm. 2) Nyakati nyingine Wakristo wa karne ya kwanza walilazimika kukutana mahali ambapo hapakuwa na watu ili kuwaepuka watesaji. Kwa kweli, zamani watumishi waaminifu wa Mungu walitamani sana kukusanyika mahali pa ibada ili ‘kufundishwa na Yehova.’—Isa. 54:13.
3 Leo pia, sehemu za umma na nyumba za watu hutumiwa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Mara nyingi nyumba za watu hutumiwa kwa ajili ya mikutano ya utumishi wa shambani. Wale wanaoruhusu mikutano hiyo ifanywe kwenye nyumba zao huliona hilo kuwa pendeleo kubwa. Wengi wanaona kwamba wamenufaika kiroho kwa kuruhusu nyumba zao zitumiwe.
JUMBA LA UFALME
4 Mashahidi wa Yehova hukutana hasa kwenye Jumba la Ufalme. Kwa kawaida, uwanja hununuliwa kisha Jumba jipya la Ufalme hujengwa, au jengo fulani linanunuliwa na kufanyiwa marekebisho. Inapowezekana, makutaniko kadhaa yanaweza kutumia Jumba moja la Ufalme ili kupunguza gharama na kulitumia kwa ukamili. Katika maeneo mengine, inalazimu kukodi jumba. Jumba jipya la Ufalme likijengwa au kufanyiwa ukarabati mkubwa, inafaa liwekwe wakfu. Hata hivyo, ikiwa Jumba la Ufalme limefanyiwa marekebisho au ukarabati mdogo tu, basi hakuna haja ya kuliweka wakfu.
5 Jumba la Ufalme halipaswi kuwa jengo lenye madoido ili kuwavutia watu. Ingawa huenda muundo wake ukatofautiana ikitegemea eneo, sikuzote majengo hayo hutimiza kusudi linalofaa. (Mdo. 17:24) Ikitegemea hali, jumba linapaswa kuwa zuri na mahali panapofaa kufanyiwa mikutano ya Kikristo.
6 Makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova huchangia gharama za matumizi, uendeshaji, na udumishaji wa Jumba lao la Ufalme. Hakuna sadaka zinazokusanywa; wala Mashahidi hawachangishi pesa kutoka kwa watu. Kuna sanduku la michango kwa ajili ya wahudhuriaji ambao huenda wangependa kuchangia gharama muhimu za matumizi ya jumba hilo. Wanachangia kwa hiari na kutoka moyoni.—2 Kor. 9:7.
7 Washiriki wote wa kutaniko hufurahia kuchangia pesa na kujitolea kulisafisha na kulidumisha Jumba la Ufalme. Kwa kawaida mzee au mtumishi wa huduma hupewa mgawo wa kuratibu kazi hiyo. Mara nyingi usafi hufanywa na vikundi vya utumishi, chini ya uongozi wa mwangalizi wa kikundi au msaidizi wake. Iwe ni ndani au nje, Jumba la Ufalme linapaswa kumwakilisha Yehova na tengenezo lake kwa njia inayofaa.
Washiriki wote wa kutaniko hufurahia kuchangia pesa na kujitolea kulisafisha na kulidumisha Jumba la Ufalme
8 Mahali ambako makutaniko kadhaa yanatumia jumba moja, wazee wa makutaniko yanayohusika huunda Halmashauri ya Uendeshaji wa Jumba la Ufalme, ili kusimamia mambo yote yanayohusiana na jengo na uwanja wa jumba. Mabaraza ya wazee humteua ndugu mmoja kuwa mratibu wa halmashauri ya uendeshaji. Ikifanya kazi chini ya mwelekezo wa mabaraza ya wazee, halmashauri hiyo husimamia usafi wa jumba, na kuhakikisha kwamba linatunzwa vizuri na kuna vifaa vya kutosha. Ili kufanikisha hilo makutaniko yanayohusika yanapaswa kushirikiana.
9 Makutaniko kadhaa yanapotumia Jumba moja la Ufalme, huenda ratiba ya mikutano ikabadilika-badilika. Wazee wanapopanga ratiba hiyo wanapaswa kuchochewa na roho ya ufikirio na upendo. (Flp. 2:2-4; 1 Pet. 3:8) Kutaniko moja halipaswi kufanya uamuzi kwa niaba ya makutaniko mengine. Mwangalizi wa mzunguko anapotembelea mojawapo ya makutaniko hayo, makutaniko mengine katika jumba hilo yatabadili muda wa mikutano yao katika juma hilo.
10 Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ikiidhinisha, Jumba la Ufalme linaweza kutumiwa kwa ajili ya hotuba ya ndoa na ya maziko. Wazee hao hufikiria ombi lililotolewa kwa uangalifu na kufanya uamuzi kupatana na mwongozo wa ofisi ya tawi.
11 Wale wanaoruhusiwa kutumia Jumba la Ufalme kwa makusudi hayo wanapaswa kujiendesha kwa njia ya Kikristo. Hakuna jambo linalopaswa kufanyika katika Jumba la Ufalme ambalo litaudhi kutaniko au kumletea Yehova suto na kuharibu sifa nzuri ya kutaniko. (Flp. 2:14, 15) Chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi, Jumba la Ufalme linaweza kutumiwa kwa shughuli nyingine za kiroho, kama vile Shule ya Huduma ya Ufalme na Shule ya Utumishi wa Painia.
12 Nyakati zote kutaniko linapaswa kuheshimu mahali pa mikutano. Mavazi, mapambo na tabia zinapaswa kuonyesha heshima inayostahili ibada ya Yehova. (Mhu. 5:1; 1 Tim. 2:9, 10) Tunaonyesha kwamba tunathamini mikutano yetu ya Kikristo tunapotii ushauri huo.
13 Ni muhimu kudumisha utaratibu mikutano inapoendelea. Inapendekezwa kwamba watoto waketi pamoja na wazazi wao. Wazazi wenye watoto wadogo wanatiwa moyo kuketi mahali ambapo hawatawakengeusha sana wasikilizaji ikiwa watahitaji kuwatoa nje watoto wao ili kuwatia nidhamu au kwa sababu nyingine.
14 Ndugu wanaostahili hupewa mgawo wa kuwa wakaribishaji wakati wa mikutano katika Jumba la Ufalme. Wanapaswa kuwa chonjo, wenye urafiki na utambuzi. Majukumu yao yanatia ndani kuwasalimu na kuwakaribisha wapya, kuwaonyesha waliochelewa mahali pa kuketi, kuandika hudhurio la mikutano, na kuhakikisha kwamba mifumo ya kupitisha hewa inafanya kazi vizuri. Inapohitajika, wakaribishaji wanapaswa kuwakumbusha wazazi wawaangalie watoto wao wasikimbie-kimbie ndani ya jumba kabla na baada ya mikutano au kucheza jukwaani. Kwa fadhili na busara, mkaribishaji anaweza kumwomba mzazi mwenye mtoto mtundu amtoe nje, ili wasikilizaji wasikengeushwe. Kazi inayofanywa na wakaribishaji huwawezesha wote kufurahia mikutano. Inafaa wazee na watumishi wa huduma watumiwe kuwa wakaribishaji.
UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME
15 Katika karne ya kwanza, Wakristo fulani walikuwa na mali kuliko wengine, ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia usawazisho, ziada yenu kwa sasa ijazie uhitaji wao, ili ziada yao pia ijazie upungufu wenu, ili kuwe na usawazisho.” (2 Kor. 8:14) Leo, kuna “usawazisho” kama huo. Michango inayokusanywa katika makutaniko ulimwenguni pote huunganishwa ili kutoa msaada wa kifedha wa kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme. Ukarimu huo wa akina ndugu ulimwenguni pote unathaminiwa sana na tengenezo na makutaniko yanayonufaishwa na michango hiyo.
16 Ikitegemea mpango na ukubwa wa eneo, ofisi ya tawi hupanga makutaniko kadhaa yatumie Majumba fulani ya Ufalme. Pia, ofisi ya tawi huamua wakati na mahali pa kujenga Majumba mapya ya Ufalme na yale yaliyopo kufanyiwa ukarabati. Majanga yanapotokea, mipango inayohitajiwa hufanywa ili kurekebisha Majumba ya Ufalme yaliyoharibika, na nyakati nyingine, kurekebisha nyumba za akina ndugu.
17 Ofisi ya tawi huratibu jinsi wajitoleaji watakavyosaidia kupata uwanja, vibali, kusanifu, kudumisha, na kujenga Jumba la Ufalme. Kwa sababu kuna uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme katika nchi nyingi, wajitoleaji wengi wanahitajiwa. Wahubiri wote waliobatizwa wanaostahili na wangependa kusaidia, wanatiwa moyo kujaza fomu na kuwapa wazee walio katika Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lao. Hata wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kusaidia kujenga au kukarabati Jumba lao la Ufalme.
MAJUMBA YA KUSANYIKO
18 Kwa kawaida, Wakristo wa karne ya kwanza walikutana katika vikundi vidogo. Hata hivyo, nyakati nyingine “umati mkubwa” ulikusanyika. (Mdo. 11:26) Vivyo hivyo, watu wa Yehova leo hufanya mikutano mikubwa kama vile makusanyiko ya mzunguko na makusanyiko ya eneo. Mara nyingi, wao hukodi sehemu za kufanyia makusanyiko hayo, hata hivyo isipowezekana, wanajenga mahali pa ibada panapoitwa Jumba la Kusanyiko.
19 Nyakati nyingine, wao hununua jengo, hulirekebisha, na kulitumia kama Jumba la Kusanyiko. Hata hivyo, mara nyingi uwanja hununuliwa na jumba jipya kujengwa. Ukubwa wa Majumba ya Kusanyiko hutofautiana ikitegemea mahitaji ya eneo. Uamuzi wa kununua au kujenga hufanywa na ofisi ya tawi baada ya kuchanganua kwa uangalifu gharama na jinsi jumba hilo litakavyotumika.
20 Ofisi ya tawi huwaweka rasmi ndugu wasimamie uendeshaji na udumishaji wa Jumba la Kusanyiko. Mipango hufanywa katika mizunguko ili jumba hilo lisafishwe kwa ukawaida, usafi mkubwa ufanywe mara mbili kwa mwaka, na ukarabati ufanyike ili kulidumisha. Ingefaa wahubiri wajitolee kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo, makutaniko yanahimizwa kuunga mkono mipango hiyo kwa moyo wote.—Zab. 110:3; Mal. 1:10.
21 Nyakati nyingine, Jumba la Kusanyiko linaweza pia kutumiwa kwa ajili ya shughuli nyingine za kitheokrasi, kama vile Shule za Biblia na mikutano ya pekee ya waangalizi wa mzunguko. Jumba la Kusanyiko ni mahali pa ibada palipowekwa wakfu sawa na Jumba la Ufalme. Tunapokutana katika Jumba la Kusanyiko, mwenendo, mavazi, na mapambo yetu yanapaswa kuwa ya heshima, kama tu tunapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme kwa ajili ya ibada.
22 Mwishoni mwa siku hizi za mwisho, watu wengi wapya wanafanya haraka kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu. Huo ni uthibitisho wa baraka za Yehova. (Isa. 60:8, 10, 11, 22) Kwa hiyo, tunapenda kuunga mkono mipango ya kupata na kudumisha mahali safi na pazuri pa ibada. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunathamini umuhimu wa mahali pa ibada katika kutusaidia kutiana moyo kadiri tunavyoona siku ya Yehova ikikaribia.
-
-
Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni PoteTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 12
Kutegemeza Kazi ya Ufalme Kwenu na Ulimwenguni Pote
MASHAHIDI WA YEHOVA wanatimiza unabii wa Yesu kuhusu siku za mwisho kwa kuhubiri habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Mt. 24:14) Ili kufanya hivyo, wametumia wakati na nguvu zao nyingi katika kuwajulisha wengine mambo ya kiroho. Kwa kuwa wanamtegemea Yehova awaandalie mahitaji yao wakiwa wafanyakazi wenzake, wanaendelea kuutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwao. (Mt. 6:25-34; 1 Kor. 3:5-9) Matokeo yanaonyesha wazi kwamba wana kibali na baraka za Yehova.
KUSHUGHULIKIA FAIDA ZA UFALME ULIMWENGUNI POTE
2 Wanapoona jinsi tunavyohubiri habari njema na kutambua kwamba Biblia na machapisho yetu yanayotegemea Biblia hutolewa bila malipo, baadhi ya watu hujiuliza hivi: “Inawezekanaje?” Ni kweli kwamba pesa zinahitajiwa ili kuchapisha Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Pia, pesa zinahitajiwa ili kulipia gharama nyingine za ujenzi na udumishaji wa Betheli kwa ajili ya wahudumu wanaoendesha mashine za kuchapisha, kusimamia kazi ya kuhubiri, na utumishi mwingine wa kueneza habari njema. Isitoshe, waangalizi wa mzunguko, wamishonari, mapainia wa pekee, na wengine ambao wako katika utumishi wa pekee wa wakati wote hupewa pesa kidogo ili kuwasaidia waendelee katika kazi yao. Ni wazi kwamba kuhubiri habari njema kunahitaji pesa nyingi, iwe ni katika eneo letu au ulimwenguni pote. Pesa hizo zote hutoka wapi?
3 Wengi wanaothamini kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuwafundisha watu Biblia hufurahia kutoa michango kwa ajili ya kazi hiyo ya ulimwenguni pote. Hata hivyo, kazi hiyo hutegemezwa na Mashahidi wenyewe, ambao baadhi yao hutuma michango ya hiari katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya kwao. Wanaonyesha roho ya utayari kama ile ya watumishi wa Mungu wa kale waliotegemeza kwa ukarimu ujenzi wa mahali pa kumwabudu Yehova. (Kut. 35:20-29; 1 Nya. 29:9) Michango mingine hutolewa ikiwa wosia, na mingine hutolewa na mtu mmoja-mmoja, makutaniko, na mizunguko. Mara nyingi pesa hizo hutolewa zikiwa michango midogo-midogo. Inapojumlishwa, michango hiyo hutegemeza huduma.
Mashahidi wa Yehova huliona kuwa pendeleo kutumia pesa na mali zao kuendeleza kazi ya kuhubiri
4 Mashahidi wa Yehova huliona kuwa pendeleo kutumia pesa na mali zao kuendeleza kazi ya kuhubiri. Yesu na wanafunzi wake walikuwa na sanduku la pesa ambazo walitumia kulipia gharama. (Yoh. 13:29) Biblia inataja wanawake ambao walitumia mali zao kumhudumia Yesu na wanafunzi wake. (Marko 15:40, 41; Luka 8:3) Mtume Paulo alikubali kwa shukrani msaada uliotolewa kwa upendo na wale waliotaka kuendeleza habari njema na kutegemeza huduma yake. (Flp. 4:14-16; 1 The. 2:9) Mashahidi wa Yehova wanaiga mifano hiyo ya kale ya watu waliotumikia kwa bidii na kutoa kwa ukarimu. Kwa njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu kila mahali wanaweza kupewa “maji ya uzima bure.”—Ufu. 22:17.
KUSHUGHULIKIA MAHITAJI YA KUTANIKO LENU
5 Gharama za kutaniko hulipwa kwa michango ya hiari. Sadaka hazikusanywi; watu hawaambiwi watoe kiasi fulani cha pesa wala hatuchangishi pesa kutoka kwa watu. Masanduku ya michango huwekwa mahali pa mikutano ili mtu anayetaka kushiriki kutoa michango afanye hivyo “kama alivyoazimia moyoni mwake.”—2 Kor. 9:7.
6 Michango hutumiwa hasa kulipia gharama za kuendesha na kudumisha Jumba la Ufalme. Baraza la wazee linaweza kuamua kwamba kiasi fulani cha pesa hizo kinaweza kutumwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili kuendeleza kazi ya ulimwenguni pote. Kutaniko linapaswa kupitisha azimio la kutuma pesa hizo. Kwa njia hiyo, makutaniko mengi hutoa michango kwa ukawaida kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Ikiwa wote kutanikoni wataelewa kwamba mara kwa mara pesa zinahitajiwa kutanikoni, haitakuwa lazima kutangaza kila wakati kuhusu michango.
KUSHUGHULIKIA MICHANGO
7 Baada ya kila mkutano, ndugu wawili hutoa pesa zilizo katika masanduku ya michango na kuweka rekodi ya pesa hizo. (2 Fal. 12:9, 10; 2 Kor. 8:20) Baraza la wazee litafanya mipango inayofaa ya kuhifadhi pesa hizo hadi zitakapotumwa kwenye ofisi ya tawi au kulipia gharama za kutaniko. Ndugu anayeshughulikia hesabu za kutaniko hutayarisha ripoti ya hesabu ya kila mwezi ambayo husomwa kutanikoni, na mratibu wa baraza la wazee hupanga ukaguzi wa hesabu za kutaniko baada ya kila miezi mitatu.
GHARAMA ZA MZUNGUKO
8 Pesa zinazotumika kugharimia makusanyiko, na vilevile gharama nyingine za mzunguko, hulipwa kwa kutumia michango inayotolewa na Mashahidi walio katika mzunguko huo. Masanduku ya michango huwekwa mahali pa makusanyiko ili michango ya hiari ikusanywe kwa ajili ya mzunguko. Zaidi ya hilo, makutaniko yanaweza kutoa michango wakati mwingine ili kushughulikia gharama zinazohitaji kuendelea kulipwa.
9 Kila mzunguko unapaswa kulipia gharama zozote za lazima zinazojitokeza, na pesa za ziada zinapaswa kutolewa zikiwa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Ikiwa pesa zilizo katika akaunti ya mzunguko hazitoshi kulipia gharama za kusanyiko lililopita au kulipia gharama za kuanzisha kusanyiko linalofuata, kama vile pesa za kukodi mahali pa kusanyiko, mwangalizi wa mzunguko anaweza kuagiza kwamba makutaniko yaandikiwe kuhusu uhitaji wa kutoa michango. Kila baraza la wazee litazungumzia jambo hilo na kuamua mchango ambao kutaniko lao litatuma kwenye hazina ya mzunguko. Kisha azimio litapitishwa kutanikoni.
10 Mambo yanayohusu pesa ambayo yanahitaji kushughulikiwa na wazee wa mzunguko yanapojitokeza, mkutano utafanywa kwenye siku ya kusanyiko la mzunguko. Maamuzi yote isipokuwa yale yanayohusiana na gharama za pekee za makusanyiko yanapaswa kuwa maazimio yaliyoandikwa na kupitishwa na wazee. Maazimio hayo yanapaswa kutaja kiasi hususa cha pesa na kuidhinishwa kila mara pesa za mzunguko zinapotumiwa.
11 Kila baada ya muda fulani, mipango hufanywa ili kukagua rekodi za pesa za mzunguko.
KUWATUNZA MASKINI
12 Kusudi moja la sanduku la pesa lililotunzwa na Yesu na wanafunzi wake lilikuwa kuwasaidia maskini. (Marko 14:3-5; Yoh. 13:29) Wajibu huo wa Kikristo unaendelea mpaka sasa, kwa kuwa Yesu alisema: “Maskini mnao sikuzote.” (Marko 14:7) Mashahidi wa Yehova hutimizaje wajibu huo leo?
13 Nyakati nyingine, huenda washiriki waaminifu kutanikoni wakahitaji msaada kwa sababu ya uzee, udhaifu, au msiba mkubwa. Watu wa familia, na wengine ambao wanajua jambo hilo wanaweza kuwasaidia. Jambo hilo linapatana na maneno ya mtume Yohana: “Yeyote aliye na mali za ulimwengu huu akimwona ndugu yake akiwa na uhitaji naye akatae kumhurumia, anawezaje kuwa na upendo wa Mungu ndani yake? Watoto wadogo, tunapaswa kupendana, si kwa neno au kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:17, 18; 2 The. 3:6-12) Ibada ya kweli inahusisha kuwatunza waaminifu ambao huenda wanahitaji msaada wa kimwili.—Yak. 1:27; 2:14-17.
14 Katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mtume Paulo alieleza jinsi msaada unavyoweza kutolewa kwa wanaostahili. Unaweza kusoma ushauri wake kwenye 1 Timotheo 5:3-21. Ni jukumu la kila Mkristo kutunza mahitaji ya watu wa nyumbani mwake. Wazee kwa umri au walio dhaifu wanapaswa kusaidiwa na watoto wao, wajukuu wao, au watu wengine wa karibu wa ukoo. Nyakati nyingine, serikali au mashirika ya kijamii hutoa misaada, kwa hiyo watu wa ukoo au wengine wanaweza kumsaidia mwenye uhitaji aombe msaada huo kwa njia inayofaa. Huenda kukatokea hali inayolazimu kutaniko lote lifikirie kuwasaidia kwa njia fulani ndugu na dada wenye uhitaji ambao wamekuwa waaminifu kwa muda mrefu. Ikiwa watu wenye uhitaji hawana washiriki wa familia au watu wengine wa ukoo wanaoweza kuwasaidia, na serikali au mashirika ya kijamii hayatoi msaada wa kutosha, baraza la wazee linaweza kutoa mapendekezo yanayofaa ili kuwasaidia kwa njia fulani. Wakristo huona kuwa ni pendeleo kuwasaidia wenye uhitaji kwa mali zao.
15 Huenda ndugu na dada wengi wakawa na uhitaji kwa sababu ya mateso, vita, matetemeko ya nchi, mafuriko, njaa, au misiba mingine ambayo ni ya kawaida katika siku hizi za hatari. (Mt. 24:7-9) Katika pindi hizo, huenda makutaniko yasiweze kuwasaidia, kwa hiyo Baraza Linaloongoza hupanga ili ndugu wa maeneo mengine wawasaidie. Wakristo wa Asia Ndogo walifanya vivyo hivyo walipowapa chakula ndugu wa Yudea kulipokuwa na njaa. (1 Kor. 16:1-4; 2 Kor. 9:1-5) Tunapoiga mfano wao, tunawathibitishia ndugu zetu kwamba tunawapenda na kuonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo.—Yoh. 13:35.
KUGAWA MACHAPISHO
16 Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia husaidia sana kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa kawaida baraza la wazee humpa mtumishi wa huduma mgawo wa kutunza machapisho ya kutaniko. Ndugu waliopewa migawo hiyo huchukua majukumu yao kwa uzito. Wanaweka rekodi nzuri ya machapisho ili kutosheleza mahitaji ya kutaniko.
17 Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tunatambua kwamba wakati wetu, akili na nguvu, vipaji, mali zetu, hata uhai wetu wenyewe ni zawadi kutoka kwa Mungu na tunapaswa kuzitumia katika utumishi wake. (Luka 17:10; 1 Kor. 4:7) Tunapotumia vizuri kila kitu tulicho nacho, tunaonyesha kwamba tunampenda sana Yehova. Tunatamani sana kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani, tukijua kwamba anapendezwa na zawadi yoyote tunayomtolea ili kuonyesha kwamba tumejitoa kwake kwa nafsi yote. (Met. 3:9; Marko 14:3-9; Luka 21:1-4; Kol. 3:23, 24) Yesu alisema: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) Tunapojitoa wenyewe na kila kitu tulicho nacho katika utumishi wa Yehova, tunapata shangwe kubwa sana.—Mdo. 20:35.
-
-
“Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 13
“Fanyeni Mambo Yote kwa Utukufu wa Mungu”
TUKIWA watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova. Mtume Paulo alitoa kanuni inayotuongoza alipoandika hivi: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Hilo linatia ndani kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova vinavyoonyesha utu wake mkamilifu. (Kol. 3:10) Ni lazima tumwige Mungu tukiwa watu watakatifu.—Efe. 5:1, 2.
2 Akikazia umuhimu wa Wakristo kuwa watakatifu, mtume Petro aliandika hivi: “Kama watoto watiifu, acheni kufinyangwa na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika hali yenu ya kutojua, lakini iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote kama Yule Mtakatifu aliyewaita ninyi, kwa maana imeandikwa: ‘Lazima muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Pet. 1:14-16) Kama Waisraeli wa kale, wote katika kutaniko la Kikristo wanapaswa kudumisha utakatifu. Hilo linamaanisha kwamba wanapaswa kubaki safi na kuepuka kuchafuliwa na dhambi na mambo yasiyofaa ya ulimwengu. Hivyo wanatakaswa kwa ajili ya utumishi wa Yehova.—Kut. 20:5.
3 Utakatifu unadumishwa kwa kufuata sheria na kanuni za Yehova zinazotajwa waziwazi katika Maandiko Matakatifu. (2 Tim. 3:16) Tulipojifunza Maandiko, tulifundishwa kumhusu Yehova na njia zake, na tukachochewa kumkaribia. Kujifunza Biblia kulitusadikisha kwamba tulihitaji kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwetu. (Mt. 6:33; Rom. 12:2) Ili kufanya hivyo, ilitubidi tuvae utu mpya.—Efe. 4:22-24.
USAFI WA KIROHO NA WA MAADILI
4 Si rahisi kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova nyakati zote. Adui yetu, Shetani Ibilisi, anajaribu kutukengeusha kutoka kwenye kweli. Pindi fulani ushawishi mbaya wa ulimwengu huu na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi hufanya mambo yawe magumu. Ili tuishi kulingana na wakfu wetu tunahitaji kupigana vita vya kiroho. Maandiko yanatuambia kwamba tusishangae tunapopingwa au kujaribiwa. Tutateseka kwa ajili ya uadilifu. (2 Tim. 3:12) Tunaweza kufurahi tunapokuwa chini ya majaribu, tukijua kwamba majaribu hayo yanathibitisha kuwa tunafanya mapenzi ya Mungu.—1 Pet. 3:14-16; 4:12, 14-16.
5 Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alijifunza utii kutokana na mateso yaliyompata. Hakukubali kamwe kushindwa na vishawishi vya Shetani au kujitakia mambo makuu ya ulimwengu. (Mt. 4:1-11; Yoh. 6:15) Yesu hakufikiria kamwe kulegeza msimamo wake. Ingawa ulimwengu ulimchukia kwa sababu ya uaminifu wake, sikuzote alishikamana na viwango vya uadilifu vya Yehova. Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu aliwatahadharisha wanafunzi wake kwamba ulimwengu ungewachukia wao pia. Tangu wakati huo, wafuasi wa Yesu wamepata dhiki nyingi, lakini wamejipa moyo kwa kujua kwamba Mwana wa Mungu aliushinda ulimwengu.—Yoh. 15:19; 16:33; 17:16.
