-
Kunaswa Katika Ndoa Isiyo na UpendoAmkeni!—2001 | Januari 8
-
-
Kunaswa Katika Ndoa Isiyo na Upendo
“Katika jamii yenye talaka nyingi, ndoa zisizokuwa na furaha huelekea kuishia katika talaka, isitoshe, ndoa zilizo nyingi huelekea kukosa furaha.”—BARAZA LA MASUALA YA FAMILIA LA MAREKANI.
IMESEMWA kwamba furaha na huzuni maishani hutoka katika chanzo kimoja—ndoa. Kwa kweli, ni mambo machache maishani yenye uwezo wa kutokeza furaha kuu—au huzuni tele kama ndoa. Kama sanduku linavyoonyesha, wenzi wengi wana huzuni tele.
Lakini takwimu za talaka hufunua sehemu ndogo tu ya tatizo hilo. Ndoa moja inapovunjika nyingine nyingi hubaki zimeungana lakini zikiwa na matatizo chungu nzima. “Hapo awali familia yetu ilikuwa na furaha, lakini katika miaka 12 iliyopita hali imekuwa mbaya sana,” akadokeza mwanamke mmoja ambaye ameolewa kwa zaidi ya miaka 30. “Mume wangu hajali hisia zangu. Kwa kweli yeye huniumiza sana kihisia-moyo.” Vivyo hivyo, mwanamume mmoja ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka ipatayo 25 alilalamika hivi: “Mke wangu ameniambia kwamba hanipendi tena. Amenijulisha kwamba iwapo tunaweza kuishi kama watu wanaopanga chumba kimoja, na kila mmoja wetu ajiamulie jinsi atakavyotumia wakati wake wa mapumziko, basi yeye yuko tayari kuendelea kuishi nami.”
Bila shaka, watu fulani wanapojikuta katika hali mbaya kama hizo, huvunja ndoa yao. Hata hivyo, talaka ni jambo lisilowezekana kwa wengi. Kwa nini? Kulingana na Dakt. Karen Kayser, watoto, kufedheheshwa na jamii, hali ya kifedha, marafiki, watu wa ukoo, na itikadi za kidini ni baadhi ya sababu zinazowafanya wenzi wengi kuishi pamoja katika ndoa isiyo na upendo. “Bila matumaini ya kupata talaka kisheria,” aendelea kusema, “hawa wenzi huamua kuishi pamoja ingawa wametalikiana kihisia-moyo.”
Je, ni lazima watu wawili ambao upendo wao umepoa waendelee kuishi pamoja katika ndoa isiyoridhisha? Je, ndoa isiyo na upendo ndiyo njia pekee badala ya talaka? Mambo yaliyoonwa yaonyesha kwamba ndoa zilizo matatani zaweza kuokolewa—kutoka kwa uchungu wa talaka na pia huzuni ya ukosefu wa upendo.
-
-
Kwa Nini Upendo Hufifia?Amkeni!—2001 | Januari 8
-
-
Kwa Nini Upendo Hufifia?
“Inaonekana kuwa rahisi sana kumpenda mtu kuliko kudumisha upendo huo.”—DAKT. KAREN KAYSER.
ONGEZEKO kubwa la ndoa zisizo na upendo yamkini si jambo la kushangaza. Ndoa ni uhusiano tata wa kibinadamu, na wengi huingia katika uhusiano huo bila kujiandaa vya kutosha. “Inatubidi kuwa na uzoefu kiasi fulani kabla ya kupokea leseni ya kuendesha gari,” asema Dakt. Dean S. Edell, “lakini cheti cha ndoa chahitaji tu sahihi.”
Kwa sababu hiyo, ingawa ndoa nyingi hunawiri na kuwa na furaha tele, ndoa kadhaa hunyong’onyea katika matatizo. Huenda mwenzi mmoja au wote wawili waliingia katika ndoa wakiwa na matumaini makubwa lakini hawana ujuzi unaohitajika ili kudumisha ndoa. “Watu wanapopendana mara ya kwanza,” aeleza Dakt. Harry Reis, “kila mmoja huwa na uhakika mno na mwenziwe.” Wao huhisi kana kwamba mwenzi wao ndiye “mtu pekee duniani mwenye maoni sawa na yao. Nyakati nyingine hisia hiyo hufifia na inapokuwa hivyo, ndoa huathiriwa sana.”
Jambo la kupendeza ni kwamba ndoa nyingi hazifikii hatua hiyo. Lakini acheni tuchanganue kwa ufupi sababu kadhaa zinazosababisha upendo kufifia katika baadhi ya ndoa.
Kutamaushwa—“Sikutarajia Hali Hii”
“Nilipoolewa na Jim,” asema Rose, “nilitarajia tungekuwa na mapenzi kama ya malkia na mfalme mwenye kuvutia katika hadithi moja—mahaba kemkemu, wororo tele na kutendeana kwa fadhili.” Lakini, baada ya kitambo kidogo, “mfalme” wa Rose akawa havutii tena. “Hatimaye alinitamausha sana,” yeye asema.
