-
Wafalme Wawili WapambanaSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Sura ya Kumi na Tatu
Wafalme Wawili Wapambana
1, 2. Kwa nini tupendezwe na unabii uliorekodiwa katika Danieli sura ya 11?
WAFALME wawili wapambana kufa na kupona ili kupata mamlaka kuu kupita zote. Miaka ipitapo, wapokezana mamlaka. Nyakati nyingine, mfalme mmoja atawala kwa ukuu ilhali yule mwingine awa asiyetenda, na kuna vipindi vya kutopambana. Lakini pigano jingine lazuka ghafula, na pambano laendelea. Baadhi ya wapambanaji hao ni Mfalme Niketa Seleuko wa Kwanza wa Siria, Mfalme Ptolemy Lagus wa Misri, Binti ya Mfalme wa Siria aliyekuwa pia Malkia wa Misri Kleopatra wa Kwanza, Wamaliki wa Roma Augusto na Tiberio, na Malkia Zenobia wa Palmyra. Pambano lielekeapo kwisha, Ujerumani ya Nazi, mataifa ya Kikomunisti, Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, Ushirika wa Mataifa, na Umoja wa Mataifa pia zimehusika. Tamati ni kisa kisichotazamiwa na mashirika hayo yote ya kisiasa. Malaika wa Yehova alimjulisha Danieli unabii huo wenye kusisimua miaka 2,500 hivi iliyopita.—Danieli, sura ya 11.
2 Lazima Danieli awe alisisimuka kama nini alipomsikia malaika akimfunulia kinaganaga ushindani kati ya wafalme wawili wajao! Ushindani huo watupendeza sisi pia, kwa kuwa kushindania mamlaka kati ya wafalme hao wawili kwaendelea hata leo. Imani yetu na uhakika wetu kwamba sehemu ya mwisho ya unabii huo bila shaka itatimizwa zitatiwa nguvu tuonapo jinsi ambavyo historia imeonyesha vile sehemu ya kwanza ya unabii huo ilivyotimizwa. Kusikiliza unabii huu kutatusaidia kuona waziwazi mahali tulipo katika mkondo wa wakati. Pia kutatia nguvu azimio letu la kutokuwamo katika mapambano hayo tungojeapo kwa subira Mungu achukue hatua kwa niaba yetu. (Zaburi 146:3, 5) Basi, na tumsikilize kwa makini malaika wa Yehova akiongea na Danieli.
DHIDI YA UFALME WA UGIRIKI
3. Malaika alimwunga mkono nani “katika mwaka wa kwanza wa Dario, Mmedi”?
3 “Tena mimi,” akasema malaika, “katika mwaka wa kwanza wa Dario, Mmedi [539/538 K.W.K.], mimi nalisimama nimthibitishe na kumtia nguvu.” (Danieli 11:1) Dario hakuwa hai, lakini malaika alirejezea utawala wake kuwa mwanzo wa ujumbe wa kiunabii. Mfalme huyo ndiye aliyeamuru Danieli atolewe kutoka kwenye tundu la simba. Dario alikuwa ameagiza pia kwamba raia zake wamche Mungu wa Danieli. (Danieli 6:21-27) Hata hivyo, malaika huyo hakusimama ili kumwunga mkono Dario Mmedi, bali alimwunga mkono Mikaeli, mshirika wa malaika huyo—yule mkuu wa watu wa Danieli. (Linganisha Danieli 10:12-14.) Malaika wa Mungu alimwunga mkono Mikaeli alipokuwa akishindana na roho waovu wa Umedi na Uajemi.
4, 5. Wafalme wanne wa Uajemi waliotabiriwa walikuwa nani?
4 Malaika wa Mungu aliendelea kusema hivi: “Tazama, watasimama wafalme watatu katika Uajemi; naye mfalme wa nne atakuwa tajiri kuliko hao wote; naye atakapopata nguvu kwa utajiri wake, atawachochea wote juu ya ufalme wa Uyunani [“Ugiriki,” NW].” (Danieli 11:2) Watawala hao wa Uajemi walikuwa kina nani?
5 Wafalme watatu wa kwanza walikuwa Koreshi Mkuu, Cambyses wa Pili, na Dario wa Kwanza. Kwa kuwa Bardiya (au pengine Gaumata, aliyejisingizia kuwa mfalme) alitawala kwa muda wa miezi saba peke yake, unabii huo haukutilia maanani utawala wake mfupi. Mwaka wa 490 K.W.K., mfalme wa tatu, Dario wa Kwanza, alijaribu kuvamia Ugiriki kwa mara ya pili. Hata hivyo, Waajemi walishindwa vibaya huko Marathon nao wakakimbilia Asia Ndogo. Ingawa Dario alipanga kwa uangalifu vita zaidi dhidi ya Ugiriki, hakuweza kupigana kabla ya kufa kwake miaka minne baadaye. Alimwachia mwana wake Shasta wa Kwanza, ambaye alitawala pia baada yake akiwa mfalme “wa nne.” Ndiye Mfalme Ahasuero aliyemwoa Esta.—Esta 1:1; 2:15-17.
6, 7. (a) Mfalme wa nne ‘aliwachocheaje wote juu ya ufalme wa Ugiriki’? (b) Vita ya Shasta dhidi ya Ugiriki ilikuwa na matokeo gani?
6 Shasta wa Kwanza kwa kweli ‘aliwachochea wote juu ya ufalme wa Ugiriki,’ yaani, yale majimbo huru ya Ugiriki yote pamoja. “Akihimizwa na maofisa wa serikali yake wenye kutaka makuu,” chasema kitabu The Medes and Persians—Conquerors and Diplomats, “Shasta alishambulia toka nchi kavu na baharini.” Mwanahistoria Mgiriki Herodotus, wa karne ya tano K.W.K., aandika kwamba “hakuna mashambulizi mengine yaliyolingana na hili.” Rekodi yake yataarifu kwamba jeshi la majini “lilijumlika kuwa watu 517,610. Askari-jeshi walikuwa 1,700,000; wapanda-farasi walikuwa 80,000; na kuongezea Waarabu waliopanda ngamia, na Walibya waliopigana wakiwa kwenye magari ya vita, ninaokadiria walikuwa 20,000. Kwa hiyo, wanajeshi wote wa nchi kavu na wa majini walijumlika kuwa watu 2,317,610.”
7 Akipanga kupata ushindi kamili, Shasta wa Kwanza aliliongoza jeshi lake kubwa likapigane na Ugiriki mwaka wa 480 K.W.K. Waajemi waliharibu kabisa Athene waliposhinda mbinu ya Ugiriki ya kukawia huko Thermopylae. Hata hivyo, walipofika Salamis walishindwa vibaya. Ugiriki ilishinda tena huko Plataea, mwaka wa 479 K.W.K. Hakuna yeyote kati ya wale wafalme saba waliotawala Milki ya Uajemi baada ya Shasta katika miaka 143 iliyofuata aliyeshambulia Ugiriki. Lakini kukazuka mfalme mwenye nguvu huko Ugiriki.
UFALME MKUBWA WAGAWANYIKA NA KUWA FALME NNE
8. Ni ‘mfalme yupi hodari’ aliyesimama, naye alipataje ‘kutawala kwa mamlaka kubwa na kutenda apendavyo’?
8 “Mfalme hodari atasimama, atakayetawala kwa mamlaka kubwa, na kutenda apendavyo,” akasema malaika. (Danieli 11:3) Aleksanda mwenye umri wa miaka 20 ‘alisimama’ akiwa mfalme wa Makedonia mwaka wa 336 K.W.K. Akawa “mfalme hodari”—Aleksanda Mkuu. Akifuata mipango ya baba yake, Philip wa Pili, aliteka mikoa ya Uajemi huko Mashariki ya Kati. Walipovuka Mto Eufrati na Mto Tigris, watu wake 47,000 walivitawanya vikosi vya Dario wa Tatu vyenye watu 250,000 huko Gaugamela. Hatimaye, Dario akakimbia, akauawa, na hivyo utawala wa Uajemi ukakoma. Ugiriki ikawa serikali ya ulimwengu, na Aleksanda ‘akatawala kwa mamlaka kubwa na kutenda apendavyo.’
9, 10. Unabii wa kwamba ufalme wa Aleksanda hautakuwa wa uzao wake ulithibitikaje kuwa kweli?
9 Aleksanda angeutawala ulimwengu kwa kipindi kifupi tu, kwa kuwa malaika wa Mungu aliongezea kusema hivi: “Naye atakaposimama, ufalme wake utavunjika, na kugawanyika katika pepo nne za mbinguni; lakini hautakuwa wa uzao wake, wala hautakuwa kama mamlaka yake ambayo alitawala kwayo; kwa maana ufalme wake utang’olewa, hata kwa ajili ya wengine zaidi ya hao.” (Danieli 11:4) Umri wa Aleksanda haukuwa umetimia miaka 33 alipougua ghafula na kufa huko Babiloni mwaka wa 323 K.W.K.
10 Milki kubwa ya Aleksanda haikuendelea kutawalwa na “uzao wake.” Ndugu yake Arrhidaeus Philip wa Tatu alitawala kwa muda unaopungua miaka saba naye akauawa mwaka wa 317 K.W.K. kwa kuwa Olympias, mama ya Aleksanda, aliomba auawe. Mwana wa Aleksanda, Aleksanda wa Nne, alitawala hadi mwaka wa 311 K.W.K. wakati Kasanda, mmojawapo wa majenerali wa baba yake, alipomwua. Heracles, mwana haramu wa Aleksanda alijitahidi kutawala kwa kutumia jina la baba yake lakini akauawa mwaka wa 309 K.W.K. Ndivyo nasaba ya Aleksanda ilivyokoma, “mamlaka yake” ikaondoka katika familia yake.
11. Ufalme wa Aleksanda ‘uligawanyikaje katika pepo nne za mbinguni’?
11 Baada ya Aleksanda kufa, ufalme wake ‘uligawanyika katika pepo nne.’ Majenerali wake wengi walizozana walipokuwa wakinyakua maeneo. Jenerali Antigonus wa Kwanza aliyekuwa chongo alijaribu kutawala milki yote ya Aleksanda. Lakini akauawa katika pigano huko Ipsus, Frigia. Kufikia mwaka wa 301 K.W.K., wanne kati ya majenerali wa Aleksanda walikuwa mamlakani wakitawala eneo kubwa ambalo kamanda wao alikuwa ameshinda. Kasanda alitawala Makedonia na Ugiriki. Lisimako akatawala Asia Ndogo na Thrasi. Niketa Seleuko wa Kwanza akatawala Mesopotamia na Siria. Na Ptolemy Lagus akatawala Misri na Palestina. Kama vile neno la kiunabii lilivyokuwa limetabiri, milki kubwa ya Aleksanda iligawanyika na kuwa falme nne za Kigiriki.
WAFALME WAWILI WENYE KUSHINDANA WATOKEA
12, 13. (a) Serikali nne za Kigiriki zilipataje kuwa serikali mbili? (b) Seleuko alianzisha nasaba gani ya watawala huko Siria?
12 Miaka michache baada ya kupata mamlaka, Kasanda akafa, na mwaka wa 285 K.W.K., Lisimako akamiliki sehemu ya Milki ya Ugiriki iliyokuwa Ulaya. Mwaka wa 281 K.W.K., Niketa Seleuko wa Kwanza alimshinda Lisimako vitani na kumiliki sehemu kubwa ya maeneo ya Asia. Gonatas Antigonus wa Pili, mjukuu wa mmoja wa majenerali wa Aleksanda, akaanza kutawala Makedonia mwaka wa 276 K.W.K. Hatimaye, Makedonia ikaanza kutegemea Roma na kisha kuwa mkoa wa Roma mwaka wa 146 K.W.K.
13 Falme mbili kati ya zile falme nne za Kigiriki ndizo zilizokuwa zimesalia zikiwa mashuhuri—ufalme mmoja ukitawalwa na Niketa Seleuko wa Kwanza na ufalme mwingine ukitawalwa na Ptolemy Lagus. Seleuko alianzisha nasaba ya watawala wa Seleuko huko Siria. Miongoni mwa majiji aliyoanzisha mlikuwemo Antiokia—jiji kuu jipya la Siria—na bandari ya Seleucia. Baadaye mtume Paulo alifundisha huko Antiokia, ambapo wafuasi wa Yesu waliitwa Wakristo kwa mara ya kwanza. (Matendo 11:25, 26; 13:1-4) Seleuko aliuawa mwaka wa 281 K.W.K., lakini watawala wa nasaba yake waliendelea kutawala hadi mwaka wa 64 K.W.K. wakati ambapo Jenerali Mroma Gnaeus Pompey aliifanya Siria kuwa mkoa wa Roma.
14. Wafalme wa nasaba ya Ptolemy walianza kutawala Misri lini?
14 Utawala wa Kigiriki uliodumu muda mrefu zaidi kati ya falme hizo nne ni ule wa Ptolemy Lagus, au Ptolemy wa Kwanza, aliyeanza kutawala mwaka wa 305 K.W.K. Nasaba ya wafalme ya Ptolemy aliyoanzisha iliendelea kutawala Misri hadi iliposhindwa na Roma mwaka wa 30 K.W.K.
15. Ni wafalme gani wawili wenye nguvu waliotokana na falme nne za Kigiriki, nao walianzisha ushindani gani?
15 Kwa hiyo, wafalme wawili wenye nguvu—Niketa Seleuko wa Kwanza aliyetawala Siria na Ptolemy wa Kwanza aliyetawala Misri—waliibuka wakiwa wafalme wawili wenye nguvu kutokana na zile falme nne za Kigiriki. Ushindani wa muda mrefu unaofafanuliwa katika Danieli sura ya 11 kati ya “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini,” ulianzishwa na wafalme hao wawili. Malaika wa Yehova hakutaja majina ya wafalme hao, kwa sababu wafalme hao na mataifa yao wangebadilika-badilika katika karne zilizofuata. Bila kutaja mambo yasiyo ya lazima, malaika huyo anataja tu watawala na matukio yanayohusiana na pambano hilo.
PAMBANO LAANZA
16. (a) Wale wafalme wawili walikuwa kaskazini na kusini mwa nani? (b) Ni wafalme gani waliokuwa “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini”?
16 Sikiliza! Akifafanua mwanzo wenye kutokeza wa pambano hilo, malaika wa Yehova asema hivi: “Mfalme wa kusini atakuwa hodari, na mmoja wa wakuu wake [wa Aleksanda]; naye [mfalme wa kaskazini] atakuwa hodari kuliko yeye, naye atakuwa na mamlaka; mamlaka yake itakuwa mamlaka kubwa.” (Danieli 11:5) Majina “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” yarejezea wafalme walio kaskazini na kusini mwa watu wa Danieli, ambao wakati huo walikuwa wamewekwa huru kutokana na utekwa wa Babiloni na walikuwa wamerudi Yuda. “Mfalme wa kusini” wa kwanza alikuwa Ptolemy wa Kwanza wa Misri. Mmojawapo wa majenerali wa Aleksanda aliyemshinda Ptolemy wa Kwanza na kutawala akiwa na “mamlaka kubwa” alikuwa Mfalme wa Siria, Niketa Seleuko wa Kwanza. Akawa “mfalme wa kaskazini.”
17. Mwanzoni mwa pambano kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini, Yuda ilitawalwa na nani?
17 Mwanzoni mwa pambano, Yuda ilikuwa ikitawalwa na mfalme wa kusini. Kuanzia mwaka wa 320 K.W.K. hivi, Ptolemy wa Kwanza aliwachochea Wayahudi waende wakae Misri. Jumuiya ya Kiyahudi ikasitawi Aleksandria, ambapo Ptolemy wa Kwanza alianzisha maktaba maarufu. Mfalme wa kusini, Misri iliyokuwa ikitawalwa na nasaba ya Ptolemy, aliendelea kutawala Wayahudi huko Yuda hadi mwaka wa 198 K.W.K.
18, 19. Kadiri wakati ulivyopita, wafalme hao wawili wenye kushindana ‘walifanyaje mapatano’?
18 Kuhusu wafalme hao wawili, malaika alitabiri hivi: “Baada ya miaka kadha wa kadha watashirikiana; kwa kuwa binti wa mfalme wa kusini atakuja kwa mfalme wa kaskazini, ili kufanya mapatano naye; lakini hatakuwa na nguvu za mkono wake sikuzote; wala mfalme yule hatasimama, wala mkono wake; lakini yule binti atatolewa, na hao waliomleta, na yeye aliyemzaa, na yeye aliyemtia nguvu, zamani zile.” (Danieli 11:6) Hilo lilitimizwaje?
19 Unabii haukumtaja mwana wa Niketa Seleuko wa Kwanza, Antiochus wa Kwanza, ambaye pia alitawala baada yake, kwa sababu hakupigana vita vya kukata maneno dhidi ya mfalme wa kusini. Lakini Antiochus wa Pili, aliyetawala baada yake, alipigana kwa muda mrefu dhidi ya Ptolemy wa Pili, mwana wa Ptolemy wa Kwanza. Antiochus wa Pili na Ptolemy wa Pili walikuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Antiochus wa Pili alimwoa Laodice, wakapata mwana aitwaye Seleuko wa Pili, ilhali Ptolemy wa Pili alikuwa na binti aitwaye Berenice. Mwaka wa 250 K.W.K., wafalme hao wawili ‘walifanya mapatano.’ Ili kulipa gharama ya mapatano hayo, Antiochus wa Pili alimtaliki mke wake Laodice na kumwoa Berenice, “binti ya mfalme wa kusini.” Berenice alimzalia mwana aliyekuwa mrithi wa kiti cha ufalme cha Siria badala ya wana wa Laodice.
20. (a) “Mkono” wa Berenice ulishindwaje kusimama? (b) Berenice, “hao waliomleta,” na “yeye aliyemtia nguvu” walishindwaje? (c) Ni nani aliyetawala Siria baada ya Antiochus wa Pili kupoteza “mkono wake,” au mamlaka yake?
20 “Mkono” wa Berenice, au nguvu zilizomtegemeza zilitokana na baba yake, Ptolemy wa Pili. Ptolemy wa Pili alipokufa mwaka wa 246 K.W.K., Berenice ‘hakuwa na nguvu za mkono wake’ kwa mume wake. Antiochus wa Pili alimkataa, akamwoa tena Laodice, na kumteua mwana wao kuwa mtawala atakayemfuata. Kama vile Laodice alivyopanga, Berenice na mwana wake wakauawa. Yaonekana kwamba wahudumu waliomleta Berenice toka Misri hadi Siria—“hao waliomleta”—waliuawa pia. Laodice hata alimtilia sumu Antiochus wa Pili, na kwa sababu hiyo “mkono wake,” au mamlaka yake, pia ‘haikusimama.’ Kwa hiyo, baba ya Berenice—“yeye aliyemzaa”—na mume wake wa Siria—ambaye alikuwa amemfanya kuwa mwenye “nguvu” kwa muda—wakafa. Basi Seleuko wa Pili, mwana wa Laodice, akawa mfalme wa Siria. Mambo yote hayo yangemfanya mfalme wa nasaba ya Ptolemy aliyefuata atendeje?
MFALME ALIPIZA KISASI KUUAWA KWA DADA YAKE
21. (a) Ni nani aliyekuwa “chipukizi la mizizi” ya Berenice, naye ‘alisimamaje’? (b) Ptolemy wa Tatu ‘aliingiaje katika ngome ya mfalme wa kaskazini’ na kumshinda?
21 “Katika chipukizi la mizizi yake atasimama mmoja mahali pake atakayeliendesha jeshi la askari, naye ataingia katika ngome ya mfalme wa kaskazini, na kuwatenda mambo, na kuwashinda,” akasema malaika. (Danieli 11:7) Ndugu ya Berenice ndiye aliyekuwa “chipukizi” la wazazi au “mizizi” ya Berenice. Baba yake alipokufa, ndugu ya Berenice ‘alisimama’ akiwa mfalme wa kusini, Farao wa Misri Ptolemy wa Tatu. Mara moja akaanza kupanga jinsi ya kulipiza kisasi kuuawa kwa dada yake. Kwa kushambulia Mfalme wa Siria Seleuko wa Pili, ambaye Laodice alimtumia kuua Berenice na mwana wake, aliingia katika “ngome ya mfalme wa kaskazini.” Ptolemy wa Tatu aliteka sehemu ya Antiokia yenye ngome na kumwua Laodice. Akielekea mashariki kupitia milki ya mfalme wa kaskazini, alipora Babilonia na kupiga mwendo hadi India.
22. Ptolemy wa Tatu alirudi na nini Misri, na kwa nini ‘alijizuia miaka kadha wa kadha asimwendee mfalme wa kaskazini’?
22 Kisha ikawaje? Malaika wa Mungu atuambia hivi: “Na miungu yao, pamoja na sanamu zao, na vyombo vyao vizuri vya fedha na dhahabu atavichukua mpaka Misri; kisha atajizuia miaka kadha wa kadha asimwendee mfalme wa kaskazini.” (Danieli 11:8) Zaidi ya miaka 200 mapema, Mfalme wa Uajemi Cambyses wa Pili alikuwa ameshinda Misri na kuichukua miungu ya Misri, “sanamu zao.” Ptolemy wa Tatu alipora Susa, lililokuwa jiji kuu la Uajemi, akachukua miungu hiyo na kuichukua ‘mateka’ hadi Misri. Pia aliteka nyara ‘vyombo vingi vizuri vya fedha na dhahabu’ na kurudi navyo nyumbani. Kwa kuwa alilazimika kurudi nyumbani akakomeshe uasi uliozuka huko, Ptolemy wa Tatu ‘alijizuia asimwendee mfalme wa kaskazini,’ na kutomdhuru zaidi.
MFALME WA SIRIA ALIPIZA KISASI
23. Kwa nini mfalme wa kaskazini ‘alirudi mpaka nchi yake mwenyewe’ baada ya kuingia katika ufalme wa mfalme wa kusini?
23 Mfalme wa kaskazini alitendaje? Danieli aliambiwa hivi: “Ataingia katika ufalme wa mfalme wa kusini, lakini atarudi mpaka nchi yake mwenyewe.” (Danieli 11:9) Mfalme wa kaskazini—Mfalme Seleuko wa Pili wa Siria—naye pia alishambulia. Aliingia ndani ya “ufalme” au milki ya mfalme wa kusini wa Misri lakini akashindwa. Jeshi lake likiwa limesalia watu wachache tu, Seleuko wa Pili ‘alirudi mpaka nchi yake mwenyewe,’ na kurudi Antiokia, jiji kuu la Siria wapata mwaka wa 242 K.W.K. Alipokufa, mwana wake Seleuko wa Tatu akatawala baada yake.
24. (a) Ni nini kilichompata Seleuko wa Tatu? (b) Mfalme Antiochus wa Tatu wa Siria ‘alifurika na kupita katikati’ ya milki ya mfalme wa kusini jinsi gani?
24 Ni nini kilichotabiriwa kuhusu uzao wa Mfalme Seleuko wa Pili wa Siria? Malaika alimwambia Danieli hivi: “Na wanawe watafanya vita, na kukusanya mkutano wa majeshi makuu; watakaokuja na kufurika na kupita katikati; nao watarudi na kufanya vita mpaka penye ngome yake.” (Danieli 11:10) Na kabla ya miaka mitatu kutimia, utawala wa Seleuko wa Tatu ukakoma alipouawa. Ndugu yake, Antiochus wa Tatu, akatawala Siria baada yake. Mwana huyo wa Seleuko wa Pili alikusanya majeshi mengi ili akamshambulie mfalme wa kusini, ambaye wakati huo alikuwa Ptolemy wa Nne. Mfalme huyo mpya wa kaskazini wa Siria alipigana dhidi ya Misri na kukomboa bandari ya Seleucia, mkoa wa Coele-Siria, jiji la Tiro na jiji la Ptolemaïs, na miji ya karibu. Aliyashinda vibaya majeshi ya Mfalme Ptolemy wa Nne na kutwaa majiji mengi ya Yuda. Masika ya mwaka wa 217 K.W.K., Antiochus wa Tatu aliliacha Ptolemaïs na kwenda kaskazini, “mpaka penye ngome yake” huko Siria. Lakini punde si punde badiliko kubwa lingetokea.
MAMBO YAGEUKA
25. Ptolemy wa Nne na Antiochus wa Tatu walipigana wapi, na ni nini ‘lililowekwa mikononi’ mwa mfalme wa kusini wa Misri?
25 Sawa na Danieli, twasikiza kwa hamu malaika wa Yehova atabiripo hivi: “Mfalme wa kusini ataingiliwa na ghadhabu, naye atatoka na kupigana naye, yaani, na mfalme wa kaskazini; naye atapanga jeshi kubwa; na jeshi hilo litawekwa mikononi mwake.” (Danieli 11:11) Akiwa na wanajeshi 75,000, mfalme wa kusini, Ptolemy wa Nne, alielekea kaskazini dhidi ya adui. Mfalme wa Siria wa kaskazini, Antiochus wa Tatu, alikuwa ‘amepanga jeshi kubwa’ la watu 68,000 limkabili. Lakini “jeshi” hilo ‘liliwekwa mikononi’ mwa mfalme wa kusini katika pigano huko Raphia, jiji lililo pwani, karibu na mpaka wa Misri.
26. (a) Ni “jeshi” gani lililochukuliwa na mfalme wa kusini katika pigano huko Raphia, na mkataba wa amani uliofanywa huko ulitia ndani nini? (b) Ni katika njia gani Ptolemy wa Nne ‘hakutumia wadhifa wake wenye nguvu’? (c) Mfalme wa kusini aliyefuata alikuwa nani?
26 Unabii huo waendelea kusema hivi: “Atakapokwisha kuchukua lile jeshi, moyo wake utatukuzwa; naye atawaangusha makumi elfu; lakini hataongezewa nguvu [“hatatumia wadhifa wake wenye nguvu,” NW].” (Danieli 11:12) Ptolemy wa Nne, mfalme wa kusini, ‘alichukua’ askari 10,000 wa miguu na askari-wapanda-farasi 300 wa Siria akawaua na kutwaa wafungwa 4,000. Kisha wafalme hao wakafanya mkataba ambamo Antiochus wa Tatu aliachiwa Seleucia, bandari yake ya Siria lakini akapoteza Foinike na Coele-Siria. Kwa sababu ya ushindi huo, moyo wa mfalme wa kusini wa Misri ‘ulitukuzwa,’ hasa dhidi ya Yehova. Ptolemy wa Nne aliendelea kutawala Yuda. Lakini, ‘hakutumia wadhifa wake wenye nguvu’ baada ya ushindi wake dhidi ya mfalme wa kaskazini wa Siria. Badala yake, Ptolemy wa Nne alianza maisha ya ufasiki, na mwana wake mwenye umri wa miaka mitano, Ptolemy wa Tano, akawa mfalme wa kusini aliyefuata miaka kadhaa kabla ya kifo cha Antiochus wa Tatu.
MPORAJI AREJEA
27. Mfalme wa kaskazini alirudije “mwisho wa zamani zile” ili kukomboa eneo lililotekwa na Misri?
27 Kwa sababu ya uporaji wake wote, Antiochus wa Tatu akaja kuitwa Antiochus Mkuu. Malaika alisema hivi juu yake: “Mfalme wa kaskazini atarudi, naye atapanga jeshi kubwa kuliko lile la kwanza; naye hakika atakuja mwisho wa zamani zile, yaani baada ya miaka kadha wa kadha, pamoja na jeshi kubwa na mali nyingi.” (Danieli 11:13) “Zamani zile” zilikuwa miaka 16 au zaidi baada ya Wamisri kuwashinda Wasiria huko Raphia. Mfalme Ptolemy wa Tano aliyekuwa mchanga alipotawazwa kuwa mfalme wa kusini, Antiochus wa Tatu alipanga “jeshi kubwa kuliko lile la kwanza” ili kukomboa maeneo yaliyokuwa yametwaliwa na mfalme wa kusini wa Misri. Ili kutekeleza lengo lake, alijiunga na Mfalme Philip wa Tano wa Makedonia.
28. Mfalme mchanga wa kusini alikuwa na matatizo gani?
28 Mfalme wa kusini alikuwa na matatizo pia ndani ya ufalme wake. “Zamani zile watu wengi watasimama ili kumpinga mfalme wa kusini,” malaika akasema. (Danieli 11:14a) Watu wengi “wa[li]simama ili kumpinga mfalme wa kusini.” Zaidi ya kukabili majeshi ya Antiochus wa Tatu na mwenzake Mmakedonia, mfalme huyo mchanga wa kusini alikuwa na matatizo nyumbani Misri. Kwa sababu mlezi wake Agathocles, aliyetawala akitumia jina lake, alikuwa akiwatenda vibaya Wamisri, wengi wao waliasi. Malaika aliongezea kusema hivi: “Wenye jeuri [“wana wa wapokonyaji,” NW] miongoni mwa watu wako watajiinua ili kuyathibitisha maono; lakini wataanguka.” (Danieli 11:14b) Hata baadhi ya watu wa Danieli walipata kuwa “wana wa wapokonyaji,” au wanamapinduzi. Lakini ‘ono’ lolote waliloona wanaume hao Wayahudi juu ya mwisho wa utawala wa wasio Wayahudi halikuwa la kweli, nao wangeshindwa, au ‘kuanguka.’
29, 30. (a)“Silaha za kusini” zilishindwaje kukabiliana na shambulio kutoka kaskazini? (b) Mfalme wa kaskazini alipataje ‘kusimama katika nchi ya uzuri’?
29 Malaika wa Yehova alitabiri hivi zaidi: “Mfalme wa kaskazini atakuja, na kufanya kilima [“atauzingira,” BHN], na kuupiga mji wenye maboma; na silaha za kusini hazitaweza kumpinga, wala watu wake wateule, wala hapatakuwa na nguvu za kumpinga. Maana ajaye kupigana naye atatenda kadiri apendavyo, walahapana mtu atakayesimama mbele yake; naye atasimama katika nchi ya uzuri, na uharibifu utakuwa mkononi mwake.”—Danieli 11:15, 16.
30 Majeshi ya Ptolemy wa Tano, au “silaha za kusini,” yalishindwa na shambulio kutoka kaskazini. Huko Paneas (Kaisaria Filipi), Antiochus wa Tatu alimfukuza Jenerali Scopas wa Misri pamoja na watu 10,000 aliochagua, au ‘wateule wake,’ hadi Sidoni, “mji wenye maboma.” Huko Antiochus wa Tatu ‘aliuzingira,’ na kuiteka bandari hiyo ya Foinike mwaka wa 198 K.W.K. Alitenda “kadiri apendavyo” kwa sababu majeshi ya mfalme wa kusini wa Misri hayakuweza kusimama mbele yake. Kisha Antiochus wa Tatu akapiga mwendo kuelekea Yerusalemu, jiji kuu la “nchi ya uzuri,” Yuda. Mwaka wa 198 K.W.K., Yerusalemu na Yuda ziliacha kutawalwa na mfalme wa kusini wa Misri na kuanza kutawalwa na mfalme wa kaskazini wa Siria. Naye Antiochus wa Tatu, mfalme wa kaskazini, akaanza ‘kusimama katika nchi ya uzuri.’ Mlikuwemo ‘uharibifu mikononi mwake’ kwa Wayahudi wote na Wamisri wote waliompinga. Mfalme huyo wa kaskazini angefanya apendavyo kwa muda mrefu kadiri gani?
ROMA YAMZUIA MPORAJI
31, 32. Kwa nini mfalme wa kaskazini hatimaye “a[li]fanya mapatano” ya amani na mfalme wa kusini?
31 Malaika wa Yehova ajibu hivi: “Naye [mfalme wa kaskazini] atakaza uso wake ili aje pamoja na nguvu zote za ufalme wake, naye atafanya mapatano naye; naye atatenda kadiri apendavyo; naye atampa binti wa watu ili amharibu; lakini hilo halitasimama wala kumfaa [“naye hataendelea kuwa wake,” NW].”—Danieli 11:17.
32 Mfalme wa kaskazini, Antiochus wa Tatu, ‘alikaza uso wake’ ili atawale Misri “pamoja na nguvu zote za ufalme wake.” Lakini hatimaye “alifanya mapatano” ya amani na Ptolemy wa Tano, mfalme wa kusini. Madai ya Roma yalikuwa yamemfanya Antiochus wa Tatu abadili mipango yake. Alipoungana na Mfalme Philip wa Tano wa Makedonia dhidi ya mfalme wa Misri mwenye umri mchanga ili watwae eneo lake, walezi wa Ptolemy wa Tano waliomba Roma iwalinde. Roma ilitwaa fursa hiyo ili kuongeza uvutano wake, ikaonyesha nguvu zake.
33. (a) Ni masharti gani ya amani yaliyowekwa kati ya Antiochus wa Tatu na Ptolemy wa Tano? (b) Kusudi la ndoa kati ya Kleopatra wa Kwanza na Ptolemy wa Tano lilikuwa nini, na kwa nini mpango huo haukufua dafu?
33 Akishurutishwa na Roma, Antiochus wa Tatu alimwekea masharti ya amani mfalme wa kusini. Badala ya kusalimisha maeneo aliyokuwa ameteka, kama vile Roma ilivyotaka, Antiochus wa Tatu alipanga kuyahamisha kwa jina tu kwa kumwoza binti yake Kleopatra wa Kwanza—“binti wa watu”—kwa Ptolemy wa Tano. Mikoa iliyotia ndani Yuda, “nchi ya uzuri,” ingetolewa ikiwa mahari. Hata hivyo, wakati wa ndoa mwaka wa 193 K.W.K. mfalme wa Siria hakuachilia mikoa hiyo imwendee Ptolemy wa Tano. Hiyo ilikuwa ndoa ya kisiasa, iliyofanywa ili kutiisha Misri chini ya Siria. Lakini, mpango huo haukufua dafu kwa sababu Kleopatra wa Kwanza ‘hakuendelea kuwa wake,’ kwa kuwa baadaye aliamua kumwunga mkono mume wake. Vita vilipozuka kati ya Antiochus wa Tatu na Waroma, Misri ilijiunga na Roma.
34, 35. (a) Mfalme wa kaskazini aliuelekeza uso wake kwenye ‘nchi zipi za pwani’? (b) Roma ilikomeshaje “aibu” kutoka kwa mfalme wa kaskazini? (c) Antiochus wa Tatu alikufaje, na mfalme wa kaskazini aliyefuata alikuwa nani?
34 Malaika alisema hivi akirejezea kushindwa huko kwa mfalme wa kaskazini: “Baada ya hayo [Antiochus wa Tatu] atauelekeza uso wake kwenye visiwa, naye atavipiga visiwa vingi [“nchi nyingi za pwani na kuzishinda,” BHN]; lakini mkuu mmoja [Roma] ataikomesha aibu iliyoletwa na yeye [Roma]; naam, aibu yake [kutoka kwa Antiochus wa Tatu] hiyo [Roma] atamrudishia mwenyewe. Ndipo [Antiochus wa Tatu] atauelekeza uso wake kwenye ngome za nchi yake mwenyewe; lakini atajikwaa na kuanguka, wala hataonekana tena.”—Danieli 11:18, 19.
35 ‘Nchi hizo za pwani’ ni Makedonia, Ugiriki, na Asia Ndogo. Vita vilizuka Ugiriki mwaka wa 192 K.W.K., na Antiochus wa Tatu akashawishiwa aende Ugiriki. Hatimaye Roma ikatangaza vita dhidi yake kwa kuwa ilikasirishwa na jitihada za mfalme wa Siria za kuteka maeneo zaidi huko. Huko Thermopylae alishindwa na Waroma. Mwaka mmoja hivi baada ya kushindwa katika vita ya Magnesia mwaka wa 190 K.W.K., alilazimika kuacha kila kitu huko Ugiriki, Asia Ndogo, na maeneo yaliyo magharibi mwa Milima Taurus. Roma ilimtoza faini kubwa na kusitawisha utawala wake juu ya mfalme wa kaskazini wa Siria. Akiwa amefukuzwa kutoka Ugiriki na Asia Ndogo na baada ya kupoteza karibu meli zake zote, Antiochus wa Tatu ‘aliuelekeza uso wake mwenyewe kwenye ngome za nchi yake mwenyewe,’ Siria. Waroma walikuwa ‘wamemrudishia aibu yake mwenyewe.’ Antiochus wa Tatu alikufa akijaribu kupora hekalu huko Elymaïs, Uajemi, mwaka wa 187 K.W.K. Kwa hiyo, ‘akaanguka’ katika kifo naye mwana wake Seleuko wa Nne, akatawala baada yake akiwa mfalme wa kaskazini aliyefuata.
PAMBANO LAENDELEA
36. (a) Mfalme wa kusini alijaribu kuendelezaje pambano, lakini akapatwa na nini? (b) Seleuko wa Nne aliangukaje, na ni nani aliyetawala baada yake?
36 Akiwa mfalme wa kusini, Ptolemy wa Tano alijaribu kuipata mikoa ambayo alipaswa kupewa ikiwa mahari ya Kleopatra, lakini alitiliwa sumu. Ptolemy wa Sita akatawala baada yake. Vipi juu ya Seleuko wa Nne? Kwa kuwa alihitaji fedha za kulipa faini kubwa aliyodaiwa na Roma, alimtuma mweka-hazina Heliodorus akatwae mali ambazo yasemekana zilikuwa zimewekwa katika hekalu la Yerusalemu. Heliodorus akamuua Seleuko wa Nne kwa kuwa alikitamani kiti cha ufalme. Hata hivyo, Mfalme Eumenes wa Pergamamu na ndugu yake Attalus wakamtawaza Antiochus wa Nne, ndugu ya mfalme aliyeuawa.
37. (a) Antiochus wa Nne alijaribuje kujionyesha kuwa mwenye nguvu kuliko Yehova Mungu? (b) Makufuru ya Antiochus wa Nne dhidi ya hekalu la Yerusalemu yalisababisha nini?
37 Mfalme mpya wa kaskazini, Antiochus wa Nne, alijaribu kujionyesha kuwa mwenye nguvu kuliko Mungu kwa kujaribu kufutilia mbali mpango wa Yehova wa ibada. Alimkaidi Yehova na kuweka wakfu hekalu la Yerusalemu kwa Zeo, au Jupita. Desemba mwaka wa 167 K.W.K., hekalu la kipagani lilijengwa juu ya madhabahu kubwa katika ua wa hekalu ambapo matoleo ya kuteketezwa yalikuwa yakitolewa kwa Yehova kila siku. Siku kumi baadaye, dhabihu ilitolewa kwa Zeo kwenye madhabahu ya kipagani. Wayahudi wakiongozwa na Wamakabayo waliasi kwa sababu ya makufuru hayo. Antiochus wa Nne alipigana nao kwa miaka mitatu. Mwaka wa 164 K.W.K., kwenye ukumbusho wa kila mwaka wa makufuru hayo, Yudasi Makabayo aliliweka wakfu tena hekalu kwa Yehova nao msherehekeo wa wakfu uitwao Hanuka, ukaanzishwa.—Yohana 10:22.
38. Utawala wa Wamakabayo ulikomaje?
38 Huenda Wamakabayo walifanya mkataba na Roma mwaka wa 161 K.W.K. na kuanzisha ufalme mwaka wa 104 K.W.K. Lakini waliendelea kuzozana na mfalme wa kaskazini wa Siria. Hatimaye, Roma ikaitwa iingilie kati. Jenerali Mroma Gnaeus Pompey akateka Yerusalemu mwaka wa 63 K.W.K. baada ya mazingiwa yaliyodumu miezi mitatu. Mwaka wa 39 K.W.K., Seneti ya Roma ikamweka rasmi Herode—Mwedomu—awe mfalme wa Yudea. Baada ya kuukomesha utawala wa Wamakabayo, aliteka Yerusalemu mwaka wa 37 K.W.K.
39. Umenufaikaje kwa kuchunguza Danieli 11:1-19?
39 Yasisimua kama nini kuona sehemu ya kwanza ya unabii juu ya wafalme wawili wanaopambana ikitimia kikamili! Kwa kweli, yasisimua kama nini kuchunguza historia ya miaka ipatayo 500 baada ya Danieli kupokea ujumbe wa kiunabii na pia kuwatambua watawala waliokuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini! Hata hivyo, pambano kati ya wafalme hao wawili liendeleapo wakati wa Yesu Kristo na hata leo, wafalme hao wawili wabadilika-badilika kisiasa. Kwa kuhusianisha mambo ya kihistoria na mambo yenye kupendeza yanayofunuliwa katika unabii huo, tutaweza kuwatambua wafalme hao wawili wenye kushindana.
-
-
Wafalme Wawili WapambanaSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
[Chati/Picha katika ukurasa wa 228]
WAFALME KATIKA DANIELI 11:5-19
Mfalme wa Mfalme wa
Kaskazini Kusini
Danieli 11:5 Niketa Seleuko wa I Ptolemy wa Kwanza
Danieli 11:6 Antiochus wa Pili Ptolemy wa Pili
(mke Laodice) (binti Berenice)
Danieli 11:7-9 Seleuko wa Pili Ptolemy wa Tatu
Danieli 11:10-12 Antiochus wa Tatu Ptolemy wa Nne
Danieli 11:13-19 Antiochus wa Tatu Ptolemy wa Tano
(binti, Kleopatra I) Mwaandamizi:
Waandamizi: Ptolemy wa Sita
Seleuko wa Nne na
Antiochus wa Nne
-
-
Wale Wafalme Wawili WabadilikaSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Sura Ya Kumi Na Nne
Wale Wafalme Wawili Wabadilika
1, 2. (a) Ni nini kilichomfanya Antiochus wa Nne akubali madai ya Roma? (b) Siria ilipata kuwa mkoa wa Roma lini?
MTAWALA wa Siria Antiochus wa Nne avamia Misri na kujitawaza mwenyewe kuwa mfalme. Mfalme Ptolemy wa Sita wa Misri aombapo msaada, Roma yamtuma Balozi Caius Popilius Laenas aende Misri. Aenda na meli nyingi zenye kuvutia na maagizo kutoka kwa Seneti ya Roma kwamba Antiochus wa Nne akane ufalme wake wa Misri na kutoka nchini humo. Mfalme wa Siria na balozi wa Roma wakutana ana kwa ana Eleusis, kitongoji cha Aleksandria. Antiochus wa Nne aomba wakati ili apate kushauriana na washauri wake, lakini Laenas achora duara kumzunguka mfalme na kumwambia ajibu kabla ya kuvuka mstari huo. Akiwa ameaibishwa, Antiochus wa Nne akubali madai ya Roma na kurudi Siria mwaka wa 168 K.W.K. Ndivyo uishavyo ushindani kati ya mfalme wa kaskazini wa Siria na mfalme wa kusini wa Misri.
2 Ikiwa na fungu kubwa katika mambo ya Mashariki ya Kati, Roma yaendelea kutawala Siria. Kwa sababu hiyo, ingawa wafalme wengine wa nasaba ya Seleuko walitawala Siria baada ya Antiochus wa Nne kufa mwaka wa 163 K.W.K., hawapati kuwa “mfalme wa kaskazini.” (Danieli 11:15) Hatimaye Siria inakuwa mkoa wa Roma mwaka wa 64 K.W.K.
3. Roma ilipata mamlaka kuliko Misri lini na jinsi gani?
3 Nasaba ya Ptolemy ya Misri yaendelea kuwa “mfalme wa kusini” kwa zaidi ya miaka 130 baada ya Antiochus wa Nne kufa. (Danieli 11:14) Wakati wa vita ya Actium, mwaka wa 31 K.W.K., mtawala wa Roma Octavian ayashinda majeshi ya muungano ya malkia wa mwisho wa nasaba ya Ptolemy—Kleopatra wa Saba—pamoja na mpenzi wake Mroma, Mark Antony. Baada ya Kleopatra kujiua mwaka uliofuata, Misri pia yawa mkoa wa Roma na kukoma kuwa mfalme wa kusini. Mwaka wa 30 K.W.K., Roma ina mamlaka kuu kuliko Siria na Misri. Je, sasa tutarajie tawala nyingine ziwe mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini?
MFALME MPYA ATUMA ‘MTOZA-USHURU’
4. Kwa nini tutarajie utawala mwingine uwe mfalme wa kaskazini?
4 Masika ya mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mwonapo mara hiyo kitu chenye kuchukiza sana ambacho husababisha ukiwa, kama kilivyosemwa kupitia Danieli nabii, kikiwa kimesimama katika mahali patakatifu, . . . ndipo waacheni wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani.” (Mathayo 24:15, 16) Akinukuu Danieli 11:31, Yesu aliwaonya wafuasi wake juu ya ‘kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa’ cha wakati ujao. Unabii huo unaohusu mfalme wa kaskazini ulitolewa miaka 195 hivi baada ya kifo cha Antiochus wa Nne, mfalme wa mwisho wa Siria aliyekuwa mfalme wa kaskazini. Bila shaka, utawala mwingine ungekuwa mfalme wa kaskazini. Nani huyo?
5. Ni nani aliyesimama akiwa mfalme wa kaskazini, na kuchukua wadhifa uliokuwa wa Antiochus wa Nne wakati mmoja?
5 Malaika wa Yehova Mungu alitabiri hivi: “Badala yake [Antiochus wa Nne] atasimama mmoja, atakayepitisha mwenye kutoza ushuru kati ya utukufu wa ufalme wake; lakini katika muda wa siku chache ataangamizwa, si kwa hasira, wala si katika vita.” (Danieli 11:20) ‘Asimamaye’ hivyo alithibitika kuwa maliki wa kwanza wa Roma, Octavian, aliyeitwa Kaisari Augusto.—Ona “Mmoja Aheshimiwa, Yule Mwingine Adharauliwa,” kwenye ukurasa wa 248.
6. (a) ‘Mtoza-ushuru alipitishwa’ lini katika “utukufu wa ufalme,” na hilo lilikuwa na umaana gani? (b) Kwa nini twaweza kusema kwamba Augusto alikufa “si kwa hasira, wala si katika vita”? (c) Mfalme wa kaskazini alibadilika akawa nani?
6 ‘Ufalme wenye utukufu’ wa Augusto ulitia ndani “nchi ya uzuri”—Yudea, mkoa wa Roma. (Danieli 11:16) Mwaka wa 2 K.W.K., Augusto alimtuma ‘mtoza-ushuru’ kwa kuagiza uandikishaji, au kuhesabiwa kwa watu, huenda ili apate kujua idadi ya watu kwa minajili ya kutoza kodi na kuwaandikisha kwa lazima kwenye utumishi wa kijeshi. Kwa sababu ya agizo hilo, Yosefu na Maria walisafiri hadi Bethlehemu wakajiandikishe, kisha Yesu akazaliwa mahali palipotabiriwa. (Mika 5:2; Mathayo 2:1-12) Agosti mwaka wa 14 W.K.—“katika muda wa siku chache,” au punde baada ya kuagiza uandikishaji—Augusto akafa akiwa na umri wa miaka 76, si “kwa hasira” mikononi mwa muuaji wala “katika vita,” bali kwa sababu ya ugonjwa. Kwa kweli, mfalme wa kaskazini alikuwa amebadilika! Kufikia sasa mfalme huyo alikuwa Milki ya Roma ikiwa na watawala wake.
‘MWENYE KUDHARAULIWA ASIMAMA’
7, 8. (a) Ni nani aliyechukua mahali pa Augusto akiwa mfalme wa kaskazini? (b) Kwa nini Kaisari Augusto alimpa mwandamizi wake “heshima ya ufalme” kwa shingo upande?
7 Akiendelea na unabii huo, malaika asema hivi: “Badala yake [Augusto] atasimama mmoja, mtu astahiliye kudharauliwa, ambaye hawakumpa heshima ya ufalme; naye atakuja wakati wa amani, naye ataupata ufalme kwa kujipendekeza [“kunyakua ufalme kwa hila,” BHN]. Na wale wenye silaha mfano wa gharika watagharikishwa mbele yake, na kuvunjika; naam, mkuu wa maagano pia.”—Danieli 11:21, 22.
8 “Mtu astahiliye kudharauliwa” alikuwa Kaisari Tiberio, mwana wa Livia, mke wa tatu wa Augusto. (Ona “Mmoja Aheshimiwa, Yule Mwingine Adharauliwa,” kwenye ukurasa wa 248.) Augusto alimchukia mwana wake wa kambo kwa sababu ya tabia yake mbaya wala hakutaka awe Kaisari baada yake. Alimpa “heshima ya ufalme” shingo upande baada ya watu wote ambao wangeweza kuwa Kaisari kufa. Augusto alimwasilisha Tiberio mwaka wa 4 W.K. na kumfanya awe mrithi wa ufalme. Baada ya Augusto kufa, Tiberio mwenye umri wa miaka 54—mwenye kudharauliwa—‘akasimama,’ akitwaa mamlaka ya kuwa maliki wa Roma na mfalme wa kaskazini.
9. Tiberio ‘alinyakuaje ufalme kwa hila’?
9 “Tiberio,” yasema The New Encyclopædia Britannica, “alitumia hila dhidi ya Seneti wala hakuiruhusu imteue awe maliki kwa zaidi ya mwezi mmoja [baada ya Augusto kufa].” Aliiambia Seneti kwamba hakuna mtu yeyote ila Augusto aliyekuwa na uwezo wa kubeba mzigo wa kutawala Milki ya Roma na akawaomba maseneta waweke kikundi cha watu kimiliki badala ya mtu mmoja. “Bila kunuia kukubali aliyosema,” akaandika mwanahistoria Will Durant, “Seneti ilibembelezana-bembelezana naye mpaka hatimaye akaikubali mamlaka hiyo.” Durant alisema hivi pia: “Pande zote mbili zilikuwa zikijifanya. Tiberio alitaka kuwa maliki wa Roma, la sivyo angalipata njia ya kuuhepa umaliki; Seneti ilimhofu na kumchukia, lakini haikutaka tena kuwa jamhuri, kama ile ya kale, ambayo ilitegemea mabunge ya watawala ya kuwaziwa tu.” Kwa hiyo, Tiberio ‘akaunyakua ufalme kwa hila.’
10. ‘Silaha mfano wa gharika zilivunjwaje’?
10 “Na wale wenye silaha mfano wa gharika”—majeshi ya falme zilizozunguka—malaika alisema hivi: “Watagharikishwa mbele yake, na kuvunjika.” Tiberio alipokuwa mfalme wa kaskazini, mpwa wake wa kiume Kaisari Germanicus alikuwa kamanda wa vikosi vya Roma kwenye Mto Rhine. Mwaka wa 15 W.K., Germanicus aliongoza majeshi yake dhidi ya shujaa Mjerumani Arminius, naye akafaulu kwa kiasi fulani. Hata hivyo, ushindi huo ulimgharimu sana, naye Tiberio akaacha mambo ya Ujerumani. Badala yake, kwa kuendeleza vita vya kikabila, alijaribu kuyazuia makabila ya Ujerumani yasiungane. Kwa kawaida, Tiberio alipendelea sera ya kujikinga na nchi za kigeni naye akakazia fikira kuimarisha mipaka. Sera hiyo ya kujikinga ilikuwa na mafanikio kwa kiasi fulani. Kwa njia hiyo “silaha mfano wa gharika” zikadhibitiwa na ‘kuvunjwa.’
11. ‘Mkuu wa maagano alivunjwaje’?
11 “Mkuu wa maagano” ambayo Yehova Mungu alikuwa amefanya na Abrahamu ili kubariki familia zote duniani ‘alivunjwa’ pia. Yesu Kristo alikuwa Mbegu ya Abrahamu iliyoahidiwa katika agano hilo. (Mwanzo 22:18; Wagalatia 3:16) Nisani 14, 33 W.K., Yesu alisimama mbele ya Pontio Pilato katika jumba la gavana wa Roma huko Yerusalemu. Makuhani Wayahudi walikuwa wamemshtaki Yesu kuwa mhaini dhidi ya maliki. Lakini Yesu alimwambia Pilato hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. . . . Ufalme wangu si kutoka chanzo hiki.” Kwa kuwa Wayahudi hawakutaka gavana Mroma amwachilie Yesu asiye na hatia, walipaaza sauti, wakisema: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari. Kila mtu anayejifanya mwenyewe mfalme asema vibaya dhidi ya Kaisari.” Baada ya kuagiza Yesu auawe, walisema hivi: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” Kulingana na sheria ya ‘uhaini,’ ambayo Tiberio alikuwa ameipanua itie ndani kumtukana Kaisari kwa njia yoyote, Pilato akamtoa Yesu ‘avunjwe,’ au atundikwe kwenye mti wa mateso.—Yohana 18:36; 19:12-16; Marko 15:14-20.
