-
Réunion2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka huo, Cléo aliyekuwa askari wa akiba, aliitwa jeshini. Anasema, “Ingawa nilikuwa na ujuzi kidogo tu wa Biblia, niliwaandikia wakuu wa jeshi na kuwaeleza msimamo wangu wa kutojiunga na jeshi. Hawakunijibu, hivyo nikaenda kuchunguza jambo hilo katika kituo cha jeshi cha Saint-Denis, upande ule mwingine wa kisiwa. Ofisa mmoja aliniambia niende nyumbani lakini nijitayarishe kufungwa gerezani. Kwa hiyo, nilisali mara nyingi na kujifunza kwa bidii. Muda si mrefu, niliitwa kwenye kituo cha jeshi. Nilipofika huko, nilimwomba ndugu niliyeandamana naye katika gari aningoje kwa muda wa saa moja. Nilimwambia, ‘Usiponiona baada ya muda huo, yaelekea sitarudi. Nisiporudi tafadhali uza gari langu kisha umpe mke wangu pesa utakazopata.’
“Nilipoingia ndani, nilikuta maofisa wakibishana kuhusu hatua ambayo wangenichukulia. Baada ya dakika 45 hivi, askari mmoja alinikaribia.
“Alisema, ‘Ondoka mbele yangu! Nenda nyumbani.’
“Baada ya kutembea hatua chache tu, aliniita na kwa upole akasema: ‘Ninyi watu mnanivutia. Nilisikia kuhusu Mashahidi wa Yehova huko Ufaransa, lakini wewe ndiye Shahidi wa kwanza kuona.’
-
-
Réunion2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka wa 1967 niliitwa jeshini. Nilieleza kwamba mimi ni Mkristo na kwa sababu hiyo siwezi kujiunga na jeshi. Kwa kuwa nilikuwa mtu wa kwanza huko Réunion kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri, wenye mamlaka hawakuelewa msimamo wangu wala hawakuukubali. Hata ofisa mmoja alinipiga mbele ya askari wapya 400, kisha akanipeleka ofisini mwake huku nikitembea kwa kuchechemea. Aliweka mavazi ya kijeshi juu ya dawati lake na kuniambia niyavae, la sivyo, angenipiga tena. Alikuwa mwenye urefu wa karibu mita 1.8, mkubwa sana kunishinda. Hata hivyo, nilipiga moyo konde na kusema, “Ukinipiga tena, nitawasilisha malalamiko rasmi, kwani kuna uhuru wa ibada chini ya utawala wa Ufaransa.” Alifoka kwa hasira na kutaka kunipiga lakini akajizuia. Kisha, akanipeleka kwa ofisa mkuu aliyeniambia kwamba ningehukumiwa kifungo cha miaka mitatu na kazi ngumu nchini Ufaransa.
Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu, lakini sikupelekwa Ufaransa wala sikupewa kazi ngumu. Baada ya kunihukumu, hakimu alinialika ofisini mwake. Alinishika mkono huku akitabasamu na kuniambia kwamba ananisikitikia lakini hakuwa na budi kufanya uamuzi kupatana na sheria. Msaidizi wa mkurugenzi wa gereza alikuwa mwenye urafiki pia, naye akapanga nifanye kazi katika chumba cha mahakama. Hata aliandamana nami sebuleni ili kuwasalimu wazazi wangu na ndugu fulani wa kutaniko letu.
Mwanzoni nilikaa pamoja na wafungwa wengine 20 hadi 30 katika chumba kimoja, lakini baadaye nikawekwa katika chumba cha watu 2. Hilo lilinipa uhuru zaidi. Niliomba taa ya umeme na jambo la kushangaza ni kwamba nilipewa moja. Kwa kawaida wafungwa hukatazwa kuwa na vifaa vya umeme kwa kuwa wanaweza kujaribu kujiua kwa kutumia umeme. Kwa sababu nilikuwa na taa hiyo, niliweza kujifunza Biblia na pia kukamilisha masomo ya hesabu kwa njia ya posta. Nilipoachiliwa mwaka wa 1970, hakimu mwenye fadhili alinisaidia kupata kazi.
-