Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Oktoba 15
    • Kuimarisha Maoni Yako Kuhusu Paradiso

      15. Kwa nini Musa hangeweza kuwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, lakini aliona nini?

      15 Fikiria jambo lingine linaloonyesha kimbele jinsi Paradiso itakavyokuwa. Baada ya Waisraeli kutanga-tanga nyikani kwa muda wa miaka 40, Musa aliwaongoza hadi nchi tambarare za Moabu, mashariki ya Mto Yordani. Kwa sababu ya kosa ambalo Musa alikuwa amefanya hapo awali, Yehova aliamua kwamba Musa hatawaongoza Waisraeli kuvuka Yordani. (Hesabu 20:7-12; 27:12, 13) Musa alimsihi Mungu hivi: “Acha nivuke, tafadhali, niione hiyo nchi nzuri iliyo ng’ambo ya Yordani.” Hata ingawa hangeingia katika nchi hiyo, bila shaka Musa alitambua kwamba hiyo ilikuwa “nchi nzuri” baada ya kupanda Mlima Pisga na kuona maeneo yake mbalimbali. Unafikiri nchi hiyo ilikuwaje?—Kumbukumbu la Torati 3:25-27.

      16, 17. (a) Nyakati za hivi karibuni, nchi hiyo inatofautianaje na Nchi ya Ahadi ya nyakati za kale? (b) Kwa nini tunaweza kuamini kwamba wakati fulani Nchi ya Ahadi ilikuwa kama paradiso?

      16 Ikiwa maoni yako kuhusu nchi hiyo yanategemea jinsi ambavyo eneo hilo limekuwa hivi karibuni, huenda ukadhani kwamba hilo lilikuwa eneo kame na lenye mchanga, lenye majangwa ya mawe-mawe, na joto kali. Hata hivyo, kuna sababu ya kuamini kwamba eneo hilo lote lilikuwa tofauti kabisa nyakati za Biblia. Katika jarida Scientific American, mtaalamu wa kilimo, Dakt. Walter C. Lowdermilk alisema kwamba nchi hiyo “imeharibika kwa sababu ya kutumiwa vibaya kwa miaka mingi.” Mtaalamu huyo aliandika: “Nchi hiyo yenye kupendeza sasa imekuwa ‘jangwa’ kwa sababu ya wanadamu wala si kwa sababu ya hali za kiasili.” Hata uchunguzi wake ulionyesha kwamba “pindi fulani nchi hiyo ilikuwa paradiso ya malisho.” Hivyo ni wazi kwamba wanadamu wametumia vibaya na kuharibu nchi ambayo ilikuwa “paradiso ya malisho.”a

      17 Kwa kufikiria mambo ambayo umesoma katika Biblia huenda ukaona ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba nchi hiyo ilikuwa kama paradiso. Kumbuka mambo ambayo Yehova aliwahakikishia Waisraeli kupitia Musa: “Nchi mnayovuka ili kuimiliki ni nchi yenye milima na nchi tambarare za mabonde. Inakunywa maji ya mvua ya mbinguni; nchi ambayo Yehova Mungu wako anaitunza.”—Kumbukumbu la Torati 11:8-12.

      18. Ni lazima andiko la Isaya 35:2 liwe liliwapa Waisraeli waliokuwa uhamishoni wazo gani kuhusu jinsi Nchi ya Ahadi ingekuwa?

      18 Nchi ya Ahadi ilikuwa yenye rutuba na yenye kuzaa sana hivi kwamba, kutaja tu maeneo fulani kulimkumbusha mtu hali za kiparadiso. Jambo hilo linaonekana wazi katika unabii wa Isaya sura ya 35, ambao ulitimizwa mara ya kwanza wakati Waisraeli waliporudi kutoka Babiloni. Isaya alitabiri hivi: “Itachanua maua bila shaka, nayo itashangilia kwa shangwe na kwa kilio cha furaha. Itapewa utukufu wa Lebanoni, fahari ya Karmeli na ya Sharoni. Kutakuwa na wale watakaouona utukufu wa Yehova, fahari ya Mungu wetu.” (Isaya 35:2) Bila shaka, kutajwa kwa maeneo ya Lebanoni, Karmeli, na Sharoni kulitokeza picha nzuri na yenye kuridhisha katika akili za Waisraeli.

      19, 20. (a) Fafanua eneo la Sharoni la kale. (b) Ni katika njia gani tunaweza kuimarisha tumaini letu katika Paradiso?

      19 Fikiria Sharoni, nchi tambarare iliyo kwenye ukingo wa bahari kati ya milima ya Samaria na Bahari Kuu, au Mediterania. (Ona picha kwenye ukurasa wa 10.) Nchi hiyo ilikuwa maarufu kwa kuwa ilikuwa nzuri na yenye kuzaa. Ilikuwa yenye maji mengi, na hivyo ilifaa kwa malisho ingawa ilikuwa na misitu ya mialoni pande za kaskazini. (1 Mambo ya Nyakati 27:29; Wimbo wa Sulemani 2:1; Isaya 65:10) Hivyo, andiko la Isaya 35:2 lilitabiri kuhusu kurudishwa na kuhusu nchi inayochanuka kwa fahari, na kuwa kama paradiso. Kupatana na maono ambayo Paulo aliona baadaye, unabii huo pia ulikuwa ukielekeza kwenye paradiso nzuri ya kiroho. Mwishowe, unabii huo pamoja na unabii mwingine mwingi huimarisha tumaini letu katika paradiso ya kidunia kwa ajili ya wanadamu.

  • Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?
    Mnara wa Mlinzi—2004 | Oktoba 15
    • a Katika kitabu The Geography of the Bible, Denis Baly anasema: “Lazima aina ya mimea iliyokuwako nyakati za Biblia iwe ilibadilika sana.” Kwa sababu gani? ‘Kwa kuwa wanadamu walihitaji miti kwa ajili ya kuni na ujenzi, walianza kukata miti na hivyo kufanya nchi iathiriwe na uharibifu unaotokana na hali ya hewa. Pole kwa pole, ukataji huo wa miti ulifanya hali ya hewa iwe kisababishi kikuu cha uharibifu huo.’

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki