Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
    • Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?

      “Nilikuwa na shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine nilijaribu kusali. Sikuwa na hakika ikiwa kuna yeyote aliyenisikiliza, lakini kusema kweli niliamini kulikuwa na mtu anayesikiliza sala. Sikuwa na furaha wala kusudi maishani. Niliogopa kuamini kwamba kuna Mungu kwa sababu nilifikiri ni watu dhaifu tu ndio walioamini Mungu.”​—⁠PATRICIA,a IRELAND.

      JE, UMEWAHI kuhisi kama alivyohisi Patricia? Je wewe husali hata kama unatilia shaka kwamba kuna Mungu? Ikiwa ndivyo, basi si wewe peke yako mwenye hisia kama hizo. Fikiria mambo yafuatayo.

      ◼ Utafiti uliohusisha raia 2,200 wa Uingereza ulionyesha kuwa ni asilimia 22 tu kati ya watu hao wanaoamini kwamba kuna Mungu aliyeumba ulimwengu na ambaye husikiliza sala. Hata hivyo, kati ya watu waliohojiwa, asilimia 55 husali mara chache tu.

      ◼ Utafiti mwingine uliohusisha watu 10,000 katika nchi mbalimbali ulionyesha kwamba wale wanaodai hakuna Mungu, karibu asilimia 30 kati yao husali.

      Kwa Nini Watu Wengi Wana Shaka?

      Allan mwanamume kutoka Uingereza anasema hivi: “Nilizoea kusema kwamba siamini kuna Mungu kwa sababu nilifikiri dini huanzishwa kwa kusudi la kuwadhibiti watu au kupata pesa. Vilevile, nilifikiri ikiwa kuna Mungu hakungekuwa na ukosefu mwingi sana wa haki. Hata hivyo, nyakati nyingine ningeketi peke yangu na kusali kwa ‘mtu’ asiyejulikana. Pia, ningejiuliza, ‘Chanzo cha uhai ni nini? ’ ”

      Kila mtu mwenye hisia kama hizo ana sababu zake zinazomfanya atilie shaka kama sala hujibiwa. Mara nyingi, wanakuwa na shaka kwa sababu ya kukosa majibu ya maswali kama vile:

      ◼ Je, kuna Muumba?

      ◼ Kwa nini mara nyingi dini inachochea watu wafanye mambo mabaya?

      ◼ Kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka?

      Ikiwa ungepata majibu ya maswali hayo, je, ungesali ukiwa na uhakika?

  • Ni Nani Msikiaji wa Sala?
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
    • Ni Nani Msikiaji wa Sala?

      IKIWA kuna Msikiaji wa Sala, basi, lazima awe ndiye Muumba. Ni nani mwingine isipokuwa yule aliyeuumba ubongo wa mwanadamu anayeweza kuelewa mawazo yetu? Ni nani mwingine angeweza kusikiliza sala na kuwapa wanadamu msaada wanaohitaji? Huenda ukajiuliza, ‘Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kuna Muumba? ’

      Watu wengi wanafikiri ili mtu aamini kuna Muumba, ni lazima apuuze sayansi ya kisasa. Lakini mawazo ya kwamba Biblia inapingana na sayansi si ya kweli. Fikiria jambo lifuatalo.

      ◼ Uchunguzi wa hivi karibuni uliohusisha maprofesa 1,646 wa sayansi kutoka vyuo vikuu bora zaidi 21 nchini Marekani ulionyesha kwamba ni asilimia 33 tu waliosema hawaamini kuna Mungu.

      Ukweli ni kwamba wanasayansi wengi wanaamini kuna Mungu.

      Mambo Yanayothibitisha Kuna Muumba

      Je,tunapaswa kuamini kuna Msikiaji wa sala bila kuwa na uthibitisho wowote? Hapana. Wazo la kwamba imani ni kuamini bila uthibitisho wowote si la kweli. Biblia inasema imani ni “uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Tafsiri nyingine inasema imani inatusaidia “kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona.” (Biblia Habari Njema) Kwa mfano, hatuwezi kuona mawimbi ya redio, lakini sauti unayosikia kupitia redio yako inathibitisha kwamba kuna mawimbi hayo yasiyoonekana, na hivyo unaamini yapo. Vivyo hivyo ingawa hatuwezi kumwona msikiaji wa sala tunaweza kuchunguza uthibitisho na kupata uhakika kwamba kwa kweli yuko.

      Tunaweza kupata wapi uthibitisho wa kwamba kuna Mungu? Tunahitaji tu kutazama vitu vinavyotuzunguka. Biblia inasema hivi: “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Je, unakubaliana na ukweli wa maneno hayo? Huenda unapotafakari jinsi ulimwengu ulivyopangwa kwa utaratibu, chanzo cha uhai, au muundo tata wa ubongo, bila shaka unafikia mkataa wa kwamba ni lazima kuna mtu mwenye uwezo zaidi kuliko wanadamu.a

      Lakini hatuwezi kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kutazama tu vitu vinavyotuzunguka. Kuchunguza uumbaji ili kupata uthibitisho wa kuwepo kwa Mungu ni sawa na kusikia hatua za mtu anayetembea nje ukiwa ndani ya nyumba ambayo imefungwa. Unajua kuna mtu nje ya nyumba, lakini ni nani? Ili ujue, unahitaji kufungua mlango. Sisi pia tunahitaji kuchukua hatua kama hiyo ili tumtambue Muumba wa vitu vyote.

      Biblia ni mlango unaoongoza kwenye ujuzi kumhusu Mungu. Unapofungua mlango huo na kuchunguza unabii wenye habari nyingi na jinsi ulivyotimia utapata uthibitisho wa kwamba kuna Mungu.b Lakini zaidi ya hayo, kuchunguza jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu kutatusaidia kujua vizuri utu wa Msikiaji wa sala.

      Msikiaji wa Sala Ana Sifa Gani?

      Biblia inafunua kwamba unaweza kumjua Msikiaji wa sala. Bila shaka, ni lazima Mungu awe na utu wenye sifa fulani ili atusikilize. Ni jambo lenye kutia moyo kusoma hivi: “Ee Msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” (Zaburi 65:2) Mungu anawasikiliza wale wanaosali kwake kwa imani. Na ana jina. Biblia inasema hivi: “Yehova yuko mbali sana na waovu, lakini huisikiliza sala ya waadilifu.”​—Methali 15:29.

      Yehova ana hisia. Yeye ni “Mungu wa upendo” na pia anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (2 Wakorintho 13:11; 1 Timotheo 1:11) Kuhusu jinsi alivyohisi wakati uovu ulipokuwa mwingi duniani, Biblia inasema hivi: “Akaumia moyoni mwake.” (Mwanzo 6:​5, 6) Ingawa watu husema Mungu husababisha kuteseka ili kuwajaribu watu, hilo si kweli. Biblia inasema hivi: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu.” (Ayubu 34:10) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Mungu ndiye Muumba mweza-yote, kwa nini ameruhusu wanadamu waendelee kuteseka?’

      Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kutumia uhuru wa kuchagua, na jambo hilo linatusaidia kujua jinsi Mungu alivyo. Je, hatuthamini uhuru wetu wa kuamua jinsi tutakavyoishi? Lakini kwa kusikitisha, watu wengi wanatumia vibaya uhuru wao na kujisababishia mateso wao wenyewe na wengine pia. Sasa swali la kufikiria kwa uzito ni hili: Mungu ataondoaje kuteseka bila kuwapokonya wanadamu uhuru wao wa kuchagua? Tutachunguza swali hilo katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi kuhusu uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu ona broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

      b Broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote na kitabu Biblia​—⁠Neno la Mungu au la Binadamu? kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kukusaidia kuchunguza uthibitisho wa kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki