-
Latvia2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka wa 1992, ndugu watatu wanaozungumza Kilatvia, ambao walilelewa Marekani, walipata pendeleo la kutumikia wakiwa wamishonari nchini Latvia. Majina yao na ya wake zao ni Valdis na Linda Purin̗š, Alfreds na Doris Elksnis, na Ivars Elksnis, ndugu ya Alfreds. Wote watano walifika Riga Julai 1992. Nyumba yao yenye vyumba vinne ilitumiwa kama makao ya wamishonari, depo ya vichapo, na ofisi ya kutafsiri.
Ucheshi humsaidia mtu anapojifunza lugha nyingine. Doris Elksnis anasema: “Nilipokuwa nikijifunza pamoja na wasichana wawili, nilijaribu kueleza jinsi Shetani alivyoongea na Hawa kwa kutumia nyoka. Lakini, nilitumia neno la Kilatvia linalotamkwa sawa na neno ‘nyoka.’ Hata hivyo, nilisema kwamba Ibilisi alizungumza kupitia nguruwe!”
-
-
Latvia2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MSAADA WA WAHITIMU WA GILEADI
Wamishonari wa kwanza kuzoezwa Gileadi walifika mapema mwaka wa 1993. Wenzi wa ndoa kutoka Sweden, Anders na Agneta Berglund na Torgny na Lena Fridlund walipewa mgawo wa kutumika Jelgava, jiji lenye wakaaji zaidi ya 60,000 na wahubiri 28. Anders, ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, anasema: “Tulipofika, tulijiunga na akina ndugu katika utumishi wa shambani, na sikuzote tulikuwa na mengi ya kufanya katika huduma! Siku fulani-fulani, kwa muda wa saa saba au nane, ni kana kwamba tulikuwa tukikimbia pamoja nao kutoka funzo moja hadi lingine bila kupumzika ili kula! Bidii yao ilituchochea. Sasa, wengi wa wanafunzi hao ni watumishi wa wakati wote.”
Torgny Fridlund anakumbuka hivi: “Baada ya kufundishwa lugha kwa miezi mitatu, tuliona kwamba tunaweza kuzungumza bila msaada. Tulichagua eneo ambalo halikuwa limehubiriwa tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, lakini hatukufanikiwa sana. Je, tulitumia mbinu zisizofaa? Baada ya kuzungumzia jambo hilo, tulijaribu mbinu nyingine, yaani, kusoma andiko kwenye kila mlango. Tangu wakati huo, tukaanzisha mafunzo kadhaa.”
Wahitimu zaidi wa Gileadi walianza kufika Aprili 1995. Hao ni kutia ndani Basse na Heidi Bergman kutoka Finland, ambao sasa wanafanya kazi ya kusafiri katika mzunguko wa Kirusi. Basse anasema: “Niliwaomba ndugu wa eneo hilo wanisahihishe ninapokosea katika huduma. Walifanya hivyo kwa bidii, nao wakanisahihisha shambani na hata mikutano ikiendelea! Siku hizi, mimi hufurahi kusikia ndugu wakisema, ‘Basse amekuwa mmoja wetu.’”
Carsten na Jannie Ejstrup, kutoka Denmark, walitumika pamoja nchini Latvia mpaka Jannie alipokufa kutokana na kansa akiwa tu na miaka 30 na kitu. Carsten anasema: “Njia bora ya kumheshimu Yehova ni kuendelea kuwa mwaminifu katika mgawo wangu wa umishonari.” Ndugu hao ni mfano bora kwelikweli!
-