-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Katika mwaka wa 1968, kijana mmoja kutoka Kočani, Makedonia, alikuwa akisoma kwenye chuo kimoja huko Zagreb, ambako alipata kweli. Aliporudi nyumbani, aliwahubiria habari njema watu wake wa ukoo na marafiki.
Stojan Bogatinov, ambaye alikuwa mtu wa kwanza kubatizwa kutoka Kočani, anakumbuka: “Kijana huyo alikuwa binamu yangu. Nilikuwa mhudumu wa hoteli, na mara nyingi mimi na wafanyakazi wenzangu tulizungumza kuhusu dini. Pindi moja baada ya mazungumzo yetu, mshiriki wa Kanisa Othodoksi aliingia hotelini kula chakula. Nilipokuwa nikimhudumia, nilimuuliza ikiwa ningeweza kupata Biblia kutoka katika kanisa lao, kwa sababu nilitaka sana kujifunza kuhusu Mungu. Aliniambia kwamba angejaribu kuniletea nakala moja. Punde si punde, nilipata nakala yangu ya ‘Agano Jipya.’ Nilifurahi sana hivi kwamba baada ya kazi nilirudi nyumbani haraka ili nianze kuisoma.
“Nikiwa njiani, nilishangaa kumwona binamu yangu, aliyerudi kutoka Zagreb. Alinialika nyumbani kwake, lakini nikamwambia kwamba singeweza kwenda kwa sababu nilikuwa na msisimko mwingi wa kurudi nyumbani ili nisome Biblia yangu. ‘Nina kitu fulani ambacho kitakupendeza,’ binamu yangu akanijibu. ‘Nyumbani nina vitabu ambavyo vitakusaidia kuielewa Biblia.’ Tulienda nyumbani kwake, na nilifurahi kuona kwamba alikuwa na Biblia nzima, broshua kadhaa, na magazeti kadhaa ya Mnara wa Mlinzi ya Kikroatia. Alinipa vichapo hivyo, nikaanza kuvisoma mara moja. Papo hapo, nilitambua kwamba nilikuwa nikisoma kitu fulani cha pekee. Sikujua jambo lolote kuhusu Mashahidi wa Yehova, lakini nilitaka kuwajua.
“Binamu yangu aliporudi Zagreb, nilienda pamoja naye. Nikiwa huko, Shahidi mmoja mkarimu, Ivica Pavlaković, alinialika nyumbani kwake, ambako nilikaa kwa muda wa siku tatu. Wakati huo niliuliza maswali mengi, na nyakati zote alijibu maswali yangu kwa kutumia Biblia, jambo ambalo lilinivutia sana. Nilihudhuria mkutano wa kutaniko na nilitiwa moyo na ushirika mchangamfu wa kindugu.
“Ivica alinipeleka Betheli huko Zagreb, na nilitoka huko nikiwa mwenye furaha na nikiwa na vichapo vingi. Baada tu ya siku chache ambazo singeweza kusahau, nilirudi Kočani nikiwa na hazina ya kiroho niliyopata. Hakukuwa na Mashahidi walioishi karibu, hivyo tulianza kuandikiana kwa ukawaida na Ivica. Barua zangu zilijaa maswali mengi, na Ivica aliniandikia majibu ya maswali hayo. Kadiri nilivyojifunza zaidi, ndivyo nilivyowaambia wengine mambo niliyojifunza, na mke na watoto wangu wakaanza kupendezwa. Punde si punde, familia yetu iliungana katika kweli, na tukajifunza mengi kuhusu Biblia. Tulifurahi, na kwa bidii tulianza kuzungumza na watu wetu wa ukoo na marafiki kuhusu habari njema; na wengi walitusikiliza. Lakini pamoja na kuhubiri mateso pia yalifuata.”
-
-
Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 182]
Stojan Bogatinov
-