-
“Bwana, Tufundishe Jinsi ya Kusali”Mnara wa Mlinzi—2004 | Februari 1
-
-
“Bwana, Tufundishe Jinsi ya Kusali”
“Mmoja wa wanafunzi wake akamwambia: ‘Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.’”—LUKA 11:1.
1. Kwa nini mmoja wa wanafunzi wa Yesu alimwomba awafunze jinsi ya kusali?
PINDI moja mwaka wa 32 W.K., mwanafunzi fulani wa Yesu alimwona akisali. Hangeweza kusikia yale Yesu aliyokuwa akimwambia Baba yake, kwa kuwa yaelekea ilikuwa sala ya kimya-kimya. Hata hivyo, Yesu alipomaliza, mwanafunzi huyo alimwambia hivi: “Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Ni nini kilichomchochea atoe ombi hilo? Sala ilikuwa jambo la kawaida katika maisha na ibada ya Wayahudi. Maandiko ya Kiebrania yana sala nyingi katika kitabu cha Zaburi na kwingineko. Hivyo, mwanafunzi huyo hakuwa akiomba afunzwe jambo ambalo hakujua au ambalo hakuwa amewahi kulifanya. Bila shaka, alijua sala za kidesturi za viongozi wa dini ya Kiyahudi. Lakini sasa alikuwa amemwona Yesu akisali, na yaelekea aliona tofauti kubwa kati ya sala za marabi za kujionyesha kuwa waadilifu na jinsi Yesu alivyosali.—Mathayo 6:5-8.
2. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakumaanisha kuwa tunapaswa kurudia sala ya kielelezo neno kwa neno? (b) Kwa nini tunapendezwa kujua jinsi ya kusali?
2 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, miezi 18 hivi awali, Yesu aliwapa wanafunzi wake sala ya kielelezo ambayo ingetumika kama msingi wa sala zao. (Mathayo 6:9-13) Inawezekana kwamba mwanafunzi huyo hakuwepo wakati huo, hivyo kwa fadhili Yesu akarudia sehemu muhimu za sala hiyo ya kielelezo. Ni wazi kwamba Yesu hakuirudia neno kwa neno, hiyo ikionyesha kwamba hakuwa anawapa sala ya kidini ya kurudia-rudia bila kufikiri. (Luka 11:1-4) Kama mwanafunzi huyo asiyetajwa jina, sisi pia tungependa kufundishwa jinsi ya kusali ili sala zetu zitusaidie kumkaribia Yehova zaidi. Kwa hiyo, na tuchunguze sehemu zote za sala hiyo ya kielelezo kama ilivyoandikwa na mtume Mathayo. Sala hiyo ina maombi saba, matatu yanahusu makusudi ya Mungu na manne yanahusu mahitaji yetu ya kimwili na ya kiroho. Katika makala hii tutazungumzia maombi matatu ya kwanza.
Baba Mwenye Upendo
3, 4. Inamaanisha nini kumwita Yehova “Baba yetu”?
3 Yesu alianza mazungumzo yake kwa kuonyesha kwamba sala zetu zinapaswa kudhihirisha uhusiano wa karibu na wenye heshima pamoja na Yehova. Akizungumza hasa kwa manufaa ya wanafunzi wake waliokuwa wamekusanyika karibu naye kwenye mlima, Yesu aliwaambia wasali kwa Yehova kwa kumwita “Baba yetu uliye mbinguni.” (Mathayo 6:9) Kulingana na msomi mmoja, hata kama Yesu alizungumza Kiebrania au Kiaramu kilichotumiwa na wengi, neno alilotumia kumaanisha “Baba” linafanana na jina ambalo mtoto humwita baba yake kwa upendo. Kumwita Yehova “Baba yetu” huonyesha kwamba tuna uhusiano mchangamfu na wenye kutumainika.
4 Kwa kusema “Baba yetu,” pia tunakiri kwamba sisi ni sehemu ya familia kubwa ya wanaume na wanawake wanaomtambua Yehova kuwa Mpaji-Uhai. (Isaya 64:8; Matendo 17:24, 28) Wakristo waliozaliwa kwa roho hufanywa kuwa “wana wa Mungu,” nao wanaweza ‘kupaaza sauti: “Abba, Baba!”’ (Waroma 8:14, 15) Mamilioni wamekuwa waandamani wao washikamanifu, nao wamejiweka wakfu kwa Yehova na kuonyesha wakfu wao kwa ubatizo wa maji. Hao “kondoo wengine” wote wanaweza pia kumfikia Yehova katika jina la Yesu na kumwita “Baba yetu.” (Yohana 10:16; 14:6) Tunaweza kusali kwa ukawaida kwa Baba yetu wa mbinguni ili kumsifu, kumshukuru kwa wema wake wote, na kumtwika mahangaiko yetu, tukiwa na hakika kwamba anatujali.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Petro 5:6, 7.
Kulipenda Jina la Yehova
5. Ni lipi ombi la kwanza katika sala ya kielelezo, na kwa nini linafaa?
5 Ombi la kwanza katika sala ya kielelezo linatanguliza mara moja mambo yanayopaswa kutangulizwa. Linasema: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Naam, tunapaswa kuhangaikia sana kutakaswa kwa jina la Yehova kwa sababu tunampenda na tunachukia kuona jinsi ambavyo jina lake limeshutumiwa sana. Wakati alipoasi na kuwashawishi wanadamu wa kwanza wasimtii Mungu, Shetani alilichongea jina la Yehova Mungu na njia yake ya kutawala ulimwengu wote ikatiliwa shaka. (Mwanzo 3:1-6) Isitoshe, tangu uasi wa kwanza, jina la Yehova limeshutumiwa kupitia matendo ya aibu na mafundisho ya wale wanaodai kumwakilisha.
6. Tutaepuka kufanya nini ikiwa tunasali jina la Yehova litakaswe?
6 Tunaposali jina la Yehova litakaswe, tunaonyesha msimamo wetu kuhusiana na suala la enzi kuu, yaani, tunaunga mkono kabisa haki ya Yehova ya kutawala ulimwengu wote. Yehova anataka ulimwengu wote ukaliwe na viumbe wenye akili ambao hujitiisha kwa hiari na kwa furaha chini ya utawala wake wa uadilifu kwa sababu wanampenda na wanapenda yote yanayowakilishwa na jina lake. (1 Mambo ya Nyakati 29:10-13; Zaburi 8:1; 148:13) Kulipenda jina la Yehova kutatusaidia tuepuke kufanya jambo lolote linaloweza kufanya jina hilo takatifu lishutumiwe. (Ezekieli 36:20, 21; Waroma 2:21-24) Kwa kuwa amani ya ulimwengu wote na ya wakaaji wake inategemea kutakaswa kwa jina la Yehova na kujitiisha kwa upendo chini ya utawala wake, tunaposali “jina lako na litakaswe” tunaonyesha uhakika wetu kwamba kusudi la Yehova litatimizwa kwa sifa yake.—Ezekieli 38:23.
Ufalme Tunaoomba
7, 8. (a) Yesu alitufunza tusali kuhusu Ufalme gani? (b) Tunajifunza nini kuhusu Ufalme huo katika kitabu cha Danieli na cha Ufunuo?
7 Ombi la pili katika sala ya kielelezo ni: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:10) Ombi hilo linahusiana sana na lile linalotangulia. Ili kutakasa jina lake takatifu Yehova atatumia Ufalme wa Kimasihi, yaani, serikali yake ya kimbingu ambayo Mwana wake, Yesu Kristo, ndiye amewekwa rasmi kuwa Mfalme anayefaa. (Zaburi 2:1-9) Unabii wa Danieli unafananisha Ufalme wa Kimasihi na “jiwe” lililokatwa kutoka ‘mlimani.’ (Danieli 2:34, 35, 44, 45) Mlima unafananisha enzi kuu ya Yehova, kwa hiyo Ufalme unaofananishwa na jiwe ni wonyesho mpya wa utawala wa Yehova juu ya ulimwengu. Katika unabii huo, jiwe nalo ‘linakuwa mlima mkubwa na kuijaza dunia yote,’ kuonyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi utawakilisha mamlaka kuu ya Mungu katika kutawala dunia.
8 Kuna wengine 144,000 ambao wanashirikiana na Kristo katika serikali hii ya Ufalme, ambao “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu” ili watawale pamoja naye wakiwa wafalme na makuhani. (Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4; 20:6) Danieli anawaita “watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi,” ambao pamoja na Kristo aliye Kichwa chao, hupokea “ufalme na utawala na ukuu wa falme zote chini ya mbingu zote . . . Ufalme wao ni ufalme unaodumu mpaka wakati usio na kipimo, na tawala zote zitawatumikia na kuwatii wao.” (Danieli 7:13, 14, 18, 27) Huo ni ufafanuzi mzuri wa serikali ya kimbingu ambayo Kristo aliwafunza wafuasi wake wasali kuihusu.
Kwa Nini Bado Tusali Ufalme Uje?
9. Kwa nini inafaa tusali Ufalme wa Mungu uje?
9 Katika sala yake ya kielelezo, Kristo alitufunza tusali Ufalme wa Mungu uje. Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kwaonyesha kwamba Ufalme wa Kimasihi ulisimamishwa mbinguni mwaka wa 1914.a Kwa hiyo, je, bado inafaa tusali Ufalme huo “uje”? Bila shaka. Kwa kuwa katika unabii wa Danieli, Ufalme wa Kimasihi unaofananishwa na jiwe, utaponda serikali za kisiasa za wanadamu, zinazofananishwa na sanamu kubwa. Jiwe hilo litaiponda-ponda sanamu hiyo iwe kama unga. Unabii wa Danieli unasema: “Ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Danieli 2:44.
10. Kwa nini tunatamani Ufalme wa Mungu uje?
10 Tunatamani kuona Ufalme wa Mungu ukija na kuharibu mfumo mwovu wa mambo wa Shetani kwa sababu hilo litamaanisha kutakaswa kwa jina takatifu la Yehova na kuondolewa kwa wanadamu wote wanaopinga enzi kuu ya Mungu. Tunasali hivi kwa bidii: “Ufalme wako na uje,” nasi tunajiunga na mtume Yohana kusema: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.” (Ufunuo 22:20) Naam, Yesu na aje kulitakasa jina la Yehova na kutetea enzi Yake kuu, ili maneno haya ya mtunga-zaburi yaweze kutimia: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zaburi 83:18.
“Mapenzi Yako na Yatendeke”
11, 12. (a) Sisi huwa tunaomba nini tunaposali mapenzi ya Mungu “yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni”? (b) Kusali mapenzi ya Yehova yatendeke kunamaanisha nini zaidi?
11 Halafu Yesu akawafunza wanafunzi wake wasali hivi: “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ulimwengu wote ulitokea kwa sababu ya mapenzi ya Yehova. Viumbe wa mbinguni wenye nguvu hupaaza sauti: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Yehova ana kusudi kuelekea “vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:8-10) Tunaposali mapenzi ya Mungu yatendeke, sisi kwa kweli huwa tunamwomba Yehova atimize kusudi lake. Isitoshe, tunaonyesha kwamba tunatamani kuona mapenzi ya Mungu yakitendeka katika ulimwengu wote.
12 Kupitia sala hiyo tunaonyesha pia kwamba tuko tayari kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova. Yesu alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:34) Kama Yesu, sisi ambao ni Wakristo waliojiweka wakfu tunafurahia kufanya mapenzi ya Mungu. Upendo wetu kwa Yehova na kwa Mwana wake hutuchochea tuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.” (1 Petro 4:1, 2; 2 Wakorintho 5:14, 15) Sisi hujitahidi kuepuka kufanya mambo tunayojua ni kinyume cha mapenzi ya Yehova. (1 Wathesalonike 4:3-5) Kwa kununua wakati wa kusoma na kujifunza Biblia, ‘tunaendelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova,’ ambayo yanatia ndani kuhubiri “hii habari njema ya ufalme.”—Waefeso 5:15-17; Mathayo 24:14.
Mapenzi ya Yehova Mbinguni
13. Mapenzi ya Mungu yalikuwa yakitendeka jinsi gani muda mrefu kabla ya uasi wa Shetani?
13 Mapenzi ya Yehova yalikuwa yakitimizwa mbinguni muda mrefu kabla mmoja wa wana wake wa kiroho kuasi na kuwa Shetani. Kitabu cha Methali humfananisha Mwana wa kwanza wa Mungu na hekima. Kinaonyesha kwamba kwa muda usio na kipimo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu ‘alikuwa akifurahi mbele zake wakati wote,’ akifurahi kufanya mapenzi ya Baba yake. Mwishowe, akawa “stadi wa kazi” wa Yehova katika kuumba vitu vyote “mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana.” (Methali 8:22-31; Wakolosai 1:15-17) Yehova alimtumia Yesu kuwa Neno, au Msemaji wake.—Yohana 1:1-3.
14. Tunaweza kujifunza nini katika Zaburi 103 kuhusu jinsi malaika wanavyotimiza mapenzi ya Yehova mbinguni?
14 Mtunga-zaburi anaonyesha kwamba enzi kuu ya Yehova iko juu ya uumbaji wote na kwamba malaika husikiliza maagizo na amri zake. Tunasoma: “Yehova amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu. Mbarikini Yehova, enyi malaika zake, mlio na uwezo katika nguvu, mnaolitenda neno lake, kwa kuisikiliza sauti ya neno lake. Mbarikini Yehova, enyi majeshi yake yote, enyi wahudumu wake, mnaofanya mapenzi yake. Mbarikini Yehova, enyi kazi zake zote, katika mahali pote pa utawala [au, “enzi kuu”] wake.”—Zaburi 103:19-22.
15. Mapenzi ya Mungu yalitendekaje mbinguni Yesu alipopokea mamlaka ya Ufalme?
15 Baada ya Shetani kuasi, bado angeweza kuingia mbinguni, kama inavyoonyeshwa katika kitabu cha Ayubu. (Ayubu 1:6-12; 2:1-7) Hata hivyo, kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba wakati ungefika ambapo Shetani na roho wake waovu wangefukuzwa mbinguni. Yaonekana wakati huo ulifika muda mfupi baada ya Yesu Kristo kupokea mamlaka ya Ufalme mwaka wa 1914. Tangu wakati huo, waasi hao hawana mahali tena mbinguni. Wamezuiwa katika ujirani wa dunia. (Ufunuo 12:7-12) Sasa hakuna yeyote mbinguni anayepinga enzi kuu ya Yehova, bali wote wameungana kumsifu “Mwana-Kondoo,” Kristo Yesu, na kumsifu Yehova kwa utii. (Ufunuo 4:9-11) Kwa kweli, mapenzi ya Yehova yanatimizwa mbinguni.
Mapenzi ya Mungu Kuhusu Dunia
16. Sala ya kielelezo inapingaje fundisho la makanisa yanayojiita ya Kikristo kuhusu tumaini la wanadamu?
16 Makanisa yanayojiita ya Kikristo hayataji dunia katika makusudi ya Mungu, yakidai kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni. Lakini Yesu alitufunza tusali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Je, tunaweza kusema kwamba mapenzi ya Yehova yanatimizwa kikamili leo katika dunia hii yenye jeuri, ukosefu wa haki, magonjwa, na kifo? Sivyo! Kwa hiyo, tunapaswa kusali kwa bidii mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kupatana na ahadi hii iliyoandikwa na mtume Petro: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya [serikali ya Ufalme wa Kimasihi wa Kristo] na dunia mpya [jamii ya wanadamu waadilifu], na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.
17. Ni nini kusudi la Yehova kuelekea dunia?
17 Yehova aliiumba dunia akiwa na kusudi. Alimwongoza nabii Isaya kwa roho yake aandike: “Yehova, Muumba wa mbingu, Yeye Mungu wa kweli, Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu, amesema hivi: ‘Mimi ni Yehova, wala hakuna mwingine.’” (Isaya 45:18) Mungu aliwaweka wenzi wa kwanza wa kibinadamu katika bustani ya kiparadiso na kuwaagiza hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:27, 28; 2:15) Ni wazi kwamba kusudi la Muumba ni kwamba dunia ikaliwe na jamii ya wanadamu wakamilifu na waadilifu, ambao hujitiisha kwa furaha chini ya enzi kuu ya Yehova na kuishi milele katika Paradiso iliyoahidiwa na Kristo.—Zaburi 37:11, 29; Luka 23:43.
18, 19. (a) Ni nini kinachopaswa kufanywa kabla ya mapenzi ya Mungu kutimizwa kikamili duniani? (b) Ni mambo gani mengine kuhusu sala ya kielelezo ya Yesu yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?
18 Mapenzi ya Yehova kuhusu dunia hayawezi kamwe kutimizwa kikamili huku dunia ikiwa na wanaume na wanawake wanaokaidi enzi kuu yake. Akitumia majeshi yenye nguvu ya viumbe wa roho chini ya uongozi wa Kristo, Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ Mfumo wote mwovu wa Shetani pamoja na dini za uwongo, siasa fisadi, biashara yenye pupa na isiyo ya unyoofu, na majeshi yenye kuleta uharibifu, yataharibiwa kabisa. (Ufunuo 11:18; 18:21; 19:1, 2, 11-18) Enzi kuu ya Yehova itatetewa na jina lake kutakaswa. Tunaomba mambo hayo yote tunaposema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
19 Hata hivyo, katika sala yake ya kielelezo, Yesu alionyesha kwamba tunaweza pia kusali kuhusu mambo ya kibinafsi. Mambo hayo ambayo yametajwa katika mafundisho yake kuhusu sala yatazungumziwa katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura ya 6 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila SikuMnara wa Mlinzi—2004 | Februari 1
-
-
Yehova Hutuandalia Mahitaji Yetu ya Kila Siku
“Acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana . . . Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo.”—LUKA 12:29, 30.
1. Yehova huwaandaliaje wanyama?
JE, UMEWAHI kumtazama shomoro au ndege mwingine akidonoa-donoa udongo? Labda ulijiuliza kama ndege huyo angepata chakula chochote kwa kufanya hivyo. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionyesha tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na jinsi Yehova anavyowaandalia ndege. Alisema: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?” (Mathayo 6:26) Yehova huwaandalia viumbe wake chakula kwa njia za ajabu.—Zaburi 104:14, 21; 147:9.
2, 3. Ni mambo gani ya kiroho tunayoweza kujifunza kutokana na uhakika wa kwamba Yesu alitufunza tuombe mkate wetu wa kila siku?
2 Kwa nini basi Yesu alitaja ombi hili katika sala yake ya kielelezo: “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii”? (Mathayo 6:11) Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na ombi hilo. Kwanza, linatukumbusha kwamba Yehova ndiye Mwandalizi Mkuu. (Zaburi 145:15, 16) Wanadamu wanaweza kupanda na kulima, lakini Mungu tu ndiye anayeweza kufanya vitu vikue kiroho na kimwili. (1 Wakorintho 3:7) Vitu tunavyokula na kunywa ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Matendo 14:17) Tunapomwomba atutimizie mahitaji yetu ya kila siku, tunamwonyesha kwamba tunathamini maandalizi hayo. Bila shaka, ombi hilo halituondolei daraka la kufanya kazi ikiwa tunaweza kufanya hivyo.—Waefeso 4:28; 2 Wathesalonike 3:10.
3 Pili, kumwomba “mkate kwa ajili ya siku hii” huonyesha kwamba hatupaswi kuhangaika kupita kiasi kuhusu wakati ujao. Yesu pia alisema: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote. Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe.” (Mathayo 6:31-34) Sala ya kuomba “mkate kwa ajili ya siku hii” inatuwekea kielelezo cha kuishi maisha rahisi ya “ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu.”—1 Timotheo 6:6-8.
Chakula cha Kiroho Siku kwa Siku
4. Ni matukio gani katika maisha ya Yesu na ya Waisraeli yanayokazia umuhimu wa kula chakula cha kiroho?
4 Sala yetu ya kuomba mkate wa kila siku inapaswa pia kutukumbusha kwamba tunahitaji chakula cha kiroho kila siku. Ingawa Yesu alikuwa na njaa kali baada ya kufunga kwa muda mrefu, alikataa kishawishi cha Shetani cha kugeuza mawe yawe mkate, aliposema: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Hapa Yesu alimnukuu nabii Musa aliyewaambia Waisraeli hivi: “[Yehova] alikunyenyekeza, akakuacha ukae na njaa, akakulisha mana, ambayo hukuwa umeijua wala baba zako hawakuwa wameijua; ili kukufanya ujue kwamba mwanadamu haishi kwa mkate tu bali mwanadamu huishi kwa kila neno la kinywa cha Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 8:3) Njia ambayo Yehova alitumia kutoa mana iliwaandalia Waisraeli chakula cha kimwili na pia kuwafunza mambo fulani ya kiroho. Mojawapo ya mambo hayo ni kwamba walipaswa “kuokota kila mtu kiasi chake siku baada ya siku.” Iwapo wangekusanya mana nyingi kuliko mahitaji yao ya siku, mabaki yangeanza kunuka na kutokeza wadudu. (Kutoka 16:4, 20) Hata hivyo, haikuwa hivyo siku ya sita ambayo walipaswa kukusanya mana kiasi cha siku mbili kwa ajili ya siku ya Sabato. (Kutoka 16:5, 23, 24) Kwa hiyo, mana hiyo iliwakumbusha kwamba walipaswa kutii na kwamba maisha yao hayakutegemea mkate tu bali “kila neno la kinywa cha Yehova.”
5. Yehova hutuandaliaje chakula cha kiroho kila siku?
5 Vivyo hivyo, tunahitaji kula chakula cha kiroho kila siku ambacho Yehova huandaa kupitia Mwana wake. Ili kutimiza kusudi hilo,Yesu amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili aandae ‘chakula kwa wakati unaofaa’ kwa ajili ya watu wa nyumba ya imani. (Mathayo 24:45) Jamii hiyo ya mtumwa mwaminifu huandaa chakula kingi cha kiroho kupitia vifaa vya kujifunzia Biblia na pia hututia moyo tusome Biblia kila siku. (Yoshua 1:8; Zaburi 1:1-3) Kama Yesu, sisi pia tunaweza kupata chakula cha kiroho kwa kujitahidi kila siku kujifunza na kufanya mapenzi ya Yehova.—Yohana 4:34.
Msamaha wa Dhambi
6. Tunapaswa kuomba msamaha kwa madeni gani, naye Yehova yuko tayari kuyafutilia mbali kwa masharti gani?
6 Ombi linalofuata katika sala ya kielelezo ni: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mathayo 6:12) Hapa Yesu hakuwa akizungumzia madeni ya pesa bali kusamehewa dhambi zetu. Katika maandishi ya Luka kuhusu sala ya kielelezo, ombi hilo linasema: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.” (Luka 11:4) Hivyo, tunapofanya dhambi, ni kana kwamba tunakuwa na deni kwa Yehova. Lakini Mungu wetu mwenye upendo yuko tayari ‘kufuta,’ au kufutilia mbali deni hilo tukitubu kikweli, ‘tukigeuka,’ na kumwomba msamaha kwa msingi wa imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo.—Matendo 3:19; 10:43; 1 Timotheo 2:5, 6.
7. Kwa nini tunapaswa kuomba msamaha kila siku?
7 Kwa upande mwingine, tunafanya dhambi tunapokosa kufikia viwango vya Yehova vya uadilifu. Kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, sote hukosea katika kusema, kutenda, na kuwaza au kwa kukosa kufanya mambo tunayopaswa kufanya. (Mhubiri 7:20; Waroma 3:23; Yakobo 3:2; 4:17) Kwa hiyo, iwe tunajua au hatujui kama tulifanya dhambi, tunapaswa kuomba msamaha wa dhambi zetu tunaposali kila siku.—Zaburi 19:12; 40:12.
8. Sala ya kuomba msamaha inapaswa kutochochea kufanya nini, nasi tutanufaikaje?
8 Kabla ya kuomba msamaha tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu, tutubu, na kuungama, tukiwa na imani katika uwezo wa kukomboa wa damu ya Kristo iliyomwagwa. (1 Yohana 1:7-9) Ili kuonyesha kwamba sala yetu ni ya unyoofu, tunapaswa kuunga mkono ombi letu la msamaha kwa “matendo yanayostahili toba.” (Matendo 26:20) Hivyo, tunaweza kuwa na imani kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe dhambi. (Zaburi 86:5; 103:8-14) Tukisamehewa dhambi tutakuwa na amani ya akili isiyo na kifani, yaani, “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira” ambayo ‘itailinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Wafilipi 4:7) Lakini sala ya kielelezo ya Yesu hutufunza mengi zaidi kuhusu yale tunayopaswa kufanya ili kusamehewa dhambi zetu.
Ili Tusamehewe Ni Lazima Tusamehe
9, 10. (a) Yesu aliongeza ufafanuzi gani katika sala ya kielelezo, nao ulikazia jambo gani? (b) Yesu alitoa mfano gani mwingine kuonyesha kwamba tunahitaji kuwa wenye kusamehe?
9 Inapendeza kuona kwamba ombi la ‘kusamehewa madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu,’ ndiyo tu sehemu ya sala ya kielelezo ambayo Yesu alifafanua. Baada ya kumaliza sala hiyo, aliongeza: “Kwa maana ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini ikiwa hamtawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.” (Mathayo 6:14, 15) Hivyo, Yesu alionyesha wazi kwamba ili Yehova atusamehe ni lazima tuwe tayari kuwasamehe wengine.—Marko 11:25.
10 Katika pindi nyingine, Yesu alitoa mfano kuonyesha uhitaji wa kusamehe ikiwa tunatarajia Yehova atusamehe. Alitaja mfalme mmoja ambaye kwa fadhili alifutilia mbali deni kubwa sana alilomdai mtumwa fulani. Baadaye, mfalme huyo alimwadhibu vikali mtumwa huyo alipokataa kufutilia mbali deni ndogo zaidi alilomdai mtumwa mwenzake. Yesu alimaliza mfano wake kwa kusema: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.” (Mathayo 18:23-35) Jambo ambalo Yesu alifunza ni wazi: Deni la dhambi ambalo Yehova amemsamehe kila mmoja wetu ni kubwa sana likilinganishwa na kosa lolote ambalo huenda tumetendewa na mtu mwingine. Isitoshe, Yehova hutusamehe kila siku. Hakika basi, tunaweza kuwasamehe wengine makosa ambayo wao hututendea mara kwa mara.
11. Tunapaswa kufuata shauri gani lililotolewa na mtume Paulo ikiwa tunatarajia Yehova atusamehe, na kutakuwa na matokeo gani mazuri?
11 Mtume Paulo aliandika: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Waefeso 4:32) Kusameheana huchangia amani kati ya Wakristo. Paulo aliendelea kuhimiza hivi: “Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:12-14) Mambo hayo yote yamo katika sala ambayo Yesu alitufunza: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”
Ulinzi Tunapopatwa na Jaribu
12, 13. (a) Ombi la pili kutoka mwisho katika sala ya kielelezo linamaanisha nini? (b) Ni nani aliye Mjaribu mkuu, na inamaanisha nini kusali tusiingizwe katika jaribu?
12 Ombi la pili kutoka mwisho katika sala ya Yesu ya kielelezo ni: “Usituingize katika jaribu.” (Mathayo 6:13) Je, Yesu alimaanisha kwamba tunapaswa kumwomba Yehova asituingize katika jaribu? La, kwa sababu mwanafunzi Yakobo aliongozwa na roho ya Mungu aandike: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Isitoshe, mtunga-zaburi aliandika: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Yehova hangojei kwa hamu tufanye makosa, naye hakika hajaribu kufanya tujikwae. Hivyo, sehemu hii ya sala ya kielelezo inamaanisha nini?
13 Shetani Ibilisi ndiye anayejaribu kufanya tujikwae, kutuangusha kwa matendo ya hila, na hata kutumeza. (Waefeso 6:11) Yeye ndiye Mjaribu mkuu. (1 Wathesalonike 3:5) Kwa kusali ili tusiingizwe katika jaribu, tunamwomba Yehova asiruhusu tuanguke tunapopatwa na jaribu. Tunamwomba atusaidie ili “Shetani asitushinde akili,” na tusishindwe na majaribu. (2 Wakorintho 2:11) Tunasali ili tudumu “mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi” na kupata ulinzi wa kiroho ambao hupewa wale wanaotambua enzi kuu ya Yehova katika yote wanayofanya.—Zaburi 91:1-3.
14. Mtume Paulo anatuhakikishiaje kwamba Yehova hatatuacha tukimtegemea tunapopatwa na jaribu?
14 Tunaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa hiyo ndiyo tamaa yetu ya unyoofu, ambayo tunaonyesha kupitia sala na matendo yetu, Yehova hatatuacha kamwe. Mtume Paulo anatuhakikishia hivi: “Hakuna jaribu ambalo limewapata ninyi ila lile lililo kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.
“Utukomboe Kutokana na Yule Mwovu”
15. Kwa nini ni muhimu zaidi sasa kusali tukombolewe kutokana na yule mwovu?
15 Kulingana na hati zenye kutegemeka zaidi za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, sala ya Yesu ya kielelezo inamalizika kwa maneno haya: “Utukomboe kutokana na yule mwovu.”a (Mathayo 6:13) Tunahitaji sana kulindwa dhidi ya Ibilisi wakati huu wa mwisho. Hiyo ni kwa sababu Shetani na roho wake waovu wanapigana na mabaki ya watiwa-mafuta “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu,” wakiwa pamoja na waandamani wao wa “umati mkubwa.” (Ufunuo 7:9; 12:9, 17) Mtume Petro aliwaonya Wakristo hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu. Lakini chukueni msimamo mkampinge yeye, mkiwa imara katika imani.” (1 Petro 5:8, 9) Shetani angependa kukomesha kazi yetu ya kuhubiri, naye hujaribu kutuogopesha kupitia wawakilishi wake duniani—wawe viongozi wa kidini, wafanyabiashara, au wanasiasa. Lakini Yehova atatukomboa tukisimama imara. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yakobo 4:7.
16. Yehova hutumia nini kuwasaidia watumishi wake wanapopatwa na majaribu?
16 Yehova aliruhusu Mwana wake ajaribiwe. Lakini Yesu alipompinga Ibilisi akitumia Neno la Mungu kuwa ulinzi, Yehova alituma malaika kumwimarisha. (Mathayo 4:1-11) Vivyo hivyo, Yehova hutumia malaika zake kutusaidia tukisali kwa imani na kumfanya kuwa kimbilio letu. (Zaburi 34:7; 91:9-11) Mtume Petro aliandika: “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.”—2 Petro 2:9.
Ukombozi Kamili Unakaribia
17. Kwa kutupatia sala ya kielelezo Yesu alionyeshaje mambo ya kutangulizwa?
17 Katika sala ya kielelezo, Yesu anaonyesha mambo ya kutangulizwa. Hangaiko letu kuu linapaswa kuwa kutakaswa kwa jina kuu na takatifu la Yehova. Kwa kuwa Yehova atatumia Ufalme wake wa Kimasihi kutekeleza jambo hilo, tunasali Ufalme huo uje ili uharibu falme au serikali zote za wanadamu ambazo si kamilifu, na kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yatatendeka kikamili mbinguni na pia duniani. Tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso linategemea kutakaswa kwa jina la Yehova na kutambuliwa ulimwenguni pote kwa enzi yake kuu ya uadilifu. Baada ya kusali kuhusu mambo hayo muhimu sana, tunaweza kusali kuhusu mahitaji yetu ya kila siku, msamaha wa dhambi zetu, na kukombolewa kutoka katika majaribu, na mbinu za ujanja za yule mwovu, Shetani Ibilisi.
18, 19. Sala ya Yesu ya kielelezo inatusaidiaje kuendelea kukesha na kufanya tumaini letu liwe “imara mpaka mwisho”?
18 Kukombolewa kabisa kutoka kwa yule mwovu na mfumo wake uliopotoka kunakaribia. Shetani anajua vizuri sana kwamba ana ‘kipindi kifupi tu cha wakati’ cha kudhihirisha ‘hasira yake kali’ duniani, hasa juu ya watumishi waaminifu wa Yehova. (Ufunuo 12:12, 17) Katika ishara yenye mambo mengi ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alitabiri matukio yenye kusisimua, ambayo baadhi yake yatatukia wakati ujao. (Mathayo 24:3, 29-31) Tutakapoona mambo hayo yakitukia, tumaini letu la kukombolewa litakuwa jangavu zaidi. Yesu alisema: “Mambo haya yanapoanza kutukia, simameni wima na kuinua vichwa vyenu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.”—Luka 21:25-28.
19 Sala fupi ya kielelezo ambayo Yesu aliwafunza wanafunzi wake inatutolea mwongozo mzuri kuhusu mambo tunayopaswa kutaja katika sala zetu mwisho unapokaribia. Na tuwe na hakika kwamba Yehova ataendelea kutuandalia mahitaji yetu ya kiroho na ya kimwili hadi mwisho kabisa. Tukiendelea kukesha katika sala tutaweza ‘kushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni imara mpaka mwisho.’—Waebrania 3:14; 1 Petro 4:7.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya Biblia za zamani kama vile Union Version, humalizia Sala ya Bwana kwa maneno haya ya kumsifu Mungu: “Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.” Kichapo The Jerome Biblical Commentary kinasema: “Maneno hayo ya kumsifu Mungu . . . hayapatikani katika [hati] zenye kutegemeka zaidi.”
-