-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KUSANYIKO LA KIMATAIFA LENYE KUSISIMUA
Mashahidi wa Yehova nchini Yugoslavia walikuwa hawajawahi kupata shangwe ya kupanga kusanyiko la kimataifa. Fikiria jinsi walivyosisimka mwaka wa 1991 Baraza Linaloongoza lilipotangaza kwamba moja ya makusanyiko ya kimataifa ya “Wapendao Uhuru” lingefanywa huko Zagreb, Kroatia!
Hata hivyo, kulikuwa na matatizo. Tangu Kroatia ilipotangaza uhuru wake kutoka kwa Yugoslavia, tishio la vita lilikuwa linakaribia zaidi na zaidi. Je, lingekuwa jambo la hekima kufanya kusanyiko? Usalama wa wajumbe kutoka nchi za kigeni na wenyeji ulikuwa ndilo jambo la maana zaidi. Baada ya kusali sana na kufikiria mambo yote, ndugu waliamua kuendelea na matayarisho ya kusanyiko hilo.
Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alienda Kroatia majuma machache kabla ya kusanyiko ili kusaidia katika matayarisho hayo. Kwa kuwa matukio mengine yote ya hadharani huko Zagreb yalikuwa yamefutwa, watu walitaka sana kujua kile ambacho kingetukia katika Uwanja wa Dinamo. Kadiri wakati wa kusanyiko ulivyokuwa ukikaribia, hali nchini iliendelea kuharibika. Kila siku ndugu walikadiria hatari, wakijiuliza swali lilelile tena na tena—Je, tunapaswa kuendelea na matayarisho, au kusanyiko linapaswa kufutwa? Ndugu waliendelea kusali kwa bidii kwa Yehova, wakiomba mwongozo wake. Jambo la kushangaza ni kwamba hali ya kisiasa ilitulia, na ndugu waliweza kufanya kusanyiko hilo toka Agosti (Mwezi wa 8) 16-18, 1991.
Kulikuwa na tofauti kubwa kama nini! Wakati nchi jirani zilipokuwa karibu kuanza vita vyenye jeuri, Mashahidi wa Yehova huko Kroatia walikuwa wakiwakaribisha maelfu ya wageni kwa ajili ya kusanyiko la kimataifa la “Wapendao Uhuru wa Kimungu.”b Wenyeji wengi walipokuwa wakikimbia kutoka nchini, ndugu na dada kutoka nchi 15 walikuwa wakikusanyika pamoja kwa upendo na uhuru. Wengi walikuja kwa ndege kutoka Marekani, Kanada, na nchi nyingine za Magharibi. Kwa sababu ya hali ya kijeshi, uwanja wa ndege wa Zagreb ulifungwa na ndege zilitua huko Ljubljana, Slovenia. Kutoka huko wajumbe walisafiri kwa basi mpaka Zagreb. Ujasiri wa ndugu wageni ulikuwa ushahidi mzuri kwa watu, na kuwapo kwao kuliwatia moyo sana ndugu wenyeji. Kundi lililokuwa kubwa zaidi lenye wajumbe 3,000 hivi lilitoka Italia. Ilionekana kwamba upendo na shauku yao ilifanya kusanyiko hilo liwe lenye kusisimua sana.—1 The. 5:19.
Lilikuwa jambo lenye kujenga imani hasa kutembelewa na washiriki watano wa Baraza Linaloongoza. Mpaka leo hii wengi wanakumbuka kwa shangwe hotuba zilizotolewa na Carey Barber, Lloyd Barry, Milton Henschel, Theodore Jaracz, na Lyman Swingle. Ndugu hao wenye uzoefu wa miaka mingi ambao hawatishwi na nyakati hizi zenye misukosuko, waliingia kwa ujasiri nchini ili kuwatia nguvu akina ndugu kupitia hotuba zao zenye kujenga.
Kwa sababu ya misukosuko ya kisiasa, wenye mamlaka waliogopa kwamba kungekuwa na vita vya kikabila kati ya wajumbe kutoka sehemu mbalimbali za Yugoslavia. Waliacha kuwa na wasiwasi walipoona wajumbe wakikusanyika pamoja kwa amani, na pia wakionyeshana shauku na upendo wa kindugu. Hesabu ya polisi waliokuja kusanyikoni ilipungua siku baada ya siku.
Kusanyiko hilo lisiloweza kusahauliwa lilionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wana undugu wa kweli wa ulimwenguni pote. Kutafakari juu ya kusanyiko hilo kungesaidia akina ndugu kudumisha umoja wakati wa majaribu yaliyokuwa mbele yao. Mabasi yaliyobeba wajumbe kutoka Serbia na Makedonia yalikuwa kati ya magari ya mwisho kuruhusiwa kurudi nyumbani kupitia kituo cha ukaguzi kati ya Kroatia na Serbia. Baada ya ndugu zetu kuvuka mpaka kwa usalama, mpaka ulifungwa. Watu wengi wanasema kuwa vita vilianza wakati huo.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
b Kwa sababu ya hali ya kisiasa, neno “Kimungu” liliongezwa kwenye kichwa cha kusanyiko ili kuonyesha uhuru ambao akina ndugu walikuwa wakitafuta.
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 192]
Milton Henschel akitoa hotuba, na chini, ubatizo kwenye Kusanyiko la Kimataifa la “Wapendao Uhuru wa Kimungu” mwaka wa 1991, Zagreb, Kroatia
-