Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mjifunze Kutoka Kwangu”
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • Tofauti Kati ya Yesu na Mafarisayo

      10. Kwa nini inanufaisha kufikiria masimulizi juu ya Yesu na yule mwanamke kwenye nyumba ya Simoni?

      10 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo yenye kuvutia? Yanachochea hisia zetu, sivyo? Hebu wazia ukiwa nyumbani kwa Simoni, ungehisije? Je, ungetenda kama Yesu, au ungehisi kidogo kama yule Farisayo aliyemkaribisha? Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, hivyo hatuwezi kuhisi na kutenda sawa kabisa na alivyotenda. Kwa upande mwingine, huenda hatungependa kuwa kama Simoni, aliyekuwa Farisayo. Ni watu wachache sana ambao wangejivunia kuwa Farisayo.

      11. Kwa nini hatungetaka kufananishwa na Mafarisayo?

      11 Kwa kuchunguza uthibitisho wa Kibiblia na wa kilimwengu, tunaweza kukata kauli kwamba Mafarisayo walijivuna kuwa waangalizi wa masilahi ya umma na ya taifa. Sheria ya Mungu ilikuwa wazi na yenye kueleweka kwa urahisi lakini hawakutosheka na jambo hilo. Walipoona kana kwamba Sheria haikueleza mambo fulani waziwazi, walijaribu kuongezea maelezo yao kuifanya iwe wazi zaidi ili kusiwe na uhitaji wa kutumia dhamiri. Viongozi hao wa kidini walijaribu kubuni sheria za kuongoza mwenendo wa watu katika kila jambo, hata mambo madogo-madogo.a

      12. Mafarisayo walijionaje?

      12 Mwanahistoria Myahudi Josephus wa karne ya kwanza anaonyesha wazi kwamba Mafarisayo walijiona kuwa watu wenye fadhili, wapole, wenye haki, na waliostahili kabisa kwa kazi yao. Hapana shaka kwamba baadhi yao walikuwa na sifa zinazokaribiana na hizo. Huenda ukamkumbuka Nikodemo. (Yohana 3:1, 2; 7:50, 51) Baada ya muda, baadhi yao waliukubali Ukristo. (Matendo 15:5) Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani, kama vile Mafarisayo: “Wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Hata hivyo, vitabu vya Injili vinaonyesha jinsi watu wa kawaida walivyowaona. Waliwaona kuwa watu wenye majivuno, wenye kiburi, wenye kujiona kuwa waadilifu, wenye kutafuta-tafuta makosa, wenye kushutumu, na kuwadharau wengine.

      Maoni ya Yesu

      13. Yesu alisema nini kuhusu Mafarisayo?

      13 Yesu aliwakemea waandishi na Mafarisayo kuwa wanafiki. “Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka juu ya mabega ya watu, lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza kwa kidole chao.” Naam, mzigo ulikuwa mzito, nayo nira ambayo watu walibebeshwa haikuwa ya fadhili. Yesu aliwaita waandishi na Mafarisayo “wapumbavu.” Mtu mpumbavu husumbua jamii. Yesu pia aliwaita waandishi na Mafarisayo “viongozi vipofu” na kusisitiza kwamba ‘walipuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’ Hakuna mtu ambaye angetaka Yesu amlinganishe na Farisayo.—Mathayo 23:1-4, 16, 17, 23.

      14, 15. (a) Yesu anafunua nini kuhusu Mafarisayo kupitia jinsi alivyomtendea Mathayo Lawi? (b) Ni mambo gani muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi haya?

      14 Karibu wasomaji wote wa masimulizi ya vitabu vya Injili wanaweza kuona kwamba Mafarisayo walikuwa wachambuzi. Baada ya Yesu kumwalika Mathayo Lawi, aliyekuwa mkusanya-kodi, awe mwanafunzi wake, Lawi alimwandalia Yesu karamu kubwa. Masimulizi hayo yanasema: “Ndipo Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kunung’unikia wanafunzi wake, wakisema: ‘Ni kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?’ Yesu aliwajibu hivi: ‘. . . Nimekuja kuita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi waje kwenye toba.’”— Luka 5:27-32.

      15 Lawi mwenyewe alielewa jambo jingine ambalo Yesu alisema wakati huo: “Nendeni, basi, na mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’” (Mathayo 9:13) Ingawa Mafarisayo walidai kwamba waliamini maandishi ya manabii Waebrania, wao hawakukubali maneno hayo kutoka katika andiko la Hosea 6:6. Waliona ni afadhali washikilie mapokeo kuliko kuonyesha rehema. Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza, ‘Je, mimi nina sifa ya kusisitiza sheria fulani zifuatwe, kama zile zinazounga mkono maoni yangu binafsi au njia za kawaida za kushughulikia mambo? Au je, wengine wanaona kwamba mimi ni mwenye rehema na mwema?’

      16. Mafarisayo walikuwa na mazoea gani na tunawezaje kuepuka kuwa kama wao?

      16 Mafarisayo walikuwa na mazoea ya kuwachambua wengine. Walitafuta kila kasoro—iwe ya kweli au ya kuwaziwa tu. Walishutumu watu kila wakati na kuwakumbusha kasoro zao. Mafarisayo walijivuna kwa kutoa sehemu ya kumi ya mimea iliyo midogo zaidi kama vile mnanaa, dili, na jira. Kwa mavazi yao walijionyesha kuwa watu wenye kumcha Mungu na walijaribu kuliongoza taifa. Kwa kweli, ili matendo yetu yapatane na kielelezo cha Yesu, ni lazima tuepuke mwelekeo wa kutafuta na kutia chumvi kasoro za wengine.

  • “Mjifunze Kutoka Kwangu”
    Mnara wa Mlinzi—2001 | Desemba 15
    • a ‘Tofauti kuu kati ya Yesu na Mafarisayo inaonyeshwa waziwazi na maoni yao tofauti kuhusu Mungu. Kulingana na Mafarisayo, Mungu hasa ndiye mwenye kudai; kulingana na Yesu, Mungu ni mwenye neema na huruma. Bila shaka Mafarisayo wanakubali kwamba Mungu ni mwema na ni mwenye upendo, lakini kulingana nao, sifa hizo zinaonyeshwa katika zawadi ya Torati [Sheria] na katika uwezekano wa kutimiza matakwa ya Torati hiyo. Mafarisayo waliona kwamba Torati ingeweza kutimizwa kwa kufuata mapokeo ya mdomo, yaliyokuwa na kanuni zilizofafanua sheria. Yesu aliyakataa mapokeo ya mdomo na badala yake akaikweza sheria ya upendo kwa Mungu na jirani (Mathayo 22:34-40) kuwa msingi unaofaa wa kuifafanua Sheria. Ufafanuzi wake ulipingana na wa Mafarisayo.’—The New International Dictionary of New Testament Theology.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki