-
Mtu Aliyeubadili UlimwenguMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Mtu Aliyeubadili Ulimwengu
Mabilioni ya watu wameishi duniani. Wengi wao wamesahaulika. Hata hivyo, wachache wamebadili hali ya watu ulimwenguni na yaelekea hata maisha yako ya kila siku.
UNAAMKA asubuhi ili kujitayarisha kwenda kazini. Unawasha taa kabla ya kuanza kujitayarisha. Unachukua kitabu au gazeti la kusoma unaposafiri kwa basi kuelekea kazini. Unakumbuka kutumia dawa ambayo umepewa na daktari kwa sababu umeambukizwa ugonjwa fulani. Ni mapema asubuhi, lakini tayari umenufaika na kazi ya watu wachache maarufu.
Michael Faraday Mwanafizikia huyu Mwingereza alizaliwa mwaka wa 1791. Alibuni mota ya umeme na chombo cha kuzalisha umeme kinachoitwa dainamo. Mambo aliyovumbua na vitu alivyobuni vimewawezesha wanadamu kutumia umeme kwa njia nyingi.
Ts’ai Lun Alikuwa afisa wa maliki wa China aliyebuni njia ya kutengeneza karatasi yapata mwaka wa 105 W.K. Ubuni huo ulisaidia kutengeneza karatasi kwa wingi sana.
Johannes Gutenberg Mnamo mwaka wa 1450, mvumbuzi huyu Mjerumani alibuni mashine ya kwanza ya kuchapia yenye herufi za kupangwa. Kwa sababu ya mashine hii, gharama za kuchapa zilipungua na hivyo watu wengi waliweza kusoma habari nyingi kuhusu mambo mbalimbali.
Alexander Fleming Mtafiti huyu Mskoti alivumbua dawa ya kuua viini aliyoiita penisilini mnamo mwaka wa 1928. Dawa za kutibu magonjwa yanayosababishwa na viini, au bakteria, zinatumiwa sana leo.
Bila shaka, uvumbuzi na vitu vilivyobuniwa na watu wachache vimewanufaisha watu wengi sana au kuboresha afya zao.
Hata hivyo, mtu mmoja amewapita wote. Umaarufu wake hautokani na uvumbuzi fulani wa kisayansi au kitiba. Badala yake, mtu huyu aliyelelewa na wazazi maskini na aliyekufa karibu miaka 2,000 iliyopita, alihubiri ujumbe wenye nguvu wa tumaini na faraja. Tunapofikiria kiwango ambacho ujumbe wake umewanufaisha watu duniani kote, wengi wanakubali kwamba yeye ndiye aliyeubadili ulimwengu kikweli.
Mtu huyu ni Yesu Kristo. Alihubiri ujumbe gani? Na wewe unaweza kunufaika na ujumbe wake jinsi gani?
-
-
Yesu Kristo—Nguvu ya Ujumbe WakeMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Yesu Kristo—Nguvu ya Ujumbe Wake
“Bila shaka jambo linalothibitisha kwamba mtu huyu mwenye hekima kutoka Kapernaumu alikuwa mtu wa pekee ni kwamba bado watu wanauamini na kuupenda ujumbe wake.”a—MWANDISHI GREGG EASTERBROOK.
MANENO yana nguvu. Yanapochaguliwa vizuri, yanaweza kuchochea mioyo ya watu, kuwapa tumaini, na kubadili maisha yao. Hakuna mtu mwingine ambaye amewahi kusema maneno yenye nguvu kama Yesu Kristo. Mtu fulani aliyesikiliza Mahubiri ya Mlimani ya Yesu, aliandika hivi baadaye: “Basi wakati Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.”—Mathayo 7:28.
Mpaka leo hii, watu duniani kote wanajua semi nyingi za Yesu. Fikiria baadhi ya semi zake zenye kujaa maana.
“Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—Mathayo 6:24.
“Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
“Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.”—Mathayo 22:21.
“Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Yesu alifanya mengi zaidi ya kusema semi muhimu na zisizosahaulika. Ujumbe aliohubiri ulikuwa wenye nguvu kwa sababu ulifunua ukweli kumhusu Mungu, uliwapa watu kusudi maishani, na ulionyesha wazi kwamba suluhisho la matatizo ya wanadamu ni Ufalme wa Mungu. Tunapochunguza mafundisho ya Yesu katika kurasa zinazofuata, tutaona kwa nini mamilioni ya watu bado “wanauamini na kuupenda ujumbe wake.”
[Maelezo ya Chini]
-
-
Mambo Ambayo Yesu Alifundisha KujihusuMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kujihusu
“Yesu hakuwa na shaka lolote kujihusu, kuhusu mahali alipotoka, sababu iliyofanya aje duniani, au kuhusu wakati wake ujao.”—MWANDISHI HERBERT LOCKYER.
KABLA ya kukubali na kuamini mambo ambayo Yesu alifundisha, tunahitaji kumjua kwa kadiri fulani. Kwa kweli, Yesu alikuwa nani? Alitoka wapi? Alikuwa na kusudi gani maishani? Tunaposoma vitabu vya Injili, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, ni kana kwamba Yesu anajibu maswali hayo.
Aliishi mbinguni kabla ya kuzaliwa duniani Yesu alisema: “Kabla ya Abrahamu kuwako, mimi nimekuwako.” (Yohana 8:58) Abrahamu aliishi miaka 2,000 hivi kabla ya Yesu kuzaliwa hapa duniani. Na bado, Yesu alikuwapo kabla ya mtu huyu mwaminifu kuishi duniani. Basi, Yesu aliishi wapi wakati huo? Alieleza hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni.”—Yohana 6:38.
Mwana wa Mungu Yehova ana wana wengi ambao ni malaika. Hata hivyo, Yesu ni wa pekee. Alijiita “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu.” (Yohana 3:18) Maneno hayo yanamaanisha kwamba ni Yesu peke yake aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Mwana huyu mzaliwa-pekee alitumiwa na Mungu kuumba vitu vingine vyote.—Wakolosai 1:16.
“Mwana wa binadamu” Alipojirejelea, Yesu alitumia maneno hayo mara nyingi kuliko majina mengine yoyote. (Mathayo 8:20) Kwa njia hiyo, alionyesha kwamba hakuwa malaika aliyetokea katika mwili wa binadamu. Alikuwa mwanadamu kabisa. Kupitia roho takatifu, Mungu alihamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni mpaka duniani, na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira Maria. Hivyo, Yesu alizaliwa akiwa binadamu mkamilifu asiye na dhambi.—Mathayo 1:18; Luka 1:35; Yohana 8:46.
Masihi aliyeahidiwa Mwanamke Msamaria alimwambia Yesu hivi: “Ninajua kwamba Masihi anakuja.” Yesu akamwambia: “Mimi ninayesema nawe ndiye.” (Yohana 4:25, 26) Maneno “Masihi” na “Kristo” yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Yesu alitiwa mafuta au kuteuliwa na Mungu, ili atimize sehemu ya pekee kuhusiana na ahadi za Mungu.
Kazi yake kuu Yesu alisema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Ingawa aliwafanyia watu mambo mengi mema, jambo muhimu maishani mwake lilikuwa kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Baadaye tutazungumzia mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu Ufalme.
Kwa kweli, Yesu alikuwa mtu wa pekee.a Kama tutakavyoona, maneno aliyosema akiwa duniani yalikuwa na maana kubwa zaidi kwa sababu alikuwa ameishi mbinguni kabla ya kuja duniani. Basi, haishangazi kwamba alihubiri ujumbe ambao ungewanufaisha mamilioni ya watu kote duniani.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kumhusu Yesu na sehemu yake katika kusudi la Yehova, ona sura ya 4 katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kumhusu MunguMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Mambo Ambayo Yesu Alifundisha Kumhusu Mungu
‘Hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na yeyote yule ambaye Mwana atapenda kumfunulia.’—LUKA 10:22, BIBLIA HABARI NJEMA.
ALIPOISHI mbinguni kabla ya kuja duniani, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa na uhusiano wa karibu na Baba yake kwa muda mrefu sana. (Wakolosai 1:15) Kwa hiyo, Mwana huyo alipata kuelewa mawazo, hisia, na njia za Baba yake. Baadaye, Mwana huyo alipokuja duniani kama mwanadamu na kuitwa Yesu, alikuwa na hamu ya kufundisha ukweli kumhusu Baba yake. Tunaweza kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kusikiliza mambo ambayo Mwana huyu alisema.
Jina la Mungu Yesu aliliona jina la Mungu, Yehova, kuwa muhimu sana. Mwana huyo mpendwa alitaka wengine walijue jina la Baba yake na kulitumia. Jina la Yesu linamaanisha “Yehova ni Wokovu.” Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha jina lako.” (Yohana 17:26) Haishangazi kwamba Yesu alilitumia jina la Mungu na kuwaeleza wengine kulihusu. Wasikilizaji wake hawangeweza kuelewa ukweli kumhusu Yehova kama hawangejua jina Lake na maana ya jina hilo.a
Upendo mkuu wa Mungu Yesu alisema hivi aliposali: “Baba, . . . ulinipenda kabla ya kuwekwa kwa msingi wa ulimwengu.” (Yohana 17:24) Yesu alikuwa amejionea upendo wa Mungu mbinguni, kwa hiyo, alipokuwa duniani alitaka watu wajue jinsi Mungu anavyoonyesha upendo huo kwa njia nyingi mbalimbali.
Yesu alionyesha kwamba watu wengi sana wanaweza kunufaika na upendo wa Yehova. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Katika andiko hili, neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ulimwengu” halimaanishi “dunia.” Katika muktadha huu, neno hili linarejelea wanadamu, kwa kweli, wanadamu wote. Upendo wa Mungu ni mwingi sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake mpendwa ili wanadamu waaminifu waweze kuwekwa huru kutokana na dhambi na kifo, na hivyo, wawe na tumaini la kuishi milele. Hatuwezi kuelewa kabisa kina cha upendo wa Mungu.—Waroma 8:38, 39.
Yesu alikazia ukweli mmoja unaotia moyo sana: Yehova anampenda sana kila mmoja wa waabudu wake. Yesu alifundisha kwamba Yehova ni kama mchungaji anayemjua na kumpenda kila kondoo katika kundi lake. (Mathayo 18:12-14) Yesu alisema kwamba hata shomoro mmoja hawezi kuanguka chini bila Yehova kujua. Yesu aliongeza hivi: “Nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote.” (Mathayo 10:29-31) Iwapo Yehova ana uwezo wa kujua kama shomoro mmoja ameanguka kutoka katika kiota chake, ni wazi kwamba anamwona na kumjali hata zaidi kila mtu anayemwabudu. Iwapo Yehova anajua na anaweza kuhesabu kila unywele kichwani mwako, basi, je, kuna mambo yoyote kutuhusu, kama vile mahitaji yetu, matatizo yetu, au mahangaiko yetu, ambayo hajui?
Baba wa mbinguni Kama habari zilizotangulia zinavyoonyesha, Yesu ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Si ajabu basi, mara nyingi Mwana huyo mpendwa alimrejelea na kumwita Yehova, “Baba.” Alipokuwa hekaluni akiwa na miaka 12, Yesu alimwita Yehova, “Baba yangu.” Hayo ni kati ya maneno ya kwanza ya Yesu yanayotajwa katika Biblia. (Luka 2:49) Neno “Baba” linatajwa mara 190 hivi katika vitabu vya Injili. Yesu alimwita Yehova “Baba yenu,” “Baba yetu,” na “Baba yangu.” (Mathayo 5:16; 6:9; 7:21) Kwa kumwita Yehova “Baba” mara nyingi hivyo, Yesu alionyesha kwamba wanadamu wenye dhambi na wasio wakamilifu wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova.
Mwenye rehema na tayari kusamehe Yesu alijua kwamba watu wasio wakamilifu wanahitaji sana rehema ya Yehova. Katika mfano wake kumhusu mwana mpotevu, Yesu alimlinganisha Yehova na baba mwenye rehema ambaye yu tayari kumsamehe mwana wake mwenye kutubu. (Luka 15:11-32) Maneno ya Yesu yanatuhakikishia kwamba Yehova anatafuta mabadiliko yoyote katika mioyo ya wanadamu wenye dhambi ili awe na msingi wa kuwaonyesha rehema. Yehova ana hamu sana ya kumsamehe mtenda dhambi anayetubu. Yesu alieleza: “Ninawaambia ninyi kwamba ndivyo kutakavyokuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja anayetubu kuliko juu ya waadilifu 99 ambao hawahitaji kutubu.” (Luka 15:7) Bila shaka, tunataka kumkaribia Mungu huyu mwenye rehema!
Msikiaji wa sala Alipokuwa mbinguni kabla ya kuja duniani, Yesu alijionea mwenyewe kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala” na kuwa anafurahia kusikia sala za watumishi wake waaminifu. (Zaburi 65:2) Kwa hiyo, wakati wa huduma yake, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake jinsi ya kusali na mambo yanayofaa kutajwa katika sala. Alitoa shauri hili: “Msiseme mambo yaleyale tena na tena.” Aliwahimiza wasikilizaji wake waombe mapenzi ya Mungu “yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Tunaweza pia kuomba tupate chakula cha kila siku, msamaha wa dhambi, na nguvu za kusimama imara tunaposhawishiwa. (Mathayo 6:5-13) Yesu alifundisha kwamba Yehova anajibu sala za watumishi Wake wanaosali kwa imani, kama ambavyo baba angemjibu mtoto wake.—Mathayo 7:7-11.
Yesu alijitahidi kuwafundisha watu ukweli kumhusu Yehova na sifa zake. Lakini kulikuwa na jambo lingine ambalo Yesu alitaka kufundisha kumhusu Yehova—jinsi ambavyo Yehova ataleta mabadiliko ulimwenguni pote ili atimize kusudi Lake kuhusu dunia na wanadamu. Hiyo ndiyo habari kuu katika mahubiri ya Yesu.
[Maelezo ya Chini]
a Jina Yehova linapatikana mara 7,000 hivi katika hati za awali za Biblia. Maana ya jina hilo ni, “nitakuwa kile nitakachokuwa.” (Kutoka 3:14) Mungu anaweza kuwa chochote anachotaka ili kutimiza kusudi lake. Jina hilo ni hakikisho kwamba siku zote Mungu atatenda kupatana na kusudi lake na kwamba atatimiza ahadi zake zote.
-
-
Mafundisho ya Yesu Kuhusu Ufalme wa MunguMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Mafundisho ya Yesu Kuhusu Ufalme wa Mungu
‘Alianza kusafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu.’—LUKA 8:1.
SOTE tunapenda kuongea kuhusu mambo tunayoyapenda na yaliyo muhimu kwetu. Yesu mwenyewe alisema, “kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Tukizingatia mambo ambayo Yesu alifundisha wakati wa huduma yake, ni wazi kwamba Ufalme wa Mungu ni muhimu sana kwake.
Ufalme wa Mungu ni nini? Ufalme ni serikali inayoongozwa na mfalme. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ni serikali iliyoanzishwa na Mungu. Yesu aliongea sana kuhusu Ufalme wa Mungu, nao ulikuwa habari kuu katika ujumbe wake. Unatajwa zaidi ya mara 110 katika vitabu vinne vya Injili. Lakini Yesu hakufundisha kwa maneno tu. Matendo yake pia yanaonyesha mengi kuhusu Ufalme wa Mungu na mambo ambayo utafanya.
Mfalme ni nani? Mfalme wa Ufalme wa Mungu hakuchaguliwa na wanadamu kwa kupiga kura. Badala yake, Mtawala huyo alichaguliwa na Mungu mwenyewe. Yesu alifundisha kwamba yeye ndiye Mfalme aliyechaguliwa na Mungu.
Yesu alijua kwamba Biblia ilitabiri kwamba Masihi aliyeahidiwa angetawala Ufalme ambao ungedumu milele. (2 Samweli 7:12-14; Danieli 7:13, 14; Mathayo 26:63, 64) Kumbuka kwamba Yesu alitangaza hadharani kwamba yeye ndiye Masihi aliyetabiriwa. Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba yeye ndiye Mfalme ambaye amewekwa na Mungu. (Yohana 4:25, 26) Hivyo, kwa kufaa Yesu alitumia maneno “ufalme wangu” mara kadhaa.—Yohana 18:36.
Pia, Yesu alifundisha kwamba wengine wangetawala pamoja naye katika Ufalme huo. (Luka 22:28-30) Aliwaita watawala wenzake “kundi dogo,” kwa kuwa idadi yao ingekuwa na mpaka. Alisema hivi kuwahusu: “Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Kitabu cha mwisho cha Biblia kinaonyesha kwamba watu 144,000 watakuwa na pendeleo la kutawala pamoja na Kristo.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1.
Ufalme unatawala kutoka wapi? Yesu alimwambia mtawala Mroma, Pontio Pilato hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Ufalme wa Mungu unaoongozwa na Kristo si serikali ya kibinadamu. Mara nyingi, Yesu aliuita Ufalme wa Mungu “ufalme wa mbinguni.”a (Mathayo 4:17; 5:3, 10, 19, 20) Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni.
Yesu alikuwa na hakika kwamba angerudi mbinguni baada ya maisha yake duniani. Alisema kwamba ‘angetayarisha mahali’ huko mbinguni, ili watawala wenzake waweze kujiunga naye.—Yohana 14:2, 3.
Ufalme unatimiza nini? Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake kusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Mapenzi ya Mungu yanatendeka mbinguni na yatatimizwa hapa duniani kupitia Ufalme huo. Ni lazima Ufalme huo utekeleze mabadiliko makubwa, ili mapenzi ya Mungu yaweze kutendeka duniani.
Ufalme utafanya nini duniani? Yesu alifundisha kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa uovu kwa kuwaangamiza watu wasiotaka kuacha kufanya maovu. (Mathayo 25:31-34, 46) Hivyo, ufisadi na uovu wote utakwisha. Yesu alifundisha kwamba dunia itajaa watu wapole, waadilifu, wenye rehema, “walio safi moyoni,” na wanaofanya amani.—Mathayo 5:5-9.
Je, waaminifu hao watalazimika kuishi kwenye dunia iliyochafuliwa? La hasha! Yesu aliahidi kwamba hali duniani ingebadilika kwa njia ya ajabu chini ya Ufalme wa Mungu. Mtu aliyekuwa ametundikwa kando ya Yesu alisema: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu akasema: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:42, 43) Naam, Ufalme wa Mungu utafanya dunia nzima iwe paradiso inayofanana na paradiso ambayo ilikuwa katika bustani ya Edeni.
Ufalme utawafanyia nini zaidi wanadamu? Yesu hakuahidi tu mambo ambayo Ufalme wa Mungu utafanya. Pia alionyesha kwa matendo mambo ambayo utafanya. Yesu aliwaponya watu wengi kimuujiza, hivyo, alionyesha kwa kadiri ndogo yale ambayo atafanya kwa kadiri kubwa zaidi Ufalme wake utakapotawala dunia. Kitabu cha Injili kinasema hivi kumhusu Yesu: “Akaenda akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya ugonjwa na kila namna ya udhaifu katikati ya watu.”—Mathayo 4:23.
Yesu aliwaponya watu wenye magonjwa mbalimbali. “Alifungua macho ya mtu aliyezaliwa akiwa kipofu.” (Yohana 9:1-7, 32, 33) Kwa kumgusa kwa upendo, alimponya mtu aliyekuwa na ugonjwa wenye kuchukiza wa ukoma. (Marko 1:40-42) Wakati ambapo “mtu aliye kiziwi na mwenye kizuizi cha usemi,” aliletwa kwake, Yesu alionyesha kwamba ana uwezo wa kuwafanya “viziwi wasikie na wasioweza kusema, waseme.”—Marko 7:31-37.
Mfalme huyo aliyewekwa na Mungu hata alikuwa na uwezo wa kuwafufua wafu. Biblia inasema kwamba watu watatu walifufuliwa na Yesu. Alimfufua mwana pekee wa mjane fulani, msichana mwenye miaka 12, na rafiki yake mpendwa Lazaro.—Luka 7:11-15; 8:41-55; Yohana 11:38-44.
Yesu alieleza jinsi maisha yatakavyokuwa kwa raia wa Ufalme wa Mungu kwa kutoa unabii huu kupitia mtume Yohana: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 1:1; 21:3, 4) Ebu wazia—ulimwengu usio na watu wanaolia kwa huzuni, usio na maumivu wala kifo! Kisha, sala ya kwamba mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama yanavyotendeka mbinguni, itatimia kikamili.
Ufalme wa Mungu utakuja lini? Yesu alifundisha kwamba angeanza kutawala katika kipindi hususa cha wakati alichokiita “kuwapo” kwake. Yesu alitoa unabii ulioonyesha kinaganaga wakati ambapo kuwapo kwake akiwa mfalme kungeanza. Katika kipindi hicho kungekuwa na matatizo duniani kote kama vile vita, njaa, matetemeko ya ardhi, magonjwa, na ongezeko la uhalifu. (Mathayo 24:3, 7-12; Luka 21:10, 11) Mambo haya na mambo mengine mengi yameonekana hasa tangu mwaka wa 1914, wakati Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipoanza. Kwa hiyo, Yesu anatawala sasa kama Mfalme. Hivi karibuni Ufalme huo utakuja na mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani.b
Kuja kwa Ufalme wa Mungu kutamaanisha nini kwako binafsi? Hilo linategemea jinsi unavyochagua kutenda unaposikia ujumbe wa Yesu.
[Maelezo ya Chini]
a Usemi “ufalme wa mbinguni” unatumiwa mara 30 hivi katika Injili ya Mathayo.
b Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi tunavyojua kwamba Ufalme wa Mungu utakuja karibuni, ona sura ya 9, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Yesu Kristo—Ujumbe Wake UnavyokuhusuMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Yesu Kristo—Ujumbe Wake Unavyokuhusu
“Nimekuja ili wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.”—YOHANA 10:10.
YESU KRISTO alikuja duniani ili kutoa wala si kupokea. Katika huduma yake, aliwapa wanadamu zawadi yenye thamani kubwa, yaani, ujumbe unaofunua ukweli kumhusu Mungu na mapenzi Yake. Kama maisha ya mamilioni ya Wakristo wa kweli yanavyoonyesha, watu wanaokubali ujumbe huu wanaweza kuwa na maisha bora leo.a Hata hivyo, ujumbe wa Yesu unategemea dhabihu ya uhai mkamilifu ambayo ni zawadi yenye thamani sana kutoka kwake. Wakati wetu ujao unategemea jinsi tunavyochagua kutenda kuhusiana na sehemu hii muhimu ya ujumbe wake.
Mungu na Kristo walitoa nini? Yesu alijua kwamba adui zake wangemtesa sana na kumuua. (Mathayo 20:17-19) Hata hivyo, katika Yohana 3:16, alisema maneno haya maarufu: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Pia, Yesu alisema kwamba alikuja “kutoa nafsi yake [au, uhai wake] kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Kwa nini alisema kwamba angetoa uhai wake badala ya kusema kwamba angeuawa?
Kwa upendo usio na kifani, Mungu alifanya mpango ili kuwaweka wanadamu huru kutokana na dhambi waliyorithi, na matokeo yake ya kutokamilika na kifo. Mungu alifanya hivyo kwa kumtuma duniani Mwana wake mzaliwa-pekee ili atoe uhai wake kama dhabihu. Yesu alikubali kwa hiari kutoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu. Huo ndio mpango wa fidia au dhabihu ya ukombozi, nayo ndiyo zawadi kubwa zaidi kutoka kwa Mungu.b Zawadi hiyo inawawezesha wanadamu kupata uzima wa milele.
Unahitaji kufanya nini? Je, fidia ni zawadi kwako binafsi? Hilo linategemea wewe. Wazia kwamba mtu anataka kukupa zawadi iliyofungwa vizuri kwa karatasi maridadi. Zawadi hiyo haitakuwa yako usipoichukua na kuikubali. Vivyo hivyo, Yehova anataka kukupa wewe zawadi ya fidia, lakini usipoichukua na kuikubali haiwezi kuwa yako. Unaweza kuichukua na kuikubali zawadi hiyo jinsi gani?
Yesu alisema kwamba ni wale tu “wanaomwamini” ambao watapata uzima wa milele. Imani inahusisha matendo yako maishani. (Yakobo 2:26) Kumwamini Yesu kunamaanisha kuishi kupatana na mambo aliyofundisha na kufanya. Ili kufanya hivyo ni lazima umjue Yesu na Baba yake vizuri. Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.
Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu Kristo alihubiri ujumbe ambao umebadili maisha ya mamilioni ya watu duniani kote. Je, ungependa kujua ujumbe huo vizuri zaidi na jinsi wewe na wapendwa wako mnavyoweza kunufaika kutokana nao, leo na hata milele? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.
Makala zinazofuata zinazungumzia mambo mengine mengi kumhusu Yesu Kristo, mtu ambaye alihubiri ujumbe unaoweza kubadili maisha yako kabisa.
[Maelezo ya Chini]
a Si kila mtu anayejidai kuwa Mkristo, ambaye ni mfuasi wa kweli wa Kristo. Wafuasi wa kweli wa Yesu wanaishi kupatana na kweli ambazo alifundisha kumhusu Mungu na mapenzi Yake.—Mathayo 7:21-23.
b Ili kupata habari zaidi kuhusu fundisho la Biblia juu ya fidia, ona sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Je, Ni Mafundisho ya Uwongo Au ya Kweli?—Ukweli Kumhusu YesuMnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Je, Ni Mafundisho ya Uwongo Au ya Kweli?—Ukweli Kumhusu Yesu
MAONI YAKO NI NINI? HABARI ZIFUATAZO NI ZA KWELI AU NI ZA UWONGO?
Yesu alizaliwa Desemba 25.
Mamajusi watatu walimtembelea Yesu baada tu ya kuzaliwa kwake.
Yesu hakuwa na ndugu wala dada.
Yesu alikuwa Mungu katika mwili wa binadamu.
Yesu hakuwa mtu mwema tu.
WATU wengi wangesema kwamba habari hizi zote ni za kweli. Huenda wengine wangesema kwamba ni vigumu na hata haiwezekani kujua ukweli wa mambo. Labda wanafikiri kwamba mradi tu mtu anamwamini Yesu, si lazima ajue majibu ya maswali hayo.
Hata hivyo, Biblia inatutia moyo tuwe “na ujuzi sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:8) Tunaweza kupata ujuzi huo kwa kuchunguza vitabu vya Injili. Vinafunua ukweli kumhusu Yesu, na hivyo kutusaidia kutofautisha ukweli na uwongo. Kwa hiyo, acheni tuone yale ambayo vitabu vya Injili vinaonyesha kuhusu mafundisho yaliyo juu.
FUNDISHO: Yesu alizaliwa Desemba 25.
NI UWONGO.
Biblia haitaji mwezi wala siku ambayo Yesu alizaliwa. Hivyo basi, tarehe ya Desemba 25 ilitoka wapi? Kitabu kimoja cha marejeo (The Encyclopædia Britannica) kinasema kwamba watu fulani waliojiita Wakristo “walitaka tarehe hiyo ilingane na sherehe ya kipagani ya Waroma ya kuadhimisha . . . siku ambapo mchana unaanza kuwa mrefu na jua linaanza kupaa juu zaidi angani.” Kitabu hicho kinasema pia kwamba desturi nyingi za Krismasi zilitokana na “sherehe za kipagani zilizohusu ukulima na ibada ya jua katikati ya majira ya baridi kali.”
Je, Yesu angekubali watu washerehekee kuzaliwa kwake siku ya Desemba 25? Fikiria hili: Siku ambayo Yesu alizaliwa haijulikani. Biblia haitoi maagizo yoyote kwamba tunapaswa kusherehekea kuzaliwa kwa Yesu, wala hakuna uthibitisho wowote kwamba Wakristo wa mapema walifanya hivyo. Kinyume cha hilo, Biblia inataja siku hususa ambayo Yesu alikufa, naye aliwaamuru wafuasi wake waikumbuke siku hiyo.a (Luka 22:19) Basi ni wazi kwamba Yesu alitaka watu wazingatie zaidi umuhimu wa kifo chake cha kidhabihu wala si kuzaliwa kwake.—Mathayo 20:28.
FUNDISHO: Mamajusi watatu (au wafalme watatu kulingana na mafundisho fulani) walimtembelea Yesu baada tu ya kuzaliwa kwake.
NI UWONGO.
Labda umeona michoro au mandhari inayoonyesha kitoto Yesu kikiwa kimelazwa kwenye hori huku kimezungukwa na mamajusi watatu walioleta zawadi. Hata hivyo, hiyo ni mandhari ya kubuniwa tu, si ya kweli.
Ni kweli kwamba watu fulani kutoka Mashariki walimtembelea mtoto Yesu. Hata hivyo, watu hao waliomtembelea walikuwa wanajimu, au wataalamu wa nyota. (Mathayo 2:1, Biblia Habari Njema) Je, walimpata Yesu akiwa amelazwa horini? Hapana; walimtembelea ndani ya nyumba. Yaelekea walifika miezi kadhaa baada ya Yesu kuzaliwa.—Mathayo 2:9-11.
Yesu alitembelewa na watu wangapi? Je, walikuwa 2, 3, au 30? Biblia haisemi. Huenda wengi wanaamini kwamba ni watatu kwa sababu Biblia inataja aina tatu za zawadi.b (Mathayo 2:11) Hata watu fulani wamedokeza kwamba kila moja ya zawadi hizo inawakilisha jamii tofauti ya wanadamu. Lakini wazo hilo halipatikani katika Biblia. Badala yake, kitabu kimoja kinachofafanua vitabu vya Injili kinasema kwamba wazo hilo lilibuniwa na “mwanahistoria mbunifu sana wa karne ya nane.”
FUNDISHO: Yesu hakuwa na ndugu wala dada.
NI UWONGO.
Vitabu vya Injili vinaonyesha wazi kwamba Yesu alikuwa na ndugu na dada. Injili ya Luka inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza” wa Maria, kuonyesha kwamba alizaa watoto wengine baadaye.c (Luka 2:7) Injili ya Marko inataja kwamba watu fulani katika jiji la Nazareti walimwona Yesu kuwa mtu wa kawaida tu, aliyekuwa sawa na ndugu na dada zake. Waliuliza hivi: “Je, Yakobo, Yosefu, Yuda na Simoni si ndugu zake? Je, si dada zake wanaishi hapa katika mji wetu?”—Marko 6:3, Contemporary English Version; Mathayo 12:46; Yohana 7:5.
Tofauti na yale ambayo vitabu vya Injili vinasema, wanatheolojia wengi wanadai kwamba Yesu alikuwa mzaliwa wa pekee wa Maria. Baadhi yao wanasema kwamba ndugu na dada za Yesu wanaotajwa katika Biblia ni binamu zake.d Wengine hufikiri kwamba ndugu na dada hao wa Yesu ni watoto wa kambo wa Maria. Lakini fikiri hili: Ikiwa Yesu hakuwa na ndugu au dada, je, watu hao wa Nazareti wangesema maneno waliyosema? Kinyume chake, yaelekea baadhi yao walimwona Maria alipokuwa na mimba za watoto wale wengine. Walijionea kwa macho yao kwamba Yesu alikuwa mmoja kati ya watoto wengi ambao Maria alizaa.
FUNDISHO: Yesu alikuwa Mungu katika mwili wa binadamu.
NI UWONGO.
Wazo kwamba Mungu alikuja duniani na kuishi kama mwanadamu Yesu, limekuwako kwa muda mrefu, na ndilo msingi wa fundisho la Utatu. Hata hivyo, fundisho hilo halikuwapo wakati wa Yesu, kama vile tu kitabu kimoja cha marejeo (The Encyclopædia Britannica) kinavyosema: “Neno Utatu, wala fundisho la wazi kama hilo, halionekani katika Agano Jipya . . . Fundisho hilo lilisitawishwa hatua kwa hatua kwa muda wa karne kadhaa na kwa mabishano mengi.”
Kwa kweli, dini zinamshushia Yesu heshima kwa kufundisha kwamba yeye ni Mungu katika mwili wa binadamu.e Kwa njia gani? Fikiria mfano huu. Wafanyakazi fulani wanamwomba msimamizi wao awafanyie jambo fulani, lakini msimamizi huyo anasema hana mamlaka ya kufanya hivyo. Ikiwa msimamizi huyo anasema kweli, anaonyesha kwa hekima kwamba anatambua mipaka yake. Lakini kama ana uwezo na anakataa kuwasaidia wafanyakazi hao, yeye ni mdanganyifu.
Yesu alifanya nini wakati wawili kati ya mitume wake walipojitakia vyeo vya umashuhuri? Aliwaambia: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mathayo 20:23) Ikiwa kwa kweli Yesu alikuwa Mungu, je, si angekuwa amesema uwongo? Badala ya hivyo, kwa kumrejelea Yule aliye na mamlaka zaidi, Yesu alituwekea mfano bora wa kuwa wenye kiasi na akaonyesha kwamba yeye si sawa na Mungu.
FUNDISHO: Yesu hakuwa mtu mwema tu.
NI KWELI.
Yesu alisema waziwazi kwamba hakuwa mtu mwema tu. Alisema: “Mimi ni Mwana wa Mungu.” (Yohana 10:36) Bila shaka, mtu yeyote anaweza kudai kuwa Mwana wa Mungu. Lakini kama madai hayo ya Yesu si ya kweli, basi yeye si mtu mwema bali mdanganyifu mkubwa!
Ushuhuda wenye kutegemeka zaidi kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu ulitoka kwa Mungu mwenyewe. Yehova alisema hivi mara mbili kumhusu Yesu: “Huyu ni Mwanangu.” (Mathayo 3:17; 17:5) Ebu fikiria hili: Kuna visa vichache tu katika Biblia ambapo sauti ya Mungu ilisikika duniani—na viwili kati ya hivyo ni wakati Yehova alipothibitisha kwamba Yesu ni Mwana wake! Huo ndio uthibitisho bora kabisa kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu kama alivyosema.
Je, umejifunza mambo yoyote kumhusu Yesu ambayo hukujua hapo awali? Ikiwa ndivyo, unaweza kuchunguza zaidi vitabu vya Injili vilivyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Uchunguzi huo unaweza kuwa wenye kufurahisha na kunufaisha. Hata Yesu mwenyewe alisema kwamba kujifunza kweli kumhusu yeye na Baba yake kunamaanisha “uzima wa milele.”—Yohana 17:3.
[Maelezo ya Chini]
a Yesu alikufa Siku ya Pasaka, au Nisani 14, kulingana na kalenda ya Wayahudi.—Mathayo 26:2.
b Mathayo anasema kwamba wageni hao “wakafungua hazina zao” na kumtolea dhahabu, ubani, na manemane. Hata hivyo, huenda familia ya Yesu—ambayo haikuwa tajiri—ilipata zawadi hizo zenye thamani kubwa wakati unaofaa kwa sababu ililazimika kukimbia nchi yao muda mfupi baadaye.—Mathayo 2:11-15.
c Ingawa Maria alichukua mimba ya Yesu kimuujiza, alichukua mimba za watoto wale wengine kwa njia ya kawaida kupitia mume wake Yosefu.—Mathayo 1:25.
d Wazo hili lililoungwa mkono na Jerome yapata mwaka wa 383 W.K. linapendwa na watu wengi wanaoamini kwamba Maria alibaki bikira maisha yake yote. Ingawa baadaye Jerome alitilia shaka wazo hili, watu wengi bado wanaliamini. Huo pia ndio msimamo wa Kanisa Katoliki.
e Kwa habari zaidi kuhusu fundisho la Utatu, ona broshua Je! Uamini Utatu? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]
Mambo Mengine Yanayoweza Kukushangaza Kumhusu Yesu
Yesu alikuwa mtu wa aina gani? Je, alikuwa mtu mwenye kujinyima raha, mgumu na mwenye kujitenga na watu hivi kwamba hangeweza kuwa na urafiki na watu wa kawaida? Huenda wengine wakafikiri hivyo. Labda hiyo ndiyo sababu inayofanya washangae kujua kwamba Yesu . . .
• alijiunga na wengine wakati wa matukio yenye shangwe.—Yohana 2:1-11.
• aliwapongeza wengine.—Marko 14:6-9.
• alifurahia kuwa pamoja na watoto.—Marko 10:13, 14.
• alilia hadharani.—Yohana 11:35.
• aliwahurumia watu.—Marko 1:40, 41.
-
-
Je, Wajua?Mnara wa Mlinzi—2010 | Aprili 1
-
-
Je, Wajua?
Kuna uthibitisho gani nje ya Biblia kwamba Yesu alikuwa mtu halisi?
▪ Waandikaji kadhaa wa mambo yasiyo ya dini ambao waliishi karibu na wakati wa Yesu, walimtaja katika maandishi yao. Mmoja kati ya waandikaji waliomtaja Yesu ni Kornelio Tasito, ambaye aliandika historia ya Roma chini ya utawala wa maliki mbalimbali. Kuhusu moto ulioharibu Roma mwaka wa 64 W.K., Tasito anasema kulikuwa na uvumi kwamba Maliki Nero ndiye aliyesababisha msiba huo. Tasito anasema, Nero alijaribu kukilaumu kikundi cha watu ambao waliitwa Wakristo. Tasito anaandika: “Kristo, ambaye jina Wakristo lilitokana na jina lake, aliuawa mikononi mwa gavana Pontio Pilato wakati wa utawala wa Tiberio.”—Annals, XV, 44.
Mwanahistoria Myahudi Flavio Yosefo pia anamtaja Yesu. Anaposimulia mambo yaliyotukia baada ya kifo cha Festo, ambaye alikuwa gavana Mroma wa Yudea yapata mwaka wa 62 W.K., na kabla ya Albino kuwa gavana, Yosefo anasema kwamba Kuhani Mkuu Ananu (Anania) “aliitisha kikao cha Sanhedrini na kumleta mbele yao Yakobo, ndugu ya Yesu aliyekuwa akiitwa Kristo, pamoja na wengine.”—Jewish Antiquities, XX, 200 (ix, 1).
Kwa nini Yesu aliitwa Kristo?
▪ Vitabu vya Injili vinasimulia kwamba malaika Gabrieli alipomtokea Maria na kutangaza kwamba angepata mimba, alimwambia kuwa alipaswa kumwita mtoto wake Yesu. (Luka 1:31) Hilo lilikuwa jina la kawaida miongoni mwa Wayahudi wa nyakati za Biblia. Mwanahistoria Myahudi Yosefo aliandika kuhusu watu 12 walioitwa Yesu, kando na wale wanaotajwa katika Biblia. Mwana wa Maria aliitwa “Mnazareti,” jina lililoonyesha kuwa Yesu alitoka Nazareti. (Marko 10:47) Pia aliitwa “Kristo,” au Yesu Kristo. (Mathayo 16:16) Jina Kristo linamaanisha nini?
Neno la Kiswahili “Kristo” linatokana na neno la Kigiriki Khri·stosʹ, ambalo lina maana sawa na neno la Kiebrania Ma·shiʹach (Masihi). Maneno hayo mawili yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta.” Kabla ya Yesu, kulikuwa na watu wengine walioitwa Masihi. Kwa mfano, Musa, Haruni, na Mfalme Daudi walitajwa kuwa watiwa mafuta, ikimaanisha kwamba Mungu alikuwa amewachagua na kuwapa mamlaka na majukumu mbalimbali. (Mambo ya Walawi 4:3; 8:12; 2 Samweli 22:51; Waebrania 11:24-26) Yesu, Masihi aliyeahidiwa, ndiye mwakilishi mkuu zaidi wa Yehova. Kwa hiyo, Yesu aliitwa “Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—Mathayo 16:16; Danieli 9:25.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Picha ya Flavio Yosefo iliyochorwa
-