Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Unaweza Kuepuka Kuzeeka?
    Amkeni!—2006 | Mei
    • Je, Unaweza Kuepuka Kuzeeka?

      “Tuna miaka sabini tu—ikiwa tuna nguvu, themanini; . . . uhai unakoma upesi, nasi tunatoweka.”—ZABURI 90:10, TODAY’S ENGLISH VERSION.

      HEBU wazia ukiishi katika upeo wa maisha daima. Wazia ukiwa na afya bora na akili chonjo wakati wote. Je, tarajio hilo zuri ni ndoto tu? Basi fikiria jambo hili lisilo la kawaida: Jamii fulani za kasuku wanaweza kuishi miaka mia moja hivi, hata hivyo, ni vigumu sana kwa panya kuishi kwa zaidi ya miaka mitatu. Tofauti hiyo kubwa ya muda ambao viumbe huishi imefanya wanabiolojia fulani wakate kauli kwamba kuzeeka husababishwa na jambo fulani, na kama ni hivyo, basi huenda kukawa na tiba.

      Kampuni nyingi za kutengeneza dawa zimetumia pesa nyingi kutafuta tiba inayofaa ya kuzuia kuzeeka. Isitoshe, hangaiko kuu la watu waliozaliwa baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu ambao sasa wana miaka 60 na kitu, limekuwa kutafuta dawa ya kuzuia kuzeeka.

      Pia utafiti kuhusu kuzeeka umekuwa jambo kuu kwa wataalamu wengi wanaochunguza chembe za urithi, molekuli, wanyama, na kuzeeka na athari zake. Kitabu Why We Age, cha Steven Austad, kinasema: “Siku hizi kunakuwa na msisimko mwingi wataalamu wanaochunguza kuzeeka na athari zake wanapokutana. Tunakaribia kuelewa sababu za msingi za kuzeeka na jinsi ambavyo uzee hutukia.”

      Watu wana maoni mengi kuhusu visababishi vya kuzeeka. Watu fulani wana maoni ya kwamba kuzeeka husababishwa na kuchakaa kwa chembe; nao wengine wanaamini kwamba kumepangwa kimbele. Baadhi ya watu wanasema kwamba maoni yote mawili ni sawa. Hata hivyo, je, watu wanaelewa kabisa jinsi ambavyo uzee hutukia? Je, kuna sababu yoyote ya kutazamia tiba inayofaa ya kuzuia kuzeeka?

      [Chati/Picha katika ukurasa wa 2, 3]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      APPROXIMATE LIFE SPANS

      Nyuki

      Siku 90

      ↓

      Panya

      Miaka 3

      ↓

      Mbwa

      Miaka 15

      ↓

      Tumbili

      Miaka 30

      ↓

      Aligeta

      Miaka 50

      ↓

      Tembo

      Miaka 70

      ↓

      Mwanadamu

      Miaka 80

      ↓

      Kasuku

      Miaka 100

      ↓

      Kobe-jitu

      Miaka 150

      ↓

      Mti mkubwa unaoitwa sequoia

      Miaka 3,000

      ↓

      Msonobari aina ya bristlecone

      Miaka 4,700

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Jamii fulani za kasuku wanaweza kuishi miaka 100, lakini wanadamu huishi miaka 80 hivi. Watafiti hujiuliza: “Ni nini husababisha kuzeeka?”

  • Kwa Nini Sisi Huzeeka?
    Amkeni!—2006 | Mei
    • Kwa Nini Sisi Huzeeka?

      “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.”—AYUBU 14:1, UNION VERSION.

      HUENDA ukawazia kwamba lazima viumbe-hai vyote vizeeke. Magari na mashini ambazo hutumiwa kila siku mwishowe huacha kufanya kazi. Huenda mtu akafikiri kwamba wanyama huzeeka na kufa kwa njia hiyohiyo. Lakini profesa wa elimu kuhusu wanyama Steven Austad anasema: “Viumbe vinatofautiana sana na mashini. Jambo kuu linalotofautisha viumbe na mashini ni kwamba viumbe vina uwezo wa kujirekebisha.”

      Inastaajabisha jinsi ambavyo mwili wako hujirekebisha baada ya kujeruhiwa, lakini inastaajabisha hata zaidi jinsi ambavyo mwili hujirekebisha kila siku. Kwa mfano, fikiria mifupa yako. “Inapotazamwa kwa nje, inaonekana kuwa haina uhai, lakini mifupa ni tishu hai ambayo daima hujiangamiza na kujirekebisha upya katika maisha yako yote,” linasema gazeti Scientific American. “Hatua hiyo ya kujirekebisha hufanyiza upya kabisa kiunzi cha mifupa ya mwanadamu kila baada ya miaka 10.” Sehemu nyingine za mwili wako hufanyizwa upya mara nyingi zaidi. Huenda chembe fulani za ngozi, ini, na matumbo zikafanyizwa upya karibu kila siku. Kila sekunde, mwili wako hutokeza chembe mpya zipatazo milioni 25. Ikiwa mwili wako haungefanya hivyo, na sehemu zote za mwili wako zisijirekebishe na kujibadili, ungezeeka ukiwa mtoto.

      Hoja ya kwamba hatuchakai ilistaajabisha zaidi wanabiolojia walipoanza kujifunza kuhusu molekuli katika chembe-hai. Chembe zako zinapofanyizwa upya, lazima kila chembe mpya iwe na nakala ya DNA yako. DNA ndiyo molekuli iliyo na habari nyingi inayohitajika ili kufanyiza upya mwili wako. Hebu wazia DNA imetokezwa mara ngapi, si tu katika mwili wako tangu ulipozaliwa, bali tangu uhai wa binadamu ulipoanza! Ili kuelewa jinsi jambo hilo linavyostaajabisha, fikiria kile ambacho kingetokea iwapo ungetumia mashini ya fotokopi kutoa nakala ya hati fulani kisha utumie nakala hiyo mpya kutokeza nakala nyingine. Ikiwa ungefanya hivyo tena na tena, ubora wa nakala ungeendelea kudhoofika na mwishowe nakala hiyo haingeweza kusomeka. Jambo la kufurahisha ni kwamba ubora wa DNA yetu haudhoofiki au kuchakaa kadiri chembe zetu zinavyotokeza chembe mpya tena na tena. Kwa nini? Kwa sababu chembe zetu zina njia nyingi za kurekebisha kasoro katika nakala ya DNA. Ikiwa hazingeweza kufanya hivyo, wanadamu wangekuwa wametoweka zamani za kale!

      Kwa kuwa sehemu zote za mwili wetu, kuanzia zile kubwa hadi molekuli ndogo kabisa hufanyizwa upya au kurekebishwa daima, kuchakaa hakuelezi kwa ukamili sababu inayofanya tuzeeke. Mifumo mingi ya mwili hujirekebisha na kujifanyiza upya kwa miaka mingi, katika njia tofauti na mwendo tofauti. Kwa hiyo, kwa nini mifumo hiyo yote huacha kufanya kazi karibu wakati uleule?

      Je, Kuzeeka Kumepangwa Kimbele?

      Kwa nini paka huishi miaka 20, lakini mnyama mwenye ukubwa sawa naye anayeitwa opossum huishi kwa miaka 3 tu?a Kwa nini popo anaweza kuishi kwa miaka 20 au 30, lakini panya huishi kwa miaka 3 tu? Kwa nini kobe-jitu anaweza kuishi kwa miaka 150 lakini tembo aishi kwa miaka 70 tu? Mambo kama vile chakula, uzito wa mwili, ukubwa wa ubongo, au ukuzi hayaelezi sababu inayofanya viumbe fulani waishi muda mrefu na wengine waishi muda mfupi. Kichapo Encyclopædia Britannica kinasema: “Chembe za urithi zina maagizo ambayo huonyesha miaka hususa ambayo viumbe fulani wataishi.” Muda ambao viumbe wataishi umeandikwa kwenye chembe za urithi. Lakini kiumbe anapokaribia kufa, ni nini hufanya utendaji wote wa mwili uache kufanya kazi?

      Mwanabiolojia wa molekuli Dakt. John Medina anaandika hivi: “Inaonekana kwamba kuna ishara zisizoeleweka ambazo hutokea nyakati fulani na kuagiza chembe ziache kufanya kazi yao ya kawaida.” Pia anasema: “Kuna chembe za urithi ambazo zinaweza kuagiza chembe nyingine, na hata mwili wote uzeeke na kufa.”

      Mwili wetu unaweza kulinganishwa na kampuni ambayo imekuwa ikifanya kazi kwa mafanikio kwa miaka mingi. Kwa ghafula, meneja wake wanaacha kuajiri na kuzoeza wafanyakazi wapya, wanaacha kurekebisha na kununua mashini mpya, na wanaacha kudumisha na kujenga upya majengo. Baada ya muda mfupi, kampuni hiyo itaanza kuzorota. Lakini kwa nini meneja hao walibadili sera zao zilizoleta mafanikio? Swali hilo ni sawa na lile ambalo wanabiolojia wanaochunguza kuzeeka wanakabili. Kitabu The Clock of Ages kinasema: “Katika utafiti kuhusu kuzeeka, jambo moja linalotatanisha sana ni kujaribu kuelewa sababu inayofanya chembe ziache kujifanyiza upya na kuanza kufa.”

      Je, Kuzeeka Kunaweza Kukomeshwa?

      Kuzeeka kumetajwa kuwa “tatizo gumu zaidi la kibiolojia kueleweka.” Baada ya kujaribu kwa miaka mingi, utafiti wote wa kisayansi haujafunua kisababishi cha kuzeeka sembuse jinsi ya kuukomesha. Mnamo 2004 gazeti Scientific American lilichapisha onyo la wanasayansi 51 wanaochunguza kuzeeka. Walionya hivi: “Hakuna bidhaa hata moja inayopatikana sasa ya kuzuia kuzeeka ambayo imethibitishwa kuwa inaweza kupunguza, kuzuia, au kufanya wazee wawe vijana tena.” Ingawa chakula bora na mazoezi yanaweza kuboresha afya yako na kupunguza hatari za kufa mapema kutokana na ugonjwa, hakuna kitu kinachoweza kuzuia kuzeeka. Mikataa hiyo inatukumbusha maneno haya ya Yesu yanayopatikana katika Biblia: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?”—Mathayo 6:27.

      Akitoa muhtasari kuhusu maendeleo ya kutafuta matibabu ya kuzeeka, Medina anaandika hivi: “Kwa kweli hatujui hasa sababu inayofanya tuzeeke. . . . Baada ya kuanzisha kampeni ya kukomesha kansa miaka mingi iliyopita, bado hatujapata tiba ya kansa. Na kuzeeka ni jambo gumu zaidi kushughulikia kuliko kansa.”

      Mkataa Muhimu Wafikiwa Baada ya Utafiti

      Utafiti kuhusu jinsi ambavyo viumbe hufanya kazi na sababu inayofanya vizeeke haujakatisha matumaini ya kuishi muda mrefu zaidi. Watu fulani wamegundua kwamba utafiti wao umewachochea kufikia mkataa muhimu ambao utawasaidia kuelewa kuzeeka. Mwanabiolojia wa molekuli Michael Behe anaandika hivi: “Kwa muda wa miaka 40 biokemia ya kisasa imefichua mambo mengi kuhusu chembe ambayo hayakujulikana awali. . . . Matokeo ya uchunguzi huo wote, yaani, kuchunguza uhai kwa kuangalia jinsi ambavyo molekuli za chembe hufanya kazi, ni uthibitisho ulio wazi na wenye kutokeza kwamba viumbe-hai ‘vilibuniwa’!” Mtu fulani alitumia akili nyingi kubuni viumbe-hai. Bila shaka, Behe siye mtu wa kwanza kufikia mkataa huo. Baada ya kufikiria muundo wa mwili wa binadamu, mtunga-zaburi wa kale aliandika hivi: “Nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.

      Ikiwa viumbe vyote vilivyo hai vimebuniwa, basi twapaswa kujiuliza swali hili lenye kuvuta fikira, Je, Mungu, yule Mbuni Mkuu aliumba wanadamu waishi kwa muda kama ule wa wanyama wengi, au je, anataka tuishi muda mrefu zaidi kuliko wanyama?

      [Maelezo ya Chini]

      a Mnyama anayeitwa opossum ni kati ya wanyama wasiokuwa na kondo na aliye na kifuko cha kubebea watoto ambaye hupatikana Amerika Kaskazini.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      ‘Tumeumbwa kwa njia ya ajabu’

      [Picha katika ukurasa wa 4, 5]

      Je, kuzeeka husababishwa na kuchakaa?

      [Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]

      DNA: Photo: www.comstock.com

  • Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?
    Amkeni!—2006 | Mei
    • Unaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

      “Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.”—AYUBU 33:25.

      MBWA anapokufa akiwa na miaka 10 au 20, huenda ikawa amefanya mambo mengi ambayo kwa kawaida mbwa hufanya. Huenda akawa amelea watoto, akafukuza paka, akazika mifupa, na kumlinda bwana wake. Lakini mwanadamu anapokufa akiwa na umri wa miaka 70 au 80, huwa ametimiza mambo machache sana kati ya mambo ambayo angeweza kufanya. Ikiwa alipenda michezo, labda alikuwa mahiri katika mchezo mmoja au miwili tu. Ikiwa alipenda muziki, huenda ikawa alijua kucheza vizuri ala moja au mbili tu. Ikiwa alipenda kuzungumza na watu katika lugha yao, pengine alizungumza kwa ufasaha lugha mbili au tatu tu. Angeweza kufurahia mambo mengi zaidi kama vile kukutana na watu, kugundua vitu vipya, na kumkaribia Mungu zaidi iwapo tu angeweza kuishi muda mrefu zaidi.

      Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu amuumbe mwanadamu akiwa na akili yenye uwezo wa kufurahia mambo mengi hivyo, kisha amkatishe tamaa kwa kutomwezesha aishi muda mrefu vya kutosha kufurahia mambo hayo?’ Maisha mafupi ya mwanadamu hayapatani na ubuni ulio na kusudi ambao unaonekana wazi katika uumbaji. Pia huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu amuumbe mwanadamu akiwa na sifa za pekee kama vile haki na huruma na wakati huohuo ampe mwelekeo wa kutenda mabaya?’

      Ukiona gari zuri likiwa limebonyea, je, utakata kauli kwamba liliundwa hivyo? La hasha! Bila shaka utakata kauli kwamba gari hilo halikupaswa kuwa hivyo. Lazima iwe lilitengenezwa vizuri, lakini baadaye mtu fulani akaliharibu. Vivyo hivyo, tunapofikiria jinsi ambavyo mwanadamu ameumbwa kwa njia ya ajabu, tunaweza kukata kauli kwamba maisha ya mwanadamu hayakukusudiwa yawe jinsi yalivyo leo. Maisha yetu mafupi na mwelekeo wa kutenda mabaya ni kama mibonyeo mibaya. Ni wazi kwamba mtu fulani aliharibu vibaya sana uhai mkamilifu wa wanadamu. Ni nani aliyefanya hivyo? Biblia inaonyesha waziwazi mtu huyo ni nani.

      Ikiwa hapo mwanzo wanadamu waliumbwa waishi milele, ni nani ambaye baadaye angeweza kuharibu uhai mkamilifu wa wanadamu? Inaweza kuwa tu babu ya wanadamu wote. Mwanadamu mwingine yeyote angeweza tu kuharibu chembe za urithi za wanadamu wachache, yaani, wazao wake. Kwa hiyo, Neno la Mungu, Biblia, linapatana na ukweli huo wa mambo, linaposema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu, mwanadamu wa kwanza] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote.” (Waroma 5:12) Kwa hiyo, Biblia inasema kwamba Adamu ndiye wa kulaumiwa kwa kuharibu uhai wetu mkamilifu. Maisha ya mwanadamu yalikusudiwa yaweje tangu mwanzo?

      Kuelewa Kusudi la Kuumbwa kwa Wanadamu

      Biblia inaposema kwamba kifo ‘kiliingia katika ulimwengu,’ inaonyesha kwamba mwanzoni wanadamu hawakukusudiwa wafe. Wanadamu wanazeeka na kufa kwa sababu mwanadamu wa kwanza alimwasi Mungu. Kwa upande mwingine, wanyama hawakukusudiwa waishi milele.—Mwanzo 3:21; 4:4; 9:3, 4.

      Watu waliumbwa kwa njia tofauti na wanyama. Uhai wetu ni wa hali ya juu zaidi kuliko wa wanyama, kama vile uhai wa malaika ulivyo wa hali ya juu kuliko wa wanadamu. (Waebrania 2:7) Tofauti na wanyama, mwanadamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:27) Pia, tofauti na wanyama, Biblia inamtaja Adamu kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Kwa hiyo, tuna sababu nzuri ya kuamini kwamba mwanadamu hakukusudiwa azeeke na kufa. Mungu hafi, wala hakuwaumba watoto wake wafe.—Habakuki 1:12; Waroma 8:20, 21.

      Tunaelewa zaidi kusudi la Mungu la kuumba wanadamu, tunapochunguza rekodi za kihistoria kuhusu vizazi vya kwanza vya wanadamu. Wakati huo, watu waliishi mamia ya miaka kabla ya kuzeeka. Adamu aliishi miaka 930. Vizazi vichache baadaye, Shemu, mwana wa Noa, aliishi miaka 600 tu, naye Arpakshadi, mjukuu wa Noa akaishi miaka 438.a (Mwanzo 5:5; 11:10-13) Baadaye, Abrahamu aliishi miaka 175. (Mwanzo 25:7) Inaonekana kwamba hatua kwa hatua dhambi imeathiri muda ambao wanadamu wanaishi, na hivyo kupunguza muda huo kadiri miaka ilivyopita tangu wanadamu wapoteze ukamilifu. Lakini mwanzoni mwanadamu aliumbwa aishi milele. Kwa hiyo, ni jambo la kawaida kujiuliza, ‘Je, bado Mungu anataka watu wafurahie kuishi milele duniani?’

      Kukombolewa Kutokana na Kuzeeka

      Kwa kuwa Yehova Mungu alikuwa amesema kwamba mtu yeyote asiyemtii angelipia dhambi yake kwa kufa, ilionekana kwamba wazao wa Adamu walikuwa katika hali isiyokuwa na tumaini. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, Maandiko yaliyoongozwa na roho, yalitoa tumaini la kwamba mtu fulani angelipa ili kuwakomboa watu kutokana na kuzeeka. Tunasoma hivi: “Mwachilie ili asishuke chini kuingia shimoni! Nimepata fidia! Nyama yake na iwe laini kuliko wakati wa ujana; na arudi kwenye siku za nguvu za ujana wake.” (Ayubu 33:24, 25; Isaya 53:4, 12) Katika andiko hili, Biblia inatoa tumaini zuri kwamba mtu fulani angelipa fidia ili kuwakomboa watu kutokana na kuzeeka!

      Ni nani angeweza kulipa fidia hiyo? Bei ya fidia haingeweza kununuliwa kwa pesa. Ikizungumza kuhusu wanadamu wasio wakamilifu, Biblia inasema: “Hakuna hata mmoja wao anayeweza kumkomboa hata ndugu, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake . . . hivi kwamba yeye aendelee kuishi milele.” (Zaburi 49:7-9) Hata hivyo, Yesu Kristo alikuwa na kitu fulani chenye thamani zaidi kuliko pesa. Alipokuwa duniani, alikuwa na uhai mkamilifu wa kibinadamu. Kwa kuwa alikuwa Mwana wa Mungu, alilindwa asirithi dhambi ya Adamu. Yesu alisema kwamba alikuja “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” Pindi nyingine alisema hivi: “Nimekuja ili wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.”—Mathayo 20:28; Yohana 10:10.

      Tumaini la kuishi milele ndilo lililokuwa jambo kuu katika mahubiri ya Yesu. Pindi moja, Petro ambaye alikuwa mfuasi wake mwaminifu alimwambia hivi: “Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:68) Biblia humaanisha nini inapotaja uzima wa milele?

      Uzima Usiokoma

      Mitume wa Yesu walitazamia wakati ambapo wangefurahia kuishi milele mbinguni wakiwa sehemu ya serikali ya Ufalme wa Yesu. (Luka 22:29; Yohana 14:3) Hata hivyo, mara nyingi Yesu alizungumza kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. (Mathayo 5:5; 6:10; Luka 23:43) Hivyo, miujiza na mafundisho ya Yesu kuhusu uzima wa milele yanathibitisha ahadi ambazo Mungu alitoa mapema sana kupitia nabii Isaya ambaye aliandika hivi: “Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Maisha ya wanadamu hayatakuwa tena miaka michache tu ya ujana yakifuatiwa na miaka ya kudhoofika na kuchakaa.

      Katika ulimwengu mpya wa Mungu, wakati ambapo wanadamu waaminifu watakuwa wakamilifu, watafurahia uhuru kutokana na kuzeeka. Biblia inasema: “Uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Wazia! Watu wataendelea kupata hekima na uzoefu. Lakini kadiri miaka itakavyosonga, hawatapoteza kamwe nguvu zao za ujana. Je, utakuwa hai wakati huo?

      Utaishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

      Kulingana na Yesu, kutakuwa na watu wachache sana duniani baada ya siku ya Mungu ya hukumu. (Mathayo 24:21, 22) Yesu alisema: “Barabara inayoongoza kwenye uharibifu ni pana na kubwa, na wengi ndio wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na wachache ndio wanaoipata.”—Mathayo 7:13, 14.

      Ili uwe kati ya watu watakaofurahia kuishi milele, unahitaji kutafuta kibali cha Mungu. Hatua ya kwanza ni kumjua Mungu. Yesu alieleza: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Ni kweli kwamba jitihada inahitajiwa ili kumjua Mungu vizuri; lakini, jitihada hiyo ina manufaa. Vivyo hivyo, jitihada inahitajiwa ili kupata pesa za chakula cha kila siku. Akilinganisha ujuzi kumhusu Mungu na chakula, Yesu alihimiza hivi: “Fanyeni kazi, si kwa ajili ya chakula ambacho huharibika, bali kwa ajili ya chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele.” (Yohana 6:27) Bila shaka, inafaa kujitahidi kadiri uwezavyo ili kupata uzima wa milele.—Mathayo 16:26.

      Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kwa hiyo, muda ambao utaishi unategemea jinsi unavyoitikia upendo wa Mungu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Watu fulani wanadai kwamba miaka inayotajwa katika simulizi hilo la Biblia ni miezi. Hata hivyo, andiko hilo linasema kwamba Arpakshadi alimzaa Shela akiwa na umri wa miaka 35. Tukichukua miaka hiyo kuwa miezi 35, basi Arpakshadi alimzaa mwana wake kabla ya kufikia umri wa miaka mitatu. Ni wazi kwamba hilo haliwezekani. Isitoshe, sura za kwanza za Mwanzo zinatofautisha miaka ya jua na miezi.—Mwanzo 1:14-16; 7:11.

      [Blabu katika ukurasa wa 7]

      Mwanadamu akiwa na umri wa miaka 80, huwa ametimiza mambo machache sana kati ya mambo ambayo angeweza kufanya

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      Wanadamu waliumbwa wakiwa na uhai wa hali ya juu zaidi kuliko wanyama

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Je, gari hili lilitengenezwa likiwa limebonyea?

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Neno la Mungu linasema kwamba wanadamu watarudia ‘siku za nguvu za ujana wao’

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki