-
Yehova Huwabariki na Kuwalinda Wale WanaomtiiMnara wa Mlinzi—2002 | Oktoba 1
-
-
Yehova Huwabariki na Kuwalinda Wale Wanaomtii
“Bali kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.”—MITHALI 1:33.
1, 2. Kwa nini ni muhimu kumtii Mungu? Toa mfano.
VIFARANGA wa rangi ya manjano wenye manyoya laini wanadonoa chakula katika nyasi fupi bila kujua kwamba kuna mwewe anayezunguka-zunguka juu. Kwa ghafula kuku atoa sauti ya juu yenye hofu na kukunjua mabawa yake. Vifaranga wanamkimbilia, na baada ya muda mfupi wote wako salama chini ya mabawa yake. Mwewe ashindwa kushambulia.a Tunajifunza nini? Kwamba utii huokoa uhai!
2 Somo hilo ni muhimu hasa kwa Wakristo leo kwa kuwa Shetani anafanya kila awezalo ili awanase watu wa Mungu. (Ufunuo 12:9, 12, 17) Lengo lake ni kuharibu uhusiano wetu na Yehova ili tupoteze kibali chake na taraja la uhai udumuo milele. (1 Petro 5:8) Hata hivyo, tukimkaribia Mungu na kuitikia upesi mwelekezo tunaopokea kupitia Neno lake na tengenezo lake, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anatulinda na anatujali. “Kwa manyoya yake atakufunika, chini ya mbawa zake utapata kimbilio,” akaandika mtunga-zaburi.—Zaburi 91:4.
Taifa Lisilotii Lawa Windo
3. Kwa sababu ya kutomtii Mungu mara nyingi, Waisraeli walipatwa na nini?
3 Taifa la Israeli lilipomtii Yehova, aliendelea kuwatunza kwa uangalifu. Hata hivyo, mara nyingi watu hao walimwacha Mfanyi wao na kuabudu miungu ya miti na mawe—“vitu vya ubatili, visivyoweza kusaidia wala kuokoa.” (1 Samweli 12:21, 22) Baada ya uasi huo uliodumu kwa karne nyingi, taifa zima lilijihusisha sana na uasi-imani hivi kwamba halingeweza kurekebishwa. Kwa hiyo, Yesu aliomboleza hivi: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na mpigaji kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja, kama vile kuku hukusanya vifaranga vyake pamoja chini ya mabawa yake! Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mathayo 23:37, 38.
4. Ni tukio gani lililoonyesha kwamba Yehova alikuwa ameliacha Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.?
4 Tukio lenye kuhuzunisha la mwaka wa 70 W.K. lilionyesha wazi kwamba Yehova amewaacha Waisraeli waasi. Mwaka huo majeshi ya Roma, yakiwa na bendera zilizorembwa kwa picha ya tai, yalishambulia Yerusalemu na kusababisha maafa makubwa. Wakati huo jiji lilikuwa na watu wengi waliokuwa wakisherehekea Sikukuu ya Kupitwa. Hawakupata kibali cha Mungu ingawa walitoa dhabihu nyingi. Hilo liliwakumbusha kwa njia ya kuhuzunisha maneno ambayo Samweli alimwambia Mfalme Sauli mwasi: “Je, BWANA huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu sawasawa na kuitii sauti ya BWANA? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu.”—1 Samweli 15:22.
5. Yehova anataka utii wa aina gani, na tunajuaje kwamba tunaweza kuonyesha utii huo?
5 Ingawa Yehova anakazia utii, yeye anajua udhaifu wetu tukiwa wanadamu wasio wakamilifu. (Zaburi 130:3, 4) Yeye anataka unyofu wa moyo, na utii unaotegemea imani, upendo, na hofu inayofaa ya kutompendeza. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13; Mithali 16:6; Isaya 43:10; Mika 6:8; Waroma 6:17) ‘Wingu kubwa la Mashahidi walioishi kabla ya Ukristo,’ walidhihirisha kwamba tunaweza kuonyesha utii huo kwa sababu walishika uaminifu-maadili chini ya majaribu makali, hata kifo. (Waebrania 11:36, 37; 12:1) Mashahidi hao waliufurahisha moyo wa Yehova kama nini! (Mithali 27:11) Hata hivyo, wengine walikuwa waaminifu hapo mwanzoni lakini hawakuendelea kuonyesha utii maishani mwao. Mfano mmoja ni Mfalme Yoashi wa Yuda la kale.
Mfalme Aliyeangamia kwa Sababu ya Mashirika Mabaya
6, 7. Yoashi alikuwa mfalme wa aina gani Yehoyada alipokuwa hai?
6 Mfalme Yoashi aliponea chupuchupu kuuawa akiwa mtoto mchanga. Yoashi alipokuwa na umri wa miaka saba, Kuhani wa Cheo cha Juu Yehoyada alimtoa kwa ujasiri mahali alipokuwa amejificha na kumfanya mfalme. Kwa sababu Yehoyada mwenye kumhofu Mungu alikuwa kama baba na mshauri kwa Yoashi, mfalme huyo mchanga “aliendelea kufanya yaliyo mema machoni pa Yehova siku zote za Yehoyada kuhani.”—2 Mambo ya Nyakati 22:10–23:1, 11; 24:1, 2.
7 Matendo mema ya Yoashi yalitia ndani kurekebisha hekalu la Yehova—tendo ambalo lilikuwa “karibu sana na moyo wa Yoashi.” Alimkumbusha Kuhani wa Cheo cha Juu Yehoyada umuhimu wa kukusanya kodi ya hekalu kutoka Yuda na Yerusalemu, kama ‘alivyoagiza Musa,’ ili kupata pesa za urekebishaji. Yaonekana, Yehoyada alifaulu kumtia moyo mfalme huyo mchanga ajifunze na kutii Sheria ya Mungu. Matokeo yakawa kwamba kazi ya hekalu na vyombo vya hekalu vilikamilishwa upesi.—2 Mambo ya Nyakati 24:4, 6, 13, 14, NW; Kumbukumbu la Torati 17:18.
8. (a) Ni nini hasa kilichomfanya Yoashi aangamie kiroho? (b) Kwa sababu ya kutotii, mfalme huyo alifanya nini hatimaye?
8 Kwa kusikitisha, Yoashi hakuendelea kumtii Yehova. Kwa nini? Neno la Mungu linatuambia: “Baada ya kufa kwake Yehoyada, wakuu wa Yuda wakamwendea mfalme, wakamsujudia. Naye mfalme akawasikiliza maneno yao. Wakaiacha nyumba ya BWANA, Mungu wa baba zao; wakatumikia maashera na sanamu; ghadhabu ikawajia Yuda na Yerusalemu kwa sababu ya hiyo hatia yao.” Uvutano usiofaa wa wakuu wa Yuda ulifanya mfalme asiwasikilize manabii wa Mungu, ambao mmoja wao alikuwa Zekaria mwana wa Yehoyada, ambaye kwa ujasiri alimkaripia Yoashi na watu wengine kwa sababu ya kutotii. Badala ya kutubu, Yoashi aliamuru Zekaria apigwe mawe na kuuawa. Yoashi akawa mtu mkatili na asiyetii kwa sababu hakujiepusha na mashirika mabaya.—2 Mambo ya Nyakati 24:17-22; 1 Wakorintho 15:33.
9. Mambo yaliyompata Yoashi na wakuu wenzake yanakaziaje upumbavu wa kutotii?
9 Ni nini kilichompata Yoashi na wakuu wenzake waovu walipomwacha Yehova? Jeshi la Washami—“watu haba”—walivamia Yuda na ‘kuwaangamiza wakuu wa watu wote.’ Wavamizi hao walimlazimisha mfalme asalimishe mali yake na vilevile dhahabu na fedha ya mahali patakatifu. Ijapokuwa Yoashi aliokoka, aliachwa akiwa dhaifu na mgonjwa. Muda mfupi baada ya hapo, baadhi ya watumishi wake walikula njama na kumwua. (2 Mambo ya Nyakati 24:23-25; 2 Wafalme 12:17, 18) Jinsi maneno ya Yehova kwa Waisraeli yalivyo kweli: “Usipotaka kuisikiza sauti ya BWANA, Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake . . . ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata”!—Kumbukumbu la Torati 28:15.
Mwandishi Aliyeokoka kwa Sababu ya Kutii
10, 11. (a) Kwa nini inafaa tutafakari shauri ambalo Yehova alimpa Baruku? (b) Yehova alimpa Baruku shauri gani?
10 Je, nyakati nyingine unahisi umevunjika moyo kwa sababu watu wengi unaowapata kwenye huduma ya Kikristo hawapendezwi na habari njema? Je, nyakati nyingine unahisi wivu kidogo kuelekea matajiri na maisha yao ya anasa? Ikiwa ndivyo, kumbuka Baruku, mwandishi wa Yeremia, na shauri la upendo alilopewa na Yehova.
11 Baruku alikuwa akiandika ujumbe wa kiunabii, wakati Yehova alipomwelekezea fikira. Kwa nini? Kwa sababu Baruku alianza kusikitikia hali yake na kutamani hali bora kuliko pendeleo lake la pekee la kumtumikia Mungu. Yehova alipoona mtazamo wa Baruku umebadilika, alimshauri waziwazi lakini kwa fadhili, akimwambia: “Je! unajitafutia mambo makuu? Usiyatafute; kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili, . . . lakini roho yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.”—Yeremia 36:4; 45:5.
12. Kwa nini tuepuke kujitafutia “mambo makuu” katika mfumo wa sasa?
12 Kwa kufikiria maneno ya Yehova kwa Baruku, je, unaweza kuona jinsi alivyomjali sana mtu huyo mzuri, ambaye alimtumikia kwa uaminifu na ujasiri pamoja na Yeremia? Vivyo hivyo leo, Yehova anawahangaikia sana wale wanaoshawishiwa kutafuta zile wanazofikiri ni hali bora za maisha katika mfumo huu wa mambo. Inafurahisha kwamba, kama vile Baruku, wengi wamekubali kurekebishwa kwa upendo na ndugu wakomavu kiroho. (Luka 15:4-7) Naam, sisi sote na tutambue kwamba wale wanaojitafutia “mambo makuu” katika mfumo huu, hawana tumaini la wakati ujao. Watu hao hukosa furaha ya kweli, na zaidi ya hilo, hivi karibuni watapita pamoja na ulimwengu huu na tamaa zake zote za kichoyo.—Mathayo 6:19, 20; 1 Yohana 2:15-17.
13. Simulizi kuhusu Baruku linatufunza nini kuhusu unyenyekevu?
13 Simulizi kuhusu Baruku pia linatufundisha somo zuri la unyenyekevu. Ona kwamba Yehova hakumshauri Baruku moja kwa moja bali alizungumza naye kupitia Yeremia, ambaye labda Baruku alifahamu kasoro zake. (Yeremia 45:1, 2) Hata hivyo, Baruku hakuonyesha kiburi; alitambua kwamba shauri hilo limetoka kwa Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 26:3, 4, 16; Mithali 18:12; 19:20) Kwa hiyo ‘tukichukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya kuijua,’ na tupokee shauri linalohitajika kutoka kwa Neno la Mungu, na tumwige Baruku aliyeonyesha ukomavu, ufahamu wa kiroho, na unyenyekevu.—Wagalatia 6:1.
14. Kwa nini inafaa tuwatii wale wanaoongoza miongoni mwetu?
14 Tunapoonyesha unyenyekevu, tunarahisisha kazi ya wale wanaotoa shauri. Andiko la Waebrania 13:17 husema: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea, kwa maana wao wanafuliza kulinda juu ya nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wapate kufanya hili kwa shangwe na si kwa kutweta, kwa maana hili lingekuwa lenye hasara kwenu.” Mara nyingi wazee husali kwa Yehova kutoka moyoni, wakimwomba awape ujasiri, hekima, na busara inayohitajiwa ili kutimiza daraka lao gumu la uchungaji. Na ‘tuwatambue watu wa namna hiyo.’—1 Wakorintho 16:18.
15. (a) Yeremia alionyeshaje kwamba alimwamini Baruku? (b) Baruku alithawabishwaje kwa sababu ya kutii kwa unyenyekevu?
15 Ni wazi kwamba Baruku alirekebisha fikira zake kwa sababu baada ya hapo Yeremia alimpa mgawo mgumu sana—wa kwenda hekaluni na kusoma kwa sauti ujumbe wa hukumu ambao yeye mwenyewe aliambiwa na Yeremia auandike. Je, Baruku alitii? Naam, ‘alifanya sawasawa na hayo yote, ambayo Yeremia nabii, alimwagiza.’ Hata aliwasomea ujumbe huohuo wakuu wa Yerusalemu, jambo ambalo lilihitaji ujasiri mkubwa. (Yeremia 36:1-6, 8, 14, 15) Jiji lilipoharibiwa miaka 18 hivi baadaye, unaweza kuwazia jinsi Baruku alivyoshukuru kwa kuokolewa kwa sababu alitii onyo la Yehova, akaacha kujitafutia “mambo makuu”!—Yeremia 39:1, 2, 11, 12; 43:6.
Waliotii Waliokoka Wakati wa Mazingiwa
16. Yehova aliwaonyeshaje huruma Wayahudi waliokuwa Yerusalemu wakati wa mazingiwa yaliyofanywa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K.?
16 Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., Mungu alionyesha huruma yake tena kwa waliotii. Mazingiwa yalipopamba moto, Yehova aliwaambia hivi Wayahudi: “Tazama naweka mbele yenu njia ya uzima, na njia ya mauti. Yeye atakayekaa katika mji huu atakufa kwa upanga, na kwa njaa, na kwa tauni; bali yeye atakayetoka, na kujitia pamoja na Wakaldayo wanaowahusuru, yeye ataishi, na maisha yake yatakuwa nyara kwake.” (Yeremia 21:8, 9) Ingawa wakazi wa Yerusalemu walistahili kuangamizwa, Yehova aliwaonyesha huruma wale waliomtii, hata wakati huo wa dharura.b
17. (a) Utii wa Yeremia ulijaribiwa katika njia gani mbili Yehova alipomwagiza awaambie Wayahudi waliozingirwa ‘wawakimbilie Wakaldayo’? (b) Tunaweza kunufaikaje na mfano wa Yeremia wa kutii kwa ujasiri?
17 Bila shaka, kuwaambia Wayahudi wasalimu amri kulijaribu utii wa Yeremia pia. Sababu moja ni kwamba alikuwa na bidii kwa ajili ya jina la Mungu. Hakutaka jina hilo lishutumiwe na maadui ambao wangedai wamepata ushindi kutoka kwa sanamu zisizo na uhai. (Yeremia 50:2, 11; Maombolezo 2:16) Isitoshe, Yeremia alijua kwamba, kwa kuwaambia watu wasalimu amri, angehatarisha sana maisha yake, kwa kuwa wengi wangeelewa maneno yake kimakosa kuwa uhaini. Hata hivyo, hakujikunyata kwa woga, bali alitii na kutangaza ujumbe wa Yehova. (Yeremia 38:4, 17, 18) Kama vile Yeremia, sisi pia tunatangaza ujumbe usiopendwa na wengi. Yesu alidharauliwa kwa kutangaza ujumbe huohuo. (Isaya 53:3; Mathayo 24:9) Kwa hiyo ‘tusiwaogope wanadamu,’ bali kama Yeremia tumtii Yehova kwa ujasiri, na kumtumaini kabisa.—Mithali 29:25.
Utii Wakati wa Shambulio la Gogu
18. Watumishi wa Yehova watakabili majaribu gani ya utii wakati ujao?
18 Hivi karibuni, mfumo wote mwovu wa Shetani utaharibiwa katika “dhiki kubwa” ambayo haijawahi kutokea. (Mathayo 24:21) Imani na utii wa watu wa Mungu utajaribiwa sana kabla na pia wakati wa dhiki kubwa. Kwa mfano, Biblia hutuambia kwamba Shetani akiwa “Gogu wa nchi ya Magogu,” atafanya shambulio la kufa na kupona dhidi ya watumishi wa Yehova, akitumia majeshi yanayotajwa kuwa “kusanyiko kubwa na jeshi kuu . . . kama wingu kuifunika nchi.” (Ezekieli 38:2, 14-16) Watu wa Mungu wasio na silaha na ambao ni wachache sana kwa kulinganishwa na maadui wao, watatafuta kimbilio katika “mbawa” za Yehova ambazo hukunjuliwa ili kuwalinda watiifu.
19, 20. (a) Kwa nini utii ulikuwa muhimu sana kwa Waisraeli walipokuwa kwenye Bahari Nyekundu? (b) Tunaweza kunufaikaje leo kwa kufikiria kwa sala mambo yaliyotukia kwenye Bahari Nyekundu?
19 Hali hii inatukumbusha wakati Waisraeli walipotoka Misri. Baada ya kupiga Misri kwa mapigo kumi yaliyosababisha uharibifu mkubwa, Yehova aliwaongoza watu wake kuelekea Bahari Nyekundu, mahali ambapo wangeweza kushambuliwa kwa urahisi, badala ya kutumia njia fupi zaidi kuelekea Bara Lililoahidiwa. Kwa kufikiria mambo kwa njia ya kijeshi, ilikuwa hatari kufanya hivyo. Ikiwa ungekuwepo wakati huo, je, ungelitii neno la Yehova kupitia Musa na kutembea kuelekea Bahari Nyekundu ukiwa na uhakika kamili, ukijua kwamba Bara Lililoahidiwa lilikuwa upande tofauti?—Kutoka 14:1-4.
20 Tunapoendelea kusoma Kutoka sura ya 14, tunaona jinsi Yehova alivyowakomboa watu wake kwa kutumia nguvu zake nyingi. Kwa kweli tunaposoma na kutafakari masimulizi hayo tunaweza kuimarisha imani yetu! (2 Petro 2:9) Kisha imani yenye nguvu hutuimarisha tumtii Yehova, hata wakati matakwa yake yanapoonekana kuwa kinyume cha maoni ya wanadamu. (Mithali 3:5, 6) Kwa hiyo jiulize, ‘Je, ninajitahidi kuimarisha imani yangu kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kusali, na kutafakari, na vilevile kushirikiana na watu wa Mungu kwa ukawaida?’—Waebrania 10:24, 25; 12:1-3.
Utii Hutupatia Tumaini
21. Wale wanaomtii Yehova, watapokea baraka gani sasa na wakati ujao?
21 Wale wanaomtii Yehova maishani mwao hata sasa wanaona utimizo wa andiko la Mithali 1:33, linalosema: “Bali kila anisikilizaye [kwa kutii] atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.” Maneno hayo yanayotoa faraja yatatimia kwa njia ya kustaajabisha kama nini katika siku ya Yehova ya kisasi inayokuja! Kwa kweli, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mambo haya yaanzapo kutukia, jisimamisheni wenyewe wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa sababu ukombozi wenu unakaribia.” (Luka 21:28) Bila shaka, wale tu wanaomtii Mungu ndio watakaokuwa na uhakika wanapotii maneno hayo.—Mathayo 7:21.
22. (a) Kwa nini watu wa Yehova wana msingi wa kuwa na uhakika? (b) Ni mambo gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?
22 Sababu nyingine inayofanya tuwe na uhakika ni kwamba “Bwana MUNGU hatafanya neno lolote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.” (Amosi 3:7) Leo, Yehova hana nabii anayeongozwa na roho yake kama ilivyokuwa nyakati za kale; badala yake, ameipa jamii ya mtumwa mwaminifu kazi ya kuandaa chakula cha kiroho kwa wakati wake kwa watu wa nyumbani mwake. (Mathayo 24:45-47) Kwa hiyo, ni muhimu kama nini kwamba tumtii “mtumwa” huyo! Kama makala ifuatayo itakavyoonyesha, utii huo huonyesha pia mtazamo wetu kuelekea Yesu, ambaye ndiye bwana wa “mtumwa” huyo. Yeye ndiye Ambaye “mataifa watamtii.”—Mwanzo 49:10.
[Maelezo ya Chini]
a Ingawa mara nyingi wanaonyeshwa kuwa waoga, “kuku watapigana hadi kifo kulinda vifaranga wao wasipatwe na madhara,” chasema kichapo kimoja cha shirika la kuwalinda wanyama.
b Andiko la Yeremia 38:19 linaonyesha kwamba Wayahudi kadhaa ‘waliwakimbilia’ Wakaldayo kwa hiyo hawakuuawa bali walipelekwa uhamishoni. Hatujui iwapo walisalimu amri kwa kutii maneno ya Yeremia. Hata hivyo, kuokoka kwao kulithibitisha maneno ya nabii huyo.
-
-
Sitawisha Utii Mwisho UnapokaribiaMnara wa Mlinzi—2002 | Oktoba 1
-
-
Sitawisha Utii Mwisho Unapokaribia
“Kwa [Shilo] kutii kwa watu kutakuwa.”—MWANZO 49:10, Zaire Swahili Bible.
1. (a) Mara nyingi kumtii Yehova kulimaanisha nini zamani? (b) Yakobo alitoa unabii gani kuhusu utii?
MARA nyingi kumtii Yehova kumemaanisha kutii wawakilishi wake. Wawakilishi hao wametia ndani malaika, wazee wa ukoo, waamuzi, makuhani, manabii, na wafalme. Kiti cha wafalme wa Israeli hata kiliitwa kiti cha enzi cha Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 29:23) Hata hivyo, inasikitisha kwamba wafalme wengi wa Israeli hawakumtii Mungu, na hivyo wakajiletea msiba pamoja na raia zao. Lakini Yehova hakuwaacha waaminifu wake pasipo tumaini; aliwafariji kwa kuwaahidi kwamba angetawaza Mfalme mnyofu, ambaye waadilifu watafurahia kumtii. (Isaya 9:6, 7) Mzee wa ukoo, Yakobo, aliyekuwa akikaribia kufa alitoa unabii huu kuhusu mfalme huyo wa baadaye, aliposema: “Fimbo haitaondoka katika Yuda, wala gongo la mutawala kati ya miguu yake hata Shilo anakuja; na kwake kutii kwa watu kutakuwa.”—Mwanzo 49:10, ZSB.
2. Neno “Shilo” linamaanisha nini, nao utawala wake ungetia ndani nani?
2 “Shilo” ni neno la Kiebrania linalomaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake” au “Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Ndiyo, Shilo angerithi haki kamili ya kuwa mfalme, kama inavyoonyeshwa na ishara ya fimbo, na pia mamlaka, kama inavyoonyeshwa na gongo la mtawala. Isitoshe, utawala wake wa kifalme utatia ndani “watu” wote, si wazao wa Yakobo peke yao. Jambo hilo linapatana na ahadi ambayo Yehova alimpa Abrahamu: “Uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:17, 18) Yehova alihakikisha kwamba “mbegu” huyo ametambulishwa mwaka wa 29 W.K. alipomtia mafuta Yesu wa Nazareti kwa roho takatifu.—Luka 3:21-23, 34; Wagalatia 3:16.
Ufalme wa Kwanza wa Yesu
3. Yesu alipokea ufalme gani alipopaa mbinguni?
3 Yesu alipopaa mbinguni, hakuanza kutawala wakazi wa dunia mara moja. (Zaburi 110:1) Hata hivyo, alipokea “ufalme” ambao raia zake walimtii. Mtume Paulo aliutambulisha ufalme huo alipoandika hivi: “[Mungu] alitukomboa kutoka katika mamlaka ya giza na kutuhamisha kuingia katika ufalme wa Mwana wa upendo wake.” (Wakolosai 1:13) Ukombozi huo ulianza Pentekoste 33 W.K., wakati roho takatifu ilipomwagwa juu ya wafuasi waaminifu wa Yesu.—Matendo 2:1-4; 1 Petro 2:9.
4. Wanafunzi wa Yesu wa mapema walionyesha utii kwa njia gani, naye Yesu aliwatambulishaje wakiwa kikundi?
4 Wakiwa “mabalozi walio badala ya Kristo,” kwa utii wanafunzi waliotiwa mafuta kwa roho walianza kukusanya wengine ambao wangekuwa ‘raia wenzao’ katika ufalme huo wa kiroho. (2 Wakorintho 5:20; Waefeso 2:19; Matendo 1:8) Kwa kuongezea, wanafunzi hao walipaswa kubaki wakiwa ‘wameunganishwa kwa kufaa katika akili ileile na fikira ileile’ ili wapate kibali cha Mfalme wao Yesu Kristo. (1 Wakorintho 1:10) Wakiwa kikundi, walifanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” au jamii ya msimamizi-nyumba.—Mathayo 24:45; Luka 12:42.
Wabarikiwa kwa Kutii “Msimamizi-Nyumba” wa Mungu
5. Yehova amewafundishaje watu wake tangu nyakati za kale?
5 Yehova amekuwa akiwaandalia watu wake walimu. Kwa mfano, baada ya Wayahudi kurudi kutoka Babiloni, Ezra na wanaume wengine wanaostahili hawakuwasomea watu Sheria ya Mungu tu, bali ‘walifafanua’ sheria hiyo, ‘wakaeleza maana’ ya Neno la Mungu.—Nehemia 8:8, NW.
6, 7. Jamii ya mtumwa imeandaaje chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kupitia Baraza lake Linaloongoza, na kwa nini inafaa kutii jamii ya mtumwa?
6 Katika karne ya kwanza, wakati suala la tohara lilipozuka mwaka wa 49 W.K., baraza linaloongoza la jamii hiyo ya mtumwa lilizungumzia jambo hilo kwa sala na kufikia uamuzi unaopatana na Maandiko. Walipotangaza uamuzi wao kupitia barua, makutaniko yalitii mwelekezo uliotolewa na kupata baraka tele za Mungu. (Matendo 15:6-15, 22-29; 16:4, 5) Vivyohivyo, nyakati za kisasa, mtumwa mwaminifu kupitia Baraza Linaloongoza ameelezea masuala muhimu kama vile kutokuwamo kwa Kikristo, utakatifu wa damu, na matumizi ya dawa za kulevya na tumbaku. (Isaya 2:4; Matendo 21:25; 2 Wakorintho 7:1) Yehova aliwabariki watu wake kwa kutii Neno lake na kumtii mtumwa mwaminifu.
7 Kwa kujitiisha kwa jamii ya mtumwa, watu wa Mungu pia huonyesha kwamba wanamtii Bwana wao, Yesu Kristo. Utii huo hudhihirika hata zaidi nyakati za kisasa kwa sababu ya mamlaka ambayo Yesu ameongezewa, kama alivyotabiri Yakobo alipokuwa anakaribia kufa.
Shilo Awa Mfalme wa Dunia Mwenye Haki Kamili
8. Mamlaka ya Kristo iliongezwa jinsi gani na wakati gani?
8 Unabii wa Yakobo ulisema kwamba ‘watu wangemtii’ Shilo. Ni wazi kwamba, utawala wa Kristo ungehusisha wengi zaidi ya Waisraeli wa kiroho. Ungehusisha nani? Andiko la Ufunuo 11:15 linajibu: “Ufalme wa ulimwengu ulipata kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” Biblia huonyesha kwamba Yesu alipokea mamlaka hiyo mwishoni mwa “nyakati saba” za kiunabii—“nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa”—mwaka wa 1914.a (Danieli 4:16, 17; Luka 21:24) Mwaka huo, “kuwapo” kwa Kristo kusikoonekana akiwa Mfalme wa Kimesiya kulianza, na pia wakati wa ‘kuwa na enzi kati ya adui zake.’—Mathayo 24:3; Zaburi 110:2.
9. Yesu alifanya nini alipopokea Ufalme wake, na hilo limewaathirije wanadamu kwa njia isiyo ya moja kwa moja, na hasa wanafunzi wake?
9 Hatua ya kwanza ambayo Yesu alichukua baada ya kupokea mamlaka ya ufalme ni kumvurumisha “chini kwenye dunia” yule anayejulikana sana kwa kutotii—Shetani—pamoja na roho wake waovu. Tangu wakati huo, roho hao waovu wamefanya wanadamu wateseke sana, na pia wanatokeza hali inayofanya iwe vigumu sana kumtii Yehova. (Ufunuo 12:7-12; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa kweli, Shetani anapigana vita hasa na watiwa-mafuta wa Yehova, “washikao amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu Yesu,” na pia wenzao ambao ni “kondoo wengine.”—Ufunuo 12:17; Yohana 10:16.
10. Ni kutimizwa kwa unabii gani kunakohakikisha kwamba Shetani atashindwa katika vita yake dhidi ya Wakristo wa kweli?
10 Hata hivyo, pasipo shaka Shetani atashindwa, kwa sababu hii ni “siku ya Bwana,” na hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yesu ‘asikamilishe ushindi wake.’ (Ufunuo 1:10; 6:2) Kwa mfano, atahakikisha kwamba yule wa mwisho kati ya Waisraeli wa kiroho 144,000 ametiwa muhuri. Pia atalinda “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.” (Ufunuo 7:1-4, 9, 14-16) Hata hivyo, tofauti na wenzao waliotiwa mafuta, hawa watakuwa raia watiifu wa Yesu watakaoishi duniani. (Danieli 7:13, 14) Kuwapo kwao duniani leo, tayari kunathibitisha kwamba kwa kweli Shilo ni Mfalme juu ya “Ufalme wa ulimwengu.”—Ufunuo 11:15.
Sasa Ndio Wakati wa ‘Kutii Habari Njema’
11, 12. (a) Ni nani pekee watakaookoka mwisho wa mfumo huu wa mambo? (b) Wale wanaofyonza “roho ya ulimwengu” husitawisha tabia gani?
11 Wote wanaotaka kuishi milele, lazima wajifunze kutii, kwa kuwa Biblia inasema waziwazi kwamba “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu” hawataokoka siku ya Yehova ya kulipiza kisasi. (2 Wathesalonike 1:8) Hata hivyo, mazingira maovu ya ulimwengu wa sasa na roho yake ya uasi dhidi ya sheria na kanuni za Biblia hufanya iwe vigumu kutii habari njema.
12 Biblia hutaja mtazamo huo wa kumwasi Mungu kuwa “roho ya ulimwengu.” (1 Wakorintho 2:12) Akieleza jinsi mtazamo huo unavyowaathiri watu, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa karne ya kwanza huko Efeso: “Wakati fulani nyinyi mlitembea kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii. Ndiyo, miongoni mwao sisi sote wakati fulani tulijiendesha wenyewe kwa kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanuiwayo na mwili na fikira, nasi kiasili tulikuwa watoto wa hasira ya kisasi sawa na wale wengine.”—Waefeso 2:2, 3.
13. Wakristo wanaweza kufanikiwaje kukinza roho ya ulimwengu, na kupata matokeo gani mazuri?
13 Inafurahisha kwamba Wakristo wa Kutaniko la Efeso hawakuendelea kuwa watumwa wa roho ya kutotii. Badala yake, Wakristo hao walikuwa watoto watiifu wa Mungu kwa kujitiisha kwa roho yake na kutokeza sifa nyingi zinazofaa. (Wagalatia 5:22, 23) Vivyo hivyo leo, roho ya Mungu—nguvu kuu zaidi ulimwenguni—inasaidia mamilioni ya watu wamtii Yehova, ili waweze kupata “uhakikisho kamili wa tumaini hadi mwisho.”—Waebrania 6:11; Zekaria 4:6.
14. Yesu aliwatahadharishaje Wakristo wanaoishi siku za mwisho kuhusu matatizo hususa ambayo yangejaribu utii wao?
14 Pia, kumbuka kwamba Shilo anatuunga mkono kwa nguvu, naye pamoja na Baba yake hataruhusu adui yeyote—awe roho mwovu au mwanadamu—ajaribu utii wetu kuliko tunavyoweza kustahimili. (1 Wakorintho 10:13) Kwa kweli, ili kutusaidia katika vita yetu ya kiroho, Yesu alitaja matatizo hususa ambayo tungekabili siku hizi za mwisho. Aliyataja katika barua saba, alizompa mtume Yohana katika maono. (Ufunuo 1:10, 11) Bila shaka, barua hizo zilikuwa na mashauri muhimu kwa Wakristo wa wakati huo, lakini zinahusu hasa “siku ya Bwana,” tangu mwaka wa 1914. Kwa hiyo inafaa kama nini kwamba tuzingatie ujumbe huo!b
Epuka Kutojali, Ukosefu wa Maadili, na Pupa
15. Kwa nini tujilinde na tatizo lililopata kutaniko la Efeso, na tunawezaje kufanya hivyo? (2 Petro 1:5-8)
15 Barua ya kwanza ya Yesu ilielekezwa kwa kutaniko la Efeso. Baada ya kusifu kutaniko hilo kwa uvumilivu wake, Yesu alisema: “Hata hivyo, nashika hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao hapo kwanza.” (Ufunuo 2:1-4) Leo, Wakristo fulani waliokuwa na bidii wameacha upendo wao wenye shauku waliokuwa nao kwa Mungu hapo awali. Kuacha upendo huo kunaweza kudhoofisha uhusiano wako na Mungu, kwa hiyo unapaswa kushughulikia jambo hilo haraka. Upendo huo unaweza kuchochewaje upya? Kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida, kuhudhuria mikutano, sala, na kutafakari. (1 Yohana 5:3) Kwa kweli, unahitaji ‘jitihada yenye bidii’ ili kutimiza mambo hayo, lakini utanufaika sana. (2 Petro 1:5-8) Ukijichunguza kwa unyofu na kuona kwamba upendo wako umepoa, basi rekebisha hali hiyo mara moja kwa kutii himizo hili la Yesu: “Kumbuka ni kutoka katika nini umeanguka, nawe tubu na kufanya vitendo vya kwanza.”—Ufunuo 2:5.
16. Kulikuwa na uvutano gani hatari kiroho katika makutaniko ya Pergamamu na Thiatira, na kwa nini maneno ambayo Yesu aliambia makutaniko hayo yanafaa leo?
16 Wakristo wa Pergamamu na Thiatira walipongezwa kwa sababu ya uaminifu, uvumilivu, na bidii yao. (Ufunuo 2:12, 13, 18, 19) Hata hivyo, waliathiriwa na watu fulani waliodhihirisha mtazamo mwovu wa Balaamu na Yezebeli, ambao waliwapotosha Waisraeli wa kale kupitia uasherati na ibada ya Baali. (Hesabu 31:16; 1 Wafalme 16:30, 31; Ufunuo 2:14, 16, 20-23) Lakini namna gani wakati wetu—“siku ya Bwana”? Je, uvutano huo mwovu upo? Ndiyo, kwa kuwa watu wengi wa Mungu hutengwa na ushirika kwa sababu ya uasherati. Kwa hiyo, ni muhimu tuepuke kushirikiana na watu wanaoweza kutupotosha kiadili, iwe ni katika kutaniko au nje ya kutaniko. (1 Wakorintho 5:9-11; 15:33) Wale wanaotaka kuwa raia watiifu wa Shilo watajiepusha na vitumbuizo vinavyokiuka maadili na pia ponografia, iwe imechapwa au iwe kwenye vitabu au Internet.—Amosi 5:15; Mathayo 5:28, 29.
17. Maoni na mtazamo wa Wakristo wa Sardisi na Laodikia kuhusu hali yao ya kiroho ulitofautianaje na mtazamo wa Yesu?
17 Kutaniko la Sardisi halikupongezwa hata kidogo isipokuwa washiriki wachache tu. Lilikuwa na “jina,” au lilionekana kuwa hai, lakini lilipuuza mambo ya kiroho sana hivi kwamba Yesu aliliona kuwa “mfu.” Lilitii habari njema kidesturi tu. Lililaumiwa kama nini! (Ufunuo 3:1-3) Hali ya kutaniko la Laodikia ilifanana na hiyo. Lilijidai kuwa tajiri, likisema, “Mimi ni tajiri,” hata ingawa machoni pa Kristo lilikuwa ‘lenye taabu na la kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.’—Ufunuo 3:14-17.
18. Mtu anawezaje kuepuka kupuuza mambo ya kiroho machoni pa Mungu?
18 Leo, Wakristo fulani waliokuwa waaminifu wakati fulani wamejikuta katika hali hiyo ya kutotii. Labda wameruhusu roho ya ulimwengu ifanye wasahau umuhimu wa nyakati hizi, na hivyo kusitawisha mtazamo wa kupuuza mambo ya kiroho kama vile kujifunza Biblia, kusali, mikutano ya Kikristo, na huduma. (2 Petro 3:3, 4, 11, 12) Wakristo hao wanapaswa kumtii Kristo kwa kutumia utajiri wa kiroho kwa njia inayofaa—naam, ‘kununua kutoka kwa Kristo dhahabu iliyosafishwa sana kwa moto.’ (Ufunuo 3:18) Utajiri huo halisi unahusisha kuwa “matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki.’ Kwa kutumia utajiri huo wa kiroho kwa njia inayofaa, ‘tunajiwekea wenyewe msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili tupate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.’— 1 Timotheo 6:17-19.
Walipongezwa kwa Utii Wao
19. Yesu alitoa pongezi na himizo gani kwa Wakristo huko Smirna na Filadelfia?
19 Kutaniko la Smirna na Filadelfia ni kielelezo kizuri cha kuonyesha utii, kwa kuwa Yesu hakushutumu makutaniko hayo katika barua alizowaandikia. Alisema hivi kuhusu kutaniko la Smirna: “Najua dhiki na umaskini wako—lakini wewe ni tajiri.” (Ufunuo 2:9) Walikuwa tofauti kama nini na wale wa Laodikia ambao kwa kweli walikuwa maskini ingawa walijigamba kuwa matajiri kimwili! Bila shaka, Ibilisi hakufurahi kuona mtu yeyote akionyesha uaminifu na utii kwa Kristo. Kwa hiyo, Yesu alionya hivi: “Usiogope mambo uliyo karibu kuteseka. Tazama! Ibilisi atafuliza kutupa baadhi yenu ndani ya gereza ili mpate kutiwa kwenye jaribu kikamili, na kwamba mpate kuwa na dhiki siku kumi. Jithibitishe mwenyewe kuwa mwaminifu hata kufikia kifo, nami hakika nitakupa taji la uhai.” (Ufunuo 2:10) Vivyo hivyo, Yesu aliwapongeza wale wa Filadelfia, akisema: “Ulitunza neno langu [au, ulinitii] na hukuthibitika kuwa asiye wa kweli kwa jina langu. Mimi ninakuja upesi. Fuliza kushika sana lile ulilo nalo, ili yeyote asipate kuchukua taji lako.”—Ufunuo 3:8, 11.
20. Mamilioni ya watu leo wametunzaje neno la Yesu, licha ya hali gani?
20 Katika “siku ya Bwana,” iliyoanza mwaka wa 1914, mabaki waaminifu na wenzao wa kondoo wengine, ambao sasa ni mamilioni kadhaa, wametunza pia neno la Yesu kwa kuhubiri kwa bidii na kudumisha uaminifu-maadili. Kama ndugu zao wa karne ya kwanza, wengine wameteseka kwa sababu ya kumtii Kristo, hata kufungwa gerezani na kwenye kambi za mateso. Wengine wametunza neno la Yesu kwa kudumisha ‘jicho sahili,’ licha ya kuzungukwa na watu wenye utajiri na pupa. (Mathayo 6:22, 23) Naam, katika mazingira na hali zote, Wakristo wa kweli wanaendelea kuufurahisha moyo wa Yehova kwa utii wao.—Mithali 27:11.
21. (a) Jamii ya mtumwa itaendelea kutimiza daraka gani la kiroho? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba kwa kweli tunataka kumtii Shilo?
21 Tunapokaribia dhiki kubwa, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ameazimia kumtii Bwana wake, Kristo. Hii inatia ndani kuwatayarishia watu wa nyumba ya Mungu chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. Kwa hiyo, na tuendelee kushukuru kwa ajili ya tengenezo zuri na la kiroho la Yehova na mambo linalotuandalia. Kwa kufanya hivyo, tutathibitisha kwamba tunajitiisha kwa Shilo, atakayewathawabisha raia wake watiifu kwa uhai udumuo milele.—Mathayo 24:45-47; 25:40; Yohana 5:22-24.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari kamili kuhusu “nyakati saba,” ona sura ya 10 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Kwa habari kamili kuhusu barua zote saba, tafadhali ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kuanzia ukurasa wa 33.
-