Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Historia ya Kisasa ya Makedonia

      “Vuka uingie Makedonia utusaidie,” hivyo ndivyo mwanamume fulani alivyomwambia mtume Paulo katika maono katika karne ya kwanza. (Mdo. 16:8-10) Paulo na wahubiri wenzake walikubali mwaliko huo kwa kuwa walikata kauli kwamba Mungu alikuwa akiwaongoza wahubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika eneo hilo lisilohubiriwa. Muda si muda, Ukristo ulianza kusitawi katika eneo hilo. Ibada ya kweli imesitawi jinsi gani katika Makedonia ya leo, ambayo iko katika eneo dogo upande wa kaskazini wa Makedonia ya zamani?

      Baada ya vita vya pili vya ulimwengu, Makedonia ilikuwa jamhuri ya kusini kabisa ya nchi ya Yugoslavia. Ilipata uhuru mwaka wa 1991. Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1993, Mashahidi wa Yehova walishangilia sana walipoandikishwa rasmi katika nchi hiyo mpya. Kwa hiyo, ofisi ya tawi ingeweza kuanzishwa huko Makedonia chini ya usimamizi wa Halmashauri ya Tawi ya Austria. Hivyo basi, katika mwaka wa 1993, nyumba ilinunuliwa kwenye Barabara ya Alžirska, huko Skopje, na kikundi cha kutafsiri vichapo vya Kimakedonia kikahamia kwenye Betheli hiyo mpya kutoka Zagreb, Kroatia.

      Michael na Dina Schieben kutoka Ujerumani walikuja kufanya kazi ya mzunguko, na Daniel na Helen Nizan, kutoka Kanada, ambao walikuwa wakitumika huko Serbia, walitumwa Makedonia. Halmashauri ya Nchi ilianzishwa, na Betheli ikaanza kufanya kazi.

      VICHAPO VINAZUIWA

      Ingawa Mashahidi wa Yehova walikuwa wameandikishwa rasmi, ilikuwa vigumu kuingiza vichapo nchini humo. Kuanzia mwaka wa 1994 mpaka 1998, serikali iliweka sheria iliyomruhusu kila mhubiri kupata gazeti moja peke yake. Kwa hiyo, ndugu walilazimika kufanya nakala za makala za funzo za Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya wanafunzi wao wa Biblia. Akina ndugu walitumiwa pia magazeti kutoka katika nchi nyingine, na wageni waliokuja Makedonia waliruhusiwa kubeba kiasi fulani cha magazeti. Mwishowe, baada ya kesi kusikizwa kwa miaka mingi, mahakama kuu ilifanya uamuzi uliowatetea Mashahidi, hivyo wakaruhusiwa kuingiza nchini vichapo vingi kadiri walivyotaka.

      Mnamo Agosti, mwaka wa 2000, hesabu ya wahubiri ilifikia 1,024. Ilikuwa mara ya kwanza kwa wahubiri zaidi ya 1,000 kushiriki katika utumishi wa shambani! Huku vichapo vingi zaidi vikichapishwa katika Kimakedonia na wahubiri wakiongezeka, jengo walilotumia kwenye Barabara ya Alžirska halikutosha tena familia ya Betheli iliyokuwa ikiongezeka. Mwaka uliofuata, nyumba nyingine tatu zilizo karibu zilinunuliwa na kubomolewa ili majengo mawili mapya yajengwe. Leo, washiriki 34 wa familia ya Betheli ya Makedonia wanafanya kazi na kuishi katika majengo matatu yenye vifaa vingi. Walifurahi wakati Guy Pierce wa Baraza Linaloongoza alipowatembelea wakati wa programu ya kuweka wakfu majengo hayo mnamo Mei 17, 2003.

      UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME

      Ndugu na dada katika nchi yote ya Makedonia wamethamini sana mpango wa kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi maskini. Kikundi cha ujenzi chenye ndugu watano kilipewa mgawo wa kusaidia makutaniko kujenga Majumba ya Ufalme nchini; na kati ya 2001 na 2007, Majumba tisa mapya ya Ufalme yalijengwa. Kikundi hicho cha ujenzi chenye wafanyakazi wanaotoka nchi mbalimbali kimetoa ushahidi mzuri kwa kufanya kazi kwa amani na umoja bila ubaguzi wa kikabila. Mfanyabiashara mmoja aliyefika kwenye Jumba la Ufalme lililokamilika aliona kwamba lilijengwa kwa ufundi wa hali ya juu sana, akasema, “Kwa kweli jengo hili lilijengwa kwa upendo.”