Sinema, vitabu, na nyimbo zinazopendwa na wengi hutoa maoni yasiyo halisi kuhusu upendo. Wanapokuwa wakichumbiana, huenda mwanamume na mwanamke wakahisi kwamba mataraja yao yametimia; lakini baada ya miaka fulani katika maisha ya ndoa, wanakata kauli kwamba hiyo ilikuwa ni ndoto tu! Maisha ya ndoa yasiposhabihi yale yanayosimuliwa katika riwaya za mahaba, wengi huona ndoa yao haiwezi kufaulu kabisa.
Pasipo shaka, matazamio fulani katika ndoa yanafaa kabisa. Kwa mfano, inafaa kutazamia upendo, ufikirio na utegemezo kutoka kwa mwenzi wa ndoa. Na bado, huenda hata matazamio hayo yasitimizwe. “Nahisi kana kwamba sijaolewa,” asema Meena, msichana mchanga aliyeolewa karibuni huko India. “Najihisi nikiwa mpweke na hakuna anayenijali.”
Kutopatana—“Hatupatani kwa Vyovyote”
“Hatupatani kwa vyovyote na mume wangu,” asema mwanamke mmoja. “Najuta kila siku kwamba niliolewa naye. Hatufaani kabisa.”
Kwa kawaida haichukui muda mrefu kwa wenzi wa ndoa kung’amua kwamba hawafaani kama walivyodhani wakati wa uchumba. “Maisha ya ndoa hufunua tabia zilizofichika wenzi hao walipokuwa waseja,” aandika Dakt. Nina S. Fields.
Kwa sababu hiyo, baada ya kufunga ndoa wenzi fulani wanaweza kukata kauli kwamba hawapatani kabisa. “Licha ya upatano fulani katika mapendezi na utu, watu wengi huingia katika maisha ya ndoa wakiwa na tofauti kubwa sana katika mtindo, tabia, na mielekeo,” asema Dakt. Aaron T. Beck. Wenzi wengi wa ndoa hawajui namna ya kutatua tofauti hizo.
Ugomvi—“Sisi Hugombana Daima”
“Tulishangazwa na ugomvi wetu wa kila mara—kurushiana maneno, na jambo baya zaidi, kunyamaziana kwa siku nyingi,” asema Cindy, akikumbuka siku za mapema za ndoa yao.
Kutokuelewana ni jambo la kawaida katika ndoa. Lakini hali hiyo ishughulikiweje? “Katika maisha mazuri ya ndoa,” aandika Dakt. Daniel Goleman, “mume na mke wako huru kulalamika. Lakini mara nyingi kwa sababu ya hasira, malalamiko hutolewa kwa njia yenye kuumiza na yenye kushambulia tabia ya yule mwenzi mwingine.”
Hali hiyo inapotukia, mazungumzo hugeuka kuwa mashindano, kila mmoja akishikilia maoni yake kwa ushupavu na hivyo hushambuliana kwa maneno badala ya kuwasiliana. Kikundi kimoja cha wataalamu chasema hivi: “Mojawapo ya matokeo mabaya zaidi ya ubishi usiodhibitiwa ni kwamba wenzi husema mambo yanayotisha usalama wa ndoa yao wenyewe.”
Ubaridi— “Tumeshindwa”
“Nimeshindwa kufanya ndoa yetu ifaulu,” akakiri mwanamke mmoja baada ya miaka mitano katika maisha ya ndoa. “Najua kwamba haitafaulu. Sasa nahangaikia watoto tu.”
Imesemwa kwamba kinyume kabisa cha upendo si chuki bali ni ubaridi. Kwa hakika, ubaridi waweza kuharibu kabisa ndoa sawa na uhasama.
Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba, wenzi wengi wa ndoa wamevumilia ndoa isiyo na upendo kwa muda mrefu hivi kwamba hawana tumaini kabisa kwamba hali itabadilika. Kwa mfano, mume mmoja alisema kwamba maisha yake ya ndoa ya miaka 23 yalingana na “kufanya kazi isiyopendeza.” Aliongezea kusema: “Wajitahidi kufanya yale uwezayo katika hali hiyo.” Vivyo hivyo, mke aitwaye Wendy amekata tamaa kuhusu mume wake ambaye ameishi naye kwa miaka saba. “Nilijitahidi mara nyingi,” yeye asema, “lakini sikuzote alinitamausha. Niliishia kushuka-moyo. Sitaki kupatwa na hali hiyo tena. Nikimtumaini tena, nitajiletea tu uchungu. Afadhali nisitumainie chochote—sitakuwa na furaha lakini angalau sitashuka moyo.”
Kutamaushwa, kutopatana, ugomvi na ubaridi ni baadhi tu ya sababu zinazoweza kuchangia ukosefu wa upendo katika ndoa. Bila shaka, kuna sababu nyinginezo—sababu chache zinazungumziwa katika sanduku lililo kwenye ukurasa wa 5. Hata sababu iwe gani, je, kuna tumaini kwa wenzi ambao waonekana kuwa wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
NDOA ZISIZO NA UPENDO—VISABABISHI VINGINEVYO
• Pesa: “Mtu aweza kuwazia kwamba kwa kupanga bajeti, wenzi wa ndoa wataweza kuungana kwa sababu ya kulazimika kushirikiana katika kutumia mapato yao ya kifedha kukimu mahitaji, na kufurahia matunda ya kazi yao. Hata hivyo, jambo hili linalopasa kuwaunganisha wenzi wa ndoa, mara nyingi huwatenganisha.”—Dakt. Aaron T. Beck.
• Kuzaa: “Tumegundua kwamba uradhi katika uhusiano wa ndoa hupungua kwa kiwango kikubwa katika asilimia 67 ya wenzi wa ndoa baada ya kupata kifungua mimba, na magomvi huongezeka mara nane. Kwa sehemu, hilo huwa kwa sababu wazazi wamechoka na hawapati wakati wa kuwa pamoja.”—Dakt. John Gottman.
• Udanganyifu: “Panapo uzinzi udanganyifu upo, na udanganyifu, pasipo shaka, huvunja kutumainiana. Kwa kuwa kutumainiana kumetajwa kuwa sehemu muhimu katika ndoa zote ambazo zimefaulu kudumu kwa muda mrefu, je, inashangaza kwamba udanganyifu waweza kuathiri vibaya uhusiano wa ndoa?”—Dakt. Nina S. Fields.
• Ngono: “Watu wanapofikia hatua ya kuomba talaka, tabia ya kunyimana ngono kwa miaka mingi huwa ya kawaida sana. Katika visa fulani uhusiano wa ngono haukuwepo kamwe, na katika visa vingine, ngono ilifanywa bila hisia, njia tu ya mwenzi mmoja kujitosheleza kimwili.”—Judith S. Wallerstein, daktari mwanasaikolojia.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
WATOTO HUATHIRIWAJE?
Je, hali ya maisha yako ya ndoa yaweza kuathiri watoto wako? Jibu ni ndiyo, kulingana na Dakt. John Gottman ambaye amefanya uchunguzi wa wenzi wa ndoa kwa miaka 20. “Katika uchunguzi aina mbili uliofanywa kwa miaka kumi,” yeye anasema, “tuligundua kwamba watoto wa wenzi wasio na furaha huwa na kiwango cha juu cha mpigo wa moyo wanapocheza na wenzao na hushindwa kujituliza wenyewe. Baada ya muda, magomvi nyumbani huongoza kwa maksi za chini shuleni licha ya kiwango cha akili cha watoto hao.” Kinyume cha hilo, Dakt. Gottman asema kwamba watoto wa wenzi wa ndoa wenye uhusiano mzuri, “hufaulu katika masomo na katika mahusiano na watu wengine, kwa sababu wamejifunza kutoka kwa wazazi wao jinsi ya kuwastahi watu wengine na pia namna ya kushughulika na mivurugiko ya kihisia.”
-
-
Je, Kuna Sababu ya Kuwa na Tumaini?Amkeni!—2001 | Januari 8
-
-
Je, Kuna Sababu ya Kuwa na Tumaini?
“Tatizo moja katika ndoa zenye matatizo makubwa ni kushikilia sana wazo la kwamba hali haiwezi kuwa bora. Wazo hilo ni kipingamizi kwa sababu huzuia jitihada yoyote yenye kujenga.”—DAKT. AARON T. BECK.
HEBU jiwazie ukiwa na maumivu na umeenda kwa daktari ili uchunguzwe. Una wasiwasi—na kwa sababu nzuri. Kwani, afya yako—hata uhai wako—huenda ukawa hatarini. Tuseme kwamba baada ya uchunguzi, daktari akupa habari njema kwamba ijapokuwa hali yako ni mbaya, yaweza kutibiwa. Kwa kweli, daktari akujulisha kwamba iwapo utashikamana na utaratibu unaofaa wa mlo na mazoezi, unaweza kutazamia kupona. Kwa hakika utahisi umetulizwa sana na utafurahia kufuata ushauri wake!
Linganisha hali hiyo na habari tunayozungumzia hapa. Je, ndoa yako ina matatizo makubwa? Bila shaka, kila ndoa hupatwa na matatizo na kutoafikiana. Kwa hivyo, kuwa na pindi yenye mkazo katika uhusiano wenu hakumaanishi kuwa ndoa yenu haina upendo. Lakini vipi hali hiyo ikiendelea kwa majuma, miezi, au hata miaka? Ikiwa ndivyo, una sababu ya kuhangaika, kwa kuwa hilo si jambo dogo. Kwa kweli hali ya maisha ya ndoa yaweza kuathiri kila sehemu ya maisha yako—na ya watoto wako. Kwa mfano, inaaminika kwamba matatizo ya ndoa yaweza kuchangia sana matatizo kama vile kushuka-moyo, uzembe kazini, na watoto kufeli mitihani shuleni. Na kuna mengi zaidi. Wakristo hutambua kwamba uhusiano wao na wenzi wao wa ndoa waweza kuathiri uhusiano wao na Mungu.—1 Petro 3:7.
Uhakika wa kuwa kuna matatizo katika ndoa yenu haimaanishi hakuna tumaini. Kukabili mambo hakika kuhusu maisha ya ndoa—kwamba kutakuwa na magumu—kwaweza kusaidia wenzi wa ndoa kuona mambo kihalisi na kutafuta suluhisho. Mume anayeitwa Isaac asema hivi: “Sikujua kwamba kwa kawaida kiwango cha furaha katika maisha ya ndoa hupanda na kushuka. Nilifikiri sisi tuna kasoro fulani!”
Hata ikiwa ndoa yako imefikia hatua ya kukosa upendo, inaweza kuokolewa. Ni kweli kwamba athari za kihisia-moyo zenye kusababishwa na uhusiano wenye matatizo zaweza kuwa mbaya sana, hasa ikiwa matatizo yameendelea kwa miaka mingi. Licha ya hilo, kuna sababu yenye nguvu ya kuwa na tumaini. Nia ni ya maana sana. Hata watu wawili walio katika ndoa yenye matatizo makubwa waweza kuboresha hali iwapo wanathamini uhusiano wao.a
Kwa hivyo jiulize, ‘Tamaa yangu ya kuwa na uhusiano wenye kuridhisha ina nguvu kadiri gani?’ Je, wewe na mwenzi wako mko tayari kujitahidi kuboresha ndoa yenu? Dakt. Beck, aliyenukuliwa awali, asema hivi: “Nimeshangaa mara nyingi ninapoona uhusiano unaoonekana kuwa mbaya ukibadilika wenzi wanapojitahidi kufanyia kazi udhaifu wao na kuimarisha sifa nzuri za ndoa yao.” Lakini vipi ikiwa mwenzi wako hakuungi mkono kuiboresha ndoa yenu? Au vipi ikiwa mwenzi wako anaonekana hang’amui kwamba kuna tatizo? Je, juhudi yako binafsi ya kuboresha hali itaambulia patupu? La, hasha! “Ukifanya mabadiliko fulani,” asema Dakt. Beck, “hilo laweza kumchochea mwenzi wako kufanya mabadiliko—na huwa hivyo mara nyingi.”
Usikate kauli upesi kwamba hilo haliwezekani katika ndoa yako. Maoni yasiyofaa kama hayo huenda yakawa ndiyo tisho kubwa zaidi kwa ndoa yako! Mmoja wenu hana budi kuchukua hatua ya kwanza. Je, inaweza kuwa wewe? Ukiimarisha juhudi zako, huenda mwenzi wako akaona umuhimu wa kukuunga mkono ili kuifanya ndoa yenu iwe na furaha.
Hivyo basi, unaweza kufanya nini—ukiwa peke yako au mkiwa nyote wawili—ili kuokoa ndoa yenu? Biblia inasaidia sana kujibu swali hilo. Acheni tuone inavyofanya hivyo.
-
-
Ndoa Yako-Yaweza KuokolewaAmkeni!—2001 | Januari 8
-
-
Ndoa Yako-Yaweza Kuokolewa
Biblia ina mashauri chungu nzima yenye kutumika yawezayo kuwanufaisha waume na wake. Jambo hilo halishangazi hata kidogo, kwa sababu Yule aliyevuvia Biblia ndiye Mwanzilishi wa mpango wa ndoa.
BIBLIA ina maoni halisi juu ya ndoa. Inakiri kwamba mume na mke watakuwa na “dhiki” au kulingana na Biblia Habari Njema, “matatizo.” (1 Wakorintho 7:28) Hata hivyo, Biblia pia husema kwamba ndoa yaweza na yapasa kuleta shangwe, hata kufurahiana. (Mithali 5:18, 19) Mawazo hayo mawili hayapingani. Yanaonyesha tu kwamba licha ya matatizo mazito, wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu na wenye upendo.
Je, ndoa yako imekosa uhusiano kama huo? Je, matatizo na kukata tamaa yameharibu ukaribu na shangwe mliyokuwa nayo hapo mwanzoni? Hata ikiwa ndoa yako imekosa upendo kwa miaka mingi, hali inaweza kurudi kama ilivyokuwa hapo mwanzoni. Bila shaka, unahitaji kuona mambo kwa njia halisi. Hakuna mwanamume na mwanamke wasio na ukamilifu wawezao kuwa na ndoa kamilifu. Hata hivyo, kuna hatua unazoweza kuchukua ili kubadilisha hali zinazoharibu ndoa.
Unaposoma habari hii jaribu kuona mambo yanayohusu hasa ndoa yako. Badala ya kukazia fikira udhaifu wa mwenzi wako, teua madokezo machache ambayo wewe unaweza kufanyia kazi, halafu tumia mashauri hayo ya Kimaandiko. Huenda ukagundua kwamba ndoa yako yaweza kuokolewa kuliko ulivyodhani awali.
Tutaanza kwa kuzungumzia mtazamo kwa sababu maoni yako kuhusu uwajibikaji na hisia zako kuelekea mwenzi wako wa ndoa ni ya muhimu sana.
Maoni Yako Kuhusu Uwajibikaji
Kuazimia kuwa pamoja kwa muda mrefu ni kwa maana iwapo unataka kuboresha ndoa yako. Kwa vyovyote, Mungu alibuni mpango wa ndoa kuunganisha watu wawili wasitengane kamwe. (Mwanzo 2:24; Mathayo 19:4, 5) Kwa sababu hiyo, uhusiano wako na mwenzi wako wa ndoa haulingani na kazi ambayo unaweza kuacha au chumba unachoweza kuhama kwa kuvunja mapatano ya kulipa kodi. Badala ya hivyo, mlipokuwa mkifunga ndoa mliweka nadhiri ya kushikamana pamoja, hata hali iweje. Uwajibikaji wenye kina unapatana na maneno yaliyosemwa na Yesu Kristo yapata miaka 2,000 iliyopita: “Kile ambacho Mungu amefunga nira pamoja msiache mtu yeyote akitenganishe.”—Mathayo 19:6.
Watu fulani huenda wakasema, ‘Bado, tunaishi pamoja. Je, hilo halionyeshi kwamba tumewajibika?’ Labda. Hata hivyo, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa mfululizo huu, wenzi fulani wanaishi pamoja wakiwa na matatizo chungu nzima, wakiwa wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo. Lengo lako ni kufanya ndoa yako iwe na furaha, si yenye kuvumilika tu. Uwajibikaji wapasa kuambatana na uaminifu katika mpango wa ndoa na kwa yule mtu ambaye umeahidi kumpenda na kumtunza.—Waefeso 5:33.
Mambo unayomwambia mwenzi wako hufunua kadiri ya uwajibikaji wako. Kwa mfano, wakati wa mabishano makali, waume na wake fulani husema hivi bila kufikiri: “Nitakuacha!” au “Nitatafuta mtu mwingine anayenithamini!” Ingawa huenda usifanye hivyo, maneno kama hayo humomonyoa uwajibikaji kwa kudokeza kwamba mnaweza kuachana wakati wowote na kwamba mwenye kusema hivyo yuko tayari daima kuondoka.
Ili kurejesha upendo katika ndoa yenu, komeni kutoa vitisho kama hivyo mnapoongea. Kwa vyovyote, je, unaweza kupamba chumba ukijua kwamba unaweza kuhama wakati wowote? Kwa sababu gani, basi, umtazamie mwenzi wako kujitahidi kuboresha ndoa iliyo katika hatari ya kuvunjika? Azimia kujikakamua kwa moyo wote kutafuta suluhisho.
Mke mmoja alifanya hivyo baada ya kuvurugana kwa muda fulani na mume wake. “Licha ya kutopendezwa naye mara kwa mara, sikufikiria kuvunja uhusiano wetu,” yeye asema. “Tulitarajia kunyoosha mambo kwa vyovyote. Na sasa, baada ya miaka miwili iliyojaa misukosuko, naweza kusema kwa moyo mweupe kwamba tunafurahia uhusiano wetu tena.”
Naam, uwajibikaji ni wa pande zote—si kuishi tu pamoja bali kujitahidi mkiwa na lengo moja. Hata hivyo, huenda ukahisi kwamba pindi hii ndoa yenu imeunganishwa na wajibu tu. Ikiwa hali yako iko hivyo, usikate tamaa. Huenda ikawa kwamba upendo waweza kurudishwa tena. Vipi?
Kumheshimu Mwenzi Wako wa Ndoa
Biblia yasema hivi: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote.” (Waebrania 13:4; Waroma 12:10) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kuheshimika” limefasiliwa kwingineko katika Biblia kama “-enye kupendwa”, “-enye kustahiwa,” na “-enye thamani.” Ikiwa tunathamini kitu sana huwa tunafanya juhudi kukitunza. Labda umepata kuona jinsi mwanamume mwenye gari jipya lenye gharama sana anavyolitunza. Yeye huliweka gari lake la thamani likiwa safi na katika hali nzuri. Gari hilo likikwaruzwa yeye huhuzunika sana! Watu wengine hutunza afya yao kwa njia iyo hiyo. Kwa nini? Kwa sababu wanapendezwa na hali yao njema, na hivyo wanatunza afya yao.
Tunza na kulinda ndoa yako vivyo hivyo. Biblia husema kwamba upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Badala ya kulemewa na maoni hasi—labda kwa kukata tamaa na kusema, “Hatukuwa na upendo wa kweli,” “Tulifunga ndoa tukiwa wachanga mno,” au “Hatukujua tulichokuwa tukifanya” —kwa nini usitarajie mema na kujitahidi uwezavyo kuboresha hali, kisha usubiri uone matokeo? “Nimewasikia wateja wangu wengi wakisema, ‘Nimeshindwa kabisa!’” asema mshauri mmoja wa maisha ya ndoa. “Badala ya wao kuchanganua uhusiano wao na kuona sehemu zinazohitaji kuboreshwa, wao huvunjilia mbali ndoa yao haraka-haraka, na kutupilia mbali sifa nzuri wanazoshiriki pamoja, mambo muhimu waliyopata kushiriki pamoja, na matumaini yoyote ya wakati ujao.”
Ni mambo gani umeshiriki pamoja na mwenzi wako? Licha ya matatizo yaliyo katika uhusiano wenu, angalau unaweza kukumbuka pindi zenye furaha, miradi mliyotimiza, na hata magumu mliyokabili mkiwa pamoja. Tafakari mambo hayo, na uonyeshe kwamba unaheshimu ndoa yako na mwenzi wako wa ndoa kwa kujitahidi kwa moyo mweupe kuboresha uhusiano wenu. Biblia huonyesha kwamba Yehova Mungu hupendezwa sana na jinsi wenzi wa ndoa wanavyotendeana. Kwa mfano, katika siku za nabii Malaki, Yehova aliwakemea waume Waisraeli waliowatendea wake zao hiana kwa kuwataliki kwa sababu zisizo na maana. (Malaki 2:13-16) Wakristo wanataka ndoa yao imletee Yehova Mungu heshima.
Ugomvi—Hali Hiyo Ni Mbaya Kadiri Gani?
Sababu kuu ya kuwa na ndoa isiyo na upendo ni kushindwa kwa mume na mke kudhibiti ugomvi. Kwa kuwa hakuna watu wawili wanaofanana kabisa, ndoa zote zitakuwa na pindi za kutoelewana. Lakini wenzi wa ndoa wanaogombana daima hukuta upendo wao umepoa baada ya miaka fulani. Huenda hata wakakata kauli hivi, ‘Sisi hatupatani kwa vyovyote. Daima tunagombana!’
Hata hivyo, ugomvi haupasi kuvunja ndoa. Swali ni, Ugomvi ushughulikiweje? Katika ndoa zenye kufanikiwa, mume na mke wamejifunza kuzungumzia matatizo yao bila kuwa kama wale ambao daktari mmoja aliwaita, “maadui wa karibu sana.”
“Uwezo wa Ulimi”
Je, wewe na mwenzi wako mnajua namna ya kuzungumzia matatizo yenu? Nyote mwapaswa kuwa na nia ya kuzungumzia matatizo pamoja. Kwa kweli, huo ni ustadi—unaoweza kuwa mgumu kujifunza. Kwa nini? Mara kwa mara sote ‘hujikwaa katika neno’ kwa sababu sisi si wakamilifu. (Yakobo 3:2) Isitoshe, watu wengine pia walilelewa na wazazi wenye kufoka kwa hasira kwa ukawaida. Tangu utotoni, kwa njia fulani walilelewa wakijua kwamba kufoka kwa hasira na usemi wenye matusi ni mambo ya kawaida. Mvulana aliyelelewa katika mazingira kama hayo huenda akawa “mtu wa hasira” na “mwenye ghadhabu” anapokuwa mtu mzima. (Mithali 29:22) Vilevile, msichana mwenye malezi kama hayo anaweza kuwa ‘mwanamke mgomvi na mchokozi.’ (Mithali 21:19) Ni vigumu kubatilisha kufikiri na kuchangamana ambako kumekita mizizi.a
Hivyo basi, kudhibiti ugomvi hutaka kujifunza mbinu mpya za kujieleza. Hilo ni jambo zito, kwa sababu mithali moja ya Biblia husema hivi: “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Naam, huenda likaonwa kuwa jambo ndogo, lakini usemi wako kuelekea mwenzi wako unaweza kuharibu au kuufufua uhusiano wenu. “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga,” yasema mithali nyingine ya Biblia, “bali ulimi wa mwenye haki ni afya.”—Mithali 12:18.
Hata ijapokuwa mwenzi wako ndiye anayeonekana kuwa mwenye makosa kwenye ugomvi huo, fikiria unayosema. Je, maneno yako yanaumiza, au yanatuliza? Je, maneno yako huchochea au hutuliza hasira? “Neno liumizalo huchochea ghadhabu,” yasema Biblia. Kinyume cha hilo, “jawabu la upole hugeuza hasira.” (Mithali 15:1) Maneno yenye kuumiza—hata yakisemwa kwa upole—yatachochea hasira.
Bila shaka, iwapo kuna jambo linalokukera, una haki ya kujieleza. (Mwanzo 21:9-12) Lakini waweza kulieleza bila kejeli, matusi, na madharau. Jiwekee mipaka imara—kuhusu mambo ambayo utaazimia kutomwambia mwenzi wako, kama vile “Nakuchukia” au “Laiti hatungeoana.” Na ingawa mtume Mkristo Paulo hakuwa akizungumzia hususa juu ya ndoa, ni hekima kutohusika katika yale aliyoita “mashindano juu ya maneno” na “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo.”b (1 Timotheo 6:4, 5) Ikiwa mwenzi wako hutumia mbinu hizo, usimwige. Kwa kadiri inavyokutegemea wewe, fuatia amani.—Waroma 12:17, 18; Wafilipi 2:14.
Ni kweli kwamba wakati wa ugomvi mkali, ni vigumu kudhibiti usemi. Yakobo, mwandikaji wa Biblia asema kwamba “ulimi ni moto. Hakuna hata mmoja kati ya wanadamu awezaye kuufuga. Ni kitu kisichotawalika chenye ubaya, umejaa sumu yenye kuleta kifo.” (Yakobo 3:6, 8) Basi, utafanyaje hasira inapoanza kupanda? Utazungumzaje na mwenzi wako ili kutuliza ugomvi badala ya kuuchochea?
Kutuliza Ugomvi Mkali
Watu fulani wamegundua wanaweza kutuliza hasira kwa urahisi wakikazia fikira hisia zao na kutatua mambo yanayohusika badala ya kukazia matendo ya mwenzi wao. Kwa mfano, kusema “Mimi nahisi nimeumizwa na mambo uliyosema” kuna matokeo mazuri kuliko kusema “Unaniudhi” au “Unajua hupaswi kusema hivyo.” Bila shaka, unapoeleza hisia zako, sauti yako haipasi kuonyesha uchungu au madharau. Kusudi lako lapasa kuwa kuzungumzia tatizo wala si kushambulia mwenzako.—Mwanzo 27:46–28:1.
Kwa kuongezea, kumbuka nyakati zote kwamba kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” (Mhubiri 3:7) Watu wawili wanaposema wakati uleule, hakuna anayesikiliza, na hakuna manufaa yoyote yanayopatikana. Kwa hiyo, zamu yako ya kusikiliza ikiwadia, uwe “mwepesi sana juu ya kusikia, wa polepole juu ya kusema.” La maana pia, uwe “wa polepole juu ya hasira ya kisasi.” (Yakobo 1:19) Usiweke maanani kila neno la kuudhi asemalo mwenzi wako; wala “usifanye haraka kukasirika rohoni mwako.” (Mhubiri 7:9) Badala yake, jitahidi kufahamu sababu ya yeye kusema hivyo. “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake” yasema Biblia, “nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” (Mithali 19:11) Busara inaweza kumsaidia mume au mke kutafuta kiini cha ugomvi.
Kwa mfano, mke anapolalamika kwamba mume hapati wakati wa kuwa pamoja naye kwa kawaida halalamiki juu ya wakati tu. Huenda ikawa anahisi hakuna anayemjali au hathaminiwi. Vivyo hivyo, mume anayelalamika kwa kuwa mke alinunua kitu kisichopangiwa huenda asiwe analalamikia matumizi mabaya ya pesa. Bali huenda ikawa analalamika kwamba hakuhusishwa katika uamuzi huo. Mume au mke mwenye busara atachunguza ili kubaini kiini cha tatizo.—Mithali 16:23.
Je, jambo hilo ni gumu sana? Bila shaka! Nyakati fulani, licha ya juhudi zote, maneno makali yatasemwa na hamaki kuwaka. Unapoona dalili hizo, huenda ukahitaji kutumia shauri la Mithali 17:14: “Acheni ugomvi kabla haujafurika.” Afadhali kuahirisha mazungumzo hayo hadi hisia ziwe zimetulia. Ikiwa mmeshindwa kuzungumza kwa utulivu, basi huenda ikafaa kuwe na rafiki mkomavu awasaidie kutatua ugomvi wenu.c
Dumisha Mtazamo Halisi
Usivunjike moyo iwapo maisha yako ya ndoa ni tofauti na ulivyodhani wakati wa uchumba. Kikundi kimoja cha wataalamu chasema hivi: “Kwa watu wengi maisha ya ndoa si raha mstarehe nyakati zote. Kuna pindi ya raha na ya huzuni.”
Naam, maisha ya ndoa huenda yasiwe kama yanavyosimuliwa katika riwaya za mahaba, wala hayapasi kuwa yenye huzuni. Ingawa kutakuwako na pindi zenye magumu baina yako na mwenzi wako, kutakuwako pia na pindi za kusahau matatizo yenu na kufurahia tu kuwa pamoja, kuwa na ushirika wenye uchangamfu, na kuzungumza pamoja kama marafiki. (Waefeso 4:2; Wakolosai 3:13) Pindi kama hizo zinaweza kutumika kuamsha tena upendo uliofifia.
Kumbuka, watu wawili wasio wakamilifu hawawezi kuwa na ndoa kamilifu. Lakini wanaweza kuwa na kadiri fulani ya furaha. Kwa kweli, hata matatizo yakiwepo, uhusiano baina yako na mwenzi wako wa ndoa waweza kuwapa uradhi kikweli. Jambo moja ni hakika: Ikiwa wewe na mwenzi wako wa ndoa mtajitahidi na kuwa tayari kunyumbulika na kutafuta faida ya yule mwingine, kuna matumaini kwamba ndoa yenu yaweza kuokolewa.—1 Wakorintho 10:24.
[Maelezo ya Chini]
a Malezi si udhuru wa kumfokea mwenzi wako wa ndoa. Hata hivyo, malezi yanatoa sababu kwa nini tabia hiyo imekita mizizi sana na kuwa vigumu kuishinda.
b Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo” laweza pia kurejezea “kuudhiana kwa vijambo vidogo.”
c Mashahidi wa Yehova wana msaada wa wazee wa kutaniko. Na ingawa hawajihusishi na mambo ya kibinafsi ya wenzi waliooana, wazee wanaweza kuwa msaada mkubwa kwa wenzi wenye matatizo.—Yakobo 5:14, 15.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
Je, maneno yako yanaumiza, au yanatuliza?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
TUPA MPIRA KWA UANANA
Biblia yasema hivi: “Acheni tamko lenu liwe na upendezi sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.” (Wakolosai 4:6) Bila shaka hilo lafaa katika ndoa! Kwa kielelezo: Katika mchezo wa kutupiana mpira, unatupa mpira kwa njia ambayo mwenzako aweza kuudaka kwa urahisi. Huvurumishi mpira kwa nguvu sana na kumwumiza mwenzio. Tumia kanuni hiyohiyo unapozungumza na mwenzi wako wa ndoa. Kumtupia maneno makali huumiza tu. Badala yake, sema kwa upole—kwa upendezi—ili mwenzi wako aweze kufahamu maoni yako.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
ZUNGUMZIA YALIYOPITA!
Soma barua na kadi za wakati uliopita. Tazama picha. Jiulize, ‘Ni nini kilichonivuta kwa mwenzi wangu? Ni sifa zipi zilizonivutia zaidi? Tulishiriki mambo gani pamoja? Tulifurahishwa na mambo gani?’ Kisha zungumzia mambo hayo yaliyopita pamoja na mwenzi wako wa ndoa. Mazungumzo yenye kuanza na taarifa “Unakumbuka wakati. . . ?” huenda yakatokeza fursa ya kuamsha hisia mlizokuwa nazo wakati uliopita.
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
MWENZI MPYA, MATATIZO YALEYALE
Wenzi fulani wa ndoa ambao wamenaswa katika ndoa isiyo na upendo hutamani kuanza upya na mwenzi mpya. Lakini Biblia hulaumu uzinzi, ikisema kwamba mtu anayetenda dhambi hiyo “hana akili kabisa” na kwamba “hujiangamiza yeye mwenyewe.” (Mithali 6:32, BHN) Hatimaye, mzinzi huyo asiyetubu hupoteza kibali cha Mungu—uangamizi ulio mbaya zaidi.—Waebrania 13:4.
Upumbavu wa mwenendo wa uzinzi hudhihirishwa katika njia nyinginezo. Kwanza, mtu huyo mzinzi anayechukua mwenzi mwingine yaelekea atakabili matatizo yaleyale yaliyotatiza ndoa yake ya kwanza. Dakt. Diane Medved, anataja jambo jingine muhimu: Yeye anasema, “Jambo la kwanza ambalo mwenzi wako mpya alijifunza kukuhusu ni kwamba wewe uko tayari kuvunja uaminifu. Yeye anajua kwamba unaweza kumdanganya mtu ambaye umeahidi kuishi naye. Kwamba wewe una tabia ya kujitetea. Kwamba unaweza kukengeushwa na kusahau ahadi yako. Kwamba kutosheleza tamaa zako za mwili au kiburi ni tanzi kwako. . . . Huyu mwenzi mpya ana uhakika gani kwamba hutapendezwa na mtu mwingine na kuondoka tena?”
[Sanduku katika ukurasa wa 14]
HEKIMA KUTOKA MITHALI ZA BIBLIA
• Mithali 10:19: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu; bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.”
Unapokuwa na hasira, huenda ukasema mambo usiyokusudia—na kujuta baadaye.
• Mithali 15:18: “Mtu wa hasira huchochea ugomvi; bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.”
Shutuma zenye kuumiza yaelekea zitamfanya mwenzi wako ajitetee, ilhali kusikiliza kwa subira kutawasaidia nyote kutafuta suluhisho.
• Mithali 17:27: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu ana busara.”
Unapohisi hasira yako ikipanda, afadhali kunyamaza ili kuzuia ugomvi mkali.
• Mithali 29:11: “Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.”
Kujidhibiti ni kwa maana. Kuropoka kwa hasira maneno yenye kuumiza kutafanya mwenzi wako ajitenge nawe.
-