-
Je, Unapenda Uhai?Mnara wa Mlinzi—1999 | Agosti 15
-
-
Je, Unapenda Uhai?
“ACHENI nione nuru.” Haya ndiyo maneno ambayo yasemekana Giacomo Leopardi, mshairi Mwitalia, aliwaambia wale waliomhudumia kabla hajafa. Maneno hayo yadokeza jinsi mwanadamu anavyoupenda uhai, ambao wafananishwa na nuru.
Kupenda uhai ni msukumo wenye thamani unaofanya watu wengi waepuke hatari na kufanya yote wawezayo kuendelea kuishi. Kwa habari hiyo, mwanadamu si tofauti sana na wanyama, ambao wana silika yenye nguvu ya kutaka kuendelea kuishi.
Lakini ni uhai wa aina gani ambao kwa kweli twastahili kuwa nao na kuupenda? Si kuishi tu kifiziolojia—kupumua tu na kutembea. Wala kutosheka kwa ujumla hakutokani na ule mtazamo wa kutaka kujinufaisha maishani kadiri tuwezavyo. Falsafa ya Waepikurea, “acheni tule na tunywe, kwa maana kesho tutapaswa kufa,” kwa kawaida haiwaridhishi watu. (1 Wakorintho 15:32) Ingawa kwa hakika mwanadamu ana mahitaji kadhaa ya kimwili yaliyo ya msingi, yeye pia ana mapendezi ya kitamaduni na ya kijamii, mbali na mahitaji ya kiroho, yanayohusu imani katika Mtu Mkuu Kuliko Wote. Kwa kusikitisha, mamia ya mamilioni, labda mabilioni ya watu wanapata mahitaji ya lazima tu ya maisha kwa sababu ya hali mbaya za kijamii na za kimazingira katika sehemu nyingi za ulimwengu. Watu wowote wanaotaka kutosheleza mahitaji yao ya kimwili tu—kula, kunywa, kuwa na mali, au kutosheleza tamaa za kingono—kwa kadiri fulani wanaishi kama wanyama, maisha yasiyoweza kuwaridhisha. Kwa hiyo, hawatumii rasilimali zenye maana zaidi zipatikanazo maishani ili kuridhisha akili na hisia za kibinadamu. Isitoshe, wowote wanaotaka kutosheleza tamaa zao za ubinafsi hawashindwi tu kunufaika kabisa maishani, bali pia hudhuru jamii ambamo wanaishi, nao hawaendelezi masilahi ya wengine.
Akithibitisha hilo, hakimu mmoja anayeshughulika na watoto wahalifu asema kwamba “matatizo ya maadili, kutukuzwa kwa violezo vya kuigwa visivyofaa, na kufanikiwa kwa njia za kutajirika upesi,” huelekea “kuendeleza roho iliyokuzwa sana ya kushindana.” Roho hiyo hutokeza tabia inayodhuru jamii na kuharibu vijana, hasa wanapoanza kutumia dawa za kulevya.”
Unajua kwamba maisha yana vivutio vingi—kwenda likizo sehemu zenye kupendeza, kusoma au kufanya utafiti wenye kupendeza, ushirika wenye kupendeza, muziki mzuri. Na kuna shughuli nyingine zinazoridhisha kwa njia mbalimbali. Wale walio na imani kubwa katika Mungu, na hasa Mungu wa Biblia, Yehova, wana sababu zaidi za kupenda uhai. Imani ya kweli ni chanzo cha nguvu na utulivu uwezao kuwasaidia watu wakabiliane na nyakati ngumu. Wanaomwamini Mungu wa kweli wanaweza kusema hivi kwa uhakika: “Yehova ni msaidiaji wangu; hakika sitaogopa.” (Waebrania 13:6) Watu wanaojua upendo wa Mungu huhisi anawapenda. Wao huitikia upendo wake, unaowaletea furaha nyingi. (1 Yohana 4:7, 8, 16) Wanaweza kuishi maisha yenye shughuli na yanayonufaisha wengine, ambayo ni chanzo cha uradhi. Ni kama vile Yesu Kristo alivyosema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Kwa kusikitisha, maisha ya sasa yahusisha mambo mengine pia. Kuteseka, ukosefu wa haki, umaskini, ugonjwa, na kifo zimeenea sana—kutaja tu baadhi ya sehemu zenye kuumiza zinazofanya maisha yawe magumu sana. Mfalme Solomoni wa taifa la Israeli la kale, aliyekuwa tajiri, mwenye uwezo, na hekima, alikuwa na rasilimali zote ziwezazo kufanya watu wawe na furaha. Hata hivyo, kuna kitu fulani kilichomsumbua—kung’amua kwamba wakati wa kufa angelazimika kumwachia mtu mwingine vitu vyote alivyokuwa amejipatia kwa ‘kazi yake yote’ aliyoifanya “kwa hekima, na kwa maarifa, na kwa ustadi.”—Mhubiri 2:17-21.
Kama Solomoni, wengi wanafahamu ufupi wa uhai, ambao hupita upesi sana. Maandiko yasema kwamba Mungu “ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo [yetu].” (Mhubiri 3:11) Huku kufahamu umilele humfanya mwanadamu afikirie kwa uzito ufupi wa uhai. Hatimaye, kwa kutopata majibu yenye kusadikisha juu ya maana ya uhai na kifo, mtu aweza kulemewa na hisia za kutazamia mabaya na ubatili. Hilo laweza kufanya maisha yawe yenye kusikitisha.
Je, kuna majibu kwa maswali yanayomsumbua mwanadamu? Je, kutapata kuwako hali zinazofanya uhai uwe wenye kupendeza na wenye kudumu?
-
-
Furahia “Uhai Ulio Halisi”Mnara wa Mlinzi—1999 | Agosti 15
-
-
Furahia “Uhai Ulio Halisi”
YEHOVA MUNGU amempa mwanadamu uwezo wa kuelewa umilele. (Mhubiri 3:11) Hilo hufanya wanadamu wahisi hawana uwezo wanapokabili kifo lakini, wakati huohuo, huamsha ndani yao tamaa yenye nguvu ya kutaka kuishi.
Biblia Takatifu, Neno la Mungu lililopuliziwa, hutupa tumaini kubwa. (2 Timotheo 3:16) Yehova, ambaye ndiye kiini cha upendo, hangeweza kumwumba mwanadamu akiwa na uwezo wa kuelewa wazo la umilele, kisha amhukumu kuishi miaka michache tu. Kutuumba ili tuteseke kwa sababu ya hali yetu ni kinyume kabisa na utu wa Mungu. Hatukuumbwa kama “wanyama wasiofikiri waliozaliwa kiasili ili kukamatwa na kuangamizwa.”—2 Petro 2:12.
Kwa kuwaumba Adamu na Hawa wakiwa na uwezo wa kiasili wa kuelewa umilele, Yehova Mungu aliumba kitu kilichokuwa “chema sana”; aliwaumba wakiwa na uwezo wa kuishi milele. (Mwanzo 1:31) Lakini yasikitisha kwamba wenzi hao wa kwanza walitumia vibaya hiari yao, kwa kutotii katazo la Muumba lililokuwa wazi na hivyo kupoteza ukamilifu wao wa awali. Kwa sababu hiyo, wakafa, baada ya kurithisha wazao wao kutokamilika na kifo.—Mwanzo 2:17; 3:1-24; Waroma 5:12.
Biblia huonyesha wazi kabisa kusudi la uhai na maana ya kifo. Hiyo yasema kwamba katika kifo “hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima” na kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, 10) Yaani, wafu wamekufa. Fundisho la nafsi isiyoweza kufa halitokani na Biblia, kwa hiyo hakuna fumbo kubwa linalohitaji kufumbuliwa kuhusu hali ya wafu.—Mwanzo 3:19; Zaburi 146:4; Mhubiri 3:19, 20; Ezekieli 18:4.a
Mungu alikuwa na kusudi; hakuiumba dunia “ukiwa.” Aliiumba “ili ikaliwe” na watu wakamilifu katika hali za kiparadiso, naye Mungu hakubadili kusudi lake. (Isaya 45:18; Malaki 3:6) Ili kulitimiza, alimtuma Mwana wake duniani. Kwa kudumu akiwa mwaminifu hadi kifo, Yesu Kristo aliandaa njia ya kufidi wanadamu kutoka katika dhambi na kifo. Kwa kweli, Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.
Mungu aliahidi zamani sana kwamba angeumba “mbingu mpya na dunia mpya.” (Isaya 65:17, NW; 2 Petro 3:13) Hilo lingehusisha kuchagua kikundi cha Wakristo waaminifu wachache ili wakaishi mbinguni. Wao pamoja na Yesu Kristo wanafanyiza kiini cha serikali. Biblia hurejezea serikali hiyo kuwa “ufalme wa mbingu,” au “ufalme wa Mungu,” utakaosimamia “vitu vilivyo duniani.” (Mathayo 4:17; 12:28; Waefeso 1:10; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3) Baada ya kuangamiza uovu wote na kuusafisha ulimwengu wetu, Mungu ataleta jamii ya kibinadamu yenye uadilifu, au “dunia mpya.” Hiyo itatia ndani watu watakaolindwa na Mungu ili waokoke uharibifu unaokaribia wa mfumo huu mwovu wa mambo. (Mathayo 24:3, 7-14, 21; Ufunuo 7:9, 13, 14) Wale watakaorudishwa kwenye uhai kupitia ufufuo ulioahidiwa watajiunga nao.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.
“Uhai Ulio Halisi” Wakati Huo
Kwa kuhakikisha ufafanuzi wenye kusisimua wa uhai kwenye Paradiso ya wakati ujao duniani, Mungu asema: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Akili ya kibinadamu haiwezi kuelewa kabisa matendo ya ajabu ambayo Mungu atafanyia wanadamu. Mungu atatokeza paradiso ya ulimwenguni pote, mfano wa Edeni. (Luka 23:43) Kama katika Edeni, umaridadi na uzuri wa rangi, sauti, na ladha zitakuwepo kwa wingi. Umaskini na upungufu wa chakula hautakuwapo tena, kwa kuwa Biblia yasema hivi kuhusu wakati huo: “Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4; Zaburi 72:16) Hakutakuwepo tena yeyote anayesema, “Mimi mgonjwa,” kwa kuwa ugonjwa utaondolewa milele. (Isaya 33:24) Naam, visababishi vyote vya maumivu vitatoweka, kutia ndani kifo ambacho ni adui wa muda mrefu wa mwanadamu. (1 Wakorintho 15:26) Katika ono lenye kushangaza la “dunia mpya,” ambayo ni jamii mpya ya wanadamu chini ya utawala wa Kristo, mtume Yohana alisikia sauti ikisema: “[Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” Je, ni kitu gani kiwezacho kuleta faraja na furaha zaidi kuliko kutimizwa kwa ahadi hii ya Mungu?
Inapofafanua uhai wa wakati ujao, Biblia hasa hukazia hali zitakazotosheleza tamaa za kiadili na za kiroho za mwanadamu. Miradi yote ya haki ambayo hadi sasa mwanadamu amejitahidi kuifikia bila kufanikiwa, itatimizwa kikamili. (Mathayo 6:10) Kati ya hiyo, kuna tamaa ya kupata haki, ambayo haijawahi kutimizwa kwa sababu mara nyingi mwanadamu ameteswa na waonezi wenye ukatili ambao wamewatawala walio dhaifu. (Mhubiri 8:9) Mtunga-zaburi aliandika kiunabii kuhusu hali zitakazokuwepo chini ya utawala wa Kristo: “Katika siku zake unyofu utasitawi, na amani kwa wingi.”—Zaburi 72:7, The New Jerusalem Bible.
Usawa ni jambo jingine ambalo limefanya wengi wajitolee mhanga. Katika ‘uumbaji-mpya,’ Mungu atakomesha ubaguzi. (Mathayo 19:28) Wote watakuwa na hadhi sawa. Huo hautakuwa usawa wenye kulazimishwa na utawala fulani wenye ukatili. Kinyume chake, visababishi vya ubaguzi vitaondolewa, kutia ndani pupa na kiburi ambacho hufanya wanadamu watake kutawala wengine au kulimbika mali nyingi sana. Isaya alitabiri: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.”—Isaya 65:21, 22.
Mwanadamu ameteseka kama nini kwa sababu ya umwagaji damu katika vita vya kibinafsi na vya watu wengi! Hali hiyo imeendelea tangu kuuawa kimakusudi kwa Abeli hadi vita vya wakati wa sasa. Wanadamu wametumaini na kungoja kwa muda mrefu kama nini, yaonekana bila mafanikio, kupatikana kwa amani! Katika Paradiso itakayorudishwa, wanadamu wote watakuwa wenye amani na wapole; “watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
Andiko la Isaya 11:9 lasema: “Dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” Kwa sababu ya kutokamilika tulikorithi, pamoja na sababu nyinginezo, hatuwezi kuelewa kabisa maana kamili ya maneno hayo. Huenda tutaendelea kujifunza zaidi jinsi ujuzi mkamilifu juu ya Mungu utakavyotuunganisha naye na kutokeza furaha kamili. Lakini kwa kuwa Maandiko hutujulisha kwamba Yehova ni Mungu mwenye nguvu, hekima, haki, na upendo mwingi sana, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atasikiliza sala zote zenye kutolewa na wakazi wa “dunia mpya.”
“Uhai Ulio Halisi” Ni Hakika—Ushike!
Kwa maoni ya wengi, uhai udumuo milele katika ulimwengu mzuri zaidi ni ndoto tu au jambo la kuwaziwa tu. Hata hivyo, kwa wale wanaoamini kikweli ahadi ya Biblia, tumaini hilo ni hakika. Ni kama nanga ya maisha yao. (Waebrania 6:19) Kama vile nanga huifanya meli imara na kuizuia isiyumbeyumbe, tumaini la uhai udumuo milele hufanya watu wawe imara na wenye uhakika nalo huwawezesha kukabili na kushinda matatizo makubwa maishani.
Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatimiza ahadi zake. Hata ametoa uhakikisho kwa kiapo, uwajibikaji usioweza kubatilishwa. Mtume Paulo aliandika: “Mungu, wakati alipokusudia kuwaonyesha kwa wingi zaidi warithi wa ahadi kule kutobadilika kwa shauri lake, aliingia kwa kiapo, ili, kupitia mambo mawili yasiyobadilika ambayo katika hayo haiwezekani Mungu kusema uwongo, sisi . . . tupate kuwa na kitia-moyo chenye nguvu tukishikilia tumaini lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 6:17, 18) “Mambo [hayo] mawili yasiyobadilika” ambayo Mungu hawezi kuyabatilisha ni ahadi yake na kiapo chake, tunazotegemea.
Imani katika ahadi za Mungu hufariji sana na kuimarisha kiroho. Yoshua, kiongozi wa watu wa Israeli, alikuwa na imani kama hiyo. Alipowatolea Waisraeli hotuba yake ya kuwaaga, Yoshua alikuwa mzee naye alijua kwamba anakaribia kufa. Hata hivyo, alionyesha uthabiti na uaminifu-mshikamanifu imara, uliotokana na kutumaini kabisa ahadi za Mungu. Baada ya kusema kwamba anaenda “njia ile waendayo watu wote wa ulimwengu,” njia iongozayo wanadamu wote kwenye kifo, Yoshua alitaarifu hivi: “Nanyi nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena BWANA, Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu hapana neno lo lote mlilopungukiwa.” Naam, Yoshua alirudia mara tatu kwamba sikuzote Mungu hutimiza ahadi zake zote.—Yoshua 23:14.
Wewe pia unaweza kuwa na imani hiyohiyo katika ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya ambao utaanzishwa karibuni. Kwa kujifunza Biblia kwa bidii, utakuja kuelewa Yehova ni nani na kwa nini astahili umtumaini kabisa. (Ufunuo 4:11) Abrahamu, Sara, Isaka, Yakobo, na waaminifu wengine wa zamani walikuwa na imani thabiti, iliyotegemea ujuzi wao wa ndani kuhusu Mungu wa kweli, Yehova. Waliendelea kuwa na tumaini lenye nguvu, licha ya uhakika wa kwamba “hawakupata utimizo wa ahadi” walipokuwa hai. Hata hivyo, “waliziona kwa mbali na kuzikaribisha.”—Waebrania 11:13.
Kwa kuelewa unabii mbalimbali wa Biblia, sasa twaona kukaribia kwa “siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” ambapo uovu wote utaondolewa duniani. (Ufunuo 16:14, 16) Kama watu waaminifu wa zamani, yatupasa kudumu tukiwa na tarajio lenye uhakika kuhusu matukio ya wakati ujao, tukichochewa na imani na vilevile upendo wetu kwa Mungu na kwa “uhai ulio halisi.” Kukaribia kwa ulimwengu mpya hutoa kichocheo chenye nguvu kwa wale wadhihirishao imani katika Yehova na kumpenda. Imani na upendo huo wahitaji kusitawishwa ili kupata upendeleo na ulinzi wa Mungu wakati wa siku yake kubwa inayokaribia.—Sefania 2:3; 2 Wathesalonike 1:3; Waebrania 10:37-39.
Kwa hiyo, je, unapenda uhai? Na je, unatamani hata zaidi “uhai ulio halisi”—uhai ukiwa mtumishi aliyekubaliwa na Mungu, ukiwa na tarajio la kuwa na wakati ujao wenye furaha, naam, ukitarajia uhai udumuo milele? Ikiwa unatafuta uhai huo, basi tii himizo la mtume Paulo, aliyeandika kwamba twapaswa ‘kuweka tumaini letu, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu.’ Paulo aliendelea kusema: ‘Iweni matajiri katika kazi zilizo bora,’ zinazomheshimu Mungu, ili “kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.”—1 Timotheo 6:17-19.
Kwa kukubali toleo la kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, unaweza kujipatia ujuzi ambao ‘wamaanisha uhai udumuo milele.’ (Yohana 17:3) Kwa upendo, Biblia hurekodi mwaliko huu ulio kama wa baba kwa wote: “Mwanangu, usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku. Na miaka ya uzima, na amani.”—Mithali 3:1, 2.
-