MKANDAMIZAJI ‘ATUNGA HILA ZAKE’
12. (a) Ni nani waliofanya maagano na Tiberio? (b) Tiberio ‘alikuwaje hodari pamoja na watu wadogo’?
12 Bado akitoa unabii juu ya Tiberio, malaika alisema hivi: “Na baada ya maagano atatenda kwa hila; maana atapanda, naye atakuwa hodari pamoja na watu wadogo.” (Danieli 11:23) Washiriki wa Seneti ya Roma walikuwa ‘wamefanya maagano’ ya kikatiba na Tiberio, naye aliwategemea kihalali. Lakini alitenda kwa hila, hata akawa “hodari pamoja na watu wadogo.” Watu hao wadogo walikuwa Walindaji wa Praetori wa Roma waliokuwa wamepiga kambi karibu na kuta za Roma. Ukaribu huo uliogofya Seneti na kumsaidia Tiberio adhibiti maasi yoyote dhidi ya mamlaka yake miongoni mwa watu wa kawaida. Tiberio aliendelea kuwa mwenye nguvu akitumia walinzi 10,000.
13. Tiberio alishindaje baba zake?
13 Malaika huyo aliongeza kusema hivi kiunabii: “Wakati wa amani atapaingia mahali palipofanikiwa sana pa wilaya hiyo; naye atatenda mambo ambayo baba zake hawakuyatenda, wala babu zake; atatawanya kati yao mawindo, na mateka, na mali; naam, atatunga hila zake juu ya ngome, hata wakati ulioamriwa.” (Danieli 11:24) Tiberio alikuwa mwenye kushukushuku sana, naye aliagiza watu wengi wauawe alipokuwa akitawala. Hasa kwa sababu ya Sejanus, kamanda wa Walindaji wa Praetori, sehemu ya mwisho ya utawala wake iliogofya sana. Hatimaye, Sejanus mwenyewe akaanza kushukiwa kisha akauawa. Tiberio alishinda baba zake katika kuwakandamiza watu.
14. (a) Tiberio alitawanyaje “mawindo, na mateka, na mali” kotekote katika mikoa ya Roma? (b) Watu walimwonaje Tiberio kufikia wakati alipokufa?
14 Hata hivyo, Tiberio alitawanya “mawindo, na mateka, na mali” kotekote katika mikoa ya Roma. Alipokufa, raia zake wote walikuwa na ufanisi. Kodi hazikuwa zenye kulemea, naye alikuwa mkarimu kwa wale waliokuwa na magumu. Iwapo askari au maofisa walimwonea yeyote au kuendeleza mambo yasiyo ya kawaida katika kushughulikia mambo, wangaliweza kutarajia kisasi cha mtawala. Kuwa na mamlaka imara kulidumisha usalama, na mfumo ulioboreshwa wa kuwasiliana ulisaidia katika biashara. Tiberio alihakikisha kwamba mambo yalifanywa bila upendeleo na kwa utaratibu ndani na nje ya Roma. Kuendeleza mabadiliko yaliyoanzishwa na Kaisari Augusto kuliboresha sheria, na mifumo ya kijamii na ya kiadili. Hata hivyo, Tiberio ‘alitunga hila zake,’ hivi kwamba mwanahistoria Mroma Tasito alimfafanua kuwa mnafiki, mwenye ustadi wa kujifanya. Kufikia wakati alipokufa Machi 37 W.K., Tiberio alionwa kuwa mkandamizaji.
15. Roma iliendeleaje mwishoni mwa karne ya kwanza na mwanzoni mwa karne ya pili W.K.?
15 Wamaliki waliotawala baada ya Tiberio ambao walikuwa wafalme wa kaskazini walitia ndani Kaisari Gayo (Caligula), Klaudio wa Kwanza, Nero, Vaspasiani, Tito, Domitiani, Nerva, Trajani, na Hadriani. “Kwa muda mrefu,” chasema kichapo The New Encyclopædia Britannica, “wamaliki waliotawala baada ya Augusto waliendeleza sera zake za kutawala na miradi yake ya ujenzi, ingawa hawakuanzisha mambo mengi nao walikuwa wenye kujionyesha sana.” Kichapo hichohicho chataarifu hivi: “Mwishoni mwa karne ya 1 na mwanzoni mwa karne ya 2, Roma ilikuwa imefikia upeo wa utukufu nayo ilikuwa na wakazi wengi zaidi.” Ingawa Roma ilikuwa na matatizo kadhaa kwenye mipaka yake, pambano lake la kwanza lililotabiriwa dhidi ya mfalme wa kusini halikutukia hadi karne ya tatu W.K.
ACHOCHEWA DHIDI YA MFALME WA KUSINI
16, 17. (a) Ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini anayetajwa kwenye Danieli 11:25? (b) Ni nani aliyekuja kuwa mfalme wa kusini, na hilo lilitukiaje?
16 Malaika wa Mungu aliendelea na unabii huo, akisema hivi: “Naye [mfalme wa kaskazini] atachochea nguvu zake na ushujaa wake juu ya huyo mfalme wa kusini kwa jeshi kubwa; na mfalme wa kusini atafanya vita kwa jeshi kubwa mno lenye nguvu nyingi; lakini [mfalme wa kaskazini] hatasimama; maana watatunga hila juu yake. Naam, walao sehemu ya chakula chake watamwangamiza, na jeshi lake litagharikishwa; na wengi wataanguka wameuawa.”—Danieli 11:25, 26.
17 Miaka 300 hivi baada ya Octavian kufanya Misri iwe mkoa wa Roma, Maliki Mroma Aurelian akawa mfalme wa kaskazini. Wakati huohuo, Malkia Septimia Zenobia wa koloni ya Roma ya Palmyra akawa mfalme wa kusini.a (Ona “Zenobia—Malkia Mpiganaji wa Palmyra,” kwenye ukurasa wa 252.) Jeshi la Palmyra lilikuwa likimiliki Misri mwaka wa 269 W.K. likisingizia kuwa lilikuwa likiifanya iwe salama kwa ajili ya Roma. Zenobia alitaka kufanya Palmyra liwe jiji kuu huko mashariki na alitaka kutawala mikoa ya mashariki ya Roma. Akishtuliwa na tamaa ya makuu ya Zenobia, Aurelian alichochea “nguvu zake na ushujaa wake” dhidi ya Zenobia.
18. Matokeo ya pambano kati ya Maliki Aurelian, mfalme wa kaskazini, na Malkia Zenobia, mfalme wa kusini yalikuwa nini?
18 Mfalme wa kusini, yaani serikali ya Zenobia, ‘alifanya’ vita dhidi ya mfalme wa kaskazini “kwa jeshi kubwa mno lenye nguvu nyingi” chini ya majenerali wawili, Zabdas na Zabbai. Lakini Aurelian aliteka Misri kisha akafunga safari kwenda Asia Ndogo na Siria. Zenobia alishindwa huko Emesa (kuitwako Homs leo), akakimbia na kwenda Palmyra. Aurelian alipolizingira jiji hilo, Zenobia alilipigania kufa na kupona lakini hakufanikiwa. Yeye na mwanaye wakakimbia kuelekea Uajemi, wakakamatwa na Waroma kwenye Mto Eufrati. Watu wa Palmyra walisalimisha jiji lao mwaka wa 272 W.K. Aurelian hakumuua Zenobia, hilo likimfanya avutie watu wengi katika ule msafara wa ushindi kupitia Roma mwaka 274 W.K. Aliishi maisha yake yaliyosalia akiwa mke Mroma.
19. Aurelian aliangukaje kwa sababu ya ‘hila zilizotungwa juu yake’?
19 Aurelian mwenyewe ‘hakusimama kwa sababu ya hila zilizotungwa juu yake.’ Mwaka wa 275 W.K., alifunga safari kwenda kupigana na Waajemi. Alipokuwa akingoja huko Thrasi ili apate fursa ya kuvuka mlango-bahari na kuingia Asia Ndogo, wale ‘waliokula sehemu ya chakula chake’ walitunga hila juu yake na ‘kumwangamiza.’ Alinuia kumwadhibu mwandishi wake Eros kwa sababu mambo hayakuwa shwari. Hata hivyo, Eros akaandika orodha bandia ya majina ya maofisa kadhaa waliotiwa alama wauawe. Maofisa hao walipoiona orodha hiyo walipanga njama na kumwua Aurelian.
20. “Jeshi” la mfalme wa kaskazini ‘liligharikishwaje’?
20 Mfalme wa kaskazini hakutoweka Maliki Aurelian alipokufa. Waroma wengine walitawala baada yake. Kwa muda fulani kulikuwa na maliki wa magharibi na maliki wa mashariki. Chini yao “jeshi” la mfalme wa kaskazini ‘liligharikishwa,’ au ‘kutawanywa,’b na wengi ‘walianguka wameuawa’ kwa sababu ya uvamizi wa makabila ya Kijerumani kutoka kaskazini. Wagothi walivuka mipaka ya Roma katika karne ya nne W.K. Uvamizi uliendelea, mmoja baada ya mwingine. Mwaka wa 476 W.K., kiongozi wa Ujerumani, Odoacer alimwondoa maliki wa mwisho aliyekuwa akitawala Roma. Kufikia mwanzoni mwa karne ya sita, Milki ya Roma ya upande wa magharibi ilikuwa imevunjwa-vunjwa, na wafalme Wajerumani walikuwa wakitawala Afrika Kaskazini, Gaul, Hispania, Italia, na Uingereza. Upande wa mashariki wa milki hiyo ulidumu hadi karne ya 15.
MILKI KUBWA YAGAWANYIKA
21, 22. Konstantino alitokeza mabadiliko gani katika karne ya nne W.K.?
21 Malaika wa Yehova aliendelea kutabiri uporaji zaidi wa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini bila kutaja mambo madogo-madogo yasiyohitajika juu ya kuvunjika kwa Milki ya Roma. Hata hivyo, kupitia kifupi mambo fulani yaliyotukia katika Milki ya Roma kutatusaidia kuwatambua wafalme hao wawili wakati ujao.
22 Katika karne ya nne, Maliki Mroma Konstantino alifanya Serikali iutambue Ukristo uliokuwa umeasi. Hata aliitisha na kusimamia baraza la kanisa huko Nisea, Asia Ndogo, mwaka wa 325 W.K. Baadaye, Konstantino alihamisha makao ya kifalme kutoka Roma hadi Byzantium, au Constantinople, akilifanya jiji hilo jipya kuwa jiji lake kuu. Milki ya Roma iliendelea chini ya utawala wa maliki mmoja hadi Maliki Theodosius wa Kwanza alipokufa Januari 17, 395 W.K.
23. (a) Milki ya Roma iligawanyikaje Theodosius alipokufa? (b) Milki ya Mashariki ilikoma lini? (c) Ni nani aliyetawala Misri kufikia mwaka wa 1517?
23 Theodosius alipokufa, wana wake waligawanya Milki ya Roma miongoni mwao. Honorius alipokea sehemu ya magharibi, naye Arcadius akapokea mashariki, Constantinople likiwa jiji lake kuu. Afrika Kaskazini, Gaul, Hispania, Italia, na Uingereza ilikuwa baadhi ya mikoa ya milki ya magharibi. Makedonia, Thrasi, Asia Ndogo, Siria, na Misri ilikuwa mikoa ya milki ya mashariki. Mwaka wa 642 W.K., Aleksandria, jiji kuu la Misri, lilianguka mikononi mwa Waarabu, na Misri ikawa mkoa wa makhalifa. Katika Januari 1449, Konstantino wa 11 akawa maliki wa mwisho wa mashariki. Waturuki wakiongozwa na Sultan Mehmed wa Pili waliteka Constantinople Mei 29, 1453, na kuikomesha Milki ya Roma Mashariki. Misri ikawa mkoa wa Uturuki mwaka wa 1517. Hata hivyo, hatimaye nchi hiyo ya mfalme wa kale wa kusini ingetawalwa na milki nyingine kutoka magharibi.
24, 25. (a) Kulingana na wanahistoria fulani, ni nini kilichoonyesha mwanzo wa Milki Takatifu ya Roma? (b) Ni nini kilichotokea hatimaye kwa lile jina la cheo “maliki” la Milki Takatifu ya Roma?
24 Askofu Mkatoliki wa Roma, aitwaye Papa Leo wa Kwanza, aliyekuwa maarufu kwa kusisitiza mamlaka ya papa katika karne ya tano W.K., alizuka upande wa magharibi wa Milki ya Roma. Hatimaye, papa huyo akajiamulia kumtawaza maliki wa upande wa magharibi. Ilitukia hivyo huko Roma kwenye Krismasi ya mwaka wa 800 W.K., Papa Leo wa Tatu alipomtawaza Mfalme Charles (Charlemagne) wa Wafaranka awe maliki wa Milki mpya ya Roma Magharibi. Kutawaza huko kulianzisha tena umaliki huko Roma na, kulingana na wanahistoria fulani, kulionyesha mwanzo wa Milki Takatifu ya Roma. Tangu wakati huo na kuendelea kulikuwa na Milki ya Mashariki na Milki Takatifu ya Roma iliyokuwa magharibi, milki zote mbili zikidai kuwa za Kikristo.
25 Kadiri wakati ulivyopita, waliotawala baada ya Charlemagne hawakuwa na matokeo yoyote. Hata kwa muda fulani hakukuwa na maliki. Wakati huohuo, Mfalme wa Ujerumani Otto wa Kwanza alikuwa ameanza kutawala sehemu kubwa ya kaskazini na ya kati ya Italia. Akajitangaza kuwa mfalme wa Italia. Februari 2, 962 W.K., Papa John wa 12 alimtawaza Otto wa Kwanza kuwa maliki wa Milki Takatifu ya Roma. Jiji lake kuu lilikuwa Ujerumani, nao wamaliki walikuwa Wajerumani, kama vile wengi wa raia zake walivyokuwa Wajerumani. Karne tano baadaye, watawala wa Kijerumani waliotawala Austria waliitwa “maliki,” nao waliendelea kuitwa hivyo kwa muda mrefu katika ile miaka iliyosalia ya Milki Takatifu ya Roma.
WALE WAFALME WAWILI WATAMBULIKA WAZIWAZI TENA
26. (a) Ni nini kiwezacho kusemwa juu ya mwisho wa Milki Takatifu ya Roma? (b) Ni nani aliyetokea akiwa mfalme wa kaskazini?
26 Napoléon wa Kwanza aliipiga na kuiangamiza Milki Takatifu ya Roma alipokataa kutambua kuwepo kwa milki hiyo baada ya ushindi wake mbalimbali huko Ujerumani mwaka wa 1805. Kwa kuwa alishindwa kuitetea taji, Maliki Francis wa Pili alijiuzulu kutoka katika utawala wa Roma Agosti 6, 1806, na kurudia serikali yake ya kitaifa akiwa maliki wa Austria. Baada ya miaka 1,006, ile Milki Takatifu ya Roma—iliyoanzishwa na Leo wa Tatu, papa Mkatoliki, na Charlemagne, mfalme Mfaranka—ikakoma. Mwaka wa 1870, Roma likawa jiji kuu la ufame wa Italia, usiotegemea Vatikani. Mwaka uliofuata, milki ya Kijerumani ikaanza, Wilhelm wa Kwanza akateuliwa kuwa kaisari. Kwa hiyo, mfalme wa kaskazini wa kisasa—Ujerumani—akatokea duniani.
27. (a) Misri ilipataje kuwa chini ya himaya ya Uingereza? (b) Ni nani aliyepata kuwa mfalme wa kusini?
27 Lakini mfalme wa kusini wa kisasa alikuwa nani? Historia yaonyesha kwamba Uingereza ilitwaa mamlaka katika karne ya 17. Akinuia kukatisha njia za kibiashara za Uingereza, Napoléon wa Kwanza alishinda Misri mwaka wa 1798. Vita vikazuka, na muungano wa Waingereza na Waturuki ukawaondolea mbali Wafaransa kutoka Misri, ambayo mwanzoni, ilitambulishwa kuwa mfalme wa kusini. Katika karne iliyofuata, uvutano wa Uingereza huko Misri uliongezeka. Baada ya mwaka wa 1882, Misri ilikuwa ikitegemea Uingereza hasa. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipozuka mwaka wa 1914, Misri ilimilikiwa na Uturuki nayo ilitawalwa na gavana. Hata hivyo, baada ya Uturuki kujiunga na Ujerumani katika vita hiyo, Uingereza ilimwondoa gavana huyo na kuitangaza Misri kuwa chini ya himaya ya Uingereza. Uingereza na Marekani zilianza kuwa na uhusiano wa karibu hatua kwa hatua na hatimaye zikawa Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Zikiwa pamoja zikawa mfalme wa kusini.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kuwa majina “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” ni majina ya cheo, yaweza kurejezea chochote chenye kutawala, kutia ndani mfalme, malkia, au mataifa kadhaa yakiwa pamoja.
b Ona kielezi-chini kwenye Danieli 11:26 katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
-
-
Wale Wafalme Wawili WabadilikaSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 248-251]
MMOJA AHESHIMIWA, YULE MWINGINE ADHARAULIWA
MMOJA alibadili jamhuri iliyojaa zogo ikawa milki ya ulimwengu. Yule mwingine akaongeza utajiri wa milki hiyo mara 20 katika miaka 23. Mmoja aliheshimiwa alipokufa, ilhali yule mwingine alidharauliwa. Maliki hao wawili walitawala Roma wakati wa maisha na huduma ya Yesu. Walikuwa nani? Na kwa nini mmoja wao akaheshimiwa, hali yule mwingine hakuheshimiwa?
‘ALIKUTA ROMA IKIWA MATUFALI AKAIACHA IKIWA MARUMARU’
Mwaka wa 44 K.W.K., Kaisari Yulio alipouawa, mjukuu wa dada yake, Gayo Octavian alikuwa na umri wa miaka 18 tu. Kwa kuwa alikuwa mwana wa kambo wa Kaisari Yulio na mrithi wake mkuu, Octavian mchanga alifunga safari mara moja kuelekea Roma akadai urithi wake. Huko alikutana na mpinzani mgumu—ofisa mkuu wa Kaisari, Mark Antony, aliyetarajia kuwa mrithi mkuu. Kisha kukawa na mgogoro wa kisiasa na kung’ang’ania mamlaka kwa muda wa miaka 13.
Octavian aliibuka akiwa mtawala wa Milki ya Roma asiyepingwa alipoyashinda majeshi ya muungano ya Malkia Kleopatra wa Misri na mpenzi wake Mark Antony (mwaka wa 31 K.W.K.). Mwaka uliofuata Antony na Kleopatra wakajiua, naye Octavian akatwaa Misri. Kwa hiyo, masalio ya Milki ya Ugiriki yakaondolewa kabisa, na Roma ikawa serikali ya ulimwengu.
Octavian alikuwa mwangalifu asirudie makosa ya Kaisari Yulio kwa kuwa alikumbuka kwamba Yulio aliuawa kwa sababu ya udhalimu wake. Ili asikiuke maoni ya Waroma ya kupendelea jamhuri, aliufanya utawala wake uonekane kana kwamba ulikuwa jamhuri. Alikataa kuitwa “mfalme” na “dikteta.” Isitoshe, alijulisha wazi kwamba alinuia kuipatia Seneti ya Roma mikoa yote iitawale na kwamba alikuwa tayari kujiuzulu kutoka katika wadhifa wake. Mbinu hiyo ilifanikiwa. Seneti yenye uthamini ilimsihi sana Octavian aendelee katika wadhifa wake na aendelee kutawala baadhi ya mikoa.
Tena, Januari 16, 27 K.W.K., Seneti ilimpa Octavian cheo “Augusto,” kinachomaanisha “Aliyekwezwa, Mtakatifu.” Octavian alikubali cheo hicho na pia akauita mwezi mmoja kutokana na jina lake na kuazima siku moja kutoka katika mwezi wa Februari ili mwezi wa Agosti uwe na siku zinazotoshana na zile za mwezi wa Julai, mwezi uliopata jina kutokana na Kaisari Yulio. Octavian akawa maliki wa kwanza wa Roma na baadaye akaja kuitwa Kaisari Augusto, au “Mwadhamu.” Baadaye akaitwa “pontifex maximus” (kuhani wa cheo cha juu), na mwaka wa 2 K.W.K.—mwaka aliozaliwa Yesu—Seneti ikamwita Pater Patriae, “Baba wa Nchi Yake.”
Mwaka huohuo, “agizo kutoka kwa Kaisari Augusto likatoka kwamba dunia yote inayokaliwa ipate kusajiliwa; . . . na watu wote wakaanza kusafiri kwenda kusajiliwa, kila mmoja kwenye jiji lake mwenyewe.” (Luka 2:1-3) Kwa sababu ya agizo hilo, Yesu alizaliwa Bethlehemu kulingana na unabii wa Biblia.—Danieli 11:20; Mika 5:2.
Serikali ya Augusto ilifuatia haki na ilikuwa na uchumi bora. Augusto alitokeza mfumo wa posta wenye matokeo, akajenga barabara na madaraja. Alipanga upya jeshi, akaunda jeshi la majini lenye kudumu, na kikundi cha mashujaa cha walinzi wa maliki walioitwa Walindaji wa Praetori. (Wafilipi 1:13) Chini ya utawala wake waandikaji kama Virgil na Horace walisitawi na wachongaji walichonga vinyago maridadi ambavyo leo huitwa mtindo bora wa kale. Augusto alimalizia kujenga majengo ambayo Kaisari Yulio hakumaliza na akajenga upya mahekalu mengi. Ile Pax Romana (“Amani ya Roma”) aliyoanzisha ilidumu kwa zaidi ya miaka 200. Augusto alikufa Agosti 19, 14 W.K., akiwa na umri wa miaka 76 naye akawa akiabudiwa kama mungu.
Augusto alijisifu kwamba ‘alikuta Roma ikiwa matufali na akaiacha ikiwa marumaru.’ Kwa kuwa hakutaka Roma irejelee siku za awali zilizojaa zogo za jamhuri iliyotangulia, alinuia kumtayarisha maliki ambaye angefuata. Lakini hakuwa na watu wengi wa kuchagua. Mpwa wake wa kiume, wajukuu wake wawili, mwana-mkwe, na mwana mmoja wa kambo, wote hao walikuwa wamekufa, na kumwacha Tiberio aliyekuwa mwana wa kambo peke yake atwae umaliki.
“ASTAHILIYE KUDHARAULIWA”
Haukupita mwezi mmoja baada ya Augusto kufa, Seneti ya Roma ikamteua Tiberio aliyekuwa na umri wa miaka 54 awe maliki. Tiberio aliishi na kutawala hadi Machi 37 W.K. Kwa hiyo, alikuwa maliki wa Roma wakati wa huduma ya Yesu ya hadharani.
Akiwa maliki, Tiberio alikuwa na sifa nzuri na sifa mbaya. Mojawapo ya sifa zake nzuri ni kwamba hakutumia fedha ovyoovyo kwa ajili ya anasa. Kwa sababu hiyo, milki yake ilisitawi naye alikuwa na fedha za kusaidia kukabiliana na misiba na nyakati mbaya. Tiberio alijiona mwenyewe kuwa mwanadamu tu, alikataa vyeo vingi vyenye kuheshimika, na kwa kawaida alielekeza ibada ya maliki kwa Augusto badala yake mwenyewe. Hakuupatia mwezi wa kalenda jina kutokana na jina lake mwenyewe kama vile Augusto na Kaisari Yulio walivyokuwa wamefanya, wala hakuwaruhusu wengine wamheshimu kwa njia hiyo.
Hata hivyo, sifa mbaya za Tiberio zilizidi sifa zake nzuri. Alikuwa mwenye kushuku sana na mwenye unafiki alipokuwa akishughulika na wengine, naye aliagiza watu wengi wauawe alipokuwa akitawala—wengi wa waliokuwa rafiki zake awali waliuawa pia. Aliibadili sheria ya lèse-majesté (uhaini) itie ndani, makufuru dhidi yake mwenyewe, zaidi ya matendo ya uchochezi. Yadhaniwa kwamba Wayahudi walimsonga Gavana Mroma Pontio Pilato aagize Yesu auawe kwa kutegemea nguvu za sheria hiyo.—Yohana 19:12-16.
Tiberio aliweka Walindaji wengi wa Praetori karibu na Roma kwa kujenga kambi zenye ngome kaskazini mwa kuta za jiji hilo. Kuwepo kwa Walindaji hao kuliogofya Seneti ya Roma, iliyokuwa ikitisha mamlaka yake, na pia kulidhibiti maasi yoyote miongoni mwa watu. Tiberio pia alitia moyo mfumo wa kushtakiana, na kipindi cha mwisho cha utawala wake kilikuwa chenye kuogofya.
Kufikia wakati wa kifo chake, Tiberio alionwa kuwa mkandamizaji. Alipokufa, Waroma walishangilia nayo Seneti ikakataa kumfanya awe mungu. Kwa sababu hiyo na nyinginezo, twaona Tiberio alitimiza unabii unaosema kwamba “astahiliye kudharauliwa” angeinuka akiwa “mfalme wa kaskazini.”—Danieli 11:15, 21.
UMEFAHAMU NINI?
• Octavian alipataje kuwa maliki wa kwanza wa Roma?
• Twaweza kusema nini juu ya mafanikio ya Serikali ya Augusto?
• Tiberio alikuwa na sifa gani nzuri na mbaya?
• Tiberio alitimizaje unabii juu ya astahiliye kudharauliwa?
[Picha]
Tiberio
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 252-252]]
ZENOBIA—MALKIA MPIGANAJI WA PALMYRA
“ALIKUWA mweusi-mweusi . . . Meno yake yalikuwa meupe kama lulu, na macho yake makubwa meusi yaling’aa kama moto usio wa kawaida, nayo yalivutia sana. Sauti yake ilikuwa yenye nguvu na tamu. Kujifunza kuliimarisha na kuboresha uelewevu wake wa kiume. Alijua Kilatini, na alijua vizuri Kigiriki, Kiaramu, na lugha za Misri.” Ndivyo mwanahistoria Edward Gibbon alivyomsifu Zenobia—malkia mpiganaji wa Palmyra, jiji la Siria.
Mume wa Zenobia ndiye Odaenathus, kabaila Mpalmyra, aliyetunukiwa wadhifa wa balozi wa Roma mwaka wa 258 W.K. kwa sababu alikuwa amefanikiwa katika vita dhidi ya Uajemi kwa niaba ya Milki ya Roma. Miaka miwili baadaye, Odaenathus alipokea kutoka kwa Maliki Gallienus wa Roma cheo cha corrector totius Orientis (gavana wa Mashariki yote). Hiyo ilikuwa kwa sababu alimshinda Mfalme wa Uajemi, Shāpūr wa Kwanza. Hatimaye Odaenathus akajiita “mfalme wa wafalme.” Huenda kwa kiasi kikubwa Odaenathus alipata ushindi mbalimbali kwa sababu ya ujasiri na busara ya Zenobia.
ZENOBIA ATAMANI KUJENGA MILKI
Mwaka wa 267 W.K., akiwa katika upeo wa ufanisi wake, Odaenathus na mrithi wake waliuawa. Zenobia akatwaa wadhifa wa mume wake kwa kuwa mwana wake alikuwa mchanga sana asiweze kuutwaa. Kwa kuwa alikuwa mrembo, mwenye kutamani makubwa, msimamizi mwenye uwezo, aliyezoea kupiga vita akiwa na mumewe, na mfasaha wa lugha kadhaa, alistahiwa na kuungwa mkono na raia zake. Zenobia alipenda kujifunza naye alishirikiana na watu wengi wenye akili. Mmoja wa washauri wake alikuwa mwanafalsafa na pia mwalimu wa ufasaha wa kusema aitwaye Cassius Longinus—yasemekana alikuwa na ‘ujuzi mwingi.’ Katika kitabu Palmyra and Its Empire—Zenobia’s Revolt Against Rome, mwandikaji Richard Stoneman aandika hivi: “Miaka mitano baada ya Odenathus kufa . . . , Zenobia alikuwa amejiimarisha akilini mwa watu wake kuwa bibi wa Mashariki.”
Uajemi ilikuwa upande mmoja wa milki ya Zenobia, ambayo yeye na mume wake walikuwa wameidhoofisha, nayo Roma iliyokuwa ikianguka ilikuwa upande wa pili. Kuhusu hali katika Milki ya Roma wakati huo, mwanahistoria J. M. Roberts asema hivi: “Karne ya tatu ilikuwa . . . wakati mbaya kwa Roma kwenye mipaka ya mashariki hali kadhalika mipaka ya magharibi, ilhali nyumbani kipindi kipya cha vita vya wenyewe kwa wenyewe na ubishi juu ya waandamizi ulikuwa umeanza. Maliki ishirini na wawili (bila kuhesabu waliojisingizia kuwa maliki) walitawala wakifuatana.” Naye bibi huyo wa Siria, alikuwa mtawala kamili aliyejiimarisha katika milki yake. “Akitawala mabaki ya milki mbili [Uajemi na Roma],” ataarifu Stoneman, “angeweza kutamani kujenga milki ya tatu ambayo ingezitawala zote mbili.”
Zenobia alipata fursa ya kuongeza nguvu zake za kifalme mwaka wa 269 W.K. wakati ambapo mtu aliyejisingizia kuwa mtawala na ambaye alikuwa akipinga utawala wa Roma alitokea huko Misri. Jeshi la Zenobia lilienda Misri upesi, likamwondolea mbali mwasi huyo na kutwaa nchi hiyo. Akijitangaza kuwa malkia wa Misri, alipiga chapa sarafu zenye jina lake mwenyewe. Ufalme wake sasa ulienea tokea mto Naili hadi mto Eufrati. Wakati huo maishani mwake ndipo Zenobia alipopata kuwa “mfalme wa kusini.”—Danieli 11:25, 26.
JIJI KUU LA ZENOBIA
Zenobia aliimarisha na kurembesha jiji lake kuu, Palmyra, kufikia kiwango cha kwamba lilikuwa miongoni mwa majiji makubwa zaidi ya ulimwengu wa Roma. Yakadiriwa kwamba ilikuwa na wakazi 150,000. Majumba makubwa ya umma, mahekalu, mabustani, nguzo, na nguzo za ukumbusho zilijaa Palmyra, jiji lililozingirwa kwa kuta ambazo yasemekana zilikuwa na mzingo wa kilometa 21. Safu ya nguzo za Korintho zenye kimo cha zaidi ya meta 15—zipatazo 1,500—zilikuwa kandokando ya barabara kuu. Sanamu na sanamu za kichwa na mabega za mashujaa na matajiri wafadhili zilijaa jijini. Mwaka wa 271 W.K., Zenobia alisimamisha sanamu yake mwenyewe na ya mume wake aliyekuwa amekufa.
Hekalu la Jua lilikuwa mojawapo ya majengo bora kabisa huko Palmyra na bila shaka wengi waliabudu humo. Huenda Zenobia mwenyewe aliabudu mungu aliyehusianishwa na mungu-jua. Hata hivyo, Siria ya karne ya tatu ilikuwa nchi yenye dini nyingi. Katika milki ya Zenobia kulikuwa na watu waliodai kuwa Wakristo, Wayahudi, na waabudu wa jua na mwezi. Alizionaje aina hizo mbalimbali za ibada? Mwandikaji Stoneman ataarifu hivi: “Mtawala mwenye hekima hatapuuza desturi zozote zionekanazo kuwafaa watu wake. . . . Ilitumainiwa kwamba . . . miungu ilikuwa imepatanishwa iunge mkono Palmyra.” Yaonekana kwamba Zenobia alivumilia dini mbalimbali.
Akiwa na utu mzuri, Zenobia alipendwa na watu wengi. Alitimiza fungu muhimu zaidi katika kuwakilisha utawala wa kisiasa uliotabiriwa katika unabii wa Danieli. Hata hivyo, utawala wake haukudumu zaidi ya miaka mitano. Maliki Mroma, Aurelian alimshinda Zenobia mwaka wa 272 W.K. na baadaye akapora Palmyra lisiweze kurekebishwa tena. Zenobia alihurumiwa. Yasemekana aliolewa na seneta Mroma na huenda akaishi maisha yake yaliyosalia akiwa amestaafu.
UMEFAHAMU NINI?
• Utu wa Zenobia umefafanuliwaje?
• Baadhi ya matendo ya Zenobia ya kijasiri yalikuwa gani?
• Zenobia alizionaje dini?
[Picha]
Malkia Zenobia akiwahutubia askari-jeshi wake
[Chati/Picha katika ukurasa wa 246]
WAFALME KATIKA DANIELI 11:20-26
Mfalme wa Mfalme wa
Kaskazini Kusini
Danieli 11:20 Augusto
Danieli 11:21-24 Tiberio
Danieli 11:25, 26 Aurelian Malkia Zenobia
Kuvunjika Milki ya Milki ya Uingereza,iliyo
kulikotabiriwa Ujerumani fuatwa na Serikali
kwa milki ya Ulimwengu
ya Roma ya Uingereza
kwatokezakwa na Marekani
[Picha]
Tiberio
[Picha]
Aurelian
[Picha]
Sanamu ndogo ya Charlemagne
[Picha]
Augusto
[Picha]
Meli ya vita ya Uingereza ya karne ya 17
[Picha katika ukurasa wa 230]
[Picha katika ukurasa wa 233]
Augusto
[Picha katika ukurasa wa 234]
Tiberio
[Picha katika ukurasa wa 235]
Kwa sababu ya amri ya Augusto, Yosefu na Maria walisafiri kwenda Bethlehemu
[Picha katika ukurasa wa 237]
Kama ilivyotabiriwa, Yesu ‘alivunjwa’ kwenye kifo
[Picha katika ukurasa wa 245]
1. Charlemagne 2. Napoléon wa Kwanza 3. Wilhelm wa Kwanza 4. Askari-jeshi Wajerumani, Vita ya Ulimwengu ya Kwanza
-
-
Wafalme Washindani Waingia Katika Karne ya 20Sikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Sura Ya Kumi Na Tano
Wafalme Washindani Waingia Katika Karne ya 20
1. Mwanahistoria mmoja husema ni nani waliokuwa viongozi wa Ulaya ya karne ya 19?
“ULAYA ya karne ya kumi na tisa ina nguvu fulani ambazo hazikuwa zimepata kuonekana awali,” aandika mwanahistoria Norman Davies. Aongeza kusema hivi: “Ulaya ilikuwa na nguvu nyingi kuliko wakati mwingine wowote: ikiwa na nguvu za kiufundi, nguvu za kiuchumi, nguvu za kitamaduni, na nguvu kuliko mabara mengine.” Viongozi wa “‘karne yenye nguvu’ na ushindi huko Ulaya,” asema Davies, “kwanza kabisa ni Uingereza . . . na makumi ya miaka baadaye, Ujerumani.”
“WATANUIA KUTENDA MADHARA”
2. Karne ya 19 ilipokuwa ikiisha, ni serikali gani zilizokuwa “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini”?
2 Karne ya 19 ilipokaribia kwisha, Milki ya Ujerumani ilikuwa “mfalme wa kaskazini” na Uingereza ilikuwa “mfalme wa kusini.” (Danieli 11:14, 15) “Katika habari za wafalme hao wawili,” akasema malaika wa Yehova, “mioyo yao watanuia kutenda madhara, nao watasema uongo walipo pamoja mezani.” Aendelea kusema: “Lakini hilo halitafanikiwa; maana mwisho utatokea wakati ulioamriwa.”—Danieli 11:27.
3, 4. (a) Ni nani aliyekuwa maliki wa kwanza wa Milki ya Ujerumani, na ni ushirikiano gani ulioundwa? (b) Maliki Wilhelm alifuata sera gani?
3 Januari 18, 1871, Wilhelm wa Kwanza akawa maliki wa kwanza wa Milki ya Ujerumani. Akamweka Otto von Bismarck awe waziri mkuu. Akinuia kuisitawisha hiyo milki mpya, Bismarck aliepuka kupambana na mataifa mengine naye akafanya ushirikiano na Austria-Hungaria na Italia, ulioitwa Shirikisho la Nchi Tatu. Lakini punde si punde masilahi ya mfalme huyo mpya wa kaskazini yakagongana na masilahi ya mfalme wa kusini.
4 Baada ya Wilhelm wa Kwanza na Frederick wa Tatu aliyetawala baada yake kufa mwaka wa 1888, Wilhelm wa Pili mwenye umri wa miaka 29 akaanza kutawala. Wilhelm wa Pili, au Maliki Wilhelm, alimlazimisha Bismarck ajiuzulu naye alitumia sera ya kuzidisha uvutano wa Ujerumani kotekote ulimwenguni. “Chini ya utawala wa Wilhelm wa Pili,” asema mwanahistoria mmoja, “[Ujerumani] ilikuwa yenye kujigamba na yenye uchokozi.”
5. Wafalme hao wawili waliketije “pamoja mezani,” nao walizungumzia nini huko?
5 Zari Nicholas wa Pili wa Urusi alipopanga kuwe na mkutano wa amani huko Hague, Uholanzi, Agosti 24, 1898, kulikuwa na wasiwasi miongoni mwa mataifa. Mkutano huo na mkutano uliofuata mwaka wa 1907 ulianzisha Mahakama Yenye Kudumu ya Mapatano huko Hague. Kuwa washiriki wa mahakama hiyo kulifanya Milki ya Ujerumani na Uingereza zionekane kana kwamba zilipendelea amani. Ziliketi “pamoja mezani,” zikionekana kuwa zenye urafiki, lakini ‘mioyo yao ilinuia kutenda madhara.’ Mbinu ya ‘kusema uwongo walipo pamoja mezani’ haingeweza kuendeleza amani ya kweli. Kuhusu tamaa za kisiasa, kiuchumi, na kijeshi, hakuna chochote ambacho ‘kingefanikiwa’ kwa sababu mwisho wa wafalme hao wawili “utatokea wakati ulioamriwa” na Yehova Mungu.
‘KINYUME CHA AGANO TAKATIFU’
6, 7. (a) Mfalme wa kaskazini alirudije “mpaka nchi yake”? (b) Mfalme wa kusini alitendaje kufuatia uvutano wenye kuongezeka wa mfalme wa kaskazini?
6 Akiendelea, malaika wa Mungu alisema hivi: “Ndipo [mfalme wa kaskazini] atakaporudi mpaka nchi yake mwenye utajiri mwingi; na moyo wake utakuwa kinyume cha hilo agano takatifu; naye atafanya kama apendavyo, na kurudi mpaka nchi yake.”—Danieli 11:28.
7 Maliki Wilhelm alirudi ‘nchini,’ au kwenye hali ya kidunia, ya mfalme wa kale wa kaskazini. Jinsi gani? Kwa kutokeza utawala wa maliki uliokusudiwa kupanua Milki ya Ujerumani na kuzidisha uvutano wake. Wilhelm wa Pili alifuatia miradi ya kuanzisha koloni katika Afrika na kwingineko. Akitaka kushindana na ukuu wa Uingereza baharini, aliunda jeshi lenye nguvu la majini. “Jeshi la majini la Ujerumani lilianza likiwa duni tu na kukua mpaka likawa la pili baada ya Uingereza katika miaka kumi hivi,” chasema kichapo The New Encyclopædia Britannica. Ili kuudumisha ukuu huo, Uingereza ililazimika kupanua jeshi lake la majini. Uingereza ilifanya maelewano na Ufaransa na maelewano kama hayo pamoja na Urusi, hivyo ikifanyiza Maelewano ya Nchi Tatu. Sasa Ulaya ilikuwa imegawanyika na kuwa kambi mbili za kijeshi— Shirikisho la Nchi Tatu upande mmoja na Maelewano ya Nchi Tatu upande wa pili.
8. Milki ya Ujerumani ilipataje “utajiri mwingi”?
8 Milki ya Ujerumani ilifanya mambo kwa hima, ikapata “utajiri mwingi” kwa kuwa Ujerumani ilikuwa sehemu kubwa ya Shirikisho la Nchi Tatu. Austria-Hungaria na Italia zilikuwa nchi za Kikatoliki. Kwa hiyo, lile Shirikisho la Nchi Tatu lilipendelewa na papa, ilhali mfalme wa kusini, na sehemu kubwa ya Maelewano ya Nchi Tatu isiyo ya Kikatoliki, hakupendelewa.
9. Mfalme wa kaskazini alikuwaje ‘kinyume cha agano takatifu’ moyoni?
9 Vipi juu ya watu wa Yehova? Kwa muda mrefu walikuwa wametangaza kwamba “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zingeisha mwaka wa 1914.a (Luka 21:24) Mwaka huo, Ufalme wa Mungu mikononi mwa Mrithi wa Mfalme Daudi, Yesu Kristo, ulianza kutawala mbinguni. (2 Samweli 7:12-16; Luka 22:28, 29) Mapema hata kufikia Machi 1880, gazeti la Watch Tower lilihusisha utawala wa Ufalme wa Mungu na kumalizika kwa “nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa,” au “nyakati za Wasio Wayahudi.” (King James Version) Lakini moyo wa mfalme wa kaskazini wa Ujerumani ulikuwa ‘kinyume cha agano takatifu la ufalme.’ Badala ya kuukiri utawala wa Ufalme, Maliki Wilhelm ‘alifanya apendavyo’ kwa kuendeleza hila za kuutawala ulimwengu. Ingawaje, kwa kufanya hivyo alipanda mbegu za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.
MFALME ‘AVUNJIKA MOYO’ VITANI
10, 11. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilianzaje, na huo ulikuwaje “wakati ulioamriwa”?
10 “Kwa wakati ulioamriwa [mfalme wa kaskazini] atarudi,” malaika akatabiri, “na kuingia upande wa kusini; lakini wakati wa mwisho mambo hayatakuwa kama yalivyokuwa wakati wa kwanza.” (Danieli 11:29) “Wakati ulioamriwa” wa Mungu wa kukomesha utawala wa Wasio Wayahudi duniani ulifika mwaka wa 1914 aliposimamisha Ufalme wa kimbingu. Juni 28 mwaka huo, haramia mmoja Mserbia alimwua Dyuki-Mkuu wa Austria Francis Ferdinand na mke wake huko Sarajevo, Bosnia. Hilo ndilo lililochochea Vita ya Ulimwengu ya Kwanza.
11 Maliki Wilhelm alihimiza Austria-Hungaria zilipize kisasi dhidi ya Serbia. Wakiwa na uhakika kwamba Ujerumani itaiunga mkono, Austria-Hungaria ikatangaza vita dhidi ya Serbia Julai 28, 1914. Lakini Urusi ikasaidia Serbia. Ujerumani ilipotangaza vita dhidi ya Urusi, Ufaransa (mshiriki wa Maelewano ya Nchi Tatu) ikaunga mkono Urusi. Kisha Ujerumani ikatangaza vita dhidi ya Ufaransa. Ili kufanya jiji la Paris lifikike kwa urahisi, Ujerumani ikashambulia Ubelgiji, ambayo ilikuwa imehakikishiwa na Uingereza kwamba haingehusika vitani. Kwa hiyo, Uingereza ikatangaza vita dhidi ya Ujerumani. Mataifa mengine yakahusika, na Italia ikahama toka upande mmoja kwenda wa pili. Wakati wa vita hiyo, Uingereza ikafanya Misri iwe chini ya himaya yake ili kumzuia mfalme wa kaskazini asiuzuie Mfereji wa Suez na kuivamia Misri, nchi ya kale ya mfalme wa kusini.
12. Wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, ni katika maana gani ‘mambo hayakuwa kama yalivyokuwa wakati wa kwanza’?
12 “Licha ya ukubwa na nguvu za Mataifa ya Muungano,” chasema kichapo The World Book Encyclopedia, “yaonekana Ujerumani ilikuwa karibu kushinda vita hiyo.” Katika mapambano ya awali kati ya wafalme hao wawili, Milki ya Roma, ikiwa mfalme wa kaskazini, ilikuwa imeshinda mfululizo. Wakati huu, ‘mambo hayakuwa kama yalivyokuwa wakati wa kwanza.’ Mfalme wa kaskazini alishindwa vitani. Akitoa sababu ya hilo, malaika alisema hivi: “Merikebu za Kitimu zitakuja kupigana naye; basi atavunjika moyo.” (Danieli 11:30a) “Merikebu za Kitimu” zilikuwa nini?
13, 14. (a) “Merikebu za Kitimu” zilizokuja kupigana na mfalme wa kaskazini zilikuwa nini hasa? (b) Merikebu zaidi za Kitimu zilikujaje vita ya ulimwengu ya kwanza ilipokuwa ikiendelea?
13 Wakati wa Danieli, Kitimu ilikuwa Saiprasi. Mapema katika vita ya ulimwengu ya kwanza, Saiprasi ilitekwa na Uingereza. Isitoshe, kulingana na kichapo The Zondervan Pictorial Encyclopedia of the Bible, jina Kitimu “hutia ndani pia M[agharibi] kwa ujumla, lakini hasa M[agharibi] yenye mabaharia.” Tafsiri ya New International Version hutafsiri maneno “merikebu za Kitimu” kuwa “merikebu za pwani za magharibi.” Wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, merikebu za Kitimu zilikuwa meli za Uingereza hasa, iliyokuwa pwani ya magharibi ya Ulaya.
14 Vita ilipoendelea polepole, Jeshi la Majini la Uingereza liliimarishwa na merikebu zaidi za Kitimu. Mei 7, 1915, nyambizi ya Ujerumani iitwayo U-20 ilizamisha merikebu ya raia iitwayo, Lusitania karibu na pwani ya kusini ya Ireland. Waamerika 128 walikuwa miongoni mwa watu waliokufa. Baadaye, Ujerumani ilipigana kwa kutumia nyambizi hadi Atlantiki. Hatimaye, Aprili 6, 1917, Rais Woodrow Wilson wa Marekani akatangaza vita dhidi ya Ujerumani. Akiwa ameongezewa ukuu na manowari na vikosi vya Marekani, mfalme wa kusini—sasa akiwa Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani—alikuwa katika vita kikamili dhidi ya mfalme mpinzani.
15. Mfalme wa kaskazini ‘alivunjika moyo’ lini?
15 Kwa kuwa alishambuliwa na Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, mfalme wa kaskazini ‘akavunjika moyo’ na kushindwa Novemba mwaka wa 1918. Wilhelm wa Pili akakimbilia uhamishoni huko Uholanzi, na Ujerumani ikawa jamhuri. Lakini mfalme wa kaskazini hakuwa ametokomea.
MFALME ATENDA “KADIRI APENDAVYO”
16. Kulingana na unabii, mfalme wa kaskazini alitendaje baada ya kushindwa?
16 “Naye [mfalme wa kaskazini] atarudi na kulighadhibikia hilo agano takatifu; na kutenda kadiri apendavyo; naam, atarudi, na kuwasikiliza walioacha hilo agano takatifu.” (Danieli 11:30b) Ndivyo alivyotabiri malaika, na ndivyo ilivyotimia.
17. Ni nini kilichoongoza kwenye kutokea kwa Adolf Hitler?
17 Baada ya vita kwisha mwaka wa 1918, Mataifa ya Muungano walioshinda waliwekea Ujerumani mkataba wa amani wa kumwadhibu. Wajerumani waliyaona masharti ya mkataba huo kuwa makali, nayo ile jamhuri mpya ilikuwa dhaifu tokea mwanzo. Ujerumani ilijikokota kwa miaka kadhaa ikiwa na taabu nyingi na ikapatwa na ule Mshuko Mkuu wa Kiuchumi ambao ulisababisha watu milioni sita wapoteze kazi zao. Mapema katika miaka ya 1930, wakati barabara wa kutokea kwa Adolf Hitler ulikuwa umetimia. Akawa waziri mkuu Januari 1933 na mwaka uliofuata akawa rais wa milki ambayo Wanazi waliita Milki ya Tatu.b
18. Hitler ‘alitendaje kadiri alivyopenda’?
18 Punde baada ya kupata mamlaka, Hitler alianzisha shambulio kali dhidi ya “agano takatifu,” lililowakilishwa na ndugu watiwa-mafuta wa Yesu Kristo. (Mathayo 25:40) Katika hilo alitenda “kadiri apendavyo” dhidi ya Wakristo hao wenye uaminifu-mshikamanifu, akiwanyanyasa wengi wao kikatili. Hitler alifanikiwa kiuchumi na kidiplomasia, akitenda “kadiri apendavyo” pia katika nyanja hizo. Baada ya miaka michache aliifanya Ujerumani kuwa serikali kubwa ulimwenguni.
19. Hitler alijiunga na nani akitafuta kuungwa mkono?
19 Hitler ‘aliwasikiliza walioacha hilo agano takatifu.’ Hao walikuwa nani? Yaonekana ni viongozi wa Jumuiya ya Wakristo, waliodai kuwa na uhusiano wa kiagano pamoja na Mungu lakini wakakoma kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Hitler alifanikiwa kuungwa mkono na “walioacha hilo agano takatifu.” Kwa kielelezo, alifanya mkataba na papa wa Roma. Mwaka wa 1935, Hitler alianzisha Wizara ya Mambo ya Kanisa. Mojawapo ya miradi yake ilikuwa kufanya makanisa ya Kievanjeli yawe chini ya serikali.
“WENYE SILAHA” WASIMAMA UPANDE WA MFALME
20. Ni “wenye silaha” gani ambao mfalme wa kaskazini alitumia, naye aliwatumia dhidi ya nani?
20 Upesi Hitler akaingia vitani, kama vile malaika alivyotabiri kwa usahihi: “Wenye silaha watasimama upande wake, nao watapatia unajisi mahali patakatifu, ndiyo ngome, nao wataondoa sadaka ya kuteketezwa ya kila siku.” (Danieli 11:31a) “Wenye silaha” walikuwa majeshi ya mfalme wa kaskazini yaliyotumiwa kupigana na mfalme wa kusini katika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Septemba 1, 1939, “wenye silaha” wa Nazi walivamia Poland. Siku mbili baadaye, Uingereza na Ufaransa zikatangaza vita dhidi ya Ujerumani ili kuisaidia Poland. Ndivyo Vita ya Ulimwengu ya Pili ilivyoanza. Poland ilishindwa haraka, na punde baadaye majeshi ya Ujerumani yakamiliki Denmark, Norway, Uholanzi, Ubelgiji, Luxembourg, na Ufaransa. “Mwishoni mwa mwaka wa 1941,” chasema kichapo The World Book Encyclopedia, “Ujerumani ya Nazi ilitawala bara hilo.”
21. Mambo yalimgeukaje mfalme wa kaskazini wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, na matokeo yakawa nini?
21 Ingawa Ujerumani na Muungano wa Sovieti ulikuwa umefanya Mkataba wa Urafiki, Ushirikiano, na Kutovuka Mipaka, Hitler alivamia eneo la Sovieti Juni 22, 1941. Tendo hilo lilifanya Muungano wa Sovieti ujiunge na Uingereza. Jeshi la Sovieti lilipigana vikali licha ya kuwa awali majeshi ya Ujerumani yalikuwa yamesonga mbele sana. Desemba 6, 1941, jeshi la Ujerumani lilishindwa huko Moscow. Siku iliyofuata, Japani iliyokuwa ikiunga mkono Ujerumani ikalipua kombora katika Bandari ya Pearl, Hawaii. Alipopata kujua juu ya hilo, Hitler akawaambia wasaidizi wake hivi: “Sasa hatuwezi kushindwa katika vita hii.” Desemba 11 alitangaza vita dhidi ya Marekani haraka-haraka bila kufikiri. Lakini alidharau nguvu za Muungano wa Sovieti na Marekani. Jeshi la Sovieti likishambulia upande wa mashariki, na Uingereza na Marekani zikishambulia upande wa magharibi, punde si punde mambo yakamgeuka Hitler. Majeshi ya Ujerumani yalipoteza eneo moja baada ya jingine. Baada ya Hitler kujiua, Ujerumani ikajisalimisha kwa hayo Mataifa ya Muungano, Mei 7, 1945.
22. Mfalme wa kaskazini ‘alinajisije mahali patakatifu na kuondoa sadaka ya kuteketezwa ya kila siku’?
22 Wenye silaha wa Nazi “watapatia unajisi mahali patakatifu, ndiyo ngome, nao wataondoa sadaka ya kuteketezwa ya kila siku,” akasema malaika. Katika Yuda la kale mahali patakatifu palikuwa sehemu ya hekalu katika Yerusalemu. Hata hivyo, Wayahudi walipomkataa Yesu, Yehova aliwakataa pamoja na hekalu lao. (Mathayo 23:37–24:2) Tangu karne ya kwanza W.K., hekalu la Yehova limekuwa la kiroho, patakatifu pa patakatifu pakiwa mbinguni na ua wa kiroho ukiwa duniani, ambamo ndugu watiwa-mafuta wa Yesu, Kuhani wa Cheo cha Juu, hutumikia. Tangu miaka ya 1930 na kuendelea, “umati mkubwa” umeabudu ukishirikiana na mabaki ya watiwa-mafuta na kwa hiyo wanasemwa kwamba wanatumikia ‘katika hekalu la Mungu.’ (Ufunuo 7:9, 15; 11:1, 2; Waebrania 9:11, 12, 24) Katika nchi zilizo chini yake, mfalme wa kaskazini alinajisi ua wa kidunia wa hekalu kwa kuwanyanyasa bila huruma mabaki watiwa-mafuta na waandamani wao. Aliwanyanyasa vikali sana hivi kwamba “sadaka ya kuteketezwa ya kila siku”—dhabihu ya hadharani ya sifa kwa jina la Yehova—iliondolewa. (Waebrania 13:15) Hata hivyo, licha ya kuteseka vibaya, Wakristo watiwa-mafuta waaminifu pamoja na “kondoo wengine” waliendelea kuhubiri wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili.—Yohana 10:16.
‘CHUKIZO LASIMAMISHWA’
23. “Chukizo” lilikuwa nini katika karne ya kwanza?
23 Mwisho wa vita ya ulimwengu ya pili ulipokaribia, jambo jingine lilitukia, kama vile malaika wa Mungu alivyokuwa ametabiri. “Nao watalisimamisha chukizo la uharibifu.” (Danieli 11:31b) Yesu pia alikuwa amesema juu ya “chukizo.” Katika karne ya kwanza, lilikuwa jeshi la Roma ambalo lilikuja Yerusalemu mwaka wa 66 W.K. ili kukomesha uasi wa Wayahudi.c—Mathayo 24:15; Danieli 9:27.
24, 25. (a) “Chukizo” ni nini leo? (b) ‘Chukizo lilisimamishwa’ lini na jinsi gani?
24 Ni “chukizo” gani “limesimamishwa” leo? Yaonekana ni mwigizo ‘wenye kuchukiza’ wa Ufalme wa Mungu. Hilo lilikuwa Ushirika wa Mataifa, yule hayawani-mwitu mwenye rangi nyekundu-nyangavu aliyeingia abiso, au aliyekoma kuwepo akiwa shirika la amani ya ulimwengu, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipozuka. (Ufunuo 17:8) Hata hivyo, “hayawani-mwitu” huyo alipaswa “kupanda kutoka katika abiso.” Alipanda wakati ambapo Umoja wa Mataifa, ukiwa na mataifa washiriki 50 kutia ndani na uliokuwa Muungano wa Sovieti, ulianzishwa Oktoba 24, 1945. Kwa hiyo, “chukizo” lililotabiriwa na malaika—Umoja wa Mataifa—likasimamishwa.
25 Ujerumani ilikuwa adui mkubwa wa mfalme wa kusini katika vita vyote viwili vya ulimwengu nayo ilikuwa mfalme wa kaskazini. Ni nani ambaye angekuwa mfalme wa kaskazini baada yake?
-
-
Wafalme Washindani Waingia Katika Karne ya 20Sikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
[Chati/Picha katika ukurasa wa 268]
WAFALME KATIKA DANIELI 11:27-31
Mfalme wa Mfalme wa
Kaskazini Kusini
Danieli 11:27-30a Milki ya Ujerumani Uingereza, kisha
(Vita ya Ulimwengu Serikali ya Ulimwengu ya
ya Kwanza) Uingereza na Marekani
Danieli 11:30b, 31 Milki ya Tatu ya Hitler Serikali ya Ulimwengu
(Vita ya Ulimwengu ya Uingereza na
ya Pili) Marekani
[Picha]
Rais Woodrow Wilson pamoja na Mfalme George wa Tano
[[Picha]
Wakristo wengi walinyanyaswa kwenye kambi za mateso
[Picha]
Viongozi wa Jumuiya ya Wakristo walimuunga mkono Hitler
[Picha]
Gari ambamo Dyuki-Mkuu Ferdinand aliuawa
[Picha]
Wanajeshi wa Ujerumani, Vita ya Ulimwengu ya Kwanza
[Picha katika ukurasa wa 257]
Huko Yalta mwaka wa 1945, Waziri Mkuu wa Uingereza Winston Churchill, Rais Franklin D. Roosevelt wa Marekani, na Waziri Mkuu wa Sovieti Joseph Stalin walikubaliana juu ya mipango ya kumiliki Ujerumani, kuunda serikali mpya huko Poland, na kufanya mkutano wa kuanzisha Umoja wa Mataifa
[Picha katika ukurasa wa 258]
1. Dyuki-Mkuu Ferdinand 2. Jeshi la majini la Ujerumani 3. Jeshi la majini la Uingereza 4. Lusitania 5. Tangazo la Vita la Marekani
[Picha katika ukurasa wa 263]
Adolf Hitler alikuwa na uhakika wa kushinda vita baada ya Japani iliyounga mkono Ujerumani wakati wa vita, kulipua Bandari ya Pearl kwa makombora
-
-
Wafalme Washindani Wakaribia Mwisho WaoSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
Sura Ya Kumi Na Sita
Wafalme Washindani Wakaribia Mwisho Wao
1, 2. Mfalme wa kaskazini alibadilika akawa nani baada ya vita ya ulimwengu ya pili?
AKIZUNGUMZIA hali ya kisiasa ya Marekani na Urusi, mwanafalsafa Mfaransa aliye pia mwanahistoria Alexis de Tocqueville aliandika hivi mwaka wa 1835: “Mmoja ana uhuru akiwa njia kuu ya utendaji; yule mwingine ana utumwa. . . . Njia zao [ni] tofauti; hata hivyo, kila mmoja aonekana kuwa amepata mwito fulani wa siri wa Mungu wa kuongoza nusu ya ulimwengu siku moja.” Utabiri huo ulikuwa sahihi kadiri gani baada tu ya Vita ya Ulimwengu ya Pili? Mwanahistoria J. M. Roberts aandika hivi: “Mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya pili, ilionekana kana kwamba ulimwengu ungetawalwa na serikali mbili kubwa zenye mifumo tofauti kabisa ya kutawala, mmoja ukitegemea iliyokuwa Urusi, mwingine ukiwa Marekani.”
2 Wakati wa zile vita mbili za ulimwengu, Ujerumani ilikuwa adui mkuu wa mfalme wa kusini—Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani—nayo ilikuwa mfalme wa kaskazini. Hata hivyo, baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, taifa hilo liligawanyika. Ujerumani Magharibi ikajiunga na mfalme wa kusini, nayo Ujerumani Mashariki ikajiunga na serikali nyingine yenye nguvu—mataifa ya Kikomunisti yakiongozwa na Muungano wa Sovieti. Mataifa hayo, au utawala wa kisiasa, yakawa mfalme wa kaskazini, yakipingana vikali na Muungano wa Uingereza na Marekani. Nao ushindani kati ya wafalme hao wawili ukawa Vita Baridi, vita iliyodumu tangu 1948 hadi 1989. Awali, mfalme wa kaskazini wa Ujerumani alikuwa ‘kinyume cha agano takatifu.’ (Danieli 11:28, 30) Mataifa ya Kikomunisti yangetendaje kuhusiana na agano hilo?
WAKRISTO WA KWELI WAANGUKA LAKINI WAWA HODARI
3, 4. Ni nani “wafanyao maovu juu ya hilo agano,” nao wamekuwa na uhusiano gani na mfalme wa kaskazini?
3 “Na wao wafanyao maovu juu ya hilo agano,” akasema malaika wa Mungu, mfalme wa kaskazini “atawapotosha kwa maneno ya kujipendekeza.” Kisha malaika akasema hivi: “Lakini watu wamjuao Mungu wao watakuwa hodari, na kutenda mambo makuu. Na hao walio wenye hekima katika watu watafundisha wengi; hata hivyo wataanguka kwa upanga, na kwa moto, na kwa kufungwa, na kwa kutekwa nyara, siku nyingi.”—Danieli 11:32, 33.
4 Wale “wafanyao maovu juu ya hilo agano” waweza tu kuwa viongozi wa Jumuiya ya Wakristo, wanaodai kuwa Wakristo lakini kulingana na matendo yao wanalichafua jina lenyewe la Ukristo. Katika kitabu chake Religion in the Soviet Union, Walter Kolarz asema hivi: “[Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili] Serikali ya Sovieti ilijitahidi kuungwa mkono kihalisi na kiadili na Makanisa ili kulinda nchi yao.” Baada ya vita hiyo viongozi wa kanisa walijaribu kudumisha urafiki, ijapokuwa serikali ya mfalme wa kaskazini ilikuwa na sera za kutoamini kuwapo kwa Mungu. Kwa hiyo, Jumuiya ya Wakristo ikawa sehemu ya ulimwengu huu kuliko wakati mwingine wowote—uasi imani wenye kuchukiza machoni pa Yehova.—Yohana 17:16; Yakobo 4:4.
5, 6. “Watu wamjuao Mungu wao” walikuwa nani, na walipatwa na hali gani chini ya mfalme wa kaskazini?
5 Vipi juu ya Wakristo wa kweli—“watu wamjuao Mungu wao” na “wenye hekima”? Ingawa walikuwa “katika ujitiisho kwa mamlaka zilizo kubwa” ifaavyo, Wakristo walioishi chini ya utawala wa mfalme wa kaskazini hawakuwa sehemu ya ulimwengu. (Waroma 13:1; Yohana 18:36) Walikuwa waangalifu kumlipa “Kaisari vitu vya Kaisari,” na kumlimpa “Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Kwa sababu hiyo, uaminifu-maadili wao ulijaribiwa.—2 Timotheo 3:12.
6 Kwa sababu hiyo, Wakristo wa kweli ‘walianguka’ na ‘wakawa hodari.’ Walianguka katika maana ya kwamba walinyanyaswa vikali, hata wengine wakauawa. Lakini walikuwa hodari katika maana ya kwamba walio wengi waliendelea kuwa waaminifu. Waliushinda ulimwengu, kama alivyofanya Yesu. (Yohana 16:33) Isitoshe, hawakuacha kuhubiri, hata ikiwa walifungwa gerezani au kwenye kambi za mateso. Kwa kufanya hivyo, ‘waliwafundisha wengi.’ Licha ya mnyanyaso katika nchi nyingi zilizotawalwa na mfalme wa kaskazini, idadi ya Mashahidi wa Yehova iliongezeka. Kwa sababu ya uaminifu wa “wenye hekima,” “umati mkubwa” unaoongezeka daima umetokea katika nchi hizo.—Ufunuo 7:9-14.
WATU WA YEHOVA WATAKASWA
7. Ni “msaada kidogo” gani ambao Wakristo watiwa-mafuta waliokuwa wakiishi chini ya mfalme wa kaskazini walipokea?
7 Watu wa Mungu “watakapoanguka, watasaidiwa kwa msaada kidogo,” akasema malaika. (Danieli 11:34a) Ushindi wa mfalme wa kusini katika vita ya ulimwengu ya pili ulitokeza utulivu kidogo kwa Wakristo waliokuwa chini ya mfalme wa kaskazini. (Linganisha Ufunuo 12:15, 16.) Hali kadhalika, walionyanyaswa na mfalme aliyetawala baadaye, walipata utulivu pindi kwa pindi. Ile Vita Baridi ilipokuwa ikipungua, viongozi wengi walipata kutambua kwamba Wakristo waaminifu hawakuwa tisho lolote na hivyo wakawapa kibali cha kisheria. Pia, msaada ulitokana na idadi kubwa yenye kuongezeka ya umati mkubwa, walioitikia kuhubiri kwa uaminifu kulikofanywa na watiwa-mafuta na kuwasaidia.—Mathayo 25:34-40.
8. Watu fulani waliambatanaje na watu wa Mungu “kwa maneno ya kujipendekeza”?
8 Baadhi ya wale waliodai kwamba wanapenda kumtumikia Mungu wakati wa ile Vita Baridi hawakuwa na makusudi mazuri. Malaika alikuwa ameonya hivi: “Lakini wengi wataambatana nao kwa maneno ya kujipendekeza.” (Danieli 11:34b) Wengi walipendezwa na kweli lakini hawakutaka kujiweka wakfu kwa Mungu. Lakini wengine ambao walionekana kana kwamba waliikubali kweli, kwa kweli walikuwa wapelelezi wa wenye mamlaka. Ripoti moja kutoka nchi moja yataarifu hivi: “Baadhi ya watu hao wasio wanyoofu walikuwa Wakomunisti sugu na walikuwa wamepenya ndani ya tengenezo la Bwana, wakajionyesha kuwa na bidii nyingi, na hata walikuwa wamewekwa katika vyeo vya juu vya utumishi.”
9. Kwa nini Yehova aliruhusu baadhi ya Wakristo waaminifu ‘waanguke’ kwa sababu ya watu waliopenya ndani ya tengenezo lake?
9 Malaika huyo aliendelea kusema hivi: “Na baadhi yao wenye hekima wataanguka, ili kuwatakasa, na kuwasafisha, na kuwafanya weupe, hata wakati wa mwisho; kwa maana ni kwa wakati ulioamriwa, ambao haujaja.” (Danieli 11:35) Watu hao waliokuwa wamepenya ndani walisababisha waaminifu waanguke mikononi mwa wenye mamlaka. Yehova aliruhusu mambo hayo yatukie ili watu wake watakaswe na kusafishwa. Kama vile Yesu “ali[vyo]jifunza utii kutokana na mambo aliyoteseka,” ndivyo waaminifu hao wamejifunza uvumilivu kwa sababu imani yao imejaribiwa. (Waebrania 5:8; Yakobo 1:2, 3; linganisha Malaki 3:3.) Kwa hiyo, ‘wanatakaswa, kusafishwa, na kufanywa weupe.’
10. Ni nini kinachomaanishwa na maneno “hata wakati wa mwisho”?
10 Watu wa Yehova wangeanguka na kutakaswa “hata wakati wa mwisho.” Bila shaka, wanatarajia kunyanyaswa hadi mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. Hata hivyo, uvamizi wa mfalme wa kaskazini unaosababisha watu wa mungu kusafishwa na kufanywa weupe ni “kwa wakati ulioamriwa.” Kwa hiyo, kwenye Danieli 11:35, “wakati wa mwisho” lazima uwe mwisho wa kipindi cha wakati kinachohitajiwa ili watu wa Mungu watakaswe huku wakivumilia mashambulio ya mfalme wa kaskazini. Yaonekana kule kuanguka kuliisha kwenye wakati ulioamriwa na Yehova mwenyewe.
MFALME AJITUKUZA
11. Malaika alisema nini juu ya mtazamo wa mfalme wa kaskazini kuelekea enzi kuu ya Yehova?
11 Kuhusu mfalme wa kaskazini, malaika aliongeza kusema hivi: “Mfalme atafanya kama apendavyo; naye atajitukuza na kujiadhimisha juu ya kila mungu, naye [akikataa kukiri enzi kuu ya Yehova] atanena maneno ya ajabu juu ya Mungu wa miungu, naye atafanikiwa mpaka ghadhabu itakapotimia; maana yaliyokusudiwa yatafanyika. Wala hataijali miungu ya baba zake; wala yeye aliyetamaniwa na wanawake; wala hatamjali mungu awaye yote; maana atajitukuza mwenyewe juu ya wote.”—Danieli 11:36, 37.
12, 13. (a) Mfalme wa kaskazini alikataaje “miungu ya baba zake”? (b) “Wanawake” ambao mfalme wa kaskazini hakuijali ‘tamaa’ yao walikuwa nani? (c) Mfalme wa kaskazini alimtukuza “mungu” gani?
12 Akitimiza maneno hayo ya kiunabii, mfalme wa kaskazini alikataa “miungu ya baba zake,” kama vile mungu wa Utatu wa Jumuiya ya Wakristo. Mataifa ya Kikomunisti yaliendeleza moja kwa moja fundisho la kukataa kuwapo kwa Mungu. Kwa hiyo, mfalme wa kaskazini alijifanya kuwa mungu, ‘akijiadhimisha juu ya kila mungu.’ Bila kujali “aliyetamaniwa na wanawake”—nchi zilizo chini yake, kama vile Vietnam Kaskazini, ambazo zilikuwa kama vijakazi vya utawala wake—mfalme alitenda “kama apendavyo.”
13 Akiendelea na unabii huo, malaika alisema hivi: “Katika mahali pake atamheshimu mungu wa ngome; na mungu ambaye baba zake hawakumjua atamheshimu, kwa dhahabu, na fedha, na vito vya thamani, na vitu vipendezavyo.” (Danieli 11:38) Kwa hakika, mfalme wa kaskazini alitumaini silaha za kivita za kisayansi za kisasa, “mungu wa ngome.” Alitafuta wokovu kupitia “mungu” huyo, akitoa mali nyingi kwenye madhabahu yake.
14. Mfalme wa kaskazini ‘alitendaje kwa matokeo’?
14 “Ataziteka nyara [“Atatenda kwa matokeo dhidi ya,” NW] ngome zenye nguvu kwa msaada wa mungu mgeni; na yeye atakayemkubali atamwongeza kwa utukufu; naye atawapa kumiliki wengi; naye ataigawa nchi kwa rushwa.” (Danieli 11:39) Akimtegemea “mungu [wake] mgeni” wa kijeshi, mfalme wa kaskazini “alitenda kwa matokeo,” akijithibitisha kuwa serikali ya kijeshi yenye nguvu sana katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Waliounga mkono dhana zake walitegemezwa kisiasa, kiuchumi, na nyakati nyingine kijeshi.
‘MSUKUMO’ WAKATI WA MWISHO
15. Mfalme wa kusini ‘alimsukumaje’ mfalme wa kaskazini?
15 “Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atashindana naye [“atamsukuma,” NW],” malaika akamwambia Danieli. (Danieli 11:40a) Je, mfalme wa kusini ‘amemsukuma’ mfalme wa kaskazini katika “wakati wa mwisho”? (Danieli 12:4, 9) Ndiyo, bila shaka. Baada ya vita ya ulimwengu ya kwanza, ule mkataba wa amani wa kumwadhibu mfalme wa kaskazini—Ujerumani—kwa kweli ‘ulimsukuma,’ ukimchochea alipize kisasi. Baada ya ushindi wake katika vita ya ulimwengu ya pili, mfalme wa kusini alimlenga mpinzani wake kwa makombora ya nyuklia yenye kuhofisha na kupanga muungano wa kijeshi wenye nguvu dhidi yake, Shirika la Kujihami la North Atlantic Treaty Organization (NATO). Kuhusu utendaji wa NATO, mwanahistoria mmoja Mwingereza asema hivi: “Ndicho kilichokuwa chombo kikuu cha ‘kuudhibiti’ [Muungano wa Sovieti], ambao sasa ulionwa kuwa tisho kuu la amani ya Ulaya. Lengo lake lilidumu kwa miaka 40, nalo lilitimizwa kwa mafanikio sana.” Miaka ya Vita Baridi ilipoendelea, kule ‘kusukumwa’ na mfalme wa kusini kulitia ndani upelelezi wa hali ya juu na vilevile mashambulio ya kidiplomasia na ya kijeshi.
16. Mfalme wa kaskazini alitendaje aliposukumwa na mfalme wa kusini?
16 Mfalme wa kaskazini alitendaje? “Na mfalme wa kaskazini atamshambulia kama upepo wa kisulisuli, pamoja na magari ya vita, na wapanda farasi, na merikebu nyingi; naye ataingia katika nchi hizo, na kufurika na kupita katikati.” (Danieli 11:40b) Historia ya siku za mwisho imeonyesha upanuzi wa mfalme wa kaskazini. Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili “mfalme” wa Nazi alipanua mipaka yake na kuingia katika nchi jirani. Mwishoni mwa vita hiyo, “mfalme” aliyetawala baada yake alijenga milki yenye nguvu. Wakati wa ile Vita Baridi, mfalme wa kaskazini alipigana na mpinzani wake kwa kutegemeza pande tofauti katika vita na maasi katika Afrika, Amerika ya Latini, na Asia. Aliwanyanyasa Wakristo wa kweli, akizuia—wala si kusimamisha kamwe—utendaji wao. Nayo mashambulio yake ya kijeshi na ya kisiasa yalimwezesha kuongoza nchi nyingi. Hilo ndilo hasa jambo ambalo malaika alikuwa ametabiri: “Tena ataingia katika hiyo nchi ya uzuri [makazi ya kiroho ya watu wa Yehova], na nchi nyingi zitapinduliwa.”—Danieli 11:41a.
17. Ni nini kilichozuia upanuzi wa mfalme wa kaskazini?
17 Hata hivyo, mfalme wa kaskazini hakuushinda ulimwengu wote. Malaika alitabiri hivi: “Lakini nchi hizi zitaokolewa na mkono wake, Edomu, na Moabu, na wakuu wa watu wa Amoni.” (Danieli 11:41b) Nyakati za kale, Edomu, Moabu, na Amoni zilikuwa katikati ya milki ya mfalme wa kusini wa Misri na milki ya mfalme wa kaskazini wa Siria. Leo zawakilisha mataifa na mashirika ambayo mfalme wa kaskazini alilenga lakini akashindwa kuyadhibiti.
MISRI HAIOKOKI
18, 19. Mfalme wa kusini alihisije uvutano wa mpinzani wake?
18 Malaika wa Yehova aendelea kusema hivi: “Naye [mfalme wa kaskazini] ataunyosha mkono wake juu ya nchi hizo, hata na nchi ya Misri haitaokoka. Lakini atakuwa na nguvu juu ya hazina za dhahabu na fedha, na juu ya vitu vyote vya Misri vyenye thamani; na Walibia na Wakushi watafuata nyayo zake.” (Danieli 11:42, 43) Hata mfalme wa kusini, “Misri,” hakuokoka matokeo ya sera za upanuzi za mfalme wa kaskazini. Kwa kielelezo, mfalme wa kusini alishindwa vibaya huko Vietnam. Vipi juu ya “Walibia na Wakushi”? Huenda kwa kufaa majirani hao wa Misri ya kale wakawakilisha mataifa ambayo ni majirani wa “Misri” ya leo (mfalme wa kusini). Nyakati nyingine, yamekuwa ‘yakifuata nyayo za’ mfalme wa kaskazini.
19 Je, mfalme wa kaskazini amepata kutawala ‘hazina za Misri’? Kwa kweli, amekuwa na uvutano wenye nguvu juu ya jinsi mfalme wa kusini ametumia mali zake. Kwa sababu ya kumhofu mpinzani wake, mfalme wa kusini ametumia kiasi kikubwa cha fedha ili kudumisha jeshi la nchi kavu, la majini, na la angani lenye nguvu sana. Kwa hiyo, mfalme wa kaskazini ‘amekuwa na nguvu juu ya,’ au amedhibiti, matumizi ya mali za mfalme wa kusini.
VITA YA MWISHO
20. Malaika afafanuaje vita ya mwisho ya mfalme wa kaskazini?
20 Ushindani kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini—uwe wa kijeshi, kiuchumi, au mwingineo wowote—wakaribia kwisha. Akifunua kinaganaga juu ya pambano lililo mbele, malaika wa Yehova asema hivi: “Habari zitokazo mashariki [“macheo ya jua,” NW] na kaskazini zitamfadhaisha [mfalme wa kaskazini]; naye atatoka kwa ghadhabu nyingi, ili kuharibu, na kuwaondolea mbali watu wengi. Naye ataweka hema zake za kifalme kati ya bahari na mlima mtakatifu wa uzuri; lakini ataifikilia ajali yake [“atakuwa amefikia kikomo chake,” BHN], wala hakuna atakayemsaidia.”—Danieli 11:44, 45.
21. Kuna mambo gani bado ya kujifunza juu ya mfalme wa kaskazini?
21 Muungano wa Sovieti ulipovunjika Desemba 1991, mfalme wa kaskazini alipatwa na madhara makubwa. Ni nani atakayekuwa mfalme huyo wakati ambapo Danieli 11:44, 45 litakapotimizwa? Je, atakuwa mojawapo ya nchi zilizokuwa Muungano wa Sovieti? Au atabadilika kabisa, kama vile ambavyo amefanya mara kadhaa? Je, kutengenezwa kwa silaha za nyuklia kunakofanywa na mataifa mengine katika shindano jingine la silaha kutabadili utambulisho wa mfalme huyo? Wakati tu ndio utakaotoa majibu ya maswali hayo. Ni jambo la hekima kwamba tusikisie-kisie. Mfalme wa kaskazini arudiapo vita yake ya mwisho, wale wote wenye ufahamu wa kina unaotegemea Biblia watauona utimizo wa unabii huo waziwazi.—Ona “Wafalme Katika Danieli Sura ya 11,” kwenye ukurasa wa 284.
22. Ni maswali gani yanayozuka juu ya shambulio la mwisho la mfalme wa kaskazini?
22 Hata hivyo, twajua hatua ambayo mfalme wa kaskazini atachukua hivi karibuni. Akichochewa na ‘habari zitokazo macheo ya jua na kaskazini,’ atapanga vita ili “kuwaondolea mbali watu wengi.” Vita hiyo itapiganwa dhidi ya nani? Nazo ni “habari” gani zinazochochea shambulio hilo?
ASHTUSHWA NA HABARI ZENYE KUSUMBUA
23. (a) Ni tukio gani lenye kutokeza ambalo lazima litukie kabla ya Har–Magedoni? (b) “Wafalme watokao macheo ya jua” ni akina nani?
23 Fikiria jambo ambalo kitabu cha Ufunuo chasema juu ya mwisho wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. Kabla ya “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” Har–Magedoni, adui huyo mkubwa wa ibada ya kweli “atachomwa kabisa kwa moto.” (Ufunuo 16:14, 16; 18:2-8) Kuharibiwa kwake kuliwakilishwa na kumwagwa kwa bakuli la sita la hasira ya kisasi ya Mungu kwenye mto wa ufananisho wa Eufrati. Mto huo wakauka ili “njia ipate kutayarishwa kwa ajili ya wafalme watokao macheo ya jua.” (Ufunuo 16:12) Wafalme hao ni nani? Si wengine ila Yehova Mungu na Yesu Kristo!—Linganisha Isaya 41:2; 46:10, 11.
24. Ni tendo gani la Yehova ambalo huenda likamsumbua mfalme wa kaskazini?
24 Kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa kwafafanuliwa kinaganaga kwenye kitabu cha Ufunuo, kinachotaarifu hivi: “Pembe kumi ulizoziona [wafalme wanaotawala katika wakati wa mwisho], na hayawani-mwitu [Umoja wa Mataifa], hawa watamchukia kahaba na watamfanya ukiwa na kuwa uchi, na watakula kabisa sehemu zake zenye nyama na watamchoma kabisa kwa moto.” (Ufunuo 17:16) Kwa nini wafalme watamharibu Babiloni Mkubwa? Kwa sababu ‘Mungu atia ndani ya mioyo yao ili watekeleze fikira yake.’ (Ufunuo 17:17) Mfalme wa kaskazini ni mmoja wa watawala hao. Huenda habari asikiazo kutoka “macheo ya jua” zarejezea tendo hilo la Yehova, atiapo ndani ya mioyo ya viongozi wa kibinadamu fikira ya kumwangamiza kahaba huyo mkubwa wa kidini.
25. (a) Lengo la pekee la mfalme wa kaskazini ni nini? (b) Mfalme wa kaskazini “ataweka hema zake za kifalme” wapi?
25 Lakini mfalme wa kaskazini ataelekeza hasira yake yenye kisasi mahali fulani pa pekee. “Ataweka hema zake za kifalme kati ya bahari [“bahari kuu,” NW] na mlima mtakatifu wa uzuri,” asema malaika. Wakati wa Danieli bahari kuu ilikuwa Meditarenia nao mlima mtakatifu ulikuwa Zayoni, ambapo hekalu la Mungu lilikuwa wakati mmoja. Kwa hiyo, katika utimizo wa unabii huo, mfalme wa kaskazini aliyekasirishwa apanga vita dhidi ya watu wa Mungu. Katika maana ya kiroho, mahali palipo ‘kati ya bahari kuu na mlima mtakatifu’ pawakilisha makazi ya kiroho ya watumishi wa Yehova watiwa-mafuta. Wametoka kwenye “bahari” ya wanadamu waliotengwa na Mungu nao wana tumaini la kutawala kwenye Mlima Zayoni wa kimbingu pamoja na Yesu Kristo.—Isaya 57:20; Waebrania 12:22; Ufunuo 14:1.
26. Kama inavyoonyeshwa na unabii wa Ezekieli, huenda habari ‘itokayo kaskazini’ yatokana na nani?
26 Ezekieli, aliyeishi wakati mmoja na Danieli, alitabiri pia juu ya shambulio dhidi ya watu wa Mungu “katika siku za mwisho.” Alisema kwamba uhasama huo ungeanzishwa na Gogu wa Magogu, yaani, Shetani Ibilisi. (Ezekieli 38:14, 16) Kwa njia ya kitamathali, Gogu atokea upande gani? “Pande za mwisho za kaskazini,” asema Yehova, kupitia Ezekieli. (Ezekieli 38:15) Hata shambulio hilo liwe kali namna gani, halitawaharibu watu wa Yehova. Tukio hilo lenye kutokeza litamfanya Yehova achukue hatua ili kuyaangamiza majeshi ya Gogu. Kwa hiyo, Yehova amwambia Shetani hivi: ‘Nitakutia kulabu katika mataya yako, nami nitakutoa.’ “Nitakupandisha toka pande za mwisho za kaskazini; nami nitakuleta juu ya milima ya Israeli.” (Ezekieli 38:4; 39:2) Kwa hiyo, habari ‘itokayo kaskazini’ ambayo yamkasirisha mfalme wa kaskazini lazima iwe yatokana na Yehova. Lakini Mungu tu ndiye atakayeamua habari kamili zitokazo ‘macheo ya jua na kaskazini’ zitakuwa nini, nao wakati utafunua.
27. (a) Kwa nini Gogu atayachochea mataifa, kutia ndani mfalme wa kaskazini, yashambulie watu wa Yehova? (b) Matokeo ya shambulio la Gogu yatakuwa nini?
27 Gogu anapanga shambulio la kufa na kupona dhidi ya ufanisi wa “Israeli wa Mungu,” ambao, pamoja na “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” si sehemu ya ulimwengu wake. (Wagalatia 6:16; Ufunuo 7:9; Yohana 10:16; 17:15, 16; 1 Yohana 5:19) Gogu awatazama kichongochongo “watu waliokusanyika toka mataifa, waliopata ng’ombe na mali [za kiroho].” (Ezekieli 38:12) Akiyaona makazi ya kiroho ya Wakristo kuwa “nchi yenye vijiji visivyo na maboma” iliyo rahisi kuteka, Gogu ajitahidi sana kufagilia mbali kipingamizi hicho apate kudhibiti kabisa wanadamu. Lakini ashindwa. (Ezekieli 38:11, 18; 39:4) Wafalme wa dunia, kutia ndani mfalme wa kaskazini, washambuliapo watu wa Yehova, ‘watakuwa wamefikia kikomo chao.’
‘MFALME ATAKUWA AMEFIKIA KIKOMO CHAKE’
28. Twajua nini juu ya wakati ujao wa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini?
28 Vita ya mwisho ya mfalme wa kaskazini haitakuwa dhidi ya mfalme wa kusini. Kwa hiyo, mfalme wa kaskazini hafikii kikomo chake mikononi mwa mpinzani wake mkuu. Hali kadhalika, mfalme wa kusini haharibiwi na mfalme wa kaskazini. Mfalme wa kusini aharibiwa, “bila kazi ya mikono” ya kibinadamu, bali na Ufalme wa Mungu.a (Danieli 8:25) Kwa hakika, kwenye vita ya Har–Magedoni, wafalme wote wa kidunia wataondolewa na Ufalme wa Mungu, na yaonekana hilo ndilo litakalompata mfalme wa kaskazini. (Danieli 2:44) Andiko la Danieli 11:44, 45 lafafanua matukio yanayoelekeza kwenye pigano la mwisho. Si ajabu basi kwamba “hakuna atakayemsaidia”!
-
-
Wafalme Washindani Wakaribia Mwisho WaoSikiliza Unabii wa Danieli!
-
-
[Chati/Picha katika ukurasa wa 284]
WAFALME KATIKA DANIELI SURA YA 11
Mfalme wa Mfalme wa
Kaskazini Kusini
Danieli 11:5 Niketa Seleuko wa I Ptolemy wa Kwanza
Danieli 11:6 Antiochus wa Pili Ptolemy wa Pili
(mke Laodice) (binti Berenice)
Danieli 11:7-9 Seleuko wa Pili Ptolemy wa Tatu
Danieli 11:10-12 Antiochus wa Tatu Ptolemy wa Nne
Danieli 11:13-19 Antiochus wa Tatu Ptolemy wa Tano
(binti Kleopatra wa I) Mwandamizi:
Waandamizi: Ptolemy wa Sita
Seleuko wa Nne na
Antiochus wa Nne
Danieli 11:20 Augusto
Danieli 11:21-24 Tiberio
Danieli 11:27-30a Milki ya Ujerumani Uingereza,
(Vita ya Ulimwengu ikifuatwa na
ya Kwanza) Serikali ya Ulimwengu ya
Uingereza na Marekani
Danieli 11:30b, 31 Milki ya Tatu ya Hitler Serikali ya (Vita ya Ulimwengu Ulimwengu ya
ya Pili) Uingereza na Marekani
Danieli 11:32-43 Mataifa ya Kikomunisti Serikali ya (Vita Baridi) Ulimwengu ya
Uingereza na Marekani
[Maelezo ya Chini]
b Unabii katika Danieli sura ya 11 hautaji majina ya tawala zinazofanyiza mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wa nyakati mbalimbali. Wanajulikana baada tu ya mambo kuanza kutukia. Isitoshe, kwa kuwa mapambano yatukia pindi kwa pindi, kuna vipindi vya kutopambana—mfalme mmoja awa na mamlaka huku yule mwingine akiwa asiyetenda.
[Picha katika ukurasa wa 271]
[Picha katika ukurasa wa 279]
‘Kusukuma’ kunakofanywa na mfalme wa kusini kumetia ndani upelelezi wa hali ya juu na utendaji wa kijeshi
-