      Kikundi cha ujenzi kilipokuwa kikijenga Jumba jipya la Ufalme katika mji wa Štip, jirani mmoja alifikiri kwamba mradi huo haungeweza kufanikiwa kwa sababu wajenzi walionekana vijana wasio na uzoefu. Hata hivyo, ujenzi ulipokamilika, alikuja kwenye jumba hilo akiwa amebeba ramani ya nyumba yake akawasihi ndugu hao vijana wamjengee nyumba hiyo. Alivutiwa sana na ubora wa kazi yao hivi kwamba alijitolea kuwalipa pesa nyingi. Alishangaa akina ndugu walipomwambia kwamba walikuwa wakijenga Jumba la Ufalme kwa sababu wanampenda Mungu na jirani, bali si kwa sababu ya kuchuma pesa.

      TAFSIRI YA ULIMWENGU MPYA

      Wakati huohuo, kikundi kingine cha wanaume na wanawake waliojitolea walikuwa wakifanya kazi tofauti, kazi ya kutafsiri Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kimakedonia. Yehova alibariki kazi yao ngumu; na katika muda wa miaka mitano tu, walitafsiri Biblia nzima ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Wajumbe walifurahi kama nini katika Kusanyiko la Wilaya la 2006 la “Ukombozi Unakaribia!” huko Skopje wakati mshiriki wa Baraza Linaloongoza Gerrit Lösch alipotangaza kutolewa kwa tafsiri hiyo mpya ya Biblia iliyo bora. Walipiga makofi kwa msisimuko sana na kwa muda mrefu, na wengi wao walitiririkwa na machozi. Baadhi yao walipopokea Biblia hiyo wakati wa chakula cha mchana waliketi chini mara moja na kuanza kuisoma tafsiri hiyo ya pekee ya Neno la Mungu katika lugha yao.

      Wamakedonia wengi wanaiheshimu sana Biblia. Kwa mfano, Orhan alianza kujifunza Biblia miaka sita iliyopita. Hakujua kusoma wala kuandika, hata hivyo, alifundishwa kusoma na kuandika na ndugu aliyekuwa akijifunza naye. Tangu alipobatizwa miaka mitatu iliyopita, ameisoma Biblia yote mara sita!

      Kwa muda fulani, Orhan ndiye aliyekuwa Shahidi pekee katika mji wa Resen. Hata hivyo, wengi walimsifu mtu huyo ambaye mwanzoni hakujua kusoma wala kuandika, na wazazi fulani waliwaomba akina ndugu wajifunze na watoto wao ili wawe kama Orhan. Wengi walianza kupendezwa na kweli, na mwishowe Funzo la Kitabu la Kutaniko la kila juma likaanzishwa katika mji huo. Mtu mmoja aliyependezwa alifikia kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na sasa Orhan ni painia wa kawaida na mtumishi wa huduma.

      KUVUKA KUINGIA MAKEDONIA

      Katika mwezi wa Julai mwaka wa 2004, mume mmoja na mke wake ambao ni mapainia wa pekee kutoka Albania walikuja Makedonia ili kuwahubiria watu wanaozungumza Kialbania, ambao ni asilimia 25 ya watu wote nchini. Muda si muda, ilikuwa wazi kwamba wenzi hao wa ndoa walihitaji msaada kwa sababu walikuwa peke yao na walihitaji kuwahubiria watu zaidi ya nusu milioni wanaozungumza Kialbania. Kwa hiyo, mwaka mmoja baadaye wenzi wengine wa ndoa walitumwa kutoka Albania ili wajiunge nao, na mapainia hao wanne wa pekee walianza kuwatia moyo watu saba wenye kupendezwa wa kikundi kidogo katika mji wa Kičevo, ulio katikati ya eneo lenye Waalbania wengi nchini Makedonia. Katika maadhimisho yaliyofuata ya Ukumbusho, kikundi hicho kidogo kilifurahi sana kuona watu 61 wakihudhuria hotuba ya Ukumbusho, ambayo ilitolewa katika Kialbania na Kimakedonia. Kuanzia wakati huo, kikundi hicho kimekuwa na wahubiri 17 wenye bidii, na kwa wastani watu 30 au zaidi wanahudhuria mikutano.

      Ili eneo lote la Makedonia liweze kuhubiriwa, Baraza Linaloongoza lilikubali kampeni ya pekee ifanywe kuanzia Aprili mpaka Julai 2007. Kusudi lilikuwa kuhubiri eneo ambalo halikuwa limehubiriwa na kueneza habari njema kwa watu wanaozungumza Kialbania.

      Ndugu na dada 337 kutoka katika nchi saba walifurahi sana kujitolea kusaidia. Walipata matokeo gani? Habari njema ilihubiriwa katika maeneo zaidi ya 200 kotekote Makedonia. Watu 400,000 hivi walihubiriwa, na ilikuwa mara ya kwanza kwa wengi wao kusikia ujumbe huo. Watu waliachiwa vitabu na broshua zaidi ya 25,000 na magazeti zaidi ya 40,000 wakati wa kampeni hiyo ya miezi minne. Wahubiri walitumia saa 25,000 katika huduma, wakaanzisha mafunzo ya Biblia zaidi ya 200.

      “Watu fulani walitokwa na machozi tulipowaambia tulikotoka na sababu ya kuwatembelea,” akaripoti ndugu mmoja. “Wengine wao waliguswa moyo na mambo waliyosoma katika Neno la Mungu, wakatiririkwa na machozi.”

      Wahubiri walioshiriki katika kampeni hiyo walieleza sana jinsi walivyothamini kutoka moyoni kampeni hiyo. Dada mmoja aliandika hivi: “Mwalimu mmoja alituambia hivi: ‘Mungu awabariki. Mnafanya kazi nzuri kabisa. Mambo mnayozungumzia yameniburudisha kwelikweli!’”

      Mhubiri fulani alisema hivi: “Ni vigumu kuacha eneo hilo ambalo linafaa kabisa umishonari. Tuliona jinsi watu walivyohitaji sana kweli, na tulihuzunika kuwaaga wanafunzi wetu wa Biblia tulipokuwa tukiondoka.”

      Wenzi fulani wa ndoa walisema: “Tunasikitika kwamba hatukuchukua siku zaidi za likizo, kwa sababu sasa tunaona jinsi uhitaji ulivyo mkubwa.”

      Wengi walihisi kama mhubiri aliyesema hivi: “Sidhani kuna wakati wowote ambapo tulifurahi sana tukiwa familia kama wakati huo.”

      Kwenye milima iliyo karibu na mji wa Tetovo, kikundi cha wahubiri kilikuwa kikihubiri katika kijiji kimoja ambacho hakikuwa kimewahi kuhubiriwa na yeyote. Wahubiri wawili walianza kuhubiri upande wa kushoto wa barabara, na wawili upande wa kulia. Kabla hawajamaliza kuhubiri nyumba tatu tu, habari zilienea katika mtaa wote kwamba Mashahidi wa Yehova wanahubiri. Punde si punde, habari hizo zilienea katika kijiji chote, na kundi kubwa la wanawake wenye kupendezwa liliwazunguka akina dada. Mbele kidogo barabarani, kikundi cha wanaume 16 kilikuwa kikiwangojea kwa hamu akina ndugu. Wenye nyumba walileta mara moja viti vinne ili wahubiri waketi, na mwanamume mmoja akawatayarishia kahawa. Wahubiri walimpa kila mtu kitabu, wakaitumia kabisa Biblia kuufundisha umati huo kweli.

      Wengi waliuliza maswali, na wote walisikiliza kwa makini. Wahubiri walipomaliza mazungumzo yao, wanakijiji wengi waliwaaga kibinafsi. Hata hivyo, ndugu hao walishtuka wakati mama mmoja mzee alipowakaribia akiwa ameinua bakora yake juu. “Nitawatwanga kwa bakora hii!” akasema, huku akiwanyooshea bakora hiyo. Wahubiri hao walikuwa wamemtendea nini mama huyo? “Mlimpa kila mtu kitabu lakini mimi hamkunipa!” akasema mama huyo. “Ninataka kile kitabu kikubwa cha manjano,” akasema, huku akionyesha kitabu cha Hadithi za Biblia ambacho jirani yake alikuwa amepewa. Bila kukawia, ndugu hao walimpa kitabu cha mwisho walichokuwa nacho.

      KUWAHUBIRIA WAROMANI

      Huko Makedonia, kuna Waromani wengi wanaozungumza Kimakedonia lakini lugha yao ni lugha ya Kiromani iliyochanganywa na lugha nyingine kadhaa za Kiromani. Inasemekana kwamba mji mkuu, Skopje, ambao una eneo kubwa zaidi la Waromani huko Ulaya, una wakaaji 30,000 hivi. Jengo lenye Majumba mawili ya Ufalme katika eneo linaloitwa Šuto Orizari linatumiwa na makutaniko matatu ya Kiromani yaliyo huko. Wahubiri 200 walio huko wanafurahia eneo lao lenye matokeo mazuri, kila mhubiri anahitaji kuwahubiria watu 150, mojawapo ya idadi ndogo zaidi ya watu katika nchi hiyo. Watu 708 waliohudhuria Ukumbusho mwaka wa 2008 wanathibitisha kwamba wengi wanaitikia huko Romani!

      Ni jitihada gani zinazofanywa ili kuwasaidia Waromani ambao ni wanyenyekevu na wenye njaa ya kweli ili wajifunze kuhusu kusudi la Mungu katika lugha yao? Muhtasari wa hotuba ya pekee ya mwaka wa 2007 ulitafsiriwa katika Kiromani, na watu 506 walisikiliza kwa makini sana mzee Mromani alipokuwa akitoa hotuba hiyo. Wahubiri wa makabila mbalimbali, kama vile, Waromani, Wamakedonia, na Waalbania, walifurahi sana wakati broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? ilipotolewa katika Kiromani katika kusanyiko la wilaya la 2007. Kabla ya wakati huo, mara nyingi wahubiri waliongoza mafunzo ya Biblia katika lugha yao wenyewe wakitumia vichapo vya Kimakedonia. Sasa wanafanikiwa kabisa kugusa mioyo ya Waromani wanyoofu kwa kutumia broshua Anataka ya Kiromani.

      Leo wahubiri 1,277 walio katika makutaniko 21 huko Makedonia wanahubiri kwa bidii sana wakifuata mfano ambao mtume Paulo aliweka katika karne ya kwanza. Itikio zuri la Wamakedonia wengi wanaotafuta kweli linaonyesha umuhimu wa kampeni ya kisasa ya ‘kuvuka kuingia Makedonia.’

  • Nchi Ambazo Zilikuwa Sehemu ya Yugoslavia
    2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 224]

      “Nilienda Gerezani Siku 11 Mapema”

      PAVLINA BOGOEVSKA

      ALIZALIWA 1938

      ALIBATIZWA 1972

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alianza kufanya upainia mwaka wa 1975 naye akawa painia wa pekee wa kwanza huko Makedonia mwaka wa 1977. Amewasaidia watu 80 kujifunza kweli.

      MARA nyingi nilipokuwa nikihubiri, watu waliniripoti kwa polisi, ambao walinishika na kunipeleka kwenye kituo cha polisi ambako nilihojiwa, nyakati nyingine kwa saa nyingi. Nilitozwa faini mara nyingi. Katika mahakama, nilishtakiwa kimakosa kwamba nilikuwa adui wa kisiasa wa Serikali na kwamba nilikuwa nikieneza propaganda za Ulaya na Marekani. Pindi moja nilihukumiwa kifungo cha siku 20 gerezani, na pindi nyingine kifungo cha siku 30.

      Nilipaswa kuwa katika kifungo cha siku 20 wakati uleule ambapo kusanyiko la wilaya lingefanywa. Niliomba mahakama iahirishe hukumu yangu; lakini ombi langu lilikataliwa, kwa hiyo nikaamua kwenda gerezani siku 11 mapema. Maofisa wa gereza walishangaa kuniona. Hawakuamini kwamba mtu anaweza kuomba kufungwa gerezani haraka iwezekanavyo. Nilipata nafasi ya kutoa ushahidi, nao wakaniahidi kwamba wangejitahidi sana kunitunza. Siku 11 baadaye, ofisa wa polisi alikuja gerezani kuona ikiwa nilikuwa nimefika. Hebu wazia jinsi alivyoshangaa alipojulishwa na maofisa wa gereza kwamba tayari nilikuwa nimekaa gerezani kwa siku 11! Mwishowe, niliweza kuhudhuria kusanyiko.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki