-
Kitabu kwa Ajili ya Watu WoteMnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 1
-
-
Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
“Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.”—MATENDO 10:34, 35.
1. Profesa mmoja aliitikiaje alipoulizwa maoni yake juu ya Biblia, naye aliamua kufanya nini?
JUMAPILI alasiri, profesa alikuwa nyumbani, bila kutarajia wageni wowote. Lakini mmojawapo wa dada zetu Wakristo, alipomtembelea nyumbani kwake, alisikiliza. Alizungumza juu ya uchafuzi wa dunia na wakati ujao wake—habari zilizomvutia. Hata hivyo, alipoingiza Biblia katika hayo mazungumzo, alionekana kuwa mwenye kutilia shaka. Kwa hiyo dada huyo akamwuliza maoni yake juu ya Biblia.
“Ni kitabu kizuri kilichoandikwa na watu fulani wenye akili,” akajibu, “lakini Biblia haipasi kuchukuliwa kwa uzito.”
“Je, umepata kuisoma Biblia?” dada akauliza.
Kwa kushtuka, huyo profesa alilazimika kukiri kwamba hakuwa ameisoma.
Kisha dada akauliza: “Waweza kutoaje usadikisho wenye nguvu juu ya kitabu ambacho hujakisoma kamwe?”
Dada yetu alitoa hoja thabiti. Profesa aliamua kuisoma Biblia kisha atoe maoni juu yake.
2, 3. Kwa nini Biblia ni kitabu kilichofungika kwa watu wengi, na jambo hilo hututolea mwito gani wa ushindani?
2 Si profesa huyo tu aliye na maoni hayo. Watu wengi wana maoni dhahiri juu ya Biblia ingawa hawajaisoma kibinafsi. Huenda wakawa na Biblia. Huenda hata wakakubali thamani yake ya kifasihi au ya kihistoria. Lakini kwa walio wengi, ni kitabu kilichofungika. ‘Sina wakati wa kuisoma Biblia,’ baadhi yao husema. Wengine hujiuliza hivi, ‘Yawezekanaje kitabu fulani kilicho cha kale kihusu maisha yangu?’ Maoni kama hayo hututolea mwito halisi wa ushindani. Mashahidi wa Yehova waamini kwa uthabiti kwamba Biblia ‘imepuliziwa na Mungu na ni yenye manufaa kwa kufundisha.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Ingawa hivyo, twaweza kuwasadikishaje watu kwamba wapaswa kuichunguza Biblia haidhuru malezi yao ya kijamii, ya kitaifa, au ya kikabila?
3 Acheni tuzungumzie sababu kadhaa zinazofanya Biblia istahili kuchunguzwa. Mazungumzo hayo yaweza kututayarisha kusababu na wale tunaokutana nao katika huduma yetu, labda tukiwasadikisha kwamba wapaswa kuchunguza yale isemayo Biblia. Wakati uleule, uchunguzi huo wapaswa kuimarisha sana imani yetu wenyewe kwamba Biblia kwa kweli ni “neno la Mungu,” kama vile idaivyo.—Waebrania 4:12.
Kitabu Chenye Kutawanywa Zaidi Sana Ulimwenguni
4. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Biblia ndicho kitabu chenye kutawanywa zaidi sana?
4 Kwanza, Biblia yastahili kuchunguzwa kwa sababu kwa mbali ndicho kitabu chenye kutawanywa zaidi sana na ambacho kimetafsiriwa sana katika historia ya kibinadamu. Miaka zaidi ya 500 iliyopita, chapa ya kwanza iliyochapwa kwa kutumia uchapaji kwa mashine ilitokezwa na matbaa ya Johannes Gutenberg. Tangu wakati huo, Biblia zikiwa nzima au sehemu-sehemu zinazokadiriwa kuwa bilioni nne, zimechapwa. Kufikia mwaka wa 1996, Biblia nzima au visehemu-sehemu vimetafsiriwa katika lugha na lahaja 2,167.a Zaidi ya asilimia 90 ya familia ya kibinadamu wanaweza kupata angalau sehemu ya Biblia katika lugha yao wenyewe. Hakuna kitabu kingine—kiwe cha kidini au kiwe tofauti—kilinganacho na Biblia!
5. Kwa nini twapaswa kutarajia Biblia iweze kupatikana kwa watu ulimwenguni pote?
5 Takwimu pekee hazithibitishi kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Hata hivyo, bila shaka twapaswa kutarajia rekodi iliyoandikwa ambayo imepuliziwa na Mungu, iwe yaweza kupatikana na watu ulimwenguni pote. Hata hivyo, Biblia yenyewe hutuambia kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Tofauti na kitabu kingine chochote, Biblia imevuka mipaka ya kitaifa na imeshinda vizuizi vya kijamii na vya kikabila. Kwa kweli, Biblia ni kitabu kwa ajili ya watu wote!
Rekodi ya Pekee ya Uhifadhi
6, 7. Kwa nini si jambo la kushangaza kwamba hakuna maandishi ya Biblia ya awali yanayojulikana kuwako, na hilo lazusha swali gani?
6 Kuna sababu nyingine ifanyayo Biblia istahili kuchunguzwa. Imeokoka vizuizi vya kiasili na vya kibinadamu. Rekodi ya vile Biblia ilivyohifadhiwa vijapokuwako vizuizi vikubwa, kwa kweli ni ya pekee miongoni mwa maandishi ya kale.
7 Kwa wazi waandikaji wa Biblia walirekodi maneno yao kwa wino juu ya mafunjo (yaliyotengenezwa kutokana na mmea wa Misri wenye jina hilohilo) na juu ya hati ya ngozi (iliyotengenezwa kutokana na ngozi za wanyama).b (Ayubu 8:11) Hata hivyo, vifaa hivyo vya kuandikia vina maadui wa asili. Msomi Oscar Paret, aeleza hivi: “Vifaa hivi viwili vya kuandikia vinahatarishwa kwa njia iliyo sawa na unyevuanga, kuvu, na funza. Twajua kutokana na mambo yatupatayo kila siku jinsi karatasi na hata ngozi nzito, ziharibikavyo kwa urahisi zikiwa nje au katika chumba chenye unyevunyevu.” Kwa hiyo haishangazi kwamba hakuna maandishi ya awali yanayojulikana kuwako; labda yaliharibiwa muda mrefu uliopita. Lakini ikiwa maandishi ya awali hayako tena, basi maandishi ya Biblia yaliokokaje hadi siku yetu?
8. Maandishi ya Biblia yalihifadhiwaje kwa karne kadhaa zilipopita?
8 Upesi baada ya maandishi ya awali kuandikwa, nakala zilizoandikwa kwa mkono zilianza kutokezwa. Kwa kweli kunakili Sheria na sehemu nyinginezo za Maandiko Matakatifu kulipata kuwa kazi ya kuajiriwa katika Israeli la kale. Kwa kielelezo, kuhani Ezra afafanuliwa kuwa “mwandishi mwenye ujuzi mwingi sana katika sheria ya [Musa].” (Ezra 7:6, Biblia Habari Njema; linganisha Zaburi 45:1.) Lakini nakala zilizotokezwa zilikuwa ziwezazo kuharibika pia; hatimaye nakala nyingine zilizoandikwa kwa mkono bado zilihitaji kuchukua mahali pa hizo. Utaratibu huo wa kunakili hizo nakala uliendelea kwa karne kadhaa. Kwa kuwa wanadamu si wakamilifu, je, makosa ya wanakili yalibadili sana maandishi ya Biblia? Uthibitisho ulio mkubwa zaidi wajibu la!
9. Kielelezo cha Wamasora chatoleaje kielezi uangalifu mkubwa na usahihi wa wanakili wa Biblia?
9 Wanakili hao walikuwa stadi sana na pia waliyastahi sana maneno waliyonakili. Neno la Kiebrania lifasiriwalo “mnakili” larejezea kuhesabu na kurekodi. Ili kutolea kielezi uangalifu mkubwa na usahihi wa wanakili, fikiria Wamasora, wanakili wa Maandiko ya Kiebrania walioishi kati ya karne ya sita na ya kumi W.K. Kulingana na msomi Thomas Hartwell Horne, walihesabu “ni mara ngapi kila herufi ya alfabeti ya [Kiebrania] ilitokea katika Maandiko ya Kiebrania.” Fikiria linalomaanishwa na hilo! Ili kuepuka kuacha hata herufi moja, wanakili hao wenye kujitoa walihesabu si maneno tu waliyonakili bali herufi vilevile. Kwani, kulingana na hesabu ya huyo msomi, yaripotiwa kwamba walihesabu herufi mojamoja 815,140 katika Maandiko ya Kiebrania! Jitihada hizo nyingi zilihakikisha usahihi wa kadiri ya juu.
10. Kuna uthibitisho gani wenye nguvu kwamba maandishi ya Kiebrania na ya Kigiriki ambayo tafsiri za kisasa zategemea yawakilisha kwa usahihi maneno ya waandikaji wa kwanza?
10 Kwa kweli, kuna uthibitisho wenye nguvu kwamba maandishi ya Kiebrania na ya Kigiriki ambayo juu yake tafsiri za kisasa zategemea, huwakilisha kwa uaminifu wenye kutokeza maneno ya waandikaji wa awali. Huo uthibitisho wafanyizwa na maelfu ya nakala-hati za Biblia zilizoandikwa kwa mkono—nakala zikadiriwazo kuwa 6,000 za Maandiko ya Kiebrania yote au sehemu zake na nakala za Maandiko ya Kikristo katika Kigiriki zipatazo 5,000—ambazo zimeokoka hadi siku yetu. Mchanganuo wenye uangalifu na wa kulinganisha nyingi za hati zilizoko umewawezesha wasomi wa maandishi kugundua makosa yoyote ya wanakili na kugundua tafsiri ya awali. Akieleza juu ya maandishi ya Maandiko ya Kiebrania, msomi William H. Green angeweza kusema hivi: “Yaweza kusemwa kwa usalama kwamba hakuna kazi yoyote nyingine ya kale ambayo imepitishwa kwa usahihi hivyo.” Twaweza kuwa na uhakika huohuo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
11. Kwa kufikiria 1 Petro 1:24, 25, kwa nini Biblia imeokoka hadi siku yetu?
11 Biblia ingaliweza kuangamia kwa urahisi kama nini kama isingalikuwa kwa sababu ya nakala zilizoandikwa kwa mkono ambazo zilichukua mahali pa zile za awali, zikiwa na ujumbe wake wenye thamani! Kuna sababu moja tu ya kuokoka kwake—Yehova ndiye Mhifadhi na Mlinzi wa Neno lake. Kama vile Biblia yenyewe isemavyo, kwenye 1 Petro 1:24, 25: “Mwili wote wenye nyama ni kama nyasi, na utukufu wao wote ni kama chanuo la nyasi; nyasi huwa yenye kunyauka, na ua huanguka, bali usemi wa Yehova hudumu milele.”
Katika Lugha Hai za Wanadamu
12. Kwa kuongezea karne nyingi za kunakiliwa upya, ni vizuizi gani vingine ambavyo Biblia ilikabili?
12 Kuokoka karne za kunakiliwa upya kulikuwa jambo gumu vya kutosha, lakini Biblia imekabili kizuizi kingine—kutafsiriwa katika lugha za wakati wetu. Lazima Biblia iseme lugha za watu ili iseme na mioyo yao. Hata hivyo, kutafsiri Biblia—yenye sura zaidi ya 1,100 na mistari zaidi ya 31,000—si kazi rahisi. Hata hivyo, katika karne zilizopita watafsiri wenye kujitoa walikabili ugumu huo kwa mteremo, wakikabili vizuizi ambavyo nyakati fulani vilionekana kana kwamba haviwezi kushindwa.
13, 14. (a) Mtafsiri wa Biblia, Robert Moffat, alikabili mwito gani wa ushindani katika Afrika mapema karne ya 19? (b) Watu wenye kuzungumza Kitswana waliitikiaje Gospeli ya Luka ilipotolewa katika lugha yao?
13 Kwa kielelezo, fikiria jinsi ambavyo Biblia ilipata kutafsiriwa katika lugha za Afrika. Mwaka wa 1800, kulikuwa na lugha karibu 12 tu zilizoandikwa katika Afrika nzima. Mamia ya lugha nyingine zilizosemwa hazikuwa na mfumo wa kuandika. Hilo ndilo tatizo lililomkabili mtafsiri wa Biblia Robert Moffat. Mwaka wa 1821, akiwa na umri wa miaka 25, Moffat alianzisha misheni miongoni mwa watu kusini mwa Afrika wenye kusema Kitswana. Ili ajifunze lugha yao isiyoandikwa, alichangamana na hao watu. Moffat alidumu na, bila msaada wa vijitabu vya masomo ya kwanza au kamusi, hatimaye akaijua kabisa hiyo lugha, akasitawisha namna ya kuiandika na kuwafundisha Watswana fulani kuisoma hati hiyo. Mwaka wa 1829, baada ya kufanya kazi miongoni mwa Watswana kwa miaka minane, alimaliza kutafsiri Gospeli ya Luka. Baadaye alisema hivi: “Nimejua juu ya watu ambao wamekuja mamia ya kilometa ili kujipatia nakala za [Gospeli ya] Mtakatifu Luka. . . . Nimewaona wakipokea sehemu za [Gospeli ya] Mtakatifu Luka, na kutoa machozi juu yazo, na kuzishika kifuani, na kububujika machozi ya shukrani, mpaka nikasema kwa zaidi ya mmoja, ‘Utaviharibu vitabu vyako kwa machozi yako.’” Moffat pia alisema juu ya mwanamume mmoja Mwafrika aliyeona watu kadhaa wakiisoma Gospeli ya Luka na kuwauliza walichokuwa wamepata. “Ni neno la Mungu,” wakajibu. “Je, hilo husema?” huyo mwanamume akauliza. “Ndiyo,” wakasema, “hilo husema na moyo.”
14 Watafsiri wenye kujitoa kama Moffat waliwapa Waafrika wengi fursa yao ya kwanza ya kuwasiliana katika maandishi. Lakini watafsiri waliwapa Waafrika zawadi yenye thamani hata zaidi—Biblia katika lugha yao wenyewe. Isitoshe, Moffat alitokeza lile jina la Mungu kwa Watswana, naye alilitumia jina hilo kotekote katika tafsiri yake.c Hivyo, Watswana waliirejezea Biblia kuwa “kinywa cha Yehova.”—Zaburi 83:18.
15. Kwa nini Biblia iko hai sana leo?
15 Watafsiri wengine katika sehemu mbalimbali za ulimwengu walikabili vizuizi vivyo hivyo. Baadhi yao hata walihatarisha uhai wao ili kuitafsiri Biblia. Fikiria hili: Ikiwa Biblia ingalibaki tu katika Kiebrania na Kigiriki, ingalikuwa “imekufa” zamani za kale, kwa kuwa baada ya muda lugha hizo zilisahauliwa kabisa na umma na hazikujulikana kamwe katika sehemu nyingi za dunia. Lakini, Biblia iko hai sana, tofauti na kitabu kingine chochote, yaweza “kusema” na watu ulimwenguni pote katika lugha yao wenyewe. Tokeo ni kwamba, ujumbe wake wabaki ‘ukifanya kazi katika waamini wake.’ (1 Wathesalonike 2:13) Tafsiri ya The Jerusalem Bible hufasili hayo maneno hivi: “Bado ni nguvu hai miongoni mwenu ambao mwaiamini.”
Yastahili Kutumainiwa
16, 17. (a) Ili Biblia iwe yenye kutumainika, ni uthibitisho gani ambao ni lazima uwepo? (b) Toa kielelezo kimoja kinachotolea kielezi uwazi wa mwandikaji wa Biblia Musa.
16 ‘Je, kwa kweli Biblia yaweza kutumainiwa?’ watu fulani huenda wakauliza. ‘Je, hiyo yarejezea watu ambao pasipo shaka waliishi, mahali halisi palipokuwako, na matukio yaliyotukia kikweli?’ Ikiwa ni lazima tuitumaini, lazima pawe na uthibitisho kwamba iliandikwa na waandikaji waliokuwa waangalifu na wenye kufuatia haki. Hilo latuleta kwenye sababu nyingine ya kuichunguza Biblia: Kuna uthibitisho thabiti wa kwamba ni sahihi na yenye kutumainika.
17 Waandikaji wenye kufuatia haki wangerekodi si mafanikio tu bali pia kushindwa, si sifa nzuri tu bali pia udhaifu mbalimbali. Waandikaji wa Biblia walionyesha uwazi wenye kuburudisha sana. Kwa kielelezo, fikiria ule uwazi wa Musa. Miongoni mwa mambo aliyoripoti wazi ni ukosefu wake mwenyewe wa ufasaha, ambao kwa maoni yake ulimfanya asistahili kuwa kiongozi wa Israeli (Kutoka 4:10); kosa zito alilofanya ambalo lilizuia kuingia kwake katika Bara Lililoahidiwa (Hesabu 20:9-12; 27:12-14); kukengeuka kwa ndugu yake, Aroni, aliyeshirikiana na Waisraeli wenye kuasi katika kutengeneza sanamuumbo ya ndama wa dhahabu (Kutoka 32:1-6); ule uasi wa dada yake, Miriamu, na adhabu yenye kudhilisha (Hesabu 12:1-3, 10); ule uchafuaji wa kitu kilicho kitakatifu wa wapwa wake wa kiume, Nadabu na Abihu (Mambo ya Walawi 10:1, 2); na kule kulalamika na kunung’unika kwa kurudia-rudia kwa watu wa Mungu mwenyewe. (Kutoka 14:11, 12; Hesabu 14:1-10) Je, kuripoti huko kwa wazi na kwa unyoofu hakuonyeshi kuhangaikia kweli kwa moyo mweupe? Kwa kuwa waandikaji wa Biblia walikuwa tayari kuripoti habari mbaya juu ya wale waliowapenda, watu wao, na hata juu yao wenyewe, je, hakuna sababu nzuri ya kutumaini maandishi yao?
18. Ni nini huthibitisha maandishi ya waandikaji wa Biblia kuwa yenye kutumainika?
18 Kupatana pia kwa waandikaji wa Biblia huthibitisha maandishi yao kuwa yenye kutumainika. Ni jambo lenye kutokeza kwamba wanaume 40 wakiandika kwa kipindi kipatacho miaka 1,600 wanaafikiana, hata juu ya mambo madogo-madogo. Hata hivyo, kupatana huko hakukupangwa kwa uangalifu sana hivi kwamba kwaweza kuamsha mashaka ya kuwako na njama. Kinyume cha hilo, ni wazi kwamba maafikiano ya mambo mbalimbali yaliyo madogo-madogo hayakukusudiwa; kwa wazi, mara nyingi huo upatano hutokea kwa sadfa.
19. Masimulizi ya Gospeli juu ya kukamatwa kwa Yesu huonyeshaje mwafikiano ambao kwa wazi haukukusudiwa?
19 Kwa kutoa kielezi, fikiria tukio fulani lililotokea usiku wa kukamatwa kwa Yesu. Waandikaji wote wanne wa Gospeli wamerekodi kwamba mmojawapo wa wanafunzi alifuta upanga na kumpiga mtumwa wa kuhani wa cheo cha juu, akiondoa sikio la huyo mwanamume. Hata hivyo, ni Luka pekee atuambiaye kwamba Yesu ‘aligusa sikio na kumponya.’ (Luka 22:51) Lakini je, tusitarajie jambo kama hilo kutoka kwa mwandikaji aliyejulikana kuwa “tabibu mpendwa”? (Wakolosai 4:14) Simulizi la Yohana latuambia kwamba kati ya wanafunzi wote waliokuwapo, yule aliyetumia upanga alikuwa Petro—jambo la hakika ambalo halishangazi kwa sababu ya mwelekeo wa Petro wa kutokuwa na subira na wa kutenda kulingana na msukumo. (Yohana 18:10; linganisha Mathayo 16:22, 23 na Yohana 21:7, 8.) Yohana aripoti jambo jingine dogo lionekanalo kuwa lisilo la lazima: “Jina la mtumwa huyo lilikuwa ni Malko.” Kwa nini Yohana peke yake ndiye atoaye jina la huyo mtu? Ufafanuzi umeandaliwa na jambo dogo la hakika ambalo limetajwa mara moja tu katika simulizi la Yohana—Yohana “alijulikana na kuhani wa cheo cha juu.” Alijulikana pia na watu wa nyumbani mwa kuhani wa cheo cha juu; yeye na hao watumishi walifahamiana.d (Yohana 18:10, 15, 16) Basi, ni jambo la asili kwamba Yohana ataja jina la huyo mwanamume aliyejeruhiwa, ilhali waandikaji wengine wa Gospeli, ambao kwao huyo mwanamume alikuwa mtu asiyejulikana, hawamtaji. Mwafaka kati ya mambo hayo madogo-madogo yote ni wenye kutokeza, lakini kwa wazi haukukusudiwa. Kuna vielelezo vingine vingi vya aina hiyo kotekote katika Biblia.
20. Watu wenye mioyo yenye kufuatia haki wahitaji kujua nini juu ya Biblia?
20 Hivyo, je, twaweza kuitumaini Biblia? Bila shaka! Uwazi wa waandikaji wa Biblia na kupatana kwa Biblia kwa ndani kwaifanya kuwa ya kweli. Watu wenye mioyo yenye kufuatia haki wanahitaji kujua kwamba wanaweza kuitumaini Biblia, kwa kuwa hiyo ni neno lililopuliziwa la “BWANA, Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Kuna sababu za ziada zifanyazo Biblia kuwa kitabu kwa ajili ya watu wote, kama zitakavyozungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Kitabu Kutoka kwa MunguMnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 1
-
-
Kitabu Kutoka kwa Mungu
“Unabii haukuletwa wakati wowote kamwe kwa mapenzi ya binadamu, bali wanadamu walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.”—2 PETRO 1:21.
1, 2. (a) Kwa nini watu fulani hushuku kama Biblia yahusu maisha ya kisasa? (b) Twaweza kutumia ithibati gani tatu ili kuonyesha kwamba Biblia ilitoka kwa Mungu?
JE, BIBLIA yawahusu watu wanaoishi kwenye ukingo wa karne ya 21? Watu fulani hufikiri haiwahusu. “Hakuna mtu awezaye kutetea matumizi ya chapa ya mwaka wa 1924 ya [kitabu] cha mafundisho ya kemia, katika darasa la kisasa la kemia—mengi mno yamejulikana juu ya kemia tangu wakati huo,” akaandika Dakt. Eli S. Chesen, akieleza ni kwa nini alihisi kwamba Biblia imepitwa na wakati. Kijuujuu, hoja hiyo yaonekana yenye maana. Hata hivyo, tangu nyakati za Biblia mwanadamu amejua mengi juu ya sayansi, afya ya kiakili, na tabia ya kibinadamu. Kwa hiyo, watu fulani huuliza hivi: ‘Kitabu hicho cha kale kingewezaje kuwa bila makosa ya kisayansi? Je, kingeweza kuwa na shauri liwezalo kutumika katika maisha ya kisasa?’
2 Biblia yenyewe yatoa jibu. Kwenye 2 Petro 1:21, twaambiwa kwamba manabii wa Biblia “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” Hivyo Biblia yaonyesha kwamba imetoka kwa Mungu. Ingawa hivyo, twaweza kusadikishaje wengine kwamba ndivyo ilivyo? Acheni tufikirie ithibati tatu zinazoonyesha kwamba Biblia ni Neno la Mungu: (1) Ni sahihi kisayansi, (2) ina kanuni zenye kudumu ambazo ni zenye kutumika katika maisha ya kisasa, na (3) ina unabii mahususi ambao umetimizwa, kama ithibitishwavyo na mambo ya hakika ya kihistoria.
Kitabu Ambacho Chakubaliana na Sayansi
3. Kwa nini mavumbuzi ya kisayansi hayaitishi Biblia?
3 Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi. Hata hivyo, ni kitabu juu ya kweli, na kweli yaweza kustahimili kwa muda wote. (Yohana 17:17) Hakuna mavumbuzi ya kisayansi ambayo yameitisha Biblia. Itajapo mambo yahusianayo na sayansi, Biblia haina dhana zozote za kale za “kisayansi” zilizothibitika kuwa ngano tu. Kwa hakika, Biblia ina taarifa zipinganazo kabisa na maoni yaliyokubaliwa ya siku yake, ambazo pia ni sahihi kisayansi. Kwa kielelezo, fikiria mwafaka uliopo kati ya Biblia na sayansi ya kitiba.
4, 5. (a) Matabibu wa kale walikosa kuelewa nini juu ya maradhi? (b) Kwa nini hakuna shaka kwamba Musa alijua sana mazoea ya kitiba ya matabibu Wamisri?
4 Matabibu wa kale hawakuelewa kabisa jinsi maradhi yaeneavyo, wala hawakung’amua umaana wa usafi wa kutunza afya katika kuzuia ugonjwa. Mazoea mengi ya kale ya kitiba yangeonekana ya kishenzi kwa kulinganishwa na viwango vya kisasa. Mojawapo ya maandishi ya kitiba ya zamani zaidi yawezayo kupatikana ni yale yaitwayo Funjo la Ebers, ambayo ni mkusanyo wa ujuzi wa kitiba wa Wamisri, wa tangu mwaka wa 1550 K.W.K. Yana tiba 700 za maumivu mbalimbali, “kuanzia yale ya kuumwa na mamba hadi maumivu ya kidole.” Tiba nyingi zilikuwa bila matokeo yoyote, lakini baadhi yazo zilikuwa hatari sana. Ili kutibu jeraha, maagizo yaliyopendekezwa yalikuwa kulipaka mchanganyiko wa kinyesi cha binadamu na vitu vingine.
5 Maandishi hayo ya tiba za Wamisri yaliandikwa yapata wakati uleule vitabu vya kwanza vya Biblia vilipoandikwa, ambavyo vyatia ndani Sheria ya Kimusa. Musa, aliyezaliwa mwaka wa 1593 K.W.K., alikulia Misri. (Kutoka 2:1-10) Akiwa amelelewa nyumbani mwa Farao, Musa “[ali]funzwa katika hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:22) Alijuana sana na “madaktari” wa Misri. (Mwanzo 50:1-3, NW) Je, maandishi yake yaliathiriwa na mazoea yao ya kitiba yaliyokuwa bila matokeo au yenye hatari?
6. Sayansi ya kisasa ya kitiba huiona kanuni gani ya usafi wa kutunza afya katika Sheria ya Kimusa kuwa ya akili?
6 Kinyume cha hilo, Sheria ya Kimusa ilitia ndani kanuni za usafi wa kutunza afya ambazo zingeonwa na sayansi ya kitiba ya kisasa kuwa za akili. Kwa kielelezo, sheria kuhusu kambi za kijeshi ilihitaji kwamba kinyesi kifunikwe kwa ardhi nje ya kambi. (Kumbukumbu la Torati 23:13) Hiyo ilikuwa hatua ya kujikinga ya hali ya juu sana. Ilisaidia kutunza vyanzo vya maji vikiwa bila uchafu na iliandaa kinga dhidi ya ugonjwa wa kuhara damu uletwao na nzi na magonjwa mengine ya kuhara ambayo huua mamilioni ya watu kila mwaka, hasa katika nchi zinazositawi.
7. Katika Sheria ya Kimusa, ni kanuni gani ya usafi wa kutunza afya iliyosaidia kuzuia kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza?
7 Sheria ya Kimusa ilikuwa na kanuni nyingine za usafi wa kutunza afya ambazo zilisaidia kuzuia kuenea kwa maradhi yenye kuambukiza. Mtu aliyekuwa na maradhi ya kuambukiza au aliyeshukiwa kuwa nayo, alitengwa na wengine. (Mambo ya Walawi 13:1-5) Mavazi na vyombo vilivyogusa mnyama aliyekufa mwenyewe (labda kutokana na maradhi) zilipasa ama kuoshwa kabla ya kutumiwa tena ama kuharibiwa. (Mambo ya Walawi 11:27, 28, 32, 33) Mtu yeyote aliyegusa maiti alionwa kuwa asiye safi na alilazimika kufuata utaratibu wa kutakaswa uliotia ndani kuosha mavazi na kuoga. Wakati wa kile kipindi cha siku saba cha ukosefu wa usafi, alilazimika kuepuka kugusana kimwili na wengine.—Hesabu 19:1-13.
8, 9. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba ule mfumo wa sheria ya usafi wa kutunza afya katika Sheria ya Kimusa, ulikuwa wa hali ya juu?
8 Mfumo huo wa sheria wa usafi wa kutunza afya hufunua hekima ya hali ya juu. Sayansi ya kitiba ya kisasa imejua mengi juu ya kuenea na kuzuia maradhi. Kwa kielelezo, hatua za kitiba katika karne ya 19 ziliongoza kwenye kuanzishwa kwa uzuiaji wa kukua kwa bakteria, yaani, usafi ili kupunguza maambukizo. Tokeo lilikuwa kupungua kwa kiwango kikubwa kwa maambukizo na vifo vya kabla ya wakati. Mwaka wa 1900, matarajio ya muda wa kuishi tangu kuzaliwa yalikuwa chini ya miaka 50 katika nchi nyingi za Ulaya na Marekani. Tangu wakati huo, yameongezeka kwa kutazamisha kwa sababu ya maendeleo ya kitiba katika kudhibiti maradhi, na pia kwa sababu ya hali bora za usafi wa kutunza afya na za kuishi.
9 Hata hivyo, maelfu ya miaka kabla sayansi ya kitiba haijajua jinsi maradhi yaeneavyo, Biblia iliagiza juu ya hatua za akili za uzuiaji zikiwa kinga dhidi ya maradhi. Haishangazi kwamba, Musa angeweza kusema juu ya Waisraeli wa siku yake ambao kwa ujumla waliishi kufikia umri wa miaka 70 au 80. (Zaburi 90:10) Musa angeweza kujuaje juu ya kanuni hizo za usafi wa kutunza afya? Biblia yenyewe yaeleza hivi: Mfumo wa Sheria “[u]lipitishwa kupitia kwao malaika.” (Wagalatia 3:19) Ndiyo, Biblia si kitabu cha hekima ya kibinadamu; ni kitabu kutoka kwa Mungu.
Kitabu Chenye Kutumika kwa Maisha ya Kisasa
10. Ingawa Biblia ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita, ni jambo gani lililo kweli kuhusu shauri lake?
10 Vitabu vyenye kutoa maagizo huelekea kupitwa na wakati navyo punde si punde hurekebishwa au vingine hutengenezwa badala yake. Lakini Biblia ni ya pekee kwa kweli. “Shuhuda zako ni amini sana,” yasema Zaburi 93:5. Ingawa Biblia ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita, maneno yake bado yaweza kutumika. Na hutumika kukiwa na matokeo sawa hata rangi yetu ya ngozi iwe gani au tuwe twaishi nchi gani. Fikiria vielelezo kadhaa vya shauri la Biblia lenye kudumu na “lenye kutumainika sana.”
11. Miongo kadhaa iliyopita, wazazi wengi waliongozwa kuamini nini juu ya kuwatia nidhamu watoto?
11 Miongo kadhaa iliyopita wazazi wengi—wakichochewa na “uvumbuzi wa mawazo mapya” juu ya kulea watoto—walifikiri kwamba “mtu hapaswi kuwatia watoto nidhamu.” Walihofu kwamba kuwawekea watoto vizuizi, kungesababisha vurugu na kukata tamaa. Washauri wenye makusudi mazuri walikuwa wakisisitiza kwamba wazazi wapaswa kuwatolea watoto wao sahihisho lisilo kali sana. Wengi wa wataalamu hao sasa “wanawahimiza wazazi wawe wakali zaidi, ili kuwatia nidhamu watoto wao,” laripoti gazeti The New York Times.
12. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “nidhamu” lamaanisha nini, na ni kwa nini watoto wahitaji nidhamu hiyo?
12 Hata hivyo, sikuzote Biblia imetoa shauri mahususi na lenye usawaziko juu ya kuzoeza mtoto. Hiyo yatoa shauri hili: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Nomino ya Kigiriki ambayo imetafsiriwa “nidhamu” humaanisha “kulea, kuzoeza, kufundisha.” Biblia husema kwamba nidhamu, au fundisho, ni uthibitisho wa upendo wa mzazi. (Mithali 13:24) Watoto husitawi chini ya miongozo dhahiri ambayo huwasaidia kusitawisha utambuzi wa mema na mabaya. Nidhamu ambayo imetolewa ifaavyo huwasaidia kuhisi salama; huwaambia kwamba wazazi wao huwajali na hujali juu ya aina ya mtu ambaye wanakuwa.—Linganisha Mithali 4:10-13.
13. (a) Biblia huwatolea wazazi hadhari gani kuhusu nidhamu? (b) Biblia hupendekeza nidhamu ya aina gani?
13 Lakini Biblia yatolea wazazi hadhari juu ya nidhamu. Mamlaka ya mzazi haipaswi kutumiwa vibaya. (Mithali 22:15) Mtoto yeyote hapaswi kamwe kutiwa adhabu kikatili. Jeuri ya kimwili hairuhusiwi katika familia ambayo huishi kupatana na Biblia. (Zaburi 11:5) Wala jeuri ya kihisia-moyo—maneno makali, uchambuzi wa daima, na kejeli yenye kuumiza, zote ambazo zaweza kuponda roho ya mtoto. (Linganisha Mithali 12:18.) Kwa hekima, Biblia yaonya hivi: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo [au, “mtawavunja moyo kabisa,” Phillips].” (Wakolosai 3:21) Biblia hupendekeza hatua za kinga. Kwenye Kumbukumbu la Torati 11:19, wazazi wahimizwa watumie kwa manufaa wasaa wa mapumziko ili kukaza katika watoto wao kanuni za kiadili na za kiroho. Shauri hilo lililo wazi na la akili juu ya kulea mtoto, ni lenye kutumika leo kama lilivyotumika nyakati za Biblia.
14, 15. (a) Biblia huandaa mengi zaidi ya shauri lenye hekima katika njia gani? (b) Ni mafundisho gani ya Biblia yawezayo kuwasaidia wanaume na wanawake wa jamii na mataifa tofauti waone mmoja na mwenzake kuwa sawa?
14 Biblia huandaa mengi zaidi ya shauri lenye hekima tu. Ujumbe wake huvutia moyo. Waebrania 4:12 lasema hivi: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na uloto wavyo, na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Fikiria kielelezo kimoja cha nguvu ya Biblia yenye kuchochea.
15 Watu leo wamegawanywa na vizuizi vya kijamii, kitaifa, na kikabila. Vizuizi hivyo bandia vimechangia kuchinjwa kijumla kwa wanadamu wasio na hatia katika vita ulimwenguni pote. Kwa upande mwingine, Biblia ina mafundisho ambayo husaidia wanaume na wanawake wa jamii na mataifa tofauti waonane kuwa sawa. Kwa mfano, Matendo 17:26 lasema kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” Hilo laonyesha kwamba kwa kweli kuna jamii moja tu—ile ya kibinadamu! Biblia yaendelea kututia moyo “[tuwe] waigaji wa Mungu,” ambaye juu yake yasema hivi: “[Yeye] si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Waefeso 5:1; Matendo 10:34, 35) Ujuzi huo ni wenye matokeo kwa wale watafutao kwa kweli kuishi kupatana na mafundisho ya Biblia. Huo hugusa hisi ya ndani kabisa—moyo—ukiharibu vizuizi vyenye kutengenezwa na watu ambavyo hugawanya watu. Je, ujuzi huo kwa kweli hufanya kazi katika ulimwengu wa leo?
16. Simulia ono moja linaloonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ni udugu wa kimataifa.
16 Bila shaka hufanya hivyo! Mashahidi wa Yehova wajulikana vizuri kwa sababu ya udugu wao wa kimataifa, ambao huunganisha watu wa malezi tofauti ambao kwa kawaida hawangekuwa na amani wao kwa wao. Kwa kielelezo, wakati wa mapigano ya kikabila huko Rwanda, Mashahidi wa Yehova wa kila kabila waliwalinda ndugu na dada zao Wakristo wa kabila lile jingine, wakihatarisha maisha zao wenyewe katika kufanya hivyo. Katika kisa kimoja, Shahidi Mhutu aliificha nyumbani mwake familia ya Watutsi sita wa kutaniko lake. Kwa kusikitisha, hiyo familia ya Watutsi iligunduliwa mwishowe na kuuawa. Huyo ndugu Mhutu na familia yake sasa walikabili hasira ya kisasi ya hao wauaji, wakalazimika kukimbilia Tanzania. Vielelezo sawa na hivyo viliripotiwa. Mashahidi wa Yehova hukiri kwa utayari kwamba muungano huo huwezekana kwa sababu mioyo yao imeguswa sana na nguvu yenye kuchochea ya ujumbe wa Biblia. Uhakika wa kwamba Biblia yaweza kuunganisha watu katika ulimwengu huu uliojaa chuki ni uthibitisho wenye nguvu kwamba imetoka kwa Mungu.
Kitabu cha Unabii wa Kweli
17. Unabii mbalimbali wa Biblia uko tofauti jinsi gani na matabiri bandia yafanywayo na watu?
17 “Hakuna unabii wa Andiko uchipukao kutokana na fasiri yoyote ya faragha,” lasema andiko la 2 Petro 1:20. Manabii wa Biblia hawakuchanganua mielekeo ya mambo yaliyokuwako ulimwenguni, kisha wakafanya matabiri yaliyotegemea ufasiri wao wa kibinafsi juu ya mambo hayo. Wala hawakutamka matabiri ambayo yangeweza kupotoshwa yafae tukio lolote tu la wakati ujao. Kwa kielelezo, acheni tuchunguze unabii wa Biblia ambao kwa kutokeza ulikuwa mahususi na ambao ulitabiri kinyume kabisa cha yale ambayo watu walioishi wakati huo, huenda wakawa walitarajia.
18. Kwa nini bila shaka wakaaji wa Babiloni walihisi kuwa salama sana, hata hivyo Isaya alikuwa ametabiri nini juu ya Babiloni?
18 Kufikia karne ya saba K.W.K., Babiloni lilionekana kuwa jiji kuu la Milki ya Babiloni lisiloweza kushindwa. Hilo jiji lilitagaa juu ya Mto Eufrati, na maji yake yalitumiwa kufanyiza handaki la maji lililokuwa pana na lenye kina, na mfumo wa mifereji. Hilo jiji pia lilikuwa limelindwa na mfumo wa kuta maradufu, zilizotegemezwa kwa minara ya ulinzi. Bila shaka wakaaji wa Babiloni walihisi wakiwa salama sana. Hata hivyo, katika karne ya nane K.W.K., hata kabla ya Babiloni kuinuka kufikia upeo wa utukufu wake, nabii Isaya alitabiri hivi: ‘Babiloni litakuwa kama Sodoma na Gomora hapo Mungu alipoiangamiza. Halitakaliwa na watu tena kabisa, wala watu hawatakaa ndani yake tangu kizazi hadi kizazi. Mwarabu hatapiga hema yake huko, wala wachungaji hawatalaza makundi yao huko.’ (Isaya 13:19, 20) Ona kwamba huo unabii ulitabiri kwamba Babiloni lingeharibiwa na pia lingekuwa bila wakaaji milele. Ni utabiri wenye ujasiri kama nini kuutoa! Je, yawezekana kuwa Isaya aliandika unabii wake baada ya kuona Babiloni lililokuwa ukiwa? Historia yajibu la!
19. Kwa nini unabii wa Isaya haukutimizwa kabisa Oktoba 5, 539 K.W.K.?
19 Usiku wa Oktoba 5, 539 K.W.K., Babiloni lilishindwa na majeshi ya Umedi na Uajemi chini ya Koreshi Mkubwa. Hata hivyo, unabii wa Isaya haukutimizwa kabisa wakati huo. Kufuatia kutwaliwa na Koreshi, Babiloni lenye wakaaji—lijapokuwa hafifu—liliendelea kwa karne nyingi. Katika karne ya pili K.W.K., yapata wakati ule Hati-Kunjo ya Baharifu ya Isaya iliponakiliwa, Waparthi walikuwa na mamlaka juu ya Babiloni, lililoonekana wakati huo kuwa jiji lisilo na kifani ambalo mataifa yaliyolizunguka yalilipigania. Mwanahistoria Myahudi, Josephus, aripoti kwamba “idadi kubwa” ya Wayahudi walikuwa wakiishi huko katika karne ya kwanza K.W.K. Kulingana na kitabu The Cambridge Ancient History, wafanya-biashara kutoka kisiwa cha Palmyra walianzisha koloni huko Babiloni mwaka wa 24 W.K. Kwa hiyo, mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., Babiloni lilikuwa bado halijawa ukiwa kabisa; hata hivyo kitabu cha Isaya kilikuwa kimekamilika muda mrefu kabla ya wakati huo.—1 Petro 5:13.
20. Kuna ithibati gani kwamba mwishowe Babiloni lilipata kuwa “magofu”?
20 Isaya hakuishi kuona Babiloni likiwa bila wakaaji. Lakini kwa utimizo wa unabii, mwishowe Babiloni lilipata kuwa “magofu.” (Yeremia 51:37) Kulingana na Jerome, msomi Myahudi (aliyezaliwa karne ya nne W.K.), kufikia siku yake Babiloni lilikuwa eneo la uwindaji ambalo ndani yake “hayawani wa kila aina” walizurura, na laendelea kuwa ukiwa hadi siku hii. Kurudishwa kokote kwa Babiloni kuwa uvutio wa watalii huenda kukavuta wageni, lakini “mwana na mjukuu” wa Babiloni wametoweka milele, kama vile Isaya alivyotabiri.—Isaya 14:22.
21. Kwa nini manabii waaminifu waliweza kutabiri juu ya wakati ujao kwa usahihi usioweza kukosea?
21 Nabii Isaya hakufanya kisio lenye kutegemea mambo aliyoona. Wala hakuandika tena historia ili kuifanya ionekane kuwa unabii. Isaya alikuwa nabii wa kweli. Na ndivyo walivyokuwa manabii wengine wote wa Biblia waliokuwa waaminifu. Kwa nini wanaume hao waliweza kufanya jambo ambalo hakuna wanadamu wengine wowote wawezao kulifanya—kutabiri wakati ujao kwa usahihi usioweza kukosea? Jibu ni wazi. Huo unabii ulitokana na Mungu wa unabii, Yehova, ‘atangazaye mwisho tangu mwanzo.’—Isaya 46:10.
22. Kwa nini twapaswa kufanya yote tuwezayo ili kuwahimiza wenye mioyo ya haki wajichunguzie Biblia?
22 Je, Biblia yastahili kuchunguzwa? Twajua kwamba yastahili! Lakini watu wengi hawasadikishwi. Wamefanyiza maoni juu ya Biblia hata ingawa huenda ikawa hawajaisoma. Kumbuka yule profesa aliyetajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia. Alikubali kuisoma Biblia, na baada ya kuichunguza Biblia kwa uangalifu, alifikia mkataa kwamba hiyo ni kitabu kutoka kwa Mungu. Mwishowe alibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na leo hutumikia akiwa mzee! Acheni tufanye yote tuwezayo kuwahimiza watu wenye mioyo ya haki wajichunguzie Biblia, kisha wapate maoni fulani kuihusu. Tuna uhakika kwamba wakijifanyia uchunguzi wa moyo mweupe na wa moja kwa moja, watakuja kung’amua kwamba Biblia ni kitabu cha pekee kwa ajili ya watu wote!
-
-
Kitabu Kutoka kwa MunguMnara wa Mlinzi—1998 | Aprili 1
-
-
Vipi Mambo Ambayo Hayawezi Kuthibitishwa?
Biblia ina taarifa mbalimbali ambazo hazina uthibitisho wa kiasili kando na Biblia. Kwa kielelezo, yale isemayo juu ya milki isiyoonekana ikaliwayo na viumbe wa roho hayawezi kuthibitishwa—au kutothibitishwa—kisayansi. Je, lazima marejezo hayo yasiyoweza kuthibitishwa yaifanye Biblia ihitilafiane na Sayansi?
Hilo ndilo lililokuwa swali lililomkabili mtaalamu wa jiolojia ya sayari aliyeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova miaka kadhaa iliyopita. “Lazima nikiri kwamba kuikubali Biblia kulikuwa jambo gumu kwangu mwanzoni kwa sababu singeweza kuthibitisha kisayansi taarifa fulani za Biblia,” yeye akumbuka. Mwanamume huyu mwenye moyo mweupe aliendelea kujifunza Biblia na mwishowe akasadikishwa kwamba uthibitisho wenye kupatikana waonyesha kwamba hilo ni Neno la Mungu. “Hilo lilipunguza tamaa nyingi ya kutaka kila jambo katika Biblia lithibitishwe likiwa peke yake,” yeye aeleza. “Mtu mwenye mwelekeo wa kisayansi lazima awe tayari kuichunguza Biblia kwa maoni ya kiroho, au hataweza kamwe kukubali kweli. Sayansi haiwezi kutarajiwa ithibitishe kila taarifa katika Biblia. Lakini kwa sababu taarifa nyingine haziwezi kuthibitishwa, hilo halimaanishi kwamba si za kweli. Jambo la maana ni kwamba iwezekanapo usahihi wa Biblia huthibitishwa.”
-