Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 15
    • 3, 4. (a) Watu katika Jumuiya ya Wakristo hupataje kuwa wahudumu? (b) Ni nani anayeonwa kuwa mhudumu katika Jumuiya ya Wakristo, na kwa nini hali ni tofauti miongoni mwa Mashahidi wa Yehova?

      3 Makasisi hudai kuwa wahudumu (kutokana na neno mhudumu, ambalo ni tafsiri ya neno la Kilatini, di·aʹko·nos, “mtumishi”).a Ili kuwa wahudumu, wanahitimu katika vyuo au seminari kisha wanawekwa rasmi kuwa makasisi. Kichapo The International Standard Bible Encyclopedia chasema: “‘Kuwekwa rasmi kuwa kasisi’ kwa kawaida hurejezea cheo cha pekee kinachopewa wahudumu au makasisi kupitia taratibu zilizoidhinishwa rasmi, zinazokazia mamlaka ya kutangaza Neno au kusimamia ushirika mtakatifu wa Kikristo, au kufanya yote mawili.” Wahudumu huwekwa rasmi na nani? Kichapo The New Encyclopædia Britannica chasema: “Katika makanisa ambayo yamehifadhi cheo muhimu cha uaskofu, kwa kawaida askofu ndiye huweka watu rasmi kuwa makasisi. Katika makanisa ya Kiprotestanti yasiyo na cheo cha uaskofu, wahudumu wa mabaraza ya mkoa ndio huweka watu rasmi kuwa makasisi.”

      4 Hivyo, katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, ni watu wachache sana wanaopewa pendeleo la kuwa wahudumu. Hata hivyo, hali ni tofauti miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Kwa nini? Kwa kuwa hali haikuwa hivyo katika kutaniko la Wakristo wa karne ya kwanza.

  • Ni Nani Walio Wahudumu wa Mungu Leo?
    Mnara wa Mlinzi—2000 | Novemba 15
    • Kuwekwa Rasmi Kuwa Mhudumu—Lini?

      9. Yesu aliwekwa rasmi kuwa mhudumu lini, na nani?

      9 Kwa habari ya ni lini na ni kupitia nani mtu huwekwa rasmi kuwa mhudumu, hebu fikiria kielelezo cha Yesu Kristo. Yeye hakuwa na cheti cha kuwekwa rasmi kuwa mhudumu au digrii kutoka seminari ili kuthibitisha kwamba alikuwa mhudumu, naye hakuwekwa rasmi na mtu yeyote kuwa mhudumu. Basi, kwa nini tunaweza kusema kwamba alikuwa mhudumu? Kwa sababu maneno haya ya Isaya yaliyopuliziwa yalitimizwa kuhusiana naye: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kutangaza habari njema.” (Luka 4:17-19; Isaya 61:1) Maneno hayo yanatuhakikishia kwamba Yesu aliidhinishwa kutangaza habari njema. Na nani? Kwa kuwa roho ya Yehova ilimtia mafuta kwa ajili ya kazi hiyo, ni wazi kwamba Yesu aliwekwa rasmi kuwa mhudumu na Yehova Mungu. Aliwekwa rasmi lini? Roho ya Yehova ilimjia Yesu alipobatizwa. (Luka 3:21, 22) Kwa hiyo, aliwekwa rasmi kuwa mhudumu wakati wa ubatizo wake.

      10. Ni kupitia nani mhudumu Mkristo anapata kuwa “na sifa za ustahili wa kutosha”?

      10 Namna gani wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza? Yehova pia ndiye aliyewaweka rasmi kuwa wahudumu. Paulo alisema: “Kuwa kwetu na sifa za ustahili wa kutosha kwatoka kwa Mungu, ambaye kwa kweli ametustahilisha vya kutosha kuwa wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:5, 6) Yehova anawastahilishaje waabudu wake kuwa wahudumu? Fikiria mfano wa Timotheo, ambaye Paulo alimwita “mhudumu wa Mungu katika habari njema juu ya Kristo.”—1 Wathesalonike 3:2.

      11, 12. Timotheo alifanyaje maendeleo ili kuwa mhudumu?

      11 Maneno yafuatayo yaliyoandikiwa Timotheo yanatusaidia kuelewa jinsi alivyopata kuwa mhudumu: “Hata hivyo, wewe endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo na kwamba tangu utoto sana umeyajua maandishi matakatifu, yawezayo kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Imani ya Timotheo, iliyomchochea kufanya tangazo la hadharani, ilitegemea ujuzi wa Maandiko. Je, alihitaji kusoma tu kibinafsi? La. Timotheo alihitaji msaada ili kupata ujuzi sahihi na uelewevu wa kiroho wa mambo aliyosoma. (Wakolosai 1:9) Hivyo Timotheo “alishawishwa kuamini.” Kwa kuwa alijua Maandiko “tangu utoto sana,” bila shaka wafunzi wake wa kwanza walikuwa mama na nyanya yake, kwa kuwa yaonekana babake hakuwa mwamini.—2 Timotheo 1:5.

      12 Hata hivyo, ili Timotheo apate kuwa mhudumu, mengi yalihusika. Kwanza, imani yake iliimarika kwa kushirikiana na Wakristo wa makutaniko ya karibu. Tunajuaje? Kwa sababu Paulo alipokutana na Timotheo mara ya kwanza, kijana huyo “aliripotiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikoniamu.” (Matendo 16:2) Isitoshe, wakati huo ndugu fulani waliyaandikia barua makutaniko ili kuyaimarisha. Nao waangalizi wakayatembelea makutaniko ili kuyatia moyo. Maandalizi hayo yaliwasaidia Wakristo kama Timotheo kufanya maendeleo ya kiroho.—Matendo 15:22-32; 1 Petro 1:1.

      13. Timotheo aliwekwa rasmi lini kuwa mhudumu, na ni kwa nini waweza kusema kwamba maendeleo yake ya kiroho hayakukoma hapo?

      13 Kwa kuzingatia amri ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, tunaweza kuwa na hakika kwamba wakati fulani imani ya Timotheo ilimchochea kumwiga Yesu na kubatizwa. (Mathayo 3:15-17; Waebrania 10:5-9) Kwa kufanya hivyo, Timotheo alionyesha ujitoaji wa nafsi yote kwa Mungu. Timotheo alipata kuwa mhudumu alipobatizwa. Tangu wakati huo na kuendelea, uhai wake, nguvu zake na chochote alichokuwa nacho kikawa cha Mungu. Hiyo ilikuwa sehemu muhimu ya ibada yake, “utumishi mtakatifu.” Hata hivyo, Timotheo hakutosheka tu na kuwa mhudumu. Aliendelea kukua kiroho, akawa mhudumu Mkristo aliyekomaa. Hilo lilitokea kwa sababu Timotheo alishirikiana kwa ukaribu na Wakristo wakomavu kama Paulo, akajifunza mwenyewe kibinafsi, na kuhubiri kwa bidii.—1 Timotheo 4:14; 2 Timotheo 2:2; Waebrania 6:1.

      14. Leo, mtu ‘aliye na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ hufanyaje maendeleo ili awe mhudumu?

      14 Leo, watu huwekwa rasmi vivyo hivyo kuwa wahudumu katika huduma ya Kikristo. Mtu ‘aliye na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele’ anasaidiwa kujifunza juu ya Mungu na makusudi yake kupitia funzo la Biblia. (Matendo 13:48) Mtu huyo hujifunza kutumia kanuni za Biblia maishani mwake na kutoa sala zenye maana kwa Mungu. (Zaburi 1:1-3; Mithali 2:1-9; 1 Wathesalonike 5:17, 18) Hushirikiana na waamini wengine na hujinufaisha na maandalizi na mipango ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47; Mithali 13:20; Waebrania 10:23-25) Hivyo yeye hufanya maendeleo akifuata utaratibu fulani wa kujifunza.

      15. Ni nini hutukia mtu anapobatizwa? (Ona kielezi-chini pia.)

      15 Baada ya kusitawisha upendo kwa Yehova Mungu na imani yenye nguvu katika dhabihu ya fidia, mwanafunzi wa Biblia hutamani kujiweka wakfu kabisa kwa Baba yake wa mbinguni. (Yohana 14:1) Yeye hujiweka wakfu kupitia sala ya kibinafsi, kisha anabatizwa kama wonyesho wa hadharani wa kitendo hicho kilichofanywa faraghani. Ubatizo wake ndiyo sherehe ya kuwekwa rasmi kwake kuwa mhudumu kwa sababu wakati huo ndipo anapotambuliwa kuwa mtumishi, di·aʹko·nos, wa Mungu aliyejiweka wakfu kabisa. Ni lazima ajitenge na ulimwengu. (Yohana 17:16; Yakobo 4:4) Amejitoa kabisa kuwa “dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu” bila vizuizi wala masharti. (Waroma 12:1)b Yeye ni mhudumu wa Mungu, anayemwiga Kristo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki