Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb07 kur. 222-255
  • Réunion

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Réunion
  • 2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • MSAADA KUTOKA UFARANSA
  • “TUMELEMEWA KIDOGO!”
  • KUHUBIRI KATIKA MAENEO YA MBALI
  • MAREKEBISHO KATIKA TENGENEZO YAHARAKISHA KAZI
  • MAPAINIA WAWEKA KIELELEZO KIZURI
  • UPINZANI WA MASHETANI
  • KUHUBIRI MASHAMBANI
  • ONGEZEKO KUBWA SANA!
  • HABARI NJEMA YAHUBIRIWA KUSINI
  • MAJUMBA YA UFALME YAJENGWA
  • MAHALI PA KUFANYIA MAKUSANYIKO YA MZUNGUKO
  • MAHALI PA KUFANYIA MAKUSANYIKO YA WILAYA
  • MAENDELEO KATIKA TENGENEZO
2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb07 kur. 222-255

Réunion

WATU wa kwanza kuona kisiwa cha Réunion, ambao yaelekea ni wafanyabiashara Waarabu, walivumbua bila kutarajia eneo lililo kama paradiso. Kisiwa cha Réunion ni kama jiwe lenye thamani la kijani-kibichi katika Bahari ya Hindi yenye rangi ya bluu. Kisiwa hicho kina mandhari nyingi tofauti-tofauti zenye kuvutia. Baadhi ya maliasili za kisiwa hicho ni fuo zenye mchanga wa volkano, maporomoko mengi ya maji, misitu ya mvua, maua mengi ya mwituni, mabonde yenye kina kirefu, vilele vya volkano vilivyochongoka, mabonde makubwa ya volkano, na volkano moja hai.

Ingawa kisiwa cha Réunion kinavutia, watu wengi wanaoishi humo wanathamini kitu fulani kinachowavutia zaidi kuliko vitu vinavyoonekana. Wanathamini kweli muhimu za Neno la Mungu. Mmishonari Robert Nisbet aliyekuwa ametumwa Mauritius, ndiye aliyekuwa mtangazaji wa kwanza wa Ufalme kufika Réunion. Alipokuwa huko kwa siku chache mnamo Septemba 1955, Robert aliwapata watu wengi waliovutiwa na Biblia. Aligawa vichapo vingi naye alipata watu wengi waliotaka kupokea magazeti ya Amkeni! kwa njia ya posta. Aliendelea kuwasiliana kwa barua na waliopendezwa.

Kati ya 1955 na 1960, Robert pamoja na mwangalizi wa eneo la dunia, Harry Arnott, walifanya ziara kadhaa fupi kisiwani Réunion. Katika 1959, ofisi ya tawi ya Ufaransa ilimwomba Adam Lisiak, painia aliyekuwa akitumika huko Madagaska, azuru Réunion. Adam alikuwa Mfaransa mwenye asili ya Poland aliyekuwa amestaafu kazi ya kuchimba makaa ya mawe. Alikaa mwezi wote wa Desemba 1959 kisiwani Réunion. Aliandika: “Asilimia 90 ya wakaaji ni Wakatoliki thabiti, lakini wengi wangependa kujua mengi zaidi kuhusu Neno la Mungu na ulimwengu mpya. Makasisi wanajaribu kuzuia kweli isienezwe. Mtu fulani alimwambia mwanamume anayepokea gazeti la Amkeni! kwa njia ya posta kuwa kasisi wa kwao anataka kuazima kitabu chetu ‘Mungu na Awe wa Kweli.’ Mwanamume huyo alisema, ‘Kasisi mwenyewe akija, nitampa.’ Kasisi huyo hakuja kamwe.”

MSAADA KUTOKA UFARANSA

Ofisi ya tawi ya Ufaransa, iliyosimamia kazi wakati huo, iliwaomba wahubiri wenye ustadi wahamie Réunion. Familia ya Pégoud—André, Jeannine, na Christian, mwana wao mwenye umri wa miaka sita—pamoja na Noémie Duray, mtu wa jamaa yao, walikubali mwito huo. Waliwasili Januari 1961. Noémie, ambaye pia huitwa Mimi, alitumika akiwa painia wa pekee kwa miaka miwili kabla ya kurudi Ufaransa.

Muda si mrefu, walipata watu wengi wenye kupendezwa na hata walifanya mikutano kwenye chumba chao hotelini katika jiji kuu la Saint-Denis. Mara tu familia hiyo ilipohamia nyumba nyingine, walianza kufanya mikutano huko. Mwaka mmoja hivi baadaye, ndugu katika kikundi hicho kipya jijini Saint-Denis walikodi ukumbi mdogo uliotoshea watu 30 hivi. Ukumbi huo uliojengwa kwa mbao na kuezekwa kwa mabati, ulikuwa na madirisha mawili na mlango mmoja. Baada ya kupata kibali, ndugu walibomoa kuta za ndani, wakajenga jukwaa dogo, na kuweka viti visivyo na sehemu ya kuegemea.

Siku za Jumapili wakati jua lilipowaka asubuhi, paa hilo la mabati lilifanya ukumbi huo uwe na joto jingi. Baada ya muda, wote waliokuwa ndani walitokwa na jasho, hasa wale waliosimama jukwaani, vichwa vyao vikiwa karibu na paa. Isitoshe, kwa kuwa mara nyingi ukumbi huo ulijaa kabisa, watu wengi walisikiliza wakiwa kwenye madirisha na mlango, na kufanya waliokuwa ukumbini wakose hewa safi.

“TUMELEMEWA KIDOGO!”

Ingawa hali hiyo ilikuwa ngumu, wote walikaribishwa vizuri mikutanoni, na mwishoni mwa mwaka wa 1961 watu 50 hivi walihudhuria mikutano kwa ukawaida. Idadi ya wahubiri wa Ufalme iliongezeka hadi watu saba, nao waliongoza mafunzo 47 ya Biblia! Baadhi ya wanafunzi wapya walijifunza mara mbili kwa juma. “Tunafurahi sanasana, lakini tumelemewa kidogo,” ndugu wakaandika.

Myriam Andrien alikuwa mmoja wa wanafunzi hao wapya, naye alianza kujifunza alipokuwa Madagaska mwaka wa 1961. Anakumbuka ukumbi huo ulitumiwa pia kama Jumba la Kusanyiko. Ndugu walipanua sehemu ya kuketi kwa kujenga kibanda cha makuti. Nyakati nyingine watu 110 walihudhuria makusanyiko hayo.

David Souris, Marianne Lan-Ngoo, na Lucien Véchot, walikuwa kati ya wale waliobatizwa katika kusanyiko moja huko Mauritius mnamo Oktoba 1961, nao walisaidia sana katika kazi ya kuhubiri. Mwaka uliofuata, idadi ya wahubiri iliongezeka hadi 32, na kila painia aliongoza mafunzo 30 ya Biblia! Watu waliohudhuria mikutano ya Jumapili waliongezeka hadi 100, nao walitoka jamii mbalimbali.

Wahindi wengi wa Réunion wanachanganya Uhindu na Ukatoliki. Ilikuwa vigumu kwa baadhi yao kuacha mazoea yao ya zamani. Lakini kwa kuwa ndugu walikuwa wenye subira, fadhili, na msimamo thabiti kwa yaliyo sawa, mara nyingi matokeo yalikuwa mazuri. Kwa mfano, mwanamke mmoja aliyejifunza na painia kwa miaka miwili alikuwa bado anabashiri na hakuwa ameacha dini ya uwongo. Pia aliishi na mtu ambaye hakuwa amefunga ndoa naye. Painia huyo alimwomba dada mwingine ajifunze na mwanamke huyo ili aone kama anaweza kumsaidia. Dada huyo anaandika: “Baada ya miezi michache, mwanamke huyo alianza kuelewa mambo vizuri zaidi, na nilifurahi sana alipoacha kubashiri. Lakini hakuwa ameandikisha ndoa. Alisema kuwa mtu aliyeishi naye alikataa. Mwishowe, aliamua kuendelea kuishi na mtu huyo. Hivyo sikuwa na lingine ila kuacha kujifunza naye.

“Siku moja nilikutana na mwanamke huyo barabarani, na akaniomba nianze kujifunza naye tena. Nilikubali mradi tu awe tayari kutenda kupatana na yale aliyokuwa amejifunza. Nilimshauri asali kwa Yehova kuhusu jambo hilo, naye akafanya hivyo. Kisha akapiga moyo konde na kuzungumza waziwazi na mtu aliyeishi naye. Alifurahi sana mtu huyo alipokubali kumwoa na kuanza kuhudhuria mikutano pamoja naye.”

Katika mwaka wa utumishi wa 1963, kulikuwa na vilele 11 vya wahubiri wa Ufalme, na cha mwisho kilikuwa cha wahubiri 93. Réunion ilikuwa na makutaniko mawili na kikundi kimoja wakati huo. Watu 20 walibatizwa katika ubatizo wa kwanza kisiwani humo uliofanywa Desemba 1962 kwenye ufuo wa St.-Gilles-les Bains. Ubatizo wa pili ulifanywa Juni 1963 na watu 38 wakabatizwa. Katika 1961, kulikuwa na mhubiri 1 kwa kila watu 41,667 kisiwani Réunion. Miaka mitatu baadaye, kulikuwa na mhubiri 1 kwa kila watu 2,286. Naam, Yehova alikuwa ‘akikuza mbegu ya ile kweli’ katika kisiwa hiki chenye rutuba ya kiroho.—1 Kor. 3:6.

KUHUBIRI KATIKA MAENEO YA MBALI

Katika 1965, miaka minne tu baada ya familia ya kwanza ya Mashahidi kufika, kutaniko jijini Saint-Denis lilikuwa na zaidi ya wahubiri 110, nao walikuwa wakihubiri na kumaliza eneo lao baada ya kila majuma matatu! Hata hivyo, hawakuwa wakihubiri katika maeneo mengine. Walifanyaje? Ndugu walikodi mabasi na kuhubiri katika miji mingine ya pwani, kutia ndani Saint-Leu, Saint-Philippe, na Saint-Pierre.

Ilichukua muda wa saa nyingi kufika katika maeneo fulani, hivyo ndugu walikuwa wakiondoka asubuhi na mapema. Walisafiri kwenye barabara ambazo katika sehemu nyingi zilikuwa nyembamba, zenye miteremko mikali, na zenye kujipinda. Leo gari huchukua muda wa dakika 15 kutoka Saint-Denis kwenda jiji la Le Port, lakini wakati huo ilikuwa safari ngumu ya muda wa saa mbili. “Tulihitaji kuwa na imani ili kusafiri kwenye barabara hiyo,” asema ndugu mmoja. Hata barabara mpya si salama kabisa kwa sababu miamba huanguka kwenye barabara hiyo. Katika maeneo fulani kuna milima yenye miteremko mikali sana kandokando ya barabara, na mara kwa mara miamba mikubwa huanguka kunaponyesha mvua nyingi. Watu kadhaa wamekufa kwenye barabara hiyo.

Christian Pégoud anasema, “Nilipokuwa na umri wa miaka minane hivi, kikundi chetu kilikuwa kikigawa Amkeni! 400 hadi 600 katika maeneo ya mbali. Mnara wa Mlinzi lilikuwa limepigwa marufuku. Waume kadhaa wasioamini ambao walipenda Mashahidi walifurahia safari hizo, hivyo waliandamana na wake zao lakini hawakuhubiri. Baada ya kuhubiri tulikula pamoja, jambo ambalo sisi watoto tulifurahia sana. Utendaji huo wa pekee ulinichochea sana maishani mwangu.”

MAREKEBISHO KATIKA TENGENEZO YAHARAKISHA KAZI

Milton G. Henschel aliyetembelea Réunion mnamo Mei 1963, ndiye mwakilishi wa kwanza kutoka makao makuu kutembelea kisiwa hicho. Alitoa hotuba ya pekee iliyosikilizwa na watu 155. Wakati wa ziara yake, ndugu wanne waliwekwa kuwa mapainia wa pekee ili kusaidia makutaniko na kuhubiri katika maeneo ambako habari njema haikuwa imehubiriwa. David Souris alitumwa Le Port, Lucien Véchot akatumwa jijini Saint-André, na Marianne Lan-Ngoo na Noémie Duray (sasa anaitwa Tisserand) wakatumwa Saint-Pierre.

Ofisi ya tawi ya Mauritius ilianza kusimamia kazi mnamo Mei 1, 1964 badala ya ofisi ya Ufaransa. Zaidi ya hilo, depo ya vichapo ilifunguliwa Réunion. Wakati huo, wahubiri waliombwa kuhubiri katika maeneo mengi ambayo hayakuwa yamegawiwa yeyote. Ndugu walihimizwa wajitahidi kufikia majukumu mbalimbali katika kutaniko ili walio wapya katika kweli watunzwe vizuri. Katika mwaka wa utumishi wa 1964, watu 57 walibatizwa—21 katika kusanyiko moja!

Katika mwaka uliotangulia, ndugu huko Saint-André waliomba kikundi chao kiwe kutaniko. Barua yao ilisema: “Mwishoni mwa Juni 1963, tutakuwa na wahubiri 12 waliobatizwa, na katika miezi miwili ijayo, inawezekana tutakuwa na wahubiri wapya 5 au 6. Ndugu wanaongoza mafunzo 30 ya Biblia.” Ombi lao lilikubaliwa, na kutaniko hilo likasimamiwa na ndugu wawili—Jean Nasseau aliyekuwa mtumishi wa kutaniko, au mwangalizi msimamizi, na Lucien Véchot msaidizi wake. Wote walikuwa wamebatizwa kwa muda usiozidi miaka miwili.

Jean mwenye umri wa miaka 38, alikuwa mtu mkubwa, mwenye fadhili, na mkarimu. Alikuwa pia mjenzi stadi aliyefundisha katika shule fulani ya ufundi. Alibatizwa 1962 na alikuwa na uwezo wa kuwachochea watu waendeleze kazi ya Ufalme. Hata aligharimia ujenzi wa Jumba la Ufalme la pili kisiwani Réunion lililojengwa kwenye kiwanja chake huko Saint-André. Jengo hilo lililojengwa kwa mbao lilikuwa thabiti na lenye kuvutia, na lilitoshea vizuri zaidi ya watu 50. Makutaniko manane yameanzishwa katika eneo hilo ambalo mwanzoni lilihubiriwa na kikundi cha Saint-André. Jean alikufa akiwa mwaminifu kwa Yehova mwaka wa 1997.

Kikundi cha tatu kilianzishwa katika jiji lenye bandari la Le Port mwanzoni mwa miaka ya 1960, na kilitia ndani watu wenye kupendezwa kutoka Saint-Paul, mji ulio umbali wa kilomita nane hivi kusini ya Le Port. Jiji la Le Port lilikuwa na nyumba za mbao zilizokuwa na ua wa mmea fulani aina ya dungusi usio na miiba. David Souris alikodi nyumba na kuanza kufanya mikutano humo. Mnamo Desemba 1963, ndugu waliomba kikundi chao kiwe kutaniko. Wahubiri wa Ufalme walikuwa 16, na 8 kati yao walikuwa wamebatizwa. Walihubiri wastani wa saa 22.5 kila mwezi. David pamoja na msaidizi wake waliongoza mafunzo 38 ya Biblia! Mwangalizi wa mzunguko alipowatembelea mwezi huo, alitoa hotuba iliyosikilizwa na watu 53.

Mapainia wa pekee Christian na Josette Bonnecaze walitumwa Le Port pia. Christian aliyebatiziwa Guiana ya Ufaransa alikuja Réunion mapema miaka ya 1960. Wakati huo alikuwa mseja, na katika familia yao hakuna mwingine aliyekuwa Shahidi. Kwa fadhili, Ndugu Souris alihamia nyumba nyingine ili Christian na mke wake Josette wakae katika nyumba iliyokuwa inatumiwa kwa ajili ya mikutano. Lakini baada ya muda, kutaniko hilo lilikua sana mpaka wenzi hao wakalazimika kuhama pia!

Wakati huo makasisi katika eneo hilo lililokuwa na Wakatoliki wengi walianza kuwachochea watu wawachukie Mashahidi. Mara nyingi vijana waliwarushia wahubiri mawe mchana. Usiku waliyarusha juu ya paa za nyumba za akina ndugu.

Mwanafunzi mpya wa Biblia Raphaëlla Hoarau aliwajua baadhi ya vijana hao. Pindi moja baada ya vijana hao kurusha mawe, mwanafunzi huyo aliwafuata nyumbani kwao na kuwaambia: “Mkiendelea kumrushia ndugu yangu mawe, nitawaonyesha cha mtema kuni.”

“Pole sana Bi. Hoarau. Hatukujua huyo ni ndugu yako,” wakasema.

Raphaëlla na mabinti wake watatu walikubali kweli na mmoja wao, Yolaine, akaolewa na Lucien Véchot.

Ijapokuwa makasisi waliwachochea watu wachukie Mashahidi, kutaniko lenye bidii lilianzishwa Le Port kwa sababu ndugu walikuwa wenye bidii na Mungu aliwabariki. Muda si mrefu, jumba walilofanyia mikutano lilijaa pomoni. Mara nyingi walio wengi walisikiliza wakiwa nje. Viti viliwekwa kila mahali, hata jukwaani, na watoto fulani waliketi ukingoni mwa jukwaa wakitazama wasikilizaji. Hatimaye, ndugu walijenga Jumba la Ufalme zuri, na sasa eneo hilo lina makutaniko sita.

MAPAINIA WAWEKA KIELELEZO KIZURI

Annick Lapierre ni mmojawapo wa mapainia wa kwanza kisiwani Réunion. Myriam Thomas anasema, “Mimi na mamangu tulifunzwa kweli na Annick. Alinitia moyo niwe mwenye bidii katika huduma, nami nikamwambia ningetaka kuwa painia. Nilibatizwa baada ya miezi sita. Wakati huo tulihubiri katika kisiwa chote, na kwa kawaida tulitembea kwa miguu kwa sababu hakukuwa na mabasi, nayo magari yalikuwa machache. Ndugu Nasseau alikuwa na gari, na ilipowezekana tulienda naye katika utumishi. Tulifurahia kuhubiri na sote tulikuwa wenye bidii sana.”

Henri-Lucien Grondin, ndugu mwenye familia anasema: “Kila mara tuliwatia moyo watoto wetu wawe mapainia. Waangalizi wa mzunguko walikazia umuhimu wa kumpa Yehova kilicho bora. Henri-Fred, mwana wetu wa kwanza ana umri wa miaka 40 na amejiunga na utumishi wa wakati wote.”

Henri-Fred anasema: “Kutaniko letu lilikuwa na vijana wengi wenye bidii na baadhi yao walikuwa wamebatizwa. Lakini mimi na vijana wengine hatukuwa tumebatizwa. Hata hivyo, wakati wa likizo za shule, sote tulihubiri muda wa saa 60. Hatukusahau miradi yetu ya kiroho, na sasa mke wangu Evelyne huandamana nami katika kazi ya mzunguko.”

UPINZANI WA MASHETANI

Kuwasiliana na pepo ni jambo la kawaida kisiwani Réunion. Jeannine Corino (aliyeitwa Pégoud) anasema: “Katika kijiji cha La Montagne nilikutana na mtu aliyesema ataniletea laana kwa kumdunga mwanasesere kwa pini. Sikuelewa alichomaanisha, hivyo nikamwomba mwanafunzi wangu wa Biblia anieleze. Aliniambia: ‘Huyo ni mchawi, naye atawaomba pepo wakuumize.’ Nilimhakikishia kuwa Yehova huwalinda wale wanaomtegemea kabisa. Sikupatwa na madhara yoyote.”

Ndugu mmoja anakumbuka kwamba alipokuwa mtoto, familia yao ilifanya mikutano ya kuwasiliana na pepo. Katika 1969, alikutana na Mashahidi wa Yehova na akaanza kujifunza Biblia. Lakini mashetani walijaribu kumvunja moyo kwa kumfanya kiziwi alipokuja mikutanoni. Hata hivyo, ndugu huyo aliendelea kuhudhuria mikutano na pia kurekodi hotuba ili aweze kuzisikiliza akiwa nyumbani. Muda si muda, mashetani hao walimwacha, na muda mfupi baadaye akaanza kuhubiri.—Yak. 4:7.

Katika 1996, Roséda Caro, mwanamke Mpentekoste, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi. Alikuwa kipofu kwa sababu alisikiliza mashauri ya marafiki wake katika kanisa lake na kuacha kutumia dawa za ugonjwa wa kisukari. Mume wake, Cledo, aliyekuwa mwanachama wa chama cha Kikomunisti, aliogopwa na watu kwa sababu ya hasira yake kali. Pia, alikuwa mchawi, alishiriki katika sherehe za Kihindu, na baadaye akawa Mpentekoste.

Roséda alipoanza kujifunza, Cledo alimpinga na hata akawatisha wazee wa kutaniko. Lakini Roséda hakuogopa. Miezi kadhaa baadaye, Cledo alilazwa hospitalini alikopoteza fahamu. Alipopata fahamu tena, dada wawili walimletea mchuzi aliofikiri ni wa mke wake.

“Hapana, Bw. Caro, mchuzi huu ni wako!” dada hao wakamwambia.

“Jambo hilo lilinivutia sana,” asema Cledo. “Hakuna Mpentekoste aliyenitembelea, lakini Mashahidi wawili, watu ambao niliwapinga vikali, wameniletea mchuzi. ‘Kwa kweli, Yehova, Mungu wa mke wangu, ni Mungu aliye hai,’ nikawaza. Kisha nikasali kimyakimya, nikiomba mimi na Roséda tuwe na imani moja.”

Cledo hakusali tu bila kufikiri. Kabla ya kuwa mgonjwa, mtazamo wake ulikuwa umebadilika kidogo naye akamruhusu mke wake awe akijifunza Biblia nyumbani kwa jirani wao. Kisha siku moja akamwambia Roséda na dada aliyekuwa akijifunza naye: “Si vizuri kujifunzia huko. Njooni nyumbani.” Wanawake hao walifanya hivyo. Bila wao kujua, Cledo alisikiliza akiwa katika chumba kingine na kuvutiwa na aliyosikia. Cledo hakujua kusoma wala kuandika, lakini alipopona alijifunza mara mbili kwa juma naye akabatizwa mwaka wa 1998. Ijapokuwa Cledo na Roséda wanakumbwa na magonjwa yanayoambatana na uzee, wanaendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu.

KUHUBIRI MASHAMBANI

Watu wachache kisiwani Réunion huishi mashambani kwenye mabonde yenye kina kirefu yanayozungukwa na milima yenye miteremko mikali na urefu wa mita 1,200 au zaidi. Wengine huishi katika mabonde yenye mimea mingi ya volkano kubwa iliyoacha kulipuka. Watu wanaoishi katika mabonde hayo hawatembei pwani mara nyingi. Kwa mfano, bonde la Cirque de Mafate laweza tu kufikika kwa miguu au kwa helikopta.

Louis Nelaupe, kutoka jamaa ya Waafrika waliokuwa watumwa, alikulia Cirque de Mafate. Alipokuwa kijana, alisaidia kumbeba kasisi Mkatoliki kwa kiti fulani maalumu. Baada ya kuhamia Saint-Denis na kuwa Shahidi, Louis alitaka kuwaeleza jamaa zake mambo mapya aliyojifunza katika Biblia. Kwa hiyo, siku moja mwaka wa 1968, Louis na mke wake Anne, na dada wengine wawili, wenye umri wa miaka 15 na 67, wakafunga safari ya kwenda mashambani kwa miguu. Walibeba mfuko, sanduku, na mkoba uliojaa vichapo.

Mwanzoni walitembea kando-kando ya mto, kisha wakafuata njia ya mlimani iliyokuwa nyembamba na yenye kujipinda. Sehemu fulani za njia hiyo zilikuwa na mwamba mkubwa upande mmoja, na mteremko mkali upande ule mwingine. Walihubiri katika kila nyumba njiani. Louis anasema, “Usiku huo Yehova alituandalia mahitaji yetu kupitia mwenye duka fulani. Yeye tu ndiye aliyekuwa na duka wilayani humo, naye alitupa kibanda chenye vyumba viwili vilivyokuwa na vitanda na jiko. Asubuhi tulianza safari tena. Tulipanda ukingo wa mlima wenye urefu wa mita 1,400, kisha tukateremka na kuingia katika bonde kubwa lenye umbo la duara.

“Hatimaye tulifika nyumbani kwa rafiki yangu wa zamani aliyetukaribisha vizuri. Kesho yake tuliacha mizigo fulani kwake na tukaanza safari kuelekea tulikokuwa tukienda. Tulikula mapera madogo ya mwituni na kuwahubiria watu wa mashambani ambao hawakuwa wamesikia kamwe ujumbe wa Ufalme. Tulifika nyumbani kwa mwanamke fulani wa jamaa yangu saa 12:00 jioni. Alifurahi kutuona, kisha akapika nyama tamu ya kuku, jambo lililotukumbusha Abrahamu na Sara waliowaandalia malaika wa Mungu chakula. (Mwa. 18:1-8) Tulimhubiria huku akipika. Tulikula saa 5:00 usiku.

“Kesho yake, Alhamisi, tulizunguka bonde hilo huku tukila mapera na kuhubiri katika nyumba zote tulizopata. Mtu fulani mwenye fadhili alitupa kahawa, nasi tukapumzika kidogo, lakini tukaendelea kumhubiria. Mtu huyo alifurahia sana mazungumzo ya Biblia hivi kwamba aliandamana nasi katika nyumba zote zilizokuwa umbali wa kilomita tisa kutoka nyumbani kwake. Alitembea huku akipiga kinanda chake.

“Mwishowe, tulirudi na kulala mahali tulipoacha mizigo yetu. Tulipofika nyumbani Ijumaa jioni, sisi wanne, kutia ndani dada yetu mwenye umri wa miaka 67, tulikuwa tumetembea kilomita 150 hivi. Pia tulikuwa tumetembelea nyumba 60 na kugawa vichapo 100. Ni kweli tulikuwa wachovu, lakini tulikuwa tumeburudika kiroho. Kwa kweli, tuliposafiri kwenda Cirque de Mafate nilihisi kama ninarudi nyumbani.”

ONGEZEKO KUBWA SANA!

Katika 1974, Christian Pégoud na mamake walihamia mji wa kusini wa La Rivière, ambao haukuwa na kutaniko wakati huo. Christian aliyekuwa amefikia umri wa miaka 20 anasema: “Tulifanya mikutano kwenye banda letu la kuwekea gari, na punde watu 30 wakaanza kuhudhuria. Nilianza kujifunza na mwanamke ambaye binti yake, Céline, alikuwa amechumbiwa na Ulysse Grondin. Ulysse alikuwa mwanaharakati wa chama cha Kikomunisti na hakutaka mchumba wake ajifunze nasi. Lakini Céline alimshawishi Ulysse atusikilize, na mamangu akaenda kumwona Ulysse na wazazi wake. Tulifurahi sana walipomsikiliza mamangu na kupendezwa na mambo waliyosikia. Familia nzima ilianza kujifunza, na mnamo 1975, Ulysse na Céline wakabatizwa, kisha wakafunga ndoa. Hatimaye, Ulysse aliwekwa kuwa mzee.”

Christian anaongeza: “Tulihubiri huko La Rivière na pia katika maeneo ya mashambani ya Cilaos, Les Avirons, Les Makes, na L’Étang-Salé. Tulipata watu wengi wenye kupendezwa huko Les Makes. Karibu na kijiji hicho, kuna eneo lililoinuka linaloitwa Le Cap, ambalo ni sehemu ya volkano iliyoacha kulipuka. Ukisimama hapo asubuhi siku isiyo na ukungu, unaweza kuona bonde kubwa la duara lenye kina cha mita 300 na mimea mingi.”

Familia ya Poudroux iliishi katika shamba dogo karibu na Le Cap. Mwana wao wa kwanza, Jean-Claude, anasema: “Mimi na ndugu zangu wanne na dada zetu watano, tulimsaidia baba yetu kulima mboga za kuuza sokoni. Pia alilima maua aina ya jireniamu yanayotumiwa kutengeneza manukato. Tulitembea kilomita tano kufika kwenye shule ya kijijini, na mara nyingi tulibeba mazao ya shambani. Nyakati nyingine tulirudi nyumbani tukiwa tumebeba kichwani vyakula vyenye uzito wa kilogramu kumi hivi.

“Baba alifanya kazi kwa bidii, na tulimheshimu kwa jambo hilo. Lakini sawa na watu wengi, alikunywa kupita kiasi, naye alikuwa mwenye jeuri alipolewa. Baba alisababisha vurugu nyumbani, na mimi na ndugu zangu tulikuwa na wasiwasi kuhusu hali ya baadaye ya familia yetu.”

Jean-Claude anaongeza: “Painia fulani alinihubiria mwaka wa 1974. Nilikuwa mwalimu huko La Rivière. Sikuwa na hakika kwamba kuna Mungu kwa sababu ya unafiki na ukosefu wa haki nilioona makanisani. Hata hivyo, nilivutiwa ndugu huyo alipotumia Biblia kujibu maswali yangu yote. Mimi na mke wangu Nicole tulianza kujifunza. Pia tuliitembelea familia yetu ili kuwaeleza kweli ya Biblia, na mara nyingi tuliongea na ndugu zangu hadi usiku wa manane. Nyakati nyingine wazazi wangu walisikiliza.

“Muda si muda, ndugu zangu Jean-Marie na Jean-Michel na dadangu Roseline wakaanza kuja nyumbani kwetu kwa ukawaida na kujiunga nasi katika funzo. Sote tulifanya maendeleo ya kiroho, tukawa wahubiri, na kubatizwa mwaka wa 1976. Kwa kusikitisha babangu alinilaumu kwamba ninawapotosha ndugu zangu, naye akaacha kuzungumza nami. Alikuwa mkorofi kiasi kwamba ilinibidi kumwepuka mahali penye watu!

“Mamangu alianza kujifunza japo hakujua kusoma wala kuandika. Ninafurahi kusema kuwa hatimaye Baba alibadili mtazamo wake. Hata alianza kujifunza Biblia mwaka wa 2002. Leo, watu 26 katika familia yetu wamebatizwa. Watu hao ni mimi na ndugu na dada zangu, wenzi wetu wa ndoa, mama yetu, ambaye bado ana bidii ingawa ana umri mkubwa. Jean-Michel na Jean-Yves walikuwa waangalizi wa mzunguko kwa muda lakini wakaacha kwa sababu ya magonjwa. Wote wawili ni wazee wa kutaniko, na Jean-Yves na mke wake Roséda ni mapainia. Mimi na mwana wangu wa kwanza ni wazee wa kutaniko.”

Wakati Christian Pégoud na mama yake walipofika mwaka wa 1974, hakukuwa na kutaniko katika mji wa La Rivière wala katika miji mingine ya karibu, lakini sasa kuna makutaniko matano katika eneo hilo. Kutaniko moja liko katika mji wa Cilaos, kwenye bonde la Cirque de Cilaos lililo juu mlimani. Mji huo ni maarufu kwa sababu ya chemchemi kadhaa za maji baridi na moja ya maji ya moto. Kutaniko la Cilaos lilianzaje? Kila Alhamisi kuanzia mwaka wa 1975 hadi 1976, wahubiri kutoka La Rivière walisafiri kilomita 37 kwenda Cilaos ambako walihubiri hadi saa 11:00 hivi jioni. Walipita barabara nyembamba, yenye kujipinda, ambayo ilijulikana kwa sababu ya miamba iliyoanguka. Bidii yao ilikuwa na matokeo, kwa kuwa sasa kuna Jumba la Ufalme na wahubiri 30 hivi mjini humo.

HABARI NJEMA YAHUBIRIWA KUSINI

Kwa sababu nzuri, watu wa Réunion huita sehemu ya kusini mwa kisiwa hicho “eneo la msukosuko.” Mawimbi makubwa hupiga fuo kwa nguvu na kufanyiza manyunyu na povu jingi katika eneo kame la pwani. Eneo hilo lina volkano kubwa hai inayoitwa, Piton de la Fournaise (Kilele cha Moto). Saint-Pierre ndio mji mkubwa katika eneo hilo. Mapainia wa pekee, Denise Mellot na Lilliane Pieprzyk, walitumwa huko mwishoni mwa miaka ya 1960. Baadaye, watu wenye kupendezwa walipoongezeka, painia wa pekee Michel Rivière na mke wake Renée, wakajiunga na dada hao wawili.

Cléo Lapierre, mjenzi aliyekubali kweli mwaka wa 1968, ni mmojawapo wa wanafunzi wa kwanza wa Biblia katika eneo hilo. Anasema: “Nilihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza chini ya mti. Kibanda kilichotumiwa kama Jumba la Ufalme kilikuwa kikibomolewa ili jumba kubwa lijengwe, nami nilishiriki katika ujenzi huo.”

Mwaka huo, Cléo aliyekuwa askari wa akiba, aliitwa jeshini. Anasema, “Ingawa nilikuwa na ujuzi kidogo tu wa Biblia, niliwaandikia wakuu wa jeshi na kuwaeleza msimamo wangu wa kutojiunga na jeshi. Hawakunijibu, hivyo nikaenda kuchunguza jambo hilo katika kituo cha jeshi cha Saint-Denis, upande ule mwingine wa kisiwa. Ofisa mmoja aliniambia niende nyumbani lakini nijitayarishe kufungwa gerezani. Kwa hiyo, nilisali mara nyingi na kujifunza kwa bidii. Muda si mrefu, niliitwa kwenye kituo cha jeshi. Nilipofika huko, nilimwomba ndugu niliyeandamana naye katika gari aningoje kwa muda wa saa moja. Nilimwambia, ‘Usiponiona baada ya muda huo, yaelekea sitarudi. Nisiporudi tafadhali uza gari langu kisha umpe mke wangu pesa utakazopata.’

“Nilipoingia ndani, nilikuta maofisa wakibishana kuhusu hatua ambayo wangenichukulia. Baada ya dakika 45 hivi, askari mmoja alinikaribia.

“Alisema, ‘Ondoka mbele yangu! Nenda nyumbani.’

“Baada ya kutembea hatua chache tu, aliniita na kwa upole akasema: ‘Ninyi watu mnanivutia. Nilisikia kuhusu Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa, lakini wewe ndiye Shahidi wa kwanza kuona.’

“Wakati huo hakukuwa na ndugu mwingine huko Saint-Pierre, hivyo niliongoza mikutano yote ya kutaniko. Hata hivyo, nilisaidiwa mara kwa mara, na katika 1979 Antoine na Gilberte Branca, mume na mke wamishonari, wakafika.”

MAJUMBA YA UFALME YAJENGWA

Mwanzoni, ndugu katika makutaniko na vikundi walikutana katika nyumba zilizobadilishwa kidogo, au za watu binafsi. Hata hivyo, walihitaji majengo thabiti zaidi kwa sababu vimbunga hutokea mara nyingi. Lakini nyumba za mawe hujengwa kwa gharama kubwa na ujenzi huchukua muda mrefu. Ingawa hivyo, kwa kuwa mkono wa Yehova si mfupi, hatimaye walianza kujenga Majumba ya Ufalme ya mawe kisiwani Réunion.—Isa. 59:1.

Kwa mfano, mjini Saint-Louis, ndugu fulani kijana alikuwa akijifunza kazi ya uashi wakati kutaniko lilipopokea ramani ya ujenzi ya Jumba la Ufalme. Ndugu huyo alimhubiria mwalimu wake, akamweleza kuhusu jumba hilo, na kumjulisha kuwa litajengwa na wafanyakazi wa kujitolea. Mwalimu huyo alifanya nini? Aliwaleta wanafunzi kwenye ujenzi ili wapate mazoezi ya kujenga! Walisaidia kuchimba msingi, na baadaye mwalimu huyo akachanga vyuma vya kujengea msingi huo.

Ndugu waliamua kutengeneza bamba la sementi lenye ukubwa wa mita 190 za mraba wakati wa sikukuu. Wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya mia moja walifika asubuhi na mapema kufanya kazi hiyo. Lakini kwa sababu fulani, maji yalikuwa yamefungwa mjini! Ndugu mmoja aliyemjua mkuu wa zimamoto alimweleza tatizo hilo, na mara moja mkuu huyo mwenye fadhili akatuma gari la zimamoto likiwa na maji ya kutosha kwa kazi hiyo.

Jumba la Ufalme lilipokamilika, mtu aliyekuwa ameanza kujifunza Biblia karibuni na aliyevutiwa na ndugu na kazi yao, alichukua kitabu chake cha hundi na kuchanga pesa ambazo karibu zilitosha kununua mfumo mpya wa sauti. Carey Barber wa Baraza Linaloongoza alipotembelea Mauritius mwaka wa 1988, alikuja Réunion ili kutoa hotuba ya kuweka jumba hilo wakfu. Jumba la kwanza lililojengwa kwa muda mfupi lilikamilishwa mnamo 1996 huko St.-Gilles-les Bains. Leo, kisiwa hicho kina Majumba ya Ufalme 17 na makutaniko 34.

MAHALI PA KUFANYIA MAKUSANYIKO YA MZUNGUKO

Kazi ya kuhubiri kisiwani Réunion ilifanikiwa sana hivi kwamba ilikuwa vigumu kupata mahali pakubwa vya kutosha kufanyia makusanyiko. Katika 1964, ndugu walipanga kusanyiko lao la kwanza la mzunguko. Walitafuta kwa miezi kadhaa mahali pa kufanyia kusanyiko nao wakapata mkahawa mmoja uliokuwa ghorofani huko Saint-Denis. Jengo hilo la zamani lilikuwa limejengwa kwa mbao na lilikodishwa pesa nyingi. Wenye jengo hilo walisema lingeweza kustahimili uzito wa watu 200 ambao tulitarajia wahudhurie.

Ndugu hawakuwa na lingine ila kukodi mkahawa huo. Mtu fulani mwenye mwelekeo mzuri alitupa mfumo wa vipaza-sauti. Siku ilipofika ndugu walijaa katika jengo hilo, na ingawa sakafu yake ilitoa sauti kubwa ya mkwaruzo, haikuporomoka. Watu 230 walihudhuria siku ya Jumapili, na 21 wakabatizwa.

Punde baadaye, kwa fadhili Louis Nelaupe, yule ndugu aliyekulia Cirque de Mafate, alitoa sehemu ya kiwanja chake huko Saint-Denis kwa ajili ya ujenzi wa Jumba la Kusanyiko la muda. Jumba hilo lililojengwa kwa nguzo za mbao na kuezekwa kwa mabati lilikuwa na kuta za makuti yaliyosokotwa.

Kusanyiko la kwanza kufanyiwa huko lilikuwa la siku tatu. Myriam Andrien aliyehudhuria kusanyiko hilo anasema: “Asubuhi siku ya kwanza, tulienda kuhubiri na kurudi kula chakula moto cha mchana cha Krioli, ambacho ni wali, maharagwe, na nyama ya kuku iliyotiwa pilipili kali. Wale ambao hawajazoea pilipili kali walipikiwa mchuzi unaoitwa rougail marmaille, usio na pilipili nyingi.”

Wahudhuriaji walipoongezeka, Jumba la Kusanyiko lilipanuliwa, nalo lilitumiwa pia kama Jumba la Ufalme. Baadaye, familia zilizokodi nyumba ambazo zilikuwa kwenye kile kiwanja zilihama, na Louis akalikabidhi kutaniko kiwanja chote. Sasa eneo hilo lina Jumba la Ufalme zuri la matofali linalotumiwa na makutaniko mawili ya Saint-Denis.

Katika 1997 Jumba la Kusanyiko lilijengwa mjini La Possession, kwenye kiwanja kilichokuwa kimenunuliwa miaka mitano mapema. Jengo hilo lisilo na kuta lina kidimbwi cha ubatizo jukwaani. Kila mwaka makusanyiko 12 hufanywa katika jumba hilo linalotoshea watu 1,600. Karibu na jumba hilo kuna makao ya wamishonari yanayotoshea watu tisa. Makao hayo yana depo ya vichapo na ofisi inayoshughulikia kazi ya kuhubiri kisiwani Réunion.

MAHALI PA KUFANYIA MAKUSANYIKO YA WILAYA

Kabla ya kujenga Jumba la Kusanyiko, ndugu walikuwa wakikodi uwanja wa michezo wa Olimpiki huko Saint-Paul kwa ajili ya makusanyiko ya wilaya. Hata hivyo, mara nyingi walilazimika kutafuta mahali pengine dakika ya mwisho kwa sababu michezo au sherehe za kitamaduni zilipewa nafasi ya kwanza. Baadaye, baraza la mji liliwaomba ndugu watumie uwanja wa maonyesho uliokuwa karibu. Kwa kuwa uwanja huo hutumiwa kwa maonyesho ya biashara, hauna viti wala paa, hivyo iliwabidi wahudhuriaji waje na viti vyao na miavuli. Kwa hiyo, badala ya kuona nyuso za watu wenye kusikiliza kwa makini, wale waliokuwa jukwaani waliona tu miavuli ya rangi mbalimbali.

Ofisi ya Réunion inaandika: “Pindi moja baraza la mji lilikodisha uwanja huo kwa Mashahidi na kwa kikundi kingine wakati uleule. Kikundi hicho kilikuwa cha wanamuziki kutoka Martinique waliocheza mchanganyiko wa muziki wa West Indies, mdundo wa Kiafrika, na rege. Baraza hilo liliwapendelea wanamuziki hao, kwa hiyo lilitupa eneo fulani la tafrija linaloitwa Pango la Wafaransa wa Kwanza, ambapo wahamiaji wa kwanza kutoka Ufaransa walishuka kutoka melini. Eneo hilo lenye miamba mirefu na miti mingi yenye kivuli lilivutia, lakini halikuwa na viti wala jukwaa, navyo vyoo vilikuwa vichache.

“Lakini tulifurahi kwamba tulienda huko kwa kuwa Jumamosi jioni wakati wa kusanyiko, dhoruba na radi ziliharibu mfumo wote wa umeme kwenye ule uwanja, na kusimamisha burudani ya muziki. Sisi hatukuathiriwa kwa sababu tulikuwa umbali wa kilomita tano kutoka kwenye uwanja huo. Wenyeji hata walisema hiyo ilikuwa ‘hukumu ya Mungu.’”

MAENDELEO KATIKA TENGENEZO

Katika Juni 22, 1967 shirika la kisheria la Mashahidi wa Yehova (Association Les Témoins de Jéhovah) lilianzishwa. Mnamo Februari 1969, Henri Zamit aliyezaliwa Algeria na kulelewa Ufaransa akawa mwangalizi wa mzunguko kisiwani Réunion. Mzunguko wake ulikuwa na makutaniko sita kisiwani Réunion, manne kisiwani Mauritius, na vikundi kadhaa. Leo Réunion ina mizunguko miwili.

Katika 1975 marufuku ya miaka 22 juu ya gazeti Mnara wa Mlinzi iliondolewa nchini Ufaransa, na mara moja ndugu wakaanza kutumia gazeti hilo katika kazi ya kuhubiri huko Réunion. Awali walitumia gazeti Bulletin intérieur. Gazeti hilo lililochapiwa Ufaransa lilikuwa na habari zilezile zilizokuwa katika Mnara wa Mlinzi lakini halikutumiwa katika kazi ya kuhubiri. Mnamo Januari 1980, ofisi ya Ufaransa ilianza kuchapa Huduma Yetu ya Ufalme katika Kifaransa. Kichapo hicho kilirekebishwa kulingana na mahitaji ya ndugu kisiwani Réunion na katika visiwa vingine vya eneo hilo. Pia, ili kuwanufaisha watu wanaoongea lugha ya Krioli ya Réunion, vichapo fulani, kutia ndani trakti, broshua, na kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele na Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli, vimetafsiriwa katika lugha hiyo. Vichapo hivyo ni uandalizi mzuri wa kiroho na vimesaidia kuendeleza habari njema katika eneo hilo la mbali baharini.

Naam, Réunion ni kisiwa kidogo tu katika Bahari ya Hindi. Lakini Mungu anasifiwa kwa njia kubwa sana huko! Jambo hilo linatukumbusha maneno haya ya nabii Isaya: ‘Na watangaze sifa za Yehova katika visiwa’! (Isa. 42:10, 12) Mashahidi wa Yehova huko Réunion na waendelee kutangaza sifa hizo kwa uthabiti na uaminifu sawa na vile mawimbi makubwa ya bluu yanavyopiga fuo za kisiwa hicho bila kukoma.

[Picha katika ukurasa wa 228, 229]

MAELEZO MAFUPI KUHUSU Réunion

Nchi

Kisiwa cha Réunion kina urefu wa kilomita 65 na upana wa kilomita 50, nacho ni kisiwa kikubwa kati ya Visiwa vya Mascarene, yaani, Mauritius, Réunion, na Rodrigues. Katikati ya kisiwa hicho kuna mabonde matatu yanayokaliwa, na ambayo yalitokea wakati volkano kubwa ya kale ilipoporomoka. Mimea mingi inasitawi katika mabonde hayo yenye miteremko mikali.

Watu

Réunion ina watu 785,200 ambao ni machotara walio wazao wa Waafrika, Wachina, Wafaransa, Wahindi, na watu kutoka Asia ya Kusini-Mashariki. Asilimia 90 hivi ni Wakatoliki.

Lugha

Kifaransa ni lugha rasmi, lakini Krioli ya Réunion ndiyo lugha ambayo watu huzungumza sana.

Kazi

Watu wengi hufanya kazi inayohusisha utalii, ukulima wa miwa, na kutengeneza bidhaa kama vile asali ya miwa na kileo kikali.

Chakula

Chakula cha kawaida ni wali, nyama, samaki, maharagwe, na dengu. Mbali na miwa kuna mazao kama vile nazi, matunda ya lichi, papai, mananasi, kabichi, letusi, nyanya, na vanila.

Hali ya hewa

Kisiwa cha Réunion kiko kaskazini kidogo ya Tropiki ya Kaprikoni, na ni chenye joto na unyevunyevu ijapokuwa kiasi cha mvua na joto kinatofautiana katika maeneo mbalimbali. Vimbunga hukumba kisiwa hicho mara nyingi.

[Ramani]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Madagaska

Rodrigues

Mauritius

Réunion

RÉUNION

SAINT-DENIS

La Montagne

La Possession

Le Port

Saint-Paul

St.-Gilles-les Bains

CIRQUE DE MAFATE

CIRQUE DE SALAZIE

Cilaos

CIRQUE DE CILAOS

Saint-Leu

Le Cap

Les Makes

Les Avirons

L’Étang-Salé

La Rivière

Saint-Louis

Saint-Pierre

Saint-Philippe

Piton de la Fournaise

Saint-Benoît

Saint-André

[Picha]

Picha iliyopigwa kutoka angani

Mawe ya volkano yaliyoyeyuka

Saint-Denis

[Sanduku katika ukurasa wa 232, 233]

Historia ya Réunion kwa Ufupi

Mabaharia Waarabu wa kale walikiita kisiwa hicho Dina Morgabin (Kisiwa cha Magharibi). Manahodha Wareno walipokivumbua mapema katika miaka ya 1500, walikiita Santa Apollonia. Wakati huo hakikuwa na wakaaji. Serikali ya Ufaransa ilianza kutawala kisiwa hicho Mfaransa Jacques Pronis alipowapeleka huko waasi 12 kutoka Madagaska mwaka wa 1642. Katika mwaka wa 1649, kilipewa jina la familia ya wafalme wa Ufaransa, na hivyo kikaitwa Île Bourbon. Familia ya Bourbon ilipoondolewa mamlakani mwaka wa 1793 wakati wa Mapinduzi ya Ufaransa, kilipewa jina Réunion kwa kumbukumbu ya muungano kati ya Walinzi wa Taifa wa Paris na wana-mapinduzi wa Marseille. Baada ya hapo jina lilibadilishwa mara kadhaa, lakini mwaka wa 1848 kisiwa hicho kikapewa tena jina Réunion. Kilifanywa kuwa jimbo la Ufaransa mwaka wa 1946.

Ufaransa ilianzisha koloni katika kisiwa hicho mapema katika miaka ya 1660. Mikahawa na miwa ilipandwa, na watumwa kutoka Afrika Mashariki wakaletwa kufanya kazi. Baada ya utumwa kukomeshwa mwaka wa 1848, serikali ya Ufaransa ilileta wafanyakazi kutoka India na Asia ya Kusini-Mashariki waliofanya kazi chini ya mkataba fulani. Watu wengi wanaoishi kisiwani humo leo ni machotara ambao ni uzao wa jamii hizo. Mapema katika miaka ya 1800 watu waliacha kupanda mikahawa na miwa ikawa zao kuu linalopelekwa nchi za nje kuuzwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 236, 237]

Niliacha Kujenga Misuli, Nikawa Painia wa Pekee

LUCIEN VÉCHOT

ALIZALIWA 1937

ALIBATIZWA 1961

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa akijenga misuli, jambo ambalo lilimletea umashuhuri. Alikuwa painia wa pekee kuanzia mwaka wa 1963 hadi 1968, na amekuwa mzee wa kutaniko tangu 1975.

NINAKUMBUKA vizuri siku moja mwaka wa 1961 nilipoenda nyumbani kwa rafiki yangu Jean ili “kumwokoa” asishambuliwe na Mashahidi wa Yehova. Mke wa Jean alikuwa amenialika, kwa sababu aliogopa kwamba Mashahidi, ambao aliwaita manabii wa uwongo, wangezusha mabishano makali na kumshambulia mumewe!

‘Wakimgusa, nitawatandika,’ niliwaza. Lakini walikuwa wenye urafiki na busara na hawakuonekana kuwa wajeuri hata kidogo. Punde nilijiunga na mazungumzo kuhusu msalaba, nao walionyesha wazi katika Biblia kwamba Yesu alikufa juu ya mti, si juu ya msalaba.

Baadaye, niliwaomba wanieleze nabii Danieli alimaanisha nini aliposema kwamba Mikaeli malaika mkuu ‘amesimama’ kwa ajili ya watu wa Mungu. (Dan. 12:1) Kwa kutumia Biblia Mashahidi walieleza kwamba Mikaeli ni Yesu Kristo naye ‘amesimama,’ yaani, ametawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu tangu mwaka wa 1914. (Mt. 24:3-7; Ufu. 12:7-10) Nilishangaa kusikia majibu hayo na kuona kwamba Mashahidi wana ujuzi mwingi wa Biblia. Kuanzia wakati huo, kila mara Mashahidi walipohubiri katika eneo letu, nilitumia pindi hizo kuzungumzia Neno la Mungu pamoja nao. Hata niliandamana nao kwenda nyumba kwa nyumba na kushiriki katika mazungumzo yao. Muda si mrefu nilianza kushirikiana na kikundi cha mbali cha Saint-André.

Sikuwa msomaji mzuri wakati huo. Hata hivyo, katika mkutano wangu wa kwanza, nilisoma baadhi ya mafungu ya gazeti Bulletin intérieur tulilotumia wakati huo badala ya Mnara wa Mlinzi. Kisha mara tu baada ya kubatizwa, nikaombwa niongoze funzo la kitabu kwa sababu hakukuwa na ndugu wengine wa kuliongoza. Lakini sikujua jinsi ya kuongoza funzo la kitabu. Dada Jeannine Pégoud alitambua wasiwasi wangu na kwa fadhili akapendekeza asome mafungu nami niulize maswali yaliyo katika kitabu. Basi ndivyo tulivyofanya, na funzo lilikuwa nzuri.

Milton Henschel alipotembelea Réunion mwaka wa 1963, aliwatia moyo wote waliostahili kuwa painia wa pekee wafikirie kufanya utumishi huo. Nilitaka kumtumikia Yehova kwa nafsi yote, kwa hiyo nilijaza fomu ya ombi na nikawekwa kuwa painia wa pekee. Nilitumwa mjini Saint-André, ambako hatimaye niliongoza mafunzo tisa ya Biblia.

Kutaniko jipya la mji huo lilifanya mikutano nyumbani kwa Jean Nasseau. Jean alipovunjika paja katika msiba wa barabarani, nilishughulikia mambo yote ya kutaniko kwa miezi sita. Ilinibidi kutoa hotuba, kuongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, na kuandika ripoti zilizotumwa kwenye ofisi ya tawi. Nilipata uzoefu muhimu katika kipindi hicho.

Tulipohubiri tulikabili ushirikina uliotokana na mchanganyiko wa mafundisho ya Kanisa Katoliki na Dini ya Hindu. Hata hivyo, watu walisikiliza habari njema. Katika familia moja angalau watu 20 walikubali kweli. Leo kuna makutaniko matano katika eneo la Saint-André.

[Picha katika ukurasa wa 238]

Imani Yangu Ilijaribiwa na Wadhihaki

MYRIAM THOMAS

ALIZALIWA 1937

ALIBATIZWA 1965

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Amekuwa painia tangu 1966.

MIMI na binamu yangu Louis Nelaupe tulipoanza kuhubiri mwaka wa 1962, tulikaribishwa katika karibu kila nyumba. Watu walitupa kahawa, maji ya limau, na hata kileo kikali! Hata hivyo, muda si muda makasisi waliwachochea watu wasitukaribishe. Baadhi ya wenye nyumba walitudhihaki. Nyakati nyingine walionyesha dharau kwa kulitamka jina la Mungu vibaya kimakusudi. Katika mji mmoja watu waliturushia mawe.

Kwa sababu hiyo baadhi yetu tuliacha kutumia jina la Mungu katika huduma. Mwangalizi wa mzunguko alitambua jambo hilo na akatuuliza kulihusu. Tuliona haya kidogo tulipomweleza sababu zetu. Kwa fadhili alitushauri na kututia moyo tuwe wenye ujasiri. Tulithamini sana mashauri yake na kuyaona kuwa nidhamu kutoka kwa Yehova. (Ebr. 12:6) Naam, subira, rehema, na roho takatifu ya Mungu zimenitia nguvu kuendelea katika utumishi wa painia kwa muda mrefu. Nimefurahia utumishi huo kwa miaka 40.

[Picha katika ukurasa wa 246]

Yehova Alinitegemeza Wakati wa Majaribu

SULLY ESPARON

ALIZALIWA: 1947

ALIBATIZWA: 1964

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU: Ni mmojawapo wa watu wa kwanza kubatizwa kisiwani Réunion. Alifungwa kwa miaka mitatu kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi.

NILIPOKUBALI kweli wazazi wangu walinifukuza nyumbani. Nilikuwa na miaka 15. Lakini hilo halikunivunja moyo nisiendelee kumtumikia Yehova. Nilianza utumishi wa painia wa kawaida mwaka wa 1964 na nikawa painia wa pekee 1965. Pia, nilikuwa na pendeleo la kusaidia kusimamia kutaniko la Saint-André lenye wahubiri 12 na la Saint-Benoît lenye wahubiri 6. Mimi na Jean-Claude Furcy tulikuwa tukisafiri kwa baiskeli tulipoenda kusaidia makutaniko hayo.

Mwaka wa 1967 niliitwa jeshini. Nilieleza kwamba mimi ni Mkristo na kwa sababu hiyo siwezi kujiunga na jeshi. Kwa kuwa nilikuwa mtu wa kwanza huko Réunion kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, wenye mamlaka hawakuelewa msimamo wangu wala hawakuukubali. Hata ofisa mmoja alinipiga mbele ya askari wapya 400, kisha akanipeleka ofisini mwake huku nikitembea kwa kuchechemea. Aliweka mavazi ya kijeshi juu ya dawati lake na kuniambia niyavae, la sivyo, angenipiga tena. Alikuwa mwenye urefu wa karibu mita 1.8, mkubwa sana kunishinda. Hata hivyo, nilipiga moyo konde na kusema, “Ukinipiga tena, nitawasilisha malalamiko rasmi, kwani kuna uhuru wa ibada chini ya utawala wa Ufaransa.” Alifoka kwa hasira na kutaka kunipiga lakini akajizuia. Kisha, akanipeleka kwa ofisa mkuu aliyeniambia kwamba ningehukumiwa kifungo cha miaka mitatu na kazi ngumu nchini Ufaransa.

Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu, lakini sikupelekwa Ufaransa wala sikupewa kazi ngumu. Baada ya kunihukumu, hakimu alinialika ofisini mwake. Alinishika mkono huku akitabasamu na kuniambia kwamba ananisikitikia lakini hakuwa na budi kufanya uamuzi kupatana na sheria. Msaidizi wa mkurugenzi wa gereza alikuwa mwenye urafiki pia, naye akapanga nifanye kazi katika chumba cha mahakama. Hata aliandamana nami sebuleni ili kuwasalimu wazazi wangu na ndugu fulani wa kutaniko letu.

Mwanzoni nilikaa pamoja na wafungwa wengine 20 hadi 30 katika chumba kimoja, lakini baadaye nikawekwa katika chumba cha watu 2. Hilo lilinipa uhuru zaidi. Niliomba taa ya umeme na jambo la kushangaza ni kwamba nilipewa moja. Kwa kawaida wafungwa hukatazwa kuwa na vifaa vya umeme kwa kuwa wanaweza kujaribu kujiua kwa kutumia umeme. Kwa sababu nilikuwa na taa hiyo, niliweza kujifunza Biblia na pia kukamilisha masomo ya hesabu kwa njia ya posta. Nilipoachiliwa mwaka wa 1970, hakimu mwenye fadhili alinisaidia kupata kazi.

[Sanduku katika ukurasa wa 249]

Vimbunga Hatari

Visiwa vya Réunion na Mauritius vilikumbwa na Kimbunga Jenny Februari 1962. Bahari ya Hindi ilichafuka sana na kusababisha mafuriko kwenye maeneo mbalimbali ya pwani ya visiwa hivyo, hasa huko Réunion. Majengo kadhaa huko Saint-Denis yaliharibika, majani ya miti yakapeperuka, na barabara zikajaa matawi yaliyokatika. Baadhi ya nguzo za umeme zilikuwa karibu kuanguka, huku nyaya za umeme zikining’inia chini ovyoovyo. Jambo la kushangaza ni kwamba lile Jumba la Ufalme dogo halikuharibika. Watu 37 walikufa, 250 wakajeruhiwa, na maelfu wakapoteza makao. Ndugu walikuwa wakihudhuria kusanyiko huko Mauritius wakati huo. Kisiwa hicho hakikuathiriwa sana, na ijapokuwa iliwabidi ndugu kungoja siku chache kabla ya kurudi nyumbani, hawakufa wala kujeruhiwa.

Katika mwaka wa 2002, Kimbunga Dina kilisababisha poromoko la ardhi lililofanya barabara ya Cilaos isipitike kwa majuma matatu. Mara moja ofisi ya Réunion ilipanga kupeleka misaada kwa ajili ya ndugu 30 walioishi huko. Gari linaloendeshwa kwa magurudumu manne lilijazwa bidhaa, nalo likajiunga na msafara wa magari mengine 15 ulioongozwa na polisi. Sehemu fulani za barabara ya lami zilikuwa zimeporomoka mtoni, na iliwabidi madereva kupitia chini ya mto, kisha kurudi barabarani. Ndugu huko Cilaos walifurahi sana gari hilo lilipofika.

[Picha katika ukurasa wa 252]

MFUATANO WA MATUKIO—Réunion

1955 Robert Nisbet atembelea Réunion mwezi wa Septemba.

1960

1961 Familia ya Mashahidi kutoka Ufaransa yafika na kupata watu wengi wanaopendezwa.

1963 M. G. Henschel kutoka makao makuu awahutubia watu 155.

1964 Ofisi ya tawi ya Mauritius yaanza kusimamia kazi badala ya ofisi ya Ufaransa; watu 230 wahudhuria kusanyiko la kwanza la mzunguko kisiwani Réunion.

1967 Shirika la Mashahidi wa Yehova (Association Les Témoins de Jéhovah) laandikishwa kisheria.

1970

1975 Marufuku juu ya Mnara wa Mlinzi yaondolewa nchini Ufaransa.

1980

1985 Idadi ya wahubiri yapita 1,000.

1990

1992 Idadi ya wahubiri yapita 2,000. Ofisi ya tawi yanunua kiwanja huko La Possession kwa ajili ya ofisi ya Réunion, Jumba la Kusanyiko, na makao ya wamishonari.

1996 Jumba la Ufalme lajengwa kwa mara ya kwanza kwa ile mbinu ya kujenga kwa muda mfupi.

1998 Kusanyiko la kwanza lafanywa katika Jumba jipya la Kusanyiko huko La Possession.

2000

2006 Kuna wahubiri watendaji 2,590 hivi kisiwani Réunion.

[Grafu]

(Ona nakala iliyochapishwa)

Jumla ya Wahubiri

Jumla ya Mapainia

3,000

2,000

1,000

1960 1970 1980 1990 2000

[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 223]

[Picha katika ukurasa wa 224]

Adam Lisiak alihubiri kwa mwezi mmoja mnamo 1959

[Picha katika ukurasa wa 224]

Noémie Duray, Jeannine Pégoud, na mwanawe, Christian, wakielekea Réunion mnamo 1961

[Picha katika ukurasa wa 227]

Jumba la Ufalme la Le Port mnamo 1965

[Picha katika ukurasa wa 230]

Mabasi yalikodishwa kwa ajili ya safari za kuhubiri mnamo 1965

[Picha katika ukurasa wa 230]

Josette Bonnecaze

[Picha katika ukurasa wa 235]

Jeannine Corino

[Picha katika ukurasa wa 235]

Kuhubiri huko Saint-Paul mnamo 1965

[Picha katika ukurasa wa 243]

Cléo Lapierre

[Picha katika ukurasa wa 244, 245]

Louis na Anne Nelaupe walihubiri katika vijiji vya mbali nao walikula mapera njiani

Cirque de Mafate

[Picha katika ukurasa wa 248]

Jumba la Ufalme lililojengwa Saint-Louis mnamo 1988

[Picha katika ukurasa wa 251]

Makusanyiko

Kusanyiko la kwanza la mzunguko kisiwani Réunion lilifanywa katika mkahawa uliokuwa ghorofani mnamo 1964

Mahali panapoitwa “Pango la Wafaransa wa Kwanza” ambapo kusanyiko la wilaya lilifanyiwa

Jengo la muda la kufanyia mikutano huko Saint-Denis mnamo 1965

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki