-
Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?Mnara wa Mlinzi—2008 | Desemba 15
-
-
Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?
“Nihukumu, Ee Yehova, . . . kulingana na utimilifu wangu.”—ZAB. 7:8.
1, 2. Ni hali gani za kawaida zinazojaribu utimilifu wa Mkristo?
FIKIRIA hali hizi tatu: Mvulana anadhihakiwa na wanafunzi wenzake shuleni. Wanamchokoza ili akasirike, na labda wanataka awatukane au apigane nao. Je, atalipiza kisasi, au atajizuia na kuondoka? Mume yuko peke yake nyumbani akifanya utafiti kwa kutumia Intaneti. Kisha, kwa ghafula, anaona kwenye kompyuta tangazo fulani kuhusu kituo cha Intaneti chenye mambo machafu. Je, atashawishiwa kufungua kituo hicho, au atakiepuka kabisa? Mwanamke Mkristo anazungumza pamoja na dada wengine. Lakini mazungumzo yao yanageuka na kuwa porojo yenye kuumiza kuhusu dada fulani katika kutaniko. Je, mwanamke huyo atachangia mazungumzo hayo, au atajaribu kuyabadili?
2 Ingawa hali hizo zinatofautiana, zinafanana angalau kwa njia moja. Zote zinahusisha pambano la kudumisha utimilifu wa Kikristo. Je, unakumbuka utimilifu wako unapofikiria mahangaiko yako, mahitaji yako, na miradi yako maishani? Kila siku, watu wanafikiria sura yao, afya yao, matatizo ya kupata riziki, uhusiano wao na marafiki wao, na labda hata mahusiano ya kimapenzi. Huenda tukafikiria sana mambo hayo. Hata hivyo, Yehova anapendezwa hasa na nini anapochunguza moyo wetu? (Zab. 139:23, 24) Utimilifu wetu.
3. Yehova ametupa pendeleo la kufanya uamuzi gani, na tutachunguza nini katika habari hii?
3 Yehova, anayetoa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu,” amempa kila mmoja wetu zawadi mbalimbali. (Yak. 1:17) Ametupa zawadi kama vile mwili, akili, afya ya kadiri fulani, na uwezo mbalimbali. (1 Kor. 4:7) Hata hivyo, Yehova hatulazimishi kuwa watimilifu. Anaturuhusu tujiamulie ikiwa tutasitawisha sifa hiyo. (Kum. 30:19) Hivyo, tunahitaji kuchunguza maana ya utimilifu. Pia, tutachunguza sababu tatu zinazoonyesha kwa nini utimilifu ni sifa ya maana sana.
Utimilifu Ni Nini?
4. Utimilifu unahusisha nini, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na sheria ya Yehova kuhusu dhabihu za wanyama?
4 Inaonekana kwamba watu wengi hawaelewi vizuri maana ya utimilifu. Wengine wanafikiri ni unyoofu. Unyoofu ni sifa ya maana, lakini ni sehemu tu ya utimilifu. Katika Biblia, utimilifu unahusisha kuwa na maadili kamili, bila kasoro. Maneno ya Kiebrania yanayohusiana na “utimilifu” yanatokana na shina linalomaanisha bila kasoro, -zima, au bila upungufu. Neno moja kati ya hayo linatumiwa kuhusiana na dhabihu zilizotolewa kwa Yehova. Yehova alimkubali mnyama aliyetolewa dhabihu ikiwa tu hakuwa na kasoro au alikuwa mzima. (Soma Mambo ya Walawi 22:19, 20.) Yehova aliwashutumu vikali wale walioasi kimakusudi mwongozo wake kwa kutoa wanyama vilema, wagonjwa, au vipofu kuwa dhabihu.—Mal. 1:6-8.
5, 6. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba tunathamini vitu vizima, au vilivyo kamili? (b) Kwa habari ya wanadamu wasio wakamilifu, je, utimilifu ni sawa na ukamilifu? Eleza.
5 Si vigumu kuelewa wazo la kutafuta na kuthamini kitu ambacho ni kizima au kamili. Tuseme mtu anayependa kukusanya vitabu amepata kitabu chenye thamani baada ya kukitafuta kwa muda mrefu, lakini anagundua kwamba hakina kurasa fulani muhimu. Anavunjika moyo na kukirudisha kwenye kabati. Au tuseme mwanamke ameenda sokoni kununua samaki waliokaushwa. Wengine wamevunjika-vunjika. Anachunguza samaki mmoja baada ya mwingine ili aone samaki wanaofaa kabisa. Unafikiri atachagua samaki wa aina gani? Atachagua samaki wazima, walio kamili, ambao hawajavunjika. Vivyo hivyo, Mungu anawatafuta watu walio kamili, au wanaomtumikia kwa moyo wote.—2 Nya. 16:9.
6 Lakini, huenda ukajiuliza ikiwa mtu anahitaji kuwa mkamilifu ili awe mtimilifu. Kwa sababu tumerithi dhambi na hali ya kutokamilika, huenda tukajilinganisha kwa kadiri fulani na kitabu kisichokamilika au samaki ambaye si kamili. Je, ndivyo unavyohisi nyakati nyingine? Uwe na hakika kwamba Yehova hatarajii tuwe wakamilifu katika maana kamili. Hatarajii tutimize mambo tusiyoweza.a (Zab. 103:14; Yak. 3:2) Lakini, anatarajia tuendelee kuwa watimilifu. Basi, je, kuna tofauti kati ya ukamilifu na utimilifu? Ndiyo. Kwa mfano: Mwanamume fulani kijana anampenda msichana fulani ambaye atakuwa mke wake. Kijana huyo angekuwa mpumbavu ikiwa angetazamia msichana huyo awe mkamilifu. Hata hivyo, ni jambo la hekima kutarajia msichana huyo ampende kwa moyo wote, yaani, amwonyeshe yeye peke yake upendo wa kimahaba. Vivyo hivyo, Yehova ni “Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.” (Kut. 20:5) Hatarajii tuwe wakamilifu, bali anataka tumpende kwa moyo wote, na kumwabudu yeye peke yake.
7, 8. (a) Yesu aliweka mfano gani kuhusu utimilifu? (b) Kulingana na Maandiko, utimilifu unamaanisha nini hasa?
7 Huenda tukakumbuka jibu la Yesu alipoulizwa ni sheria gani iliyo kuu zaidi kati ya zote. (Soma Marko 12:28-30.) Yesu hakujibu tu; alionyesha hivyo kwa matendo. Aliweka mfano bora zaidi wa kumpenda Yehova kwa akili, moyo, nafsi, na nguvu zake zote. Alionyesha kwamba utimilifu hauonyeshwi kwa maneno matupu, bali kwa matendo mazuri yanayochochewa na nia nzuri. Ili tuendelee kuwa watimilifu tunahitaji kufuata hatua za Yesu.—1 Pet. 2:21.
8 Basi, kulingana na Maandiko, utimilifu unamaanisha hasa: kujitoa kwa moyo wote kwa Mtu mmoja aliye mbinguni, Yehova Mungu, na kujitoa kutimiza mapenzi na kusudi lake. Kuendelea kuwa watimilifu kunamaanisha kwamba katika maisha ya kila siku, tutajitahidi hasa kumpendeza Yehova Mungu. Tutatanguliza maishani mambo anayoyaona kuwa ya maana zaidi. Acheni tuchunguze sababu tatu zinazoonyesha kwa nini hilo ni jambo la maana sana.
1. Utimilifu Wetu na Suala la Enzi Kuu
9. Kuna uhusiano gani kati ya utimilifu wetu na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima?
9 Enzi kuu ya Yehova, haitegemei utimilifu wetu. Enzi yake kuu ni ya haki, ya milele, na ya ulimwengu wote mzima. Itakuwa hivyo nyakati zote, hata kiumbe yeyote yule aseme au afanye nini. Hata hivyo, enzi kuu ya Mungu imeletewa suto kubwa mbinguni na duniani. Hivyo, utawala wake unahitaji kutetewa mbele ya viumbe wote wenye akili, yaani, kuthibitishwa kuwa unafaa, ni wa haki, na wenye upendo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunapenda kuzungumzia enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote mzima pamoja na mtu yeyote aliye tayari kusikiliza. Hata hivyo, tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba sisi binafsi tumechukua msimamo kuhusiana na suala hilo? Tunaonyesha jinsi gani kwamba tumekubali Yehova awe Mtawala wetu Mkuu? Kwa kuendelea kuwa watimilifu.
10. Shetani ametoa shtaka gani kuhusu utimilifu wa wanadamu, na ungependa kujibu shtaka hilo jinsi gani?
10 Hebu ona jinsi utimilifu wako unavyohusika. Shetani amedai kwamba hakuna mwanadamu atakayeunga mkono enzi kuu ya Mungu, kwamba hakuna yeyote atakayemtumikia Yehova akichochewa na upendo usio na ubinafsi. Ibilisi alimwambia Yehova hivi mbele ya kusanyiko kubwa la viumbe wa roho: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” (Ayu. 2:4) Ona kwamba Shetani hakudai hivyo kumhusu yule mwanamume mwadilifu Ayubu tu bali kuhusu wanadamu wote kwa jumla. Hivyo, Biblia inamwita Shetani “mshtaki wa ndugu zetu.” (Ufu. 12:10) Anamdhihaki Yehova akidai kwamba Wakristo—kutia ndani wewe—hawataendelea kuwa waaminifu. Shetani anadai kwamba unaweza kumsaliti Yehova ili uiokoe nafsi yako. Unahisi jinsi gani kuhusu mashtaka hayo yanayokuhusu? Je, hungefurahi kupata nafasi ya kumthibitisha Shetani kuwa mwongo? Kwa kuendelea kuwa mtimilifu, unaweza kumthibitisha kuwa mwongo.
11, 12. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba maamuzi tunayofanya kila siku yanahusiana na suala la utimilifu wetu? (b) Kwa nini ni pendeleo kuendelea kuwa mtimilifu?
11 Hivyo, kwa sababu ya suala la utimilifu wako, mwenendo na maamuzi unayofanya kila siku ni ya maana sana. Fikiria tena zile hali tatu zilizotajwa mwanzoni. Yule mvulana, mume, na mke wangefanya nini ili kuendelea kuwa watimilifu? Yule mvulana anayedhihakiwa na wanafunzi wenzake anashawishiwa sana kulipiza kisasi, lakini anakumbuka shauri hili: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Rom. 12:19) Hivyo, anaamua kuondoka. Yule mume anayetumia Intaneti angeweza kutazama picha zinazosisimua tamaa ya ngono, lakini anakumbuka kanuni iliyo katika maneno haya ya Ayubu: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Vivyo hivyo, mwanamume huyo anaepuka kutazama picha hizo zinazochukiza, anaziepuka kama sumu. Yule mwanamke anayezungumza na akina dada wengine wakati ambapo mazungumzo yanageuka na kuwa porojo yenye kuumiza anajizuia asichangie porojo hizo, akikumbuka agizo hili: “Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake.” (Rom. 15:2) Ikiwa angechangia porojo hizo, hangesema mambo yenye kujenga. Angekuwa akimharibia sifa dada yake Mkristo; naye hangempendeza Baba yake wa mbinguni. Kwa hiyo, mwanamke huyo anazuia ulimi wake na kubadili mazungumzo.
12 Katika hali zote hizo, kupitia uamuzi wanaofanya, ni kana kwamba Wakristo hao wanasema: ‘Yehova ni Mtawala wangu. Nitajitahidi kufanya mambo yanayompendeza katika jambo hili.’ Unapofanya maamuzi ya kibinafsi, je, unaona mambo kwa njia hiyo? Ukifanya hivyo, basi utakuwa ukitii maneno haya yenye kutia moyo ya Methali 27:11: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Tuna pendeleo kubwa kama nini la kuufanya moyo wa Mungu ushangilie! Basi, je, hatupaswi kufanya yote tuwezayo ili kuendelea kuwa watimilifu?
2. Mungu Anatuhukumu kwa Msingi wa Utimilifu Wetu
13. Maneno ya Ayubu na ya Daudi yanaonyesha jinsi gani kwamba Yehova anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu?
13 Tunaona kwamba utimilifu unatuwezesha kuunga mkono enzi kuu ya Yehova. Hivyo, Mungu anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu wetu. Ayubu alielewa vizuri ukweli huo. (Soma Ayubu 31:6.) Ayubu alijua kwamba Mungu anawapima wanadamu wote katika “mizani sahihi,” akitumia kiwango Chake kikamilifu cha haki ili kuona ikiwa sisi ni watimilifu. Pia, Daudi alisema hivi: “Yehova mwenyewe atavihukumu vikundi vya watu. Nihukumu, Ee Yehova, kulingana na uadilifu wangu na kulingana na utimilifu wangu. . . . Na Mungu akiwa mwadilifu anapima moyo na figo.” (Zab. 7:8, 9) Tunajua kwamba Mungu anaweza kumchunguza mtu ndani kabisa, yaani, anaweza kuchunguza “moyo na figo” za mfano. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kile anachotafuta. Kama Daudi alivyosema, Yehova anatuhukumu kulingana na utimilifu wetu.
14. Kwa nini hatupaswi kufikiri kwamba hali yetu ya kutokamilika inatuzuia tusiendelee kuwa watimilifu?
14 Yehova Mungu anachunguza mabilioni ya mioyo ya wanadamu leo. (1 Nya. 28:9) Unafikiri ni mara ngapi ambapo anampata mtu ambaye anadumisha utimilifu wa Kikristo? Ni mara chache sana! Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba tuna makosa mengi sana hivi kwamba hatuwezi kudumisha utimilifu. Badala yake, kama Daudi na Ayubu, tuna sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova atatupata tukidumisha utimilifu, hata ingawa sisi si wakamilifu. Kumbuka kwamba kuwa wakamilifu hakumaanishi kwamba tutaendelea kuwa watimilifu. Ni wanadamu watatu tu wakamilifu ambao wameishi duniani, na wawili kati yao, Adamu na Hawa, walishindwa kuendelea kuwa watimilifu. Hata hivyo, mamilioni ya wanadamu wasio wakamilifu wamefaulu kuendelea kuwa watimilifu. Wewe pia unaweza kufaulu.
3. Utimilifu Ni Sifa ya Maana kwa Tumaini Letu
15. Daudi alionyesha jinsi gani kwamba utimilifu ni wa maana kwa tumaini lake la wakati ujao?
15 Kwa kuwa Yehova anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu wetu, utimilifu ni wa maana kwa tumaini letu la wakati ujao. Daudi alijua ukweli wa jambo hilo. (Soma Zaburi 41:12.) Daudi alithamini sana tumaini la kukubaliwa na Mungu milele. Kama Wakristo wa kweli leo, Daudi alitumaini kuishi milele na kuendelea kumkaribia Yehova Mungu huku akimtumikia. Daudi alijua kwamba alihitaji kuendelea kuwa mtimilifu ili aone tumaini hilo likitimia. Vivyo hivyo, Yehova anatutegemeza, anatufundisha, anatuongoza, na anatubariki tunapoendelea kuwa watimilifu.
16, 17. (a) Kwa nini umeazimia sikuzote kushikilia kabisa utimilifu wako? (b) Habari inayofuata itazungumzia maswali gani?
16 Ili tuwe wenye furaha tunahitaji kuwa na tumaini. Tumaini linaweza kutuletea shangwe tunayohitaji ili kuvumilia hali ngumu. Pia, tumaini linaweza kulinda fikira zetu. Kumbuka kwamba Biblia inafananisha tumaini na kofia ya chuma. (1 The. 5:8) Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa cha askari-jeshi aliye vitani, tumaini linalinda akili zetu ili zisipenywe na mawazo yasiyofaa ambayo Shetani anaendeleza kupitia ulimwengu huu wa kale unaopitilia mbali. Ni wazi kwamba bila tumaini, maisha hayana kusudi. Tunahitaji kujichunguza kwa unyoofu, na kuchanganua kwa makini hali ya utimilifu wetu na tumaini linalohusiana nalo. Usisahau kwamba unapoendelea kuwa mtimilifu, unaunga mkono enzi kuu ya Yehova na kulinda tumaini lako la wakati ujao lenye thamani. Ndiyo, shikilia kabisa utimilifu wako sikuzote!
17 Kwa kuwa utimilifu ni sifa ya maana sana, tunahitaji kufikiria maswali mengine. Tunajenga utimilifu jinsi gani? Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa watimilifu? Na mtu anaweza kufanya nini ikiwa alishindwa kuwa mtimilifu kwa muda fulani? Habari inayofuata itazungumzia maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Yesu alisema: “Lazima ninyi basi muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Inaelekea alielewa kwamba hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuwa kamili, au wakamilifu kwa kadiri fulani. Tunaweza kutimiza amri ya kuwapenda wengine kutoka moyoni, na hivyo kumpendeza Mungu. Hata hivyo, Yehova ni mkamilifu katika maana kamili. Neno “utimilifu” linapotumiwa kumhusu, linahusisha pia ukamilifu.—Zab. 18:30.
-
-
Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?Mnara wa Mlinzi—2008 | Desemba 15
-
-
Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?
“Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—AYU. 27:5.
1, 2. Tunahitaji kushiriki katika mradi gani wa ujenzi, na tutazungumzia maswali gani?
WAZIA unachunguza ramani za ujenzi za nyumba fulani. Unastaajabia jinsi nyumba hiyo itakavyokuwa yenye manufaa. Unachangamka unapofikiria faida ambazo wewe na familia yako mtapata mnapoishi katika nyumba hiyo. Hata hivyo, je, hukubali kwamba kuchunguza ramani hizo na kufikiri tu kuhusu nyumba hiyo ni kazi bure usipoijenga, usipoishi ndani yake, na kuitunza?
2 Vivyo hivyo, huenda tukaona utimilifu kuwa sifa ya maana inayoweza kutunufaisha sana na wale tunaowapenda. Lakini kuwa tu na maoni mazuri kuhusu utimilifu hakutatunufaisha sana ikiwa hatutajitahidi kujenga na kudumisha utimilifu wetu wa Kikristo. Katika ulimwengu wa leo, mara nyingi miradi ya ujenzi inagharimu pesa nyingi sana. (Luka 14:28, 29) Kwa njia hiyohiyo, wakati na jitihada nyingi zinahitajiwa ili kujenga utimilifu, lakini kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Basi, acheni tuzungumzie maswali matatu: Tunaweza kufanya nini ili tuwe watimilifu? Tunaweza kufanya nini ili tudumishe utimilifu wetu wa Kikristo? Mtu anaweza kufanya nini ikiwa hakuonyesha utimilifu wakati fulani?
Tunaweza Kufanya Nini ili Tuwe Watimilifu?
3, 4. (a) Yehova anatumia njia gani kutusaidia kujenga utimilifu? (b) Tunaweza kujenga utimilifu jinsi gani kama Yesu?
3 Katika habari iliyotangulia tuliona kwamba Yehova ametuonyesha heshima kwa kuturuhusu tujiamulie ikiwa tutakuwa watimilifu. Hata hivyo, Yehova hatuachi tu bila msaada. Anatufundisha jinsi ya kujenga sifa hiyo yenye thamani, naye anatupa kwa wingi roho yake takatifu ambayo inatusaidia kutumia mafundisho yake. (Luka 11:13) Zaidi ya hayo, anawalinda kiroho wale wanaojitahidi kutembea kwa utimilifu.—Met. 2:7.
4 Yehova ametumia njia gani kutufundisha kuwa watimilifu? Njia kuu zaidi aliyotumia ni kumtuma Mwana wake, Yesu, duniani. Yesu alitii kikamilifu. Alikuwa “mtiifu mpaka kifo.” (Flp. 2:8) Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni katika mambo yote, hata ilipokuwa vigumu sana kufanya hivyo. Alimwambia Yehova: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi ni mtiifu kama Yesu?’ Tukiendelea kuwa watiifu huku tukichochewa na nia nzuri, tutashikilia utimilifu wetu. Fikiria hali fulani maishani ambazo hasa zinahitaji utii.
5, 6. (a) Daudi alikazia jinsi gani umuhimu wa kuendelea kuwa mtimilifu hata wakati ambapo wanadamu wengine hawatuoni? (b) Wakristo leo wanakabili hali gani zinazojaribu utimilifu wao wanapokuwa peke yao?
5 Tunahitaji kumtii Yehova hata inapoonekana kwamba tuko peke yetu. Mtunga-zaburi Daudi aliona kwamba ni jambo la maana kuwa mtimilifu hata katika pindi ambazo alikuwa peke yake. (Soma Zaburi 101:2.) Akiwa mfalme, mara nyingi Daudi alikuwa pamoja na watu. Pindi nyingi, alikuwa kati ya mamia ya watu, hata maelfu ya watu. (Linganisha na Zaburi 26:12.) Lilikuwa jambo la maana kudumisha utimilifu katika pindi hizo, kwa kuwa mfalme alipaswa kuwawekea watu wake mfano mzuri. (Kum. 17:18, 19) Hata hivyo, Daudi alijifunza kwamba nyakati ambazo huenda alikuwa peke yake—‘ndani ya nyumba yake’—bado alihitaji kutembea kwa utimilifu. Namna gani sisi?
6 Katika Zaburi 101:3, tunapata maneno haya ya Daudi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.” Kuna hali nyingi leo zinazoweza kutufanya tuweke mbele ya macho yetu vitu visivyofaa, hasa tunapokuwa peke yetu. Wengi wamejaribiwa wanapotumia Intaneti. Ni rahisi kushawishiwa kutazama habari zisizofaa, au hata ponografia (picha au habari za ngono). Lakini je, kufanya hivyo ni kumtii Mungu aliyemwongoza Daudi kuandika maneno hayo? Ponografia inamdhuru mtu, kwa kuwa inachochea tamaa zisizofaa na za pupa, inachafua dhamiri, inavunja ndoa, na kumshushia heshima kila mtu anayehusika.—Met. 4:23; 2 Kor. 7:1; 1 The. 4:3-5.
7. Ni kanuni gani inayoweza kutusaidia kuendelea kuwa watimilifu tunapokuwa peke yetu?
7 Kwa kweli, hakuna mtumishi yeyote wa Yehova ambaye anakuwa peke yake wakati wowote ule. Baba yetu anatutazama kwa upendo. (Soma Zaburi 11:4.) Yehova anafurahi kama nini anapoona ukishinda kishawishi fulani! Kwa kufanya hivyo, unatii onyo la Yesu katika Mathayo 5:28. Azimia kutotazama picha zinazoweza kukushawishi kutenda mabaya. Usipoteze utimilifu wako wenye thamani kwa sababu ya tendo lenye kuaibisha la kutazama au kusoma ponografia!
8, 9. (a) Utimilifu wa Danieli na marafiki wake ulijaribiwa jinsi gani? (b) Vijana Wakristo leo wanamfurahisha jinsi gani Yehova na Wakristo wenzao?
8 Pia, tunaweza kuwa watimilifu kwa kumtii Yehova tunapokuwa na watu ambao si waamini. Mfikirie Danieli na marafiki wake watatu. Wakiwa vijana, walipelekwa utekwani Babiloni. Wakiwa huko, katikati ya watu ambao hawakuwa waamini na ambao hawakumjua Yehova hata kidogo, Waebrania hao wanne walishinikizwa wale vyakula vilivyokatazwa na Sheria ya Mungu. Wavulana hao wangetoa visingizio vingi ili wasitii sheria hiyo ya Mungu. Wazazi wao, makuhani, na wazee hawangeona mambo ambayo vijana hao wanne walikuwa wakifanya. Je, kuna mtu yeyote ambaye angejua? Ni Yehova tu ambaye angejua. Kwa hiyo, walisimama imara na kumtii hata ingawa walishinikizwa na walikabili hatari.—Dan. 1:3-9.
9 Ulimwenguni pote, vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova wanasimama imara pia, na wanashikilia kanuni za Mungu zinazowaongoza Wakristo na kupinga vishawishi vyenye kudhuru kutoka kwa vijana wenzao. Ninyi vijana mnapokataa kutumia dawa za kulevya, kutenda jeuri, kutumia usemi wa matusi, kufanya uasherati, na mambo mengine mabaya, mnamtii Yehova. Hivyo, mnaendelea kushikilia utimilifu wenu. Mnapata faida, nanyi mnamfurahisha Yehova na Wakristo wenzenu!—Zab. 110:3.
10. (a) Ni maoni gani yasiyofaa kuhusu uasherati ambayo yamefanya vijana fulani wasiendelee kuwa watimilifu? (b) Utimilifu unatuchochea kufanya nini kuhusiana na hatari ya uasherati?
10 Pia tunahitaji kuwa watiifu tunaposhughulika na watu wa jinsia tofauti. Tunajua kwamba Neno la Mungu linakataza uasherati. Hata hivyo, ni rahisi kuacha kuwa watiifu na kuanza kukubali mambo mengine yasiyofaa. Kwa mfano, vijana fulani wamejihusisha na ngono ya mdomo au ulawiti au zoea la kupigana punyeto wakifikiri kwamba mambo hayo si mabaya sana kwa sababu kwa maoni yao “hawafanyi ngono” kihalisi. Vijana hao wanasahau—au huenda wanapuuza—kwamba neno ambalo Biblia inatumia kwa ajili ya uasherati linatia ndani mazoea yote hayo, mazoea mabaya ambayo yanaweza kumfanya mtu atengwe na ushirika.a Na jambo baya hata zaidi ni kwamba wanapuuza utimilifu. Kwa kuwa tunajitahidi kuendelea kuwa watimilifu, hatutafuti visababu vya kutofuata sheria. Hatujaribu kukaribia sana kufanya dhambi eti kwa sababu hatutaadhibiwa. Hatufikiri tu kuhusu nidhamu ya kihukumu ambayo tunaweza kupata kwa kufanya dhambi. Badala yake, tunajitahidi kufanya mambo yatakayompendeza Yehova na kuepuka mambo ambayo yataumiza hisia zake. Badala ya kufikiria ni kwa kadiri gani tunaweza kukaribia kufanya dhambi bila kuadhibiwa, tunaepuka kabisa dhambi na ‘kuukimbia uasherati.’ (1 Kor. 6:18) Hivyo, tunaonyesha kwamba kwa kweli sisi ni watimilifu.
Tunaweza Kufanya Nini ili Tuendelee Kuwa Watimilifu?
11. Kwa nini kila tendo la utii ni la maana? Toa mfano.
11 Tunajenga utimilifu kwa kutii, hivyo, tunaendelea kuwa watimilifu kwa kuendelea kutii. Huenda tukaona tendo moja la utii kuwa jambo dogo sana ambalo halina maana sana. Hata hivyo, matendo hayo ya utii yanatusaidia tuwe watimilifu siku baada ya siku. Kwa mfano: Huenda tofali likaonekana kuwa dogo sana, lakini tukiunganisha matofali mengi pamoja, tunaweza kujenga nyumba yenye kupendeza. Kwa hiyo, tukiendelea kutii siku baada ya siku, tunaendelea kuwa watimilifu.—Luka 16:10.
12. Daudi aliweka mfano gani wa kuendelea kuwa mtimilifu alipoteswa na kutendewa isivyo haki?
12 Utimilifu wetu unaonekana hasa tunapovumilia matatizo, mateso, au ukosefu wa haki. Fikiria mfano wa Biblia wa Daudi. Alipokuwa kijana, alivumilia mateso kutoka kwa mfalme aliyepaswa kuwakilisha mamlaka ya Yehova. Hata hivyo, Mfalme Sauli alikuwa amepoteza kibali cha Yehova na alimwonea wivu sana Daudi, aliyekubaliwa na Mungu. Hata hivyo, Sauli aliendelea kutawala kwa muda na alitumia jeshi la Israeli kumfukuza na kumfadhaisha Daudi. Yehova aliruhusu ukosefu huo wa haki uendelee kwa miaka fulani. Je, Daudi alimkasirikia Mungu? Je, aliona kwamba hakuna haja ya kuvumilia? Hapana. Aliendelea kuheshimu sana cheo cha Sauli akiwa mtiwa-mafuta wa Mungu na akakataa kulipiza kisasi juu ya Sauli alipopata nafasi ya kufanya hivyo.—1 Sam. 24:2-7.
13. Tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuwa watimilifu hata tunapoumizwa au kukasirishwa?
13 Daudi alituwekea mfano mzuri kama nini! Sisi ni sehemu ya kutaniko la ulimwenguni pote la wanadamu wasio wakamilifu, na yeyote kati ya wanadamu hao anaweza kutukosea au hata kutokuwa mwaminifu. Bila shaka, tuna pendeleo la kuishi wakati ambapo watu wa Yehova kwa ujumla hawawezi kupotoshwa. (Isa. 54:17) Hata hivyo, tutafanya nini mtu fulani anapotuvunja moyo au kuumiza hisia zetu? Tukimfungia kinyongo mwabudu mwenzetu, tutakuwa tukihatarisha utimilifu wetu kwa Mungu. Mwenendo wa wengine haupaswi kamwe kuwa kisingizio cha kumkasirikia Mungu au kuacha kuwa waaminifu. (Zab. 119:165) Kuvumilia hata wakati wa majaribu kutatusaidia kuendelea kuwa watimilifu.
14. Watu watimilifu wanafanya nini kunapokuwa na marekebisho katika utaratibu wa kufanya mambo na katika mafundisho?
14 Pia, tunaweza kuendelea kuwa watimilifu kwa kuepuka kutafuta-tafuta makosa ya wengine au kuwachambua-chambua. Bila shaka, hilo linamaanisha tuwe washikamanifu kwa Yehova. Anawabariki watu wake sasa kuliko wakati mwingine wowote. Ibada safi haijapata kamwe kuinuliwa duniani kama ilivyo sasa. (Isa. 2:2-4) Marekebisho yanapofanywa katika uelewaji wa maandiko ya Biblia au katika utaratibu wa kufanya mambo, tunapaswa kuyakubali. Tunafurahi kuona uthibitisho wa kwamba nuru ya kiroho inaongezeka. (Met. 4:18) Tukiona ni vigumu kuelewa badiliko fulani, tunamwomba Yehova atusaidie kuelewa jambo hilo. Na wakati huohuo tunaendelea kuwa watiifu, ndiyo, tunaendelea kuwa watimilifu.
Namna Gani Mtu Akiacha Kuwa Mtimilifu?
15. Ni nani tu anayeweza kukunyang’anya utimilifu wako?
15 Hilo ni swali zito, sivyo? Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, utimilifu ni sifa ya maana sana. Bila utimilifu, hatuwezi kuwa na uhusiano na Yehova wala tumaini halisi. Kumbuka: Ni mtu mmoja tu katika ulimwengu wote anayeweza kukunyang’anya utimilifu wako. Mtu huyo si mwingine ila wewe. Ayubu alielewa kabisa jambo hilo la kweli. Alisema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Ukiwa na azimio hilohilo na ukiendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, hutapoteza kamwe utimilifu wako.—Yak. 4:8.
16, 17. (a) Mtu akitumbukia katika dhambi nzito, hapaswi kufanya nini? (b) Anapaswa kufanya nini?
16 Hata hivyo, wengine wanashindwa kuendelea kuwa watimilifu. Kama ilivyokuwa wakati wa mitume, leo wengine wanazoea kutenda dhambi nzito. Ikiwa uko katika hali hiyo, je, inamaanisha kwamba huna tumaini lolote? Si lazima iwe hivyo. Unaweza kufanya nini? Acheni kwanza tuzungumzie mambo ambayo hupaswi kufanya. Mwelekeo wa mwanadamu ni kuficha kosa ili wazazi, Wakristo wenzake, au wazee wasijue. Hata hivyo, Biblia inatukumbusha hivi: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Met. 28:13) Wale wanaojaribu kuficha dhambi wanafanya kosa hatari sana, kwa maana Mungu hawezi kufichwa lolote. (Soma Waebrania 4:13.) Wengine hata wanajaribu kuwa na nyuso mbili, wanajifanya wanamtumikia Yehova huku wakiendelea kutenda dhambi. Hayo si maisha ya utimilifu—ni kinyume kabisa cha utimilifu. Yehova hapendezwi na matendo ya ibada yanayofanywa na watu wanaoficha dhambi nzito. Badala yake, unafiki huo unamkasirisha.—Met. 21:27; Isa. 1:11-16.
17 Ikiwa Mkristo amefanya dhambi nzito, anajua wazi hatua ya kuchukua. Anapaswa kutafuta msaada kutoka kwa wazee Wakristo. Yehova amefanya mpango wa kuwashughulikia watu wenye ugonjwa hatari wa kiroho. (Soma Yakobo 5:14.) Usikose kutafuta matibabu ya kiroho eti kwa sababu unaogopa kutiwa nidhamu au kurekebishwa. Je, mtu mwenye hekima ataepuka kutibiwa ugonjwa unaoweza kusababisha kifo eti kwa sababu anaogopa maumivu ya muda ya kudungwa sindano au kufanyiwa upasuaji?—Ebr. 12:11.
18, 19. (a) Mfano wa Daudi unaonyesha jinsi gani kwamba mtu anaweza kuwa mtimilifu tena? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusiana na utimilifu wako?
18 Je, kuna tumaini la kupona kabisa? Je, mtu aliyepoteza utimilifu anaweza kuwa mtimilifu tena? Fikiria tena mfano wa Daudi. Alitumbukia katika dhambi nzito. Alimtazama mke wa mtu mwingine kwa tamaa, akafanya uzinzi naye, na kufanya mipango ili mume wake asiye na hatia auawe. Ni wazi kwamba Daudi hakuwa mtimilifu wakati huo, sivyo? Hata hivyo, je, inamaanisha kwamba hakuwa na tumaini lolote? Daudi alihitaji na alipokea nidhamu kali. Hata hivyo, Yehova alimwonyesha rehema kwa kuwa alitubu kikweli. Daudi alijifunza kutokana na nidhamu hiyo na akawa mtimilifu tena kwa kumtii Mungu na kuendelea kuwa mtiifu. Maisha ya Daudi yalithibitisha maneno haya ya Methali 24:16: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” Matokeo yalikuwa nini? Fikiria yale ambayo Yehova alimwambia Sulemani kumhusu Daudi baada ya kifo cha Daudi. (Soma 1 Wafalme 9:4.) Mungu alimkumbuka Daudi kuwa mtu mtimilifu. Ndiyo, Yehova anaweza kusafisha madoa ya watenda-dhambi wanaotubu, hata dhambi zao nzito.—Isa. 1:18.
19 Ndiyo, utakuwa mtimilifu ukitii kwa upendo. Endelea kuwa mvumilivu na mshikamanifu, na ukitenda dhambi nzito, onyesha toba ya kweli. Utimilifu ni hazina iliyoje! Acheni kila mmoja wetu aazimie hivi kama Daudi: “Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu.”—Zab. 26:11.
[Maelezo ya Chini]
-