-
Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?
“Nilikuwa na shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine nilijaribu kusali. Sikuwa na hakika ikiwa kuna yeyote aliyenisikiliza, lakini kusema kweli niliamini kulikuwa na mtu anayesikiliza sala. Sikuwa na furaha wala kusudi maishani. Niliogopa kuamini kwamba kuna Mungu kwa sababu nilifikiri ni watu dhaifu tu ndio walioamini Mungu.”—PATRICIA,a IRELAND.
JE, UMEWAHI kuhisi kama alivyohisi Patricia? Je wewe husali hata kama unatilia shaka kwamba kuna Mungu? Ikiwa ndivyo, basi si wewe peke yako mwenye hisia kama hizo. Fikiria mambo yafuatayo.
◼ Utafiti uliohusisha raia 2,200 wa Uingereza ulionyesha kuwa ni asilimia 22 tu kati ya watu hao wanaoamini kwamba kuna Mungu aliyeumba ulimwengu na ambaye husikiliza sala. Hata hivyo, kati ya watu waliohojiwa, asilimia 55 husali mara chache tu.
◼ Utafiti mwingine uliohusisha watu 10,000 katika nchi mbalimbali ulionyesha kwamba wale wanaodai hakuna Mungu, karibu asilimia 30 kati yao husali.
Kwa Nini Watu Wengi Wana Shaka?
Allan mwanamume kutoka Uingereza anasema hivi: “Nilizoea kusema kwamba siamini kuna Mungu kwa sababu nilifikiri dini huanzishwa kwa kusudi la kuwadhibiti watu au kupata pesa. Vilevile, nilifikiri ikiwa kuna Mungu hakungekuwa na ukosefu mwingi sana wa haki. Hata hivyo, nyakati nyingine ningeketi peke yangu na kusali kwa ‘mtu’ asiyejulikana. Pia, ningejiuliza, ‘Chanzo cha uhai ni nini? ’ ”
Kila mtu mwenye hisia kama hizo ana sababu zake zinazomfanya atilie shaka kama sala hujibiwa. Mara nyingi, wanakuwa na shaka kwa sababu ya kukosa majibu ya maswali kama vile:
◼ Je, kuna Muumba?
◼ Kwa nini mara nyingi dini inachochea watu wafanye mambo mabaya?
◼ Kwa nini Mungu ameruhusu kuteseka?
Ikiwa ungepata majibu ya maswali hayo, je, ungesali ukiwa na uhakika?
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina katika mfululizo huu yamebadilishwa.
-
-
Ni Nani Msikiaji wa Sala?Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
Ni Nani Msikiaji wa Sala?
IKIWA kuna Msikiaji wa Sala, basi, lazima awe ndiye Muumba. Ni nani mwingine isipokuwa yule aliyeuumba ubongo wa mwanadamu anayeweza kuelewa mawazo yetu? Ni nani mwingine angeweza kusikiliza sala na kuwapa wanadamu msaada wanaohitaji? Huenda ukajiuliza, ‘Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kuna Muumba? ’
Watu wengi wanafikiri ili mtu aamini kuna Muumba, ni lazima apuuze sayansi ya kisasa. Lakini mawazo ya kwamba Biblia inapingana na sayansi si ya kweli. Fikiria jambo lifuatalo.
◼ Uchunguzi wa hivi karibuni uliohusisha maprofesa 1,646 wa sayansi kutoka vyuo vikuu bora zaidi 21 nchini Marekani ulionyesha kwamba ni asilimia 33 tu waliosema hawaamini kuna Mungu.
Ukweli ni kwamba wanasayansi wengi wanaamini kuna Mungu.
Mambo Yanayothibitisha Kuna Muumba
Je,tunapaswa kuamini kuna Msikiaji wa sala bila kuwa na uthibitisho wowote? Hapana. Wazo la kwamba imani ni kuamini bila uthibitisho wowote si la kweli. Biblia inasema imani ni “uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Tafsiri nyingine inasema imani inatusaidia “kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona.” (Biblia Habari Njema) Kwa mfano, hatuwezi kuona mawimbi ya redio, lakini sauti unayosikia kupitia redio yako inathibitisha kwamba kuna mawimbi hayo yasiyoonekana, na hivyo unaamini yapo. Vivyo hivyo ingawa hatuwezi kumwona msikiaji wa sala tunaweza kuchunguza uthibitisho na kupata uhakika kwamba kwa kweli yuko.
Tunaweza kupata wapi uthibitisho wa kwamba kuna Mungu? Tunahitaji tu kutazama vitu vinavyotuzunguka. Biblia inasema hivi: “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Je, unakubaliana na ukweli wa maneno hayo? Huenda unapotafakari jinsi ulimwengu ulivyopangwa kwa utaratibu, chanzo cha uhai, au muundo tata wa ubongo, bila shaka unafikia mkataa wa kwamba ni lazima kuna mtu mwenye uwezo zaidi kuliko wanadamu.a
Lakini hatuwezi kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kutazama tu vitu vinavyotuzunguka. Kuchunguza uumbaji ili kupata uthibitisho wa kuwepo kwa Mungu ni sawa na kusikia hatua za mtu anayetembea nje ukiwa ndani ya nyumba ambayo imefungwa. Unajua kuna mtu nje ya nyumba, lakini ni nani? Ili ujue, unahitaji kufungua mlango. Sisi pia tunahitaji kuchukua hatua kama hiyo ili tumtambue Muumba wa vitu vyote.
Biblia ni mlango unaoongoza kwenye ujuzi kumhusu Mungu. Unapofungua mlango huo na kuchunguza unabii wenye habari nyingi na jinsi ulivyotimia utapata uthibitisho wa kwamba kuna Mungu.b Lakini zaidi ya hayo, kuchunguza jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu kutatusaidia kujua vizuri utu wa Msikiaji wa sala.
Msikiaji wa Sala Ana Sifa Gani?
Biblia inafunua kwamba unaweza kumjua Msikiaji wa sala. Bila shaka, ni lazima Mungu awe na utu wenye sifa fulani ili atusikilize. Ni jambo lenye kutia moyo kusoma hivi: “Ee Msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” (Zaburi 65:2) Mungu anawasikiliza wale wanaosali kwake kwa imani. Na ana jina. Biblia inasema hivi: “Yehova yuko mbali sana na waovu, lakini huisikiliza sala ya waadilifu.”—Methali 15:29.
Yehova ana hisia. Yeye ni “Mungu wa upendo” na pia anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (2 Wakorintho 13:11; 1 Timotheo 1:11) Kuhusu jinsi alivyohisi wakati uovu ulipokuwa mwingi duniani, Biblia inasema hivi: “Akaumia moyoni mwake.” (Mwanzo 6:5, 6) Ingawa watu husema Mungu husababisha kuteseka ili kuwajaribu watu, hilo si kweli. Biblia inasema hivi: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu.” (Ayubu 34:10) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Mungu ndiye Muumba mweza-yote, kwa nini ameruhusu wanadamu waendelee kuteseka?’
Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kutumia uhuru wa kuchagua, na jambo hilo linatusaidia kujua jinsi Mungu alivyo. Je, hatuthamini uhuru wetu wa kuamua jinsi tutakavyoishi? Lakini kwa kusikitisha, watu wengi wanatumia vibaya uhuru wao na kujisababishia mateso wao wenyewe na wengine pia. Sasa swali la kufikiria kwa uzito ni hili: Mungu ataondoaje kuteseka bila kuwapokonya wanadamu uhuru wao wa kuchagua? Tutachunguza swali hilo katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu ona broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote na kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kukusaidia kuchunguza uthibitisho wa kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Inakufanya Uwe na Shaka?
Inasikitisha kwamba dini ndiyo inayofanya watu wengi watilie shaka kwamba kuna Msikiaji wa sala mwenye huruma. Kwa sababu dini imejihusisha na vita, ugaidi, na kutochukua hatua yoyote watoto wanapotendewa vibaya kingono, hilo linafanya hata watu wanaosali waseme, “Siamini kuna Mungu.”
Kwa nini mara nyingi dini imewachochea watu watende mambo mabaya? Kwa ufupi: Watu wengi wamefanya mambo mabaya wakidai ni kwa sababu ya imani yao ya kidini. Biblia ilitabiri kwamba watu waovu wangeingia katika Ukristo na kutenda kinyume cha mapenzi ya Mungu. Mtume Paulo aliwaambia hivi waangalizi Wakristo: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”—Matendo 20:29, 30.
Mungu anachukizwa na dini ya uwongo. Kwa kweli, Neno la Mungu, Biblia, linashutumu dini ya uwongo kwa hatia ya kumwaga “damu . . . ya wale wote ambao wameuawa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Kwa sababu dini ya uwongo imeshindwa kuwafundisha watu kumhusu Mungu wa kweli ambaye sifa yake kuu ni upendo, dini hizo zina hatia ya damu machoni pa Mungu.—1 Yohana 4:8.
Msikiaji wa sala anawasikitikia wale wanaoteseka kwa sababu ya kukandamizwa na dini. Hivi karibuni, upendo wa Mungu kuelekea wanadamu utamchochea amtumie Yesu kuwahukumu wanafiki wote wa kidini. Yesu alisema hivi: “Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako?’ . . . Hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”—Mathayo 7:22, 23.
-
-
Kwa Nini Msikiaji wa Sala Anaruhusu Watu Wateseke?Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
Kwa Nini Msikiaji wa Sala Anaruhusu Watu Wateseke?
HATA ingawa watu fulani husali, bado wanashuku ikiwa kuna Mungu. Kwa nini wanatilia shaka? Labda ni kwa sababu wanaona watu wakiteseka sana ulimwenguni. Je, umewahi kujiuliza kwa nini Mungu ameruhusu watu wateseke?
Je, kweli Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa katika hali waliyo nayo sasa, yaani, hali ya kutokamilika na kupatwa na mateso? Ingekuwa vigumu kumheshimu mungu ambaye angewaumba wanadamu ili wateseke. Lakini fikiria mfano huu: Ikiwa ungetazama gari jipya huku ukivutiwa nalo, kisha utambue kwamba limeharibika upande mmoja, je, ungefikiria kwamba lilitengenezwa hivyo? Bila shaka, la! Huenda ungefikia mkataa kwamba lilitengenezwa “bila kasoro” na kwamba liliharibiwa na mtu au kitu fulani.
Vivyo hivyo, ikiwa tungetazama na kuvutiwa na mpangilio na ubuni wa ajabu katika mazingira yetu kisha tuone machafuko na ufisadi unaowasumbua wanadamu, tungefikia mkataa gani? Biblia inafundisha kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wa kwanza wakiwa wakamilifu lakini baadaye wakajisababishia matatizo. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Habari njema ni kwamba Mungu ameahidi kuondoa matatizo hayo kwa kuwarudishia wanadamu watiifu hali yao ya ukamilifu. Hata hivyo, kwa nini amekawia?
Kwa Nini Amekawia Sana?
Jibu linahusiana na swali lililozuka kuhusu ni nani anayepaswa kuwatawala wanadamu. Yehova hakukusudia kamwe wanadamu wajitawale wenyewe. Angekuwa Mtawala wao. Biblia yenyewe inasema: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wa kwanza waliamua kuasi utawala wa Mungu. Kwa kumwasi Mungu, wakawa watenda dhambi. (1 Yohana 3:4) Matokeo ni kuwa walipoteza hali yao ya ukamilifu na wakajisababishia matatizo wao wenyewe na wazao wao pia.
Kwa maelfu ya miaka, Yehova amewaruhusu wanadamu wajitawale, na historia imethibitisha kwamba wanadamu hawana uwezo wa kujitawala wenyewe. Imeonyesha kwamba serikali zote za wanadamu zinasababisha mateso. Hakuna hata moja ambayo imefaulu kuondoa vita, uhalifu, ukosefu wa haki, au magonjwa.
Mungu Atarekebishaje Mambo?
Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu ataleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Wale tu wanaoamua kuwapenda wenzao na kumpenda Mungu ndio watakaoruhusiwa kuishi katika ulimwengu huo.—Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19, 20.
Pia, Biblia inasema kwamba katika “siku ya hukumu” ambayo inakaribia haraka, Mungu ataondoa mateso na wale wanaoyasababisha. (2 Petro 3:7) Baadaye, Yesu Kristo, Mtawala aliyechaguliwa na Mungu, atawatawala wanadamu watiifu. (Danieli 7:13, 14) Utawala wa Yesu utatimiza mambo gani? Biblia inasema: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
Akiwa Mfalme mbinguni, Yesu ataondoa matatizo kama vile magonjwa, kuzeeka, na kifo ambayo yalianza baada ya wanadamu kumwasi Mungu ambaye ni “chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Yesu atawaponya watu wote wanaojitiisha chini ya utawala wake wenye upendo. Chini ya utawala wake, ahadi hizi za Biblia zitatimizwa:
◼ “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ Watu wanaokaa katika nchi hiyo watakuwa wamesamehewa kosa lao.”—Isaya 33:24.
◼ “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.
Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa mateso yote? Kwa sasa, hatupaswi kuwa na shaka kwamba anasikiliza sala zetu, hata kama ameruhusu wanadamu wateseke kwa muda.
Mungu yupo. Anaweza kukusikiliza, hata unapomweleza kuhusu mambo yanayokutia uchungu na huzuni. Na anatamani kuona wakati ambapo utafurahia maisha bila kuwa na shaka na bila maumivu yoyote.
-
-
Mkaribie Msikiaji wa SalaMnara wa Mlinzi—2012 | Julai 1
-
-
Mkaribie Msikiaji wa Sala
WATU wengi wanaodai kwamba wanaamini kuna Mungu hawawezi kuthibitisha kwa nini wana imani. Wala hawawezi kueleza kwa nini mara nyingi dini inatenda mabaya au kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke. Jambo wanaloweza tu kufanya ni kusali kwa Mungu ambaye hawamwelewi.
Hata hivyo, wewe unaweza kumkaribia Mungu hata zaidi. Unaweza kujenga imani yako juu ya msingi wa kumwelewa Mungu na hivyo kumpenda na kumthamini. Imani ya kweli inategemea mambo yaliyothibitishwa. (Waebrania 11:1) Ukijifunza ukweli kumhusu Mungu, unaweza kumjua na kuzungumza naye kama rafiki. Fikiria mambo ambayo watu fulani waliokuwa wakisali walijionea ingawa walikuwa na shaka ikiwa kuna Mungu.
◼ Patricia aliyetajwa katika makala ya kwanza. “Siku moja nilikuwa na marafiki wangu kumi hivi tulipoanza kuzungumzia mambo ya dini. Niliwaambia kwamba niliondoka nyumbani ili kuhepa mazungumzo kati ya Shahidi mmoja wa Yehova aliyetutembelea nyumbani na baba yangu, ambaye hakuamini kuna Mungu. ‘Labda Mashahidi wa Yehova wana ukweli,’ akasema rafiki yangu mmoja.
“‘Kwa nini tusihudhurie mikutano yao ili tujionee? ’ akasema mwingine. Na hivyo ndivyo tulivyofanya. Ingawa tulikuwa na shaka, baadhi yetu tuliendelea kuhudhuria kwa sababu tu Mashahidi walituonyesha urafiki.
“Hata hivyo, Jumapili moja nilisikia jambo ambalo lilibadili mtazamo wangu. Msemaji alifafanua kwa nini watu huteseka. Sikuwahi kuwazia mbeleni kwamba mwanadamu aliumbwa mwanzoni akiwa mkamilifu na kwamba dhambi na kifo kilianza na mwanadamu mmoja na kuenea kwa wanadamu wote. Vilevile, msemaji alieleza kwa nini kifo cha Yesu kilihitajika ili kuwarudishia wanadamu hali ambayo mwanadamu wa kwanza alipoteza.a (Waroma 5:12, 18, 19) Kwa ghafula, nilianza kuelewa kila kitu. ‘Kwa kweli kuna Mungu anayetujali,’ nikawaza. Niliendelea kujifunza Biblia na baada ya muda, kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nikatambua kwamba ningeweza kusali kwa Mungu aliye halisi.”
◼ Allan, aliyetajwa pia katika makala ya kwanza. “Siku moja Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani, na mke wangu akawakaribisha kwa sababu alipendezwa na mambo waliyosema kuhusu kuishi milele duniani. Nilikasirika. Hivyo, nikawaacha wageni sebuleni na nikamwita mke wangu jikoni na kumwambia, ‘Usiwe mpumbavu. Huwezi kuamini mambo kama hayo! ’
“‘Basi, wewe rudi na uwathibitishie kwamba mambo wanayosema ni ya uwongo,’ akanijibu.
“Bila shaka, sikuwa na uthibitisho wowote. Lakini walikuwa wenye fadhili sana na wakaniachia kitabu ambacho kinafafanua ikiwa uhai ulitokana na uumbaji au mageuzi. Maelezo yake yalikuwa wazi na yenye kupatana na akili hivi kwamba nikaamua ninahitaji kujua mengi zaidi kumhusu Mungu. Nilianza kujifunza Biblia na Mashahidi, na muda si muda nikatambua kwamba mambo ambayo Biblia ilisema ni tofauti kabisa na mambo niliyowazia kuhusu dini. Nilipoendelea kujifunza kumhusu Yehova, nilianza kusali kwake nikimweleza mambo hususa. Nilikuwa na mitazamo fulani mibaya, hivyo, nilisali nikiomba msaada. Nina hakika kwamba Yehova alijibu sala zangu.”
◼ Andrew, anayeishi Uingereza. “Ingawa nilishikilia sana maoni fulani na nilivutiwa na sayansi, niliamini nadharia ya mageuzi kwa sababu tu watu wengine walisema ilikuwa ya kweli. Sikuamini kuna Mungu kwa sababu ya mambo mabaya yanayotendeka duniani.
“Hata hivyo, nyakati fulani ningejiambia: ‘Ikiwa kuna Mungu mbinguni, basi ninahitaji kumjua. Kwa nini kuna vita na uhalifu mwingi?’ Nilipopata matatizo, nyakati fulani nilisali ili nipate msaada, lakini sikujua nilikuwa nikisali kwa nani.
“Kisha mtu fulani akampa mke wangu trakti iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova yenye kichwa Je, Ulimwengu Huu Utaokoka? Nilikuwa nikijiuliza swali hilo mara kwa mara. Trakti hiyo ilifanya nijiulize swali hili kuhusu Biblia, ‘Je, ni muhimu kuchunguza majibu yake?’ Baadaye, nilipokuwa likizoni, mtu fulani alinipa kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?b Nilipotambua kwamba Biblia inakubaliana na sayansi ya kweli, nilihisi kuwa nilihitaji kujifunza mengi kuhusu Biblia. Hivyo, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipojitolea kunifundisha Biblia, nilikubali. Nilipoendelea kuelewa kusudi la Yehova, nilihisi nimemjua Mungu kuwa mtu halisi, mtu ambaye ningeweza kuzungumza naye kwa uhuru kupitia sala.”
◼ Jan, aliyelelewa akiwa Mprotestanti huko London. “Unafiki wa dini na kuenea kwa matatizo kulinifanya niache kuwa mwanadini. Pia, niliacha kwenda chuoni na nikaanza kuimba na kucheza gitaa ili nipate pesa. Huo ndio wakati niliokutana na Pat. Alikuwa amelelewa akiwa Mkatoliki na kama mimi, hakufuata dini.
“Tuliishi katika nyumba fulani pamoja na vijana wengine walioacha masomo na ambao walipendezwa na dini za Mashariki. Tulitumia saa nyingi usiku tukizungumza kwa undani kuhusu kusudi la uhai. Ingawa mimi na Pat hatukuamini kuna Mungu, tulihisi kwamba lazima kuwe na nguvu fulani ‘zinazotegemeza uhai.’
“Baada ya kuhamia kaskazini mwa Uingereza ili tutafute kazi, mwana wetu alizaliwa. Siku moja usiku alishikwa na ugonjwa, na nikajipata nikisali kwa Mungu ambaye sikumwamini. Muda mfupi baadaye uhusiano kati yangu na Pat uliharibika, na nikamchukua mtoto wetu na kuondoka. Kwa mara nyingine, nilisali ili nipate msaada, nikitumaini kwamba kuna mtu aliyekuwa akinisikiliza. Sikujua kwamba Pat pia alikuwa akisali.
“Baadaye siku hiyo, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea Pat na kumwonyesha mashauri fulani ya Biblia. Alinipigia simu na kuniuliza ikiwa ningetaka kujifunza Biblia pamoja naye na wale Mashahidi. Baada ya muda tulijifunza kwamba ili tumpendeze Mungu tulipaswa kuhalalisha ndoa yetu. Lilionekana kuwa jambo lisilowezekana kwa sababu uhusiano wetu ulikuwa na matatizo.
“Tulitaka kujua mengi zaidi kuhusu utimizo wa unabii wa Biblia, chanzo cha mateso, na maana ya Ufalme wa Mungu. Pole kwa pole, tulitambua kwamba Mungu anajali na tulitaka kufanya mambo anayosema. Tulifunga ndoa. Hekima inayopatikana katika Neno la Mungu imetusaidia kuwalea watoto wetu watatu. Tuna hakika kwamba Yehova alisikiliza sala zetu.”
Chunguza Uthibitisho
Kama mamilioni ya watu wengine, watu waliotajwa katika makala hii walitambua uwongo wa dini na wakagundua kwa nini Mungu anaruhusu watu wateseke. Je, umetambua kwamba katika kila kisa ujuzi sahihi wa Biblia ndio uliowasadikisha watu hao kuwa kwa kweli Yehova anasikiliza sala.
Je, ungependa kuchunguza mambo yanayothibitisha kwamba Mungu yupo? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze ukweli kumhusu Yehova na jinsi unavyoweza kumkaribia “Msikiaji wa sala.”—Zaburi 65:2.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate habari zaidi kuhusu thamani ya kukomboa ya kifo cha Yesu, ona sura ya 5 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
“Nilipoendelea kuelewa kusudi la Yehova, nilihisi nimemjua Mungu kuwa mtu halisi, mtu ambaye ningeweza kuzungumza naye kwa uhuru kupitia sala”
[Picha katika ukurasa wa 9]
Imani ya kweli inategemea mambo yaliyothibitishwa na tamaa ya kujua ukweli kumhusu Mungu
-