-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kujifunza kwa Kutegemea Kumbukumbu
András Molnos anasema hivi: “Nilipata mazoea mazuri ya kiroho gerezani.” Vipi? Aliona umuhimu wa kukusanyika pamoja na ndugu kila juma ili kujifunza Neno la Mungu. András anasema: “Mara nyingi, hatukuwa na vitabu wala magazeti, kwa hiyo tulitegemea kumbukumbu. Ndugu walijitahidi kukumbuka makala za Mnara wa Mlinzi walizojifunza kabla ya kufungwa. Ndugu wachache walikumbuka kila kitu katika gazeti, hata maswali ya makala za funzo!” Baadhi yao walikumbuka vizuri makala hizo kwa sababu walikuwa wamezinakili kwa mkono kabla ya kukamatwa.—Ona sanduku, “Njia za Kufanya Nakala,” kwenye ukurasa wa 132-133.
Walipopanga mikutano ya Kikristo ndugu wenye madaraka walitangaza habari ambayo ingezungumziwa, na kila mfungwa alijitahidi kukumbuka yote aliyojua kuhusu habari hiyo kama vile maandiko na mambo aliyokuwa amesoma katika vitabu vya Kikristo vya kujifunzia Biblia. Hatimaye, wote walikutana ili kuzungumzia habari hizo. Kiongozi aliyeteuliwa kwenye mkutano alifungua kwa sala na kuongoza mazungumzo kwa kuuliza maswali. Baada ya wengine wote kutoa maelezo, ndugu huyo alitoa maelezo yake, kisha akauliza swali lingine.
Majadiliano kama hayo hayakuruhusiwa katika magereza fulani. Lakini ndugu hawakushindwa kujifunza. Ndugu mmoja anasema hivi: “Tulikuwa tukitoa kioo cha dirisha la bafu, na kukipaka mchanganyiko wa maji, sabuni, na chokaa tuliyokuwa tumetoa ukutani. Kilipokauka, tuliandika somo la siku hiyo kwenye kioo hicho. Ndugu mmoja alinong’ona maneno, huku mwingine akiyaandika.
“Tulikaa katika seli kadhaa za gereza, na vikundi vya funzo vilipangwa katika seli hizo. Kila somo lilipitishwa kutoka ndugu mmoja hadi mwingine katika ile seli yenye kioo. Ndugu katika zile seli nyingine walipataje habari hizo? Mmoja wetu aliziwasilisha kwa mfumo wa mawasiliano wa Morse kwa kugongagonga polepole ukuta au mabomba ya kupasha joto. Wakati huohuo, kila ndugu katika zile seli nyingine alitumia kikombe chake kama kifaa cha kukuza sauti kwa kukiweka ukutani au kwenye mabomba na kuweka sikio kwenye kikombe hicho. Wale ambao hawakujua mfumo wa Morse hawakuwa na budi kujifunza mfumo huo.”
-
-
Rumania2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/picha katika ukurasa wa 124, 125]
Tulikumbuka Mistari 1,600 ya Biblia
Dionisie Vârciu
Alizaliwa: 1926
Alibatizwa: 1948
Maelezo mafupi kumhusu: Kuanzia mwaka wa 1959, alikaa katika magereza mbalimbali na kambi za kazi ngumu kwa zaidi ya miaka mitano. Alikufa mwaka wa 2002.
Tulipokuwa gerezani, tuliruhusiwa kuwasiliana na familia zetu, na kila mwezi waliruhusiwa kutuletea kifurushi cha zawadi chenye uzani wa kilo tano. Wale tu waliomaliza kazi zao ndio waliopewa vifurushi vyao. Tulikuwa tukigawanya chakula katika sehemu 30 hivi ili kila mmoja wetu apate kiasi sawa na mwenzake. Pindi moja tuligawanya matofaa mawili katika sehemu 30 hivi. Ni kweli kwamba kila sehemu ilikuwa ndogo, hata hivyo ilipunguza njaa yetu.
Hata ingawa hatukuwa na Biblia au vichapo vya kujifunzia Biblia, tulidumisha hali yetu ya kiroho kwa kujikumbusha mambo tuliyokuwa tumejifunza kabla ya kutiwa gerezani na kwa kuyazungumzia pamoja na wengine. Tulipanga kwamba kila asubuhi ndugu mmoja akumbuke na kukariri mstari fulani wa Biblia. Kisha tukaurudia-rudia kwa sauti ya chini na kuutafakari asubuhi tulipokuwa katika matembezi ya kulazimishwa yaliyochukua dakika 15 hadi 20. Tuliporudi kwenye seli yetu yenye upana wa meta mbili na urefu wa meta nne ambapo 20 kati yetu tulikuwa tukikaa, tulitumia dakika 30 hivi kutoa maelezo kuhusu mstari huo. Tulikumbuka jumla ya mistari 1,600 ya Biblia. Alasiri, tulizungumzia habari mbalimbali kutia ndani maandiko 20 hadi 30 yanayohusiana na habari hizo. Sote tuliziweka habari hizo akilini.
Mwanzoni ndugu fulani alifikiri kwamba alikuwa mzee sana asiweze kukariri maandiko mengi ya Biblia. Lakini alikuwa tu akipuuza uwezo wake. Baada ya kutusikia tukikariri maandiko mara 20 hivi, yeye pia aliweza kukumbuka na kukariri maandiko mengi, na jambo hilo likamfurahisha sana!
Naam, tulikuwa wenye njaa na dhaifu kimwili, lakini Yehova aliendelea kutulisha na kutuimarisha kiroho. Hata baada ya kuachiliwa, tulihitaji kudumisha hali yetu ya kiroho kwa kuwa maofisa wa Idara ya Upelelezi waliendelea kutunyanyasa wakitarajia kwamba tutakana imani yetu.
-