Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb07 kur. 176-221
  • Latvia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Latvia
  • 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • “UHURU KWA AJILI YA WATU”
  • UPINZANI WATOKEA
  • MAENDELEO LICHA YA UPINZANI
  • USAJILI HAUKUDUMU
  • YEHOVA ANAWAFARIJI WASHIKAMANIFU WAKE
  • KUPELEKWA SIBERIA
  • WALIOBAKI, WAHEPA KGB
  • “SOTE TULITUMIA GAZETI MOJA TU LA MNARA WA MLINZI”
  • WATU WA AINA ZOTE WANAKUBALI KWELI
  • “KUMBE NI KAMUSI”
  • WANAWAPENDA WATU BADALA YA RAHA
  • UHURU WA KUHUDHURIA MAKUSANYIKO MAKUBWA
  • KIPINDI CHA ONGEZEKO LA HARAKA
  • “NINAFURAHI KWAMBA SIKURUDI NYUMA”
  • IMANI YA KIKRISTO INAJARIBIWA
  • WANAUME WAKOMAVU KIROHO WATIMIZA UHITAJI MUHIMU
  • MSAADA WA WAHITIMU WA GILEADI
  • WAHITIMU WA SHULE YA MAZOEZI YA KIHUDUMA WAFIKA
  • KUTAFSIRI KATIKA KILATVIA
  • ZAWADI
  • KUTAMBULIWA KISHERIA
  • KUPATA MAHALI PA KUKUTANIA
  • MSAADA KUTOKA FINLAND
  • KAMPENI ZA PEKEE ZA KUHUBIRI
  • WENGI WANAPATA UHURU WA KWELI
2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb07 kur. 176-221

Latvia

Kwenye Barabara ya Brīvības (au, Barabara ya Uhuru) iliyo katikati ya Riga, jiji kuu la Latvia, kuna Mnara wa Ukumbusho wa Uhuru wenye urefu wa mita 42. Mnara huo ulizinduliwa mwaka wa 1935, nao unawakilisha uhuru wa kisiasa. Lakini kuna uhuru bora zaidi ambao watu wa Latvia wamepata tangu miaka ya 1920, uhuru unaotokana na kujua kweli ya Biblia. Ripoti moja ilisema hivi kuhusu uhuru huo wa kiroho: “Watu wa kawaida, . . . wanaume kwa wanawake, wanaukubali ujumbe kwa machozi ya shangwe.” Kwa makumi ya miaka, maadui walijaribu kukandamiza ujumbe huo wenye thamani, nao walifanikiwa kwa kadiri fulani. Hata hivyo, kama vile masimulizi haya yatakavyoonyesha, hakuna mamlaka yoyote duniani inayoweza kuzuia mkono wa Mweza-Yote au wa Mwana wake, ambaye utawala wake unapita mipaka yote ya kisiasa.—Ufu. 11:15.

Tangu enzi za kundi fulani (Teutonic Knights) lililoanzisha jiji la Riga mwaka wa 1201 hadi enzi za utawala wa Ukomunisti huko Sovieti, Latvia imevamiwa na kutawaliwa na serikali mbalimbali, kutia ndani Poland, Sweden, Ujerumani, na Urusi. Mwaka wa 1918, Latvia ilipata uhuru kwa mara ya kwanza. Lakini mwaka wa 1940, nchi hiyo ikawa jamhuri ya Sovieti. Mwaka wa 1991, ilipata uhuru tena na kuwa Jamhuri ya Latvia.

Hata hivyo, uhuru wa kisiasa si uhuru wa kweli. Yehova tu ndiye anayeweza kuwapa wanadamu uhuru kamili, na ahadi yake ya uhuru ni sehemu yenye kupendeza ya habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Luka 4:18; Ebr. 2:15) Habari hiyo njema ilifikaje Latvia? Masimulizi yetu yanaanza kwa sala ya baharia Ans Insberg.

Ans aliandika hivi: “Nikiwa baharini usiku mmoja wenye nyota nyingi, nilimmiminia Bwana moyo wangu na kumwomba anielekeze kwa watu wanaomwabudu kwa roho na kweli. (Yoh. 4:24) Nilikuwa nimeona unafiki mwingi wa wafuasi wa dini katika nchi yetu ya Latvia, nami nilichukizwa na unafiki huo. Kisha, mwaka wa 1914 nilipokuwa Cleveland, Ohio, Marekani, nikaona ile sinema ya Biblia ya ‘Photo-Drama of Creation,’ ambayo ilitayarishwa na Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Sala yangu ilijibiwa; nilipata kweli! Nilibatizwa Januari 9, 1916, na kuanza kazi ya kuhubiri. Kila nilipoishiwa na pesa, nilirudia ubaharia kwa muda.”

Muda mfupi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Ans alieneza sana ujumbe wa Ufalme nchini Latvia. Alifanya mpango ili matangazo kuhusu Ufalme wa Mungu yachapishwe katika magazeti ya Latvia, naye akalipia matangazo hayo. Mwalimu mstaafu anayeitwa Krastin̗š alijifunza kweli kupitia matangazo hayo, na inaelekea yeye ndiye Mwanafunzi wa Biblia wa kwanza nchini Latvia kujiweka wakfu kwa Yehova. Mwaka wa 1922, Ans alianza kufanya kazi kwenye makao makuu ya Wanafunzi wa Biblia huko Brooklyn, New York. Akiwa huko, alikuwa akienda bandarini kwa ukawaida, kwenye ‘jukwaa lake la kuhubiri,’ kama alivyoliita kwa mzaha, ili kuwaeleza mabaharia wenzake kweli ya Biblia. Alikufa Novemba 30, 1962, akiwa na tumaini la kwenda mbinguni.

Mwaka wa 1925, Ofisi ya Ulaya Kaskazini ilifunguliwa huko Copenhagen, Denmark. Ilisimamia kazi katika nchi tatu za Baltiki: Estonia, Latvia, na Lithuania. Pia ilisimamia kazi nchini Denmark, Finland, Norway, na Sweden. Mnamo Julai 1926, Rees Taylor, kutoka Uingereza, alipewa mgawo wa kusimamia kazi nchini Latvia. Alianzisha ofisi huko Riga na kupanga kusanyiko dogo. Kati ya wale 20 waliohudhuria, 14 walishiriki kampeni ya kwanza ya utumishi wa shambani nchini humo. Kisha, akina ndugu waliruhusiwa na polisi kufanya mikutano ya hadhara, na watu 975 walisikiliza hotuba za Biblia jijini Riga, Liepaja, na Jelgava. Hotuba hizo zilitolewa katika Kijerumani, lugha ya pili ya Walatvia wengi. Wengi walitaka kuwe na mikutano zaidi.

“UHURU KWA AJILI YA WATU”

Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1927, wajumbe 650 hivi kutoka Estonia, Latvia, na Skandinavia walikusanyika Copenhagen kumsikia Joseph F. Rutherford kutoka kwenye makao makuu akitoa hotuba yenye kichwa “Uhuru kwa Ajili ya Watu.” Mwaka uliofuata, kijitabu chenye kichwa hicho kilitafsiriwa katika Kilatvia, na makolpota, au mapainia, wakaongoza katika kazi ya kukisambaza.

Mapainia hao wa mapema walitia ndani angalau ndugu kumi kutoka Ujerumani waliofika Latvia kusaidia kufanya kazi. Mmoja wao ni Johannes Berger, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 22. Aliandika hivi: “Mapainia walipofika katika jiji la mgawo wao, walianza kwa kutoa hotuba za watu wote. Hivyo, tulitoa hotuba katika karibu majiji yote ya Latvia. Katika jiji la Sloka, tulikodi jumba la sinema, nami nilitoa hotuba kila Jumatatu (Siku ya 1) wakati wa majira ya baridi kali. Watu walitoka mbali huku wakiendesha farasi wao wadogo.” Akikumbuka nyakati hizo, anaongeza hivi: “Nilikuwa na mapendeleo mengi ya utumishi, ingawa sikuwa na elimu nyingi.”

Wahubiri wa Ufalme wapatao 40, 15 kati yao wakiwa wamebatizwa, walishiriki kazi ya kuhubiri mwaka wa 1928. Mwaka wa 1929, ofisi ilipohamishiwa Barabara ya Šarlotes, Riga, tisa wengine walibatizwa, na zaidi ya vitabu na vijitabu 90,000 viligawanywa shambani.

Mapema mwaka wa 1927, kijana mmoja anayeitwa Ferdinand Fruck na mama yake, Emilie, walibatizwa. Miaka minne baadaye, Ferdinand alipokuwa akihubiri katika duka la kuoka mikate katika mji wa kwao wa Liepaja, alikutana na mwanamume ambaye baadaye alikuja kuwa painia mwenzake. Mwokaji huyo alienda mbio kwenye duka jirani la kinyozi aliyekuwa ndugu yake, na kumwambia, “Heinrich! Njoo haraka!” Kisha akasema: “Kuna mtu dukani kwangu ambaye anasema mambo nisiyoweza kuyaamini.” Kinyozi huyo, Heinrich Zech, hakuona vigumu kuamini kweli ya Biblia, naye akabatizwa baada ya muda mfupi. Alijiunga na Ferdinand, na wote wawili wakatembelea majiji mengi kwa baiskeli ili kueneza ujumbe wa Ufalme.

UPINZANI WATOKEA

Ingawa akina ndugu walikuwa wachache, bidii yao iliwakasirisha makasisi. Kasisi fulani huko Riga alitisha kumfukuza yeyote ambaye angehudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Huko Liepaja, makasisi waligawanya vikaratasi vilivyosema kuwa akina ndugu hawamwamini Yesu Kristo na kuwahimiza watu wakatae vichapo vyao. Pia, walitumia gazeti kuu la kanisa kuwapaka matope Wanafunzi wa Biblia.

Mwaka wa 1929, serikali ilisikiliza madai ya kanisa na kuwafukuza makolpota Wajerumani kutoka Latvia. Kufikia mwaka wa 1931, vichapo vingi vya kujifunza Biblia vilikuwa vimepigwa marufuku. Je, upinzani huo uliwanyamazisha akina ndugu? Ofisi ya Latvia iliandika hivi: “Upinzani wa Ibilisi . . . unatuchochea kuwa waaminifu zaidi. Kufanya kazi huku kunatuletea shangwe nyingi . . . , nasi tumeazimia kusonga mbele.”

Mwaka wa 1931, ndugu kadhaa kutoka Uingereza walikubali mwito wa mapainia kuhamia nchi za Baltiki. Baadhi ya ndugu hao walisaidia kuingiza chakula cha kiroho nchini Latvia kutoka katika maeneo jirani ya Estonia na Lithuania. Edwin Ridgewell, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 18, alitumwa Lithuania. Sasa Ndugu Ridgewell ana miaka 90 na kitu, naye anakumbuka hivi: “Mimi na wenzangu wawili, Andrew Jack na John Sempey, tulipata mgawo wa pekee wa kupeleka vichapo Latvia. Tulikuwa tukipanda gari-moshi la usiku kwenda Riga nasi tulificha vichapo ndani ya vifurushi ambavyo vingeweza kutoshea chini ya viti, ambapo matandiko yalikuwa yakiwekwa mchana. Kabla ya kushuka, tuliingiza vifurushi hivyo na nguo kadhaa ndani ya mikoba ya pekee ambayo ingeweza kupanuliwa. Kila tulipofaulu kufikisha vichapo hivyo, tulisherehekea. Percy Dunham, ambaye alisimamia kazi, angetupeleka kusherehekea kwenye mkahawa fulani huko Riga.”

Mara nyingi, Ferdinand Fruck alikutana na akina ndugu kwenye mpaka wa Lithuania. Walimpa vichapo, naye akaviweka chini ya nyasi kavu katika dari la ghala lake. Hata hivyo, wenye mamlaka waligundua shughuli zake, na tangu wakati huo polisi wakawa wakisaka nyumba yake kutafuta vichapo vilivyopigwa marufuku. Pindi moja walipokuja kufanya msako, ofisa mmoja hakutaka kupanda katika dari la ghala, kwa hiyo akamwamuru Ferdinand apande badala yake! Ili amtulize ofisa huyo, Ferdinand alirudi na magazeti machache ya zamani ya Mnara wa Mlinzi na kumpa. Ofisa huyo akaridhika na kwenda zake.

MAENDELEO LICHA YA UPINZANI

Percy Dunham kutoka Scotland, ambaye alitajwa juu, alipewa mgawo wa kusimamia eneo la Latvia mwaka wa 1931. Percy alikuwa Mwanafunzi wa Biblia kabla ya mwaka wa 1914, naye alikuwa na uzoefu uliosaidia sana. Mwishoni mwa mwaka wa 1931, ofisi iliandika hivi: “Kazi inafanywa chini ya hali ngumu na wale ambao ni maskini katika ulimwengu huu lakini matajiri katika imani kumwelekea Mungu. . . . Watu wanazidi kupendezwa na ujumbe wetu. . . . Kila juma watu wanakuja ofisini kuomba vitabu na kuulizia wakati vingine vitakapopatikana.” Kisha, ripoti hiyo ikataja hatua muhimu sana ya kiroho: “Hivi karibuni, kwenye mkutano uliofanyiwa Riga, sote tulipitisha azimio na kukubali kwa shangwe jina jipya [Mashahidi wa Yehova], ambalo Bwana amewapa watu wake.”

Mwaka wa 1932, ofisi ilihamishiwa Barabara ya Cēsu, jijini Riga. Mwaka huohuo, Margaret (Madge) Brown, painia kutoka Scotland aliyetumikia Ireland na kubatizwa mwaka wa 1923, alihamia Latvia na kuolewa na Percy Dunham. Wakati huo upinzani ulizidi kuongezeka. Madge anaandika hivi: “Mnamo Februari 9, 1933, gazeti fulani la Riga lilidai sisi ni Wakomunisti. Asubuhi iliyofuata, mlango ulibishwa nami nikaufungua. Polisi waliingia kwa fujo huku wakiwa na bunduki zao na kuamuru kwa sauti, ‘Mikono juu!’ Kwa saa saba, walitafuta vitabu vilivyopigwa marufuku. Wakati wa mchana, niliwapa chai, nao wakanywa.

“Akiba kuu ya vichapo vya akina ndugu ilikuwa imefichwa darini. Mapema, ofisa-msimamizi alipopekua mifuko ya nguo ya mume wangu, alipata funguo. Akauliza, ‘Ni za wapi?’ Percy akamjibu, ‘Ni za chumba cha dari.’ Lakini polisi hawakupanda kwenye chumba hicho. Ajabu ni kwamba kabla ya kuondoka, ofisa huyo alimrudishia Percy funguo! Ingawa walikagua vichapo fulani, walisema hawakuona haja ya kuvichukua.

“Hata hivyo, walivichukua pamoja na barua, pesa, mashini ya kuchapisha na taipureta. Polisi walifanya misako mingine katika nyumba za familia sita za Mashahidi Walatvia lakini hawakupata uthibitisho wowote wa uvunjaji wa sheria wala hawakuwashtaki.”

Wakati huo, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme chini ya 50 nchini. Hata hivyo, ili waendeshe mambo kisheria, akina ndugu walituma maombi ya kusajiliwa. Wazia jinsi walivyoshangilia wakati shirika la International Bible Students Association liliposajiliwa rasmi Machi 14, 1933! Ingawa hawakuruhusiwa kuingiza vichapo vya Biblia nchini, akina ndugu walitumia haki yao ya kisheria kuchapisha vijitabu fulani nchini. Aleksandrs Grīns, mwandishi maarufu na mhariri mkuu wa gazeti la Rīts, alitafsiri vichapo katika Kilatvia.

USAJILI HAUKUDUMU

Mapinduzi yaliyotukia Mei 1934, yalifanya sheria za kijeshi zianze kutumiwa. Maadui wa ile kweli walitumia msukosuko huo wa kisiasa kuwashtaki watu wa Mungu kuwa Wakomunisti. Mnamo Juni 30, waziri wa mambo ya ndani alifunga ofisi ya shirika la International Bible Students Association na kuchukua vitabu na vijitabu zaidi ya 40,000 na kiasi kidogo cha pesa. Makasisi walipewa kazi ya kufunga hesabu za ofisi hiyo! Maombi ya kusajiliwa upya yalikataliwa.

Mwaka wa 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza, na Juni 1940, jeshi la Urusi liliingia Latvia. Mwezi wa Agosti, Latvia ikawa jamhuri ya 15 ya Muungano wa Sovieti, nayo ikaitwa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Latvia. Mnamo Oktoba 27, akina Dunham walilazimika kuondoka Latvia na kuwaacha ndugu na dada zao wapendwa. Walitumwa kwenye ofisi ya tawi ya Australia, ambako Percy alikufa mwaka wa 1951, na Madge akafa mwaka wa 1998, wote wakiwa na tumaini la kwenda mbinguni.

Kufungwa kwa ofisi, kufukuzwa kwa akina ndugu waliokuwa wakiongoza, majaribu ya vita, na ile miaka ya utawala mkali wa Ukomunisti iliathiri sana kazi. Katika miaka ya 1990 vizuizi hivyo vikali viliondolewa mwishowe.

YEHOVA ANAWAFARIJI WASHIKAMANIFU WAKE

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wachache waliokuwa Latvia hawangeweza kuwasiliana na makao makuu. Lakini waliendelea kuwa na tumaini “kupitia faraja kutokana na Maandiko.” (Rom. 15:4) Baada ya vita, mwisho-mwisho wa miaka ya 1940, hatimaye ofisi ya tawi ya Ujerumani ilifaulu kuwatumia barua akina ndugu huko Jelgava, Kuldīga, Riga, na Ventspils.

Huko Kuldīga, mji ulio umbali wa kilomita 160 magharibi mwa Riga, Ernests Grundmanis, ambaye alikuwa katika kweli kwa miaka 20, alipokea barua kadhaa kutoka Ujerumani zilizokuwa na chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. “Katika mambo yote,” barua moja ilisema, “mtegemee Yehova Mungu, Baba yetu mwema. Atakutegemeza na kukutia nguvu kwa wakati unaofaa.” Kisha, barua hiyo ikanukuu andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linalosema: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” Kwa kweli barua hizo zilikuja wakati unaofaa, nazo zilitia moyo sana!

Akina ndugu walitumia kila nafasi kuhubiri isivyo rasmi. Kwa mfano, Marta Baldone, ambaye alifanya kazi ya kuwakanda watu katika kituo cha afya huko Ventspils, aliwahubiria wateja wake. Mmoja wao ni Alexandra Preklonskaya (sasa Rezevskis). Alexandra anakumbuka hivi: “Marta alinifundisha kwamba jina la Mungu ni Yehova, nami nikalipenda sana jina hilo.”

Baba ya Alexandra, Peter, aliyezaliwa mwaka wa 1880, alipata kweli ya Biblia pia. Binti yake anaandika hivi: “Baba alijiunga na chama cha Kikomunisti kabla ya mapinduzi ya mwaka wa 1917, naye aliishi katika jiji la St. Petersburg [lililokuwa likiitwa Petrograd kuanzia 1914 mpaka 1924 na Leningrad kuanzia 1924 mpaka 1991]. Hata hivyo, kwa kuwa Baba alitamaushwa na matokeo ya mapinduzi hayo, alirudisha kadi yake ya chama na kulazimika kuhama jiji hilo. Alikuja Latvia, ambako nilimjulisha kwa Marta. Baba alikuwa mnyoofu na mwenye fadhili na alikubali kweli kwa utayari. Mwaka wa 1951, alirudi Urusi akiwa mfungwa wa imani yake. Alifia Siberia mwaka wa 1953.”

KUPELEKWA SIBERIA

Nchini Latvia, kama katika nchi nyingine zilizokuwa chini ya Sovieti, serikali mpya ilianza kufanya taasisi za kitamaduni na za kisiasa ziwe kama za Sovieti. Pia, Wakomunisti walijumuisha mashamba ya watu binafsi ili yasimamiwe na serikali. Kwa sababu ya mradi huo, kulikuwa na visa vingi vya kuwahamisha watu, ambavyo viliisha mwaka wa 1949. Walatvia 100,000 hivi walihamishiwa Urusi Kaskazini, kutia ndani Siberia. Miaka miwili baadaye, Wakomunisti waliwageukia Mashahidi wa Yehova na kuhamisha maelfu kutoka kwenye mashamba, kutia ndani angalau 20 kati ya wahubiri 30 hivi waliobaki Latvia.

Ingawa hakuwa amebatizwa, Valija Lange, kutoka Ventspils, ni mmoja wa waliokamatwa na KGB (Halmashauri ya Usalama wa Kitaifa ya Sovieti) katika misako ya Septemba 1950. Alipohojiwa usiku wa manane huko Riga, aliulizwa: “Kwa nini unapinga serikali na wewe ni raia wa Muungano wa Sovieti?” Valija akajibu kwa utulivu na heshima: “Ninakusudia tu kumtumikia Yehova Mungu, kuelewa mafundisho yake, na kuwaeleza wengine mafundisho hayo.”

