-
Mungu ni Kimbilio Langu na Nguvu ZanguMnara wa Mlinzi—1997 | Mei 1
-
-
“Bila shaka kuteseka miaka tisa chini ya Hitler ni jambo lenye kusifika,” akasema hakimu Mkomunisti. “Wewe kwa kweli ulipinga vita, lakini sasa unapinga amani yetu!”
ALIKUWA akirejezea kufungwa kwangu kwa mapema zaidi na Nazi na usoshalisti katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani. Hapo kwanza nilikuwa nisiyeweza kusema lakini ndipo nilipojibu: “Mkristo hawezi kushindania amani ya kweli katika njia ileile watu wengine hushindania.” Najaribu tu kufuata amri ya Kibiblia kupenda Mungu na jirani yangu. Neno la Mungu hunisaidia kudumisha amani katika neno na tendo.”
Siku hiyo, Septemba 4, 1951, Wakomunisti walinihukumu miaka minane gerezani—muda unaopungua mwaka mmoja wa kile kifungo cha Nazi.
-
-
Mungu ni Kimbilio Langu na Nguvu ZanguMnara wa Mlinzi—1997 | Mei 1
-
-
Suluhisho la Adui—Kifungo
Iliwezekana kutokeza gazeti Mnara wa Mlinzi kisiri katika Chemnitz hadi vuli ya 1935. Baada ya hapo mashine ya kunakili iliyotumiwa ilipaswa kupelekwa Beierfeld katika Milima ya Ore ambako ilitumiwa kutokeza fasihi hadi Agosti 1936. Käthe nami tuligawanya nakala kwa ndugu ambao anwani zao baba alitupatia. Mambo yalikuwa shwari kwa muda fulani. Lakini ndipo Gestapo waliponiweka chini ya uangalizi, na katika Agosti 1936 walinikamata nyumbani mwangu na kunitia kizuizini, nilikongojea kesi.
Katika Februari 1937, ndugu 25 na dada 2—pamoja nami—tulienda mbele ya mahakama ya pekee katika Saxony. Ilidaiwa kwamba tengenezo la Mashahidi wa Yehova lilikuwa lenye kufitini serikali. Wale ndugu waliokuwa wakitokeza Mnara wa Mlinzi walihukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani. Nilihukumiwa miaka miwili.
Badala ya kuachiliwa huru baada ya kumaliza kifungo changu, nilikamatwa na Gestapo. Nilipaswa kutia sahihi julisho rasmi kwamba singeweza tena kuwa mtendaji nikiwa Shahidi wa Yehova. Nilikataa kwa uthabiti, ndipo afisa akaghadhibika, akasimama ghafula, na kutoa hati ya kuamuru nitiwe kizuizini. Hiyo hati imeonyeshwa pichani. Bila kuruhusiwa kuona wazazi wangu, nilipelekwa mara moja katika kambi ndogo ya mateso ya wanawake katika Lichtenburg kwenye mto Elbe. Muda mfupi baada ya hapo nilikutana na Käthe. Alikuwa amekuwa katika kambi ya mateso katika Moringen tangu Desemba 1936, lakini kambi hiyo ya mateso ilipofungwa, yeye, pamoja na dada wengine wengi, wakaja Lichtenburg. Baba yangu alikuwa kizuizini pia, na sikumwona tena hadi 1945.
Katika Lichtenburg
Sikuruhusiwa kujiunga na wale Mashahidi wengine wa kike mara moja, kwa kuwa walikuwa wakiadhibiwa kwa sababu fulani. Katika mojawapo ya kumbi, niliona vikundi viwili vya wafungwa—wanawake walioketi kwa kawaida kwenye meza na Mashahidi waliopaswa kuketi siku nzima juu ya vibago na ambao hawakupewa chochote cha kula.b
Nilikubali kwa utayari mgawo wowote wa kazi, nikitumaini kukutana na Käthe kwa njia fulani. Na hivyo ndivyo ilivyotokea. Alikuwa akienda kazini pamoja na wafungwa wengine wawili tulipokutana. Nikiwa mwenye shangwe mno, nilimkumbatia. Lakini mlinzi wa kike alituripoti mara moja. Tulihojiwa, na kutoka wakati huo na kuendelea, tukatenganishwa kwa kusudi. Hilo lilikuwa jambo gumu sana.
Matukio mengine mawili katika Lichtenburg hayawezi kusahaulika. Katika pindi moja wafungwa wote walipaswa kukusanyika uani kusikiliza mojawapo ya hotuba za kisiasa za Hitler redioni. Sisi Mashahidi wa Yehova tulikataa, kwa kuwa sherehe za kizalendo zilihusika. Hivyo walinzi walitugeuzia mabomba, wakitupuliza na maji yenye kutoka kwa nguvu na kutufukuza sisi wanawake tusio na kinga kutoka orofa ya nne hadi uani. Hapo ilitubidi kusimama tukiwa tumelowa kabisa.
Katika pindi nyingine mimi, pamoja na Gertrud Oehme na Gertel Bürlen, tuliamuriwa kurembesha makao makuu ya mkuu wa gereza kwa taa za umeme, kwa kuwa siku ya kuzaliwa ya Hitler ilikuwa ikikaribia. Tulikataa, huku tukitambua mbinu za Shetani za kujaribu kutuongoza kuvunja uaminifu-maadili wetu kupitia maridhiano mbalimbali kwa mambo madogo-madogo. Ikiwa adhabu, kila mmoja wetu dada vijana alipaswa kukaa majuma matatu yaliyofuata akiwa peke yake katika seli ndogo, yenye giza. Lakini Yehova alikuwa karibu nasi na, hata katika mahali penye kuogofya kama hapo, alijithibitisha mwenyewe kuwa kimbilio.
Katika Ravensbrück
Katika Mei 1939 wafungwa katika Lichtenburg walihamishwa hadi kambi ya mateso ya Ravensbrück. Huko nilipewa mgawo kwenye dobi, pamoja na dada Mashahidi wengine kadhaa. Muda mfupi baada ya vita, tulipaswa kupata ile bendera ya swastika, jambo tulilokataa. Tokeo ni kwamba, wawili wetu, Mielchen Ernst nami, tuliwekwa katika nyumba ya adhabu. Hiyo ilikuwa mojawapo ya adhabu zilizokuwa kali zaidi na ilimaanisha kwamba tulipaswa kufanya kazi ngumu kila siku, hata Jumapili, hata halihewa iweje. Kwa kawaida, hukumu ya juu zaidi ilikuwa miezi mitatu, lakini tuliendelea kuwa huko kwa mwaka mmoja. Bila msaada wa Yehova, singalisalimika kamwe.
Katika 1942, hali kwetu sisi wafungwa ilikuwa nafuu kidogo, nami nilipewa mgawo wa kufanya kazi nikiwa mtunza-nyumba wa familia ya SS ambayo haikuwa mbali na kambi. Hiyo familia iliniruhusu kadiri fulani ya uhuru. Mathalani, siku moja nilipokuwa nikiwapeleka watoto kwa matembezi, nilikutana na Josef Rehwald na Gottfried Mehlhorn, wafungwa wawili wakiwa na pembetatu za rangi ya zambarau, ambao pamoja tuliweza kubadilishana maneno fulani ya kitia-moyo.c
-
-
Mungu ni Kimbilio Langu na Nguvu ZanguMnara wa Mlinzi—1997 | Mei 1
-
-
Chini ya Marufuku na Kizuizi kwa Mara Nyingine Tena
Mji wa Magdeburg uko katika ile sehemu ya Ujerumani iliyokuja kuongozwa na Wakomunisti. Walipiga marufuku kazi yetu katika Agosti 1, 1950, na kufunga Betheli ya Magdeburg. Hivyo utumishi wangu katika Betheli ukaisha, ambao ulikuwa wakati wa mazoezi yenye thamani. Nilirudi Chemnitz, nikiwa nimeazimia hata chini ya Wakomunisti kuendelea kushika kwa mkazo kweli na kupiga mbiu juu ya Ufalme wa Mungu kuwa ndio tumaini la pekee la wanadamu wenye msononeko.
Katika Aprili 1951, nilisafiri pamoja na ndugu fulani kwenda Berlin kuchukua nakala za Mnara wa Mlinzi. Tuliporudi, tulipigwa na butwaa kupata kwamba stesheni ya reli katika Chemnitz imezingirwa na polisi. Kwa wazi walikuwa wakitutarajia, nasi tulikamatwa papo hapo.
Tulipofika kizuizini kungojea kesi, nilikuwa nimebeba hati zilizothibitisha kwamba nilikuwa nimefungwa kwa miaka kadhaa na Nazi. Basi, walinzi walinitendea kwa staha. Mmojawapo wa walinzi wakuu wa kike alisema hivi: “Nyinyi Mashahidi wa Yehova si wahalifu; nyinyi si watu wa gerezani.”
Wakati mmoja alikuja katika seli yangu, ambako nilikuwa na dada wengine wawili, na kuweka kitu kisiri chini ya kimojawapo cha vitanda. Kilikuwa kitu gani? Biblia yake mwenyewe, aliyoturuhusu tuwe nayo. Katika pindi nyingine, alitembelea wazazi wangu nyumbani, kwa kuwa hawakuishi mbali na gereza. Alipata nakala za Mnara wa Mlinzi na chakula, akaficha vitu vyote yeye mwenyewe, na kuviingiza selini mwangu.
Kuna jambo lingine mimi hupenda kulikumbuka. Nyakati nyingine Jumapili asubuhi, tuliimba nyimbo zetu za kitheokrasi kwa sauti kubwa hivi kwamba wale wafungwa wengine walipiga makofi kwa furaha baada ya kila wimbo.
Nguvu na Msaada Kutoka kwa Yehova
Wakati wa mashtaka ya mahakama katika Septemba 4, 1951, hakimu alitoa elezo lililotajwa mwanzoni wa makala hii. Nilitumikia kifungo changu katika Waldheim, kisha katika Halle, na hatimaye katika Hoheneck. Tukio moja au mawili yataonyesha jinsi Mungu alivyokuwa kimbilio na nguvu kwetu Mashahidi wa Yehova na jinsi Neno lake lilivyotutia nguvu.
Kwenye gereza katika Waldheim, sote dada Mashahidi tulikutana pamoja kwa ukawaida katika ukumbi mmoja, hivi kwamba tuliweza kufanya mikutano ya Kikristo. Kalamu na karatasi hazikuruhusiwa, lakini dada fulani walipata visehemu vya nguo na wakafaulu kutengeneza beramu ndogo yenye andiko la mwaka la 1953, lililokuwa: “Mwabuduni BWANA kwa uzuri wa utakatifu.”—Zaburi 29:2.
Mmojawapo wa walinzi wa kike alitufumania na kuturipoti bila kukawia. Mkuu wa gereza alikuja na kuambia dada wawili kati yetu wainue hiyo beramu. “Nani alitengeneza hii?” akauliza. “Hii inamaanisha nini?”
Mmojawapo wa dada alitaka kukiri na kuchukua lawama kwa ajili yetu, lakini tulinong’onezana haraka, tukikubaliana kwamba sisi sote twapaswa kushiriki hilo daraka. Hivyo tulijibu hivi: “Tuliitengeneza ili kutia imani yetu nguvu.” Hiyo beramu ilitwaliwa, na tulinyimwa milo ikiwa adhabu. Lakini wakati wote wa mahojiano, dada waliiinua hivi kwamba tungeweza kukazia akilini mwetu hilo andiko lenye kutia moyo.
Gereza ya wanawake katika Waldheim ilipofungwa, sisi dada tulihamishwa hadi Halle. Hapa tuliruhusiwa kupokea vifurushi, na ni nini kilichoshonelewa kwenye jozi la sapatu alilonitumia baba? Makala za Mnara wa Mlinzi! Bado naweza kukumbuka zile zilizokuwa na vichwa “Upendo wa Kweli Ni Wenye Kutumika” na “Uwongo Huongoza Kwenye Kupoteza Uhai.” Hizi na makala nyinginezo zilikuwa chakula kitamu kweli, na tulipozipokezana kisiri, kila mmoja alijifanyia maandishi.
Wakati wa uvamizi mmoja, mmojawapo wa walinzi alipata maandishi yangu ya kibinafsi yamefichwa katika godoro langu la majani. Baadaye, aliniita kunihoji na kusema kwamba alitaka kwa kweli kujua maana ya hii makala “Matazamio ya Wahofuo Yehova ya Mwaka wa 1955.” Yeye, akiwa Mkomunisti, alikuwa amehangaika sana juu ya kifo cha kiongozi wake, Stalin, katika 1953, na wakati ujao ulionekana wenye huzuni. Kwa habari yetu, wakati ujao ungeleta hali bora gerezani, lakini sikujua hilo. Nilieleza kwa uhakika kwamba matazamio kwa Mashahidi wa Yehova yalikuwa mazuri zaidi. Kwa nini? Nilinukuu andiko la kichwa la hiyo makala, Zaburi 112:7: “Hataogopa habari mbaya; moyo wake u imara ukimtumaini BWANA.”
Yehova Abaki Kuwa Kimbilio Langu na Nguvu Zangu
Kufuatia ugonjwa mbaya, niliachiliwa kutoka gerezani miaka miwili mapema, katika Machi 1957. Maofisa wa Ujerumani Mashariki walinisonga tena kwa sababu ya utendaji wangu mbalimbali katika utumishi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, katika Mei 6, 1957, nilichukua fursa ya kuponyoka kwenda Berlin Magharibi, na kutoka hapo nilienda Ujerumani Magharibi.
-