-
Latvia2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kufikia mwaka wa 1931, vichapo vingi vya kujifunza Biblia vilikuwa vimepigwa marufuku.
-
-
Latvia2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka wa 1931, ndugu kadhaa kutoka Uingereza walikubali mwito wa mapainia kuhamia nchi za Baltiki. Baadhi ya ndugu hao walisaidia kuingiza chakula cha kiroho nchini Latvia kutoka katika maeneo jirani ya Estonia na Lithuania. Edwin Ridgewell, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 18, alitumwa Lithuania. Sasa Ndugu Ridgewell ana miaka 90 na kitu, naye anakumbuka hivi: “Mimi na wenzangu wawili, Andrew Jack na John Sempey, tulipata mgawo wa pekee wa kupeleka vichapo Latvia. Tulikuwa tukipanda gari-moshi la usiku kwenda Riga nasi tulificha vichapo ndani ya vifurushi ambavyo vingeweza kutoshea chini ya viti, ambapo matandiko yalikuwa yakiwekwa mchana. Kabla ya kushuka, tuliingiza vifurushi hivyo na nguo kadhaa ndani ya mikoba ya pekee ambayo ingeweza kupanuliwa. Kila tulipofaulu kufikisha vichapo hivyo, tulisherehekea. Percy Dunham, ambaye alisimamia kazi, angetupeleka kusherehekea kwenye mkahawa fulani huko Riga.”
Mara nyingi, Ferdinand Fruck alikutana na akina ndugu kwenye mpaka wa Lithuania. Walimpa vichapo, naye akaviweka chini ya nyasi kavu katika dari la ghala lake. Hata hivyo, wenye mamlaka waligundua shughuli zake, na tangu wakati huo polisi wakawa wakisaka nyumba yake kutafuta vichapo vilivyopigwa marufuku. Pindi moja walipokuja kufanya msako, ofisa mmoja hakutaka kupanda katika dari la ghala, kwa hiyo akamwamuru Ferdinand apande badala yake! Ili amtulize ofisa huyo, Ferdinand alirudi na magazeti machache ya zamani ya Mnara wa Mlinzi na kumpa. Ofisa huyo akaridhika na kwenda zake.
-