Jina la Valija, na majina ya Mashahidi 19 wengine, yaliorodheshwa katika hati moja ya Oktoba 31, 1950. Wote walioorodheshwa humo walihukumiwa kifungo na kazi ngumu kwa miaka kumi huko Siberia, na wakanyang’anywa mali yao. Wengine waliruhusiwa kurudi nyumbani lakini wakashtakiwa tena. Kwa mfano, Paulīne Serova alipelekwa tena Siberia kwa miaka mingine minne wakati wenye mamlaka walipogundua anapokea vichapo vya Biblia kupitia posta.

Akina ndugu waliendelea kuhubiri na kufanya wanafunzi kambini. Mmoja wa wanafunzi hao ni Jānis Garšk̗is. Alibatizwa mwaka wa 1956 na sasa anaishi Ventspils. Anasema: “Nashukuru kwamba Mungu aliacha nipelekwe katika kambi ya kazi ngumu, la sivyo singejifunza kweli.” Huo ni mtazamo mzuri kama nini!

Tekla Onckule, ambaye ni mzaliwa wa Latvia, alishtakiwa kwa uchochezi wa kisiasa, naye akapelekwa Siberia. Alipokuwa katika jiji la mbali la Omsk, alipata kweli kutoka kwa Mashahidi waliohamishwa. “Sitasahau kamwe siku niliyobatizwa,” Tekla anasema. “Nilibatizwa usiku sana katika mto wenye maji baridi kama barafu. Nilitetemeka sana kwa sababu ya baridi, lakini nilifurahi sana.” Mwaka wa 1954, Tekla aliolewa na Aleksei Tkach, ambaye alibatizwa mwaka wa 1948 huko Moldavia (sasa Moldova) na baadaye akahamishwa mpaka Siberia. Mwaka wa 1969, wenzi hao wa ndoa na Mashahidi wengine wachache walirudi Latvia. Kwa kuhuzunisha, wengi wa wale wengine waliohamishwa kutoka Latvia walikufa kambini.

WALIOBAKI, WAHEPA KGB

Mashahidi wachache waliepuka kukamatwa. Alexandra Rezevskis anaandika hivi: “Niliepuka kuhamishwa kwa kuhamahama, kufanya kazi katika mashamba mbalimbali, na kuwapiga chenga KGB. Wakati huohuo, niliendelea kuwahubiria wote niliokutana nao. Watu walisikiliza, na wengine wakaingia katika kweli.” Wawakilishi wa KGB walijaribu sana kuwapata Mashahidi wachache waliotawanyika ambao walibaki Latvia, na kuwashtaki kwa kupinga utawala wa Sovieti. Serikali hata iligawanya kijitabu kilichowashutumu kwa uwongo Mashahidi kuwa wapelelezi wa Marekani. Kwa kuwa walichunguzwa kwa uangalifu na watoa-habari wa Ukomunisti, akina ndugu walilazimika kuhubiri kwa busara na kufanya mikutano kwa siri katika sehemu tofauti-tofauti.

Baada ya kuolewa na Kārlis Rezevskis, Alexandra na mume wake walihamia nyumba ndogo ya wazazi wa Kārlis. Nyumba hiyo ilikuwa katika msitu karibu na mji wa Tukums, kilomita 68 kutoka Riga, nayo ilifaa sana kwa mikutano katika majira ya baridi kali. Dita Grasberga, ambaye wakati huo alikuwa akiitwa Andrišaka, anakumbuka hivi: “Nilikuwa mtoto familia yetu ilipokuwa ikihudhuria mikutano katika nyumba ya akina Rezevskis. Nilifurahia kwenda Tukums kwa basi na kutembea katikati ya msitu huku kukiwa na theluji. Kisha, tulipofika kwenye nyumba hiyo, mara nyingi tulisikia harufu nzuri ya mchuzi mtamu uliokuwa ukipikwa.”

Kwa kawaida, Kārlis alificha vichapo msituni. Wakati fulani, alizika mifuko miwili iliyojaa vitabu na kutia alama mahali hapo kwa uangalifu. Lakini usiku huo dhoruba kali iliondoa alama hiyo. Kārlis alijaribu kutafuta mifuko hiyo asiipate. Mpaka leo, mifuko hiyo ingali imefukiwa katika msitu huo.

Wakati wa kiangazi, akina ndugu walifanya mikutano katika misitu, kando ya maziwa, au kando ya bahari. Kama ilivyo katika nchi nyingine za Sovieti, walitumia sherehe za ndoa na maziko kutoa hotuba za Biblia. Katika miaka ya 1960 na 1970, Ndugu Viljard Kaarna, Silver Silliksaar, na Lembit Toom na wengineo kutoka Estonia, walitembelea Latvia kwa ukawaida kutoa hotuba, kupeleka vichapo, na kuchukua ripoti za wahubiri 25 hivi waliobatizwa ambao walikuwa huko. Ndugu hao walifurahia hasa kupokea Mnara wa Mlinzi katika Kirusi, ambalo Pauls na Valija Bergmanis walitafsiri katika Kilatvia huku wakiandika katika madaftari ya wanafunzi.

“SOTE TULITUMIA GAZETI MOJA TU LA MNARA WA MLINZI”

Katika miaka ya 1970 na 1980, ndugu kutoka Estonia walikuwa wakipata filamu yenye maandishi madogo ya Mnara wa Mlinzi huko Urusi na kuiingiza Latvia kwa siri. Kwa kuwa upigaji-picha ulipendwa sana wakati huo, haikuwa vigumu kwa akina ndugu kusafisha filamu hiyo nyumbani, kutoa nakala, na kuzigawanya kwa sababu walikuwa na njia za kufanya hivyo. Mara kwa mara, vichapo vingine viliingia nchini kupitia njia hiyohiyo, hasa kutoka Lithuania na Ukrainia.

“Sote tulitumia gazeti moja tu la Mnara wa Mlinzi,” anasema Vida Sakalauskiene, ambaye wakati huo alikuwa na miaka kumi hivi. “Kwa muda fulani, kila kikundi kilipokea gazeti likiwa kwenye karatasi ya picha baada ya filamu kusafishwa, kisha familia moja ikapokeza familia nyingine gazeti hilo ili wote wasome na kuandika mambo makuu. Hakuna aliyeruhusiwa kuwa na gazeti kwa zaidi ya saa 24. Kwenye mkutano, kiongozi alikuwa na gazeti, nasi tulijibu maswali ya funzo kutokana na kumbukumbu au mambo makuu tuliyoandika.” Maandalizi hayo ya kiroho yalimsaidia Vida kuitetea kweli alipokuwa shuleni. Pia, yalimsaidia ndugu yake, Romualdas, kudumisha utimilifu alipofungwa kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo.

WATU WA AINA ZOTE WANAKUBALI KWELI

Kwa miaka 27, Vera Petrova alikuwa mwanachama mwenye bidii wa chama cha Ukomunisti. “Mojawapo ya majukumu yangu,” anasema, “lilikuwa kwenda kanisani kuona ni wanachama wangapi wa Ukomunisti walikuwa huko kisha kumweleza ofisa wa chama wa eneo letu. Wakati huo, mmoja wa dada zangu wawili aliingia katika kweli na kuanza kunihubiria. Nikiwa nimependezwa, nilimwomba Biblia kasisi wa Kanisa la Othodoksi la Urusi.

Aliuliza hivi, “‘Kwa nini unataka Biblia?’

Nikamjibu: “‘Nataka kujua ikiwa mambo unayofundisha yanapatana nayo.’ Kwa kuwa alikataa kunipa Biblia, niliitafuta, nikaipata kwingineko na kuanza kuisoma. Upesi nikatambua kwamba mafundisho ya kanisa hilo hayapatani na Biblia. Niliendelea kufanya maendeleo ya kiroho, nikaondoka katika chama cha Ukomunisti, kisha nikabatizwa mwaka wa 1985.”

Kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, muuguzi anayeitwa Teofīlija Kalvīte aliolewa na meya wa Daugavpils. Kwa kuhuzunisha, muda mfupi baada ya vita kuanza, ilitangazwa kwamba mume wake amepotea. Teofīlija mwenyewe alipata shida nyingi na kuona mateso na vifo vingi. Baada ya vita, akawa msimamizi wa Shirika la Msalaba Mwekundu la Latvia, na serikali ikampa angalau tuzo 20 katika miaka 61 ya kazi yake ya kitiba. Teofīlija alipokuwa na miaka 65 hivi, alikutana na Shahidi anayeitwa Paulīne Serova, ambaye alimweleza yale ambayo Biblia inasema kuhusu sababu ya Mungu ya kuruhusu uovu. Teofīlija alikubali kweli, na tangu wakati huo akawa na pendeleo zuri la kuwasaidia watu kupata afya ya kiroho. Alikufa akiwa mwaminifu mwaka wa 1982.

“KUMBE NI KAMUSI”

Mwaka wa 1981, Yurii Kaptola alikuwa na miaka 18 alipofungwa gerezani kwa miaka mitatu kwa kudumisha msimamo wa Kikristo wa kutokuwamo. Yurii anasema: “Nilifungwa kwa miaka miwili Siberia, ambako tuliishi katika mahema na kufanya kazi misituni, hata wakati ambapo hali ya joto ilifikia nyuzi 30 Selsiasi chini ya kiwango cha mgando!a Yehova alinitunza kiroho nyakati zote. Kwa mfano, wakati fulani Mama alinitumia Maandiko ya Kigiriki katika kifurushi cha chakula. Mlinzi alipokuwa akikagua kifurushi hicho, inspekta aliona kitabu hicho.

Akauliza hivi, “‘Hiki ni kitu gani?’

“Kabla sijamjibu, inspekta aliyekuwa karibu akasema, ‘Kumbe ni kamusi,’ naye akaniruhusu nibaki nacho.

“Niliachiliwa mwaka wa 1984. Badala ya kukaa Ukrainia, nchi ya nyumbani, nilihamia Riga, ambako nilishirikiana na kikundi kidogo cha Mashahidi kwa miaka miwili hivi. Lakini, kwa kuwa bado Latvia ilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti, niliitwa tena jeshini. Ikawaje? Mnamo Agosti 26, 1986, nilihukumiwa tena kifungo na kazi ngumu, wakati huu kwa miaka minne nchini Latvia. Baada ya kufungwa kwa muda huko Riga, nilienda kwenye kambi fulani karibu na jiji la Valmiera. Mapema mwaka wa 1990, katika kesi ya kuamua ikiwa nitaachiliwa, hakimu alisema: ‘Yurii, uamuzi wa kukufunga uliotolewa miaka minne iliyopita haukuwa halali. Hukupaswa kuhukumiwa.’ Mara moja nikawa huru!”

Mwaka wa 1991, Yurii akawa mshiriki wa kutaniko pekee lililokuwa Latvia, naye alikuwa mmoja wa wazee wawili wa huko. Anaandika hivi: “Kwa kweli mashamba yalikuwa meupe kwa ajili ya mavuno.”

Yurii alipofika Latvia kwa mara ya kwanza, alizungumza na mwanamke aliyekuwa akipamba kaburi. Anaeleza jinsi ilivyokuwa: “Nilipomuuliza kwa nini maisha yanaonekana kuwa mafupi sana, alisogea hatua chache kunielekea kisha tukazungumza. Dakika chache baadaye, tawi kubwa la mti lilivunjika na kuanguka kwa kishindo mahali palepale alipokuwa ametoka kufanya shughuli zake. Ikiwa angeendelea kusimama hapo, angeangukiwa na tawi hilo. Alinipa anwani yake, nami nikapanga dada fulani amtembelee. Mwanamke huyo, mwana wake, na binti-mkwe wake walibatizwa mwaka wa 1987.”

WANAWAPENDA WATU BADALA YA RAHA

Vijana wengine wengi kutoka sehemu mbalimbali za Muungano wa Sovieti walihamia Latvia kusaidia kazi. Maisha yao hayakuwa rahisi, lakini walikuwa tayari kujidhabihu. Kwa mfano, Anna Batnya, ambaye sasa ni painia wa pekee, alipata kazi katika kiwanda cha kushona na makao katika bweni fulani. Anasema: “Hali zilikuwa ngumu sana. Tulihubiri isivyo rasmi katika magari-moshi, vituo vya magari-moshi, mabustani, makaburi, na karibu na makanisa.

“Katika magari-moshi, ambayo yalijaa nyakati zote, tulihubiri behewa kwa behewa tukiwa wawili-wawili. Mmoja wetu alihubiri huku yule mwingine akiwa macho. Mara nyingi watu waliokuwa karibu walishiriki mazungumzo. Nyakati nyingine tulirushiwa maswali kutoka kila upande. Gari-moshi liliposimama, tulihamia behewa lingine, ikiwa lazima. Tulifurahia sana kuona Yehova akibariki huduma yetu.”

Angelina Tsvetkova alisikia kweli kwa mara ya kwanza baada ya kusali kanisani. Anasema hivi: “Mwaka wa 1984, Shahidi wa Yehova anayeitwa Aldona Dron̗uka alinijia na kuniuliza ikiwa nimewahi kusoma Biblia. Nikamjibu: ‘Nimesoma sehemu fulani lakini siielewi vizuri, nami nina maswali mengi.’ Tulipeana anwani zetu na kuzungumzia Neno la Mungu kwa ukawaida. Miezi michache baadaye, Aldona alinialika kwenye sherehe ya ndoa huko Lithuania, nami nikakubali kwenda. Watu wapatao 300 walihudhuria. Kwenye karamu, tulisikiliza hotuba za Biblia, na hilo lilinishangaza kidogo.

“Huko ndiko nilikogundua kwamba nimekuwa nikijifunza na Mashahidi wa Yehova na kwamba sherehe hiyo ni kusanyiko pia! Niliguswa moyo na upendo na umoja wa watu hao wanyenyekevu. Nilibatizwa mwaka wa 1985 na kuanza upainia mwaka wa 1994. Sasa, watano kati ya watoto wangu sita wamebatizwa, na yule mdogo ni mhubiri ambaye hajabatizwa.”

UHURU WA KUHUDHURIA MAKUSANYIKO MAKUBWA

Katikati ya miaka ya 1980, vizuizi vingi viliondolewa katika nchi nyingi za Ukomunisti, na Mashahidi wa Yehova wakakutana waziwazi zaidi. Mwaka wa 1989, wajumbe 50 hivi kutoka Latvia walihudhuria Kusanyiko la Wilaya la “Ujitoaji Kimungu” nchini Poland. Marija Andrišaka, ambaye sasa ni painia wa pekee anasema: “Kuwa pamoja na ndugu na dada wote hao kulinisaidia sana kukua kiroho.”

Mwaka wa 1990, wajumbe zaidi ya 50 kutoka Latvia walihudhuria Kusanyiko la “Lugha Iliyo Safi” lililofanyiwa Poland tena. Mmoja wao, Anna Mančinska, alijitahidi juu chini kuhudhuria. Anakumbuka hivi: “Nilipokuwa nikienda kwenye kituo cha gari-moshi, niligundua nimesahau hati zinazohitajiwa mpakani. Basi, nikakodi gari linirudishe nyumbani, nikachukua hati hizo, kisha nikarudi kituoni, lakini gari-moshi lilikuwa limeondoka. Nilienda haraka kwenye kituo kinachofuata, lakini nikachelewa. Kwa hiyo, nikasafiri kwa gari nililokuwa nimekodi mpaka Lithuania na mwishowe nikalifikia gari-moshi likiwa umbali wa kilomita 250 kutoka Riga. Ingawa nililipa pesa nyingi kwa kukodi gari hilo, sijuti hata kidogo!” Sasa Anna ni mshiriki wa familia ya Betheli ya Latvia.

Mwishowe, katika mwaka wa 1991, akina ndugu waliruhusiwa kufanya makusanyiko waziwazi katika maeneo ambayo zamani yalikuwa jamhuri za Sovieti. Wajumbe kutoka Latvia walisafiri kwa mabasi kadhaa mpaka Tallinn, Estonia, ili wahudhurie Kusanyiko la “Wapendao Uhuru wa Kimungu.” Kichwa hicho kilifaa kama nini!

Ruta Barakauska kutoka Vain̗ode, alimsihi mume wake, Ādolfs, ambaye si Shahidi, aandamane naye kwenda Tallinn. “Sikukusudia kuhudhuria kusanyiko hilo,” asema Ādolfs. “Nilitaka tu kununua vifaa vya kurekebisha gari langu. Lakini baada ya kuhudhuria kipindi cha kwanza, nilivutiwa sana na hotuba, urafiki wa Mashahidi wa Yehova, usemi wao safi, na upendo walioonyeshana hivi kwamba nilihudhuria kusanyiko lote. Niliporudi nyumbani, nilianza kujifunza Biblia na kujaribu sana kuzuia hasira. Mwaka wa 1992, nilijiunga na mke wangu kuwa Shahidi wa Yehova aliyebatizwa.”

Mapema katika miaka ya 1990, haingewezekana kukodi mahali panapofaa kwa ajili ya makusanyiko ya wilaya nchini Latvia, kwa hiyo akina ndugu walienda hasa Estonia na Lithuania. Kusanyiko la kwanza kufanyiwa nchini Latvia ni lile la “Njia ya Mungu ya Maisha,” lililofanywa mwaka wa 1998 katika jumba kubwa la michezo jijini Riga. Jumba hilo liligawanywa katika sehemu tatu kulingana na lugha: Kilatvia, Kirusi, na Lugha ya Ishara ya Latvia. Baada ya sala ya mwisho, wote walipiga makofi, na wengi wakatokwa na machozi ya furaha, wakimshukuru Yehova kwa tukio hilo la pekee.

KIPINDI CHA ONGEZEKO LA HARAKA

Baada ya enzi ya Ukomunisti, kazi ilisonga mbele haraka nchini Latvia. Kabla ya mwaka wa 1995, Huduma Yetu ya Ufalme haikupatikana katika Kilatvia, kwa hiyo akina ndugu hawakuwa na ustadi sana wa kuhubiri. Hata hivyo, Mashahidi hao walikuwa na bidii. Dace Šk̗ipsna anasimulia jinsi alivyopata kweli kwa mara ya kwanza: “Mwaka wa 1991, nilinunua kitabu kinachozungumzia moto wa mateso na maisha baada ya kifo katika kibanda kilichokuwa kando ya barabara. Baada ya kutembea hatua chache tu nilisikia sauti kutoka nyuma ikisema, ‘Umenunua sumu!’

“Niliposikia maneno hayo, nilisimama mara moja. Mashahidi wawili wa Yehova, mume na mke, walijitambulisha, kisha tukazungumzia Biblia. Tulizungumzia karibu mambo yote: Hadesi, Gehena, Krismasi, msalaba, na mwishowe, siku za mwisho! Lazima nikubali kwamba sikuelewa mambo mengine, lakini nilifurahia yale niliyoyasikia. Tulipeana namba za simu, na kwa majuma machache yaliyofuata, wenzi hao Mashahidi walijibu mengi ya maswali yangu ya Biblia.”

“NINAFURAHI KWAMBA SIKURUDI NYUMA”

Jānis Folkmanis alikuwa bingwa wa Muungano wa Sovieti katika mchezo wa kuinua uzani, na katika mashindano ya mwisho aliyoshiriki, mnamo Machi 1993, akawa bingwa wa Latvia. Jānis anasema: “Mwaka wa 1992, mfanyakazi mwenzangu, Jānis Cielavs, alinialika nihudhurie funzo lake la Biblia. Tukio hilo lilibadili maisha yangu. Miezi mitatu baada ya kuwa bingwa wa Latvia katika mchezo wa kuinua uzani, nikawa mhubiri wa Ufalme. Nilibatizwa Agosti 1993. Nilipohubiri katika ukumbi wa kufanyia mazoezi, mwalimu wangu alikasirika. Lakini ninafurahi kwamba sikurudi nyuma. Rafiki zangu Eduards Eihenbaums na Edgars Brancis wataeleza sababu.”

Eduards: “Jānis Folkmanis aliniuliza ikiwa ningependa kujifunza Biblia bila malipo. Nilimjibu, ‘Ikiwa hakuna malipo, tunaweza kuanza sasa hivi.’ Na ikawa hivyo! Mambo niliyojifunza yalipatana na akili, hasa fundisho la ufufuo, ambalo lilipatana na akili kuliko lile fundisho la kwamba nafsi haiwezi kufa. Mke wangu alianza kujifunza pia, nasi tukabatizwa mwaka wa 1995.”

Edgars: “Jānis alihubiri kwa bidii katika ukumbi wa kufanyia mazoezi. Aliniuliza mara nne ikiwa ningependa kujifunza Biblia, na kila mara nilikataa. Lakini nilikubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Wakati huohuo, nilijiuliza, ‘Kwa nini mwanamichezo maarufu kama huyo apendezwe na Biblia?’ Kwa kuwa nilitaka kupata jibu la swali hilo, nilianza kujifunza. Ikawaje? Nilibatizwa mwaka wa 1995 na sasa mimi ni painia wa pekee.”

Wengine walihitaji kuacha mazoea mabaya ili wampendeze Mungu. Kwa mfano, Aivars Jackevičs alikuwa na tatizo la kunywa pombe kupita kiasi. Anasema hivi: “Mwishoni mwa juma kiamsha-kinywa changu kilikuwa pombe na chupa moja ya vodka. Jioni moja ya Januari 1992, nilikuwa nyumbani nikiwa nimefungwa bendeji mkononi. Nilikuwa nimeshuka moyo sana nikifikiria kujiua. Vilevile mtu fulani alikuwa ameniibia nilipokuwa nimelewa. Kisha nikasikia mlango ukibishwa. Kumbe ni jirani yangu, yuleyule aliyekuwa amezungumza nami kuhusu Biblia mara kadhaa. Tulizungumza, akaniuliza ikiwa ningependa kujifunza Biblia, nami nikakubali.

“Siku za funzo, sikunywa pombe, na hilo lilinisaidia kufanya maendeleo. Baada ya kujifunza ukweli kuhusu hali ya wafu na kwamba sitaungua katika moto wa mateso, jambo ambalo niliogopa sana, nilianza kujifunza mara tatu kwa juma. Baada ya miezi minne hivi, nikawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Hata hivyo, Biblia inatuonya hivi, ‘Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.’ Kwa upumbavu, jioni moja nilishirikiana na mashirika mabaya, nikanywa kupita kiasi, na kwa mara nyingine nikafikiria kujiua. Lakini Yehova ni mwenye rehema na mwenye subira, na ndugu fulani wenye upendo walikuja kunisaidia. Nilijifunza somo kubwa! Mwaka wa 1992, nilibatizwa, na leo mimi ni mshiriki wa familia ya Betheli ya Latvia.”—1 Kor. 10:12; Zab. 130:3, 4.

Māris Krūmin̗š, ambaye pia anatumika Betheli, alihitaji kufanya mabadiliko makubwa maishani ili amtumikie Yehova. “Baada ya kutumikia jeshini,” anasema Māris, “nilikosa mwelekeo maishani. Baadaye, nilifukuzwa chuoni kwa kukosa mihadhara fulani. Kwa sababu sikuwa na kusudi maishani, niliingilia uhalifu, na jioni moja baada ya kusababisha fujo nikiwa mlevi, nikakamatwa. Nikiwa gerezani, nilifikiria sheria ambazo nilikuwa nimevunja, nami nikagundua kwamba nyingi zinatokana na sheria za Mungu. Kwa mara ya kwanza maishani, nilimwomba Mungu msamaha na kuahidi kwamba nitamtafuta.

“Baada ya kuachiliwa kutoka gerezani, nilienda katika makanisa mbalimbali lakini kila mara nilitamaushwa. Hivyo, nilianza kusoma Biblia na vitabu vingine vya dini. Mwaka wa 1990, nilipokuwa ndani ya gari-moshi, nilikutana na mtu ambaye tulikuwa tumesomea shule moja, naye akanieleza kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Katika safari hiyo fupi, Yehova alifungua moyo wangu nilipokuwa nikimsikiliza rafiki yangu wa zamani akinieleza kusudi la Mungu kwa wanadamu na sababu ya mateso yaliyo ulimwenguni. Nilianza kujifunza, kisha nikawa mhubiri mwaka wa 1991. Nilibatizwa 1992. Mwaka mmoja baadaye, nikawa mshiriki wa familia ya Betheli ya Latvia, na mwaka wa 1995 nikamwoa Simona, painia kutoka Finland.”

Edgars Endzelis alikuwa akisomea sheria. Edgars anasema: “Mapema katika miaka ya 1990, watu wengi walitazamia mabadiliko ya kisiasa. Nilikuwa katika shule ya sheria jijini Riga, na wanafunzi wengi walikuwa wakizungumzia kusudi la uhai. Nilisoma vitabu vya falsafa na dini za Mashariki. Pia nilicheza mchezo fulani wa mieleka unaoitwa aikido. Kisha mimi na mke wangu, Elita, tukakutana na Mashahidi wa Yehova.

“Kwenye mkutano wetu wa kwanza, akina ndugu wanaozungumza Kilatvia na Kirusi walitukaribisha kwa moyo mkunjufu. Upendo huo wa kweli ulituvutia sana. Karibu wakati huohuo, nilishangaa wakati mwalimu wetu wa mieleka aliposema kwamba wafuasi wa Ubudha wa Zen ndio tu wanaoweza kuwa mabingwa wa aikido. Sikufuatilia tena mchezo huo! Muda mfupi baadaye, nilikata nywele zangu ndefu, na mnamo Machi 1993, mimi na Elita tukabatizwa. Tangu wakati huo, nimekuwa na pendeleo la kutumia ujuzi wangu wa sheria kusaidia ‘kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema’ nchini Latvia.”—Flp. 1:7.

IMANI YA KIKRISTO INAJARIBIWA

Mwaka wa 1993, imani ya wanafunzi wanne wa muziki jijini Jelgava ilijaribiwa wakati kwaya yao ilipoagizwa kuimba katika sherehe ya Siku ya Uhuru. Ingawa walikuwa wapya katika kweli, wasichana hao waliazimia kumpendeza Mungu. Kwa hiyo, walimwandikia msimamizi wa kwaya na kumwomba kwa heshima awaruhusu wasihudhurie maadhimisho hayo kwa sababu ya dhamiri yao ya Kikristo. Msimamizi huyo alitendaje? Aliwaandikia wazazi wa wasichana hao barua yenye masharti makali, akisema kwamba wanafunzi hao watafukuzwa shuleni wasipoimba. Sawa na wale Waebrania watatu, wasichana hao walimtii Yehova.—Dan. 3:14, 15, 17; Mdo. 5:29.

Mmoja wa wasichana hao ni Dace Puncule. Anakumbuka hivi: “Kusali kwa Mungu na msaada wa akina ndugu ulitusaidia kuendelea kuwa waaminifu. Tulifukuzwa, lakini sijuti kamwe kwamba nilisimama imara kwa ajili ya kweli. Kusema kweli, Yehova amenitunza sana. Baada ya miezi kadhaa, nilipata kazi katika ofisi ya sheria, na uzoefu niliopata huko ulinisaidia baadaye Betheli, ambako nimetumika tangu 2001.”

Utimilifu wa wengine umejaribiwa kuhusiana na suala la damu. Mnamo Septemba 6, 1996, msichana mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Yelena Godlevskaya aligongwa na gari na kuvunjika sehemu kadhaa za mfupa wa nyonga. Kutokana na ukomavu wake wa kiroho, Yelena aliazimia moyoni kujiepusha na damu. (Mdo. 15:29) Wakati huo, madaktari wengi nchini Latvia hawakujua mbinu za kuwatibu wagonjwa bila damu, kwa hiyo madaktari waliomshughulikia walikataa kumfanyia upasuaji. Kisha, usiku fulani karibu juma moja baadaye, madaktari wawili walimtia Yelena damu kwa lazima na kwa ukatili, naye akafa.

Wakati huo Marina, mama ya Yelena, hakuwa Shahidi. Marina anasema: “Nilishangaa kuona jinsi binti yangu alivyomwamini sana Yehova na ahadi zake. Alikataa katakata.” Sasa Marina amebatizwa, naye na familia yake wanatazamia kumkumbatia Yelena wakati wa ufufuo.—Mdo. 24:15.

WANAUME WAKOMAVU KIROHO WATIMIZA UHITAJI MUHIMU

Kwa sababu ya ongezeko la haraka katika idadi ya wahubiri, wanaume wakomavu kiroho wanahitajiwa kuongoza. Mwaka wa 1992, ndugu watatu wanaozungumza Kilatvia, ambao walilelewa Marekani, walipata pendeleo la kutumikia wakiwa wamishonari nchini Latvia. Majina yao na ya wake zao ni Valdis na Linda Purin̗š, Alfreds na Doris Elksnis, na Ivars Elksnis, ndugu ya Alfreds. Wote watano walifika Riga Julai 1992. Nyumba yao yenye vyumba vinne ilitumiwa kama makao ya wamishonari, depo ya vichapo, na ofisi ya kutafsiri.

Ucheshi humsaidia mtu anapojifunza lugha nyingine. Doris Elksnis anasema: “Nilipokuwa nikijifunza pamoja na wasichana wawili, nilijaribu kueleza jinsi Shetani alivyoongea na Hawa kwa kutumia nyoka. Lakini, nilitumia neno la Kilatvia linalotamkwa sawa na neno ‘nyoka.’ Hata hivyo, nilisema kwamba Ibilisi alizungumza kupitia nguruwe!”

Mwaka wa 1994, Peter na Jean Luters walifika kutoka Australia. Peter, ambaye alibatizwa 1954, alizaliwa Latvia lakini akalelewa Australia. Kwa kuhuzunisha, Jean, ambaye alipata marafiki haraka kwa sababu ya kuwa mwenye upendo na fadhili, alikufa 1999. Peter aliamua kukaa Latvia na sasa anatumika katika Halmashauri ya Tawi. Peter anasema: “Tulipofika, tulipata kwamba akina ndugu Walatvia ni wahubiri wenye bidii. Lakini makutaniko hayakuwa yamegawiwa eneo hususa, na sehemu fulani za Riga hazikuwa zikihubiriwa. Pia, ni makutaniko machache tu yaliyopangia hotuba za watu wote kwa ukawaida. Mambo yote hayo yalishughulikiwa haraka.”

MSAADA WA WAHITIMU WA GILEADI

Wamishonari wa kwanza kuzoezwa Gileadi walifika mapema mwaka wa 1993. Wenzi wa ndoa kutoka Sweden, Anders na Agneta Berglund na Torgny na Lena Fridlund walipewa mgawo wa kutumika Jelgava, jiji lenye wakaaji zaidi ya 60,000 na wahubiri 28. Anders, ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, anasema: “Tulipofika, tulijiunga na akina ndugu katika utumishi wa shambani, na sikuzote tulikuwa na mengi ya kufanya katika huduma! Siku fulani-fulani, kwa muda wa saa saba au nane, ni kana kwamba tulikuwa tukikimbia pamoja nao kutoka funzo moja hadi lingine bila kupumzika ili kula! Bidii yao ilituchochea. Sasa, wengi wa wanafunzi hao ni watumishi wa wakati wote.”

Torgny Fridlund anakumbuka hivi: “Baada ya kufundishwa lugha kwa miezi mitatu, tuliona kwamba tunaweza kuzungumza bila msaada. Tulichagua eneo ambalo halikuwa limehubiriwa tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, lakini hatukufanikiwa sana. Je, tulitumia mbinu zisizofaa? Baada ya kuzungumzia jambo hilo, tulijaribu mbinu nyingine, yaani, kusoma andiko kwenye kila mlango. Tangu wakati huo, tukaanzisha mafunzo kadhaa.”

Wahitimu zaidi wa Gileadi walianza kufika Aprili 1995. Hao ni kutia ndani Basse na Heidi Bergman kutoka Finland, ambao sasa wanafanya kazi ya kusafiri katika mzunguko wa Kirusi. Basse anasema: “Niliwaomba ndugu wa eneo hilo wanisahihishe ninapokosea katika huduma. Walifanya hivyo kwa bidii, nao wakanisahihisha shambani na hata mikutano ikiendelea! Siku hizi, mimi hufurahi kusikia ndugu wakisema, ‘Basse amekuwa mmoja wetu.’”

Carsten na Jannie Ejstrup, kutoka Denmark, walitumika pamoja nchini Latvia mpaka Jannie alipokufa kutokana na kansa akiwa tu na miaka 30 na kitu. Carsten anasema: “Njia bora ya kumheshimu Yehova ni kuendelea kuwa mwaminifu katika mgawo wangu wa umishonari.” Ndugu hao ni mfano bora kwelikweli!

WAHITIMU WA SHULE YA MAZOEZI YA KIHUDUMA WAFIKA

Kuanzia 1994, zaidi ya wahitimu 20 wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kutoka Uingereza, Ujerumani, na Poland, walitumwa Latvia. Wa kwanza kufika ni Michael Udsen na Jess Kjaer Nielsen kutoka Denmark. Walitumwa kwenye jiji lenye viwanda la Daugavpils, la pili kwa ukubwa nchini Latvia.

Jess anasema: “Alasiri moja yenye baridi katika mwezi wa Januari, tulifunga safari ya kwenda Daugavpils, kilomita 240 hivi kusini-mashariki mwa Riga. Theluji ilikuwa ikimwagika huko Riga tulipopanda gari letu, lililokuwa zee na lililojaa vichapo. Ndugu ambaye aliendesha gari hilo hakujua Kiingereza hata kidogo, nasi hatukujua Kilatvia wala Kirusi. Baada ya karibu kila kilomita 50, alisimamisha gari na kuchokora-chokora injini. Tunachojua ni kwamba hakuwa akirekebisha kifaa cha kupasha joto, kwa kuwa kulikuwa na baridi kali ndani ya gari kama ilivyokuwa nje! Baada ya safari hiyo ya kurushwa-rushwa, tulifika Daugavpils karibu usiku wa manane. Wakati huo, kulikuwa na wahubiri 16 katika jiji hilo. Kufikia mwishoni mwa mwaka uliofuata, idadi hiyo ilikuwa imeongezeka karibu mara mbili.”

KUTAFSIRI KATIKA KILATVIA

Kabla ya 1992, vichapo vilipatikana hasa katika Kirusi, ambacho Walatvia wengi walikijua. Hata hivyo, wengi walipendelea lugha yao ya kienyeji. “Kwa kupendeza,” kulingana na ripoti moja, “miongoni mwa mamia ya wahubiri hao wapya kulikuwa na wale wanaoweza kutafsiri, nasi tuliona roho takatifu ya Mungu ikielekeza kazi ya ndugu na dada hao vijana waliojitoa kwa hiari.”

Kwa sababu ya bidii ya watafsiri hao, mnamo Januari 1995 gazeti la Mnara wa Mlinzi lilianza kuchapishwa mara moja kwa mwezi katika Kilatvia, kisha likaanza kuchapishwa mara mbili kwa mwezi Januari 1996. Sasa kuna vichapo vingine vya Kilatvia, vitabu na broshua kadhaa, na gazeti la Amkeni!

Mapema mwaka wa 1993, watafsiri walihama ile ofisi ndogo katika makao ya wamishonari huko Riga na kuingia nyumba iliyo kwenye Barabara ya Brīvības. Kisha, Agosti 1994, walihamia ofisi zilizorekebishwa kwenye Barabara ya 40 Miera. Akina ndugu walipataje ofisi hizo?

ZAWADI

George Hakmanis na mke wake, Sigrid, waliondoka Latvia wakiwa wakimbizi wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wenzi hao walijifunza kweli London, Uingereza, na kubatizwa mwaka wa 1951. Mwaka uliofuata, walihamia Marekani, na mwaka wa 1992 wakarudi Latvia kwa miaka mitano.

Baada ya Latvia kujiondoa kwenye Muungano wa Sovieti mwaka wa 1991, watu wangeweza kudai haki ya kumiliki tena mali yao iliyochukuliwa na serikali. Kwa kuwa Sigrid na dada yake, ambaye pia ni Shahidi, walihifadhi hati za familia yao kwa miaka zaidi ya 50, walifaulu kurudishiwa mali yao iliyokuwa kwenye Barabara ya 40 Miera. Kisha, wakaitoa iwe mali ya tengenezo la Yehova. Halafu akina ndugu wakakarabati jengo lililokuwapo likawa kituo cha kutafsiri chenye orofa tano na makao ya watu 20.

Milton G. Henschel wa Baraza Linaloongoza alihudhuria kuwekwa wakfu kwa jengo hilo mnamo Agosti 20, 1994. Alipokuwa huko, aliwashauri akina ndugu wanunue uwanja ulioko kwenye Barabara ya 42 Miera, ambao unapakana na ofisi hiyo. Uwanja huo ulikuwa na jengo la orofa sita. Mwenyewe, anayeishi Marekani, alikubali kuuza uwanja huo. Jengo hilo pia lilirekebishwa kabisa, na familia ya Betheli ikaongezeka kufikia watu 35. Tangu wakati huo, upanuzi zaidi umefanywa na sasa kuna ofisi na vyumba zaidi kwa ajili ya Wanabetheli 55.

KUTAMBULIWA KISHERIA

Bado kuna ugumu wa kusajili kazi nchini Latvia. Mwaka wa 1996, maofisa walitumia maelezo yasiyofaa ya waandishi wa habari kuhusu Yelena Godlevskaya kuwa msingi wa kukataa kutusajili. Hata mbunge mmoja alidokeza kwamba huenda kazi yetu ikapigwa marufuku! Lakini akina ndugu waliendelea kukutana na maofisa na kuwaeleza kuhusu kazi yetu. Mwishowe, Oktoba 12, 1998, mkurugenzi wa Ofisi ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu alitangaza kwamba makutaniko mawili, yaani, Riga Center and Riga Torn̗akalns, yamesajiliwa kwa kipindi cha majaribio cha mwaka mmoja. Mwezi mmoja baadaye, kutaniko lililo Jelgava lilisajiliwa pia.

Kulingana na sheria za Latvia, makutaniko mapya yanapaswa kusajiliwa upya kila mwaka. Ili kupata usajili wa kudumu, makutaniko angalau kumi yanapaswa kusajiliwa kila mwaka kwa muda wa miaka kumi. Katika kipindi hicho, makutaniko yanayosubiri kusajiliwa yanaweza kukutanika bila kusumbuliwa na serikali.

KUPATA MAHALI PA KUKUTANIA

Kutokana na ongezeko la haraka katika miaka ya 1990, majumba makubwa zaidi yalihitajiwa kwa ajili ya mikutano. Mwaka wa 1997, jengo fulani linalofaa lilipigwa mnada huko Daugavpils, na akina ndugu tu ndio waliotaka kulinunua. Kazi ya kulirekebisha ilianza Desemba 1998, na miezi minane baadaye, wahubiri zaidi ya 140 wa jiji hilo walifurahia kukusanyika katika Jumba lao wenyewe la Ufalme.

Jumba la Ufalme la kwanza kujengwa toka mwanzo mpaka mwisho lilikamilishwa huko Jūrmala mwaka wa 1997. Mwanafunzi mmoja wa Biblia wa eneo hilo alifurahishwa sana na ubora wa kazi iliyofanywa hivi kwamba akawaomba Mashahidi wamjengee nyumba! Akina ndugu walimwambia haitawezekana na kwamba hatufanyi biashara bali kazi yetu ni ya kidini. Wakati huohuo, ndugu katika eneo la Torn̗akalns huko Riga waliuziwa kwa bei nafuu jumba la sinema lililoungua. Kufikia Agosti 1998, jengo hilo lililokuwa limeungua lilibadilishwa kuwa Majumba mawili maridadi ya Ufalme!

MSAADA KUTOKA FINLAND

Akina ndugu huko Finland wamefanya mengi ili kuendeleza kazi nchini Latvia, hata kwa kusimamia kazi kuanzia 1992 mpaka 2004. Pia, magazeti yote yanayotumiwa Latvia yanachapishiwa Finland, na kwa miaka mingi ndugu wengi wenye ustadi kutoka nchi hiyo wametumiwa kuelekeza kazi. Wanatia ndani Juha Huttunen na mke wake, Taina, ambao walikuja Latvia mwaka wa 1995. Sasa Juha anatumika katika Halmashauri ya Tawi. Pia, Ruben na Ulla Lindh, ambao kwa jumla wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 80, walisaidia sana kazi. Ndugu Lindh alitumikia katika Halmashauri ya Nchi ya Latvia kwa miaka minne kabla ya kurudi Finland.

Kwa kuongezea, zaidi ya ndugu 150 kutoka Finland wamesaidia katika miradi mbalimbali ya ujenzi. Kutokana na kazi zote hizo za upendo na baraka nyingi za Yehova juu ya huduma ya wahubiri, mapainia, na wamishonari nchini Latvia, nchi hiyo ilipata kuwa ofisi ya tawi Septemba 1, 2004.

KAMPENI ZA PEKEE ZA KUHUBIRI

Wahubiri wengi nchini Latvia wanaishi karibu na majiji na miji mikubwa. Mapema katika mwaka wa 2001, makutaniko yalipokea barua iliyowaalika wahubiri watumie muda fulani wa likizo yao kushiriki kampeni ya pekee ya kuhubiri katika maeneo ya mbali. Wahubiri 93 waliojitolea waligawanywa katika vikundi tisa na kutumwa katika miji na vijiji vya mashambani.

Vjačeslavs Zaicevs, mshiriki wa familia ya Betheli, alichukua likizo ili ashiriki kampeni hiyo. “Hiyo ilikuwa pindi nzuri ya kuwajua vizuri ndugu na dada wengine,” anasema. “Baada ya kuhubiri, tulikula pamoja, tukasimulia mambo yaliyoonwa, na kupangia siku iliyofuata. Kisha tukacheza kandanda na kuogelea katika ziwa. Tulionja Paradiso.”

Akina ndugu walitumia saa zaidi ya 4,200 katika huduma—wastani wa saa zaidi ya 41 kwa kila mhubiri—nao wakagawa vichapo zaidi ya 9,800, wakafanya ziara za kurudia 1,625, na kuongoza mafunzo ya Biblia 227. Tangu wakati huo, kampeni kama hizo zimepangwa kila mwaka.