6 Ili tusiwe sehemu ya ulimwengu, tunahitaji kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova kama alivyofanya Bwana wetu. Mbali na kuepuka mambo ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu huu, tunapaswa kupinga maadili yake mapotovu. Tunapaswa kutii ushauri wa andiko la Yakobo 1:21: “Ondoeni uchafu wote na ubaya wote, na pokeeni kwa upole kupandwa kwa lile neno linaloweza kuwaokoa.” Tunapojifunza na kuhudhuria mikutano, ‘tunapanda lile neno’ la kweli akilini na mioyoni mwetu, na hatutatamani hata kidogo mambo ya ulimwengu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Yak. 4:4) Kwa sababu hiyo, Biblia inatuhimiza kwa uthabiti tufuate viwango vya uadilifu vya Yehova na kujitenga na ulimwengu.
7 Neno la Mungu linatuonya kwamba tusishiriki katika mwenendo wa aibu na mpotovu. Linasema hivi: “Uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi au pupa visitajwe kamwe miongoni mwenu, kama inavyowafaa watu watakatifu.” (Efe. 5:3) Kwa hiyo, hatutaruhusu kamwe akili yetu iendelee kufikiria mambo machafu ya aibu au yaliyopotoka, wala hatutaruhusu kamwe mambo hayo yaingie katika mazungumzo yetu. Kwa kufanya hivyo, tunathibitisha kwamba tunataka kufuata viwango safi na vya uadilifu vya Yehova kuhusu maadili.
USAFI WA KIMWILI
8 Mbali na usafi wa kiroho na wa maadili, Wakristo hutambua umuhimu wa kuwa safi kimwili. Katika Israeli la kale, Mungu mtakatifu aliwaagiza wadumishe usafi kambini. Sisi pia tunapaswa kuwa safi ili Yehova “asione kitu chochote kichafu” ndani yetu.—Kum. 23:14.
9 Katika Biblia, utakatifu unahusianishwa na usafi wa kimwili. Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Wapendwa . . . acheni tujisafishe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.” (2 Kor. 7:1) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kujitahidi kuwa safi kimwili kwa kuoga na kufua nguo zao kwa ukawaida. Ijapokuwa hali hutofautiana katika nchi mbalimbali, kwa kawaida tunaweza kupata sabuni na maji ya kutosha kuoga na kuhakikisha kwamba watoto wetu ni wasafi.
10 Tunajulikana sana katika jamii kwa sababu ya kazi yetu ya kutoa ushahidi. Kudumisha mpangilio mzuri na usafi, ndani na nje ya nyumba, ni njia mojawapo ya kuwatolea ushahidi jirani zetu. Familia nzima inaweza kushiriki kufanya hivyo. Akina ndugu wanapaswa kuzingatia usafi wa nyumba na mazingira yake, wakijua kwamba mazingira mazuri ya nyumbani huwavutia wengine. Kuzingatia usafi na pia kuongoza katika mambo ya kiroho, huonyesha kwamba wanasimamia vyema nyumba zao. (1 Tim. 3:4, 12) Akina dada pia wana jukumu la kudumisha usafi, hasa ndani ya nyumba. (Tito 2:4, 5) Watoto waliozoezwa vizuri hutimiza jukumu lao kwa kuwa wasafi na kudumisha mpangilio mzuri na usafi wa vyumba vyao. Hivyo, familia hushirikiana kusitawisha utaratibu wa usafi ambao tutafuata katika ulimwengu mpya chini ya Ufalme wa Mungu.
11 Watumishi wengi wa Yehova leo hutumia magari kwenda kwenye mikutano. Katika maeneo fulani, inalazimu kuwa na gari katika huduma. Gari hilo linapaswa kuwa safi na kudumishwa vizuri. Nyumba na magari yetu yanapaswa kuonyesha kwamba sisi ni watu wa Yehova walio safi na watakatifu. Kanuni hiyo inahusu pia mikoba na Biblia tunazotumia katika utumishi wa shambani.
12 Mavazi na mapambo yetu yanapaswa kupatana na kanuni za Mungu. Hatuwezi kwenda mbele ya watu mashuhuri tukiwa tumevaa isivyofaa au ovyoovyo. Je, hatupaswi kuvaa vizuri hata zaidi tunapomwakilisha Yehova katika utumishi wa shambani au jukwaani? Mavazi na mapambo yetu yanaweza kuathiri jinsi wengine wanavyoiona ibada ya Yehova. Bila shaka haingefaa kuvaa kwa njia isiyo na kiasi au bila kuwajali wengine. (Mika 6:8; 1 Kor. 10:31-33; 1 Tim. 2:9, 10) Kwa hiyo, tunapojitayarisha kwenda utumishi wa shambani, mikutanoni au makusanyikoni, tunapaswa kukumbuka yale ambayo Biblia husema kuhusu usafi wa kimwili, mavazi na mwonekano wetu. Sikuzote tunataka kumheshimu na kumtukuza Yehova.
Tukiwa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu, tuna wajibu wa kusema na kufanya mambo yote kwa utukufu wa Yehova
13 Tunapaswa kufuata kanuni hiyo pia tunapotembelea makao makuu au ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Kumbuka kwamba jina Betheli linamaanisha “Nyumba ya Mungu.” Kwa hiyo, tunapaswa kuvaa, kujipamba, na kujiendesha kama tunavyofanya tunapohudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme.
14 Hata tunapokuwa katika tafrija na burudani, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na mapambo yetu. Tunaweza kujiuliza, ‘je, mavazi na mapambo yangu yatanifanya nione aibu kutoa ushahidi isivyo rasmi?’
TAFRIJA NA BURUDANI ZINAZOFAA
15 Tunahitaji kupumzika na kujiburudisha kwa ajili afya. Wakati fulani Yesu aliwaambia wanafunzi wake waende naye mahali patulivu ili ‘wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Vipindi vya mapumziko, tafrija au burudani inayofaa zinaweza kustarehesha. Vinaweza kutupa nguvu za kuendelea na shughuli zetu za kawaida.
16 Kwa sababu kuna aina nyingi za tafrija, Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu na kutumia hekima ya Mungu katika kila jambo wanalofanya. Ingawa tafrija ni muhimu, haipaswi kuwa jambo kuu maishani. Tunaonywa kwamba katika “siku za mwisho,” watu ‘watapenda raha badala ya kumpenda Mungu.’ (2 Tim. 3:1, 4) Tafrija na burudani nyingi leo haziwafai wale wanaotamani kufuata viwango vya uadilifu vya Yehova.
17 Wakristo wa mapema walikataa mtazamo usiofaa wa ulimwengu uliofuatia sana raha. Wakati wa michezo ya Waroma, watazamaji walitumbuizwa kwa kuwatazama wengine wakiteseka. Watu wengi waliburudishwa kwa kutazama jeuri, umwagaji wa damu, na upotovu wa maadili kingono, lakini Wakristo wa mapema hawakujihusisha na mambo hayo. Leo, burudani nyingi ulimwenguni zina mambo kama hayo ambayo yamekusudiwa kutosheleza tamaa zisizofaa za wanadamu. Tunahitaji ‘kuendelea kuangalia sana’ jinsi tunavyotembea, tukiepuka burudani zinazopotosha maadili. (Efe. 5:15, 16; Zab. 11:5) Hata ingawa huenda burudani isiwe mbaya, mara nyingi kuwepo kwa watu wa ulimwengu na ushawishi wao unaweza kutuathiri.—1 Pet. 4:1-4.
18 Kuna tafrija na burudani zinazofaa ambazo Wakristo wanaweza kufurahia. Wengi wamefaidika kwa kufuata ushauri wa Maandiko na mapendekezo mazuri yanayopatikana katika machapisho yetu.
19 Nyakati nyingine, huenda familia kadhaa zikaalikwa katika nyumba fulani kufurahia ushirika wa Kikristo. Au ndugu na dada wanaweza kualikwa harusini au kwenye matukio mengine kama hayo. (Yoh. 2:2) Wale wanaoalika wageni wanapaswa kutambua kuwa watawajibika kwa mambo yote yatakayotokea. Kwa kweli, ni muhimu kuwa waangalifu ikiwa kutakuwa na watu wengi. Hali ya starehe katika vikusanyiko kama hivyo imewafanya wengine wavuke mipaka ya mwenendo unaowafaa Wakristo, na hivyo kula na kunywa kupita kiasi na hata kutumbukia katika dhambi nyingine nzito. Wakristo wenye utambuzi wanaona ni jambo la hekima kuweka idadi hususa ya watu watakaohudhuria na muda wa vikusanyiko hivyo. Ikiwa kutakuwa na pombe, inapaswa kutumiwa kwa kiasi. (Flp. 4:5) Wakristo wakijitahidi kuhakikisha kwamba tafrija zao zinajenga na kuburudisha kiroho, vyakula na vinywaji havitakuwa jambo kuu katika pindi hizo.
20 Ni vizuri kuwa wakaribishaji wageni. (1 Pet. 4:9) Tunapowaalika Wakristo wengine nyumbani kwetu kwa ajili ya chakula, viburudisho, starehe, na ushirika, tunapaswa kuwakumbuka wale wenye uhitaji. (Luka 14:12-14) Tunapoalikwa, mwenendo wetu unapaswa kupatana na ushauri unaopatikana kwenye Marko 12:31. Sikuzote ni vizuri kuthamini fadhili tunazotendewa na wengine.
21 Wakristo hufurahia zawadi nyingi kutoka kwa Mungu na wanajua kwamba wanaweza “kula na kunywa na kufurahia kazi [yao] yote ngumu.” (Mhu. 3:12, 13) Tunapofanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu,” wale walioandaa tafrija na vilevile wageni watakumbuka jinsi walivyoburudishwa kiroho.
KAZI ZA SHULENI
22 Watoto wa Mashahidi wa Yehova hunufaishwa na elimu ya msingi. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi kujifunza kusoma na kuandika vizuri. Mambo mengine ambayo vijana husoma shuleni yanaweza kuwasaidia wanapojitahidi kufikia malengo yao ya kiroho. Wanapokuwa shuleni, wanajitahidi sana ‘kumkumbuka Muumba wao’ kwa kutanguliza mambo ya kiroho.—Mhu. 12:1.
23 Ikiwa wewe ni kijana Mkristo uliye shuleni, uwe mwangalifu sana ili usishirikiane isivyo lazima na vijana wa ulimwengu. (2 Tim. 3:1, 2) Kwa kuwa Yehova hukupa ulinzi unaohitaji, una mengi ya kufanya yanayoweza kukusaidia kuepuka vishawishi vya ulimwengu. (Zab. 23:4; 91:1, 2) Hivyo, ili ujilinde, tumia kikamili maandalizi ya Yehova.—Zab. 23:5.
24 Ili kujitenga na ulimwengu wakiwa wangali shuleni, vijana wengi Mashahidi huamua kutojihusisha katika shughuli za baada ya masomo. Huenda wanafunzi wenzako na walimu wasielewe msimamo wako. Hata hivyo, jambo muhimu ni kumpendeza Mungu. Ili kufanya hivyo, unahitaji kufuata dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia na kuazimia kabisa kutohusika katika mashindano ya kilimwengu au mambo ya kizalendo. (Gal. 5:19, 26) Mkisikiliza ushauri wa Maandiko kutoka kwa wazazi wenu Wakristo, na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko, ninyi vijana mtashika viwango vya uadilifu vya Yehova.
KAZI NA WATU TUNAOSHIRIKIANA NAO
25 Vichwa vya familia wana wajibu wa Kimaandiko wa kuandalia mahitaji watu wa nyumbani mwao. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, wakiwa wahudumu wanatambua kwamba kuutafuta Ufalme ni muhimu zaidi kuliko kazi ya kimwili. (Mt. 6:33; Rom. 11:13) Wanaepuka mahangaiko na mitego ya kufuatilia vitu vya kimwili kwa kumtumikia Mungu kwa bidii na kuridhika na chakula na mavazi.—1 Tim. 6:6-10.
26 Wakristo wote waliojiweka wakfu wanapaswa kukumbuka kanuni za Maandiko katika kazi zao za kimwili. Tunapaswa kuwa wanyofu tunapotafuta riziki, na hivyo kuepuka mambo yanayovunja sheria za Mungu au sheria za nchi. (Rom. 13:1, 2; 1 Kor. 6:9, 10) Tukumbuke hatari ya kushirikiana na marafiki wabaya. Tukiwa wanajeshi wa Kristo, tunaepuka kufanya biashara zinazovunja viwango vya Mungu, zinazoweza kulegeza msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, au zinazohatarisha hali yetu ya kiroho. (Isa. 2:4; 2 Tim. 2:4) Pia, hatushirikiani na “Babiloni Mkubwa,” adui wa kidini wa Mungu.—Ufu. 18:2, 4; 2 Kor. 6:14-17.
27 Kufuata viwango vya uadilifu vya Mungu, kutatuepusha kutumia vibaya ushirika wetu wa Kikristo ili kuendeleza biashara au faida zetu za kibinafsi. Kusudi la kushirikiana na wenzetu kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo ni kumwabudu Yehova. Tunalishwa katika meza yake ya kiroho na tunafurahia ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12; Ebr. 10:24, 25) Kwenye ushirika huo tunapaswa kuzungumzia mambo ya kiroho.
KUKAA KATIKA UMOJA WA KIKRISTO
28 Ili watu wa Yehova wafuate viwango vyake vya uadilifu wanahitaji “kudumisha roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:1-3) Badala ya kujifikiria wenyewe, kila mmoja hujitahidi kufanya mambo yanayowapendeza wengine. (1 The. 5:15) Bila shaka umejionea roho hiyo katika kutaniko lako. Bila kujali kabila, taifa, jamii, hali yetu ya kiuchumi au elimu yetu, sote tunaongozwa na viwango vilevile vya uadilifu. Hata watu wasio Mashahidi wameona sifa hiyo ya pekee ya watu wa Yehova.—1 Pet. 2:12.
29 Akikazia msingi wa umoja, mtume Paulo aliandika hivi: “Kuna mwili mmoja, na roho moja, kama mlivyoitwa kwenye tumaini moja; Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja ambaye ni Baba wa wote, aliye juu ya wote, na kupitia wote na katika wote.” (Efe. 4:4-6) Maneno hayo yanatuchochea tuwe na ufahamu uleule wa mafundisho ya msingi na pia mafundisho yenye kina ya Biblia ili tuonyeshe kwamba tunatambua mamlaka kuu ya Yehova. Kwa kweli, Yehova amewapa watu wake lugha safi ya kweli inayowawezesha wamtumikie bega kwa bega.—Sef. 3:9.
30 Umoja na amani ya kutaniko la Kikristo huwaburudisha wote wanaomwabudu Yehova. Tumeshuhudia utimizo wa ahadi hii ya Yehova: “Kwa umoja nitawaweka kama kondoo zizini.” (Mika 2:12) Tunataka kudumisha umoja na amani hiyo kwa kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova.
31 Wenye furaha ni wale waliokubaliwa katika kutaniko safi la Yehova! Tunapaswa kujidhabihu kwa njia yoyote ile ili tuitwe kwa jina la Yehova. Tunapodumisha uhusiano wetu wenye thamani na Yehova, tutajitahidi sana kufuata viwango vyake vya uadilifu na kuwafundisha wengine kufanya hivyo.—2 Kor. 3:18.
-
-
Kudumisha Amani na Usafi wa KutanikoTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 14
Kudumisha Amani na Usafi wa Kutaniko
KAMA unabii wa Biblia ulivyotabiri, kila mwaka maelfu ya watu humiminika kwenye nyumba ya Yehova ya ibada safi. (Mika 4:1, 2) Tunafurahia kwelikweli kuwakaribisha katika “kutaniko la Mungu”! (Mdo. 20:28) Wanathamini sana kumtumikia Yehova pamoja nasi na kufurahia mazingira safi na yenye amani ya paradiso yetu ya kiroho. Roho takatifu ya Mungu na hekima ya Neno lake inatusaidia kudumisha amani na usafi wa kutaniko.—Zab. 119:105; Zek. 4:6.
2 Tunapofuata kanuni za Biblia, tunavaa “utu mpya.” (Kol. 3:10) Hatutilii maanani mabishano madogo-madogo na tofauti za kibinafsi. Tunashinda ushawishi unaosababisha migawanyiko ulimwenguni, na kufanya kazi kwa umoja tukiwa undugu wa kimataifa kwa sababu tuna maoni kama ya Yehova.—Mdo. 10:34, 35.
3 Hata hivyo, mara kwa mara matatizo hutokea ambayo huathiri amani na umoja wa kutaniko. Yanasababishwa na nini? Katika visa vingi, husababishwa na kutofuata ushauri wa Biblia. Bado tunapambana na mwelekeo wetu mbaya tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. Hakuna hata mmoja wetu asiyetenda dhambi. (1 Yoh. 1:10) Huenda mtu fulani akachukua hatua isiyofaa ambayo inaweza kuchafua maadili au usafi wa kiroho wa kutaniko. Tunaweza kumkosea mtu fulani kwa kutenda au kusema bila kufikiri, au huenda tukakwazika kwa sababu ya jambo ambalo mtu fulani amesema au kutenda. (Rom. 3:23) Katika hali kama hizo, tunaweza kufanya nini ili kunyoosha mambo?
4 Kwa upendo Yehova amefikiria mambo yote hayo. Neno lake linatushauri kuhusu kutatua matatizo yanapotokea. Msaada wa kibinafsi unapatikana kutoka kwa wachungaji wenye upendo, yaani wazee. Kwa kufuata ushauri wao wa Kimaandiko, tunaweza kurejesha uhusiano mzuri na wengine na kudumisha msimamo mzuri na Yehova. Ikiwa tunatiwa nidhamu au kukaripiwa kwa sababu ya kosa fulani tulilofanya, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anaturekebisha kwa kuwa anatupenda.— Met. 3:11, 12; Ebr. 12:6.
KUTATUA TOFAUTI NDOGO-NDOGO
5 Nyakati fulani huenda kukatokea mabishano au kutoelewana kati ya ndugu na dada kutanikoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Hali hiyo inapaswa kutatuliwa haraka na kwa roho ya upendo wa kindugu. (Efe. 4:26; Flp. 2:2-4; Kol. 3:12-14) Huenda ukatambua kwamba matatizo ya kibinafsi yanayohusu uhusiano wako na Mkristo mwenzako kutanikoni yanaweza kutatuliwa kwa kufuata ushauri huu wa mtume Petro: “Pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Biblia inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Kwa kufuata ile Kanuni Bora, yaani, kuwatendea wengine kwa njia ambayo tungependa watutendee, mara nyingi tunaweza kusamehe na kusahau makosa madogo ya wengine.—Mt. 6:14, 15; 7:12.
6 Ukitambua kwamba umemkosea mtu fulani kwa yale uliyosema au kutenda, unapaswa kuchukua hatua ili kufanya amani bila kukawia. Kumbuka kwamba uhusiano wako pamoja na Yehova pia unaathiriwa. Yesu aliwashauri wanafunzi wake hivi: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo unakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, iache zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, uende zako. Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.” (Mt. 5:23, 24) Huenda mmoja wenu ameelewa jambo fulani kimakosa. Ikiwa ndivyo, zungumzieni jambo hilo waziwazi. Mawasiliano mazuri kati ya washiriki wote wa kutaniko husaidia kuzuia kutoelewana na kutatua matatizo yanayotokea kwa sababu ya kutokamilika.
KUTOA USHAURI WA MAANDIKO
7 Nyakati nyingine, huenda waangalizi wakaona kwamba wanapaswa kumshauri mtu fulani ili arekebishe maoni yake. Kwa kawaida si rahisi kufanya hivyo. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Galatia: “Akina ndugu, hata mtu akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole.”—Gal. 6:1.
8 Wanapolichunga kundi, waangalizi hulinda kutaniko dhidi ya hatari za kiroho na hivyo kuzuia matatizo makubwa yasitokee. Wazee wanapaswa kujitahidi kulitumikia kutaniko kama Yehova alivyoahidi kupitia Isaya: “Na kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo, na mahali pa kujisitiri kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha jabali kubwa katika nchi iliyokauka.”—Isa. 32:2.
KUWATIA ALAMA WATU WASIOFUATA UTARATIBU
9 Mtume Paulo aliwaonya watu fulani ambao wangeweza kuwa na ushawishi mbaya ndani ya kutaniko. Paulo alisema hivi: “Sasa akina ndugu, tunawaagiza . . . mjiepushe na kila ndugu asiyefuata utaratibu na desturi mlizopokea kutoka kwetu.” Kisha akafafanua taarifa yake kwa kuandika hivi: “Lakini ikiwa yeyote hatii maneno yetu kupitia barua hii, mtieni alama na mwache kushirikiana naye, ili aone aibu. Lakini msimwone mtu huyo kama adui, bali endeleeni kumwonya kama ndugu.”—2 The. 3:6, 14, 15.
10 Pindi fulani, huenda mtu akapuuza kimakusudi viwango vya Biblia vya Kikristo ingawa hajafanya dhambi nzito inayoweza kumfanya atengwe na kutaniko. Hilo linaweza kutia ndani mambo kama vile kuwa mvivu, mchambuzi, au mchafu kupita kiasi. Huenda ‘anajiingiza katika mambo yasiyomhusu.’ (2 The. 3:11) Au huenda anawatumia wengine kwa hila kujipatia faida za kimwili au anafurahia burudani ambayo kwa wazi haifai. Mwenendo huo usiofaa ni jambo zito linaloharibu sifa ya kutaniko, na pia unaweza kuenea kati ya Wakristo wengine.
11 Kwanza wazee watamsaidia mtu asiyefuata utaratibu kwa kumpa ushauri unaotegemea Biblia. Hata hivyo, ikiwa mtu huyo anaendelea kupuuza kanuni za Biblia licha ya kushauriwa tena na tena, wazee wanaweza kuamua hotuba ya kuonya itolewe kutanikoni. Wazee watatumia utambuzi kuamua ikiwa hali fulani ni nzito vya kutosha na inasumbua wengine hivi kwamba hotuba ya kuonya inahitaji kutolewa. Msemaji atatoa ushauri unaofaa kuhusu mwenendo huo, lakini hatataja jina la mtu huyo asiyefuata utaratibu. Kwa hiyo, wale wanaojua kisa kinachozungumziwa katika hotuba hiyo watachukua tahadhari na kupunguza ushirikiano na mtu huyo, ingawa wataendelea kushirikiana naye kiroho na “kumwonya kama ndugu.”
12 Tunatumaini kwamba, Wakristo waaminifu wa kutaniko wakichukua msimamo imara, jambo hilo litamchochea asiyefuata utaratibu kuonea aibu njia zake na hilo litamchochea kubadilika. Inapokuwa wazi kwamba mtu huyo ameacha mwenendo wake usiofaa, hakuna haja ya kuendelea kumtendea kama mtu aliyetiwa alama.
KUTATUA MAKOSA FULANI MAZITO
13 Kuachilia au kusamehe makosa hakumaanishi kwamba tunapuuza au tunakubali makosa hayo. Si makosa yote yanayosababishwa na kutokamilika; wala haifai kuachilia makosa mazito. (Law. 19:17; Zab. 141:5) Agano la Sheria lilionyesha kwamba dhambi fulani ni nzito kuliko nyingine, na ndivyo ilivyo pia katika mpango wa Kikristo.—1 Yoh. 5:16, 17.
14 Yesu aliorodhesha hatua hususa za kutatua matatizo yanayohusu makosa mazito yanayoweza kutokea kati ya Wakristo. Ona hatua alizotaja: “Ndugu yako akitenda dhambi, [1] nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yenu. Akikusikiliza, umempata ndugu yako. Lakini asipokusikiliza, [2] nenda pamoja na mtu mmoja au wawili, ili kwa ushahidi wa mashahidi wawili au watatu kila jambo lithibitishwe. Asipowasikiliza hao, [3] liambie kutaniko. Asipolisikiliza kutaniko pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na kama mkusanya kodi.”—Mt. 18:15-17.
15 Katika mfano ulio katika Mathayo 18:23-35 ambao Yesu alitoa baada ya kutaja hatua hizo, inaonekana kwamba mojawapo ya dhambi zinazotajwa katika Mathayo 18:15-17 zinahusu mambo ya kifedha au mali, kama vile, kutolipa kitu fulani au kutenda kwa njia ya udanganyifu. Au uchongezi unaoweza kuharibu sana sifa ya mtu.
16 Ikiwa una uthibitisho kwamba mtu fulani kutanikoni amekutendea mojawapo ya dhambi hizo, usiwe na haraka ya kuwaomba wazee waingilie kati. Kama Yesu alivyoshauri, zungumza kwanza na yule aliyekukosea. Jaribu kutatua jambo hilo kati yenu bila kumhusisha mtu mwingine. Kumbuka kwamba Yesu hakusema ‘nenda ufunue kosa lake, mara moja tu.’ Kwa hiyo, ikiwa mtu huyo hakubali kosa lake na kuomba msamaha, huenda ikafaa ufikirie kumwendea tena baadaye. Ikiwa jambo litatatuliwa kwa njia hiyo, yule aliyetenda dhambi atathamini kwamba hukuwaambia wengine dhambi yake wala kumharibia sifa yake nzuri kutanikoni. Utakuwa “umempata ndugu yako.”
17 Ikiwa yule aliyetenda kosa anakubali kosa lake, anaomba msamaha, na anachukua hatua ya kurekebisha kosa hilo, hakuna haja ya kuchukua hatua nyingine. Ingawa makosa yanayotajwa ni mazito, makosa ya aina hii yanaweza kutatuliwa na watu wanaohusika.
18 Ikiwa umeshindwa kumpata ndugu yako kwa kuchukua hatua ya kufunua kosa lake “kati yako na yeye peke yenu,” sasa unaweza kufanya kama Yesu alivyoshauri, “nenda pamoja na mtu mmoja au wawili,” na uzungumze na ndugu yako tena. Wale unaowachukua wanapaswa pia kuwa na lengo la kumpata ndugu yako. Inafaa uchukue watu walioshuhudia kosa linalodaiwa, lakini ikiwa hakuna walioshuhudia kosa hilo, unaweza kuamua kuchukua mtu mmoja au wawili washuhudie mazungumzo hayo. Huenda wakawa na ujuzi wa jambo linalohusika na wanaweza kuamua ikiwa kwa kweli kosa lilifanywa. Ukiwachukua wazee wakashuhudie hawatawakilisha kutaniko kwa kuwa baraza la wazee halijawapa mgawo hususa wa kufanya hivyo.
19 Ikiwa jambo hilo halijatatuliwa hata baada ya jitihada za kumrudia tena na tena, yaani, umezungumza naye peke yake na umeenda kwake na mtu mmoja au wawili, na unahisi huwezi kuachilia kosa hilo, basi unapaswa kuripoti jambo hilo kwa waangalizi wa kutaniko. Kumbuka kwamba lengo lao ni kudumisha amani na usafi wa kutaniko. Baada ya kuwafikia wazee, liache jambo hilo mikononi mwao na umtumaini Yehova. Usiruhusu kamwe mwenendo wa mtu mwingine ukukwaze au kukufanya ukose shangwe unapomtumikia Yehova.—Zab. 119:165.
20 Wachungaji wa kundi watachunguza jambo hilo. Ikionekana wazi kwamba mtu huyo amekutendea dhambi nzito naye hajatubu wala kuonyesha nia ya kurekebisha jambo hilo inavyofaa na kwa kadiri anavyoweza, huenda waangalizi wakalazimika kumtenga na ushirika mkosaji asiyetubu. Hivyo, wanalilinda kundi na kudumisha usafi wa kutaniko.—Mt. 18:17.
KUSHUGHULIKIA VISA VYA MAKOSA MAZITO
21 Baadhi ya dhambi nzito, kama vile uasherati, uzinzi, ngono kati ya watu wa jinsia moja, kukufuru, uasi imani, kuabudu sanamu, na dhambi nyingine nzito kama hizo, zinahitaji mengi zaidi ya kusamehewa tu na mtu aliyekosewa. (1 Kor. 6:9, 10; Gal. 5:19-21) Kwa sababu usafi wa kiroho na wa kiadili wa kutaniko uko hatarini, dhambi hizo nzito zinapaswa kuripotiwa kwa wazee ili wazishughulikie. (1 Kor. 5:6; Yak. 5:14, 15) Huenda mtu binafsi akawafikia wazee ili kuungama dhambi yake mwenyewe au kuwajulisha kuhusu makosa ya wengine anayoyajua. (Law. 5:1; Yak. 5:16) Wazee wanapopata habari zozote kwa mara ya kwanza kuhusu kosa zito lililofanywa na Shahidi aliyebatizwa, uchunguzi utaanza kufanywa na wazee wawili, haijalishi chanzo cha habari hizo. Ikithibitika kwamba habari hiyo ni ya kweli na kuna uthibitisho kwamba dhambi nzito imefanywa, baraza la wazee litaunda halmashauri ya hukumu yenye angalau wazee watatu ili kushughulikia jambo hilo.
22 Wazee huwa macho kulichunga na kulilinda kundi ili lisiathiriwe kiroho na kitu chochote. Pia, wao hujitahidi kutumia Neno la Mungu kwa ustadi ili kumkaripia yeyote ambaye amefanya kosa na kumsaidia arudie tena hali yake nzuri ya kiroho. (Yuda 21-23) Hilo linapatana na maagizo ambayo Timotheo alipewa na mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Nakuagiza kwa uzito mbele za Mungu na Kristo Yesu, ambaye atawahukumu walio hai na wafu, . . . Karipia, kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha.” (2 Tim. 4:1, 2) Huenda kufanya hivyo kukahitaji wakati mwingi, lakini hiyo ni sehemu ya kazi ya wazee. Kutaniko huthamini jitihada zao na huona kuwa wanastahili “heshima mara mbili.”—1 Tim. 5:17.
23 Katika kila kisa ambacho kosa limethibitishwa, kusudi kuu la waangalizi ni kurudisha hali nzuri ya kiroho ya mkosaji. Ikiwa anatubu kikweli nao wanaweza kumsaidia, waangalizi watamkaripia faraghani au mbele ya mashahidi wowote waliotoa ushahidi wakati wa kikao hicho cha hukumu, jambo litakalomtia nidhamu mkosaji na kuwafanya watazamaji hao wawe na woga unaofaa. (2 Sam. 12:13; 1 Tim. 5:20) Katika visa vyote karipio la hukumu linapotolewa, vizuizi vitawekwa. Hivyo mkosaji anaweza kusaidiwa kuifanyia miguu yake “mapito yaliyonyooka.” (Ebr. 12:13) Baada ya muda, vizuizi hivyo huondolewa maendeleo ya kiroho ya mtu huyo yanapoonekana wazi.
TANGAZO LA KARIPIO
24 Halmashauri ya hukumu ikiona kwamba mtu fulani ametubu lakini huenda jambo hilo likajulikana kutanikoni au katika jamii au ikiwa kutaniko linahitaji kulindwa dhidi ya mtenda dhambi aliyetubu, tangazo fupi litafanywa katika Mkutano wa Huduma na Maisha. Linapaswa kusema hivi: “[Jina la mtu] amekaripiwa.”
IKIWA UAMUZI NI KUTENGA NA USHIRIKA
25 Katika visa fulani, mkosaji anaweza kuwa amezama sana katika mwenendo wenye dhambi na hivyo ashindwe kukubali jitihada za kusaidiwa. Huenda “matendo yanayoonyesha toba” yasionekane wazi wakati wa kikao cha hukumu. (Mdo. 26:20) Ni hatua gani inayopaswa kuchukuliwa? Katika visa hivyo, ni lazima mkosaji asiyetubu aondolewe kutanikoni, na hivyo kumzuia asishirikiane na watu wa Yehova walio safi. Ushawishi mbaya wa mkosaji huyo huondolewa kutanikoni, na hivyo kulinda usafi wa kiadili na wa kiroho na sifa nzuri ya kutaniko. (Kum. 21:20, 21; 22:23, 24) Baada ya kupata habari kuhusu mwenendo wa aibu wa Mkristo fulani wa kutaniko la Korintho, mtume Paulo aliwahimiza hivi wazee: “Mumkabidhi mtu wa namna hiyo kwa Shetani . . . , ili roho [ya kutaniko] iokolewe.” (1 Kor. 5:5, 11-13) Paulo aliripoti pia kuhusu wengine katika karne ya kwanza ambao walitengwa na ushirika kwa sababu ya kuasi kweli.—1 Tim. 1:20.
26 Inapoamuliwa kwamba mkosaji asiyetubu anapaswa kutengwa na ushirika, halmashauri ya hukumu inapaswa kumjulisha uamuzi huo, na kumweleza wazi sababu ya (za) Kimaandiko ya (za) kumtenga na ushirika. Inapomjulisha mkosaji uamuzi wao, halmashauri ya hukumu itamwambia kwamba ikiwa anahisi kuwa wamekosea katika uamuzi waliofanya na angependa kukata rufaa, anapaswa kufanya hivyo kupitia barua, akieleza waziwazi sababu zake za kukata rufaa. Atapewa siku saba za kufanya hivyo tangu uamuzi wa hukumu ulipotolewa. Ikiwa baraza la wazee limepokea rufaa, linapaswa kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko, ambaye atachagua wazee wanaostahili watumikie wakiwa halmashauri ya rufaa ili wasikilize kesi hiyo tena. Wazee hao watajitahidi kusikiliza kesi hiyo kabla juma moja halijapita baada ya kupokea barua hiyo. Ikiwa mkosaji amekata rufaa, tangazo la kutengwa na ushirika litaahirishwa. Katika kipindi hicho, mshitakiwa atazuiwa kutoa maelezo na sala kwenye mikutano na kuzuiwa mapendeleo ya pekee ya utumishi.
27 Kuruhusiwa kukata rufaa ni tendo la fadhili linalompa mshtakiwa nafasi nyingine ya malalamiko yake kusikilizwa. Hivyo, ikiwa mkosaji hajafika kimakusudi kwenye kikao cha rufaa, tangazo la kutengwa na ushirika litatangazwa baada ya wazee kujitahidi kadiri wawezavyo kuwasiliana naye.
28 Ikiwa mkosaji hangependa kukata rufaa, halmashauri ya hukumu itamweleza kuhusu uhitaji wa kutubu na vilevile hatua anazoweza kuchukua ili arudishwe baada ya muda. Kufanya hivyo ni njia ya kumsaidia na kumwonyesha fadhili, nao wazee wanapaswa kufanya hivyo wakitumaini kwamba atabadili njia zake na baadaye astahili kurudi katika tengenezo la Yehova.—2 Kor. 2:6, 7.
TANGAZO LA KUTENGA NA USHIRIKA
29 Inapokuwa lazima kumtenga na ushirika wa kutaniko mkosaji asiyetubu, tangazo fupi hutolewa linalosema: “[Jina la mtu] si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena.” Hilo litawatahadharisha ndugu na dada waaminifu kutanikoni waache kushirikiana na mtu huyo.—1 Kor. 5:11
KUJITENGA NA USHIRIKA
30 Usemi “kujitenga na ushirika” hurejelea hatua inayochukuliwa na mtu ambaye ni Shahidi aliyebatizwa lakini anakana kimakusudi msimamo wake wa Kikristo kwa kusema kwamba hataki tena kutambuliwa, au kujulikana kuwa Shahidi wa Yehova. Au huenda amelikana kutaniko la Kikristo kupitia matendo yake, kama vile kwa kujiunga na shirika la kilimwengu lenye malengo yanayopingana na mafundisho ya Biblia ambalo litahukumiwa na Yehova Mungu.—Isa. 2:4; Ufu. 19:17-21.
31 Mtume Yohana aliandika hivi kuhusu wale walioikana imani ya Kikristo katika siku zake: “Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi.”—1 Yoh. 2:19.
32 Machoni pa Yehova, hali ya mtu aliyejitenga na ushirika ni tofauti kabisa na ya Mkristo asiyetenda ambaye hashiriki tena katika huduma ya shambani. Huenda mtu asiyetenda aliacha kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida. Au labda amepoteza bidii yake ya kumtumikia Yehova kwa sababu ya matatizo ya kibinafsi au mateso. Wazee na wengine kutanikoni wataendelea kumpa Mkristo huyo asiyetenda msaada wa kiroho unaofaa.—Rom. 15:1; 1 The. 5:14; Ebr. 12:12.
33 Hata hivyo, kwa Mkristo ambaye ameamua mwenyewe kujitenga na ushirika, tangazo hili fupi litatolewa ili kulijulisha kutaniko: “[Jina la mtu] si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena.” Mtu huyo hutendewa sawa na mtu aliyetengwa na ushirika.
KURUDISHWA
34 Mtu aliyetengwa na ushirika au yule aliyejitenga na ushirika wa kutaniko anaweza kurudishwa akionyesha wazi kwamba ametubu na muda wa kutosha umepita ili kuonyesha kwamba ameacha mwenendo wake wenye dhambi. Anaonyesha kwamba anatamani kuwa na uhusiano mzuri na Yehova. Wazee huwa waangalifu kwa kuruhusu muda wa kutosha upite—miezi mingi, mwaka, au muda mrefu zaidi, ikitegemea hali—ili mtu huyo athibitishe kwamba ametubu kikweli. Baraza la wazee linapopokea barua ya ombi la kutaka kurudishwa, halmashauri ya kurudisha itazungumza na mtu huyo. Halmashauri hiyo itachunguza uthibitisho wa “matendo yanayoonyesha toba” kwa mkosaji huyo na kuamua ikiwa itamrudisha wakati huo au la.—Mdo. 26:20.
35 Ikiwa mtu anayeomba kurudishwa alitengwa na kutaniko lingine, halmashauri ya kurudisha ya kutaniko la mahali alipo itakutana naye na kufikiria ombi lake. Ikiwa washiriki wa halmashauri hiyo wanaamini kwamba mtu huyo anapaswa kurudishwa, watatuma pendekezo lao kwenye baraza la wazee la kutaniko ambalo lilishughulikia kisa hicho. Halmashauri zinazohusika zitashirikiana ili kuhakikisha mambo yote yamechunguzwa na uamuzi unaofaa umefanywa. Hata hivyo, uamuzi wa kumrudisha utafanywa na halmashauri ya kurudisha ya kutaniko lililoshughulikia kisa hicho.
TANGAZO LA KURUDISHWA
36 Halmashauri ya kurudisha ikisadikishwa kwamba mtu aliyetengwa na ushirika au aliyejitenga na ushirika ametubu kikweli na anastahili kurudishwa, tangazo la kumrudisha hutolewa katika kutaniko lililoshughulikia kisa chake. Ikiwa sasa mtu huyo yuko kutaniko lingine, tangazo litatolewa katika kutaniko hilo pia. Tangazo hilo linapaswa kusema: “[Jina la mtu] amerudishwa, naye sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”
VISA VINAVYOHUSU WATOTO AMBAO WAMEBATIZWA
37 Makosa mazito yanayofanywa na watoto ambao wamebatizwa yanapaswa kuripotiwa kwa wazee. Wazee wanaposhughulikia makosa mazito yanayowahusu watoto, inafaa wazazi waliobatizwa wa mtoto huyo wawepo. Itafaa washirikiane na halmashauri ya hukumu, bali si kujaribu kumtetea mtoto aliyefanya kosa ili asichukuliwe hatua ya kutiwa nidhamu. Sawa na vile inavyoshughulikia watu wazima waliofanya kosa, halmashauri ya hukumu hujitahidi kumkaripia na kumrekebisha mkosaji. Hata hivyo, ikiwa mtoto huyo haonyeshi toba, hatua ya kumtenga na ushirika itachukuliwa.
WAHUBIRI AMBAO HAWAJABATIZWA WANAPOFANYA KOSA
38 Namna gani ikiwa wahubiri ambao hawajabatizwa wamefanya makosa mazito? Kwa kuwa wao si Mashahidi waliobatizwa, hawawezi kutengwa na ushirika. Hata hivyo, labda hawaelewi vizuri viwango vya Biblia, na huenda wakahitaji kushauriwa kwa busara ili kuwasaidia waifanyie miguu yao “mapito yaliyonyooka.”—Ebr. 12:13.
39 Ikiwa mhubiri ambaye hajabatizwa hajaonyesha toba baada ya wazee wawili kukutana naye na kujaribu kumsaidia, basi kutaniko linahitaji kujulishwa. Tangazo fupi hutolewa linalosema: “[Jina la mtu] hatambuliwi tena kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa.” Kisha, kutaniko litamwona mkosaji huyo kama mtu wa ulimwengu. Ingawa mkosaji huyo hatengwi na ushirika, Wakristo huwa waangalifu wanaposhirikiana naye. (1 Kor. 15:33) Hatakubaliwa kutoa ripoti za utumishi wa shambani.
40 Baada ya muda, huenda mhubiri ambaye hajabatizwa aliyeondolewa kuwa mhubiri, akataka tena kuwa mhubiri. Katika hali hiyo, wazee wawili watakutana naye ili kuchunguza maendeleo yake ya kiroho. Ikiwa anastahili, tangazo fupi linaweza kutolewa linalosema: “[Jina la mtu] anatambuliwa tena kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa.”
YEHOVA HUBARIKI IBADA SAFI NA YENYE AMANI
41 Wote wanaoshirikiana na kutaniko la Mungu leo wanaweza kufurahia paradiso ya kiroho ambayo Yehova amewapa watu wake. Tuna chakula kingi cha kiroho na maji mengi yenye kuburudisha ya kweli. Pia, tunalindwa na Yehova kupitia mpango wake wa kitheokrasi chini ya ukichwa wa Kristo. (Zab. 23; Isa. 32:1, 2) Kuwa katika paradiso ya kiroho katika siku hizi zenye taabu kumetufanya tujihisi tukiwa salama.
Tunapodumisha amani na usafi wa kutaniko, tunaendelea kuacha nuru yetu ya kweli ya Ufalme iangaze
42 Tunapodumisha amani na usafi wa kutaniko, tunaendelea kuacha nuru yetu ya kweli ya Ufalme iangaze. (Mt. 5:16; Yak. 3:18) Mungu atatubariki, nasi tutashangilia kuona watu wengi zaidi wakimjua Yehova na wakijiunga nasi ili kufanya mapenzi yake.
-
-
Faida za Kujitiisha Katika Mpango wa KitheokrasiTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 15
Faida za Kujitiisha Katika Mpango wa Kitheokrasi
NI LAZIMA tujitiishe kwa Mungu, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, ili tuwe sehemu ya tengenezo linalofanya mapenzi ya Yehova. Tunatambua kwamba Mwana wake ndiye Kichwa cha kutaniko la Kikristo na pia tunafuata kanuni ya ukichwa katika mambo mengine maishani. Kila mtu anayejitiisha katika mpango huo wa kitheokrasi hufaidika.
2 Wanadamu walijulishwa kwa mara ya kwanza kabisa kuhusu mpango wa kujitiisha chini ya mamlaka katika bustani ya Edeni. Mpango huo unafafanuliwa katika amri za Mungu zilizo kwenye Mwanzo 1:28 na 2:16, 17. Wanyama wangeongozwa na wanadamu, na Adamu na Hawa walipaswa kujitiisha kwa mapenzi na mamlaka ya Mungu. Kutii mamlaka ya Mungu kungeleta amani na utaratibu mzuri. Kanuni ya ukichwa inakaziwa tena katika 1 Wakorintho 11:3. Mtume Paulo aliandika hivi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” Hilo linaonyesha kwamba kila mtu yuko chini ya ukichwa fulani katika mpango huo, isipokuwa Yehova.
3 Watu wengi leo hawaheshimu wala kutii kanuni ya ukichwa. Kwa nini? Tatizo lilianzia Edeni wazazi wa wanadamu walipochagua kimakusudi kutojitiisha chini ya ukichwa wa Mungu mwenye enzi kuu. (Mwa. 3:4, 5) Hata hivyo, hawakupata uhuru zaidi. Badala yake, walijitiisha chini ya kiumbe mwovu wa roho, Shetani Ibilisi. Uasi wa kwanza uliwatenganisha wanadamu na Mungu. (Kol. 1:21) Ndiyo sababu wanadamu wengi leo wako chini ya nguvu za yule mwovu.—1 Yoh. 5:19.
4 Tunapojifunza na kuishi kupatana na kweli ya Neno la Mungu, tunakataa kuongozwa na uvutano wa Shetani. Tukiwa Mashahidi waliojiweka wakfu na kubatizwa, tunamkubali Yehova kuwa Mtawala Mkuu wa maisha yetu. Tunakubaliana na Mfalme Daudi, aliyekiri kwamba Yehova ndiye “mkuu juu ya vyote.” (1 Nya. 29:11) Bila shaka tunakiri hivi kwa unyenyekevu: “Jueni kwamba Yehova ni Mungu. Yeye ndiye aliyetuumba, na sisi ni mali yake. Sisi ni watu wake na kondoo wa malisho yake.” (Zab. 100:3) Tunatambua kwamba Yehova ni mkuu na tunapaswa kujitiisha kwake kikamili kwa kuwa aliumba vitu vyote. (Ufu. 4:11) Tukiwa wahudumu wa Mungu wa kweli, tunamfuata Yesu Kristo, ambaye aliweka kielelezo kikamilifu cha kujitiisha kwa Mungu.
5 Yesu alijifunza nini kutokana na mateso yaliyompata alipokuwa duniani? Andiko la Waebrania 5:8 linajibu hivi: “Ingawa alikuwa mwana, alijifunza kutii kutokana na mateso yaliyompata.” Naam, Yesu aliendelea kujitiisha kwa ushikamanifu kwa Baba yake wa mbinguni hata alipokabili magumu. Zaidi ya hayo, Yesu hakufanya lolote kwa uamuzi wake mwenyewe. Hakusema mambo aliyotunga yeye mwenyewe; wala hakutafuta utukufu wake mwenyewe. (Yoh. 5:19, 30; 6:38; 7:16-18) Wakati wa huduma yake, alifurahia kufanya mapenzi ya Baba yake, hata ingawa alipingwa na kuteswa kwa kufanya hivyo. (Yoh. 15:20) Hata hivyo, Yesu alijitiisha kwa Mungu. Yesu “alijinyenyekeza” mpaka “kifo juu ya mti wa mateso.” Kujitiisha kwake kikamili kwa Yehova kulikuwa na faida nyingi. Kuliwaletea wanadamu wokovu wa milele, kulifanya apandishwe cheo, na kulimtukuza Baba yake.—Flp. 2:5-11; Ebr. 5:9.
TUNAPASWA KUJITIISHA KWA NANI?
6 Tunapojitiisha kwa Mungu kwa kufanya mapenzi yake, tunaepuka mahangaiko na mambo mengi yenye kuvunja moyo yanayowapata wale wanaokataa kujitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova. Adui yetu, Ibilisi, hujaribu kila wakati kutumeza. Tutakombolewa kutoka kwa mwovu huyo ikiwa tutachukua msimamo dhidi yake na kujinyenyekeza mbele za Yehova kwa kujitiisha kwake kwa kupenda.—Mt. 6:10, 13; 1 Pet. 5:6-9.
7 Katika kutaniko la Kikristo, tunatambua ukichwa wa Kristo na mamlaka ambayo amempa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Jambo hilo huathiri jinsi tunavyowaona na kuwatendea wengine kutanikoni. Kujitiisha kwa mpango wa Mungu kutanikoni kutatuchochea kutii Neno la Mungu katika sehemu zote za ibada yetu. Utii huo unatia ndani huduma yetu, kuhudhuria na kushiriki mikutano, uhusiano wetu na wazee, na kuunga mkono mipango ya kitengenezo.—Mt. 24:45-47; 28:19, 20; Ebr. 10:24, 25; 13:7, 17.
8 Kujitiisha kwa Mungu huchangia amani, usalama, na utaratibu mzuri wa kutaniko la Kikristo. Watu wanaojitiisha kwa Mungu huonyesha sifa bora za Yehova. (1 Kor. 14:33, 40) Mambo ambayo tumejionea katika tengenezo la Yehova yametuchochea tuhisi kama Mfalme Daudi. Baada ya kuona tofauti kati ya watumishi wa Yehova na waovu, Daudi aliimba hivi kwa shangwe: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!”—Zab. 144:15.
9 Katika mpango wa ndoa na familia, “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” Wakati huohuo, wanaume nao wanapaswa kujitiisha kwa Kristo, nacho Kichwa cha Kristo ni Mungu. (1 Kor. 11:3) Wake wanapaswa kujitiisha kwa waume zao, na watoto kwa wazazi wao. (Efe. 5:22-24; 6:1) Kila mmoja katika familia anapotii kanuni ya ukichwa, kunakuwa na amani.
10 Mume anapaswa kutumia ukichwa kwa upendo, na hivyo kumwiga Kristo. (Efe. 5:25-29) Akitumia vizuri na kutopuuza ukichwa wake, mke na watoto wake hufurahia kujitiisha. Jukumu la mke ni kuwa msaidizi au kikamilisho. (Mwa. 2:18) Anapomheshimu na kumuunga mkono mume wake bila kulalamika, anapata kibali cha mume wake na kumletea Mungu sifa. (1 Pet. 3:1-4) Waume na wake wanapotii shauri la Biblia kuhusu ukichwa, wanawawekea watoto wao mfano mzuri wa kujitiisha kwa Mungu.
Ujitiisho wa kitheokrasi hugusa kila sehemu ya maisha
11 Kujitiisha kwa Mungu huathiri pia mtazamo wetu kuelekea “mamlaka zilizo kubwa,” ambazo “zimewekwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.” (Rom. 13:1-7) Wakiwa raia wanaotii sheria, Wakristo hulipa kodi, wakimlipa “Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.” (Mt. 22:21) Pia, mipango ya kuhubiri eneo kikamili hupatana na sheria za kulinda taarifa zinazotumiwa. Tukijitiisha na kuheshimu mamlaka halali katika mambo yote ambayo hayapingani na sheria ya Yehova ya uadilifu, tutatumia vizuri nguvu zetu zote katika kazi ya kuhubiri.—Marko 13:10; Mdo. 5:29.
12 Ujitiisho wa kitheokrasi hugusa kila sehemu ya maisha. Kwa macho ya imani, tunatazamia kuiona siku ambayo wanadamu wote watajitiisha kwa Yehova Mungu. (1 Kor. 15:27, 28) Wale wanaokubali kwa shangwe enzi kuu ya Yehova watabarikiwa sana wanapoendelea kujitiisha kwake kwa umilele wote!
-
-
Undugu Wenye UmojaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 16
Undugu Wenye Umoja
YEHOVA MUNGU alishughulika na Waisraeli kwa miaka 1,500 hivi wakiwa taifa lake. Baadaye, Yehova ‘alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’ (Mdo. 15:14) Watu kwa ajili ya jina la Yehova wangekuwa mashahidi wake, nao wangefikiri na kutenda kwa umoja popote walipo duniani. Kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake ingetokeza kukusanywa kwa watu kwa ajili ya jina la Mungu. Aliwaagiza hivi: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”—Mt. 28:19, 20.
Wewe ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wenye umoja ambao hawatenganishwi na tofauti za kitaifa, kikabila, au kiuchumi
2 Umekuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo kwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Wewe ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wenye umoja ambao hawatenganishwi na tofauti za kitaifa, kikabila, au kiuchumi. (Zab. 133:1) Kwa sababu hiyo, unawapenda na kuwaheshimu ndugu zako Wakristo kutanikoni. Huenda zamani usingeweza kushirikiana na baadhi yao kwa sababu ya tofauti za kijamii, kitaifa, au kielimu. Mmeunganishwa kwa upendo wa kindugu ulio imara na wenye nguvu kuliko uhusiano mwingine wowote wa kijamii, wa kidini, au wa familia.—Marko 10:29, 30; Kol. 3:14; 1 Pet. 1:22.
KUBADILI MTAZAMO
3 Ikiwa wengine wanaona ni vigumu kushinda ubaguzi wa rangi, wa kisiasa, wa kitabaka, au ubaguzi wa aina nyingine yoyote, wanaweza kuwafikiria Wakristo Wayahudi wa karne ya kwanza, ambao walihitaji kufanya juu chini ili waache kuwabagua watu wengine ambao hawakuwa wa dini ya Kiyahudi. Petro alipoagizwa aende nyumbani kwa Kornelio, ofisa wa jeshi wa kikosi cha Roma, Yehova alimtayarisha Petro kwa ajili ya mgawo huo kwa njia ya fadhili.—Matendo sura ya 10.
4 Katika maono, Petro aliambiwa achinje na kula wanyama fulani waliokuwa najisi kulingana na desturi za Wayahudi. Petro alipokataa, sauti kutoka mbinguni ilimwambia: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” (Mdo. 10:15) Mungu alihitaji kuingilia kati ili Petro abadili mtazamo wake kuhusu mgawo ambao angepewa wa kwenda kumtembelea mtu wa mataifa. Alipotii mwelekezo wa Yehova, Petro aliwatangazia hivi wale waliokusanyika: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine, lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi. Basi nilipoitwa nilikuja bila kupinga.” (Mdo. 10:28, 29) Baadaye, Petro alijionea uthibitisho wa kwamba Yehova alikuwa amemkubali Kornelio na watu wa nyumbani mwake.
5 Sauli wa Tarso, Farisayo mwenye elimu ya juu, alihitaji kujinyenyekeza ili kushirikiana na watu wa jamii ambayo hapo zamani hangekubali kushirikiana nao. Hata alihitaji kukubali mwongozo kutoka kwao. (Mdo. 4:13; Gal. 1:13-20; Flp. 3:4-11) Ni wazi kwamba watu kama vile Sergio Paulo, Dionisio, Damari, Filemoni, Onesimo, na wengine walihitaji kubadili kabisa mtazamo wao walipokubali habari njema na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Mdo. 13:6-12; 17:22, 33, 34; Flm. 8-20.
KUDUMISHA UMOJA WETU WA ULIMWENGUNI POTE
6 Bila shaka upendo wa ndugu na dada katika kutaniko lenu ulikusaidia umkaribie Yehova na tengenezo lake. Uliona alama ya pekee ya upendo na umoja ambayo inawatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, kama alivyosema: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:34, 35) Ulimthamini zaidi Yehova na tengenezo lake ulipotambua kwamba upendo unaoonyeshwa kutanikoni ni kionjo tu cha upendo unaoonyeshwa na ushirika wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova. Unajionea utimizo wa unabii wa Biblia wa kukusanywa kwa watu katika siku za mwisho ili wamwabudu Yehova kwa amani na umoja.—Mika 4:1-5.
7 Kwa kuwa kuna mambo mengi leo yanayosababisha migawanyiko, ni nani angefikiri kwamba ingewezekana kuwaunganisha watu “kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha”? (Ufu. 7:9) Fikiria tofauti zilizopo kati ya jamii ya watu wenye elimu ya kisasa na wale wanaoshikilia desturi za kale za kikabila. Hebu fikiria mizozo ya kidini kati ya watu wa kabila na taifa moja. Kwa sababu ya uzalendo, watu wamegawanyika zaidi kisiasa kuliko wakati mwingine wowote. Pia, unapofikiria tofauti kubwa za kiuchumi na mambo mengine mengi yanayosababisha migawanyiko, kuwaunganisha watu wa mataifa, lugha, vikundi, na tabaka mbalimbali katika kifungo kisichoweza kuvunjika cha upendo na amani, ni muujiza ambao unaweza kufanywa tu na Mungu Mweza-Yote.—Zek. 4:6.
8 Lakini umoja huo ni halisi, na ulipojiweka wakfu na kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, ulijiunga na undugu huo. Ili ufaidike na umoja huo, una jukumu la kuudumisha. Unaweza kufanya hivyo kwa kutii maneno ya mtume Paulo katika Wagalatia 6:10: “Tukiwa bado na nafasi, acheni tuwatendee watu wote mema, na hasa wale ambao ni ndugu zetu katika imani.” Pia, tunafuata ushauri huu: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” (Flp. 2:3, 4) Maadamu tunajizoeza kuwaona ndugu na dada zetu kama Yehova anavyowaona, wala si kulingana na wanavyoonekana kwa nje, tutaendelea kufurahia uhusiano wenye amani pamoja nao.—Efe. 4:23, 24.
KUTUNZANA
9 Kama mtume Paulo alivyofafanua, wote kutanikoni hawana mgawanyiko, bali ni viungo vya mwili mmoja vinavyotunzana kwa njia ileile. (1 Kor. 12:14-26) Huenda tukawa mbali sana na baadhi ya ndugu zetu, lakini bado tunawahangaikia. Baadhi ya ndugu zetu wakiteswa, sisi huhuzunika sana. Ikiwa baadhi ya akina ndugu wana uhitaji fulani au wamekumbwa na msiba, vita, au mizozo ya kikabila, sisi sote hujitahidi sana kutafuta njia za kuwasaidia kiroho na vilevile kimwili.—2 Kor. 1:8-11.
10 Kila siku sisi sote tunapaswa kusali kwa ajili ya ndugu zetu. Kuna ndugu wanaoshawishiwa kufanya mambo mabaya. Huenda mateso ya baadhi ya ndugu zetu yanajulikana. Hata hivyo huenda tusijue upinzani ambao wengine wanakabili kila siku kutoka kwa wafanyakazi wenzao na familia zilizogawanyika kidini. (Mt. 10:35, 36; 1 The. 2:14) Sote tunahangaishwa na hali hizo kwa sababu sisi ni undugu wa ulimwenguni pote. (1 Pet. 5:9) Pia, miongoni mwetu tuna wale wanaofanya utumishi wa Yehova kwa bidii, wakiongoza katika kazi ya kuhubiri na kusimamia makutaniko. Na kuna wale wanaosimamia kazi ya ulimwenguni pote. Wote wanahitaji sala zetu, na kupitia sala, tunaonyesha kwamba tunawajali na kuwapenda ndugu zetu kikweli hata wakati ambapo hakuna lolote ambalo sisi wenyewe tunaweza kufanya ili kuwasaidia.—Efe. 1:16; 1 The. 1:2, 3; 5:25.
11 Kwa sababu ya misukosuko ya siku hizi za mwisho, watu wa Yehova wanapaswa kuwa tayari kusaidiana. Wakati mwingine, majanga kama vile matetemeko ya nchi na mafuriko yanapotokea, huenda tukahitaji kukusanya na kutuma misaada mingi ya kimwili. Wakristo wa karne ya kwanza waliweka mfano mzuri katika jambo hilo. Wakikumbuka ushauri wa Yesu, wanafunzi huko Antiokia walifurahi kutuma msaada kwa ndugu zao waliokuwa Yudea. (Mdo. 11:27-30; 20:35) Baadaye, mtume Paulo aliwatia moyo Wakorintho waunge mkono mipango ya kutoa msaada kwa utaratibu. (2 Kor. 9:1-15) Leo, ndugu zetu wanapopatwa na hali ngumu na kuhitaji msaada, tengenezo na Wakristo mmoja-mmoja hutenda haraka na kuandaa msaada unaohitajika.
WAMECHAGULIWA ILI KUFANYA MAPENZI YA YEHOVA
12 Undugu wetu wenye umoja wa ulimwenguni pote umepangwa ili kufanya mapenzi ya Yehova. Wakati huu, mapenzi yake ni kwamba habari njema ya Ufalme ihubiriwe katika dunia yote ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote. (Mt. 24:14) Tunapofanya kazi hiyo, ni mapenzi ya Yehova kwamba sikuzote mwenendo wetu upatane na viwango vyake vya juu vya maadili. (1 Pet. 1:14-16) Ili kutimiza kazi ya Yehova, sote tunapaswa kuwa tayari kujitiisha kila mmoja kwa mwenzake na kuunga mkono kazi ya kuhubiri habari njema. (Efe. 5:21) Huu si wakati wa kutafuta mapendezi yetu bali ni wakati wa kujitahidi kabisa kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwetu. (Mt. 6:33) Tunapozingatia jambo hilo na kufanya kazi pamoja kwa umoja kwa ajili ya habari njema, tunaridhika na kupata shangwe sasa na kutazamia baraka za milele.
13 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi ni watu wa pekee, watu waliochaguliwa kutoka kwa wanadamu wengine wakiwa watu safi ili tumtumikie Mungu wetu kwa bidii. (Tito 2:14) Ibada yetu kwa Yehova inatufanya tuwe tofauti. Mbali na kufanya kazi bega kwa bega na ndugu zetu duniani pote, tunazungumza lugha moja ya kweli na kutenda kupatana na kweli tunayozungumza. Hilo lilitabiriwa Yehova alipotangaza hivi kupitia nabii Sefania: “Nitabadili lugha ya mataifa iwe lugha safi, ili wote waweze kuliitia jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.
14 Kisha, kupitia roho takatifu, Yehova alimwongoza Sefania kufafanua undugu wa ulimwenguni pote ambao ni halisi leo: “Waisraeli watakaobaki hawatatenda mambo yasiyo ya uadilifu; hawatasema uwongo, wala hawatakuwa na ndimi za udanganyifu vinywani mwao; watakula na kulala, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.” (Sef. 3:13) Baada ya kuelewa Neno la Yehova la kweli, kufanya upya akili zetu, na kupatanisha maisha yetu na viwango vya Yehova, tunaweza kufanya kazi kwa umoja. Tunatimiza mambo ambayo wale walio na mtazamo wa kimwili wanafikiri kwamba haiwezekani kuyatimiza. Kwa kweli, sisi ni watu tofauti, watu wa Mungu, tunaomletea heshima duniani pote.—Mika 2:12.
-
-
Shikamana na Tengenezo la YehovaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 17
Shikamana na Tengenezo la Yehova
MWANAFUNZI Yakobo aliandika hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Ijapokuwa sisi si wakamilifu, Yehova hayuko juu sana au mbali sana asiweze kusikia sala zetu. (Mdo. 17:27) Tunawezaje kumkaribia Mungu? Kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unaotia ndani kusali kwa bidii. (Zab. 39:12) Pia, tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu kwa kujifunza kwa ukawaida Neno lake, Biblia. Tunapofanya hivyo, tunazidi kumjua Yehova Mungu, makusudi yake, na mapenzi yake. (2 Tim. 3:16, 17) Kwa njia hiyo, tunajifunza kumpenda Yehova, tunasitawisha woga unaofaa na kuepuka kumchukiza.—Zab. 25:14.
2 Hata hivyo, njia pekee ya kumkaribia Yehova ni kupitia Mwana wake, Yesu. (Yoh. 17:3; Rom. 5:10) Hakuna mwanadamu anayeweza kutusaidia kufahamu maoni na hisia za Yehova kama alivyofanya Yesu. Alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yake hivi kwamba alisema hivi: “Hakuna mtu anayemjua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Kwa hiyo, tunapojifunza mambo ambayo Injili zinafunua kuhusu maoni na hisia za Yesu, kwa kweli tunajifunza maoni na hisia za Yehova. Ujuzi huo unatuwezesha kumkaribia zaidi Mungu wetu.
3 Chini ya ukichwa wa Mwana wa Mungu, tunasitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova kwa kushikamana na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova linalotufundisha kufanya mapenzi ya Mungu. Kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:45-47, Bwana, Yesu Kristo, amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ili aliandalie kutaniko ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ Leo, mtumwa mwaminifu hutuandalia chakula kingi cha kiroho. Kupitia mtumwa huyo, Yehova hutushauri tusome Neno lake kila siku, tuhudhurie mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri “habari njema ya Ufalme.” (Mt. 24:14; 28:19, 20; Yos. 1:8; Zab. 1:1-3) Hatutaki kamwe kuwa na maoni yasiyofaa kuelekea mtumwa huyo. Tunapaswa kujitahidi kushikamana na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova na kufuata mwelekezo wake. Hilo litatufanya tumkaribie zaidi Mungu wetu, Yehova, na litatuimarisha na kutulinda licha ya majaribu.
KWA NINI MAJARIBU YANAONGEZEKA?
4 Labda umekuwa katika kweli kwa miaka mingi. Ikiwa ndivyo, bila shaka unajua changamoto za kuvumilia utimilifu wetu unapojaribiwa. Hata ikiwa umeanza kumjua Yehova na kushirikiana na watu wake hivi karibuni, bila shaka unajua kwamba Shetani Ibilisi humpinga mtu yeyote anayejitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova. (2 Tim. 3:12) Hivyo, iwe umevumilia machache au mengi, usiogope wala kuvunjika moyo. Yehova anaahidi kwamba atakutegemeza na kukuthawabisha kwa kukukomboa na kukupa uzima wakati ujao.—Ebr. 13:5, 6; Ufu. 2:10.
5 Huenda sote tukakabili majaribu makali katika siku hizi za mwisho za mfumo wa Shetani. Tangu Ufalme wa Mungu uliposimamishwa mwaka wa 1914, Shetani hajaruhusiwa kuingia kwenye mbingu za Yehova. Yeye na malaika zake waovu wamekuwa duniani tangu walipotupwa kutoka mbinguni. Ongezeko la ole duniani, kutia ndani kuongezeka kwa mateso dhidi ya watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, ni matokeo ya hasira ya Shetani na ni uthibitisho kwamba tunaishi katika siku za mwisho za utawala mwovu wa Shetani juu ya wanadamu.—Ufu. 12:1-12.
6 Akiwa na hasira kwa sababu ya kushushwa, Shetani anajua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati. Akisaidiwa na roho wake waovu, yeye hujitahidi juu chini kuvuruga kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kuvunja umoja wa watumishi wa Yehova. Kwa hiyo, tunapigana vita vya kiroho vinavyofafanuliwa kuwa “[mapambano], si dhidi ya damu na mwili, bali dhidi ya serikali, dhidi ya mamlaka, dhidi ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Ili tushinde na kubaki upande wa Yehova, hatupaswi kukata tamaa na kuacha kupigana bali tunapaswa kuendelea kuvaa mavazi kamili ya silaha zetu za kiroho. Ni lazima ‘tusimame imara dhidi ya matendo yenye hila ya Ibilisi.’ (Efe. 6:10-17) Ili tufanye hivyo, tunahitaji kuwa na uvumilivu.
KUSITAWISHA UVUMILIVU
7 Uvumilivu ni “uwezo wa kustahimili hali ngumu, taabu, au mkazo.” Katika Biblia, uvumilivu unafafanuliwa kuwa sifa ya kuwa thabiti katika kufanya yaliyo sawa licha ya hali ngumu, upinzani, mateso, au jambo lolote linalokusudiwa kutukengeusha tuache azimio letu la kuwa watimilifu kwa Mungu. Lazima uvumilivu wa Kikristo usitawishwe. Hilo linahitaji muda. Uwezo wetu wa kuvumilia huongezeka kadiri tunavyofanya maendeleo ya kiroho. Tunapovumilia majaribu madogo ya imani yetu tangu mwanzo wa maisha yetu ya Kikristo, tunapata nguvu zaidi za kuvumilia majaribu magumu zaidi tutakayokabili. (Luka 16:10) Hatupaswi kungoja mpaka tukabili majaribu makubwa ndipo tuazimie kusimama imara katika imani. Tunapaswa kufanya uamuzi thabiti kabla ya majaribu kuja. Akionyesha kwamba tunapaswa kusitawisha uvumilivu pamoja na sifa nyingine za Kikristo, mtume Petro aliandika hivi: “Jitahidini kabisa kuongeza kwenye imani yenu wema wa adili, kwenye wema wenu wa adili ujuzi, kwenye ujuzi wenu kujizuia, kwenye kujizuia kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu ujitoaji-kimungu, kwenye ujitoaji-kimungu wenu upendo wa kindugu, kwenye upendo wenu wa kindugu upendo.”—2 Pet. 1:5-7; 1 Tim. 6:11.
Uvumilivu wetu huongezeka siku baada ya siku tunapokabiliana na kushinda majaribu
8 Umuhimu wa kusitawisha uvumilivu unakaziwa katika maneno haya yaliyoandikwa na Yakobo: “Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapopata majaribu mbalimbali, mkijua kwamba sifa iliyojaribiwa ya imani yenu hutokeza uvumilivu. Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yak. 1:2-4) Yakobo anasema kwamba Wakristo wanapaswa kuyakubali majaribu na kuyaona kuwa shangwe kwa sababu yanatusaidia kusitawisha uvumilivu. Je, hivyo ndivyo unavyoyaona majaribu? Kisha Yakobo anaonyesha kwamba uvumilivu wenyewe una kazi ya kufanya katika kukamilisha utu wetu wa Kikristo na kutufanya tuwe wenye kukubalika kabisa mbele za Mungu. Naam, uvumilivu wetu huongezeka siku baada ya siku tunapokabiliana na kushinda majaribu. Nao, uvumilivu hutokeza sifa nyingine zenye kupendeza tunazohitaji.
9 Uvumilivu wetu unampendeza Yehova; utamchochea atupe thawabu ya uzima wa milele. Yakobo alisema hivi pia: “Mwenye furaha ni yule anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu atakapokubaliwa atapokea taji la uzima, ambalo Yehova aliwaahidi wale wanaoendelea kumpenda.” (Yak. 1:12) Naam, tunachochewa kuvumilia kwa sababu tunatarajia kupata uzima. Tusipovumilia, hatuwezi kuendelea kuwa katika kweli. Tukishindwa na mikazo ya ulimwengu, tutarudi katika ulimwengu. Tusipovumilia, hatutaendelea kuwa na roho ya Yehova, na hivyo, hatutaweza kuzaa tunda la roho yake maishani mwetu.
10 Ili tuendelee kuvumilia katika nyakati hizi ngumu, tunahitaji kuwa na maoni yanayofaa kuhusu kuteseka tukiwa Wakristo. Kumbuka kwamba Yakobo aliandika hivi: “Oneni yote kuwa shangwe.” Huenda isiwe rahisi kudumisha shangwe tunapoteseka kimwili au kiakili. Hata hivyo, kumbuka kwamba uhai wetu wa wakati ujao unahusika. Mfano wa mitume unatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kushangilia tunapoteseka. Simulizi moja linapatikana katika kitabu cha Matendo, na linasema hivi: “Wakawaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu, kisha wakawaacha waende. Basi wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 5:40, 41) Walielewa kwamba mateso yao ni uthibitisho wa kwamba wanatii amri ya Yesu na kwamba wana kibali cha Yehova. Miaka kadhaa baadaye, alipokuwa akiandika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho, Petro alitaja faida za kuteseka kwa ajili ya uadilifu.—1 Pet. 4:12-16.
11 Mfano mwingine ni ule wa Paulo na Sila. Walipokuwa katika kazi ya umishonari huko Filipi, walikamatwa na kushtakiwa kwa kulisumbua jiji na kutangaza desturi zisizo halali. Matokeo ni kwamba walipigwa vibaya na kutupwa gerezani. Simulizi hilo la Biblia linatuambia kwamba walipokuwa gerezani wakiwa bado na majeraha, “karibu katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo, nao wafungwa walikuwa wakiwasikiliza.” (Mdo. 16:16-25) Paulo na mwenzake waliyaona mateso yao kwa ajili ya Kristo kuwa uthibitisho wa utimilifu wao mbele za Mungu na wanadamu, na vilevile kuwa njia ya kutoa ushahidi zaidi kwa wale ambao huenda wakawa na mwelekeo wa kusikiliza habari njema. Uhai wa wengine ulihusika. Usiku huohuo, mlinzi wa jela na watu wa nyumbani mwake walisikiliza na kuwa wanafunzi. (Mdo. 16:26-34) Paulo na Sila walimtumaini Yehova, nguvu zake, na nia yake ya kuwategemeza katika mateso yao. Hawakukata tamaa.
12 Leo pia, Yehova ametuandalia yote tunayohitaji ili kututegemeza nyakati za majaribu. Anataka tuvumilie. Ametupa Neno lake lililoongozwa na roho ambamo tunapata ujuzi sahihi kuhusu kusudi lake. Hilo huimarisha imani yetu. Tuna fursa za kushirikiana na waamini wenzetu, na kufanya utumishi mtakatifu. Pia tuna pendeleo la kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova mwenyewe kupitia sala. Yeye husikiliza tunapomsifu na kumwomba kwa bidii atusaidie kudumisha msimamo safi mbele zake. (Flp. 4:13) Hatuwezi pia kupuuza nguvu tunazopata kwa kutafakari tumaini lililowekwa mbele yetu.—Mt. 24:13; Ebr. 6:13; Ufu. 21:1-4.
KUVUMILIA MAJARIBU MBALIMBALI
13 Majaribu tunayokabili leo ni kama yale ambayo wanafunzi wa Yesu Kristo wa karne ya kwanza walikabili. Leo, Mashahidi wa Yehova wametukanwa na kuteswa na wapinzani ambao wameambiwa habari za uwongo kuwahusu. Kama ilivyokuwa katika siku za mitume, upinzani mwingi huchochewa na wafuasi sugu wa dini ambazo mafundisho na mazoea yake ya uwongo hushutumiwa katika Neno la Mungu. (Mdo. 17:5-9, 13) Nyakati nyingine, watu wa Yehova hupata kitulizo kwa kudai haki za kisheria zilizowekwa na serikali za kisiasa. (Mdo. 22:25; 25:11) Hata hivyo, watawala pia wamepiga marufuku kazi yetu, wakijaribu kukomesha huduma yetu ya Kikristo. (Zab. 2:1-3) Chini ya hali kama hizo, sisi hufuata kwa ujasiri mfano wa mitume waaminifu na kuendelea ‘kumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’—Mdo. 5:29.
14 Kadiri roho ya uzalendo inavyozidi kuongezeka duniani pote, ndivyo wahubiri wa habari njema wanavyoshinikizwa zaidi waache huduma yao waliyopewa na Mungu. Watumishi wote wa Mungu wanafahamu vizuri zaidi onyo lililo kwenye Ufunuo 14:9-12 kuhusu kumwabudu “yule mnyama wa mwituni na sanamu yake.” Tunaelewa umuhimu wa maneno haya ya Yohana: “Hapa ndipo watakatifu wanapohitaji uvumilivu, wale wanaoshika amri za Mungu na kushika imara imani kwa Yesu.”
15 Majaribu yanayosababishwa na vita, mapinduzi, au mateso na marufuku yanaweza kufanya iwe vigumu kuendelea na ibada ya Kikristo hadharani. Huenda msiweze kufanya mikutano mkiwa kutaniko. Huenda msiweze kuwasiliana na ofisi ya tawi. Huenda ziara za waangalizi wa mzunguko zikakatishwa. Huenda machapisho yasifike. Lolote kati ya mambo hayo likitokea, mtafanya nini?
16 Jibu ni, fanyeni mambo mnayoweza kufanya kadiri hali zenu zinavyoruhusu. Huenda isiwe vigumu kujifunza kibinafsi. Kwa kawaida vikundi vidogo vinaweza kukutana katika nyumba za akina ndugu ili kujifunza. Biblia na machapisho tuliyojifunza wakati uliopita yanaweza kutumiwa katika mikutano hiyo. Usiogope wala kuwa na wasiwasi. Kwa vyovyote vile, Baraza Linaloongoza litatafuta haraka njia ya kuwasiliana na ndugu wenye madaraka.
17 Hata ukiwa mbali na ndugu zako Wakristo, kumbuka kwamba Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo hawako mbali nawe. Tumaini lako linaweza kuendelea kuwa imara. Bado Yehova anaweza kusikia sala zako na kukuimarisha kwa roho yake. Mtegemee akuongoze. Kumbuka kwamba wewe ni mtumishi wa Yehova na mwanafunzi wa Yesu Kristo. Kwa hiyo, tumia vizuri fursa za kuhubiri unazopata. Yehova atabariki jitihada zako, na muda si muda, huenda wengine wakajiunga nawe katika ibada ya kweli.—Mdo. 4:13-31; 5: 27-42; Flp. 1: 27-30; 4: 6, 7; 2 Tim. 4:16-18.
18 Hata unapokabili kifo kama mitume na wengine, mtumaini “Mungu ambaye huwafufua wafu.” (2 Kor. 1:8-10) Kuamini tumaini la ufufuo kunaweza kukusaidia kuvumilia hata upinzani mkali sana. (Luka 21:19) Kristo Yesu alituwekea mfano; alijua kwamba uaminifu wake chini ya jaribu ungewaimarisha wengine ili wavumilie. Unaweza kuwaimarisha ndugu zako kwa njia hiyohiyo.—Yoh. 16:33; Ebr. 12:2, 3; 1 Pet. 2:21.
19 Mbali na mateso na upinzani, huenda ukalazimika kuvumilia hali nyingine ngumu. Kwa mfano, wengine wamevunjika moyo kwa sababu watu katika eneo lao hawapendezwi na habari njema. Wengine wamepambana na magonjwa ya kimwili au kihisia au kuvumilia hali nyingine zinazosababishwa na udhaifu wa kibinadamu. Nyakati nyingine mtume Paulo alivumilia jaribu fulani lililoathiri au kufanya utumishi wake uwe mgumu. (2 Kor. 12:7) Pia, Epafrodito, Mkristo katika karne ya kwanza kutoka Filipi, ‘alihuzunika kwa sababu rafiki zake walisikia alikuwa mgonjwa.’ (Flp. 2:25-27) Kutokamilika kwetu na kwa wengine kunaweza pia kusababisha matatizo ambayo si rahisi kuyavumilia. Kutoelewana kunaweza kutokea kati yetu na Wakristo wenzetu au watu wa familia. Hata hivyo, kufuata shauri la Neno la Yehova kunaweza kutusaidia kuvumilia na kushinda matatizo kama hayo.—Eze. 2:3-5; 1 Kor. 9:27; 13:8; Kol. 3:12-14; 1 Pet. 4:8.
AZIMIA KUENDELEA KUWA MWAMINIFU
20 Ni lazima tushikamane na yule ambaye Yehova amemweka rasmi kuwa Kichwa cha kutaniko, Kristo Yesu. (Kol. 2:18, 19) Tunahitaji kushirikiana na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na pia wale waliowekwa rasmi kuwa waangalizi. (Ebr. 13:7, 17) Tukifuata kwa ukaribu mipango ya kitheokrasi na kushirikiana na wale wanaoongoza, tutakuwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova. Tunahitaji kutumia kikamili pendeleo la sala. Kumbuka kwamba kuta za gereza wala kifungo cha upweke hakiwezi kutuzuia kuwasiliana na Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo wala kuvuruga umoja uliopo kati yetu na waamini wenzetu.
21 Kwa uvumilivu, na tuazimie kufanya yote tunayoweza ili kutimiza utume wetu wa kuhubiri, tukidumu katika kazi ambayo Yesu Kristo aliyefufuliwa aliwaagiza wafuasi wake wafanye: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru. Na tazama! mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Kama Yesu, natuvumilie. Acheni tukazie macho tumaini la Ufalme na tarajio la uzima wa milele lililo mbele yetu. (Ebr. 12:2) Tukiwa wanafunzi waliobatizwa wa Kristo, tuna pendeleo la kushiriki kutimiza unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Alisema hivi: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:3, 14) Tukifanya kazi hiyo kwa moyo wetu wote wakati huu, tutafurahia uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu!
-
-
NyongezaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
Nyongeza
Ujumbe kwa Wazazi Wakristo:
Ukiwa mzazi, ungependa kuwasaidia watoto wako wapendwa wampende Yehova na kujiweka wakfu kwake. Unaweza kufanya nini ili uwasaidie wajitayarishe kwa ajili ya ubatizo? Utajuaje kwamba wako tayari kwa ajili ya hatua hiyo muhimu?
Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwabatiza.’ (Mt. 28:19) Kulingana na agizo hilo, takwa la msingi ili mtu astahili kubatizwa ni kuwa mwanafunzi, yaani, anapaswa kuelewa, kuamini, na kujitahidi kuishi kupatana na mafundisho ya Yesu. Hata watoto wanaweza kutimiza jambo hilo.
Wawekee watoto wako kielelezo chema, na ukazie sheria za Yehova mioyoni mwao. (Kum. 6:6-9) Unaweza kutumia habari zilizo katika kitabu Furahia Maisha Milele! ili kuwafundisha kweli za msingi na jinsi ya kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Wasaidie watoto wako wajue jinsi ya kueleza mambo wanayoamini kwa maneno yao wenyewe wanapoongea na wengine. (1 Pet. 3:15) Kitia-moyo na ujuzi wanaopokea kutoka kwako pamoja na mambo wanayojifunza kibinafsi, ibada ya familia, mikutano ya kutaniko, na marafiki wazuri, yatawasaidia kufikia ubatizo na kufanya maendeleo zaidi. Wasaidie wajiwekee miradi ya kiroho.
-