WENGI WANAPATA UHURU WA KWELI

Masimulizi yetu yalianza kwa maneno ya Ans Insberg, Mlatvia aliyemmiminia Mungu moyo wake alipokuwa baharini usiku mmoja wenye nyota nyingi. Ans alitaka kuwapata watu wanaomwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:24) Yehova alisikia maombi hayo ya unyoofu. Tangu wakati huo, watu zaidi ya 2,400 wenye mioyo minyoofu nchini Latvia wamepata ujuzi wa kweli ya kiroho, na wengine wengi wanajifunza Biblia. Naam, bado kazi ni nyingi!—Mt. 9:37, 38.

Mashahidi wa Yehova nchini Latvia wanatamani sana kuwasaidia wote wanaotafuta uhuru wa kweli, si kwa kuwaelekeza kwa jambo linalowakilishwa na ule Mnara wa Ukumbusho wa Uhuru kwenye Barabara ya Brīvības, bali kwa kuwaelekeza kwenye Ufalme wa Mungu. Hivi karibuni, wote wanaotazamia kwa hamu Ufalme huo na kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli” watakuwa huru, bila maumivu na mateso ya aina zote. Naam, watapata uhuru kamili, “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:21.

[Maelezo ya Chini]

a Masimulizi ya maisha ya Yurii Kaptola yalichapishwa katika Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 2005.

[Blabu katika ukurasa wa 190]

“Sitasahau kamwe siku niliyobatizwa. Nilibatizwa usiku sana katika mto wenye maji baridi kama barafu. Nilitetemeka sana kwa sababu ya baridi, lakini nilifurahi sana.”

[Blabu katika ukurasa wa 203]

“Nilisikia sauti kutoka nyuma ikisema, ‘Umenunua sumu!’”

[Picha katika ukurasa wa 184, 185]

MAELEZO MAFUPI KUHUSU Latvia

Nchi

Latvia ina ukubwa wa kilomita 450 kutoka mashariki hadi magharibi na kilomita 210 kutoka kaskazini hadi kusini. Asilimia 45 hivi ya nchi hiyo ni misitu. Kuna wanyama kama vile buku, fisi-maji, kulungu, mbwa-mwitu, nguruwe-mwitu, paa, paka-mwitu, na sili. Pia, kuna ndege wengi kama vile kigogota, kinega, korongo-mweusi, na kulasitara.

Watu

Zaidi ya theluthi moja ya wakaaji milioni 2.3, wanaishi Riga, jiji kuu la nchi hiyo. Dini kuu ni dini ya Lutheri, Katoliki, na Othodoksi ya Urusi. Hata hivyo, Walatvia wengi hawafuati dini.

Lugha

Lugha kuu zinazozungumzwa ni Kilatvia, kinachozungumzwa na asilimia 60 hivi ya watu, na Kirusi, kinachozungumzwa na zaidi ya asilimia 30. Wengi wanazungumza zaidi ya lugha moja.

Kazi

Karibu asilimia 60 ya watu wanafanya biashara mbalimbali, na wale wengine wanafanya kazi ya kilimo na katika viwanda.

Chakula

Mazao yanatia ndani nafaka, shayiri, viazi, viazi-sukari, na mboga nyingine mbalimbali. Mifugo inatia ndani kondoo, mbuzi, ng’ombe, na nguruwe. Wengi wanapenda kufuga kuku pia.

Hali ya Hewa

Kuna unyevu mwingi, na kwa kawaida anga huwa na mawingu. Joto si jingi katika majira ya kiangazi, na katika majira ya baridi kali, baridi haiwi kali mno.

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ESTONIA

RUSSIA

LATVIA

Valmiera

RIGA

Jūrmala

Sloka

Tukums

Ventspils

Kuldīga

Liepaja

Vain̗ode

Jelgava

Daugavpils

LITHUANIA

BAHARI YA BALTIKI

Ghuba la Riga

[Picha]

Riga

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 186]

Maeneo Manne ya Latvia

Kwa ujumla, Latvia imegawanyika katika maeneo manne ya kijiografia na kitamaduni, kila moja la maeneo hayo likiwa na maumbile yake yenyewe yenye kupendeza. Karibu na Ghuba ya Riga, kuna eneo la Vidzeme, ambalo ndilo eneo kubwa zaidi. Huko ndiko iliko miji ya Sigulda na Cēsis, hali kadhalika Riga, jiji kuu la Latvia. Sigulda na Cēsis ni miji tajiri ya kihistoria yenye makasri mengi. Upande wa mashariki mna nyanda za chini za maziwa ya bluu yaliyo katika eneo la Latgale, na vilevile Daugavpils, jiji la pili kwa ukubwa nchini. Eneo la Zemgale ndilo hukuza nafaka kwa wingi, nalo liko kusini mwa Mto Western Daugava, unaotiririka kutoka Belarus kupitia Latvia hadi Ghuba ya Riga. Eneo hilo lina ikulu mbili zilizobuniwa na msanifu-majengo Mwitaliano anayeitwa Rastrelli ambaye pia alibuni Ikulu ya Majira ya Baridi Kali huko St. Petersburg, Urusi. Kurzeme, eneo la nne, lina mashamba, misitu, na fukwe. Pia, eneo hilo linatia ndani Pwani ya Baltiki, majiji ya Ventspils na Liepaja, na vijiji vingi vinavyotegemea uvuvi.

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

1 VIDZEME

2 LATGALE

3 ZEMGALE

4 KURZEME

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 192, 193]

Kumhubiria Kasisi Kulibadili Maisha Yangu na Yake

ANNA BATNYA

ALIZALIWA 1958

ALIBATIZWA 1977

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Akiwa amelelewa katika familia ya Kikristo huko Ukrainia, amesaidia watu zaidi ya 30 kufikia ubatizo, na sasa ni painia wa pekee.

NILIPOSIKIA kwamba kuna uhitaji wa wahubiri nchini Latvia, nilihamia huko mwaka wa 1986. Hatukuweza kuhubiri waziwazi, kwa hiyo niliificha Biblia yangu katika kikapu na kuwaendea watu waliokuwa katika mabustani na sehemu nyingine za umma. Tulikazia tumaini la Ufalme na kutumia Biblia wakati tu mtu anapopendezwa. Kwa kuwa waliwaogopa watu wa ukoo au majirani, mara nyingi watu hawakutukaribisha nyumbani kwao, kwa hiyo kwa kawaida tulijifunza na watu mahali tulipowakuta.

Vichapo havikupatikana kwa urahisi. Kwa miaka kadhaa, kutaniko letu lilikuwa na nakala moja tu ya kitabu cha kujifunzia Biblia, Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, katika Kirusi. Tulikitumia vizuri kitabu hicho shambani, hata hivyo, hatukumruhusu yeyote aende nacho!

Tulipokuwa tukihubiri karibu na kanisa moja, mimi na mwenzangu tulikutana na kasisi anayeitwa Pyotr Batnya. Ili kuanzisha mazungumzo naye, tulimwomba atuonyeshe ni wapi tunapoweza kuinunua Biblia. “Mimi pia naipenda Biblia,” akajibu. Kisha, tukawa na mazungumzo mazuri sana. Siku iliyofuata, tulikutana na Pyotr katika bustani iliyokuwa karibu, tukamwonyesha habari zilizomo katika kitabu Kweli, na kumuuliza habari ambayo angependa kuzungumzia. Alichagua kichwa, “Desturi Zinazopendwa na Watu Wengi Zinazomchukiza Mungu.” Mazungumzo hayo yalikuwa na matokeo na mwishowe ndugu fulani akaanza kujifunza naye Biblia kwa ukawaida.

Akiwa na ujuzi sahihi wa Biblia, Pyotr alianza kuwauliza makasisi wenzake maswali, naye akagundua kwamba hawakuweza kueleza hata mafundisho ya msingi ya Biblia! Punde baadaye, Pyotr alijiuzulu kutoka kanisani, akajiweka wakfu kwa Yehova.

Mwaka wa 1991, mimi na Pyotr tulioana, kisha tukawa mapainia. Inahuzunisha kwamba alikufa katika msiba wa barabarani miaka michache baadaye. Ni nini ambacho kimenisaidia kuvumilia hali hiyo? Kujishughulisha sana na huduma, nikiwasaidia wengine wamjue “Mungu wa faraja yote.” (2 Kor. 1:3, 4) Mwaka wa 1997, nilipata pendeleo la kuwa painia wa pekee.

[Picha]

Pyotr

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 200, 201]

Nilitamani Serikali ya Haki

INDRA REITUPE

ALIZALIWA 1966

ALIBATIZWA 1989

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa Mkomunisti awali. Alianza upainia mwaka wa 1990, naye amewasaidia watu zaidi ya 30 kufikia ubatizo.

NILIPOKUWA nikikua, sikumwamini Mungu wala Biblia. Hata hivyo, sikuzote nilijitahidi kutetea lililo haki nami sikuelewa kamwe kwa nini wanadamu wameshindwa kabisa kusimamisha serikali nzuri na ya haki.

Nilipokutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, nilishangazwa na mambo waliyonionyesha katika Biblia. Maneno yao yalipatana na akili! Mambo niliyojifunza kuhusu Ufalme wa Mungu na haki ambayo Yesu alikazia yaliuchochea sana moyo wangu. Mwaka wa 1989, nilibatizwa katika ziwa, na miezi sita baadaye nikaanza kutumikia nikiwa painia wa kawaida. Wakati huo, mimi na mume wangu tulikuwa na mtoto mmoja. Baadaye, tukapata mapacha. Mume wangu, Ivan, ambaye pia ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, amenitegemeza kwa upendo, nami nimeweza kuendelea katika utumishi wa wakati wote.

Watoto walipokuwa wadogo, mara nyingi nilishiriki katika mahubiri yasiyo rasmi barabarani na kwenye mabustani. Mapacha hao walifanya iwe rahisi kutoa ushahidi kwa sababu waliwavutia watu na kuwafanya wastarehe zaidi na kutaka kuzungumza nami.

Nilipokuwa nikihubiri katika bustani fulani jijini Riga, nilikutana na mwanamke anayeitwa Anna. Alikuwa ameketi kwenye benchi akisubiri maonyesho fulani yaanze na tayari alikuwa amekata tiketi. Hata hivyo, alikuwa na hamu kubwa ya kujifunza mengi zaidi kuhusu tumaini la Biblia kwa wanadamu hivi kwamba hakwenda kuona maonyesho hayo. Tulisoma maandiko pamoja na kupanga kukutana tena kwenye bustani hiyo. Miezi sita baadaye, Anna (kulia) akawa dada yetu na sasa anatumikia katika ofisi ya tawi akifanya kazi ya kutafsiri. Naam, moyo wangu hujaa shangwe ninapofikiria jinsi ambavyo Yehova amebariki huduma yangu.

[Picha]

Nikiwa pamoja na familia yangu

[Picha katika ukurasa wa 204]

Ni Kana Kwamba Walijua Kilichokuwa Akilini Mwangu

ANDREY GEVLYA

ALIZALIWA 1963

ALIBATIZWA 1990

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Akiwa pamoja na mke wake, Yelena, katika picha. Yeye ni painia, mwangalizi wa mzunguko wa badala, na mwangalizi wa jiji.

NIKIWA katika gari-moshi kuelekea Riga mnamo Januari 1990, wanawake wawili waliniuliza iwapo nimewahi kuisoma Biblia. Ni kana kwamba walijua kilichokuwa akilini mwangu, kwa sababu kwa muda mrefu nilitaka kuisoma Biblia lakini sikuweza kuipata. Nikawapa wanawake hao, mmoja wao alikuwa Indra Reitupe, anwani na namba yangu ya simu. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 200-201.) Siku chache baadaye, walifika kwangu wakanikuta nikiwasubiri kwa hamu. Nilivutiwa kuona jinsi walivyoitumia Biblia kwa ustadi kujibu maswali yangu. Muda mfupi baadaye, Pyotr Batnya, mhudumu wa wakati wote ambaye wakati mmoja alikuwa kasisi, akaanza kujifunza nami Biblia.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 192-193.

Miezi minne baadaye, nilihudhuria mkutano wa kwanza. Wakati wa kiangazi, mikutano ilikuwa ikifanywa msituni mara moja kwa mwezi, kuanzia saa 4:00 asubuhi mpaka saa 12:00 jioni. Akina ndugu walizungumzia sehemu zilizoteuliwa za Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, na kwa kawaida mtu alibatizwa, kwa hiyo tulikuwa na hotuba ya ubatizo kabla ya mapumziko ya mchana.

Ujuzi niliokuwa nimepata na upendo wa kindugu nilioonyeshwa mikutanoni ulinipa shangwe. Nilitaka kubatizwa haraka iwezekanavyo. Tamaa hiyo ilitimizwa mwishoni mwa Agosti mwaka huo, nilipobatizwa katika ziwa.

Mapema katika miaka ya 1990, nilijifunza Biblia na watu kadhaa katika chumba changu cha sanaa. Baadhi yao wakawa ndugu zangu wa kiroho. Katika mwaka wa 1992, Yehova alizidisha shangwe yangu, mke wangu mpendwa Yelena alipojifunza na kuwa dada yangu wa kiroho.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 208]

Kurudi Nyumbani Baada ya Miaka 50

ĀRIJA B. LEIVERS

ALIZALIWA 1926

ALIBATIZWA 1958

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mwenyeji wa Latvia, aliishi katika nchi mbalimbali kabla ya kurudi Latvia kutumikia mahali penye uhitaji zaidi.

WAKATI wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Baba aliamua familia yetu ifunge virago na kuondoka Latvia. Baadaye nikaolewa, nami na mume wangu tukahamia Venezuela. Tukiwa huko nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, nikakubali kujifunza Biblia pamoja na dada mmoja mmishonari. Tulijifunza katika Kijerumani. Nilipoanza kuhudhuria mikutano, nikajifunza Kihispania, lugha rasmi nchini Venezuela.

Mwaka wa 1958, familia yetu ilihamia Marekani, na miezi miwili baadaye nikabatizwa. Baada ya kifo cha mume wangu, mimi na binti yangu tulihamia Hispania, ambako nilifanya upainia. Jenerali Franco alikuwa mtawala wa kimabavu wakati huo, nao watu wanyenyekevu, wanaomwogopa Mungu walikuwa na kiu ya kweli. Kwa miaka 16 ambayo niliishi Hispania, nilikuwa na pendeleo la kuwasaidia watu 30 hivi kufikia ubatizo.

Kufuatia kuanguka kwa Muungano wa Sovieti mwaka wa 1991, nilitembea Latvia nikaona kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme. Tamaa yangu ya kurudi nyumbani kufanya upainia ilitimia mwaka wa 1994—miaka 50 kamili baada ya kuondoka.

Kwa kweli, eneo la Latvia lilikuwa tayari kwa ajili ya mavuno. Kwa mfano, nilimhubiria mtu mmoja aliyeomba kimojawapo cha vitabu vyetu. Mtu huyo alisema kwamba binti yake anapendezwa na mambo ya kiroho, naye anataka kumpa kitabu hicho. Nilichukua anwani ya binti huyo, nikaanza kujifunza Biblia naye, kisha akabatizwa mwaka huohuo. Namshukuru Yehova kwa kunipa pendeleo na nguvu za kufanya upainia nyumbani kwetu baada ya kuwa mbali kwa muda mrefu hivyo.

[Picha]

Nilipokuwa na umri wa miaka 20

[Chati/Grafu katika ukurasa wa 216, 217]

MFUATANO WA MATUKIO—Latvia

1916 Baharia Ans Insberg abatizwa. Baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, aweka matangazo katika magazeti ya Latvia kutangaza Ufalme wa Mungu.

1920

1926 Ofisi yaanzishwa jijini Riga.

1928 Kijitabu Freedom for the Peoples chatolewa, kikiwa kichapo cha kwanza cha sosaiti cha Kilatvia. Makolpota wawasili kutoka Ujerumani.

1931 Percy Dunham awekwa kusimamia ofisi.

1933 Shirika la International Bible Students Association (IBSA) lasajiliwa.

1934 Serikali yafunga ofisi ya IBSA.

Hakuna ripoti zozote za 1939 mpaka 1992.

1940

1940 Latvia yawa sehemu ya Muungano wa Sovieti; Ndugu na Dada Dunham walazimika kuondoka.

1951 Mashahidi wahamishiwa Siberia.

1960

1980

1991 Latvia yapata uhuru wake wa kisiasa.

1993 Wamishonari wa kwanza waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wawasili.

1995 Mnara wa Mlinzi lachapishwa mara moja kwa mwezi katika Kilatvia.

1996 Halmashauri ya Nchi yaundwa jijini Riga.

1997 Jumba la Ufalme jipya la kwanza lajengwa Jūrmala.

1998 Makutaniko mawili jijini Riga yasajiliwa kisheria.

2000

2001 Kampeni ya kwanza ya pekee ya kuhubiri yapangwa.

2004 Septemba 1, Latvia yawa ofisi ya tawi.

2006 Upanuzi wa ofisi ya tawi wamalizika; kuna wahubiri zaidi ya 2,400 watendaji nchini Latvia.

[Grafu]

(See publication)

Jumla ya Wahubiri

Jumla ya Mapainia

2,000

1,000

1920 1940 1960 1980 2000

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 176]

[Picha katika ukurasa wa 178]

Jengo hili ndilo lililokuwa ofisi ya kwanza ya Wanafunzi wa Biblia huko Riga, 1926

[Picha katika ukurasa wa 178]

Kijitabu “Freedom for the Peoples” cha Kilatvia kilikuwa na ujumbe wenye kufurahisha, 1928

[Picha katika ukurasa wa 178]

Rees Taylor

[Picha katika ukurasa wa 180]

Ferdinand Fruck, alibatizwa 1927

[Picha katika ukurasa wa 180]

Heinrich Zech na mke wake, Elsa, mbele ya duka lao huko Liepaja

[Picha katika ukurasa wa 183]

Edwin Ridgewell (kushoto) na Andrew Jack waliingiza vichapo kwa siri nchini Latvia

[Picha katika ukurasa wa 183]

Percy na Madge Dunham

[Picha katika ukurasa wa 183]

Wanabetheli na Mashahidi wengine, miaka ya 1930

[Picha katika ukurasa wa 191]

Orodha ya KGB ya Mashahidi ambao walikamatwa mwaka wa 1950. Wengi wao walihamishiwa Siberia

[Picha katika ukurasa wa 191]

Siberia, mapema katika miaka ya 1950

[Picha katika ukurasa wa 194]

Akina ndugu walisikiliza hotuba za Biblia mahali ambako wengi walikusanyika, kama vile kwenye maziko haya

[Picha katika ukurasa wa 194]

Pauls na Valija Bergmanis walitafsiri “Mnara wa Mlinzi” katika Kilatvia, kwa kuandika katika madaftari ya wanafunzi

[Picha katika ukurasa wa 194]

Kwa kutumia filamu yenye maandishi madogo (picha zinaonyesha ukubwa halisi), akina ndugu walisafisha, kutokeza nakala, na kugawanya “Mnara wa Mlinzi”

[Picha katika ukurasa wa 197]

Paulīne Serova alimweleza kweli kwa mara ya kwanza muuguzi anayeitwa Teofīlija Kalvīte

[Picha katika ukurasa wa 199]

Yurii Kaptola, 1981

[Picha katika ukurasa wa 199]

Leo, akiwa mbele ya gereza alimofungwa

[Picha katika ukurasa wa 202]

Kusanyiko la “Njia ya Mungu ya Maisha” la 1998, la kwanza kufanyiwa Latvia, lilikuwa na sehemu ya lugha ya ishara

[Picha katika ukurasa wa 207]

Miezi mitatu baada ya Jānis Folkmanis kuwa bingwa wa mchezo wa kuinua uzani nchini Latvia, akawa mhubiri wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 207]

Akiwa gerezani, Māris Krūmin̗š alisali kwa Mungu kwa mara ya kwanza

[Picha katika ukurasa wa 210]

Dace Puncule alifukuzwa shuleni kwa kukataa kuimba nyimbo za kitaifa

[Picha katika ukurasa wa 210]

Yelena Godlevskaya alikufa baada ya kutiwa damu mishipani kwa lazima

[Picha katika ukurasa wa 210]

Waangalizi wanaosafiri, na wake zao, wanaimarisha makutaniko

[Picha katika ukurasa wa 215]

Familia ya Betheli ya Latvia

[Picha katika ukurasa wa 215]

Halmashauri ya Tawi, 2006

Peter Luters

Anders Berglund

Hannu Kankaanpää

Juha Huttunen

[Picha katika ukurasa wa 215]

Majengo matatu ya tawi kwenye Barabara ya Miera, Riga

[Picha katika ukurasa wa 218]

Sasa watu wa Yehova nchini Latvia wanaweza kuhubiri waziwazi

[Picha katika ukurasa wa 218]

Jengo hili la sinema lililoungua (kushoto) lilirekebishwa na kuwa Majumba mawili ya Ufalme (chini)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki